Kamati ya nidhamu tff imekosa nidhamu ijiuzulu.

Alfu Lela Ulela

JF-Expert Member
Oct 29, 2010
1,255
77

KAMATI YA NIDHAMU TFF IMEKOSA NIDHAMU IJIUZULU

Kamati ya nidhamu ya TFF iliyo chini ya mwenyeiti wa Sunday Kayuni imekosa nidhamu kwa Watanzania na inapaswa ijizulu. Kamati hii ilifanya kituko cha mwaka kwa kutoa adhabu ya uongo,iliyokosa ushahidi,badala yake ikazingatia majungu,umbea na chuki binafsi.



Mwenyekiti wa kamati hiyo Sunday Kayuni aliwaambia waandishi wa Habari kuwa wamemwadhibu Golikipa nambari moja wa klabu ya Simba Juma Kaseja faini ya sh. laki tano na kumfungia mechi tatu za ligi kuu,kutokana na kitendo chake cha kugoma kumsalimia mhe.Abass Kandoro (mkuu wa Mkoa wa Mwanza) aliyekuwa mgeni rasmi katika pambano la Simba na Yanga lilifanyika CCM Kirumba mwezi uliopita.



Tena katika kusisitiza Kayuni akasema kitendo alichokifanya Kaseja ni utovu mkubwa wa nidhamu na kinapaswa kulaaniwa na kila mpenda soka.Hapa ni kama vile Kayuni alikuwa anatuambia kuwa kutomsalimia mgeni Rasmi ni kosa kubwa,lisolopaswa kuvumiliwa. Mgeni Rasmi anawakilisha watanzania,hivyo kumkosea mgeni rasmi ni kuwakosea watanzania.



Kwa hiyo adhabu aliyopewa Kaseja ilikuwa inaendana na kosa lake KUTOMSALIMIA Mgeni RASMI.



Lakini siku hiyohiyo Kaseja alipohojiwa na vyombo vya habari alinukuliwa akikanusha kosa hilo na kusema alimsalimia mgeni rasmi.Tena kuomba uhakika wa maneno yake akaomba TFF waangalie mikanda ya video watabaini ukweli.



Lakini kama filamu vile,Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Bw.Abass Kandoro naye akatoa tamko.
Kwanza akaonesha kushangazwa na HUKUMU ya TFF,lakini akakiri kuwa alisalimiana na Kaseja na hata mkanda alionao unaonesha hivyo.Haikupita muda,vyombo vya habari navyo,vikachapisha picha ya Kaseja akisalimiana na Kandoro. TFF wakapata kihoro,wakaaibika,wakafadhaika.Aibu ikawavaa kuanzia utosini hadi kwenye unyayo wa miguu yao.




Hii ina maana walitoa hukumu,bila kuzingatia ushahidi (facts).Kwa sababu kama walipata malalamiko kuwa Kasega hakumsalimia Kandoro ilipaswa watafute ushahidi wa kutosha. Na sehemu ya ushahidi huo iwe ni mkanda wa video wa mechi hiyo. Lakini vilevile kabla ya kutoa hukumu wazingatie natural Justice,kwa kumwita mlalamikiwa ambaye ni Kaseja ajibu tuhuma,na hatimaye ndio TFF watoe hukumu.



Kwa kufanya hivyo wangetoa hukumu ya haki;hukumu ambayo haingeonesha upendeleo wowote na hakuna mtu awaye yeyote ambaye angehoji hukumu hiyo.Hata Kaseja mwenyewe.



Lakini kinachoonekana ni kuwa wajumbe wa kamatI ya nidhamu ya TFF baada ya kupokea malalamiko,walikutana,wakanywa chai, wakajigawia posho ya kikao,kisha wakaandika majina yao kwenye karatasi kwa ajili ya kumbukumbu wakasaini na kuondoka.



Kwa maana hiyo,shauri la Kaseja lilitolewa maamuzi kwenye “vikao vya chai vya TFF”.Kamati hii imekosa umakini na inapaswa ijiuzulu. Kukosa umakini katika mambo makini,ni kunajisi jamii unayoitumikia. Ni aibu chombo nyeti kama TFF,badala ya kukutana na kujadili mambo kwa kina, ili kufikia maamuzi sahihi, wanakutana kwenye vikao vya chai ili kugawana posho.



