Haya ndiyo maisha ya Mchaga hapa duniani na Akhera toka mwanzo wa dunia

toplemon

JF-Expert Member
Mar 26, 2017
4,583
4,615
MAISHA YA MCHAGA DUNIANI NA AKHERA

UCHAMBUZI WA KITABU *Maisha Ya Mchagga Hapa Duniani Na Ahera” By Mangi Petro Itosi Marealle*
Mangi Petro Itosi Marealle Alikuwa Mangi Mwitori Wa Vunjo, Uchagga. Baba Yake Alikuwa Ni Mangi Ndegoruo Kilamia “Marealle”, Aliyekuwa Mangi Wa Marangu Ambaye Alikuwa Mtoto Wa Mangi Ndaalio Aliyetawala Kuanzia Kiruo Vunjo Mpaka Usseri, Rombo. Kwa Hiyo Mangi Petro Itosi Marealle Alikuwa Mjukuu Wa Mangi Ndaalio Aliyetawala Kuanzia Kirua Vunjo Mpaka Usseri, Rombo.

Mangi Petro Itosi Marealle*
Mangi Petro Itosi Marealle Aliyekuwa Kijana Msomi Na Mwenye Kujitambua Sana Alifanya Utafiti Mkubwa Na Kufikia Mwaka 1946 Aliandika Kitabu Hiki Ili Kuhifadhi Tamaduni Nzuri Na Mambo Mengine Mazuri Ya Nchi Ya Uchagga Yaliyoonekana Kuelekea Kuathiriwa Na Mwingiliano Na Jamii Nyingine Za Kigeni Kutoka Maeneo Tofauti Ya Dunia. Lengo Hasa La Mwandishi Mangi Petro Itosi Marealle Ilikuwa Ni Kuhifadhi Mambo Haya Mazuri Katika Kitabu Hiki Ambacho Ni Zawadi Kwa Vijana Na Wasichana Wa Uchagga Ambao Anategemea Watatunza Kuenzi Na Kurithisha Tamaduni Hizi Nzuri Kwa Vizazi Vinavyofuata, Alikuwa Anategemea Jamii Hii Ya Wachagga Itaendelea Kustaarabika Na Kukua Bila Kuiacha Misingi Yake Na Tamaduni Zake Ambazo Ndio Zitasababisha Jamii Hii Kuendelea Kuwepo Na Kuendelea Kufanya Vizuri Zaidi Na Zaidi Bila Kupoteza Asili Hii Iliyodumu Kwa Maelfu Ya Miaka

Mwandishi Wa Kitabu Hiki Mangi Petro Itosi Marealle Pia Amegusia Kwa Kiasi Maendeleo Yaliyoletwa Na Wachagga Mpaka Kufikia Mwaka 1946 Kupitia Kile Alichokiita “Ujamaa Wa Wachagga” Chini Ya Chama Cha Ushirika Cha Wachagga Cha KNCU(Kilimanjaro Native Cooperation Union) Ambacho Ndio Chama Kikongwe Kabisa Cha Ushirika Katika Barani Afrika Kilichoanzishwa Mwaka 1933.

Sasa Twende Pamoja Katika Uchambuzi Wa Kitabu Hiki Ambacho Alikiandika Kama “Dedication” Kwa Vijana Na Wasichana Wa Uchagga Akitarajia Kutokea Hapa Wafanye Mambo Makubwa Na Pia Kuandika Vitabu Vingine Vingi Na Bora Zaidi.

Maisha Ya Mchagga Hapo Zamani Yalikuwa Katika Mpangilio Kuanzia Kabla Mimba Haijatungwa Mpaka Mwisho Wa Maisha Yake Hapa Duniani

Utaratibu Uliofutwa Kabla Ya Kuzaliwa Mtoto;
-Kabla Ya Mtu Kuoa kwa desturi alichagua mke wa umbo na sura nzuri aliye wa ukoo bora au ukoo wa watu makini wasio na matatizo ya asili kama vile magonjwa na mambo mengine yasiyofaa. Kabla ya kufanya chochote ilitakiwa wawe wameoana kwanza kwa kufuata taratibu zote zilizopangwa. Ni tofauti na sasa ambapo mtu unakutana na mtu mjini wala hujui alipotoka, hujui asili yake huelewi matatizo ya kwao unalazimisha tu kuingia naye kwenye maisha hammalizi hata mwaka mnashindwana au mnabaki katika ndoa ya kujilazimisha katika maisha au unaishia kuzaa watoto wenye tabia za ajabu au magonjwa ya ajabu ajabu.

