Hotuba ya Balozi Seif alipofunga mkutano wa pili wa BLW

Kakke

JF-Expert Member
Dec 4, 2010
1,883
1,482
Wednesday, June 29, 2016

363.jpg


HOTUBA YA MAKAMU WA PILI WA RAIS WA ZANZIBAR, MHESHIMIWA BALOZI SEIF ALI IDDI YA KUFUNGA MKUTANO WA PILI WA BARAZA LA WAWAKILISHI, ZANZIBAR TAREHE 29 JUNI, 2016

UTANGULIZI:
Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kutujaalia uhai na afya njema na kutuwezesha kufanikiwa vizuri kushiriki na kukamilisha Mkutano huu wa Pili wa Baraza la Tisa la Wawakilishi ulioanza tarehe 18 Mei, 2016 kwa lengo la kujadili Bajeti ya Serikali yetu ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mwaka wa fedha 2016/2017. Kwa uwezo wake Mola Mtukufu, kazi zote zilizopangwa katika ratiba ya mkutano huu wa pili tumezikamilisha kwa mafanikio mkubwa.

Mheshimiwa Spika, shukrani maalum nazitoa kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, kwa kuendelea kuiongoza nchi yetu katika hali ya amani na utulivu. Tunamuomba Mwenyezi Mungu amzidishie uwezo, hekima na busara ili aendelee kuiongoza na kuzidi kuiletea maendeleo nchi yetu katika kipindi hiki cha pili cha uongozi wake.
Mheshimiwa Spika, kwa heshima kubwa, napenda kutoa shukurani zangu za dhati kwako wewe binafsi, Naibu Spika, Wenyeviti na wasaidizi wako wote kwa kukusaidia kuliendesha Baraza hili Tukufu kwa umahiri na umakini mkubwa. Pia, nawashukuru Waheshimiwa Wenyeviti na Wajumbe wa Kamati mbali mbali za Kudumu za Baraza hili kwa michango, ushauri na maelekezo yao kwa Serikali katika utekelezaji wa majukumu yake.

Mheshimiwa Spika, nawapongeza Waheshimiwa Wajumbe wote wa Baraza hili la Tisa la Wawakilishi, Mawaziri, na Naibu Mawaziri kwa umahiri wao mkubwa katika kuchangia mijadala na hoja mbali mbali ndani ya Baraza hili. Aidha, nawashukuru Makatibu Wakuu, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya na Watendaji wote wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuendelea kutekeleza majukumu yao ya kila siku kwa mafanikio makubwa.

Mheshimiwa Spika, nachukua pia fursa hii kuelezea kuridhika kwangu na upeo na uelewa mkubwa walionao Waheshimiwa Wawakilishi kwa jinsi walivyotoa michango ya kujenga na sio ya kubomoa, kushutumiana au kukomoana. Nawapongeza sana kwa uelewa na ukomavu wao kisiasa na jamii kubwa ya Wazanzibari na wengine wanajifunza kwa utendaji wetu vipi kiongozi anapaswa kuwa hasa anapojadili masuala ya wananchi. Katika kuchangia hoja mbali mbali za Serikali, wapo waliochangia kwa hamasa, wapo waliochangia kwa upole, wapo waliochangia kwa jazba na hata kulia lakini wote hao nia yao ni kuikosoa na kuishauri Serikali ili ifanye kazi zake kwa usahihi zaidi.

Mheshimiwa Spika, nimeona dalili ya baadhi yetu kutetea mambo ya kibinafsi kuliko yale ya wananchi walio wengi, hili naomba tuliache, tuwasilishe katika chombo chetu hichi mambo ambayo wananchi yanawagusa na ambayo wametutuma tuje kuyatetea, tupite kwa wananchi tujadiliane nao na mnachokubaliana nao ndicho tukiwasilishe katika Baraza hili Tukufu. Haitokuwa vyema tukaongea vitu ambavyo tukirudi Majimboni kwetu wananchi wakatueleza kuwa yale uliyokuwa unaongea Barazani sio shida zetu au sio tuliyoyapa kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii kuwaomba Waheshimiwa Wawakilishi wajitahidi kuwatumikia wananchi wao kwa nguvu zao zote na hasa wale walioshinda katika Majimbo ambayo kipindi cha nyuma yakishikiliwa na wawakilishi wa Chama cha Upinzani, ambao wengi wao hawakuwa wanawaletea maendeleo wananchi wao ambao wengi wao walihama katika Majimbo yao na kukimbilia mijini. Na baadhi yao kutoka Majimbo ya Pemba walikimbilia na kuhamia Unguja. Wananchi wa Majimbo hayo walikata tamaa na sasa nakuombeni sana mkae na wananchi hao na kuwarejeshea matumaini na pia waweze kuona faida ya kuwa na Wawakilishi kutoka CCM.

