Jambazi lauawa Zanzibar katika mapambano na polisi

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
Mtu mmoja anayesadikiwa kuwa ni jambazi, ameuawa katika mapambano na polisi baada ya majambazi kadhaa kuvamia hoteli ya kitalii ya Samaki Lodge eneo la Uroa Kusini, Zanzibar.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kusini Unguja, Augustino Ollomi, aliiambia Nipashe kuwa katika tukio hilo, pia polisi wawili walijeruhiwa.
Alisema tukio hilo lilitokea saa 7:00 usiku baada ya watu wanne wanaosadikiwa kuwa ni majambazi kuvamia hoteli hiyo muda mfupi baada ya kufungwa na watalii kuingia kwenye vyumba vyao.
Alimtaja alieuawa kuwa ni Hassan Mohamed Abdallah, (44), ambaye alikufa baada ya kupigwa rungu kichwani na mlinzi wa Kimasai.
Alisema jambazi huyo alikufa njiani wakati akikimbizwa hospitali ya Mnazi Mmoja ambapo katika tukio hilo askari wawili walijeruhiwa mmoja kichwani na mwingine mkononi.
Alimtaja askari aliyejeruhiwa kichwani ni C 8539 Koplo Mohamed Salum ambaye alijeruhiwa sehemu ya kichwani na shingo na anaendelea vizuri pamoja na Kamanda wa Polisi wa Wilaya ya kati Unguja, ASP Juma Sadi ambae alijeruhiwa mkononi baada ya kukatwa na kiwembe katika mapigano hayo na askari walilazimika kufyatua risasi katika kupambana na majambazi hayo.
Akielezea tukio hilo, alisema majambazi hao walivunja mlango mkubwa wa hoteli na kumvamia mmiliki wa wake aliyefahamika kwa jina moja la Fabian. raia wa Italia.
Hata hivyo, alisema mwekezaji huyo alipambana na majambazi kabla ya kupata msaada kutoka kwa Polisi waliokuwa doria katika eneo hilo.
Alisema wakati askari wakisonga mbele kupambana na majambazi hao, wawili kati yao walikimbilia kichakani lakini jambazi mmoja marehemu Ny’ambo alimvamia askari Koplo Mohamed akitaka kumpokonya silaha kabla ya mlinzi wa Kimasai kutokea na kumpiga rungu kichwani na kupoteza fahamu.
Alisema kwamba katika mapambano hayo, polisi walifanikiwa kumkamata jambazi mmoja Abdalla Juma Faki (45,) mkazi wa Mwembemakumbi aliyelazwa katika Hospitali ya Mnazi Mmoja baada ya kujeruiwa na wananchi wenye hasira.
Kamanda Ollomi alisema polisi wanaendelea na msako wa kuwatafuta majambazi wawili waliokimbilia msituni na kutelekeza mabegi mawili na kompyuta aina ya Laptop moja.
Hata hivyo alisema kwamba majambazi hao hawakufanikiwa kuiba fedha au vitu baada ya muwekezaji huyo kugoma kutii amri na kuanza kupambana na majambazi hao kabla ya kupata msaada toka kwa walinzi wa kimasaai wakiwa gholofa ya kwanza ya hoteli hiyo.
Kamanda huyo alisema marehemu Ny’ambo alikuwa ni jambazi sugu kwa vile amewahi kufikishwa mahakamani kwa kesi mbalimbali za kuhusika na wizi wa kutumia silaha.
 
Back
Top Bottom