-Ilikuwa inashauriwa wanapokutana mke na mume kwa ajili ya kupata mtoto wasiwe wamekunywa pombe kwani inaweza kumuathiri mtoto atakayezaliwa. Wakiwa wameingiliana usiku kama mwanamke anataka kuzaa mtoto wa sura na umbo zuri ilhali mume hana sura nzuri basi mwanamke hutoka nje asubuhi kutazama maua ya mgomba na maua ya mwitu yaitwayo “machemeri” kwa muda kabla ya kurudi ndani. Wakati wa ujauzito pia mwanamke alikuwa anakula udongo wa kichuguu akiamini kwamba kwa kufanya hivyo mtoto atakayezaliwa atakuwa mwenye afya na nguvu pia wakati huu wa mimba mwanamke hula udongo mwekundu uitwao “kimaande” kutokana na uchu wa mimba.
Wakati Wa Kuzaliwa Mtoto

-Baba na mama mkwe ambaye ni mama wa mume ndio huhangaika sana wakati wa kuzaliwa mtoto. Wanaweza kumwita mkunga kusaidia kuzalisha kama wataona ni vyema, kama mkungwa asipokuwa mama mkwe anaweza tu kuwa mama mwingine ambaye kwa kichagga huitwa “mkeku moende mana”. Mtoto akishazaliwa mkunga huagiza majani yaitwayo kwa kichagga “masunzuku” ambayo huyachovya ndani ya maji ya uvuguvugu na kisha kumfuta nayo mtoto mwili mzima na kumpaka siagi mwili mzima. Mtoto wa umri huu huitwa “mnangu”, maana yake mtoto mchanga.

-Mtoto hupewa dawa fulani ili akitumia maziwa ya mama yasimdhuru kisha hupewa maji ya chemchemi au ndizi iitwayo “mrarao” iliyovumbikwa ndani ya majivu ya moto kabla ya kumenywa ili ipate kuiva vizuri na kuwa laini. Ndizi hii ikishaiva hutafunwa na kutemewa mtoto kinywani ameze. Chakula hiki cha kwanza huitwa “kelya ketocha mana ulaka” maana yake, chakula cha kutoboa koo la mtoto.

-Ilikuwa hairuhusiwi kumwona mtoto kabla yakutimiza miezi mitatu kutokana na imani kadhaa zilizokuwepo. Alama ya kuonyesha nyumba au mahali palipofanywa marufuku ni kusimika mti uitwao kwa kichagga “sale” ulio na majani yaliyopigwa fundo na kusimikwa karibu na mlango wa nyumba ya mzazi. Mtoto apatapo umri wa mwezi mmoja mama huanza kumpikia chakula cha ndizi kinachotiwa maziwa yasiyochacha ndani ya chungu kidogo kiitwacho kwa kichagga “kitosho” na kukipakulia katika kisahani kidogo cha mti ambacho huitwa “iriko” au “kimborikoe”. Kila mlo wa mtoto huitwa kwa kichagga “ndutsa”.

-Mtoto huweza kuwa na tabia mbaya ambazo huaminika kwamba amerithi kwa wazazi hasa baba, au wakati mama ni mjamzito huenda baba au mama alimcheka mtu mwenye sura mbaya, au kucheka mlio wa wanyama au ndege na kadhalika. Tabia hizi ambazo huitwa kwa kichagga “mbaka mbicho” baada ya kugundulika huondolewa kwa mtoto kuoshwa kwa maji yaliyotafutwa ya mvua au chemchemi asubuhi mapema. Taratibu hii ya kuondoa “mbaka mbicho” haifanywi mara moja tu hufanyika tena mtoto aanzapo kubalehe.

-Mtoto akifikisha umri wa miezi mitatu huitwa “mkoku” naye hutafutiwa Yaya ambaye huitwa kwa kichagga “Mori” maana yake mwezi. Yaya huyu hukaa na mtoto wakati wazazi wapo katika shughuli. Na ikiwa wazazi hawawezi kumwajiri yaya, huwa ni kazi yao kumtunza kwa zamu.

Wimbo ambao Yaya humwimbia mtoto wa miezi mitatu ni huu
“Mana kutsie he, eh kutsie, He, nyi kiki kyakapa mana kalia;
“Nyi kiki kyakapa mnangu kalia; He kutsie mana kutsie”.
Maana yake
”Mtoto jinyamazie he, kitu gani kimempiga mtoto akalia, ni kitu gani kilimpiga malaika akalia, jinyamazie mtoto, jinyamazie”.
-Mtoto huendelea kutunzwa mpaka anapofikia kuota meno na hapo hufanyika sherehe kubwa ya kumwimbia na kumshangilia sana na kuchinjiwa mnyama. Kuota meno ni hatua muhimu na ni swala zito sana kwa mchagga na ndio maana ukimpiga na kwa bahati mbaya ukamng’oa jino mchagga kwa desturi utalipa ng’ombe jike na mbuzi mmoja kama fidia.

