Elections 2010 JK: Wagombea uchaguzi mkuu wa Oktoba 31 wasibughudhiwe

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,316
33,112
Rais Jakaya Kikwete amewataka wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya na makatibu tawala nchini kuhakikisha wagombea wa nafasi mbalimbali katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 31 mwaka huu hawabugudhiwi.

Rais Kikwete aliyasema hayo jana katika kikao cha siku mbili cha wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya na makatibu tawala kinachofanyika mjini Dodoma.

Alisema uchaguzi ukiharibika viongozi hao ndio wa kulaumiwa na kwamba hataki walaumiwe kwa jambo hilo.
"Uchaguzi mkuu unakaribia kufanyika na ukiharibika ni nyinyi wa kulaumiwa, sitaki mlaumiwe… …mhakikishe kuwa wagombea hawabugudhiwi,"alisema.

Aliwataka viongozi hao kuhakikisha kuwa viongozi hao wanapewa nafasi ya kuendesha mikutano yao na siku ya kupiga kura, wapiga kura wanapewa haki zao za kupiga kura.

Aidha, aliwataka viongozi hao kuendelea kusimamia shughuli za maendeleo wakati wa uchaguzi mkuu kwa sababu ni lazima shughuli hizo ziendelee.

Kwa upande wa kutimiza ahadi walizotoa wakati wakiingia madarakani, Rais alisema kuwa yale ambayo hayajatekelezwa kwa kipindi cha bajeti nne zilizopita, yanaendelea kukelezwa katika bajeti ya mwaka huu.

Hata hivyo, alisema serikali ya awamu nne imefanikiwa sana kutekeleza yale waliyodhamiria na kwamba yaliyobakia ni machache sana.

Akimkaribisha Rais, Waziri Mkuu Mizengo Pinda, alisema katika ziara zake alizozifanya kwenye mikoa mbalimbali amefarijika sana kuona shughuli za maendeleo zikitekelezwa vizuri.

"Nimefarijika sana, ninayo imani kuwa utashinda kwa kishindo katika uchaguzi mkuu…umeandaa jeshi zuri kama kuna watakaokuponyoka ni wale ambao watakwenda kugombea ubunge,"alisema.

Alisema viongozi hao wamechangamkia sana shughuli za maendeleo hasa kwa upande wa kilimo.

Naye Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, (Tamisemi), Celina Kombani, alisema kikao hicho kinalenga katika kupokea maelekezo na kutekeleza.

Pia kinalenga katika kukumbushana masuala ya msingi kama kilimo kwanza, uchaguzi na kutoa maelezo nini cha kufanya kwa viongozi wa kada hizo wanaotaka kugombea.

CHANZO: NIPASHE JUMAPILI
 
Back
Top Bottom