Zinduna
JF-Expert Member
- Nov 6, 2011
- 2,378
- 3,379
Katika makuzi yangu kama binti wa Kiafrika nimefunzwa mambo mengi kuhusu maisha na wajibu wangu kama mtoto wa kike.
Baada ya kuvunja ungo nilianza kuandaliwa kuwa mke mtarajiwa wa mwanaume nisiyemfahamu.
Nimefunzwa kupika, nimefunzwa usafi wangu wa mwili, nimefunzwa usafi wa nyumba, nimefunzwa kuvumilia maisha ya ndoa na nikaaminishwa kwamba mwanaume ndiye kichwa cha nyumba na nikafunzwa wajibu wangu katika kumtumikia, lakini pia nikafunzwa kupanga bajeti na kuweka akiba ili huyu mume ambaye ni kichwa cha nyumba akikwama kupata mkate wa kila siku kwa ajili ya familia niweze kumsaidia.
Kwa kifupi ni kwamba nilifunzwa mambo mengi lakini yote hayo yakiniaminisha kwamba siku isiyo na jina lazima nitaolewa na kuwa chini ya mwanaume ambaye atakuwa ndiye kila kitu kwangu.
Nakumbuka wakati fulani baada ya mama kuona mabinti ambao nalingana nao umri na wengine nikiwa nimewazidi umri wakiolewa pale mtaani mama alianza kunidodosa kama sijapata mtu kama wenzangu.
Lakini pia alijaribu kutumia misamiati mbalimbali na mafumbo lakini nilielewa kwamba alikuwa anamaanisha nisiwe mgumu sana kwa wanaume kwani sijui aliyevutiwa na mimi na anayetaka kunioa.
Nadhani alikuwa anataka kufikisha ujumbe kuwa umri unasonga na wenzangu wanaolewambona miye sisomeki?
Naamini si mimi peke yangu, ninayekabiliana na changamoto hizi za wazazi na jamii kwa ujumla.
Ukweli ni kwamba malezi ya mtoto wa kike yanamuandaa kuwa mke wa mtu, yanamuandaa kuolewa na yanamuaminisha kwamba ndoa ndiyo kila kitu.
Kwa nini nasema hivyo?
Ni kwa sababu kuna baadhi ya watu wanawaona wanawake wasioolewa kama vile wana kasoro au hawana thamani ukilinganisha na wale walioolewa na hii imetokana na jamii kuwapa heshima zaidi wanawake walioolewa na kuwadharau wanawake wasioolewa.
Si hivyo tu, lakini pia ndugu, marafiki na jamii huweza kumsakama mwanamke ambaye hajaolewa kwa maswali lukuki na hivyo kumjengea picha kuwa kutoolewa ni tatizo na hivyo kumfanya ajitilie mashaka na kushusha kiwango chake cha kujiamini. Jambo hili linawakwaza wanawake wengi amboa hawajapata waume wa kuolewa nao na kuyaona maisha bila kuolewa kama vile ni nuksi na wana kasoro. Hata hivyo pamoja na mtoto wa kike kufunzwa namna ya kuishi na mume na mafundisho mengine ya ndoa katika makuzi yake lakini hiyo haimhakikishii kwamba ni lazima atakapofikisha umri wa kuolewa, ataolewa.
Hivi wazazi wanapomuandaa mtoto wa kike kwa mafundisho ya ndoa unatarajia binti ambaye amefikisha umri wa kuolewa kwa mujibu wa jamii halafu akawa hajaolewa ataishi akiwa na furaha na amani moyoni?
Nadhani kuna haja ya ndugu, marafiki na jamii kwa ujumla kubadili mfumo wa malezi kwa watoto wa kike kuhusiana na swala zima la ndoa kwamba hata wasipoolewa haimaanishi kwamba wana kasoro ili ikitokea hawajapata wanaume wa kuwaoa waendelee kuyafurahia maisha wakiwa single na siyo kujuta na kuumia moyoni kwa kujihisi kama wana kasoro. Naamini wengi tunajua ni jinsi gani wanaume siku hizi walivyo wagumu kuoa na mazoea yametufundisha kwamba mwanamke ni wa kusubiri hadi atakapojitokeza mwanaume wa kumposa.
Nini kifanyike?
Kwanza jamii inapaswa kuzungumzia maisha ya kutoolewa au kuolewa kwa namna ambayo haitaathiri mitizamo ya watoto wa kike kwamba kuolewa ni ukamilifu kwa mtoto wa kike na kutoolewa ni nuksi na dalili kwamba mwanamke huyo ana kasoro au hana thamani. Tatizo ni kwamba wapo baadhi ya wanawake huzungumzia swala la kuolewa kwa namna ambayo inamfanya mtoto wa kike aone kama vile kutoolewa ni nuksi kabisa jambo ambalo si kweli.
Wanajenga dhana kwa mtoto wa kike kwamba haweza kuwa na furaha na amani kama hataolewa. Iwapo wanawake watajifunza na kuona kuna furaha na amani katika maisha ya aina yoyote, yaani maisha ya kuwa single na maisha ya ndoa naamini hakutakuwa na presha kwa wasichana wasioolewa kulazimisha kuolewa kwa namna yoyote hata kama hawajawapata wanaume wa ndoto zao.
Pili bibi zetu wanapaswa kubadilika na kuwafunza watoto wa kike watambue kwamba hata kama wasipoolewa thamani yao iko pale pale kama mwanamke na wanapaswa kuishi kwa furaha na amani na kujiamini kwa sababu hawana kasoro na furaha iko ndani mwao na si lazima ipateikane kwa kuolewa.
Mwisho wanawake wasioolewa wanapaswa wawe mfano kwa kuishi kwa kujiamini na kuyafurahia maisha na waache kulalamika kwa sababu wako single. Najua jambo hilo litakuwa gumu kwao kulikubali kwa sababu katika makuzi yao hawakupata kufundishwa kukubaliana na hali hiyo ya kuwa single na kuishi maisha ya furana na amani.