-Yaya huendelea kumtunza mtoto na kumfundisha vitu vingi kadiri anavyokuwa, humsaidia utamkaji wa maneno mbalimbali, humwelekeza aina nyingi za vitu, miti wadudu, wanyama na vitu ambavyo atahitaji kuchezea kadiri anavyoendelea kukua. Ilikuwa ni marufuku pia mtoto kutumia mkono wa kushoto hivyo ilikuwa ni kazi ya yaya kuhakikisha mtoto anazoe kutumia mkono wa kulia na alipokuwa anakuwa mgumu kutumia mkono wa kulia yaya aliripoti hilo kwa wazazi ambao waliufunga mkono wa kushoto na kitu kizito ili atumie ule wa kulia.

-Mtoto anapoendelea kukua hubadilishiwa mapishi ya chakula chake yakawa tofauti kidogo na yale ya kwanza, mtoto huanza kupikiwa chakula kiitwacho “kimantine” ambacho kwa sehemu kubwa ni chakula cha ndizi.

-Basi mtoto akiendelea vizuri na hatua ya kutembea wazazi waliweza kumpa yaya wake ruhusa aende zake ikiwa wazazi hawa si watu wenye wanyama wengi au upendo; mama na baba watamtunza mtoto wenyewe. Yaya alipewa ujira wake kumlea mtoto. Ujira wa Yaya ni mbuzi mmoja. Jinsi Mchagga ajuavyo kutunza mali yake ya wanyama, wazazi wa yaya wakiwa wema walimsaidia yaya kubadilisha yule mbuzi wapate ng’ombe kwa kumpa mbuzi mwingine wakawa wawili.

Ikiwa wazazi wa mtoto na wa yaya ni watu wanaopendana, yaya aliweza kuzidi kumsaidia mtoto kwa muda zaidi ya mwaka mmoja, lakini gharama huwa ile ile, yaani mbuzi mmoja na chakula. Yaya hodari, mwenye utii na kusaidia vema mtoto alipendwa , na amalizapo kazi yake ya kulea mtoto hakusahaulika kwa wazazi wa mtoto wala kwa mtoto akuapo. Alikaribishwa nyumbani kila mara.

Kumchagulia mtoto jina
-Mtoto akifikisha umri huu baba na mama humchagulia jina. Basi mtoto mzaliwa wa kwanza ikiwa babu yake ni marehemu huitwa jina la babu wa upande wa baba, na ikiwa babu yake yu hai ataitwa jina la babu wa babu wake. Binti hupewa jina la bibi mkubwa. Wazaliwao baadaye hupewa majina ya wajomba zao, au majina yanayoendana na vitendo vilivyowatokea wazazi au watu wan chi nzima vya furaha au vya kuhuzunisha. Mfano mara kwa mara husikia Mchagga akiitwa “Ndemasa”. Maana yake “Nilichuma mali, Mungu ni mwema”, vile vile kwa jina hili likiwa limeongezwa mwishoni “Ndemasandalye” maana yake ni nyingine yaani “Nilichuma mali lakini sikuitumia”, labda kwa kuwa iliharibika, ilipotea au alinyang’anywa na kadhalika.

Mwingine humwita mtoto “Ngao”, Maana yake amekumbuka jinsi siku moja au wakati mmoja alipokuwa akipigana vita ngao yake ikamsaidia sana, ama kwa msaada wa kitu chochote kilichomlinda na kumfaa siku za shida. Mwingine humwita mtoto “Kirama” maana yake “Umoja ni nguvu”. Mwingine humwita mtoto “Maangie” maana yake “Aliyeshangiliwa”. Mwingine humwita mtoto “Kikari” maana yake “Shujaa” au “Jasiri” na kadhalika.

-Hakika majina ya Wachagga mengi yana sababu zake. Hufuata ukoo na mambo za hali za watu. Mengine ni kwa ajili ya ushujaa, hata mengine ni kama siri ya historia, kwa mfano “Msagoni” maana yake amezaliwa wakati usio na ng’ombe. Wanawake hupewa majina ya bibi na mengine ya vitendo kama vile “Mkunde”(Aliyependeka). Mkamsuri(Mwanamke Tajiri). Au huitwa majina ya ukoo au ya mahali katika nchi, na majina hasa yanayotokana na vitendo vya taabu na furaha.
-Mtoto akifika umri huu hubadilisha chakula na kuanza kula vyakula vya watu wazima na kula muda ambao watu wazima wanakula, wazazi hawajali tena kwamba mtoto anahitaji kuendelea kujaliwa vyakula vya afya ili azidi kuimarika anapoendelea kukua. Kati ya makosa ambayo wazazi wa Kichagga hufanya ni kutokuweka nguvu tena kwenye kujali malezi ya mtoto hasa kiafya kutokana na kujishughulisha sana na kazi na hivyo mara mwingine hupelekea mtoto hudhoofika kiafya. Mtoto huendelea kufundishwa kazi ndogo ndogo za nyumbani na shughuli za kilimo, biashara na ufugaji. Waendapo shamba huchukua ndizi mbivu za kula au chakula. Chakula cha kulia shamba kwa Kichagga huitwa “kichau”.

