nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
Monday, 26 September 2011 08:05 |
MWANANCHI wa Kitongoji cha Mwamsungu,Jimbo la Igunga, Nzile Faregaro, amembana Katibu mkuu mstaafu wa CCM, Philip Mangula, awahakikishie kuwa mgombea wao, Dk Dalaly Kafumu, hataiga hulka na tabia za mtangulizi wake, Rostam Aziz. Tukio lilitokea jana kwenye mkutano wa hadhara wa kampeni za CCM wa kinyanganyiro cha uchaguzi mdogo Jimbo la Igunga, ambao ulihudhuriwa pia na Naibu Waziri wa Uchukuzi, Dk Athuman Mfutakamba. Baada ya kumaliza kuhutubia, makada hao wa CCM waliruhusu maswali matatu ndipo muuliza swali wa tatu, Faregaro alipoibua hoja hiyo kwamba tangu wamchague Rostam hawajawahi kumwona kwa miaka 15. Tangu tumchague Rostam hajawahi kututembelea kwa miaka 15 sisi tutawapa kura, lakini tunataka mumlete mgombea hapa tumuulize maswali na atuhakikishie kama hatatutelekeza kama alivyofanya Rostam, alisema Faregaro. Akizungumza kwa hisia kali, mzee huyo aliongeza kuwa hata kama anatuona ni wajinga, lakini alitakiwa kuja tu siyo kuishia huko mjini na ndiyo maana tunamtaka Kafumu aje hapa tumuulize maswali. Hata hivyo, Dk Kafumu hakuwapo katika mkutano huo kutokana na utaratibu wa CCM, ambao wamejigawa makundi 12 kushambulia mikutano ya hadhara na Dk Kafumu alikuwa kwenye mkutano mwingine. Pia, Faregaro alitaka fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf) Sh30 milioni ambazo zimetolewa na Serikali kwa kitongoji hicho kujenga Lambo kwa ajili ya mifugo, zitolewe ili zitumike kwa kazi hiyo. Hata hivyo, swali hilo ambalo lilielekezwa meza kuu, lilijibiwa na Dk Mfutakamba ambaye aliwaahidi wananchi hao kumpeleka mgombea huyo, ili awahakikishie kuwa yeye ndiye mkombozi wa kero mbalimbali zinazowakabili. Kuhusu fedha za Tasaf, Dk Mfutakamba alisema masharti ya fedha hizo ni wananchi walitakiwa kuchangia asilimia 10 ya gharama za mradi ambazo ni Sh3 milioni, lakini hadi sasa wananchi wamechangia Sh1.5 milioni. Mzee mwingine, Mboje Mkete, yeye alienda mbali na kusema japokuwa watamchagua Dk Kafumu, lakini wanataka ikifika Oktoba 20, ambazo ni siku 18 baada ya uchaguzi ahakikishe malambo yote kijijini hapo yamejengwa. Awali, akihutubia mkutano huo, Mangula aliwataka wananchi wa jimbo hilo kuepuka kuingia katika mtego wa kuwa sehemu ya kuanzisha vurugu, akiwataka kusimama imara na mwanasiasa atakayewashawishi hivyo wamwambie hapana. Mangula alisema yapo mambo mazuri aliyoyaanzisha Rostam ikiwamo ujenzi wa sekondari na mwaka 1994, jimbo hilo lilikuwa na shule tatu, sasa lina shule 36 hivyo akawaomba wamchague Dk Kafumu ayaendeleze. |