Hii ndiyo siri ya Chama Cha Mapinduzi (CCM)

Vancomycin

Senior Member
Jan 7, 2011
171
111

M. M. Mwanakijiji

amka2.gif

KAMA wewe ni mwanachama au umewahi kuwa mwanachama wa Chama Cha Mapinduzi, usiendelee kusoma makala hii. Unaweza ukajikuta unashikilia “Roho Mkononi.” Makala hii imewalenga wale wote ambao hawajui siri kubwa ya CCM, siri ambayo leo nitaifunua. Kwa vile wana CCM wenyewe wanaijua siri hii, hivyo kitendo changu cha kuiweka hadharani leo ni kama vile mtu kutoboa siri ya sanaa ya mazingaombwe na kuvunja mwiko wa usiri unaotawala fani hiyo.
Hivyo, kwa wale wana CCM mtajitendea hisani kubwa kama mtaacha kuendelea kusoma makala hii kwa sababu kuendelea kuisoma kunaweza kukusababishia chuki, hasira, kero, n.k. dhidi ya mwandishi. Ni onyo hilo.

Chama Cha Mapinduzi kinataka wananchi wajue mambo mengi sana. Kinataka wajue kuwa ni chama safi, ni chama ambacho kinapigana na ufisadi, na ndicho ambacho kimefungua milango ya “maendeleo” nchini. Kinawapenda wananchi “wafumbue macho” na kuona mafanikio ya aina mbalimbali ambayo yametokea nchini chini ya utawala wa serikali yake.
Mara nyingi viongozi wake wamekuwa wakisisitiza kuwa asiyeona maendeleo ambayo yametokana na utawala wa CCM, basi huyo si mkweli kwani mtu yeyote anaweza kuona maendeleo hayo na kuyahusisha na utawala wa Chama Cha Mapinduzi. Haya yote serikali ya CCM inataka ujue.

Hata hivyo, kuna mambo ambayo CCM haitaki wananchi wajue kwani ni kama siri ya familia ambayo haitakiwi kutoka “nje” mitaani. Ni kama vitu vinavyofanywa “Nyuma ya Mapazia.” Ni jambo la siri kubwa ambalo endapo Watanzania watalijua, kwa hakika linaweza kusababisha matatizo makubwa kwa Chama Cha Mapinduzi.

Jambo hili CCM inajitahidi kila kukicha kulificha kama mtu afichaye hazina aliyoipata kwa taabu. Hivyo, juhudi zozote za kutoa siri hii ambayo CCM haitaki itoke na kupokelewa, zitakumbana na upinzani mkali, kejeli, vitisho, dharau na hata uadui wa wazi. Hiki wanachokificha ndiyo siri kubwa ya familia ya CCM, siri ambayo leo tutaiweka wazi ili wananchi wajue nini kinaendelea.

Chama Cha Mapinduzi hakitaki wananchi wajue kuwa ni kutokana na uongozi wake, sera, utendaji, na mwelekeo wake ndiyo sababu ya kuwa na migongano tunayoishuhudia leo hii kitaifa.

Ni kutokana na utawala wa CCM, ndiyo maana hadi leo hii Jiji la Dar es Salaam limeshindwa kuweka mfumo mzuri wa maji taka ambao ungeondoa kabisa tatizo la mafuriko katika barabara zetu na kulifanya Jiji la Dar es Salaam kuendelea kupendeza, siyo kwa kwa kuwa na majengo marefu tu yenye rangi nzuri lakini likiwa na mazingira mazuri na ya kuvutia hata wakati wa mvua! Kukosekana kwa miundombinu mizuri ya maji taka karibu miaka 50 ya utawala wa CCM ni matokeo ya chama hicho na serikali yake. Hili hawataki watu wajue.

Chama Cha Mapinduzi hakitaki wananchi wajue kuwa tatizo la utoaji mikopo na upatikanaji elimu ya juu nchini ni matokeo ya sera, na mwelekeo wa serikali iliyoundwa na chama hicho.

Leo hii tunavyozungumza, yawezekana utakuwa umeshasikia kuwa baadhi ya wanafunzi wamepiga kambi katika ofisi ya bodi ya mikopo wakikata rufaa kupinga walivyoenguliwa kwenye mikopo licha ya kuwa na sifa.