Kwa hali ivyoonekana huu ndio utendaji kazi wa kamati ya Nidhamu ya TFF. Je,ni mashauri mangapi yaliwahi kuwasilishwa kwenye kamati hii yakihitaji kujadiliwa kwa kina,lakini badala yake yakaishia kwenye “Vikao vya chai”kama la Kaseja?




Kamati ya maadili TFF imekosa maadili,nani wa kuiadilisha? Kamati imetumia dhambi kukemea dhambi.Imemdhalilisha Kaseja,imemshushia heshima,Inapaswa imwombe radhi.




Vinginevyo soka la Tanzania haliwezi kuendelea maana limejaa majungu na chuki binafsi.Majungu baina ya wachezaji wenyewe,majungu kwa viongozi wa soka na hata kwa makocha.




Ni nani asiyekumbuka kauli ya kocha wa zamani wa Taifa stars Marcio Maximo kuwa eti Kaseja hatacheza timu ya Taifa,labda yeye aondoke nchini.Alipoulizwa sababu akasema ni utovu wa nidhamu,lakini hakutaka kueleza ni utovu gani huo wa nidhamu Kaseja aliomfanyia.Haya kama si majungu ni nimi?




Maximo kwa nini hakutaja utovu wa nidhamu aliokuwa nao Kaseja? Kwanini aliachwa hadi akaondoka na siri yake moyoni? Hata alipoulizwa na viongozi wa serikali kuwa Kaseja kakufanyia kosa gani kubwa hivyo lisilosameheka? Aliishia kujing’atang’ata kwa Kiingereza chake cha kuombea maji “He is Indiscipline”.




Lakini Maximo yeye kama Mwalimu alichukua hatua gain juu ya utovu wa nidhamu wa Kaseja?Alimwonya mara ngapi? Na alitumia njia gani kumuonya?.
Kama alimuonya hakubadilika aliripoti kwa nani? Na alickukua muda gani kumwonya Kaseja kabla hajaamua kumtangazia hiyo adhabu yake ya “milele”.



Katika hili Maximo naye alikuwa mnafiki. Alimhukumu Kaseja kwa majungu,umbea,na chuki binafsi kama Sunday Kayuni alivyofanya. Maximo kwa kukataa kutaja “Indiscipline ya Kaseja” yeye ndiye alikuwa “Indiscipline”.



Sasa kwa hali hii tunategemea soka la Tanzania kukua? Tusipoacha majungu ,umbea na chuki binafsi tutaendelea kuwa wa mwisho kwenye viwango vya FIFA,maana wachezaji wenye uwezo na vipaji wataachwa na kuchezeshwa wasio na uwezo.



Lakini katika hali ya kushangaza zaidi mwenyekiti wa kamati ya maadili ya TFF Bw.Sunday Kayuni baada ya kutoa hukumu yenye utata,akajitokeza tena hadharani na kusema kuwa kosa la Kaseja si kutokumsalimia Mgeni rasmi bali wachezaji kadhaa wa Yanga. Lakini katika hali ya utata zaidi hao wachezaji wa Yanga ambao inadaiwa hawakusalimiwa na Kaseja hawakutajwa. Ebo! Hii ni picha ya kihindi.



Lakini Kayuni akatoa kali ya mwaka pale aliposema kuwa adhabu ya Kaseja itabaki palepale licha ya kosa la wali kubatilishwa.



Hivi huyu ni Sunday Kayuni au Sunday Kayumba?Maana akili zake zimekaa kikayumbakayumba.



Tangu lini makosa mawili yasiyofanana yakabebeana adhabu?Kuhamisha adhabu ya kosa moja kwenda jingine bila maelezo,inaonesha ukayumba wa fikra alionao Kayuni.



