Hivi Ndivyo Unavyoweza Kutajirika Kwa Kuanza Na Shilingi Elfu Moja

Makirita Amani

JF-Expert Member
Jun 6, 2012
1,781
3,074
Moja ya sababu kubwa ambayo watu wengi husema kwamba inawazuia kufanya biashara ni mtaji. Mimi huwa nakataa sana sababu hii kwa sababu haiwezekani leo huna mtaji, mwaka kesho huna mtaji na hata miaka mitano ijayo huna mtaji.

Nasema mtaji ni kigezo tu ambacho watu wengi hutumia kuficha sababu halisi ya kutokuingia kwenye biashara ambayo ni kutokujipanga na kutokuwa tayari.


Leo nakushirikisha siri moja ambayo itakuwezesha kufikia mafanikio makubwa sana japo utaanza kidogo. Kupitia siri hii unaweza kuanza na tsh elfu moja na baadae ukapata mtaji ambao utakuwezesha kufanya biashara kubwa. Pia tutaangalia kama ukianza na kiasi kikubwa kidogo itakavyokuwa bora zaidi.

ANGALIZO; Mambo utakayoyasoma hapa yatabadili kabisa maisha yako kama ukiyatumia. Ila kama utayasoma na kupita utaendelea kuwa na maisha magumu huku ukilalamika bila ya msaada wowote. Hivyo chukua hatua, huu ndio ukombozi wako.

Siri kubwa nitakayoizungumzia hapa ni kuweka akiba kidogo kidogo kila siku na kwa muda mrefu ili kuweza kuondoka kwenye tatizo la fedha uliloko nalo sasa. Na akiba hii hitaiweka benki ambako utawafaidisha sana na hela yako kuliwa na mfumuko wa bei, bali utaiweka kwenye mfuko wa dhamana ambao una uhakika wa kukua kwa asilimia sio chini ya kumi kwa mwaka. Mfano wa mfuko wa dhamana ni Umoja Fund wa UTT (Unit Trust of Tanzania) maarufu kama mfuko wa umoja au vipande vya umoja.


Kupitia mfuko huu unanunua vipande ambavyo vinakua kwa thamani kadiri muda unavyokwenda. Kwa mwaka vinakua sio chini ya asilimia kumi na mara nyingi inakuwa zaidi ya hapo. Hivyo hii ni njia nzuri sana ya wewe kukuza mtaji wako hata kama unaanzia sifuri.

Sasa tuone maajabu ya kuweka fedha kwa muda mrefu.

1. Kama utaanza kuweka tsh elfu moja kwa siku.
Naamini kama unasoma hapa huwezi kukosa tsh elfu moja kila siku. Hata uwe ni mmachinga, mama ntilie, au mpiga debe unaweza kupata tsh elfu moja kila siku. Usiidharau elfu moja hiyo maana ni njia yako ya kuelekea kwenye utajiri.


Kama kila siku utaweka tsh elfu moja, kwa mwezi itakuwa tsh elfu 30, kwa mwaka itakuwa tsh 360,000/=. Kama utaweka fedha hii kwenye mfuko unaokua kwa asilimia 10 kwa mwaka, kwa miaka mitano itakuwa tsh 2,997,403.20 hii ni sawa na tsh milioni tatu. Hiki ni kiasi ambacho huenda hujawahi kukipata kutoka kwenye vyanzo vyako mwenyewe ndani ya miaka mitano iliyopita.

Kama utaweka elfu moja hiyo kila siku kwa miaka kumi itakuwa tsh 7,244,967.43, milioni saba ni fedha ambayo huenda hujawahi kuota kuishika.

Kama bado ni kijana na ukaiweka fedha hii kwa miaka 20 itakuwa tsh 25,102,799.78(milioni 25) na ukiiweka kwa miaka 30 itakuwa tsh 71,421,417.80(milioni 71). Yaani kama wewe una miaka 35 au chini ya hapo, kama utaanza kuweka tsh elfu moja kila siku na ukaiweka fedha hii kwenye mfuko wa umoja utakapokuwa na miaka 60 utakuwa na tsh milioni sabini.

2. Kama utaanza na tsh elfu hamsini kwa mwezi.
Kama unafanya kazi ila una mshahara kidogo sana bado unaweza kujikusanya na kupata mtaji wa kutosha kukuondoa hapo ulipo. Kwa mfano kama mshahara wako uko kati ya laki mbili mpaka laki tano, kwa njia yoyote ile unaweza kujikaza na ukaweka pembeni tsh elfu 50 kila mwezi.