Badala yake watoto wa vigogo ambao hawakupaswa kupata mikopo hiyo, ndiyo waliofanikiwa kupata na kuwaacha watoto wa masikini wakiendelea kutaabika.

Matatizo ya elimu ya juu leo hii nchini hayakuletwa kama zinavyoletwa “Salamu toka Kuzimu.” Matatizo haya hayakutumwa na “Malaika wa Shetani,” bali ni matatizo ambayo yametokana na uongozi wa kisiasa wa Chama tawala Cha Mapinduzi. Kwa muda mrefu sasa sisi wengine tumepigia kelele suala la bodi ya mikopo, na jinsi gani bodi hiyo imeoza na ina kila harufu ya ufisadi. Tulipopiga kelele baadhi ya watu walituona tuna “Roho ya Paka.” Walituona kama watu ambao tunajaribu kutafuta sifa au kujaribu kudhalilisha watu fulanifulani.

Hata hivyo, miaka miwili baadaye ukweli unazidi kudhihirika kuwa serikali ya CCM imetelekeza elimu ya juu na badala yake imeiacha idode kwa kufuata sera ambazo hazifanyi kazi, za kibabe na ambazo msingi wake ni ubaguzi wa hali ya maisha ya watu.

Mara nyingi msemo wa viongozi wa serikali ya CCM ni kuwa leo hii Tanzania hatuwezi kutoa elimu ya juu bure. Kuna baadhi ya watu wanataka watu waamini hivyo. Ukweli ni kwamba, bado Tanzania tungekuwa na viongozi wazuri, wenye maono ya mbali; na wenye ujasiri wa maamuzi, tungeweza kabisa kutoa elimu ya juu kwa kila kijana wa Kitanzania.

Tatizo la elimu ya juu nchini siyo suala la uwezo hata kidogo bali ni suala la uamuzi.
Juni mwaka huu, Chuo Kikuu cha Dodoma kilifungwa, wanafunzi walitimuliwa na serikali ikajisifu kwa kukaza uzi uleule. Hata hivyo walichokifanya kilijulikana, nacho ni kuwa serikali ya Chama cha Mapinduzi haina nia ya kutatua matatizo ya elimu ya juu. Nimebahatika kuona ripoti iliyotathmini matatizo ya taasisi za elimu ya juu ambayo ilikuwa imekusudia kutafuta chanzo cha migomo mbalimbali ambayo imekuwa ikijirudia rudia.

Mara nyingi migomo hii imewafanya wanafunzi wa vyuo vyetu vya elimu ya juu wajisikie kama vile wamo “Mikononi mwa Nunda.”
Ripoti hiyo ambayo unaweza kuisoma kwenye mwanakijiji.com inaeleza kwa undani kabisa hali ilivyo kwenye vyuo vyetu vikuu na kutoa mapendekezo ya hatua gani zichukuliwe kukabiliana na matatizo mbalimbali. Hata hivyo kama ilivyokuwa ripoti nyingine zinazotolewa na serikali ya CCM, ilibakia kuwa ni ripoti tu ambayo haijafanyiwa kazi inavyostahili. Hii iripoti ilikabidhiwa kwa waziri tarehe 1 Juni, 2004. Leo hii miaka minane baadaye imefichwa kabatini na serikali ya CCM inaendelea kutumia mabavu ya kunyamazisha sauti za wanafunzi.
Kitu ambacho serikali hii haitaki watu wajue ni kuwa haina uwezo, nia, au ujasiri wa kukabiliana na matatizo ya elimu ya juu nchini. Ni rahisi zaidi kwa viongozi wa serikali kutumia nguvu ya polisi na kukamata watu usiku na kuwapeleka mahakamani kwa mbwembwe kuliko kutokaa chini na kukabiliana na matatizo ya wanafunzi.