Mwanasheria mmoja ambaye alikerwa nu uchakachuzi wa Kayuni alisema hakuna adhabu za jumla kisheria.Kila kosa huwa na hukumu yake kulingana na uzito wa kosa lenyewe,lakini pia kulingana na ushahidi uliotolewa.



Kuhamisha adhabu ya kosa A kwenda kosa B ni ulimbukeni wa fikra.Katika hili Kayuni ameonesha namna alivyo na fikira kurupushi,kwenye kutoa maamuzi.




Kama adhabu ya kutomsalimia mgeni rasmi inalingana na adhabu ya kutomsalimia mchezaji mwenzako basi hadhi ya mgeni rasmi haipo.



Kisheria kamati ya Nidhamu ya TFF ilipaswa iombe radhi kutokana na kupotosha watanzania,imwombe na Kaseja radhi kwa kumchafua.Wafute adhabu zote za awali.Halafu kamati ikae upya kujadili shutuma mpya za Kaseja kutosalimiana na wachezaji wa Yanga. Baada ya kujiridhisha,adhabu itolewe kulingana na uzito wa kosa.




Lakini pamoja na yote hayo badoyanaibuka maswali kuhusu walamikaji haswa wa shutuma hizi.

Katika shitaka la kwanza Kandoro ndiye aliyepaswa kuwa mlalamikaji. Je ni kweli yeye ndiye aliyewasilisha malalmiko TFF kuwa hakusalimiwa na Kaseja? Jibu ni HAPANA. Kandoro aliyepaswa kuwa Mlalamikaji aligeuka na kuwa mtetezi wa Kaseja (shahidi namba moja wa upanole wa utetezi)
Akesema alisalimiana na Kaseja .TFF wakaumbuka!



Kama Kandoro alipinga kuwa Mlalamikaji, je ni nani mlalamikaji wa kesi hii?Ni nani aliwasilisha tuhuma TFF dhidi ya Kaseja?



Lakini hata katika hili la pili alilozuliwa Kaseja kuwa hakusalimiana na wachezaji wa Yanga,ni nani mlalamikaji?Je ni wachezaji wa Yanga?(mbona hawajatajwa?Je ni viongozi wa Yanga?Au ni mfadhili Mkuu wa Yanga Yusufu Manji? Jamani mlalamikaji wa kesi hii ni nani? Aliyewasilisha malalamiko TFF kuwa Kaseja hakusalimia wachezaji wa Yanga ni nani?



Jibu la uhakika ni moja tu.TFF ndio walalamikaji wa mashtaka yote mawili na haohao ndio Mahakimu.Ni ajabu lakini kweli.!! Na katika hili TFF wameweka rekodi ya aina yake duniani. Yaani kuwa mahakimu wa kesi ambayo wao wenyewe ndio walalamikaji.



Ili kufikia hitimisho la Mjadala huu,kamati ya Nidhamu ya TFF inapaswa kufanya mambo mawili.



La kwanza ni kuomba radhi.

Kamata inapaswa imwombe radhi Juma Kaseja kwa kumzisha,kumpakazia,na kumshushia heshima.Pia kamati imwombe radhi Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe.Abas Kandoro kwa kumzushia na kumchonganisha na Juma Kaseja.



Mwisho Kayuni na kundi lake wawaombe radhi watanzania kwa kuwapa taarifa za uongo,zilizokosa udhibitisho (facts). Taarifa za majungu na za kutunga. Na wakiri kuwa wanachuki binafsi na Kaseja, na kwamba walikuwa wanashirikiana na Maximo kumwua Kaseja kisoka.




Baada ya kuomba radhi jambo la pili kamati yote ya nidhamu ya TFF ijiuzulu.Wajumbe wa kamati (wakiongozwa na Kayuni) wajiuzulu kwa maslahi ya umma,na iundwe kamati mpya itakayo zingatia HAKI na MAADILI.
Kwa kufanya hivyo tutakuwa tumechangia kukuza soka la Tanzania kwa kiasi kikubwa.

muzeezaidi@gmail.com
 
Hili Jukwaa la Siasa ndg yangu Umefulia! Mods hamisha hii thread!
 
Back
Top Bottom