Kama fedha hii utaiweka kwenye mfuko wa umoja, kwa miaka mitano itakuwa tsh 4,995,672.00(milioni 5), miaka kumi tsh 12,074,945.71, miaka 20 tsh 41,837,999.64 na miaka 30 tsh 119,035,696.34. Milioni tano kwa miaka mitano, 12 kwa miaka kumi, 41 kwa miaka 20 na 119 kwa miaka 30 ni fedha ambazo unaweza kuanzia nazo na ukafanya mabadiliko makubwa kwenye maisha yako.

3. Kama utaanza na laki moja kwa mwezi.
Kama unafanya kazi na mshahara wako ni kati ya laki tano na milioni moja kwa mwezi, unaweza kujibana na kuweka pembeni tsh laki moja kila mwezi. Kama utaiweka fedha hii kwenye mfuko wa umoja unaokua kwa asilimia 10 kwa mwaka mambo yatakuwa hivi;

Miaka mitano tsh 9,991,344.00(milioni 10), miaka 10 tsh 24,149,891.43, miaka 20 tsh 83,675,999.27 na miaka 30 tsh 238,071,392.67. Milioni kumi kwa miaka 5, 24 kwa miaka 10, 83 kwa miaka 20 na hata milioni mia mbili na arobaini kwa miaka 30 ni fedha ambayo inaweza kubadili kabisa maisha yako kama utaanza kuweka tsh laki moja kila mwezi.


Hii ndio siri kubwa ninayokushirikisha leo na kama utaanza kuitumia leo, namaanisha leo hii utaona mabadiliko makubwa sana. Kama usipoitumia naomba unitafute tarehe 10/10/2019 (miaka mitano ijayo) na uniambie ni kipi kikubwa ulichofanya. Miaka mitano sio mingi kabisa rafiki yangu, kama unafikiri ni mingi kumbuka ni lini ulifanya uchaguzi mkuu na mwaka kesho ni uchaguzi mwingine.

Hoja yangu kubwa ni kwamba kama umeweza kuteseka kwenye kazi kwa miaka zaidi ya kumi na huoni mabadiliko makubwa kwa nini usijipe miaka kitano tu au kumi tu na uweke kiasi fulani cha akiba na baada ya hapo upate mtaji wa kuanzia?

Na katika miaka hii mitano au kumi ambayo mtaji wako unakua na unaendelea kuuweka, jifunze kuhusu biashara unayotaka kufanya. Jifunze kwa kujisomea, jifunze kwa kufanya utafiti na pia jifunze kwa kufanya kazi inayohusiana na biashara unayotaka kuja kufanya. Kama kila siku kwamiaka motano au kumi utajifunza kuhusiana na kitu unachotaka kufanya utaona fursa nyingi sana za wewe kutoka.

Uanzie wapi?
1. Leo hii nenda katika ofisi za UTT(kama upo dar nenda sukari house ghorofa ya kwanza, unaweza kutembelea tovuti yao www.utt-tz.com), jiandikishe kuwa mwanachama na watakupa utaratibu wa kuwa unatuma fedha zako hata kwa mpesa, hivyo huna haja ya kwenda benk au ofisini kila mara. Ukisema unasubiri jumatatu au mwisho wa mwezi tayari fursa hii imekupita, na miaka mitano ijayo utajuta sana.

2. Baada ya hapo weka tsh elfu moja pembeni kila siku, unaweza kuwa unaiweka kwenye mpesa halafu kila mwisho wa mwezi unatuma UTT tsh elfu 30. Pia unaweza kutuma zaidi ya hapo kulingana na mipango yako, hiyo 30 kwa mwezi ni kiwango cha chini ambacho kila mtu ambaye yuko makini na maisha yake anaweza kukiweka. Kama unataka kuweka kiwango tofauti na nilivyotumia hapo juu au kwa miaka tofauti bonyeza maandishi haya na utakuta fomula niliyotumia.

3. Wakati unaendelea kuweka fedha hizi na kuzikuza endelea kujifunza kuhusiana na biashara unayotaka kufanya. Unaweza kukaribia kwenye kundi letu la TANZANIA VORACIOUS READERS ambapo tunapanga kusoma vitabu 500 kwa miaka mitano(nitumie email kujua zaidi kuhusu kundi hilo, amakirita@gmail.com). Kama kwa miaka hii 5 utasoma vitabu 500 na wakati huo unaendelea kukuza mtaji, mambo yataanz akufunguka kabla hata hujafika miaka hiyo mitano.

Chukua hatua sasa hivi, kama unafikiri haiwezekani kaendelee kulalamika. Kama umechoka kulalamika huu ndio wakati wa kushika hatamu ya maisha yako.
Nakutakia kila la kheri katika safari yako ya kufikia mafanikio makubwa.

