Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,476
- 39,995
Baadhi ya viongozi na hata wanachama wa kawaida wa upinzani wanapokosoa CCM wanakosoa zaidi watu na chama kama chama. Katika kikao cha Bunge kilichopita kwa mfano ni wachache sana ambao wamefanya mashambulizi ya moja kwa moja (direct assault) ya sera za CCM. Nimeanza kuwa na wasiwasi kuwa yawezekana wapo watu ambao wanaamini kuwa sera za CCM "kimsingi" ni nzuri na kuwa "ziko vitabuni" na hivyo wanaamini CCM ikibadilisha watendaji mbalimbali basi sera hizo zitaanza kutekelezeka.
Matokeo ya maono haya ni kuwa CDM inaweza isijikte sana katika kuhamasisha wananchi kuelewa sera zake na mipango yake ambayo ni 'tofauti' na ile ya CCM. Hili linaweza kuwafanya baadhi ya viongozi na wanachama kutokujali sana kuzisoma na kuelewa makosa ya msingi (fundamental errors) za sera za CCM na hivyo kuzikosoa na kupendekeza sera za CDM kuwa ni bora.
Hii inawezekana kutokea kwa sababu ama baadhi ya viongozi au mashabiki hao wa CDM hawaamini kuwa sera za CDM ni bora kuliko zile za CCM. Kwangu mimi huu ndio msingi wa mgongano unavyopaswa kuwa; kwamba tofauti zetu za kisiasa zisiwe kwa ajili ya msingi wa watu - yaani badala ya kushambulia mtu au kundi la watu ishambuliwe sera. Mfano mzuri wa kuelewa hili ni kuangalia kampeni ya urais ya Marekani ambapo watu wa Republicans hawasiti kuonesha waziwasi na kudai kuwa sera za Obama zimeshindwa katika maeneo mbalimbali huku Obama akirudia hoja ya kuwa wamarekani wasizirudie zile "sera zilizoshindwa za zamani". Iwe ni kwenye masuala ya kodi, nishati, mazingira, usalama n.k hoja ni kulinganisha sera za vyama hivyo viwili na sera zile zinazokubalika zaidi ndizo ambazo zitakipatia chama husika ushindi.
Kwa muda sasa hatujasikia ukosoaji huu wa sera za CCM mara nyingi tunasikia ukosoaji wa matokeo ya sera zenyewe bila kujali sana sera zilivyo. Kwa mfano, tatizo la nishati nchini kwa watu wengi yawezekana likaonekana ni tatizo la nani anasimamia wizara ya nishati au watendaji fulani; lakini kwa mtu yeyote anayeangalia anaweza kuona kuwa tatizo ni sera nzima ya nishati ni mbovu tangu ilipoundwa upya mwaka 1992 na mabadiliko ya baadaye. Ni sera ambayo kushindwa kwake hakuna utata kwani matokeo yanajulikana. Watu lazima waseme pasipo utata kuwa sera ya CCM ya nishati imeshindwa! Lakini sera ya CDM ni ipi?
Ukiamini kuwa tatizo ni 'watu' na siyo sera CCM na serikali itaitikia kwa kubadilisha watu na siyo sera! Matokeo yake wataingizwa watu na kutoka na matatizo yatabakia pale pale kwa sababu tatizo la msingi ni zaidi ya watu. Wapinzani (iwe CDM au wengine huru) wanapolalamikia matokeo ya sera - elimu, ajira au maji - na kutaka "serikali" ibadilishe au "ilete" mpango fulani wanafanya hivyo wakionesha kuamini kuwa wanakubaliana na sera yenyewe at least in principle! Hili ni kosa la kimkakati na ni kosa la kisiasa. Kwa sababu kama serikali ikisikiliza na kufanya mabadiliko ya juu juu wapinzani hawa wanaweza kujikuta wanatoa pongezi "kuwa serikali imetusikiliza" wakati sera ya msingi inabakia pale pale!
Lakini hatari zaidi ambayo ninaiona ni kuwa kwa kushindwa kutangaza sera mbadala za sekta mbalimbali (alternative policies) CDM kama chama kinaweza kujikuta kikijulikana zaidi kwa kufichua ufisadi, kuilaumu sserikali na kuikosoa serikali kuliko kujulikana kwa sera zake mbadala. Kwa mfano, ni wangapi wanachama wa CDM wanaojua sera za CDM kuhusu nishati, elimu, maji, ulinzi na usalama, michezo n.k? Ni wangapi kwa mfano ambao huimba na kusema "people's power" kwa furaha wanajua CDM inamtazamo gani wa kisera kuhusiana na misaada ya kigeni? Je viongozi wote wa CDM wanajua sera zao na wanaweza kuzipambanua? Katika mikutano mbalimbali ya CDM ni lini na wapi ambapo kumewahi kuwepo na mkutano wa "policy discussion" ambapo wananchi walikaa na viongozi wao kuzungumzia sera zao? Kwa mfano, wadau wa sekta ya utalii wakiuliza hivi CDM sera yenu ya utalii ni ipi nani anaweza akatoa jibu ambalo kila mwana CDM analijua?
Sasa majibu tuliyayozea ni yale yale - Sera za nini tunataka kwanza CCM watoke madarakani halafu tutazungumzia sera na kuwa sera za CDM zipo kwenye tovuti kwa mtu yeyote kujisomea! Majibu yote yana hatari ndani yake. Hatari yake ni kuwa watu wanaweza kujikuta wanajitahidi kukosoa serikali kwa nguvu sana na kukosoa matokeo ya sera za CCM kumbe wakifanya hivyo wanaonesha wanakubali moyoni uzuri wa sera za CCM na hivyo kumbe wanagombania kupata nafasi ya kuzitekeleza sera za CCM na siyo sera za CDM!
Jiulize: Kama wewe ni mwana CDM au shabiki (kama mimi) je tatizo lako na CCM ni nini hasa? Je, ni kwamba CCM imekosa watu wenye uwezo na uadilifu wa kusimamia sera zao na hivyo wawaondoe ili waitawale nchi vizuri au tatizo lako ni sera za CCM kuwa zimeshindwa na hivyo ni bora CCM wote waondoke ili hatimaye CDM ije kushika madaraka na kutekeleza sera zake ambazo yumkini ni bora kuliko za CCM? Je unaamini sera za CDM kwa kila eneo ni bora kuliko za CCM?