JamiiTalks Interview with Maxence Melo: The story of JamiiForums - history and operations of the platform

JamiiForums

Official JF Response
Nov 9, 2006
6,200
4,984
Habari za wakati huu mabibi na mabwana, waungwana wote kwa ujumla, wale tulio kwenye mfungo, hongereni kwa hilo na natanguliza kheri na salamu za sikukuu ya Idi.

Itakumbukwa kuwa Jumanne ya tarehe 14/08/2012 ilianzishwa hoja na Roulette na kukaribishwa maswali kwa ajili ya kumuhoji Maxence Melo juu ya JamiiForums kwa ujumla na safari hii ya miaka 6 toka kuanzishwa kwake (Link to Roulette's thread). Ikumbukwe kuwa JamiiForums imekuwa maarufu nchini Tanzania, kitu ambacho kinaipa changamoto za kutosha. ni namna gani changamoto hizi zinashughulikiwa kutuhakikishia, sio tu ustawi; bali na uwepo wa JF katika siku za usoni.


539a26f4-2144-4189-8a3b-62a21ff4419f.jpeg
Maxence M. Melo
Tulipokea maswali mengi. Mengine yakiwa marudio (Link to the latest interview of Maxence Melo). Tumejitahidi kuyaweka kwenye mtiririko muafaka kwa ajili ya kuokoa muda na kutengeneza picha halisi. Maxence Melo yupo hapa kuyajibu. Kamata kahawa yako, ama kinywaji chako baridi and stay tuned.
 
Swali #1:
Maxence Melo kwa ufupi tuambie Maxence Melo ni nani?
Mimi ni Mtanzania, mzaliwa wa Mkoa wa Kagera, kijiji cha Kantare katika Wilaya Nkenge.

Nimesoma Shule ya Msingi Kantare, sekondari nilikuwa Shule ya Wavulana Bwiru (Mwanza), na baadae nikajiunga Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) nikajiunga na mafunzo ya Ufundi Mchundo (FTC) kisha kuchukua masomo ya uhandisi hapohapo DIT (B.Eng).

Nimezaliwa mwaka 1976 mwezi Mei. Nina mke na watoto watatu, mmoja wa kike na wawili wa kiume.

Nadhani kwa kifupi nimejibu (walau) swali lako

EDIT: Kwa sasa nina watoto 3 si wawili tena baada ya kupata mtoto mwingine 2014
 
Asante kwa majibu fasaha Max.

Swali #2:

Kwa kiasi kikubwa kwa wale ambao ni watumiaji wa Jamii Fourms tunafahamu kuwa Maxence Melo na Mike Mckee ni waanzilishi wa Jamii Forums. Tunaomba kutambua yafuatayo:-

A) Jamii Forums ilianzishwa lini? Na kwanini ikaitwa Jamii Forums na si jina lingine?
Ni kitu gani kiliotesha mbegu ya kuanzisha Jamii Forums? Kwa maneno mengine; Nini Malengo na makusudio ya kuanzisha Jamii Forums? Ni mkakati uliokuwa umepangwa muda mrefu ama ilitokea tu siku moja hao mkakurupuka na kuamua kuanzisha Jamii Forums?

B) Matumizi ya JF unaona yana kidhi matakwa ya watumiaji?

C) Kwa mtazamo wako unaona kuwa JF inatumika ipasavo na washiriki (members) wake?

Naomba utoe maelezo ya jibu lako kama unakubaliana ama kukataliana na hili.
 
Asante kwa majibu fasaha Max.
Shukrani.
Swali #2:

Kwa kiasi kikubwa kwa wale ambao ni watumiaji wa Jamii Fourms tunafahamu kuwa Maxence Melo na Mike Mckee ni waanzilishi wa Jamii Forums. Tunaomba kutambua yafuatayo:-
Shukrani, naam:

A) Jamii Forums ilianzishwa lini? Na kwanini ikaitwa Jamii Forums na si jina lingine?
JamiiForums (jina) limeanza Mei 2008 lakini JamboForums (jina) lilianza mwaka 2006 Machi.

Kimsingi, historia ya JF (aidha iitwe JamiiForums au JamboForums) iko hivi:

JF imeanza mwaka 2006 mwezi Machi, ni baada ya kuwa tuna majukwaa mbalimbali kama Uchaguzi Tanzania, Tanzania Economic Forum, Habari Tanzania, Jambo Network, Jambo Radio na Jambo Videos.

Mkusanyiko wa majukwaa haya ulipelekea kuwa na kusanyiko moja ambalo kwa wakati huo (2006) tuliamua kuliita JamboForums.com, jina ambalo tulilitumia hadi mwezi Mei 2008 lakini ikatupelekea kubadilisha jina kwenda JamiiForums kutokana na mgongano wa matumizi ya jina la JamboForums ambapo tulikuwa hatujachukua copyrights (haki miliki) za jina ingawa baadaye tulifanikiwa kulimiliki kihalali. Hatukutaka kusimamisha moja kwa moja matumizi ya JF hivyo tukafikiria jina mbadala la JamboForums na kubaini kuwa tayari hili kusanyiko la wadau ni kusanyiko la Jamii, na bado Jamii ilikuwa ikiendelea kutunza JF kama wengi wanavyopenda kufupisha.

Ni kitu gani kiliotesha mbegu ya kuanzisha Jamii Forums? Kwa maneno mengine; Nini Malengo na makusudio ya kuanzisha Jamii Forums? Ni mkakati uliokuwa umepangwa muda mrefu ama ilitokea tu siku moja hao mkakurupuka na kuamua kuanzisha Jamii Forums?
Ukiangalia majibu yangu ya awali unaweza kubaini kuwa tulikuwa na tovuti nyingi zenye wadau wa sekta tofauti au wenye mapenzi na vitu tofautitofauti lakini usimamizi ulizidi kuwa mgumu. Kila tovuti tulikuwa na malengo tofauti lakini yote yakilenga kuwahudumia watu wa nyanja husika kuweza kupata sehemu ya kusemea au kubadilishana mawazo.

