Return Of Undertaker
JF-Expert Member
- Jun 12, 2012
- 4,572
- 26,868
Kwa ufupi
Mgombea wa CCM, Rais John Magufuli alishinda nafasi ya urais katika uchaguzi wa Oktoba 25, 2015 akipata kura 8,882,935 sawa na asilimia 58.46 huku mpinzani wake wa karibu Edward Lowassa wa Chadema akijipatia kura 6,072,848 sawa na asilimia 39.97 ya kura zote.
Ikiwa imepita miaka mitatu tangu CCM ishinde urais, utata umejitokeza katika utekelezaji wa ilani yake ya (2015-2020) kutokana na baadhi ya ahadi kubaki njia panda hadi sasa.
Mgombea wa CCM, Rais John Magufuli alishinda nafasi ya urais katika uchaguzi wa Oktoba 25, 2015 akipata kura 8,882,935 sawa na asilimia 58.46 huku mpinzani wake wa karibu Edward Lowassa wa Chadema akijipatia kura 6,072,848 sawa na asilimia 39.97 ya kura zote.
Kabla ya uchaguzi huo uliokuwa na ushindani mkali, vyama hivyo na vingine vilikwenda kwa wananchi kunadi sera ambako pia vilitoa ahadi mbalimbali na chama kilichoshinda, kinatazamiwa kutoa mrejesho katika utekelezaji.
Mimba kwa wanafunzi
Miongoni mwa ahadi ambazo CCM ilitoa katika ilani yake ya uchaguzi ni kuwaruhusu wanafunzi wa kike wanaopata mimba kuendelea na masomo, suala ambalo kiwa siku za karibuni limezuia mjadala mzito, hadi Benki ya Dunia kuingilia kati.
Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa 2015 fungu la 52 kifungu (i) kinachosema: Kuhuisha miongozo ya Elimu na Mafunzo ili kuondoa vikwazo vinavyosababisha mwanafunzi kushindwa kukamilisha mzunguko wa elimu au mafunzo ili kuhakikisha kwamba:- (ii) Wasichana wote wa Elimumsingi wanaoacha shule kwa sababu ya kupata ujauzito wataendelea na masomo; na
(iii) Wanafunzi wanaomaliza mzunguko wa elimu katika ngazi ya Elimumsingi wanaongezeka kutoka asilimia 67 mwaka 2015 hadi asilimia 95 mwaka 2020.
Wakati ilani ikisema hivyo, msimamo wa Rais Magufuli ni tofauti.
Akihitimisha ziara ya siku tatu mkoani Pwani Juni 2017, Rais Magufuli alisema ndani ya utawala wake hakuna mwanafunzi mwenye mimba atakayerudi shuleni.
“Nataka niwaambie hizi NGO (taasisis zisizo za kiserikali) na ninyi wote mnaosikia, ndani ya utawala wangu kama Rais, hakuna mwenye mimba atakayerudi shuleni. Narudia, hakuna mtu mwenye mtoto, katika elimu la darasa la kwanza mpaka sekondari atakayerudi shuleni,” alisisitiza Rais Magufuli.
Akizungumzia suala hilo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Humphrey Polepole alisema suala hilo ni la kisera na kwamba kuna mifumo miwili ya utoaji wa elimu ikiwa pamoja na mfumo rasmi na mfumo usio rasmi.
“Mfumo wa kwanza ni mfumo rasmi. Mantiki katika mfumo huu ni kumjenga mtoto asome katika mazingira ya kumwongezea nidhamu, umahiri, heshima katika masomo mbalimbali,” alisema Polepole.
Hata hivyo, kwa upande wa elimu, Rais Magufuli ametekeleza sehemu ya ilani hiyo katika utoaji wa elimu bila malipo kwa shule za msingi na sekondari.
Eneo jingine lenye utata ni suala la mikopo ya elimu ya juu ambako licha ya ongezeko la idadi ya wanafunzi wanaopata mikopo katika Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB), bado kumekuwa na malalamiko ya wanafunzi wengi kutoipata baada ya kuongezwa vigezo vinavyowaengua.
