Elections 2010 Kama CCM hawawezi, kwanini wanagombea?

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,475
39,991
M. M. Mwanakijiji (Tanzania Daima Jumatano)


SIPENDI kweli watu wenye kuamini kuwa hawawezi. Na sipendi zaidi viongozi ambao wanatumia lugha ya kutokuweza. Leo hii tumeanza kutukuza kutokuweza na kuanza kuamini kama imani ya kidini.


Wapo kati yetu wagombea ambao wanatuhubiria kuwa “hatuwezi” na wapo wananchi ambao wanarudia kauli hii kana kwamba wamekula yamini kuwa wasiporudia basi makubwa yatawakuta.


Na kinachoniudhi ni hoja kwamba hatuwezi kuwapatia watoto wetu elimu ya bure hadi kidato cha sita na kuhakikisha kuwa kila kijana wa Kitanzania anayetaka shahada ya kwanza anaweza kuipata.


Wanasiasa, mashabiki wao na baadhi ya watu wanataka tuamini uongo kuwa haiwezekani kuwapatia watoto wetu elimu ya bure. Wanasema hivi kwa kujiamini na kama kwa kujisifia. Lakini watu hawa hawa tukiwabana kuwauliza wanakuja juu na kudai mengine yanawezekana.


Ni hawa hawa waliotuambia kuwa “hatuwezi” kuendelea bila wawekezaji na hivyo wameendelea kupiga magoti katika madhabahu ya wawekezaji na ni hawa hawa waliotuambia kuwa hatuwezi kuwalipa wafanyakazi wetu mishahara minono yenye kuendana na hali ya uwezo wetu wa kiuchumi. Na ni hawa hawa ambao wanarudia kutuambia kuwa hatuwezi kupigana na ufisadi!


Ati kuwapatia watoto wetu elimu ya bure haiwezekani lakini mengine ya kwao yanawezekana!


Wao wameweza kununua dege la Rais kwa karibu bilioni 50 kwa ajili ya matumizi ya mtu mmoja na kikundi cha watu wachache wenye uwezo wa kukodi.
Hata tungemuuliza msimamizi wa ndege za serikali atuambie ni kiasi gani cha gharama ya ununuzi wa ndege hizo kimeweza kurudi karibu miaka kumi baada ya kununuliwa na itachukua muda gani tutaweza kukirudisha?


Tulipowaambiwa kuwa haiwezekani wafanye hivi walikuwa juu na mmoja wao akatuambia kuwa ati hata kula nyasi tutakula lakini serikali “itaweza” kununua dege hilo! Kuwapa watoto wetu elimu ya bure ati haiwezekani!


Wakanunua rada ya kijeshi ambayo kwa nchi yetu tungeweza kupata rada nyingine bora zaidi. Tena wakanunua kwa bei ya kuruka wakiwa na suti zao na tai tena kwa mbwembwe! Kwa shilingi nyingine karibu bilioni 40 wakanununa rada hiyo. Tukawapigia kelele na kusema haiwezekani fedha hizo tungeingiza kwenye elimu na kusaidia watoto wetu. Wakatubeza na kudai kuwa “sisi nchi huru tutafanya tunalotaka bila kuingiliwa na nchi yoyote”. Kumbe wakatuambia ati tunaweza! Kuwapa watoto wetu elimu ya bure wanasema haiwezekani!


Wakajenga uwanja wa Taifa wa Mpira wa Soka kwa mbwembwe kwa shilingi nyingine bilioni 50 ambao hadi hivi sasa sikumbuki ni lini umeweza kujaza maelfu ya watu maana hata mechi ya Brazili ilishindwa kujaza watu! Uwanja huo mzuri na wenye kusifiwa ukiwa na vikolombwezo vya kila aina uko kilomita chache tu kutoka shule zenye madirisha mabovu na nyingine bado watoto wake wakisoma kwenye vumbi! Tukiwauliza tuliwezaje kufanya hilo wanatuambia kwa sababu “tunaweza”. Lakini kuwapa watoto wetu elimu ya bure haiwezekani.


