Mwanahabari Huru
JF-Expert Member
- Mar 9, 2015
- 14,243
- 34,899
=======
MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dodoma imetoa amri ya kutofanyika uchaguzi wa Ubunge katika Jimbo la Arumeru Mashariki, mpaka shauri la madai Na. 22/2019 lililofunguliwa na aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Joshua Nassari litakapotolewa uamuzi.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa umma leo tarehe 20 Machi 2019 na Nassari inaeleza kuwa, amri hiyo ya mahakama imetolewa leo baada ya shauri hilo lililofunguliwa tarehe 18 Machi mwaka huu, kuitwa kwa ajili ya kutajwa.
Nassari alifungua shauri hilo chini ya hati ya dharula dhidi ya Spika wa Bunge, Job Ndugai na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Prof. Abelardus Kilangi kuomba kibali cha mahakama ili kufungua shauri la kufuta na kutengua uamuzi wa bunge wa kumvua ubunge.
“Shauri hilo liliitwa leo tarehe 20 Machi 2019 mbele ya Jaji L. Mansoor kwa ajili ya kutajwa,” inaeleza sehemu ya taraifa hiyo.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa, baada ya mahakama hiyo mbele ya Jaji Mansoor kusikiliza hoja za pande zote mbili, ilitoa siku saba kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuwasilisha majibu ya madai ya Nassari, kisha tarehe 27 Machi mwaka huu, shauri litaanza kusikilizwa.
“Itakumbukwa kwamba tarehe 17 Machi 2019 nilizungumza na wanahabari na wananchi kuhusu kutoridhishwa kwangu na uamuzi wa spika wa bunge, wa kunivua ubunge bila hata ya kunisikiliza na bila kuzingatia sababu ambazo nilimwandikia awali,” inaeleza sehemu ya taarifa ya Nassari.
Mnamo tarehe 14 Machi 2019 Spika wa Bunge, Job Ndugai kupitia Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano wa Kimataifa cha Ofisi ya Bunge, alitoa taarifa ya kumvua ubunge Nassari, huku akieleza sababu zilizopelekea kuchukua hatua hiyo.
Miongoni mwa sababu zilizotolewa katika taarifa hiyo, ni pamoja na Nassari kukiuka katiba ya nchi kwa kutohudhuria vikao vya mikutano ya Bunge mitatu mfululizo.
Mikutano hiyo ni mkutano wa 12 wa tarehe 4 hadi 14 Septemba 2018, mkutano wa 13 wa tarehe 6 hadi 16 Novemba 2018 na mkutano wa 14 wa tarehe 29 Januari hadi 9 Februari mwaka huu.
Katika taarifa hiyo,ilieleza kwamba Spika Ndugai alimwandikia barua Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Semistacle Kaijage akimtaarifu kwamba Jimbo la Arumeru Mashariki lipo wazi kutokana na mbunge wake kupoteza sifa za kuendelea kuwa mbunge.
“Kufuatia barua hiyo, Tume ya Taifa ya Uchaguzi inaweza kuendelea na mchakato wa kumpata mbunge wa kujaza nafasi hiyo iliyo wazi ya jimbo la Arumeru Mashariki,” ilieleza sehemu ya taarifa ya Spika Ndugai wakati akitangaza uamuzi wa kumvua ubunge Nassari.