Jinsi Eric Shigongo alivyojiunga Chuo Kikuu akiwa na elimu ya msingi

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Apr 29, 2016
20,744
25,425
Licha ya kufeli darasa la saba, mbunge wa Buchosa, Eric Shigongo amefanikiwa kuhitimu chuo kikuu akiibuka mwanafunzi bora aliyefaulu kwa kiwango cha juu zaidi.

Kabla ya kwenda chuo kikuu, anasema alijifunza lugha ya Kiingereza mtaani, kama wengine wanavyojifunza lugha ya makabila.

Shigongo aliibuka mwanafunzi bora Chuo Kikuu cha Tumaini alikohitimu shahada yake baada ya kupata GPA ya 4.8.

Akizungumza na gazeti hili kwenye mahojiano maalumu yaliyofanyika nyumbani kwake, Ipagala jijini Dodoma mwishoni mwa wiki, Shigongo alisema alifeli mara mbili darasa la saba na akadhani hiyo itakuwa mwisho wa safari yake kielimu.

Lakini, alipata bahati ya kwenda kusoma kozi ya mwaka mmoja ya unesi msaidizi wilayani Sikonge mkoani Tabora, lakini kutokana na mshahara kuwa mdogo anasema aliacha kazi na kukichana cheti alichokuwa nacho.

Kujifunza Kiingereza
Shigongo anasema alijifunza Kiingereza mtaani. “Kiukweli sikufundishwa, naongea Kiingereza kama lugha ya kikabila, ukiniambia adjective nini sijui, sijui adverb yale mambo mimi siyajui kabisa mimi naongea kama kabila.

“Mimi (Sikonge) nilikutana na kijana anaitwa Jesse alikuwa mtoto wa daktari anaitwa Camstra, ambaye ni surgeon (daktari wa upasuaji) aliyetokea Uholanzi.

Sasa mwanawe Jesse alikuwa hajui Kiswahili akawa rafiki yangu, mimi namfundisha Jesse Kiswahili yeye ananifundisha Kiingereza, kwa hiyo nikashika pale lugha.

“Kwa hiyo nilifundishwa namna ya kuzungumza siyo kujua hii ni adverb au adjective. Baadaye nilipojua Kiingereza nikaanza kuwa nasikiliza redio na kusoma gazeti la Sunday News. “Nikawa najifunza Kiingereza, nikisoma Sunday News na ‘dictionary’ (kamusi) lazima iwe pembeni.

Nilikuwa napenda sana kusoma safu za Wilson Kaigarula. Nimesoma sana ‘articles’ (makala) zake. Nasikiliza BBC English Service, nasikiliza KBC ya Kenya ya Kiin[1]gereza.

“Kama unaweza kujifunza Kisukuma bila kufundishwa darasani ni hivyohivyo, sasa nikaanza kusoma ‘noval’ (riwaya) za Sidney Sheldon, kitabu chake cha ‘The other side of midnight’.

“Sidney akanimeza, yaani ikawa mimi nasoma riwaya za Sidney mpaka nikawa naweza kukesha nasoma kitabu. Yaani sisi tulikuwa vijana wa mwanzo tukitembea na ‘noval’ mtaani. “Nikajenga utamaduni wa usomaji wa vitabu.

Sidney ndiye aliyeniathiri mimi style (mtindo) yake ya kuandika, nikawa napenda anavyoandika ‘flashback style’ anaanzia mwisho wa story, halafu anakuja kukupitisha,” anasema Shigongo.

Kufeli darasa la saba
Shigongo ambaye ni mjasiriamali na mwandishi wa habari anasema alianza darasa la kwanza mwaka 1977 Shule ya Msingi Gembe iliyopo jimbo la Solwa mkoani Shinyanga.

Baadaye anasema familia yao ilihamia mkoani Mwanza, eneo la Nyakato, ambako aliendelea darasa la pili mpaka alipohitimu elimu ya msingi.

“La saba nikafeli na wala sikushangaa kwa sababu nilikuwa sijawahi kufaulu mtihani wowote huko chini, mimi sikuwa mjinga ila mazingira niliyokulia nyumbani maskini, tumezungukwa na matajiri, kila ninakopita najiona kama fukara, hakuna mtu ananithamini, shuleni walimu wananigombeza, kwa hiyo nilikuwa nimejikatia tamaa.

“Hata wakati wa mtihani sifanyi juhudi yoyote ile, yaani kama niliwahi kupata maksi nzuri sana darasani ni asilimia 25, sijawahi kufaulu zaidi ya maksi hizo.

“Siku nilipopata asilimia 25 mwalimu alishangaa. Akaja kaka yangu mmoja akasema lazima usome, akanichukua na kunipeleka Buchosa kule tuliotoka kwenda kurudia shule.

Zamani ulikuwa unaweza kufeli halafu ukarudia.

“Nikaenda kurudia shule moja inaitwa Luhama nikasoma pale la saba nikafeli tena. Nilipofeli nikasema shule itakuwa imeshindikana hapa, la muhimu ni kufanya biashara,” anasema Shigongo.

Baadaye anasema alisikia taarifa kuhusu chuo cha uuguzi kilichopo Sikonge mkoani Tabora, akaamua kwenda kusoma kozi ya mwaka mmoja.