Lengo kuu la JF likawa ni kuanzisha Jamvi moja ambapo wadau (nisisitize, sijasema watanzania) watakutana na kubadilishana mawazo huku wakikubali kutokubaliana (utofauti wa mawazo) na kujenga mijadala endelevu. Katika Jambo Network (JamboNetwork.com) au JamboRadio.com mijadala ilikuwa kwa mtindo wa chat ambapo hakukuwa na kumbukumbu (archive) baada ya mjadala, hii ilipelekea mijadala mingi kuwa inarudiwa na kusababisha kukosa mwelekeo kabisa.

Lengo letu kubwa lilikuwa ni kuwafikia wazungumzaji wa kiswahili wa eneo la Maziwa Makuu na hata watumiaji wengi wa Kiingereza lakini wenye kupenda kujua habari za ukanda huu.

Sasa, waweza kuona kama aidha tulikurupuka au kulikuwa na mchakato wa muda mrefu kufikia tulipofikia hadi kuanzisha JamboForums (JamiiForums kwa sasa).

Lakini, yote tisa - wanaostahili heshima na umiliki ni wadau wa JamiiForums na si waanzilishi wake. Wanachama wamekuwa ni chachu ya uwepo wa jukwaa na kusema kweli tunapata mafunzo mengi kwa changamoto wanazotoa kwetu. Imetusaidia sana kufanya maboresho kila mara na kujifunza jinsi ya kuwahudumia. Ni wengi wanaweza kutengeneza tovuti (websites) kama hii; lakini wachache wanaoweza kusimamia tovuti kama hii iendelee kusimamia kile kilichoianzisha na hata kubadilika kwa kadiri teknolojia inavyobadilika na watumiaji wake wanavyobadilika.

B) Matumizi ya JF unaona yana kidhi matakwa ya watumiaji?
Kwa kiwango flani yanakidhi haja ya watumiaji lakini pia kwa kiwango flani upande wa waanzilishi bado tunaona mapungufu mengi, yanafanyiwa kazi na huenda ningeulizwa swali hili ndani ya siku 90 zijazo lingeulizwa kwa mtindo tofauti na huu.

Dhamira ya kuifanya JF iwe bora zaidi ya ilivyo ipo. Tutaongeza ukubwa wa timu inayosimamia maudhui na kutoa mafunzo ya namna ya kusimamia content katika JF. Aidha, tutaongeza umakini zaidi katika kusikiliza maoni ya wadau na kuyafanyia kazi.
C) Kwa mtazamo wako unaona kuwa JF inatumika ipasavo na washiriki (members) wake?
Naam, wanachama wetu wanajitahidi sana kwa namna wanavyosaidiwa na wahariri wetu (moderators), wasimamizi wa ubora wa maudhui (content quality controllers) na wasimamizi wa majukwaa (content managers) kuitumia vema JF lakini bado asilimia kubwa ya watumiaji hawaitumii inavyotakiwa kutumiwa; tunaelewa kuwa huenda wengine ni kwa makusudi lakini walio wengi ni wazi ni kwa kutokujua au kuingia JF wakiwa na mitizamo flani (huenda ya kusikia toka kwa waliowaalika kuja JF au vinginevyo) hivyo kuitumia JF tofauti na tunavyotarajia itumike.

Wanachama wa JF walio wengi nawapongeza kwa kuwa mstari wa mbele kuhakikisha JF inabakia sehemu salama na nzuri kwa mijadala yenye tija kwao na kwa jamii inayoitumia JF. Wengi husema "JF wanajifanya wasomi" lakini sidhani kuna mwanachama wa JF amewahi kujigamba kuwa "SISI NI WASOMI WA JF". Ni kuwa mijadala iliyopo humu humfanya anayeingia hapa kuhisi amefika kwa wasomi. Anakuwa hajakosea, takwimu zetu (demographics) zinaonyesha kuwa asilimia kubwa ya watumiaji wa JF ni wahitimu wa walau kidato cha sita na wengi ni kuanzia miaka 25 na kuendelea.

Naomba utoe maelezo ya jibu lako kama unakubaliana ama kukataliana na hili.
Nadhani kifupi nitakuwa nimeeleweka hapo vema, lakini bado tuna nafasi ya kubadilika na sisi kama waendeshaji tunafahamu wapi penye upungufu na tunaufanyia kazi. Karibuni (nimeahidi ndani ya siku 90) yataonekana mabadiliko ambayo ni wazi yanaweza kuwasaidia wengi kupata urahisi wa kuitumia JF na hata kujiepusha na kufungiwa (ban) kusikokuwa na sababu.

Kwa pamoja, (sisi na wanachama) tukiamua tunaweza kuhakikisha JF inaendelea kuwa sehemu ya mijadala anuai na yenye kufikirisha.
 
Dear members,

Due to some technical problems beyond their capacity, both Maxence Melo and King'asti cannot participate in this interview in an interactive manner. We therefore postpone the interview to Monday the 20th, at 11:00 AM.

Thanks for your understanding.

In the mean time, we continue to receive questions in this thread: JF Focus: Side Comments: Exclusive Interview with JamiiForums founder - Maxence Melo

Nashukuru kwa uelewa wenu; kuna tatizo la umeme maeneo mengi ya Dar. Nami nimeathiriwa na kukatikiwa umeme, hata hivyo nahisi hata mwongoza mjadala naye atakuwa kaathirika kwa namna moja ama nyingine. Kushiriki kikamilifu ni vema kutumia tarakirishi (computer) badala ya simu au tablets.