TUKO PAMOJA.
Endelea kutembelea AMKA MTANZANIA ili kujifunza zaidi.
 
Tuwe tunaongea vitu vinavyowezekana.Kuweka ela 1000 kila mwezi kwa miaka 30 haliwezekani.
Nasema aliwezekani sababu jamii yetu matatizo hayaishi ukiweka ela zikifika kiasi fulani lazima utatumia tu.

Hivyo kuweka 1000 kwa miaka 30 haliwezekani.

Pili kusoma vitabu 500 nalo haliwezekani katika jamii,muda wa kusoma vitabu 500 utaupata wap?

Pia ni kujichanganya na kudata.Kusoma vitabu ni vizuri lakin soma vitabu ambavyo vitakusaidia na vinaendana na kile unachotaka kukifanya.

kusoma vitabu 500 kwenye jamii yetu ni ngumu kwanza ni gharama na muda haupo.

Tuongee vitu vinavyowezekana siyo KUSADIKIKA
 
Kwenye biashara kuna kupata na kukosa,na ukitaka kufanikiwa siri ni kutokata tamaa.

Sasa endapo nikawekeza na baada ya hiyo miaka 10 nikatupia akiba yangu yote kwenye biashara alafu kwa bahati mbaya nikaangukia pua. Je nitakuwa na moyo kwa kuanza safari nyingine ya miaka 10???

Nimeona wastaafu waliotumia viinua mgongo vyao kufanya biashara wakati hawana uzoefu,wengi wao wamekufa kwa pressure baada ya mambo kuwa sio.
 
Kama unasema haiwezekani endelea kulalamikia maisha halafu baadae utatuambia kulalamika kwako kumekusaidia nini.

Miaka 20 au 30 nimetumia tu kuonesha ukuaji, target kubwa ni miaka mitano au kumi ambapo mabadiliko ya fedha yanakuwa sio makubwa sana na unaweza kuendelea kujifunza kuhusiana na biashara husika.

Milioni kumi ya mwaka 2009 na milioni kumi ya leo ina tofauti gani kwenye kuanzisha biashara? Ipo lakini sio kubwa sana kiasi cha kukufanya ushindwe kuanza biashara. Tatizo kubwa la watanzania ni kutokujifunza na kuishi kwa mazoea tu na mwisowe kusema kitu hakiwezekani kwa sababu wewe hujawahi kufanya au hujawahi kumuona mtu anafanya.

Kwa miaka mitatu iliyopita nimesoma vitabu karibu mia tatu, sasa unasema kwa kujiamini kabisa kwamba miatano haviwezekani?
Nakuambia uweke elfu moja pembeni, elfu moja ambayo ungekunywa soda isiyo na maana kwenye maisha yako au kutumia hovyo tu na baada ya muda itakua na kufikia kiwango kikubwa kidogo, unasema pia haiwezekani?

Naweza kukuambia neno moja tu, KAFE MASIKINI.
 
Kama unasema haiwezekani endelea kulalamikia maisha halafu baadae utatuambia kulalamika kwako kumekusaidia nini.
Miaka 20 au 30 nimetumia tu kuonesha ukuaji, target kubwa ni miaka mitano au kumi ambapo mabadiliko ya fedha yanakuwa sio makubwa sana na unaweza kuendelea kujifunza kuhusiana na biashara husika.
Milioni kumi ya mwaka 2009 na milioni kumi ya leo ina tofauti gani kwenye kuanzisha biashara? Ipo lakini sio kubwa sana kiasi cha kukufanya ushindwe kuanza biashara.
Tatizo kubwa la watanzania ni kutokujifunza na kuishi kwa mazoea tu na mwisowe kusema kitu hakiwezekani kwa sababu wewe hujawahi kufanya au hujawahi kumuona mtu anafanya.
Kwa miaka mitatu iliyopita nimesoma vitabu karibu mia tatu, sasa unasema kwa kujiamini kabisa kwamba miatano haviwezekani?
Nakuambia uweke elfu moja pembeni, elfu moja ambayo ungekunywa soda isiyo na maana kwenye maisha yako au kutumia hovyo tu na baada ya muda itakua na kufikia kiwango kikubwa kidogo, unasema pia haiwezekani?
Naweza kukuambia neno moja tu, KAFE MASIKINI.

Umasikini sifi nao lakini njia yako situmii samahani kwa hilo!
 
Kusoma vitabu 500 eti ili utajirike ni kujitafutia uchizi.Hawa matajiri tulionao wengi hawajasoma vitabu ata 20.Wengine hawajasoma kabisa.