TAARIFA YA MAMBO MBALI MBALI:
(i) HALI YA KISIASA:
Mheshimiwa Spika, baada ya Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar kupitia Mwenyekiti wake kufuta matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2015 kufuatia kubainika kwa kasoro nyingi ambazo zingeyafanya matokeo hayo kutokuwa ya uhuru na haki, Katibu Mkuu wa Chama cha CUF Maalim Seif Sharif Hamad amekuwa akipita maeneo mbali mbali kuwadanganya wananchi hasa wanachama wa chama chake na Jumuiya za Kimataifa kwamba, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete alitoa amri kwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchanguzi Zanzibar, Mhe. Jecha Salum Jecha, kufuta matokeo hayo jambo ambalo sio la kweli, na kauli hiyo ilikuwa kama tusi kwa Dk. Shein, maana amemaanisha kuwa kama Dk. Kikwete asingemwamuru Mhe. Jecha kufuta uchaguzi, Dk. Shein angekubali kudhumuliwa. Hii ni porojo tu.

Mheshimiwa Spika, napenda ieleweke kuwa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ni chombo huru chenye mamlaka na kinafanya kazi zake bila ya kuingiliwa na mtu au chombo kingine chochote. Maamuzi ya kufuta matokeo hayo yalikuwa ni halali baada ya kubainika kwa kasoro nyingi, ukiukwaji mkubwa wa sheria na kanuni za uchaguzi hasa Kisiwani Pemba. Tume ya Uchaguzi inafanya kazi zake ili kusimamia haki na kuhakikisha matakwa na ridhaa za wananchi katika kuwachagua viongozi wanaowataka zinatimia bila ghilba na udanganyifu wowote.

(ii) ZIARA ZA MAALIM SEIF SHARIF HAMAD:
Mheshimiwa Spika, tokea kumalizika kwa uchaguzi wa marejeo uliofanyika tarehe 20 Machi, 2016 na CCM kupata ushindi wa kishindo, Katibu Mkuu wa Chama cha CUF, Seif Sharif Hamad pamoja na viongozi wengine wa chama hicho wamekuwa wakifanya ziara mbali mbali ndani na nje ya nchi. Serikali imezifuatilia kwa karibu ziara hizo na kubaini kwamba msingi wake ni kutapatapa kwa kiongozi huyu baada ya kushindwa uchaguzi huo wa marejeo. Ziara hizo zimekuwa ni muendelezo wa vitendo vya uchochezi na hujuma, kwani anayoyasema wakati wa ziara hizo yanaongeza chuki na uhasama miongoni mwa wananchi wa Zanzibar. Tunayaona au kuyasikia yanayotokea huko Pemba hivi sasa.

Mheshimiwa Spika, nawaomba wananchi wasibabaishwe na kauli hizo za Seif Sharif Hamad kwani haziwezi hata kidogo kuiteteresha Serikali halali inayoongozwa na Chama cha Mapinduzi iliyowekwa madarakani na wananchi wa Zanzibar katika uchaguzi wa marejeo uliofanyika tarehe 20 Machi, 2016. Wala kauli zao hizo haziwezi kututoa kwenye malengo yetu ya kuwaletea wananchi maendeleo. Uchaguzi huo aliukataa yeye mwenyewe na kilichobakia ni kusubiri uchaguzi mwengine hapo mwaka 2020 panapo majaaliwa. Huko nchi za nje nako alisikika akidai kuundwa kwa Serikali ya Mpito ya miezi sita itakayoongozwa na Mzanzibari asiyefungamana na upande wowote wa kisiasa, Zanzibar na baada ya hapo uitishwe Uchaguzi Mkuu utakaosimamiwa na Jumuiya au Taasisi ya Kimataifa. Huu ni upuuzi mwingine kwani jambo hilo haliwezekani kutokea hata siku moja. Tunachojua sisi ni kuwa uchaguzi umekwisha, uchaguzi mwingine hadi 2020. Kabla ya hapo hakuna Serikali ya Mpito wala ya Mpeta. Hapa ni Kazi tu ya kuwatumikia wananchi ya kuzitatua kero zao na kutekeleza ahadi tulizozitoa kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya 2015 – 2020.

(iii) MATUKIO YA UHALIFU NA HUJUMA:
Mheshimiwa Spika, nchi yetu imeshuhudia matukio mbali mbali ya uhalifu na hujuma yanayopangwa na kutekelezwa na baadhi ya wafuasi wa Chama cha Upinzani cha CUF wasioitakia mema nchi yetu, ikiwa ni utekelezaji wa maagizo ya viongozi wao ambao wana nia ya kuhatarisha hali ya amani na utulivu uliopo. Matukio hayo yamejitokeza kabla na baada ya uchaguzi wa marejeo uliofanyika tarehe 20 Machi, 2016, ikiwemo uchomaji moto nyumba, ofisi za CCM na vituo vya afya; wananchi kunyimwa au kubaguliwa kwenye huduma za kijamii; na kukata na kuharibu mikarafuu na mazao mengine, ikiwemo mpunga, muhogo, migomba na vipando vingine.