Naahidi kuendelea kujibu maswali (ikiwezekana yote) hiyo Jumatatu.

Shukrani
 
Habari wana JF,

Nafurahi kuwepo mahala hapa; Nafurahi zaidi kuweza pata hii nafasi ya kumhoji mmoja wa JF Founders - Maxence Melo kwa maswali kadhaa katika nyanja mbali mbali. Nimearifiwa na kupewa feedback ya swala zima lilipoanzia na kuishia pia. Naomba nimshukuru na King'asti pia kwa kwa hapo alipoanzia hadi hapa alipoishia; iliyopelekea mwanzo mzuri wa majadala, ambao kwa leo mimi pamoja na mhojiwa tunatumai tutafika mahala fulani mbali na hapa.

Nikiwa kama mwendesha mpya wa huu mjadala, naomba kwa niaba ya waandaaji na wote na washriki walioweza kufanikisha hili nitoe SAMAHANI na POLE ya usumbufu wote kwa members uliotokea kwa kuahirisha kila mara. Tunaomba ushirikiano wenu wana JF kwa kutusoma na kuendelea kutoa hoja /maswali na comments katika thread ya pembeni pale Jukwaa la Siasa iliyopostiwa na Fang.

Pamoja saana.
 
Swali # 3

Katika Uzi ulioandaliwa kukusanya maswali toka kwa wajumbe wa Jamii Forums kumekuwa na pongezi nyingi sana juu ya uwepo wa hii Forum na namna ambavo ni msaada wa taarifa toka Nyanja mbali mbali kwa wengi wanaoutumia, swala ambalo tunaamini linatia faraja. Hata hivyo kuna upande wa pili wa shilling wa lawama za hapa na pale toka kwa washiriki wachache ambao ni wazoefu na wapo kwa kitambo hapa. Unajibu vipi hizo lawama kwa kuzingatia mpangilio huu ufuatao:

A]. Sasa hivi kumekuwa na wimbi la washiriki wengi JF ambao wamekuwa wakivamia kwa kasi kwa tabia za ambazo ni hatarishi kwa hadhi ya JF. Kama vile uandishi ambao ni maarufu kutumika kwa njia ya text message, vi thread visivo vya msingi (member anafungua thread kwa kimstari kimoja bila maelezo kama kakurupuka tu) n.k. Mmejipanga vipi kuepusha huu uvamizi/mabadiliko ambayo yanaweza shusha hadhi ya JF?

B]. Kukua kwa JF kutakuwa kumesababisha challenges nyingi upande wa wanachama wachache wa kitambo; kwa mfano naomba ninukuu "JF used to be more of 'WIKILEAKS' kind of, and over the years, I have observed JF undergoing complete 'metamorphosis' into some form of a SOCIAL MEDIA". Unakubaliana na hizi tuhuma baridi dhidi ya JF?
ZINGATIA: Baada ya kutoa maelezo yako kama wakubali ama wakataa, tafadhali toa maoni yako ya jinsi uionavo JF ilipo kwa upande wa kutoa habari na kama ilivo sasa inakuridhisha.​

C]. Ni kwa kiasi gani msemo wa mahala penye uhuru wa kuongea (where you dare express openly) inazingatiwa katika Jamii Forums?

D]. Kuna madai toka kwa members baadhi kuwa kuna habari nyeti zinaletwa hapa jamvini lakini ndani ya muda mfupi zinafutwa bila maelezo ya kutosha; inayowatia mashaka baadhi ya hao members; unasemaje kuhusu hili?
 
Kimsingi swali hili ni zaidi ya 1 lakini nitalijibu kwa namna hii:

Hata hivyo kuna upande wa pili wa shilling wa lawama za hapa na pale toka kwa washiriki wachache ambao ni wazoefu na wapo kwa kitambo hapa.
Nikiulizwa kuhusiana na 'wazoefu wa JF' binafsi naweza kuwataja walau 100 (ninaowakumbuka kichwani) ambao ni 'active' (wapo mpaka sasa) hapa JF na tumekuwa nao tangu 2006 hadi 2009; hawa ndio naweza kusema kuwa ni JF haswa; wao wanaweza kumjibu mtu na huyo anayejibiwa akahisi huenda hao ni moderators; hawa wameona mabadiliko kadhaa ndani ya JF, ya kufurahisha na ya kusikitisha; baadhi ni hawa:
Abdulhalim, Mkandara, Kibunango, Mzee Mwanakijiji, Sikonge, Ibrah, MgonjwaUkimwi, Ogah, Kiranga, Zitto, Alpha, Lunyungu, Halisi, Shadow, Mchambuzi, JokaKuu, Mpita Njia, Gembe, Kakalende, SMU, Bongolander, Questt, Ngambo Ngali, Chamoto, The Boss, jmushi1, Semilong, Kang, Nyambala, KiuyaJibu, PakaJimmy, Zogwale, Kinyau, Saharavoice, Amoeba, Ndahani, Mfamaji, MAMMAMIA, Mwazange, Crashwise, zomba, Bujibuji, Nyani Ngabu, Mpenda Kwao, BAK, Binti Maringo, Nyamgluu, Steve Dii, Desidii, Mdondoaji, Mvina, Kivumah, Power to the People, Kisusi Mohammed, Msanii, Mafuchila, FirstLady1, Fixed Point, Mbogela, Balantanda, Pretty, TANMO, Riwa, Hofstede, Nemesis, Kaa la Moto, Remmy, MamaParoko, Mama Joe, simplemind, AmaniGK, Buchanan, Bramo, Gbollin, MwanajamiiOne, Masaki, Bubu Msemaovyo, Freetown, Amina Thomas, Choveki, MwanaFalsafa1, TIMING, X-PASTER, BelindaJacob, Saikosisi, MziziMkavu, Injinia, Original Pastor, Preta, Zion Daughter, Chamoto, NGULI, vivian, rmashauri, Susuviri, MwanaHaki, Masanilo, Yegomasika, Belo, Mahesabu, Kaizer, Gaijin, King'asti, MpigaKelele, Mag3, Nicholas, Mlalahoi nk

Hawa, wanaweza kuielezea JF wanavyoifahamu; imepitia kipindi gani; imekumbana na 'challenges' gani na wao wanaona wapi pana kasoro na wameshiriki vipi katika kuhakikisha inaboreshwa.

