Hili la Ngulume ni ushahidi wa kilio cha wananchi

marshal

JF-Expert Member
Nov 1, 2010
353
157
Thursday, 11 November 2010 18:54 0diggsdigg

Dismas Lyassa
MWANZONI mwa wiki hii, gazeti hili liliripoti kwamba aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Mbalali, Mkoani Mbeya Hawa Ngulume, ni mgonjwa na amekosa msaada wa kupata tiba ya rufaa kubaini maradhi yanayomtesa.

Akizungumza na gazeti hili nyumbani kwake, Goba Kinzudi, Dar es Salaama, Ngulume ambaye ameshika wadhifa huo katika wilaya mbalimbali kwa miaka 18 alisema: "Nimeona nitumie chombo cha habari kufikisha ujumbe (wa ugonjwa) kabla sijafa.”

Alisema ameanza kuugua miezi mitatu iliyopita na kwamba sasa yuko hoi na hawezi kutembea bila kusaidiwa na hivyo kuiomba serikali imsaidie aweze kwenda kutibiwa nje ya nchi.
Unaweza kujiuliza, kwa nini atumie chombo cha habari kuomba msaada wa serikali kwani ameshindwa kuwapigia simu viongozi wake na hata wa CCM ambako ni kada mwandamizi?

Jibu ni kwamba tayari alishafanya mawasiliano hayo lakini hakufanikiwa kuonana na viongozi. Kama alivyonukuliwa, Ngulume alisema: “Nilipeleka taarifa kwenye chama changu kwamba ninaumwa nahitaji msaada, lakini sikujibiwa; pia nimefanya juhudi za kutaka kumwona Waziri Mkuu ili anisaidie, juhudi hazikuzaa matunda. Nimeona nitumie chombo cha habari kufikisha ujumbe kabla sijafa.”

Ngulume alianza kusumbuliwa na mapafu mara baada ya kumalizika kwa mchakato wa kura za maoni za chama hicho. Alikuwa miongoni mwa wana CCM waliokuwa wamejitokeza kuomba ridhaa ya chama hicho kuwa mgombea ubunge katika Jimbo la Singida Mjini na kushindwa na Mohammed Dewji aliyekuwa akitetea nafasi hiyo.

Baada ya kushindwa, alirejea Dar es Salaam na siku chache baadaye alianza kuugua. Alikaririwa akisema kuwa amekuwa akitibiwa katika Hospitali za Lugalo, IMTU na Ocean Road zote za Dar es Salaam lakini hali yake imekuwa ikiendelea kudorora.

“Kuna kipimo ambacho nilitakiwa kuwekewa kwenye kinywa katika Hospitali ya Ocean Road ili kiweze kubaini kama kwenye mapafu kuna maji au la, ilishindikana kwa sababu ya kukosa pumzi na hawana kipimo cha aina nyingine.”

Anasema alishauriwa kwamba aende India ambako kuna vipimo vya aina nyingi ili kuweza kubaini maradhi yanayomsumbua.

Ngulume amewahi kushika wadhifa huo katika wilaya kadhaa zikiwemo za Bagamoyo, Kinondoni na Kibaha hivyo kumfanya kuwa maarufu na mwenye uzoefu mkubwa katika kushughulikia kero na mahitaji ya wananchi.

Nimefuatilia mrejesho wa wananchi baada ya kuandikwa kwa taarifa hii ya kusikitisha. Wapo walioungana na wenzao kumsikitikia mama huyu na kuiomba serikali ikumbuke mchango wake alioutoa kuitumikia nchi hii kwa kumpatia matibabu.

Lakini wapo pia ambao pamoja na kumsikitikia walisema hicho ni kipimo tosha kwamba kua tatizo kubwa la utoaji wa huduma za afya na jamii nchini. Wanasema kama kiongozi mkubwa kama Ngulume analia kwa kukosa huduma ya matibabu, hali ikoje katika vijiji vya wilaya alizokuwa akimwakilisha Rais?