-Basi tukiangalia katika umri huu binti huwa amezidishiwa kazi zake kuliko mtoto wa kiume wa rika lake. Watoto wa kiume hufundishwa ufugaji pamoja na shughuli nyingi za kijasiri. Watoto wote wa kike na wa kiume hufanya michezo mbalimbali ya kutumia nguvu kama vile kupigana na mieleka, kuruka juu ya miti na kutengeneza mashimo na mahandaki wanakojificha na kukimbizana. Watoto wa kiume walipigana vita vya michezo viitwavyo “kimandolu”, wakijiweka tayari na silaha zao hizi, na katika mapigano haya mtu aweza kuumia lakini ni hali ya mchezo tu. Nao watoto wa kike huenda sokoni, kulima na kuchuma majani ya ng’ombe. Katika michezo yao ya wakati huu ambayo ni ya juhudi sana, iwapo yuko mvulana au msichana aliaye hovyo kwa sababu ya maumivu ya michezo, wenzake humwimbia wimbo wa kumcheka ili aache kulia. Wimbo wenye ndio huu;

“Manene korio kelya kya mbuonyi, Mikasia ukoriosepfo kingi”.
Maana yake; Mlialia hovyo alishwe chakula cha puani badala ya mdomoni na kikiisha azidhishiwe kingine huko huko puani.

-Watoto wadogo hukaa nyumbani lakini wakifikia umri mkubwa wa kubalehe huchukuliwa kwenda kukaa na bibi na babu ili wafundishwe na kulelewa nao. Wakiwa kwa bibi na babu yao hujifunza mengi na kufanya kazi nyingi za mikono. Chakula kikiwa jikoni bibi huwasimulia hadithi nyingi za Kichagga kwa mfano hadithi ya Mregho ambayo nitaielezea baadaye.

-Watoto wa kiume hucheza mchezo wa “Oro” ambao mwandishi ameuelezea vizuri huku kwenye kitabu, ni mchezo mzuri wa ushindani na unaoweza kuburudisha sana watazamaji. Mchezo huu ulifaa sana kwa kuwafundisha watu kuweza kulenga wanyama wanaokimbia na adui vitani mikuki. Uliwafundisha pia umoja na utaratibu wa kufanya vita, kwani taratibu na sheria za mchezo huu ni ngumu na zilifuatwa kwa uangalifu sana. Huu ni mchezo ambao tungeweza kuundeleza na kuwa hodari sana katika huu mchezo na ukatupatia umaarufu mkubwa na manufaa ya kiuchumi.

-Kwa wastani wasichana walikaa kwa bibi zao kwa muda usiopungua miaka minane, watoto wa kiume hukaa muda mfupi zaidi kwa sababu wao huwa na mashughuli mengi yanayohusika na utawala wa Mangi wao na kusaidia nchi siku za shida.
Mafundisho babu na bibi wafundishayo watoto kama hawa wakati huu wa usiku ni kama haya;-

Hiki ni kichagga cha zamani kidogo kwa hiyo kuna baadhi ya misamiati imeshamezwa sana na Kiswahili kwa siku hizi, hivyo usijali sana kama kuna baadhi ya maneno yatakupa utata kuyaelewa.

“Mafundo ga mku ni matetera”. Maana yake: mafundisho na methali ya watu wetu wa kale huongoza maisha vema. Methali zenyewe ni hizi;-
i. “Meku o ngoru kalima na ngocha”. Tafsiri yake: “Mzee wa heshima alima akivaa majani”. Ufafanuzi wake ni huu: “Usiwaache wazazi wako katika hali ya shida, hasa wakiwa hawana nguo za kusitiri miili yao; wasaidie upesi.
ii. “Pora yako ngamekurina iyoe ngama undine-wo”. Tafsiri yake: “Ewe kijana wangu uliye jandoni nimekutahiri nawe kesho unitahiri”. Ufafanuzi wake: “Wazazi wamewalea na sasa hawana nguvu tena, kwa hiyo wasaidieni na muwaheshimu”.

iii. “Ipfo nuka kuipfo mdi mlotsu nyama”. Tafsiri yake: “Huko porini kuna mti mzuri wenye nyama”. Ufafanuzi wake: “Enyi watoto mnaopenda kuchungulia mizigo ya watu iliyofungwa kama kwamba mna nyama ndani, jihadharini; mkifuata desturi hii itawaletea madhara. Msidhani kila mzigo mnaouona una nyama ndani.

