EasyFit
JF-Expert Member
- Jul 4, 2011
- 1,269
- 1,082
- Waziri Kombani atimuliwa
- Atuhumiwa kubadili muswada wa Katiba mpya
WAZIRI wa Sheria na Katiba, Celina Kombani, juzi jioni alitimuliwa ndani ya kikao cha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kwa madai ya kukiuka maagizo ya Bunge kuhusiana na muswada wa upatikanaji wa Katiba mpya ya nchi.
Akizungumza na Tanzania Daima Mbunge wa Muhambwe ambaye pia ni mjumbe wa kamati hiyo, Felix Mkosamali (NCCR-Mageuzi), alisema walifikia hatua ya kumtimua waziri huyo baada ya kubaini kuwa aliwasilisha muswada wa Katiba, badala ya kufanyia marekebisho vipengele kadhaa kama ilivyoamriwa na Bunge katika kikao cha Aprili, mwaka huu.
"Kwa mujibu wa kanuni za Bunge kifungu cha 84 na 85, muswada ukishawasilishwa bungeni ni mali ya Bunge, lakini kilichofanywa na waziri huyo ni kuandaa muswada mpya kinyume cha taratibu," alisisitiza Mkosamali.
Alisema kama waziri angetaka kuandaa muswada mpya alipaswa kuishirikisha kamati ya Bunge katika mchakato mzima kuliko alivyofanya kinyume na maagizo aliyopewa na Bunge ya kubadili baadhi ya vifungu na kuiweka katika lugha ya Kiswahili.
Mbunge huyo alisema mara baada ya kuwasilisha muswada bungeni ambao ulizua manung'uniko kutoka kwa wananchi wa pande zote mbili za nchi-bara na visiwani-hasa baada ya kugundua kuwa Rais amepewa madaraka ya uundaji wa Katiba mpya.
"Rais wa Tanzania analalamikiwa kuwa na madaraka makubwa mno na sasa katika uandikaji wa Katiba ya Watanzania wote bado anapewa kusimamia kila kazi inayohusiana na Katiba hii, hili hapana," alisema Mkosamali.
Akithibitisha kukataliwa kwa muswada huo Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Pindi Chana, alisema leo atatoa ufafanuzi kuhusu sakata hilo.
"Siwezi kusema sana juu ya hilo na hivi sasa ninaingia katika kikao cha IDEA ndugu yangu," alisema Pindi.
Muswada huo unaonyesha kuwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) na ile ya Zanzibar (ZEC) bado zinapewa mamlaka ya kusimamia masuala ya kura ya maoni ya wananchi wakati wa kupitisha Katiba.
Katika muswada huo mpya mkuu wa wilaya na watendaji wa kata, vijiji na mitaa wamepewa kazi ya kusimamia taratibu za ukusanyaji wa maoni ngazi ya chini hali ambayo haikubaliki.
Akizungumza na Tanzania Daima kwa njia ya simu jana, Waziri Kombani alikiri kutimuliwa na kuongeza kwamba yeye hana hatia kwa vile amefanya kilichotakiwa na kuwataka wabunge wanaoupinga wamuulize Spika.
"Nimefanya lililo ndani ya uwezo wangu lakini hilo la kusema kama muswada mpya au la aulizwe Spika yeye ndiye msemaji wa mwisho kwenye hilo," alisema Waziri Kombani.