Malalamiko hayawezi kuisha lakini vema tukatoa ufafanuzi kama ambavyo umeniuliza:

Unajibu vipi hizo lawama kwa kuzingatia mpangilio huu ufuatao:

A]. Sasa hivi kumekuwa na wimbi la washiriki wengi JF ambao wamekuwa wakivamia kwa kasi kwa tabia za ambazo ni hatarishi kwa hadhi ya JF. Kama vile uandishi ambao ni maarufu kutumika kwa njia ya text message, vi thread visivo vya msingi (member anafungua thread kwa kimstari kimoja bila maelezo kama kakurupuka tu) n.k. Mmejipanga vipi kuepusha huu uvamizi/mabadiliko ambayo yanaweza shusha hadhi ya JF?
Kungekuwa na mfano ningeshukuru kwakuwa tungeutumia kutoa ufafanuzi; hata hivyo, niseme uandishi wa ki-SMS ni wa vijana wetu wengi walio vyuoni na walio katika sekondari. Wengine ndio kwanza wamehitimu vyuoni, hili halitokei kwenye majukwaa yote; ni baadhi ya majukwaa kama Jukwaa la Elimu, MMU, ChitChat nadhani na kwenye Jokes. Ni nadra kukuta wanafanya hivyo kwenye siasa, timu ya wasaidizi wetu inajitahidi kufanya uhariri ili maandishi hayo yasomeke na kuweza kuwasaidia wale wasioelewa kilichoandikwa.

Nikuhakikishieni, hili ni suala la msimu tu na litapita tu. Kwa ambao wameitumia JF muda mrefu wanaelewa namaanisha nini kwa kusema hivi.

'Rating' ya hoja ili ionekane si ya msingi inategemeana na anayethaminisha hoja. Hata hivyo, JF ni mkusanyiko wa JAMII; ni lazima tukumbane na watu wa namna hii, kuwafukuza si kuwatendea haki, kuwafungia si kuwatendea haki pia; ni kuwarekebisha taratibu nao ni wazi watajifunza. Ni wengi wamebadilika, wahariri wetu hujitahidi kuwafahamisha wanaokosea kwa mitindo hii na wengi wanaonekana kubadilika.

Hata hivyo, tumeweka viunganishi vya kuwashtua wahariri wetu ili kama kuna hoja haijakaa sawa watuarifu ili ifanyiwe kazi haraka. Dawa si kuwafukuza wahusika, ni kuwaelekeza kistaarabu, wakikosa ustaarabu basi hawastahili kuwa sehemu yetu, tunawaweka kando kwa kuwafungia! Tunajaribu kujenga Taifa lenye critical thinkers, huwezi tarajia kupata critics bila kuwa na wanaokosea. Naamini kwenye kuwajenga wasio na uwezo wa kujenga hoja katika kujenga jamii yenye kuchambua hoja na matatizo yanayowakabili.

Kitufe cha REPORT ABUSE kikitumika kikamilifu, basi hili litarahisishwa sana.

B]. Kukua kwa JF kutakuwa kumesababisha challenges nyingi upande wa wanachama wachache wa kitambo; kwa mfano naomba ninukuu "JF used to be more of 'WIKILEAKS' kind of, and over the years, I have observed JF undergoing complete 'metamorphosis' into some form of a SOCIAL MEDIA". Unakubaliana na hizi tuhuma baridi dhidi ya JF?
Naam, kukua hakukwepeki; na tunapokua tunakumbana na mengi njiani.

- Kwamba JF 'used to be' lakini bila kusema nani alikuwa anasababisha iwe hivyo 'WikiLeaks' tunazunguka mbuyu. Ni nani alikuwa anaweka hizo 'nyaraka nyeti'? Ameondoka JF? Yupo? Hao niliowataja hapo juu wanaweza kufafanua wana uzoefu gani. The "key guy" is still around!

Nini kilipelekea kuacha kufanya hivi (kusitisha kwa muda)?
- Wengi waliomba tusiendelee kumwaga mambo ya UFISADI, ilifikia wakati watu wakaanza kuichukia nchi yao, hili si lengo letu! Ikumbukwe kuwa mengi yaliyokuwa yakiwekwa JF yaliwekwa na aidha sisi au mtu wetu wa karibu. Ilikuja EPA, Ikaja CIS, Ikaja MEREMETA, Ikaja Deep Green, Ikaja RICHMOND/DOWANS, zikafuatana nyingi kweli; watu wakakosa mwelekeo, wakaanza kuona kama nchi haifai hata kuishi! Nakumbuka mwaka 2008 ilitolewa tip juu ya fedha zilizofichwa Uswiss, ni wachache walioelewa; wengi walishakata tamaa, walishachoka kusoma habari za UFISADI au wizi wa aina yoyote. Limekuja kuibuka 2012, linaonekana ni jipya. Watu hawakujiuliza, tuna majina ya watu hao? Tuna details gani? Walitaka kujua tuhuma za mwanzo zinafanyiwaje kazi au ndio tunaendelea kupiga kelele lakini hakuna anayejali.

JF isilaumiwe kwa hili, kila mmoja achukulie kuwa kulinda rasilimali za nchi ni jukumu letu sote.