Mheshimiwa Spika, Serikali inasikitishwa sana na matukio hayo, ambayo sio tu yanaathiri wananchi walengwa, bali pia yanaleta athari kubwa za kimazingira kutokana na uharibifu mkubwa wa miti ya mikarafuu na mazao mengine. Wanaofanya vitendo hivi ni wahujumu uchumi na watakaopatikana ni bora kushitakiwa chini ya Sheria ya Uhujumu Uchumi.

Mheshimiwa Spika, uchunguzi uliofanywa na Jeshi la Polisi Zanzibar unaonyesha kwamba Chama cha CUF kimekuwa na mpango wa kuendeleza hujuma hizo katika maeneo mbali mbali, ikiwemo nyumba za Viongozi Waandamizi wa Serikali na Chama cha Mapinduzi. Kwa mujibu wa uchunguzi huo, vitendo hivi vinatokana na maelekezo ya Chama cha CUF yaliyotolewa na Katibu Mkuu wao, Seif Sharif Hamad. Aidha, upo ushahidi wa kutosha kwamba Seif Sharif Hamad amekuwa akitoa hotuba za uchochezi kupitia mikutano yake ya ndani aliyoifanya katika maeneo mbali mbali, hasa Kisiwani Pemba. Serikali inakamilisha taratibu za kuwachukulia hatua za kisheria wale wote waliohusika na vitendo hivyo. Wasije wakailalamikia Serikali kwa hatua itakazochukua.

Nichukue fursa hii kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kutoa pole kwa wananchi wa Pemba kwa madhila waliyoyapata ya kuharibiwa na kuchomewa nyumba zao, kukatiwa vipando vyao mbali mbali na kubaguliwa, Serikali iko pamoja nao. Serikali itawashughulikia wahalifu hao vipasavyo.

Mheshimiwa Spika, nawashukuru sana na kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri kwa kutoa ufafanuzi wa hoja zilizotolewa na kujibu maswali ya Waheshimiwa Wajumbe kwa ufasaha. Pia nawashukuru waandishi wa habari na wakalimani wa lugha ya alama kwa kazi yao nzuri ya kuwapatia taarifa wananchi kuhusu majadiliano ya Baraza katika mkutano huu. Shukrani maalum nazitoa kwa Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC) kwa kutangaza na kuonesha moja kwa moja (live) shughuli zote za mkutano huu bila kusita.

Mheshimiwa Spika, mwisho napenda kuvipongeza vyombo vyote vya ulinzi na usalama pamoja na Idara Maalum za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mchango wao mkubwa katika kudumisha usalama na utulivu uliopo hapa nchini.
60. Mheshimiwa Spika, zipo kauli zinazosambazwa kupitia mitandao ya kijamii kuwa Serikali itachinja ng’ombe waliowakamata na kuuza nyama kwa bei rahisi ya Shs. 3,000 kwa kilo na kutolewa tahadhari kuwa watu wasinunue nyama hiyo eti siyo halali na ni nyama ya kifo. Napenda kuweka bayana kuwa kauli hizo hazina ukweli wowote. Hakuna ng’ombe yoyote atakayechinjwa na Serikali na kuuzwa Maisara kwa bei rahisi. Huu ni uongo na uzushi mtupu. Vile vile kuna kauli nyeingine ya kuwazuia watoto wasiende kufurahi Mnazi Mmoja wakati wa Sikukuu eti kutatokea fujo na vurugu. Huu ni uongo mkubwa na uzushi usio na kifani. Serikali inawahakikishia wananchi kuwa hali ya nchi yetu iko salama na utulivu na itabaki hivyo siku zote. Kauli hizo ni propaganda za wapinzani kutaka kuwahamanisha wananchi wapenda amani. Wananchi wanahakikishiwa kuwa viwanja vyote vya sikukuu vitakuwa salama.

Mheshimiwa Spika, tukiwa tumo katika kumi la mwisho la Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, tunamuomba Mwenyezi Mungu atukubalie swaumu zetu na atujaaliye kumaliza faradhi hii kwa salama. Kwa vile hatutokaa tena katika kikao kama hiki kabla ya kumalizika mwezi Mtukufu wa Ramadhan, nachukua fursa hii kuwatakia Waheshimiwa Wawakilishi pamoja na wananchi wote sikukuu njema ya Eid-el-Fitri inayotarajiwa hivi karibuni INSHAALLAH. Kuluam wa Antum Bukheir.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo, sasa naomba kutoa hoja ya kuliakhirisha Baraza lako Tukufu hadi siku ya Jumatano, tarehe 21 Septemba, 2016 saa 3.00 barabara za asubuhi panapo majaaliwa.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.

Chanzo ZanziNews
 
wapinzani tuuuuuuuuuu sefu sharifu hamad ttuuuuuuu, maendeleo ya kujivunia yako wapiiiiiiii? bei za vitu zimepanda tusio penda siasa tunataka kujua kuhusu maendeleo tokea sheni aingie madaraka kwa second term
 
Seif kawakaa kooni.....hotuba ni kumsakama yeye badala ya maendelo ...na dubai walohadaa watu wao
 
Back
Top Bottom