Alipomaliza kozi hiyo, Shigongo anasema alirudi kijijini alikoanza kufanya kazi kwenye moja ya zahanati zilizopo lakini aliokuwa akilipwa akilinganisha na umasikini uliopo kwenye familia yake akaona hautoshi kukidhi mahitaji yake, hivyo akaacha kazi.

“Mimi mshahara ule bwana ulinishinda, nikasema familia yangu ni maskini, wanalala chini na wanalala njaa, wazazi wangu wanadharauliwa na kila mtu na pale tunapokaa matajiri ni wengi wanatupa takataka kwetu kwa sababu kulikuwa na nafasi wanapafanya dampo.

“Nikasema lazima nifanye kitu, kile cheti cha nesi nilikichana nikaamua kwenda machimboni,” anasema Shigongo.

Alivyojiunga chuo kikuu

Kuhusu alivyoingia chuo kikuu ilhali yeye ni mhitimu wa darasa la saba, tena aliyefeli, Shigongo anasema hiyo ilitokana na kipaji chake cha kuandika.

“Mwaka 2017 nikasikia hiyo habari ya Recognition of Prior Learning (RPL) kutoka kwa Godwin Gondwe. Na mimi kwa wakati huo nilikuwa nimeshaandika kwa miaka mingi sana.

“Nimeandika kwa zawadi ya Mungu bila kufundishwa na mtu yeyote wala mahali popote.

Sasa nilikuwa nimeandika vitabu vingi sana, na kumiliki kampuni ya habari.

Lakini, wakati wote huo sikuwahi kusoma ‘mass communication’ mahali popote na elimu yangu ikiwa bado ni ya darasa la saba.

“Sijawahi kusoma sekondari mahali popote duniani, mtu ambaye haamini anaweza kwenda kule baraza la mitihani kama kuna mtu anaitwa Shigongo amewahi kusoma sekondari mahali popote.

“Nilipopata taarifa zile mimi nikachukua vitabu vyangu nikaenda pale TCU (Tanzania Commission for Universities) nikamkuta Profesa Mwesiga Baregu na nikaweka vitabu vyangu mezani nikamwambia vitabu vyote hivi nimeviandika mimi bila elimu rasmi, ni vitabu vyenye kurasa 500.

“Akashangaa na akaniambia hapa kwetu kuna mfumo unaitwa RPL unaweza ukafanya mtihani wewe, ukipasi unaingia kusoma shahada chuo kikuu.

“Nikaufanya ule mtihani mwaka wa kwanza nikafeli, ilikuwa 2016, mwaka 2017 nilipofanya ule mtihani nikafaulu. Nilipofaulu nikajiunga na Chuo Kikuu cha Tumaini Dar es Salaam Turdaco (Tumaini University Dar es Salaam College).

“Nikaanza kusoma shahada ya kwanza ya mawasiliano ya umma, kutoka darasa la saba kwenda chuo kikuu. Nimesoma kwa miaka mitatu. Nimemaliza pale nikiwa ‘one of the best students’ mwenye GPA ya 4.8 yaani nilipata B tatu katika muda wote niliosoma shuleni,” anasema Shigongo.

UDSM yamkataa

Shigongo anasema baada ya kumaliza shahada yake ya kwanza alitamani kusoma shahada ya uzamivu, lakini alipopeleka maombi yake Chuo Kikuu cha Dar es Salaam walimtaka apeleke cheti cha kidato cha nne ambacho hakuwa nacho.

Kiuhalisia hana kabisa cheti hicho. Anasema aliwaambia hakuwahi kusoma sekondari wakamkatalia, akaenda TCU wakamwandikia barua kwenda UDSM wakishauri Shigongo aruhusiwe kuendelea na shahada ya pili licha ya kukosa cheti hicho cha kuhitimu kidato cha nne lakini hawakukubali.

“Yaani mimi nataka nisome masters (shahada ya uzamili). Nataka nisome tu nipate elimu halafu wananiambia lete cheti cha form four, sina hicho cheti.

Nikaenda TCU wakaniandikia barua kwamba huyu mtu amefaulu vizuri, nikapeleka UDSM wakasema hawataki,” anaeleza Shigongo jinsi safari yake ya elimu ilivyokwamia UDSM anakotamani kujiunga.

Chanzo: Mwananchi
 
“Akashangaa na akaniambia hapa kwetu kuna mfumo unaitwa RPL unaweza ukafanya mtihani wewe, ukipasi unaingia kusoma shahada chuo kikuu.
CHUO ALIJIUNGA VP SASA??
Huu mfumo wautangeze zaidi hao tcu kuna darasa la7 wengi tu now ukiwaingiza chuo wanatoka na degree nzuri tu kuliko walio kwenye mfumo rasmi.

Pia vyuo vyote nchi vinapaswa kujua elimu ni kitu cha muhimu na kama mtu anataka kusoma kujiendeleza zaidi basi wampokee kwa mikono miwili na wamuelimishe ili awe msomi mzuri..

Elimu sio dhabi au sio lazima uwe na elimu ya form 4 kama hapa kwetu ndio ujulikane ulisoma isiwe hivyo wanataaluma wa vyuo vikuu mnapaswa kuja na njia tofauti tofauti ili kuhakikisha watu wengi zaidi wanapata fursa ya elimu kama wanauwezo huo.
 
24 Reactions
Reply
Back
Top Bottom