- Hatujasitisha moja kwa moja, kuna mengi yameibuliwa JF tangu hiyo 2008/2009. Naelewa, wengi hawajajua watayaona vipi, siku takribani 90 zijazo yataonekana kirahisi na ndilo hili tunalifanyia kazi kuhakikisha JF inakuwa rahisi kutumiwa na wengi na ikiwezekana na kila mtumiaji.

- Watanzania wengi ni waoga, nahisi wengine kupitiliza; hata jinsi ya kuelezea inakuwa vigumu. Kuna nyaraka kadhaa zilikuwa zikiwekwa JF, wao wanaogopa hata kuzipakua (download). Inaweza kuchekesha lakini ndiyo hali halisi.

- Habari za 'UFISADI' kwa sasa ni kama zimezoeleka masikioni mwa watanzania, si habari tena! Wengi wamekata tamaa, hata ukiweka ni wachache sana wanaozisoma! Woga umeenda mbali, hata kusoma thread ambayo ina 'sensitive' data mtu anasoma akiwa aidha amejificha au akiwa na wasiwasi mwingi.

Watakuita 'Jembe' lakini ikitokea ukapata matatizo kila mtu atadai 'nilijua tu' au 'anaonewa' lakini hawatachukua hatua kivitendo kuhakikisha unatoka matatizoni! Ndivyo tulivyo.
C]. Ni kwa kiasi gani msemo wa mahala penye uhuru wa kuongea (where you dare express openly) inazingatiwa katika Jamii Forums?
Ni vigumu kujibu hili, lakini anayelalamika huenda hajasoma Sheria za JF. Zipo kila sehemu na ziko wazi kabisa.

Napendekeza mtu asome hii thread - JamiiForums' Community Engagement Guidelines imesheheni mengi yanayojibu maswali juu ya hili na juu ya mengine ambayo huwa naona watu wanauliza hapa JF.

D]. Kuna madai toka kwa members baadhi kuwa kuna habari nyeti zinaletwa hapa jamvini lakini ndani ya muda mfupi zinafutwa bila maelezo ya kutosha; inayowatia mashaka baadhi ya hao members; unasemaje kuhusu hili?
Kama nilivyojibu hapo juu; wengi hawajasoma hiyo link niliyotoa. Ufafanuzi juu ya hili umetolewa hapa: Topic gani hufungwa au kufutwa kabisa JF?
 
Hio Post Melo ni ndefu mno, naomba nitakuwa si qoute. Kimsingi nina IMANI kwa kiasi kikubwa wale wote walio kuwa na maswali ya mithili hio wameridhia na majibu. Naomba nigusie kuwa tatizo huwa kuwa mara nyingi members na hata katika jamii vitu vyote ambavo vinahusiana na sheria ambazo zinahusiana na matumizi ya kitu atumiacho huwa ni ngumu kidogo kukalisha na kupitia kanuni. Nashukuru kwa majibu yako ulojibu kwa kirefu kabisa... Naomba nisonge na swali lifuatalo:-

Swali # 4

Kumekuwepo pia maswali ambayo yanahusisha washiriki moja kwa moja. Yanakuwa kama ya kizushi lakini kimsingi yana umuhimu ya kupata majibu pia.

A]. Mnatambua vipi kuwa mshiriki ana ID zaidi ya moja? Je kwa vigezo na masharti ya JF mshiriki anaruhisiwa kuwa na ID zaidi ya moja kwa vigezo vipi?

B]. Kwa kuzingatia kuwa kuna members wana ID zaidi ya moja, ushahidi ni baadhi ya matangazo katika jukwaa letu la Matangazo & Malalamishi ya post za Invisible - ya kuambatanisha hizo ID kama ilivokuwa kwa TUNTEMEKE; Ni vigezo gani vinavo fanya ID za mshiriki zi ambatanishwe (merged)?

C]. Kumekuwa na malalamiko kwa baadhi ya washiriki kupigwa ganzi (BAN) ya akaunti zao kwa tuhuma za kuonewa na kuwa wanakatishwa kijanja kusema yalo kweli; unasemaje kuhusu hili?

D]. Imewahi tokea tukio lolote ambalo ulilazimika kutoa IP Iddress/Physical address ya member yeyote ambaye ni mshiriki wa JF?

E]. Mzee Mwanakijiji ni nani hapa JF? Je ni mmoja wa wamiliki? Unaweza kuzungumzia lolote kuhusu ushiriki wake hasa kwenye Jukwaa la Siasa?

F]. Kuna baadhi ya mods walikuwepo kitambo ambao wanauliziwa. Baadhi ya waliotajwa ni Farida, Painkiller na Snail. Vipi bado wapo kimya kimya ama hawapo tena?
 
Hio Post Melo ni ndefu mno, naomba nitakuwa si quote.
Vema, kunukuu ujumbe mrefu ni kuwachosha wanaotumia simu.

A]. Mnatambua vipi kuwa mshiriki ana ID zaidi ya moja? Je kwa vigezo na masharti ya JF mshiriki anaruhisiwa kuwa na ID zaidi ya moja kwa vigezo vipi?

B]. Kwa kuzingatia kuwa kuna members wana ID zaidi ya moja, ushahidi ni baadhi ya matangazo katika jukwaa letu la Matangazo & Malalamishi ya post za Invisible - ya kuambatanisha hizo ID kama ilivokuwa kwa TUNTEMEKE; Ni vigezo gani vinavo fanya ID za mshiriki zi ambatanishwe (merged)?
Nahisi hili lilitakiwa kuwa swali moja, lakini nitalijibu kama lilivyotenganishwa bila kuathiri lengo:

A: Ni wazi JF imepita kipindi kigumu kama ambavyo tumeongea awali, ni wazi tulishaanza kuona kuanza kwa watu kusajili zadi ya jina moja kwa dhamira mbaya na wengine kwa dhamira njema. Hapa, tukalazimika kutengeneza namna ya kuweza kuwanasa wanaojisajili kwa zaidi ya jina moja kwenye pc moja. Lakini, bado hili halitoshi kwani yawezekana watu wakatumia pc moja lakini wakawa ni watu wawili tofauti. Hapa, kuna utambuzi wa namna mtu anavyochapa kwenye kompyuta yake ili tusije tukaunganisha watu kwa uonevu.