Leo hii tunaishi kama tuko kwenye “Dimbwi la Damu” ya ufisadi. Ukiangalia kwa harakaharaka unaweza kufurahia kusikia watuhumiwa wa wizi wa fedha za EPA, wamefikishwa mahakamani. Kuna watu ambao wanatarajia wananchi watoe pongezi au kuonesha kuridhika na viini macho hivyo. Ukweli ni kuwa serikali ya CCM haijaamua kushughulikia matatizo ya benki kuu na ufisadi uliokithiri pale na matokeo yake wamechagua “ka akaunti” ka EPA kuwa kama geresha ya utawala wa sheria.

Serikali hiyohiyo inajua kabisa ni mambo mangapi ya kifisadi yametokea benki kuu na ambayo hata kuanza kuyachunguza hasa haijaanza. Suala la Mwananchi Gold, Deep Green Finance, Meremeta, Minara Miwili ya Benki Kuu, ni mfano tu wa matatizo ambayo gharama yake ni mara nyingi ya ‘tujisenti’ tulichotwa benki kuu. Hili serikali ya CCM haitaki wananchi wajue.

Chama Cha Mapinduzi na serikali yake kimeshindwa kuonyesha uongozi wa msingi katika kuleta matumaini kwa wananchi hasa kwa kusimamia utawala wa sheria. Leo hii sheria zetu zinafanywa zionekane kuwa ni za upendeleo kwa watu wachache, huku watu wengine wakijifanya kuwa ni miungu watu.

Mara kadhaa mwaka huu, Jeshi letu la Polisi ambalo liko chini ya serikali inayoongozwa na Chama Cha Mapinduzi, limeendelea na unyanyasaji kwa wananchi kwa kukamata watu kinyume na sheria na kuwaweka kizuizini. Nakumbuka jinsi yule mlemavu alivyoswekwa lupango kwa kosa la kutaka kufuatilia ahadi ya rais wake.

Ina maana kuwa katika utawala wa serikali hii ya CCM bado wananchi wanaishi kwa hisani ya watawala kwani watawala kwa kutumia vyombo vyao vya dola, wamejishawishi kuamini kuwa wanaweza kufanya lolote lile, kwa mtu yeyote yule na jaribio lolote lile la kuwahoji litachukuliwa kama ni “kupanda chuki, kuleta uchochezi na kutishia amani!”
Ndugu zangu, serikali ya CCM, ndiyo chanzo cha migomo hiyo kwani ni wao pekee wenye uwezo wa kutafuta suluhisho la kweli. Hivi ni kwanini hadi watu watishie mgomo ndiyo uhakiki wa madai ya walimu unafanywa tena kwa kasi ya ajabu? Ni kwanini hadi watu watishie migomo ndio serikali inaingilia Shirika la Reli?

Je, wakati umefika sasa kwa watumishi wa ATCL nao kugoma ili serikali iingilie kati? Je, wakati umefika kwa wananchi wa Tabora kuanza kuandamana labda serikali itakumbuka kuna watoto 19 waliokufa kizembe kwenye jengo la NSSF?

Wakati umefika tusizungushane na kuhadaiana; kama mafanikio yaliyopo leo Tanzania ni matokeo ya sera nzuri na uongozi mzuri wa CCM basi matatizo yaliyopo nayo ni lazima wawe tayari kuyakubali kuwa yametokana na sera na uongozi wao mbaya. Haiwezekani kocha apewe sifa wakati timu imeshinda lakini wakati timu ikifungwa tuanze kutafuta wachawi!

Chama Cha Mapinduzi ndicho kinahusiana moja kwa moja na utendaji kazi wa taasisi za serikali. Taasisi hizi ni zile ambazo unaweza kuziona hata “Dar es Salaam usiku,” zote zinahusiana moja kwa moja na chama tawala.

Hata hivyo, swali kubwa ambalo sisi sote tunakabiliwa nalo ni kuwa, kama kweli tunataka kuikabili CCM kama ilivyo na kuweza kuisababisha ibadilike, yawezekana tukarudi na akili zetu, lakini je, “Tutarudi na roho zetu”?