Ni hawa hawa chini ya utawala wao ambapo wizi mkubwa wa zaidi ya bilioni 133 ulitokea na upotevu mwingine wa mabilioni ya shilingi kutoka Benki Kuu. Katika ujanja wao wanaoujua wao wakaweza “kurudisha” kama bilioni 60 (msiniulize zilitoka wapi, kwa nani, zilirudishwa vipi na wapi). Na hapo hapo wakazisamehe bilioni nyingine nyingi huku kesi za wahusika zikiendelea kuzunguka taratibu katika baraza la haki. Ndipo tukajua kuwa kuna fedha nyingi tu zimechezewa na wajanja benk kuu. Yote hayo yaliwezekana. Lakini kuwapa watoto wetu elimu ya bure ati haiwezekani!


Na ni watawala hao hao walioshindwa ambao walisimamia chini yao makampuni hewa yaliyochotewa mabilioni ya fedha na hadi hivi sasa hawataki hata kuyazungumzia kwenye kampeni zao. Makampuni ya Meremeta, Tangold, Deep Green, n.k yote yalishirikiana kuchota mabilioni ya fedha kama vile kisimani na yakatokomea huku wahusika wake wakipigiwa kampeni kurudi tena Bungeni na wengine wakipewa pongezi mbalimbali za kutulizwa. Karibu bilioni 200 zimetoweka hivi hivi kupitia mikono ya wajanja hawa. Hilo linawezekana. Lakini kuwapa watoto wetu elimu ya bure ati haiwezekani.


Ni hawa hawa ambao wameweza kutenga mabilioni ya shilingi kila mwaka kwa ajili ya samani na chai katika maofisi yao katika kile wanachokiita kukirimia wageni. Mwaka mmoja tu uliopita walitenga bilioni 30 hivi za chai! Ati hilo linawezekana! Watawala wetu wanatuamini kuwa ipo haja ya lazima sana kutenga kiasi hicho cha fedha lakini upande wa pili wanawaambia watoto wetu kuwa “haiwezekani” kuwapatia elimu ya bure kwa sababu “Taifa halina fedha”!


Niseme nini tena? Nirudie mifano gani mingine ya upotevu wa karibu shilingi trilioni 3 katika miaka hii michache tu iliyopita. Niseme nini kuhusu matumizi ya Halmashauri, Taasisi na Wakala mbalimbali? Niseme juu ya kiasi kinachotengwa kwa ajili ya posho za vikao si mtazimia? Mnataka nikumbushe posho wanayolipwa mawaziri, wabunge na watendaji wa serikali wanaposafiri ndani na nje ya nchi? Niseme kuhusu ununuzi dege la Airbus? Nikumbushie suala la mikataba ya umeme (Richmond, IPTL, Dowans n.k)? Nirudie kwenye suala la mikataba ya madini kuanzia ya Buzwagi? Mnataka nigusie mauzo ya mbuga zetu na nyara zetu? Au mnataka nizungumzie upotevu wa utajiri wa Tanzanite na Dhahabu yetu?



Yaani yote hayo “yanawezekana” chini ya watawala wetu walioshindwa isipokuwa suala la kuwapa watoto wetu elimu ya bure?


Lakini kipo kingine kinachoniudhi mimi zaidi. Wapo watu kati yetu ambao kweli wanaamini haiwezekani. Nimemuona mwandishi mmoja juzi kwenye kipindi kimoja cha TV akishangaa inawezekana vipi? Nimewasikia watangazaji kwenye radio moja nao wakihoji hilo linawezekana vipi? Yaani, wapo watu kati yetu kabisa ambao wanaamini haiwezekani kuwapa watoto wetu elimu ya bure na kuwaandaa kwa elimu ya juu! Naam wapo wagombea urais, ubunge na udiwani ambao wanaamini haiwezekani!


Sasa ninajiuliza kama hawa watu wanaona haiwezekani kutumia kila aina ya uwezo na raslimali zetu kuwapatia watoto wetu tunu na zawadi na haki ya elimu tutumie fedha zetu kwa vitu gani? Naam! Tunajua baadhi ya vitu tunavyotaka kutumia fedha hizo. Lakini inakuwaje mamilioni ya watu wetu wanaamini uongo huu na kuukumbatia?


