Je, Marekani inaogopa nini kwa kuhujumu mara kwa mara hadhi ya China kama nchi inayoendelea?

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,034
VCG41N1198668373.jpg

Baraza la Wawakilishi la Marekani hapo awali lilipitisha mswada wa sheria iliyolenga kuivua China hadhi yake ya "nchi inayoendelea". Hivi karibuni, Bunge la Marekani lilipendekeza azimio lingine la kupinga hadhi ya nchi inayoendelea ya China katika Shirika la Biashara Duniani WTO. Kwa kujibu hilo, Wizara ya Mambo ya Nje ya China ilisema kuwa China haiwezi kuvaa kofia ya "nchi iliyoendelea" ambayo Marekani inataka kuipa China.

Kwanza kabisa, iwe nchi iliyoendelea au nchi inayoendelea, mashirika ya kimataifa yana vigezo, na Marekani haina uamuzi wa mwisho. Kulingana na vigezo vipya vya Benki ya Dunia, nchi yenye pato la taifa kwa mtu mmoja mmoja la zaidi ya dola za Kimarekani elfu 13 inaorodheshwa kama nchi yenye kipato cha juu. Mwaka 2022, Pato la Taifa la China kwa mtu mmoja mmoja lilikuwa dola 12,700, ni juu kidogo ya wastani wa kiwango hicho duniani, moja ya tano ya kiwango hicho cha nchi zilizoendelea, na moja ya sita ya kile cha Marekani. Uchumi mkubwa lakini pato dogo la taifa kwa mtu mmoja mmoja daima ni sifa kuu ya China kama nchi yenye idadi kubwa ya watu. Kama alivyosema Keith Rockwell, aliyekuwa msemaji wa WTO kwa karibu miaka 30, kwamba "China sio tu ina miji ya kisasa kama vile Beijing, Shanghai, na Guangzhou, lakini pia kuna maeneo ya magharibi ambayo yamejikwamua kwenye lindi la umaskini uliokithiri hivi majuzi tu ."

Hii si mara ya kwanza kwa Marekani kujaribu kudhoofisha hadhi ya China ya "nchi inayoendelea". Ili kuhalalisha kushindwa kwa "vita vya kibiashara dhidi ya China", serikali iliyopita ya Marekani iliyoongozwa na Donald Trump iliiomba mara kwa mara WTO kufuta hadhi ya China ya "nchi inayoendelea". Kwa maneno ya Trump mwenyewe: Kama nchi inayoendelea, China imepata manufaa mengi ambayo Marekani haina. Lakini hali halisi ni kuwa, China haijawahi kutumia hadhi hiyo kama sababu yake ya kukwepa majukumu ya kimataifa. Kinyume chake, katika suala la kukuza amani na maendeleo ya dunia, mchango wa China unazidi kwa mbali ule unaostahiki kwa nchi zinazoendelea, na hata kuzidi nchi zilizoendelea.

Kwa mujibu wa Benki ya Dunia, kuanzia mwaka 2013 hadi 2021, wastani wa kiwango cha mchango wa China katika ukuaji wa uchumi wa dunia ulikuwa 38.6%, juu ya jumla ya mchango uliotolewa na kundi la G7. Tangu sera ya mageuzi na ufunguaji mlango ianze kutekelezwa, watu milioni 770 nchini China wameondokana na umaskini, na kuchangia katika kupunguza umaskini duniani kwa zaidi ya 70%, na kufikia lengo la Umoja wa Mataifa la kupunguza umaskini mwaka 2030 miaka 10 kabla ya muda uliopangwa. China pia ni nchi ya pili kwa mchango mkubwa katika Umoja wa Mataifa, na ya pili kwa mchango mkubwa katika shughuli za kulinda amani. Aidha, pendekezo la "Ukanda Mmoja, Njia Moja" na "Mipango Mitatu Duniani" iliyotolewa na China yote inalenga kukuza ushirikiano wa kimataifa na kujenga jumuiya ya binadamu yenye mustakabali wa pamoja. Hii kimsingi ni tofauti na Marekani, nchi iliyoendelea ambayo inachukulia maslahi ya nchi nyingine kuwa si kitu na kutoa vitisho na vikwazo.

Mara kwa mara Marekani imeunda mtego wa kauli ya "China si nchi inayoendelea". Kwanza, kuiondoa China kwenye kundi la nchi zinazoendelea kutaongeza gharama za kujitafutia maendeleo za China na kuifanya nchi hiyo kubeba majukumu zaidi ya uwezo wake. Pili, inaweza pia kuharibu uhusiano kati ya China na nchi zinazoendelea, na kuifanya China kuwa "ya kipekee", na tatu, pia itakandamiza kasi ya ongezeko la ushawishi wa jumla wa nchi zinazoendelea, na kudumisha utawala wa Marekani. China haikubaliani na njama kama hiyo, na hata nchi nyingine zinazoendelea pia hazitakubali.
 
Back
Top Bottom