Mtambuzi
Platinum Member
- Oct 29, 2008
- 8,810
- 15,398
Kuna hii tabia ya toka zamani ya wazazi au mzazi mmoja kukataa kumkubali mpenzi wa binti yao ambayo limekuwa kama limepitwa na wakati. Lakini wapo baadhi ya wazazi wanaishi katika zama za giza wakiamini kwamba bado wanayo mamlaka ya kuwachagulia mabinti zao wenza.
Kwa miaka mingi sana karne na karne mtoto wa kike amekuwa kama bidhaa ya kesho ambayo itakuja kuuzwa wakati ukifika lakini siku hizi biashara hiyo imekuwa ikifanywa kitaalamu zaidi kwa kigezo cha kuipandisha thamani kabla ya kuwekwa sokoni.
Zamani mtoto wa kike hakuwa na umuhimu wa kupewa elimu kwa sababu alichukuliwa kama mtu wa kuolewa na wazazi kulipwa mahari. Kulikuwa na familia ambazo ili mtoto wa kiume amudu kuoa ilibidi wazazi wasubiri binti yao apate mchumba au kulazimishiwa ndoa ili wapate mahari ya kaka yake kuoa. jambo hili lilikuwepo na hadi sasa kuna baadhi ya makabila yanaendelea na utamaduni huu japo kwa siri sana.
Hivi sasa wazazi wengi wamebadilika na kuwapeleka watoto wa kike shule, wengi tunadhani lengo ni kumwezesha binti ili aweze kumudu maisha mbele ya safari bila kuwategemea wazazi. Inawezekana ni kweli lakini wapo wazazi ambao kuwapeleka watoto wa kike shule ni katika kujihami kwamba wasipoolewa basi wataweza kuwasitiri uzeeni kwa kuwasaidia kimaisha pindi wakistaafu.
Ni kweli watoto wanayo haki ya kuwasaidia wazazi wao, maana jambo hilo limezungumzwa hata kwenye vitabu vya dini, lakini kuna agenda nyingine imejificha kwa baadhi ya wazazi. Nayo ni ile ya kumpandisha binti yao thamani ili akipata elimu ya juu hata akiolewa basi atapata mtu mwenye fedha au tajiri au anayetokea kwenye familia ya kisomi na yenye kujimudu kimaisha.
Hizi ni ndoto za baadhi ya wazazi wengi na ukitaka kuona hasira zao, ni pale binti yao atakapoleta mwanaume asiye na mbele wala nyuma kwa maana ya kwamba siyo msomi na anatoka katika familia duni. haijalishi wamependana kiasi gani, wazazi wanachojali ni maslahi yao zaidi. kwenye akili yao ni kwamba binti yao atakwenda kuinufaisha familia ya mumewe.
Naamini humu jukwaani wapo baadhi yetu wamewahi kupambana na visa hivi vya wazazi katika kipindi cha kutafuta mwenza au labda wana hizo changamoto wakati huu. lakini pia wapo ambao labda mpaka sasa hawajaolewa kwa sababu ya kukataliwa wachumba wanaowapeleka kwa wazazi wao mpaka umri ukawatupa mkono na hivi sasa wamebaki kuwa single mother kwa kuzaa bila ndoa au hata mtoto hawana.
Zipo sababu nyingi lakini nitataja chache zinazosababisha wazazi kuwakataa wachumba wa mabinti zao.
1.Wanamuona binti yao kama bidhaa waliyowekeza.
Hii nimeizungumza hapo juu. Ni kweli wazazi wametumia pesa zao nyingi tena kwa kujinyima kwa jasho na damu kuhakikisha binti yao anapata elimu iliyo bora halafu anaolewa na mwanaume ambaye huenda atamzuia kufanya kazi na kumgeuza kuwa mama wa nyumbani. Hilo ni jambo ambalo linawatia hofu wazazi wengi pale wanapopelekewa mchumba na mabinti zao.
2.Mvulana yuko tofauti na sifa wanazotaka
Wazazi kwa kumwangalia binti yao wanajua ni mwanaume gani anaweza kumfaa binti yao, wanakuwa na vigezo vyao huko kichwani, hii wanayo wazazi wengi. Sasa ikitokea umemleta mtu ambaye hafikii vile vigezo walivyovitarajia wataanza sarakasi na kama mwanamke asipokuwa makini na mpambanaji hatoolewa na mwanaume anayemtaka.
3. Ile kujua kwamba binti yao keshamegwa...
Duh, hili nalo ni tatizo kwa baadhi ya wazazi. Kuna baadhi ya wazazi bado wanadhani kwamba binti zao wanaishi kama malaika. Kwa kuwa labda wao walikuja kufanya tendo la ndoa baada ya kufunga ndoa takatifu wanatarajia mabinti zao wawe kama wao. Kwa vile hivi sasa uchumba kwa watoto wetu unakwenda mbali zaidi kwa kushiriki tendo mapema kabla hata ya kupelekana kwa wazazi kwa hiyo kitendo cha kumtambulisha kinawapa picha kwamba binti yao keshamegwa na kuna baadhi ya wazazi jambo hilo linawaumiza sana ndani kwa ndani hususan kama kijana wanamuona kama asiyekidhi viwango vyao
4.Kuna chuki za kifamilia au ukoo wa mwanaume
Kuna wakati binti anaweza kumleta mwanaume wmenye sifa zote ambazo hata wazazi wamezikubali lakini kunatokea kikwazo. Kuliwahi kutokea ugomvi wa kiukoo zama za kale za vizazi kumi vilivyopita ambavyo hata wewe huvijui na katika ugomvi huo mzee mmopja wa ukoo akatoa kauli kwamba ukoo huu asitokee yeyote kuchangamana nao iwe ni urafiki au kuoleana na wazazi wakaishi na jambo hilo kwa karne, sasa binti anakatiliwa penzi kwa hadithi za alfu lela ulela na ndoa inaota mbawa. lakini pia yako maugomvi ya kifamilia katika kugombea mipaka ya shamba, kuibiana mifugo, kudhulumiana katika biashara nk, yote haya yanaweza kuathiri mahusiana ya mabinti iwapo wataangukia kwenye mapenzi na wanaume wanaotokea kwenye familia zisizokubalika kiukoo au kifamilia.
5. Mwanaume hana kazi ya maana
Kuna wazazi ukishawatamkia una mchumba swali la kwanza ni anafanya kazi gani. Mabinti wengi hukataliwa kuleta wachumba wanaowapenda kwa sababu kazi wanazofanya hazikidhi viwango wanavyotaka wazazi. Kuna visa vingi sana vya namna hii.
6. Mwanaume aliwahi kuwa na mahusiano na mwanamke wanayemfahamu
Ujana maji ya moto, vijana hususan wa kiume wakishabalehe huwa na mihemko ya kutembea na wanawake ili kukidhi mahitaji ya kimwili. wakati huo vijana hupenda kuonyesha ushujaa na siku hizi huweza kutembea na wanawake waliowazidi umri na wakati mwingine kama mama zao. sasa itokee mama wa binti akajua kijana aliwahi kuwa na uhusiano na shogake au mfanyakazi mwenzie. jambo hilo litaleta shida ile mbaya.
Naomba niwaachie na nyie mtaje sababu mnazozijua...