iv. “Ndewon ngungu, ndanwone chilyilyi”. Tafsiri yake: “Nimemwona mwewe bila kuona kundi la watu lililokusanyika kwa kusudi fulani”. Ufafanuzi wake: “Uendapo kuwinda porini ukaona kwa mbali ndege wakirukaruka karibu yake, ukadhani ni tai wanaruka karibu na mzigo wa nyama usifanye haraka. Chungulia polepole upate kuhakikisha: inaweza kuwa maharamia wamechoka, wakaketi chini ya mti ya mti ule na kutupa viatu vyao angani ili kushawishi wapiti njia au wawindaji wadhani kuwa viatu vile ni ndege warukao, wafuate mnyama aliyeko chini ya mti, na hivi maharamie wawarukie na kuwafanyia uharamia.

v. “Nyiku ndaina ndutu ya oro ilewuta pfinya ikakima ndafu?”. Tafsiri yake: Ni wapi beberu mdogo alipopata nguvu akaweza kumwonea beberu mkubwa maksai?”. Ufafanuzi wake. “Hata ukiwa na nguvu namna gani au uwezo, usijaribu kumwonea baba, kaka, au mkubwa wako yeyote. Waheshimu na kuwasaidia kwani ndio waliokulea”.

vi. “Kipfilepfile kirundu kechiwa mvuo kilawe”. Tafsiri yake: “Manyunyu ya kiwingu kidogo kilijaribu kwa mvua kisiwe”. Ufafanuzi wake: “Usione mawingu angani ukasema kwamba mvua itanyesha, jaribu kutumia maji ya mfereji ili kunywesha shamba lako”.

vii. “Koicho umbe lo Mangi lomkapo ma ulatire”. Tafsiri yake: “Ukisikia tarumbeta la Mangi likipigwa usikose kwenda”. Ufafanuzi wake: “Lazima uhudhurie kwenye mahitaji yote ya mtawala wako, ukikosa kuhudhuria utaweza kuadhibiwa. Pengine nchi yako iko katika hatari kubwa, na unahitajiwa usaidie”.

viii. “Nyi kiki kyaworo mregoni?”. Tafsiri yake: “Ni kitu gani kimenaswa kwenye mtego?”. Ufafanuzi wake: “Unapotembea ukashtukia mtego ambao umenasa mnyama, na ikiwa hujui mwenye mtego usimwondoe Yule mnyama. Ukimwondoe na mwenyewe akapata kujua, anaweza kukudhuru wewe na nchi yako”. (Methali hii imepata kutokea maeneo ya Kilimanjaro. Kwa mfano mtu wa maeneo ya Kirua Vunjo aliondoa mnyama ambaye alikuw amenaswa katika mtego uliotegwa na mtu wa maeneo ya Kilema iliyo jirani. Watu wa Kilema walipogundua, waliwadai watu wa Kirua mwishowe wakalipwa kwa sehemu ya Kirua ambayo ilichukuliwa na kuwa sehemu ya Kilema.

ix. “Mtoori o umbe nyi mka”. Tafsiri yake: “Mwenye kutoa habari za siri zako ni mwanamke”. Ufafanuzi wake: “Usizungumze siri na mwanamke hasa siri ya ng’ombe na mali nyingine ya wanyama walioko nyumbani.” (Sababu ya methali hii ni kuwa wanawake huenda kukata majani na humo huenda na humo huenda wakizungumza habari za mali bwana zao walizonazo. Kwa njia hii hutokea Mangi akadai ushuru wa utawala wake kwani amekwisha sikia kwamba fulani anayo mali kadha wa kadha kwa sababu ya uvumi wa mazungumzo ya wanawake).

x. “Ndaiya Mawuki-o-Kisima-Makyaala”. Tafsiri yake: Niite Mawuki bin Kisima wa Mtaa wa Kyaal”. Ufafanuzi wake: (Watu wa Mtaa wa Kyaala eneo la Marangu husemwa kuwa ni watu bahili, kwa hiyo wakikusaidia kitu watakuharibia).
xi. “Ipfue limwi soromu, gengi gakusoroma gakafo”. Tafsiri yake: “Nyani mmoja ametoka lakini huongezeka kidogo kidogo wakazidi”. “Ufafanuzi wake: “Ukiona watu watembeao mmoja mmoja mpakani mwa nchi yenu, kama vile nyani wanavyotembea wakienda kuiba mahindi, nenda pole pole uwachungulie, na wakiwa maadui nenda upesi umpashe Mangi habari”.

