JK akwepa waandishi baada ya kutua Dar

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,007
JK akwepa waandishi baada ya kutuaDar

na Mobini Sarya
Tanzania Daima

IKIONEKANA ni mwendelezo wa kukwepa kujibu tuhuma, maswali na ukosoaji dhidi ya serikali kutoka kwa waandishi wa habari, jana, Rais Jakaya Kikwete, alionekana dhahiri kukwepa kuzungumza na waandishi wa habari, waliojitokeza katika mapokezi katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu J.K. Nyerere, Dar es Salaam.

Rais Kikwete ambaye amekuwa hana kawaida ya kukataa kuzungumza na waandishi wa habari mara anaporejea kutoka safari za nje ya nchi, baada ya kuwasili uwanjani hapo jana, alionekana kusalimiana na viongozi mbalimbali wa chama na serikali waliofika kumpokea.

Hali hiyo ilionekana kuwakatisha tamaa waandishi wa habari waliofika mapema uwanjani hapo wakiwa na shauku ya kupata ufafanuzi juu ya ziara yake sanjari na masuala mbalimbali yanayoendelea nchini hivi sasa.

Wakati Rais Kikwete akikwepa kuzungumza na waandishi wa habari nchini, ameonekana kukubali kuzungumza na vyombo vya habari, yakiwamo magazeti ya nje ya nchi.

Rais Kikwete amerejea nchini huku akikutana na matukio kadhaa ya mawaziri wake kuzomewa na wananchi wakati wakiwa katika ziara za kuelezea ubora wa bajeti mikoani, ambayo ilisomwa bungeni na Waziri wa Fedha, Zakia Meghji, miezi kadhaa iliyopita.

Mlolongo wa matukio hayo, pamoja na shinikizo kutoka kwa mabalozi wa nchi za nje, viongozi wa dini, wanaharakati na wananchi wanaotaka serikali ijisafishe dhidi ya tuhuma za ufisadi na zile za Benki Kuu ya Tanzania (BoT), unaonekana kumtesa Rais Kikwete.

Jana, rais baada ya kusalimiana na mawaziri na watendaji wengine wa ngazi za juu serikalini, alitoka nje ya chumba cha watu mashuhuri (VIP) na kusalimiana na makada wa CCM na wananchi wengine kabla ya kuingia katika gari na kuondoka na msafara wake.

Kabla ya kuwasili uwanjani hapo, umati wa watu wakiwamo makada wa CCM, walijitokeza wakiwa wamevalia sare za CCM huku wakiimba nyimbo za kuwakejeli wapinzani.

Mapokezi hayo yalitekwa na wafuasi wa CCM walioanza kuingia uwanjani hapo kwa mabasi ya abiria huku wakiwa na mabango yenye ujumbe wa kumsifu rais.

Baadhi ya mabango hayo yalikuwa na ujumbe unaosomeka: ‘Hongera Mheshimiwa… kwa kutangaza kuwapata wawekezaji,’ sisi ni CCM tawi la……, ‘Karibu Mwenyekiti… tuko pamoja na wewe’, huku wakisaliana kwa salamu za kichama.

Ujumbe na mabango hayo kwa ujumla, yalionekana kuwakera baadhi ya wananchi wa kawaida waliofika uwanjani hapo kumlaki rais.

Baada ya kushuka kwenye ndege, rais alilakiwa na Waziri Mkuu, Edward Lowassa, Waziri wa Fedha, Zakia Meghji, Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi, Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko, Basil Mramba, Spika Samuel Sitta na viongozi wengine wa chama na serikali.

Baada ya rais kuingi VIP, baadhi ya wasaidizi wake walisikika wakiwaambia waandishi waliokuwa wamemtangulia, kuwa hawakuwa na taarifa kama rais angekutana na waandishi wa habari.

Kwa mazingira hayo, waandishi wa habari walitoka nje baada ya kuelezwa kwamba baada ya muda rais atatoka nje kuwasalimia wananchi waliofika uwanjani hapo kumlaki.