Kwa walionufaika na kuhitimu masomo nao wamekumba na kupandishiwa riba ya mkopo kutoka asilimia nae walizoingia mkataba hadi 15.
Katiba Mpya
Ilani ya CCM kifungu cha 145 kinasema: Ili kuendeleza Utawala Bora, Demokrasia na Uwajibikaji, katika kipindi cha miaka mitano ijayo (2015-2020), CCM itahakikisha kuwa, Serikali inakamilisha mchakato wa Katiba mpya. Ahadi hiyo imo kwenye kifungu kidogo (g) kinachosema: “Kukamilisha mchakato wa kutunga Katiba mpya na kuanza kuitekeleza kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.”
Hata hivyo, mara kadhaa Rais Magufuli ameeleza kutokuwa na nia ya kukamilisha mchakato huo akisema si kipaumbele chake.
Akizungumza katika kongamano la siasa na uchumi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam hivi karibuni, Rais Magufuli alisema licha ya kufahamu hamu ya Watanzania kuwa na Katiba mpya anashindwa kuelewa mchakato uanzie wapi, kwenye Katiba pendekezwa au katika rasimu iliyoandaliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Novemba 4, 2016 alipozungumza na wahariri Ikulu Dar es Salaam baada ya kutimiza mwaka mmoja madarakani, Rais alisema hakuwahi kuahidi suala hilo kwenye kampeni, bali anataka kutekeleza ahadi alizowaahidi wananchi.
Sh50 milioni kila kijiji
Katika fungu la 57 (d) la ilani hiyo chama hicho kinazungumzia kuwawezesha wananchi kiuchumi kuwa “CCM itaielekeza Serikali kutenga kiasi cha Sh50 milioni kwa kila kijiji kama mfuko wa mzunguko (Revolving Fund) kwa ajili ya kukopesha vikundi vya wajasiriamali kupitia Saccos.”
Hadi sasa mfuko huo haujaanza na hivi karibuni akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Kazuramimba wilayani Uvinza, Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan alisema wananchi wasitegemee kupelekewa fedha hizo badala yake zitakwenda kufanya miradi mbalimbali ya maendeleo.
Alisema kuliko kutoa fedha hizo kwa kila kijiji, Serikali imeamua kuwekeza katika elimu, afya, barabara pamoja na maji, lengo likiwa ni kupeleka maendeleo kwa wananchi.
Nyongeza ya mshahara
Ilani ya CCM ambayo iligusa karibu kila nyanja ya maisha, katika fungu la 174 (a) inaahidi “Kuhakikisha kwamba mfanyakazi atalipwa kima cha chini cha mshahara kinachokidhi mahitaji muhimu ya maisha kwa kuzingatia uwezo wa kiuchumi wa Taifa.”
Pamoja na ahadi hiyo, kumekuwa na mdai kwamba mishahara ya wafanyakazi haijaongezwa na kuwa gharama za maisha zimepanda.
Akizungumza katika kilele cha Siku ya Wafanyafakazi 2018 kitaifa katika Uwanja wa Samora mjini Iringa, Rais Magufuli alisema, “Masuala yote niliyotaja yanategemea chungu kimoja cha fedha na kupanga siku zote ni kuchagua, kwamba unaweza kuamua tujenge reli, hospitali, tujenge hospitali, tutoe elimu bure, tujenge barabara au tujipandishie mishahara?
“Au tuyapeleke kwa pamoja tupandishe mishahara na hayo yote tuyafanye? Hapo ndipo changamoto ninayoiona mimi,” alisema Rais Magufuli.
“Kwangu mimi naona ukijenga reli ‘Standard Gauge’ utabeba mizigo mingi hasa kwenye nchi ambazo ni ‘land locked countries’ kama Rwanda, Burundi, DRC nk, ukibeba mizigo mingi utatengeneza pesa nyingi ambazo utazitumia hata kama ni kujiongezea mishahara,” alifafanua.