Ndugu zangu, wapiga kura wa Tanzania wamepewa uchaguzi mwepesi kweli na wa moja kwa moja. Vijana wa Tanzania wamepewa uchaguzi huo na wazazi wa Tanzania wamepewa uchaguzi huo huo. Kwamba waendelee kuchagua watu wenye fikra za kutokuweza kutoa elimu ya bure kwa watoto wetu au kujaribu wale wanaoamini kuwa wanaweza kufanya hili.


Kwa wale ambao wanajua haiwezekani ni lazima wachague CCM na wagombea wake wote kwani watakuwa wamepigia kura kukata kwao tamaa!


Watakuwa wamepigia kura kutokujaribu na kutokuweza. Kwa kadiri ya kwamba CCM haitaki kuamini kuwa elimu ya bure inaweza kutolewa (aidha kwa kuwaogopa IMF au Benki ya Dunia miye sijui) basi wamechagua kuwa chama cha kutokuweza.


Wanachama na mashabiki wake lazima washangilie na kuchekelea kutokuweza huku. Wale wote wanaoamini kuwa “hatuna uwezo” wa kutoa elimu bure kwa watoto wetu ni LAZIMA wachague CCM kwani kwa kufanya hivyo watakuwa wamefuata dhamira zao.


Kwa wale ambao wanaamini inawezekana kufanya hivyo na kuwa tunao uwezo wa raslimali wa kuweza kutoa elimu ya bure kwa watoto wetu uchaguzi wao nao uko wazi na watatakiwa kufuata mioyo yao. Kuna vyama viwili ambavyo vinaahidi elimu ya bure.
Wapo CUF na wapo CHADEMA. Linapokuja suala muhimu kama elimu ambalo kwangu naamini ni muhimu sana basi mpiga kura ni lazima ajiulize je nataka mtoto wangu asome bure hadi kidato cha sita au chuo kikuu?


Akijibu “ndiyo” basi ni lazima achague mojawapo ya vyama hivyo kuendana na ajenda zao nyingine. Na akisema hapana kwa sababu “haiwezekani” ni lazima achague CCM. Ni chaguo la kimantiki.


Wanasema kwa mapozi, hili haliwezekani,

Kama wao hawawezi, kura waomba za nini?
Kama hili kwao kazi, tuwachague kwa nini?
Nawauliza jamani, si bora waje wengine?
 
Kweli kabisa ndugu yangu, ni bora waje wengine. Hata wao wenyewe wanaosema kuwa hawawezi, wanajua watanzania wanataka uongozi mwingine!

Ndio maaana wanahangaika kila kukicha kusimika mabango makubwa barabarani, utadhani wanafanya kampeni za kibiashasa. Kama wanadhani tunajua wanaweza, kwanini wanajihangaisha, kwanini wanataharuki, hadi kuweka mabango yanayokiuka sheria?
 
Mwenzao hana hata bango moja ila wanamwogopa kiasi hicho,je naye angekuwa na mabango sijui wangesemaje?
 
Asante MMJ

Niseme nini tena? Nirudie mifano gani mingine ya upotevu wa karibu shilingi trilioni 3 katika miaka hii michache tu iliyopita. Niseme nini kuhusu matumizi ya Halmashauri, Taasisi na Wakala mbalimbali? Niseme juu ya kiasi kinachotengwa kwa ajili ya posho za vikao si mtazimia? Mnataka nikumbushe posho wanayolipwa mawaziri, wabunge na watendaji wa serikali wanaposafiri ndani na nje ya nchi? Niseme kuhusu ununuzi dege la Airbus? Nikumbushie suala la mikataba ya umeme (Richmond, IPTL, Dowans n.k)? Nirudie kwenye suala la mikataba ya madini kuanzia ya Buzwagi? Mnataka nigusie mauzo ya mbuga zetu na nyara zetu? Au mnataka nizungumzie upotevu wa utajiri wa Tanzanite na Dhahabu yetu?
 