Kama itakuwa hivyo, nina uhakika Watanzania wote siku moja watatambua ni kwa kiasi gani Chama Cha Mapinduzi kimekwaza kasi ya mafanikio na maendeleo ya taifa letu. Na siku hiyo ambapo Watanzania watakaoweza kuibadili CCM kwa chama kingine kuweza kushika hatamu za uongozi wa taifa, hapo ndipo kwa hakika sisi sote tutafurahia “Zawadi ya Ushindi.” Ushindi ambao wengi wetu tunauongojea na kuufanyia kazi; ushindi ambao kwa hakika utakuwa ni ushindi mnono tena mtamu.
Hii ndiyo siri; siri ambayo Chama Cha Mapinduzi hakitaki wananchi wajue kuwa matatizo yanayotokea sasa ambayo tukiyaorodhesha yatajaza juzuu, ni matokeo ya utawala wa Chama Cha Mapinduzi. Wananchi watambue kuwa wakati wowote viongozi wa CCM wanajaribu kukana kuwa CCM haijamtuma mtu kufanya ufisadi; wanajaribu kuruka kitu ambacho hakiwezekaniki.

Ni rahisi kwa mama kumkana mtoto wake kuliko kwa CCM kukana ufisadi nchini. Ni mpaka watakapokubali kuwa wao ni sehemu ya tatizo, hapo ndipo chama cha Mwalimu kitakapoanza kweli kujisafisha kutoka ndani. Kwa sasa hivi, hawataki kujiangalia kuwa yawezekana tunachokiona huku nje ni dalili tu ya kile kilichomo ndani.
 
Good analysis.
One day in history, one philosopher named MALCOLM X Uttered these words "...nobody can give you freedom, nobody can give you equality or even justice. If you are a man take it..."

I like these words and what this analysis depicts, it is high time CCM to call a spade a spade and not a big spoon
 
nimesoma kwa makini ndugu na kugundua kuna logic hapo! ccm hawapendi kabisaaaaa wananchi wajue kuwa kuna mambo wameshindwa kutokana na "ulegelege wao" unaozaa viongozi na serikali legelege au kwa msamiati mzuri "serikali rojorojo"!
 
Nimeipenda hii.
Bold and clear.
Serikali ambayo mpaka itishiwe kwa mgomo ndipo inapoweza kufanya kazi. What a shame.
 
Wakati umefika tusizungushane na kuhadaiana; kama mafanikio yaliyopo leo Tanzania ni matokeo ya sera nzuri na uongozi mzuri wa CCM basi matatizo yaliyopo nayo ni lazima wawe tayari kuyakubali kuwa yametokana na sera na uongozi wao mbaya. Haiwezekani kocha apewe sifa wakati timu imeshinda lakini wakati timu ikifungwa tuanze kutafuta wachawi!

Amen, kuna wakati huwa unaamua kuwa fair.
 
CCM sasa hvi haina mwelekeo wowote ule imeshashindwa kwa kila kitu wanachokifanya sa hvi ni kufuata nyendo za CHADEMA kiujanja ujanja hvi,na wanataka waonekane kwamba hawazifuati. Mfan mzuri ni Magamba ambayo wanajivua bila siku zao za kuyafua hazijafika.. Lakini ukiangalia chanzo ni taarifa mbaya zilizotoka CDM kuhusu wao.... Naisuburi kwa hamu 2015 Mungu atujalie tufany maamuzi sahihi. 2mewachokaaaaaaaa CCM
 
Sasa hapo kuna siri yoyote uliyotoa au ni mwendelezo wa makelele ya Slaa anapokuwa jukwaani? We Mwanakijiji maandiko yako mengi huwa hayana mashiko kabisa na yanabeba maelezo marefu yanayojirudiarudia. Unashindwa hata na Kubenea kwa kujenga hoja zenye mvuto lakini kwa kutumia maneno machache.
 
Sasa hapo kuna siri yoyote uliyotoa au ni mwendelezo wa makelele ya Slaa anapokuwa jukwaani? We Mwanakijiji maandiko yako mengi huwa hayana mashiko kabisa na yanabeba maelezo marefu yanayojirudiarudia. Unashindwa hata na Kubenea kwa kujenga hoja zenye mvuto lakini kwa kutumia maneno machache.

Siri ni CCM kufanya mambo kwa siri na kuwahadaa wananchi waone CCM inafanya mambo mazuri tu na isione kasoro zo zote katika utendaji unaorudisha nyuma maendeleo.

