Ijue vyema tafsiri ya Megawati 2115 za umeme

Mpinzire

JF-Expert Member
Jan 18, 2013
7,206
12,907
Kama kuna jambo ambalo Rais John Magufuli atakumbukwa sana na vizazi vya sasa na vijavyo ni kuamua kuendelea na ujenzi wa mradi wa kuzalisha umeme wa maji katika Mto Rufiji, mradi ambao ulipingwa sana na mabeberu.

Hata hivyo, baadhi ya Watanzania wanasikia kuhusu habari ya utekelezaji wa mradi huo mkubwa uliobuniwa na Mwalimu Nyerere tangu miaka ya 1975 kwamba utazalisha megawati za umeme 2,115, lakini pengine hawaelewi vyema maana yake.

Leo imenipendeza niumulike kidogo mradi huu wa umeme ili tujue ni nini tafsiri ya kuwa na mradi huu katika uchumi wetu, hasa kwa kuzingatia uamuzi wa serikali ya awamu ya tano kuamua kujenga uchumi unaotegemea viwanda. Ikumbukwe umeme na ujenzi wa viwanda vya uhakika ni sawa na ulimi na mate kwa jinsi vinavyotegemeana.

Mradi huu wa kuzalisha umeme unatajwa kama wa nne katika uzalishaji wa umeme barani Afrika na unatarajia kugharimu Sh trilioni 6.5 mpaka utakapokamilika mwaka 2022 kwa kutegemea fedha zetu za ndani. Kutokana na kupingwa na mabeberu na taasisi zao, bila shaka ingekuwa vigumu kuukamilisha kama tungetegemea fedha zao.

Azma ya utekelezaji wa mradi huo inakuja wakati nchi ikiwa kwenye ujenzi wa uchumi wa viwanda ambao kwa kiwango kikubwa unategemea sana nishati umeme. Viwanda ni umeme na umeme ni viwanda.

Kuzielewa megawati 2,115 zitakazozalishwa na ukubwa wake ni rahisi ukipitia na kujua matumizi ya umeme na mahitaji ya umeme kwa taifa letu. Mfano mwepesi ni kwamba, mahitaji halisi ya umeme kwa mikoa kama ya Mtwara na Lindi ili umeme usikatike hata sekunde moja ni megawati 22 hadi 30 tu. Hii ina maana katika zile megawati 2,115 tunakuwa na ‘chenji’ kama ya megawati 2,085.

Tanzania ina mikoa 31, hivyo ukifanya uhitaji wa umeme wa kila mkoa ni wastani wa megawati 50 tu kwa makadirio ya juu hata kwa mikoa isiyozidi matumizi hayo maana yake ni sawa na kupeleka ‘bahari’ ya umeme kila mkoa na bado ukabaki na akiba kibindoni ya megawati 565.

Kwa kuwa na umeme huu ina maana hapo tunaenda kuua kabisa habari ya nchi kukumbwa na mgawo wa umeme. Wenye viwanda vikubwa, vya kati na vidogo watazalisha bidhaa zao bila tatizo na zuri zaidi itakuwa ni kwa gharama nafuu za umeme kulinganisha na sasa ambapo umeme tunaozalisha ni ghali na gharama zake ziko juu.

Kimsingi, bwawa la Mwalimu Nyerere pekee linakwenda kutupa umeme wa uhakika tena wa maji ambao ni rahisi zaidi kuliko aina nyingi za umeme.

Takwimu zilizopo zinaonesha kwamba uniti moja inayozalishwa na umeme wa maji ni shilingi 36 tu wakati umeme wa nyuklia ni shilingi 65 kwa uniti, umeme wa jua shilingi 103.05, upepo Sh 103.05, makaa ya mawe Sh 18, gesi asilia Sh 147 na mafuta ni Sh 426.

Hii maana yake ni kwamba umeme huu utashusha maradufu bei ya umeme kwa watumiaji na hivyo mfumuko wa bei wa bidhaa za viwandani kuwa himilivu katika nchi yetu.

Kushuka kwa bei ya umeme kutahamasisha pia matumizi ya umeme kwa ajili ya nishati ya kupikia majumbani na hivyo kupunguza athari za kimazingira zinazosababisha Watanzania wengi kuendelea kutumia kuni na mkaa.

Watanzania wanaoendelea kuanzisha viwanda vidogo kwa vikubwa watanufaika zaidi kutokana na gharama ndogo za umeme na kuchangia kupungua kwa gharama za uzalishaji wa bidhaa, hali itakayoleta neema na unafuu mkubwa kwa walaji.

Unapokuwa na umeme wa uhakika, tena wa gharama nafuu ya bei tayari unavutia wawekezaji wengi zaidi wa ndani na nje kuja kujenga viwanda hapa Tanzania. Uhakika wa umeme tena wenye unafuu ni mambo ya msingi yanayozingatiwa sana na wawekezaji.

Vipi, umefikiria kuhusu hizo megawati tutazobaki nazo kibindoni baada kujihakikishia uhakika wa umeme nchi nzima bila kuangalia zile zinazozalishwa kwa sasa takribani megawati 1600? Hapo tunaweza kuamua kuuza kwa majirani zetu wengi ambao bado wanasumbuka na umeme wa uhakika kama tulivyo sisi kwa sasa.

