Ijue shule ya msingi Bunge, hatua 200 kutoka Ikulu lakini wana uhaba uliokithiri wa vyoo

Majs

JF-Expert Member
Dec 21, 2012
229
485
Rooney* ni miongoni mwa wanafunzi wachache waliobahatika kusoma shule za msingi za umma maarufu nchini. Kila asubuhi ya siku za wiki huamka na kuanza safari ya kwenda kutimiza ndoto za kielimu katika Shule ya Msingi Bunge jijini Dar es Salaam.

Wazazi wanaamini mtoto wao anasoma shule yenye mazingira mazuri ikizingatiwa ipo mita 200 tu kutoka Ikulu. Watoto wenzie anaokaa nao Tabata Kisukuru wanamuonea wivu kusoma katika shule hiyo ya ghorofa iliyopo katikati ya jiji.

Kitu ambacho wengi hawajui ni kwamba Rooney, anayesoma darasa la sita shuleni hapo, huitaji kupanga foleni kwa zaidi ya dakika tatu kwenda msalani kujisaidia kutokana na uhaba wa matundu ya vyoo.

“Najivunia tu kusoma Bunge lakini huko chooni siyo kuzuri,” anasema.

“Kuna wakati hapa baadhi yetu hubanwa na kushindwa kujizuia hivyo hulazimika kujisaidia nje ya choo au kuingia wawili choo kimoja na kila mtu kugeukia upande wake.”

Rooney (siyo jina lake kamili) anasema kuna wakati mtu unaweza shindwa kuingia chooni kutokana na maji machafu kutapakaa kila kona na wakati mwingine chemba iliyopo chooni inakua na maji machafu ya kijani kutokana na kutofanyiwa usafi kwa muda mrefu.

bunge-3.jpg

Sehemu ya vyoo vinavyotumiwa na wasichana wa Shule ya Msingi Bunge iliyopo Manispaa ya Ilala. Picha na Aurea Simtowe.​

Licha ya kuwa vyoo hivyo husafishwa na moja ya wahudumu, Rooney anasema; “mtu mwenyewe anaesafisha vyoo mara nyingi amekuwa akisafisha vya walimu na kuacha vya wanafunzi.”

Foleni anayopanga Rooney wakati wa kwenda msalaani siyo ya bahati mbaya. Shule hiyo ni miongoni mwa zenye uhaba mkubwa wa vyoo nchini ikiwa na wanafunzi 2,155 wanaotumia matundu saba tu yanayofanya kazi kwa sasa.

Kati ya hayo, matundu matano ni kwa ajili ya wasichana huku wavulana zaidi ya 1,000 wakipambana katika mawili yaliyosalia jambo linalopoteza muda wa masomo na kuhatarisha afya zao.

Hii ina maana kuwa tundu moja la choo linatumiwa na wastani wa watoto 307 kinyume na utaratibu wa tundu moja kwa wavulana 25 na kwa wasichana 20.

Kilomita saba kutoka shule anayosoma Rooney, ipo shule ya Msingi Buguruni iliyopo kwenye eneo linalofahamika kukaliwa na watu wenye kipato cha chini.

Katika shule hiyo ya Buguruni anayosoma Omar Suleiman Omar, hali ni tofauti kidogo.

Tofauti na Bunge, Buguruni ina matundu 40 ya vyoo huku wanafunzi wakiwa 1,477 tu.

Hapa Buguruni tundu moja linatumika na wastani wa watoto 36 ikiwa ni ahueni takriban mara tisa ya wale wa Bunge licha ya kuwa bado kiwango hicho kipo juu kidogo ya utaratibu unaotakiwa.

“Ni mara chache sana kukuta foleni chooni kwetu,” anasema Omar.

“Matundu ya vyoo yapo na tunajitahidi kuyafanyia usafi kila siku kuendana na ratiba iliyowekwa tukisimamiwa na mwalimu wa zamu.”

Uhaba wa vyoo unaikabili Bunge angalau kidogo siyo miujiza kwa kuwa mkoa wa Dar es Salaam ni miongoni mwa yenye uhaba mkubwa wa vyoo katika shule za msingi za umma nchini ikishika nafasi ya pili baada ya Geita kwa mujibu wa Takwimu za msingi za elimu mwaka 2016.

Mikoa ya Kilimanjaro na Iringa Pekee ndio mikoa inayoonekana kuwa na afadhali katika idadi ya matundu ya choo huku kiwango cha watumiaji ikikikaribia kile kilichowekwa na Serikali yaani tundu moja la choo kutumiwa na wasichana 20 na 25 kwa wavulana.

CHANZO: Mwananchi
 
Back
Top Bottom