xii. “Lya Marashire lilepfaama lyikeera nyama ya Ndafu”. Tafsiri yake: “Manukato yamenukia kupita nyama ya beberu maksai”. Ufafanuzi wake: “Uendapo ukatumwa na Mangi ukamkuta mke wake, ambaye hunukia manukato, usipite karibu yake. Ukipita karibu yake unaweza kuambukizwa harufu ya yale manukato ya mke wake, na ukirudi kwa Mangi, akakusikia ukinukia manukato ya mke wake, ataweza kukudhania umezini na mke wake, hivyo utakuwa katika hatari ya kuuawa”.

xiii. “Aiyo mbero ngifunje kungo, ikalemberia Mkocha”. Tafsiri yake “Huyo ndege anayefanana na kipanga, amevunjika bawa lake, akamsingizia mtu aitwaye Mkocha(maana yake mtu mchokozi).” Ufafanuzi wake: “Usimwone kilema ukamcheka au kucheza naye ukazidi kumuumiza, unaweza kutozwa fidia”.

xiv. “Mooro mecha nyi ga mbogo, ka mooro ga nguwe nyi kiki?” Tafsiri yake. “Urithi mzuri ni wa nyati, je urithi wa nguruwe una faida gani?” Ufafanuzi wake: “Usifanye urafiki na kufanya ukahaba na mwanamke mjane, kwani unaweza kumaliza mali yako kwa kumhonga, na ukijaaliwa kuzaa mtoto, utachukuwa taabu zake zote na za mtoto. Ukizini na mwanamke mwenye bwana utalipa fidia mara moja tu, mke atabaki na mume wake”.

xv. “Molaa tengoni nyi mooru o saro una kigoro kii wanda, mbororo tsikayenda kwi?” Tafsiri yake. “Mwenye kulala katika kibanda kidogo kinachojengwa nyuma ya nyumba kubwa ni sawa sawa na mzinga wa nyuki wenye kitu kisichojulikana ndani yake”. Ufafanuzi wake. “Usimwoe mwanamke mgeni bila ya kuwajua wazazi wake na tabia zao na asili ya ukoo wake. Usiangalie uzuri wa mwili kuliko tabia na asili ya ukoo wake, anaweza kuwa na magonjwa mabaya ambayo yataharibu ukoo wako”.

Watoto hujifunza methali zote hizi na nyinginezo nyingi pamoja na mambo mengi ya kuhusu jamii ya kichagga na maisha kwa ujumla.
-Msichana anapoendelea kukua alifundishwa mambo mbalimbali ya kuhusu nafasi yake kama mwanamke hasa katika ndoa, mafundisho haya yaliitwa “shigha” na “mregho” ambapo waliweza kujifunza mambo mengi ambayo yaliwasaidia katika maisha yao. Msichana ambaye hakufundishwa “shigha” na “mregho” tunaweza kumfananisha na mtu ambaye hajasoma na yule ambaye alifundishwa mambo haya alipata heshima kubwa sana katika jamii. Wanaume walifundishwa mafundisho ya “ngasi” na waliweza kujifunza “mregho” wakiamua.

-Kuna mchoro uliokuwa kama fimbo uliokuwa na maeneo mawili moja ya juu kama mfuniko uliitwa “MSHINGO” na eneo la chini ambalo ndio sehemu kubwa liliitwa “MREGHO”, ambayo ilikuwa na sehemu nyingi zilizogawanyika zenye michoro aina tofauti tofauti na kila mchoro ulikuwa na maana yake. Vijana hawa walifundishwa namna ya kuchora mchoro huu wa “mregho” ambao ulichorwa katika mti ulioitwa “mringonu” kwa kukata michoro kwenye maganda yake ungali mbichi na kuacha ukakauka. Urefu wake ni kama mkongojo mzima, unaweza kuwa mfupi zaidi, bora tu michoro iweze kuenea na kusomeka.

-Kila aina ya mchoro huu una maana yake ambao huelezwa kwa mafumbo. Imegawanyika katika sehemu mbalimbali kadiri ya maeneo ya uchagga yaliyokuwa na michoro yao. Sehemu zenyewe za fimbo hii ni kama zifuatazo;-
i. Kirongocha: Huu ni mchoro wa upande wa chini wa fimbo ambako kumepekechwa tundu mbili ndogo fupi, moja ni kubwa kuliko nyingine. Wachagga huitaja sehemu hii hivi: “Kirongocha kilekurongocha cha lilya wakeku(bibi wakubwa) akurongocha kawada njia yeende mana, ma kima alalewada njia yeende mana nyi kwui awu na wama wawechiida wache ilufee?”
Tafsiri yake: “Kirongocha ni kipekecho kilichopekechwa kama vile bibi alivyoumbwa akawa na viungo vya uzazi akaweza kumzaa baba na mama, kwa sababu kama hakuwa na njia ya uzazi asingaliweza kuwazaa wazazi wetu. Ufafanuzi wake; Farji ya mwanamke

ii. Moselu: Hii ni picha ya kitu kilichochongeka, nayo husemwa hivi; Moselu alikuseluo cha lilya mendi awu na wama waseluo nyi ambo(kisu cha kutahiri) lilya mendi warino wakayeremka mbiu yawo wakawa wandu warine, wakakundana, wakaalikana, naaho wakafee wana wakaghorokia uruka lu na Mangi yawo meendi ghalya neenu”.