B] Kama nilivyojibu hapo juu katika [A] inaeleweka basi jibu la B linakuwa halina maelezo marefu, japo nahisi Jukwaa hilo ni lile la Pongezi na Malalamiko (si matangazo).

C]. Kumekuwa na malalamiko kwa baadhi ya washiriki kupigwa ganzi (BAN) ya akaunti zao kwa tuhuma za kuonewa na kuwa wanakatishwa kijanja kusema yalo kweli; unasemaje kuhusu hili?
Ukisoma sheria za JF zinasema wazi, kuwa ukifungiwa una nafasi ya kukata rufaa. Haiwezekani wahariri wetu wakawa sahihi mara zote, wanaweza kumwonea mtu lakini inapotokea mtu akakata rufaa huwa tunaziangalia.

Niseme, hatupendi hii 'fungiafungia' lakini huwa tunalazimika. Haipendezi kweli.

Link nilizotoa hapo awali zina maelezo yaliyo wazi na yanayotoa majibu kwa swali hili pia; tatizo watu hawasomi link hizo. Sheria za JF, sheria namba 8 inasema hivi:
8 - Circumventing a Ban:
If you log onto the forums and receive a message that you have been banned, please submit an unban request and wait for a staff member to get in touch with you. You may NOT re register under a new name if the software lets you. But, if you try to sign up again and we caught you, then it will become a permanent IP Ban. We do NOT send out notices that you have been banned.

D]. Imewahi tokea tukio lolote ambalo ulilazimika kutoa IP Iddress/Physical address ya member yeyote ambaye ni mshiriki wa JF?
Swali zuri, mpaka sasa JF hakuna crime. Najua kuna watu wanaodai wamepewa IP za wateja wa JF na huenda kuna wengine wanajigamba wanaona IP za watu. Huu ni uwongo, bado hakuna CRIME imefanyika katika JF ambayo hata sisi tunaona mhusika ametushinda tunalazimika kumfikisha kwenye vyombo vya dola. Hatujawahi kutoa data za mtu na hatutarajii hili litatokea!

Hata hivyo, IP address za Tanzania bado ni tatizo, sina uhakika sana lakini naamini watanzania wenye kusajili IP address zao ni wachache, hawazidi 500 (japo sina takwimu sahihi). Wengi tunatumia IP ambazo tunashirikishana (shared IPs).
E]. Mwanakijiji ni nani hapa JF? Je ni mmoja wa wamiliki? Unaweza kuzungumzia lolote kuhusu ushiriki wake hasa kwenye Jukwaa la Siasa?
Mzee Mwanakijiji,

Naweza kumwelezea kama rafiki, mmoja kati ya wanachama wakongwe wa JF, mzalendo wa kweli na mwenye kuipenda nchi yake, mpiganaji asiyechoka! Ni mwenye kujiamini na aliye tayari kuitetea JF na nchi yake.

attachment.php

Ni wazi ukienda BRELA ukaangalia nyaraka hutokuta jina la Mzee Mwanakijiji, uzalendo wake ndio unawapelekea wengi kudhani ni mmoja wa wamiliki. Lakini, endapo JF inaweza ikaingiza kipato kizuri, ni wazi huyu hatuwezi kumsahau!

Lakini, hata ChitChat ina wakongwe wake, same applies kwa MMU - Mtambuzi, Bishanga n.k
. Kuna baadhi ya mods walikuwepo kitambo ambao wanauliziwa. Baadhi ya waliotajwa ni Farida, Painkiller na Snail. Vipi bado wapo kimya kimya ama hawapo tena?
Hapana, PainKiller ni mod aliye online muda mwingi sana. Yeye ni mtendaji zaidi, na hata ninavyoandika yupo! Aidha, Farida yupo pia.

Snail si moderator tena, ana majukumu mengine na hata hilo jina halipo JF kwa sasa, labda mtu mwingine ajisajili kwa jina hilo.
 
Mkuu naona umeua! Mie nilijua ni Jukwaa la matangazo pia - Nashukuru kwa masahihisho hayo. Naomba kwa niaba ya walio ridhika na hayo majibu uliotowa kama mimi nishukuru tena kwa majibu hayo ya kina. Nisonge swali lifuatalo:

Swali # 5

Ni wazi kuna waendesha/waongoza Forum kwenda sawa sawa na kutoa huduma kwa washiriki maarufu kwa jina la Moderators a.k.a Mods.

A]. Je mtu yeyote anaruhusiwa kuomba kuwa Mod?

B]. Ukizingatia kuwa mtu kuwa mod ana nguvu Fulani ya kuweza toa maamuzi; ni vigezo gani vinatumika mtu kuwa Mod hasa kujua kama ni muaminifu na anafaa?

C]. Imewahi tokea mkaweka mod ambae akaharibu kazi kwa makusudi na kusababisha matatizo makubwa kwa sababu zozote zile? Kama ndio utajali kueleza ilikuwa vipi?

D]. Kuna mod mkuu maarufu hapa JF kama Invisible nafasi yake inaweza kugombewa?
 
Swali # 5

Ni wazi kuna waendesha/waongoza Forum kwenda sawa sawa na kutoa huduma kwa washiriki maarufu kwa jina la Moderators a.k.a Mods.