Kumekuwa na malalamiko mengi juu ya huduma mbovu za afya zinazotolewa kwa umma. Pia kumekuwa na malalamiko juu ya huduma hizo kutolewa ama kwa rushwa au kujuana jambo ambalo limekuwa likiwakatisha tamaa wananchi na kutoona umuhimu wa kwenda hospitali.

Ngulume anathibitisha hili aliposema kwamba alipoteza muda mwingi katika Hospitali ya Taifa Muhimbili ambako madaktari na wauguzi walikuwa wakimpita bila ya kumpatia msaada wowote... “Ndipo mtu mmoja anayenifahamu aliyekuwa akipita nilipoketi, akanisalimia kwa kuniita mheshimiwa. Muuguzi mmoja jina ninalihifadhi akaja kutaka kunihudumia, nikamwambia ina maana siwezi kupata huduma hadi niwe mheshimiwa, nikaondoka kwa hasira."

Mikakati mingi ya kusaidia sekta ya afya ni kama imeshindwa kuleta faraja kwa walio wengi. Haya anayokumbana nayo Ngulume leo yalikuwepo tangu enzi na enzi, ni bahati mbaya tu kwamba amekumbana nayo katika kipindi hiki kigumu kwake.

Wananchi mijini na vijijini wanalia kila kukicha si kwenye mikutano ya hadhara, wanapokuwa hospitali na hata kupitia vyombo vya habari kama alivyofanya Ngulume.

Hapa ikumbukwe kwamba tatizo halipo katika ukosefu wa huduma tu, hata pale ambako inapatikana, utoaji wake umekuwa kero na usumbufu mkubwa. Angalau Ngulume ameliona hilo hapo Muhimbili lakini hayo ni mambo ya kawaida kwa wagonjwa katika sehemu karibu zote zinazotoa huduma ya afya ya umma.

Haya ndiyo mambo ambayo tunaamini kwamba wabunge wetu watayazungumza kwa uchungu na kutoa mifano hai kama huu wa Ngulume ili kuwapunguzia wananchi matatizo yanayowakabili. Wala hatutegemei katika kipindi hiki kwamba watazungumzia posho na marupurupu yao kabla ya kupatia ufumbuzi matatizo ya msingi yanayowakabili wananchi kama haya.

Lakini pamoja na serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), kushtuka na kuahidi kumsaidia kiongozi huyo wa zamani, umefika wakati kwa serikali kuangalia jinsi ya kuwahudumia viongozi na wananchi wake.

Haileti picha nzuri kusikia kilio cha mama huyu kupitia katika vymbo vya habari na ndiyo maana wengi walijiuliza kwamba ikiwa mtu ambaye alishika wadhifa wa ukuu wa wilaya tena chini ya mwaka mmoja tu analalamika, hali ikoje kwa watu kama sisi!
Dismas Lyassa ni mwandishi wa makala gazeti la Mwananchi
 
Hiyo ndio serikali ya CCM, ukisha toka ndio umetoka; wamekuwa na tabia za wahindi ambao huwathamini "GORO" pale tu wanapokuwa na shida lakini baada yakutimiza matakwa yao basi hawana tena na habari nao!!
 
Wabunge wetu wapya wanapaswa kukumbushwa kuhusu suala hili ili wapayuke ndani ya jengo na serikali ifanye jitihada za kuboresha huduma ya afya.

Wakati Ngulume akiwa DC hakuweza kuuona uozo uliopo kwenye sekta ya afya na kama aliuona aliendelea kukaa kimya ili asiwaudhi wakubwa zake. Sasa analipa gharama. Nyerere alisema makosa mengine adhabu zake zinapatikana hapahapa duniani. Nafasi za uongozi alizokuwa nazo Bi. Hawa Ngulume kwenye ngazi ya wilaya hakuzitumia ipasavyo kuboresha huduma ya afya ili kuokoa maisha ya watanzania. Jambo muhimu tunalopenda atambue ni kwamba hiyo ni miongoni mwa shida na karaha wanazokumbana nazo wananchi wa kawaida mitaani.
 
Back
Top Bottom