Tafsiri yake: “Moselu ni kkitu kilichochongeka kama vile wazazi walivyotahiriwa kwa kile kisu cha kutahiria walipokuwa katika ujana wao wakatakata, wakapendana, wakaoana wakazaa na wana ambao wamesimamia nchi wakasaidiana na Mangi wao mpaka hivi leo.

Ufafanuzi wake: “Tohara ya wazazi ni takaso kabla ya ndoa”.
-Sehemu ya 3, 11, nay a 15 zote huitwa kwa jina la “MSHINGO”, maana yake ni kizibo. Mshingo wa kwanza husemwa hivi; “Mshingo ulekushinga cha Msanya akushinga lya Ndaalyio lya mendi au wusunyi”.
Tafsiri yake: “Kizibo kimejiziba kama vile Msanya(jina la mwanamke) alivyojiziba alipokuwa na mimba ya mtoto wake Ndaalyio”.

Ufafanuzi wake: “Mwanamke mwenye mimba haingii mwezini”.
Sehemu nyingine za mshingo zinazidi kueleza kwa mafumbo kama fumbo hili mambo yanayohusu mwanamke kuingia mwezini.

iv. Sehemu ya 4, 6, 8, 10, 12, 16 na ya 18 huitwa kwa jumla “MREGHO” maana yake “Mchoro”. Zote zina miviringo ambayo jumla yake ni miviringo 65. Hueleza habari za mtoto anavyopata viungo vyake katika tumbo la mama yake. Kila mviringo unataja kiungo kimoja na kazi yake jinsi mifano ifuatayo inavyotuonyesha.

a. “Mregho ulekuregha cha kiki, ulekuregha cha ili mndu mka akurega na monoke usunyi, more ochiumba kaghamba lako nyi ashimbo nyi ndewu numa kakoya nyi more. Tafsiri yake: “Mchoro umejichora kama vile mwanamke mzito anapokuwa na mimba ya kwanza akadhani kwamba amevimbiwa, lakini kwa sababu ya kujua “Shigha” na “Mregho” akafahamu kwamba hakuvimbiwa bali kichwa cha mtoto kinaumbwa katika tumbo lake. Ufafanuzi wake: Kichwa cha mtoto kinaumbwa katika tumbo la mama.

b. “Mregho ulekuregha cha kiki, ulekuregha cha simba ikakuregha na monoyo ikawara mawoko maapfinya ikaowesha mando goose ikawona nyama”. Tafsiri yake: “Mchoro umejichora kama vile simba jike mwenye mimba alivyojitunza hivi kwamba mtoto aliye tumboni akapata mikono yenye nguvu, akatisha wanyama wote porini, akapata nyama za kula”. Ufafanuzi wake: “Mikono ya mtoto inaumbwa tumboni mwa mama yake ili apate kufanya nayo kazi ajipatie riziki yake.
c. “Mregho ulekuregha cha kiki, ulekuregha cha kilodanga(sungura) akuregha na monoke karosa maru gearanyia”. Tafsiri yake: “Mchoro umejichora kama sungura aliye na mimba alivyomlea mwanawe tumboni akaota masikio ya kusikiliza”. Ufafanuzi wake: “Mtoto anaota masikio tumboni mwa mama yake”.

d. “Mregho ulekuregha cha kiki, ulekuregha cha njofu ikuregha na monoyo ikalya na mara ga mtsuru ilyi iwei na uroo woyo imana lyikawada madende maapfiya gechumia ipfo ngurunyi. Tafsiri yake: “Mchoro ulijichora kama vile tembo alivyolea mimba yake kwa kula majani ya msituni, mtoto wake akapata miguu ya nguvu ili aweze kutembea msituni”. Ufafanuzi wake: “Mchoro unaonyesha miguu ya mtoto inaumbwa tumboni mwa mama yake”.

e. “Mregho ulekuregha cha kiki, ulekuregha cha mbeta ikuregha na ialeya lyalo likachewara meso makaramtsu yekuringa na mlasi”. Tafsiri yake. Mchoro umejichora kama njiwa alivyojichora na makinda yake yakapata macho ya kumwezesha apate kujificha mwindaji anapokaribia. Ufafanuzi wake: “Macho yanakuwa tumboni mwa mama yake”.
Michoro hii ya Mregho huendelea kutajwa hivi kwa mafumbo, kila mviringo ukatajiwa mnyama fulani mwenye uzuri wa mwili au kiungo kinachopatana na uzuri au kiungo kile cha mtoto kinachoumbwa katika tumbo la mama.

