Jaji Werema na suala la kujiuzulu kwake kwa kukataa katiba mpya.

Lokissa

JF-Expert Member
Nov 20, 2010
7,446
2,490
Jaji Werema sijiuzulu kwa Dowans, Katiba Send to a friend
werema.jpg
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema

SIKU moja baada ya wadau mbalimbali kumshukia Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema na kumtaka ajiuzulu kwa kauli zake kuhusu Katiba na Dowans, Mwanasheria huyo wa Serikali, ameibuka na kusema "Sijiuzulu ng'o."

Werema aliliambia gazeti hili jana akiwa likizoni kijijini kwake mkoani Mara kuwa hawezi kujiuzulu kwa shinikizo la watu kuhusu kauli hizo kwa kuwa anajua anachofanya katika wadhifa wake.

''Wanaotaka nijiuzulu ni wale wasiofikiria, kwani kila mtu ana nafasi yake ya kuongea kuhusu katiba. Mimi nimetoa mawazo yangu na wengine wakitaka watoe ya kwao," alisema Jaji Werema.

Aliendelea, ''Kunitaka nijiuzulu ni fikra za kichanga sana na potofu. Mtu mwenye upeo mpana hawezi kusema Mwanasheria Mkuu ajiuzulu kwa hili,"alisema.


Baadhi ya watu waliomshinikiza Jaji Werema ajiuzulu ni Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa na Naibu wake, Zitto Kabwe, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha St Agustine, Profesa Mwesiga Baregu, Mwanasheria maarufu nchini, Profesa Abdallah Safari na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Benson Bana.

Wengine ni Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila, Mahadhari wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Bashiru Ally, Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chadema, Erasto Tumbo na Mkurugenzi wa Shirika lisilokuwa la Kiserikali la Agenda Participation 2000, Joseph Ulaba.

Mbali na kugoma kujiuzulu, Werema alivilaumu vyombo vya habari kwa kile alichoeleza kuwa vimemnukuu vibaya kuhusu suala la katiba akidai kuwa yeye alichosema ni katiba kufanyiwa marekebisho kwa kuongeza au kupunguza vitu fulani na siyo kuwekewa viraka.

"Ninyi waandishi pia mnachangia kuvurugu mambo, mmenikoti (mmeninukuu) vibaya. Mimi nilisema katiba ifanyiwe marekebisho, lakini, ninyi mkaeleza kuwa nimesema iwekewe viraka. Haya basi tukubaliane marekebisho, ndio viraka," alisema Jaji Werema.

Akiwa Ikulu kwenye hafla ya kuapishwa Jaji Mkuu mpya, Mohamed Othman Chande Desemba 27 mwaka huu, Werema alisema, “Kuandika Katiba mpya hapana, lakini kufanya marekebisho kwa kuondoa au kuongeza mambo fulani kwenye katiba, ruksa.”

"Suala la kubadilisha ibara zinazoonekana kutokidhi haja na kuingiza mambo mapya kwenye katiba, linakubalika na kwamba hayo yamekuwa yakifanyika." alisisitiza Jaji Werema na kutolea mfano mabadiliko ya katiba yaliyoruhusu kuingizwa kwa haki za binadamu.
Hata hivyo, alisema maoni ya watu yanayotolewa kuhusu katiba mpya ni sahihi kwani kila Mtanzania ana haki ya kutoa maoni yake kwa mujibu wa katiba iliyopo.
“Raha yangu ni kuona Watanzania tunajadili suala hili maana kila mtu ana haki ya kusema na ni sahihi, lakini, tunatofautiana tu kama kila maoni ni sawa,” alisema Jaji Werema na kuongeza:
“Lakini si kila mtu analolisema lifuatwe. Tukisema kila mtu anachokisema tukifuate haitakuwa sawa. Kwa mfano mimi kule kwetu wafugaji nao watataka mambo ya ng’ombe wao yaingizwe kwenye katiba, na Wahaya pia wanaweza kusema tuingize kwenye katiba ndizi zao, hii si sawa;” alisisitiza Jaji Werema.

Werema alitoa kauli hiyo akipingana na viongozi kadhaa nchini akiwamo Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa, mawaziri wakuu wa zamani, Joseph Warioba na Frederick Sumaye na Jaji Mkuu Mstaafu Augustino Ramadhani ambao wametaka katiba mpya.

Madai ya Katiba mpya pia yamewahi kutolewa na Msajili wa Vyama vya Siasa Nchini, John Tendwa ambaye alisema bayana kuwa katiba mpya iandikwe mapema kabla ya mambo kuwa mabaya, akitoa mfano wa mapungufu ya katiba ya sasa kuwa ni Rais kupewa madaraka makubwa.

Hata hivyo, msimamo wa mwanasheria huyo wa serikali umekuja wakati tayari Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akiwa ameshaweka wazi nia ya kuyafanyia kazi madai hayo yaliyoanzishwa na Chadema na kuungwa mkono na watu wa kada mbalimbali.

Kuhusu suala la Dowans, Werema alisema hana hatia ya kumfanya ajiuzulu kwani ametoa kauli ya Tanzania kutakiwa kuilipa kampuni hiyo, kisheria zaidi.

Alirudia kauli yake kuwa kuhusu Dowans, mjadala umefungwa, hakuna cha kujadili tena na kwamba wanaomtaka ajiuzulu kwa sababu ya kauli hiyo, hawalifahamu vizuri suala hilo.

"Nasema hapo lilipofikia (suala la Dowans), hakuna namna ya kulikwepa," alisisitiza Jaji Werema jana na kuongeza:

"Mimi nipo kijijini sasa hivi lakini, kwa kweli kwa hili la mimi kutakiwa kujiuzulu kwa sababu ya kufunga mjadala wa Dowans au kusema katiba iwekewe viraka, sioni kama kuna sababu za msingi."

Msimamo wa Jaji Werema wa kuilipa kampuni ya kufua umeme ya Dowans Tanzania Ltd fidia ya Sh185 bilioni na kutaka katiba ifanyiwe marekebisho badala ya kuandikwa upya, uliwakera wasomi, wanasiasa na wanaharakati ambao kwa pamoja, walimtaka akae kimya kwa kuwa hana mamlaka ya kuwaamulia Watanzania mambo yao.

Wadau hao walisema, kuwa mwanasheria Mkuu wa Serikali, Werema hana mamlaka kisheria kuwaamulia Watanzania mambo yao zaidi ya kuishauri Serikali kuhusu mambo ya kisheria na hasa mikataba, kazi ambayo walieleza pia kuwa imeonekana kumshinda.

Walisema Jaji Werema hana mamlaka ya kutangaza kufungwa kwa mjadala wa Dowans na Katiba vinginevyo aseme nani kampa madaraka hayo au ana maslahi gani na masuala hayo.

Ulipaji wa fidia hiyo unafuatia uamuzi uliotolewa na Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Migogoro ya Biashara (ICC Court), Novemba 15, mwaka huu chini ya Mwenyekiti Gerald Aksen na wasuluhishi Swithin Munyantwali, Jonathan Parker ukiamuru Tanesco iilipe Dowans kiasi hicho cha fedha.

WANAJAMII MWASEMAJE KUHUSU MATAMSHI YA HUYU BWANA.JE ANATUFAA WKT HUU WANANCHI TUKIWA NA KILIO CHA KATIBA MPYA? AU NDO KATI YA MAJAJI WALIOKUWA WACHELEWESHAJI WAKUBWA WA KESI MAHAKAMANI?
 
Back
Top Bottom