Mwanakijiji,

Nimesoma hii article, na nilivyofika mstari wa mwisho machozi yamenilenga.
Nashindwa kuamini kwanini watanzania walio wengi hawabadiliki, na wako mstari wa mbele kuserebuka kwenye mikutano ya CCM. Nikiona wanavyoserebuka...inasikitisha kwa kweli...sijui wanataka wafumbuliwe macho vipi?

Hivi si inawezekana baada ya uchaguzi CHADEMA na CUF wakaunganisha matokeo ya kura zao?? Kwa sababu honestly CCM has to come out, they are disgracing


Asante sana
 
Mwanakijiji... Jua tu kwamba waliolishwa yamini ya hatuwezi, haiwezekani na ni vigumu kutekelezeka ni WAVIVU WA KUFIKIRI AU FIKRA ZAO ZIMEISHIA ukingoni... watawezaje ili hali shibe ni mwana malevya.. Kama wangekuwa na njaa ya kuweza basi wangeweza lakini wakati huu hawahajui njaa ni mwana malegeza... WAMESHIBA Tayari na kila kitu kwao haiwezekani...

Sijui Mungu atupe nini sisi watanzania ili tuweze chambua pumba na mchele haraka na tufamye maamuzi ya Busara na tulete mabadiriko ya maisha safi kwetu na vizazi vijavyo!!!

Kwa jinsi wanavyosema hatuwezi inanifanya nifikirie... je Hivi wakati wa kupigania uhuru pia kulikuwepo na watu wa aina hiyo wa HAiwezekani? Ilikuwaje Nyeyere akaweza kuwashawishi mpaka wakakubali kumtoa mkoloni...ni mawazo hayo hayo yananijia pia wakati wa vita ya maji majimaji...mbona watu waliweza kupambana vilivyo na mkoloni ingawaje alishinda lakini alitambua ari ya watu na kuja na mbinu mpya... May be inafaa turudi ukolonini ili tuweze na akina Dr.Nyerere wafufuliwe kwa lazima na akina sheikh Yahya wanaoweza kutoa ulinzi usioneekana...
 
MMJ
makala yako imebeba ujumbe mzito katika lugha inayoeleweka moja kwa moja.
Wadanganyika wataelewa taratibu, japo inachukua muda kubadili mindset ya wengi wetu.
 
I used to be CCM dam-damu but increasingly I just dislike it. Even worrying, is the fact that I now hate uongozi wa CCM. Emphatically HATE!! Conduct yao kwenye kura za maoni ya wagombea uchaguzi huu umeleta hisia hii, haswa kuhusiana na kuenguliwa watu walioshindwa na kutoa sababu zenye uongo na ufitini mkubwa, na kule kuruhusu kadi feki zitumike ili mradi liende imeniudhi vibaya sana. Wameharibu chama vibaya sana!!
 
Wadanganyika wataelimika tuu, watake wasitake hakuna kurudi nyuma mpaka kieleweke!!!! Vote for President SLAA 2010
 
Waliutangazia umma **** theruthi za bajeti ya nchi (mfano mwaka huu ni takribani trilioni 3.5) zinapotea kuujanjaujanja. Halafu wanasema elimu ya bure kwa watoto wetu haiwezekani!
 
Kama wao hawawezi, kura waomba za nini?
Kama hili kwao kazi, tuwachague kwa nini?
Nawauliza jamani, si bora waje wengine?

CCM hawawezi, kufanya kitu muhimu,
Yabidi wavue jezi, na kuipumzisha timu,
Chadema wavae jezi, kutuletea utamu,
CHADEMA anza zoezi, la kuzishika hatamu.

Elimu bure utoe, kwa watoto vijana pia,
Matibabu nayo bure, pasi hata kulipia,
Mishara nayo bwerere, maslahi kutupatia
CUF CHADEMA chagua, nuru zao twaziona.

Msinitolee mimacho, hiyo yawezekana
Tatizo ni kile kificho, za mali kutonekana
CHADEMA yapinga hicho, ili tupate neema
Inuka kapige kura, CUF CHADEMA chagua



 
Back
Top Bottom