A]. Je mtu yeyote anaruhusiwa kuomba kuwa Mod?
Naam, yeyote anaweza kuwa moderator lakini endapo atakidhi vigezo tunavyovihitaji. Hatuna vizingiti, na ukweli tunahitaji wahariri sana kadiri jukwaa linavyozidi kukua.

B]. Ukizingatia kuwa mtu kuwa mod ana nguvu Fulani ya kuweza toa maamuzi; ni vigezo gani vinatumika mtu kuwa Mod hasa kujua kama ni muaminifu na anafaa?
Hatumkabidhi mtu 'rungu' kabla ya kumdadisi mienendo yake katika jukwaa. Ni lazima awe mtu anayestahili kuhudumia wenzake. Mtu ambaye hana 'trend' ya matusi, kejeli, mnazi wa vyama n.k ni vigumu kumkabidhi rungu, ni wazi yeyote atakayeenda kinyume anavyofikiria yeye atachukua maamuzi yatakayotugharimu kama timu.

Nichukue fursa hii kuwapongeza mods wote kwani kwa kiwango kikubwa wanafanya kile ambacho wana JF wanatarajia toka kwao; hawawezi kuwa wakamilifu asilimia mia moja, lakini walau wanajitahidi kwa kiwango kikubwa sana.
C]. Imewahi tokea mkaweka mod ambae akaharibu kazi kwa makusudi na kusababisha matatizo makubwa kwa sababu zozote zile? Kama ndio utajali kueleza ilikuwa vipi?
Naam, imewahi. Hatuwezi kuwataja majina (watatu) lakini ndio hivyo, uzoefu ule ulitufundisha kuweza kupata muda wa kuchunguza kabla ya kutoa uwezo huo kwa mwanachama.

MFANO: Mmoja alikuwa akiziweka kapuni posts zote zilizokuwa zikienda kinyume na anavyotaka, mwingine alikuwa akitumia jina lake la uhariri kwenye kuandika (jina moja kwa uhariri na ushiriki wa mijadala), yeyote aliyeonekana kumkosoa alikuwa akizibadili post zake ili aonekane amejibiwa anavyotaka.

Ni mifano hai, tumeiona lakini imekuwa fundisho kwetu.

D]. Kuna mod mkuu maaruru hapa JF kama Invisible nafasi yake inaweza kugombewa?
Invisible ni Admin, ana access level kubwa; nafasi yake haigombewi, tukipata wahariri zaidi ni wazi wanaweza kuwa maarufu zaidi yake. Tayari kuna wanne wanaandaliwa, lengo ni kuboresha kilichopo JF na kiingiacho JF.

Nisisitize, tunahitaji sana wahariri, ikibidi kila jukwaa liwe na wahariri wake; tukipata watu kujitolea kwa hili watakuwa wametusaidia katika kutekeleza majukumu mengine ya kuiboresha JF.
 
Nisisitize, tunahitaji sana wahariri, ikibidi kila jukwaa liwe na wahariri wake; tukipata watu kujitolea kwa hili watakuwa wametusaidia katika kutekeleza majukumu mengine ya kuiboresha JF.


Nimekupata vema katika maelezo na majibu yako ya swali # 5.

Hata hivo hiki kipengele kimenifanya nivutiwe na kunifanya nitake kuelewa zaidi. Kwa faida yangu na wale wote wenye kupenda kutambua hili kwa kina; Naomba nitambue kama hutajali;


  • Kuna matangazo tayari ambayo yamewekwa kwa members kuhusu kuhitajika kwa hao wahariri?
  • Na je vigezo vya uhariri vyote ni sawa kwa kila Jukwaa... Kwamba kama mtu anajua kuhariri basi inatosha kumpa hio nafasi kwa msingi tu wa kusema kakubali kujitolea?
  • Kuna vigezo na masharti yameainishwa mahala ili wale wenyewe wanavutiwa wajipime kwa kusoma kama wanafuzu kuomba nafasi?
 
Kuna matangazo tayari ambayo yamewekwa kwa members kuhusu kuhitajika kwa hao wahariri?
Hapana

Na je vigezo vya uhariri vyote ni sawa kwa kila Jukwaa... Kwamba kama mtu anajua kuhariri basi inatosha kumpa hio nafasi kwa msingi tu wa kusema kakubali kujitolea?
Kama nilivyosema awali, moderator (haijalishi ni wa jukwaa gani) lazima azingatie vigezo nilivyogusia. Asiwe mnazi wa siasa, mwenye kuegemea upande flani (tunazipitia posts zake kwanza); asiwe mwenye matusi/dharau/kejeli kwa wengine, awe tayari kuwasaidia wanachama wenzake pale wanapokosea, awe tayari kuzingatia kanuni za uhariri za JF (zipo, akishapata uwezo huo anaziona moja kwa moja) na awe anaelewa kuwa anahudumia watu wazima.
Kuna vigezo na masharti yameainishwa mahala ili wale wenyewe wanavutiwa wajipime kwa kusoma kama wanafuzu kuomba nafasi?
Hapana, hatudhani ni sahihi kufanya hivyo; lakini kwa rai hii basi wale ambao wapo tayari kutusaidia tutawafahamisha kwa pembeni (PM) nini tunahitaji na wao watwambie utayari wao.
 
Asante kwa majibu ya maswali ya nyongeza...

Swali # 6


Maxence Melo naomba tuingie kwenye siasa kidogo, na kabla ya kosonga mbele kama hutajali naomba tuambie, wewe upo Chama kipi? Kwa mshiriki wa mara kwa mara hapa Jamii Forums kati kati ya mabandiko mbali mbali - (nayo tokana na misimu) kunakuwa na shutuma mbali mbali kama vile:- JF ya CHADEMA, mara tena utakuta JF imenunuliwa na CCM, mara tena JF inamilikiwa na wakubwa. Hizi shutuma zipi ni kweli? AMA zipi zinaelekeana na ukweli?
 