Hata hivyo, baada ya kutoka nje, waandishi walikuwa na wakati mgumu wa kupata nafasi ya kumuuliza maswali, huku wasaidizi wake wakionekana kutotoa nafasi hiyo hadi alipopanda gari na kuondoka uwanjani hapo.

Katika hatua nyingine, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (CHADEMA), jana aligongana ana kwa ana na Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi.

Mbunge huyo, aliyesimamishwa kuhudhuria vikao vya Bunge kwa miezi sita baada ya kudaiwa kulidanganya Bunge kusema uongo kuhusu kusainiwa kwa mkataba wa Buzwagi, aligeuka kuwa kivutio katika mapokezi hayo, baada ya kugongana ana kwa ana na Karamagi, aliyesaini mkataba huo nchini Uingereza.

Zitto alisimamishwa baada ya kutoa hoja ya kutaka kuundwa kwa kamati teule ya Bunge kuchunguza mazingira yaliyofanya mkataba huo kusainiwa London, Uingereza, Februari mwaka huu huku kukiwa na tamko la rais la kusitisha kusainiwa mikataba mipya.

Katika tamko hilo la Desemba mwaka juzi, Rais Kikwete alitaka kusitishwa kusainiwa kwa mikataba mipya hadi mikataba iliyopo itakapopitiwa upya.

Baada ya kukutana jana, Zitto alionekana kumchangamkia Karamagi aliyekuwa na Waziri Meghji, kwa kusalimiana nao na kisha kuondoka eneo hilo.

Zitto, alikuwa anarejea nchini akitokea Kenya alikokuwa amealikwa kwenda kuhudhuria uzinduzi wa kampeni za Chama cha Orange Democratic Movement cha Raila Odinga, ambako alikaa kwa siku tatu.

Rais Kikwete alikuwa ziarani nchini Marekani, ambako pamoja na mambo mengine, alihudhuria Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.

Katika ziara hiyo aliyoianza Septemba 15, Kikwete amefanya mambo mengi katika nyanja za siasa, uwekezaji, utalii, madini, michezo, biashara, elimu na utamaduni.
 
Baada ya kushuka kwenye ndege, rais alilakiwa na Waziri Mkuu, Edward Lowassa, Waziri wa Fedha, Zakia Meghji, Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi, Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko, Basil Mramba, Spika Samuel Sitta na viongozi wengine wa chama na serikali.

Kweli Tanzania watu hawana kazi inamaana mawaziri wote hawa hawana kazi hadi wakamlaki raisi au hili ni changa la macho kwa kikwete? Duh kweli Tanzania ni Tanzania.
 
Mobini Sarya said:
Kwa mazingira hayo, waandishi wa habari walitoka nje baada ya kuelezwa kwamba baada ya muda rais atatoka nje kuwasalimia wananchi waliofika uwanjani hapo kumlaki.

Hata hivyo, baada ya kutoka nje, waandishi walikuwa na wakati mgumu wa kupata nafasi ya kumuuliza maswali, huku wasaidizi wake wakionekana kutotoa nafasi hiyo hadi alipopanda gari na kuondoka uwanjani hapo.

Sio huyu rais aliyekuwa akisema waandishi wa habari waachwe wafanye kazi yao? Leo imekuwa hivi tena amepata kugugumizi.
 
hao mamia ya wanaccm walioenda kumpokea bosi wao walihongwa kwa kupewa 5000 na magari ya bure usifikili mtu ana wakati wabure wakupoteza kwenda kumpokea fisadi.
 
hao mamia ya wanaccm walioenda kumpokea bosi wao walihongwa kwa kupewa 5000 na magari ya bure usifikili mtu ana wakati wabure wakupoteza kwenda kumpokea fisadi.

Gharama ya kupokelewa kwa mbwembwe uwanja wa kimataifa wa JKN ni £2.00 au $5.00 kweli tumekwisha yuko wapi yule aliyesema nikifufuka .......................................
 
daahh kumbe we jamaa mkongwe humu!daahh 2007 miaka kumi sasa
 
Back
Top Bottom