Hiyo kuweka 1000 pia kwa miaka 30 ni ngumu haiwezekani hakuna mtanzania anaweza.

Hiyo ya vitabu 500 pia ni ngumu.unacomplicate maisha.

Ni vizuri mtu akasoma vitabu vichache vinavyoweza kumsaidia kulingana na fani yake au shuguli yake.

Pia kuweka Akiba ni muhimu lakin sio kwa njia ya Kusadikika yani elfu moja kwa miaka 30

Hii ni ngumu mzeee
 
Umasikini sifi nao lakini njia yako situmii samahani kwa hilo!

Mimi nimeweka vipande huko kwa kweli watu hawajui tu kuna faida na nikauliza dse stock of exchange wanasema watanzsnia wengi hawanufaiki na soko ls hisA ila wageni ndio zaid.kuna mtanzania aliweka kdogo kdgo akafikisha mil kumi baada ya miaka mitatu akapata mil120 anaitwa emiliani busara na kaandika vitabu vizur sana vya uwekezaji tafuta kwenye maduka pale mliman site na eagt city centre kwa pastor katunzi sabasaba utavikuta bei kuanzia elf tano ni vizur sana.
 
Mmmmh nikianza kuweka 1000 leo nikifikisha miaka 60 ntakuwa na mil.70.... Za nini? yani hapo maisha yangu yote nimekuwa maskini wa kutupwa then at 60 napata mil 70...what for?

Fanya kama umetoa mchango Wa harusi tu
 
hahahaha 1000 miaka 30? kwa mwaka hauishi lazma utumie hyo hela mtoa mada unless otherwise unaongelea watu wasiikua na uhitaji wa hela
 
Ila asante kwa ushauri wako endelea kutupa ushauri ila kwa ushauri huu wenye moyo mgumu na roho ngumu watajilipua kuufata.

Nakutakia kazi njema ya kuelimisha jamii na pia katika kazi zako binafsi.

Ubarikiwe mtoa mada

Mkuu nimekuambia usiseme haiwezekani sema wewe huwezi. Maana akati wewe unasema haiwezekani wenzako tunafanya hayo.

Asante nakutakia kazi njema pia.
TUKO PAMOJA.
 
Mkuu hii njia ni nzuri najua ingawa financial market yetu haijakua sana lakini faida ipo hasa kwa watu ambao soko wanalijua na ukuaji wa sector ya gas na mafuta utakuza sana soko la hisa hapa kwetu na njia nzuri ni kununua na kuuza kuliko kusubiri gawio watu tunakosa muda wa kujifunza jinsi ya kukuza mitaji kwa njia hii ni njia nzuri sana hasa miaka kama mitano ijayo naamini tutakua tumefika mbali sana lakini suala la kuweka buku buku daaaah ngumu jamani kuna mambo mengi hutokea hapa kati kati kwa sisi wenye kipato cha chini

Sasa kama unajua miaka mitano ijayo mambo yatakuwa mazuri kwenye soko la hisa umejiandaaje?

Kama una kipato kidogo kama unavyosema nakushauri sana uanze na hii buku buku. Hapa utakuza mtaji na baadae kuingia kwenye hisa. Sidhani kama unaweza kununua hisa kwa buku ndio maana nakushauri uanze kukuza mtaji kwa njia hii.

Sasa kataa halafu kesho kutwa tu 2019 utakuwa wa kwanza kulalamika kwamba wachina wanatajirikia kwenye nchi yako wakati wewe bosi wako anaendelea kukufanya mtumwa.
 
Nakuunga mkono, ushauri mzuri lakini mgumu kutekelezeka kwa akina siye tunaoishi kutoka mkononi kwenda mdomoni (from hand to mouth). Kuweka elfu zifike 30,000 kwa mwezi ndo uzitume wakati shida kibao zinakukabili, ila penye nia pana njia.
Mkuu hii njia ni nzuri najua ingawa financial market yetu haijakua sana lakini faida ipo hasa kwa watu ambao soko wanalijua na ukuaji wa sector ya gas na mafuta utakuza sana soko la hisa hapa kwetu na njia nzuri ni kununua na kuuza kuliko kusubiri gawio watu tunakosa muda wa kujifunza jinsi ya kukuza mitaji kwa njia hii ni njia nzuri sana hasa miaka kama mitano ijayo naamini tutakua tumefika mbali sana lakini suala la kuweka buku buku daaaah ngumu jamani kuna mambo mengi hutokea hapa kati kati kwa sisi wenye kipato cha chini
 
Back
Top Bottom