Miradi mingi inasinyaa kwa ajili ya binafsi kama mradi wa mabasi yaendayo kasi na dalili za wazi ni pale viongozi wanapopingana kikauli na maamuzi ambayo ni viongozi kujali maslahi binafsi badala ya umma. Kwa nini wapinganie hadharani wakati jambo lilishaamuliwa vikaoni na mambo mengine ni sheria ya nchi?

Rais anaongea chake, waziri mkuu chake, mkuu wa mkoa chake, waziri mhusika na wizara yake chake na kesho yake yanatokea maamuzi tatanishi kinyume cha alivyoamua jana kama ya Jairo ni aibu tu.

Maamuzi ya madiwani wa arusha serikali imejivika aibu hata wanashindwa kutoa kauli sababu ya siri za ubinafsi CCM.

Mimi si mwanachama wa chama cho chote lakini yanayoendelea ndani ya CCM ni kichefuchefu tupu.
 
Mkubwa umenena!!! Mimi nipo Tabora, yaliyotokea pale NSSF niliyashuhudia. Kesi imetulizwa kisiasa wakati watoto wamekufa, hata hivyo hakuna jitihada zozote za kugharamia roho za marehemu.

Dereva wa basi la Mohamed Trans alipindua gari kwenye mtaa ambao ofisi yao ilikuwepo, yaani mita chache tu kutoka ofisini kwao. Nilishuhudia dereva yule kakosa dhamana na hatimae alifungwa miaka 30 kwa kosa la kupindua gari na kusababisha kifo cha mtu mmoja. Lakini kesi ya vifo vya watoto mpaka sasa ni kimya, na watuhumiwa ni member wa UVCCM-Tabora.
 
It's a high time to call for the court of mass justice; we need political leaders and not political rulers. CCM has shown all kinds of failure to manage formulation of policies for development of poor majority.

They are just copying incompatible pieces of policy tools from developed countries for their personal graft greediness.

 
<font size="4">Good analysis.<br />
One day in history, one philosopher named <b>MALCOLM X</b> Uttered these words &quot;...nobody can give you freedom, nobody can give you equality or even justice. If you are a man take it...&quot;<br />
<br />
I like these words and what this analysis depicts, it is high time <b><i>CCM </i></b>to call a spade a spade and not a big spoon</font>
<br />
<br />

kwempa, I like your post, surely this is the saying of the wise!
 
makala nzuri na ya kueleweka,hao waatoke tu nchi ishawashinda na "pesa zao zinanuka"ufisadi na uonevu
 
CCM imetupumbaza sana hasa wananchi wanaoishi vijijini.Chonde chonde CCM itakula kwenu soon watu wameshaanza kufunguka!
PIPOZ PAWAAAAAAAAAAAAAA!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!
 
Sasa hapo kuna siri yoyote uliyotoa au ni mwendelezo wa makelele ya Slaa anapokuwa jukwaani? We Mwanakijiji maandiko yako mengi huwa hayana mashiko kabisa na yanabeba maelezo marefu yanayojirudiarudia. Unashindwa hata na Kubenea kwa kujenga hoja zenye mvuto lakini kwa kutumia maneno machache.

Watanzania msimalize nguvu zenu kwa huyu Masaburi, ipo siku ataelewa tu tumpeni muda wa kujifikiria na kuamka kama amekunywa maji ya bendera basi ipo siku pia atayatapika.
 
Ni kweli kabisa mkuu ila kuna vilaza ambao wamenyweshwa libwata na CCM,hawasikii hawaambiwi kama mwita25 huyu nafikiri walimu overdoz badala ya kumpa nusu kikombe,wakampa jagi zima matokeo yake amekuwa zezeta.
 
Tatizo la Viongozi wa CCM na wafuasi wake hawasomi kama wangekuwa speculative wangebadilika hapa naamini kwamba sikio la kufa halisikii dawa
aah !!! Acha chama kife tu maana wenye nacho wameamua kukiulia mbali
 
SISIEM INACHOWAFANYIA WANAINCHI WAKE HAKIKA IKO SIKU WATAJIONA WAKO UCHI MCHANA. Wasubirie kiduchu tu.
 
14 Reactions
Reply
Back
Top Bottom