- Makada wake wakamatwa kwa kuchoma bendera za Chadema
Waliotiwa mbaroni juzi jioni ni Katibu wa Msaidizi wa CCM ambaye pia ni Mhasibu wa CCM Wilaya ya Sikonge, Bw. Bakari Luasa na Bw. Rajabu Said ambao walikamatwa katika kijiji cha Chagana Kata ya Itumba.
Viongozi hao, walikamatwa saa 5:00 asubuhi juzi muda mfupi kabla ya msafara wa mgombea wa CCM, Dkt. Dalaly Kafumu na Katibu Mkuu wa chama hicho, Bw. Wilson Mukama na viongozi wengine kuwasili eneo hilo.
Bw. Mukama na msafara wake walikuta tafrani baada ya wafuasi wa Chadema kuwashikilia viongozi hao na kuwadhiti hadi walipowakabidhi kwa polisi.
Makada hao wa CCM walipandishwa kwenye gari la polisi aina ya Toyota Land Cruiser yenye namba za usajili PT 1946 hadi Kituo cha Polisi mjini Igunga ambako walikabidhiwa kwa Mkuu wa Kitengo cha Tathmini, Ufuatiliaji na Upelelezi wa Makosa ya Jinai katika uchaguzi huu, Bw. Isaya Mngulu.
Wakazi wa kijiji hicho wakiwamo wafuasi wa Chadema walikuwa na marungu, mapanga na mikuki ili kuwashughulikia, lakini jitihada zilizofanywa na kiongozi mmoja wa Chadema, Bw. Kibende Mwang'ombe ziliwatuliza.
Mwang'ombe aliiambia Majira kuwa waliokamatwa walifika katika eneo hilo kufanya uhalifu wakiwa na mtu mwingine ambaye jina lake halikufamika mara moja, lakini alikimbia baada ya ugomvi kuanza.
"Siku zote CCM wemekuwa mabingwa wa kueneza siasa za propaganda kwamba Chadema tunafanya fujo, nadhani ninyi wenyewe mmejionea. Jambo lililonifurahisha ni kwamba viongozi waandamizi wa CCM wamejionea wenyewe," alisema Mwang'ombe.
Mwenyekiti wa Wazazi CCM Wilaya ya Igunga, Bw. Selemani Majilanga, aliwaomba wananchi na wafuasi wa Chadema wasiwafanyie fujo wahalifu hao.
"Nawaomba ndugu zangu wananchi msifanye fujo kwa watu hao, wako mikononi mwa polisi, basi acheni sheria ichukue mkondo wake, watashughulikiwa kwa taratibu zote zinazostahili," alisema Majilanga.
Baada ya watuhumiwa kuondolewa, mkutano huo, uliendelea huku, Bw. Mukama akijinadi kwa wananchi kuwa ametumwa na Rais Jakata Kikwete kuwaomba wananchi hao kumpa kura za ndiyo mgombea wa CCM, Dkt. Kafumu ili awe mbunge wao.
Kwa upende wake, Mratibu wa Kampeni wa CCM ambaye pia ni Katibu wa Fedha na Uchumi, Bw. Mwigulu Nchemba aliwataka wananchi kutokuchagua wapinzani kwa sababu hawana serikali.
Katika mkutano huo, mwananchi mmoja alilipandisha dumu la maji machafu lita 20 na kumuuliza mgombea wa CCM, Dkt. Kafumu atachukua hatua gani kuondoa adha ya kukosa maji iliyodumu miaka mingi.
"Nimekuletea maji haya unayoone mwenyewe, sisi tunakunywa maji machafua kiasi hiki, je, ukipata ubunge utafanyaje ili tuondokane na aibu hii ambayo sasa imeonekana kuwa ya kawaida kila kukicha," alihoji mwananchi huyo.
SOURCE: MAJIRA