Bunge la Ujerumani liliwahi kupitisha muswada wa kuitaka serikali ya Ujerumani kuwasiliana na ya Tanzania kusitisha mradi huo kwa madai kwamba utaharibu mazingira.

Lakini bila shaka majibu ya Rais John Magufuli yamewatosheleza. Rais amekuwa akisema kwamba kuamua kuanzisha mradi huo hawakukurupuka bali walitumia muda wa kutosha kutafakari na kugundua kwamba mradi huo, licha ya kuwa na faida lukuki, hauharibu mazingira kama inavyodhaniwa na badala yake unayaboresha.

Rais Magufuli alizidi kufafanua kwamba mradi huo utatumia asilimia tatu pekee ya mbuga ya wanyama ya Selous yenye ukubwa wa kilomita 50,000 za mraba.

Ikaelezwa pia kwamba umuhimu wa bonde hilo kutumika kuzalisha umeme unatokana pia na ukweli kwamba chanzo chake ni cha uhakika na maji yake yanatoka katika mito inayotoa wastani wa mvua. Vilevile bwawa hilo lina uwezo wa kuzalisha umeme kwa zaidi ya miaka 60 ijayo.

Rais pia amekuwa akisema kwamba bado gharama za kukamilisha mradi huo ni ndogo kulinganisha na miradi mingine, ikiwemo ya kuvuna gesi ambayo sehemu kwa sasa iko katikati ya bahari.

Kulikuwa na hofu kwamba kujenga bwawa la kuzalisha umeme lenye urefu wa kilomita 100 na kilomita 25 kwa upana itakuwa ndiyo mwanzo wa kuiua hifadhi hiyo ya Selous ambayo ilitangazwa na Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa (UNESCO) kuwa urithi wa dunia lakini maelezo ya serikali yanaonesha hofu hiyo ilikuwa ya kufikirika zaidi kulinganisha na uhalisia na umuhimu wa mradi huo kwa Tanzania.

Sambamba na ujenzi wa bwawa hilo la umeme, pori la akiba la Selous pia limegawanywa katika maeneo mawili ya kuanzishwa mbuga ya Wanyama ya Nyerere kwani shughuli za uwindaji wa wanyama unaofanyika katika pori hilo umekuwa ukilikosesha taifa mapato halisi ya shughuli za uwindaji zinazofanywa katika pori hilo.

Rais Magufuli alikaririwa akiwataka Watanzania wakatae “kulaliwa” na wajanja wachache kwa manufaa yao binafsi wakisingizia vitu mbalimbali ikiwemo masuala ya kuharibu mazingira.

Chanzo: Habari Leo
 
Mtera, Kidatu, pangani, Nyumba ya Mungu si yalijengwa na watangulizi wake pia?
Reli ya kati si imejengwa na raisi pia? cha ajabu?
Njoo na hoja mbadala.

Eti reli ya kati iijengwa na Rais?

Inasikitisha sana mtu anashinda humu hata historia ya nchi haijui.
 
Kama JPM angekua mwoga asinge thubutu kuanzisha uu ujenzi wa bwawa, baadhi ya Mabeberu wamepiga sana mkwara uu mradi usianzishwe. Hongera JPM utakumbukwa kwa Transiformesion uliyo ifanya Tanzania.
 
..huo mradi unaishi lini?

..tulitakiwa tuwe na miradi midogo na ya kati inayokamilika haraka zaidi.

..Ni kweli tunahitaji umeme mwingi, lakini tunatofautiana jinsi ya kufikia lengo hilo.
nenda kaulize site
 
Hizo blah blah za umeme tumeshazichoka. Hazina jipya.

Wakati ule wa kuchimba gesi ya Mtwara, CCM hii hii, na Magufuli akiwa waziri mwandamizi, mpiga mapambio ya kusifu na kuabudu, tuliambiwa tungepata umeme wa bei ya bure na gesi ingekuwa bwerere kiasi ambacho matumizi ya kuni na mkaa yangebakiwa kuwa historia.
Kiko wapi sasa?
 
Mradi huu ni bora kuliko miradi yote ya serikali ya awamu ya tano lakini sio bora kuliko UHURU WA WATU, UHURU WA HABARI,MAISHA YA WATU NA USTAWI WA FAMILIA.

Unadhani familia ya Azori inahitaji megawati ngapi kumfidia? He wazazi wa Ben Saanane utawapa megawar ngapi?
Risasi za Tundu zinafidiwa na megawati ngapi.

Alfonso Mawazo ni megawati ngapi? MPAKA ZIPATIKANE HIZO MEGAWATI 2000, NI DSMU KIASI GANI ITAKUWA IMEMWAGIKA?
 
Kama JPM angekua mwoga asinge thubutu kuanzisha uu ujenzi wa bwawa, baadhi ya Mabeberu wamepiga sana mkwara uu mradi usianzishwe. Hongera JPM utakumbukwa kwa Transiformesion uliyo ifanya Tanzania.
Hata Hitler kule ujerumani anakumbukwa mpaka leo hii kwa miundo mbinu mingi na imara iliyopatikana kwa za njia za hila, dhuluma, damu na mateso dhidi ya wanyonge.
 
Back
Top Bottom