Swali # 6

Maxence Melo naomba tuingie kwenye siasa kidogo, na kabla ya kusonga mbele kama hutajali naomba tuambie, wewe upo Chama kipi?
Nadhani hapa unamaanisha chama cha siasa.

Tangu nizaliwe sijawahi kuwa na kadi ya chama chochote cha siasa, zaidi nakumbuka niliwahi kuimba 'Naapa naahidi.....' na huenda wengi wako kama mimi. Lakini, niliimbishwa na sikuwa najua maana yake. Nadhani ni wengi wa aina yangu, wengine wana mapenzi na vyama, lakini nina wasiwasi kama ni wanachama wa vyama wanavyoshabikia.

Kuna mazuri nayaona pande zote, upinzani na chama tawala; lakini vilevile kuna madhaifu nayaona pande zote. Mpaka sasa, nimeshiriki chaguzi kadhaa na nilichagua mtu badala ya chama.
Kwa mshiriki wa mara kwa mara hapa Jamii Forums kati kati ya mabandiko mbali mbali - (nayo tokana na misimu) kunakuwa na shutuma mbali mbali kama vile:- JF ya CHADEMA, mara tena utakuta JF imenunuliwa na CCM, mara tena JF inamilikiwa na wakubwa. Hizi shutuma zipi ni kweli? AMA zipi zinaelekeana na ukweli?
Swali hili na hata lililotangulia, niliwahi kuyatolea ufafanuzi zaidi hapa:
Maxence Melo: Wamiliki wa JF ni Watanzania wanaoitumia

Naamini maswali mengine kama hili yatakuwa yamefafanuliwa kwenye mahojiano haya niliyofanya na BongoCelebrity.com
 
Mkuu wewe mwalimu wa lugha nini? Duh' hata hivo nishukuru kwa masahihisho, naona najifunza huku kazi inaenda. Kwa muktadha wa majibu ambayo umejibu hapo juu ya Chama gani cha siasa upo, naamini kuwa basi maswali yanayofuata yatajibiwa sio kwa msingi wa ushabiki bali Utambuzi zaidi. Swala ambalo ni muhimu na msingi zaidi.

Naomba utambue pia kuwa swali linalofuata ambalo ni # 7 ni refu, kwa namna unavojibu kwa kina limegaiwa kwa makundi mawili. Hii post ina kundi la kwanza na post itayofuata ya maswali itakuwa na kipengele cha pili cha swali la 7.

Swali # 7 (kundi A)

Siasa ipo katika wakati ambao imekuwa na changamoto nyingi, mabadiliko mengi, mwamko mkubwa kwa wanachi. Tokana na mchango wa Jukwaa la Siasa hasa kwa watumiaji - unaweza fuzu kama mmoja wa wanaharakati. Tunaoamba kujua ni nini mtazamo wako katika yafuatayo:

A]. Nafasi ya CCM na CHADEMA katika kipindi hiki hasa kabla ya Uchaguzi?

B]. Nini msimamo wako juu ya Rais Kijana kwa Tanzania 2015, kama vile Zitto Kabwe na January Makamba?

C]. Unakubaliana na dhana kuwa "UDINI" unaikumba taifa la Tanzania?
 
A]. Nafasi ya CCM na CHADEMA katika kipindi hiki hasa kabla ya Uchaguzi?
Kwanini CHADEMA & CCM tu?

Lakini, kwakuwa umewagusia hawa vema nitoe mawazo yangu kulingana na swali.

CCM:
Ni chama tawala, kina nafasi ya kufanya mengi (miaka 2 na zaidi) ya kuwafanya watanzania warejeshe imani, lakini ni lazima maamuzi magumu yachukuliwe. Kuna tatizo ndani ya CCM, ukweli hawaukubali, ni tatizo kubwa ambalo nahisi linakigharimu chama. Kuiondoa CCM madarakani 2015 inahitaji kazi nzito!

CHADEMA:
Wanazidi kupata mafanikio makubwa kisiasa, hata wale wanaosema NCCR ilikuwa hivi nadhani wanaona kuwa sio hivi tena, kasi waliyo nayo ikiendelea hivi, basi 2015 haitashangaza wengi kusikia CHADEMA imechukua madaraka. Lakini, kazi inaweza kuwa rahisi endapo utatokea mpasuko ndani ya CCM na kukatokea kundi ambalo linaweza kuongeza nguvu CHADEMA.
B]. Nini msimamo wako juu ya Rais Kijana kwa Tanzania 2015, kama vile Zitto Kabwe na January Makamba?
Nadhani kwangu si ujana wala uzee. Binafsi nadhani kama taifa tunahitaji rais mwenye kuthubutu, rais mwenye uchungu na nchi (mzalendo) n.k. Sipingi hoja ya kushusha umri wa kugombea nafasi hii, ni suala la kuangaliwa; lakini sidhani kama ujana wala uzee kwangu ni hoja kubwa pindi nikiwa namchagua rais.
C]. Unakubaliana na dhana kuwa "UDINI" unaikumba taifa la Tanzania?
Siwezi kusema mengi, tahadhari ilishatolewa hapa JF, mapema sana (5yrs ago); wana JF waliongea waliyoweza kuyaongea, hii hapa ni hoja ya mwaka 2007:
Tupende, tusipende: Tanzania inanyemelewa na udini!

Siwezi kuongeza zaidi ya kilichoandikwa kwenye mjadala huu, cha muhimu ni watanzania kushirikiana, kuhakikisha hili tunalishinda kwa pamoja.
 
71 Reactions
Reply
Back
Top Bottom