Kama viongozi wa CCM na serikali ndiyo hawa .... basi tuna kazi kubwa!

Keil

JF-Expert Member
Jul 2, 2007
2,214
803
Walioandamana kumpinga Dk. Ngasongwa kushitakiwa

na George Maziku

WANANCHI walioandamana wilayani Ulanga, mkoani Morogoro kumpongeza Rais Jakaya Kikwete kwa kumwacha Dk. Juma Ngasongwa katika uteuzi mpya wa Baraza la Mawaziri alioufanya hivi karibuni, wameingia matatani na wanaweza kufikishwa mahakamani wakati wowote kuanzia sasa, Tanzania Daima imegundua.
Katika hali ya kushangaza na inayoashiria kuwa suala hilo lina shinikizo la kisiasa, Mkuu wa Wilaya ya Ulanga, Dk. Rajabu Rutengwe na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani humo Suleiman Magoto, ndio wanaoshika bango la kutaka wananchi hao washitakiwe.

“Tumeamua kuwakamata na kuwafikisha mahakani watu wote walioandamana siku hiyo kwa sababu maandamano yao hayakuwa na kibali,” alisema mkuu huyo wa wilaya alipozungumza na gazeti hili juzi kupitia simu yake ya kiganjani.

Pia mwandishi wa habari wa gazeti lililoripoti kuhusu maandamano hayo (si Tanzania Daima) anatafutwa na viongozi hao wa serikali na CCM ili aunganishwe na wananchi hao kujibu mashitaka yanayowakabili.

Dk. Rutengwe anamlalamikia mwandishi wa gazeti lililoandika habari ya maandamano hayo kwa kile alichodai kuwa kwanza mwandishi hakuwa na kibali cha viongozi wa wilaya hiyo cha kumruhusu kuripoti habari hiyo, pili habari yenyewe ni ya kuchochea chuki.

“Huyu mwandishi kwanza ni mchochezi, anaandika habari za kuchonganisha wananchi na viongozi wao, na isitoshe hakupata kibali chetu kama viongozi wa wilaya kumruhusu kuandika habari hiyo, hayo ni makosa makubwa”, alisisitiza Dk. Rutengwe.

Siku mbili tu baada ya Rais Kikwete kutangaza baraza jipya la mawaziri, kufuatia kujiuzulu kwa aliyekuwa Waziri Mkuu wa Tanzania, Edward Lowassa, ambapo aliwatupa nje baadhi ya mawaziri waliokuwa katika baraza la kwanza akiwemo Dk. Ngasongwa, gazeti moja la kila siku liliripoti kuwa wananchi wa tarafa za Malinyi na Mtimbira wilayani humo, waliandamana kumpongeza Rais Kikwete kwa kutomteua Dk. Ngasongwa katika baraza hilo.

Naye mwenyekiti wa CCM wilayani humo, aliliambia gazeti hili kwa njia ya simu ya kiganjani kuwa uongozi wa chama hicho wilayani Ulanga ulikuwa umekasirishwa mno na kitendo cha wananchi hao kuandamana kwa kumkejeli Dk. Ngasongwa, ambaye ni mmoja wa wabunge wawili wa CCM wilayani humo.

“Tumekubaliana na DC ambaye ni mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama wa wilaya yetu kuhakikisha watu wote walioandamana, pamoja na mwandishi aliyeandika habari hiyo wanakamatwa na kufikishwa mahakamani haraka.

“Si uungwana hata kidogo watu kushangilia kuanguka kwa mwenzao. Ngasongwa bado ni mbunge, kitendo cha kuandamana kumpongeza rais na kumkejeli mbunge ni kosa, ni lazima wahusika watuambie wamepata wapi utamaduni huo,” alisisitiza Magoto.

Lakini wananchi walioshiriki maandamano hayo, walipoongea na gazeti hili kwa njia ya simu za kiganjani, kwa nyakati tofauti na kwa sharti la kutotajwa, walisema hawakufanya kosa lolote kwa kuandamana kumpongeza rais wao kwa kuteua baraza zuri la mawaziri.

Pia walisema hawakutenda kosa lolote kwa kuonyesha hisia zao dhidi ya mbunge wao, ambaye walidai hajatekeleza ahadi nyingi alizozitoa wakati wa kampeni za uchaguzi wa 2005, na kwamba kama watakamatwa na kushitakiwa kwa kitendo hicho basi huo ni udikteta wa hali ya juu.

“Hii ni demokrasia gani? Hivi kweli hata tukitaka kumpongeza rais kwa kazi nzuri lazima tuombe kibali? Huyu DC ni wa kizazi kipi? Mbona anataka kubana uhuru wa binadamu?” alihoji mmoja wa watu walioshiriki maandamano hayo ambaye aliliambia gazeti hili kuwa huenda yeye akawa mshitakiwa namba moja katika kesi hiyo.

Hata hivyo, baadhi ya watu walioshiriki maandamano hayo wameapa kupambana na kwamba wapo tayari kufunga safari kwenda Dar es Salaam kuonana na Rais Kikwete, ili wamfikishie kilio chao kuhusu manyayaso waliyodai kuyapata kutoka kwa viongozi wao wa wilaya kutokana na kitendo chao cha kuandamana kumuunga mkono.

Source: Tanzania Daima
 
Makubwa haya jamani!!
Kama mpaka kuandika habari mpaka upate kibari kutoka kwa wahusika hiyo nayo kali
Hawa nao eti ni viongozi jamani, wanadiliki kusema eti kuachwa kwa Mbunge kwenye mabara ni kuanguka kisiasa, kwani alikuwa na ndoa na uwaziri??
na Bado wanawakata wananchi wasimpongeze raisi kwa kazi nzuri(Sijui kama ni nzuri kweli) kwa kumuacha Bogasi wao

The, the, the, Makubwa, Hawa ndo viongozi wa Tanzania, Nchi yenye amani

Mimi naweza kusema kwamba haya ni mambo ya kasi mpya . Hivi hata Ngasongwa mwenyewe hawezi kuamka na kusema hapana maana jina lake linatumika vibaya na kumuweka pabaya zaidi .Huko kutampa hard time akienda kuwaomba kura zao tena ama hawa si wapiga kura ? Mkuu wa Wilaya na mwenzake wanajua kweli utawala wa sheria ?
 
Back
Top Bottom