Sehemu ya 5, nay a 7 huitwa “MOLEMA”. Maana yake ni mchoro ulikunjwa. Huitwa hivi kwa sababu kila sehemu ina michoro saba iliyokunjika, hivi jimla ya michoro ni kumi na mine. Kila mmoja wa michoro hii unaeleza kwa mafumbo habari, kazi na taratibu za utawala wa Mangi, kama mifano ifuatayo inavyotuonyesha.

a. “Molema ulekulema cha Mangi alema uruka kalusanyia handu hamwi lulanyanyarike”. Tafsiri yake: “Mchoro umekunjika kama Mangi alivyokunja nchi akaikusanya pamoja ili isitawanyike”. Ufafanuzi wake. “Mangi ndiye mlinzi wa nchi, huzunguka nchi yake akajishughulisha hivi ili watu wake wasitawanyike, bali wawe pamoja chini yake. Hivi Mangi huikunja nchi akaikusanya”.

b. “Molema ulekulema cha njofu ikulema ikashaa mana kawada membe, Mangi kawutaho membe tso karing natso uruka na wusuri woke”. Tafsiri yake: Mchoro umejikunja kama ndovu alivyojikunja akazaa mtoto, akaota pembe, Mangi akazichukua pembe hizi akalinda nchi na utajiri wake”. Ufafanuzi wake: “Pembe za tembo ni zenye thamani sana, kwani kwazo Mangi hulinda nchi pamoja na utajiri wake(kwa mfano watu wakichukuliwa mateka Mangi hulipa pembe za tembo ili kuwakomboa; au ikiwa nchi ina deni la nchi nyingine Mangi hulipa pembe za tembo.

c. “Molemo ulekulema cha uruka lo Mangi lukulema na marasa yalo na ngyuruka tsa mrasenyi”. Tafsiri yake: “Mchoro umejikunja kama nchi ya Mangi ilivyojikunja mipakani inapopakana na nchi za majirani”. Ufafanuzi wake: “Matengenezo ya utawala kati ya nchi za majirani”.

d. “Molema ulekulema cha Mangi na njama tsake kulya mengenyi yake kasungusiapfo wandu na moondu yawo woose, uruka lukoramia”. Tafsiri yake. “Mchoro umejikunja kama vile Mangi aketivyo na raia zake kwenye uwanja wa baraza, akaweza kuonana na kuamua mashauri ya raia wote. Ufafanuzi wake: Kuamua mashauri ya watu.
Michoro hii huendelea kutaja mafundisho ya namna hii kwa mafumbo.

Sehemu ya 9, 13 na ya 17 huitwa “MONJARO”, maana yake ni “Michoro” au “Mchoro” wa mkwaruzo. Hii ni michoro ambayo katika sehemu zote imo jumla ya michoro 25. Kila mmoja hueleza kwa mafumbo mbalimbali, shughuli zote zinazohusu raia wa nchi na ubora wake, kama ukulima, biashara, ufugaji, mapishi na vinginevyo. Mifano ifuatayo inaonyesha jinsi mafumbo haya yanavyotajwa.

a. Monjaro alekucharuo cha wandai, ma sile wandai nyi kwi muwechirema shelya” Tafsiri yake: “Mchoro umejikwaruza kama ardhi ilivyotokea kwani ardhi isingalikuwako tungelilima wapi tupate chakula?”. Ufafanuzi wake: “Ukulima”
b. Monjaro alekucharuo cha mtsana o menya akucharua na ng’anya yake lilyamandi alutsanyia ng’ori ikalasa umbe waka wakanyo mlaso”. Tafsiri yake: “Mchoro umejikwaruza kama vile mhunzi alivyojikwaruza alipokuwa akitufulia chuma cha mshale ya kutobolea vena ya ng’ombe akiwa hai ili wanawake wazazi wapate damu yake yenye nguvu wainywe. Ufafanuzi wake: “Uhunzi”.

c. Monjaro alekucharuo cha mmbe ikucharuo kulya mmba ko Msanya(jina la mwanamke) ikashaa lukanyopfo maruwa, na sari yealyia nginda”. Tafsiri yake: “Mchoro umejikwaruza kama vile ng’ombe alivyojikwaruzo kwenye nyumba ya Msanya akazaa, tukapata mazima ya kunywa na mbolea ya kustawisha mashamba yetu. Ufafanuzi wake: “Kwa ufugaji wa ng’ombe tunapata maziwa ya kuwapa mama wazazi na mbolea ya kustawisha mashamba yetu”.

Sehemu ya 21 “MOFULU” , hii ndio mwisho wa fimbo na ni tundu dogo iliyopekechwa ndani, nayo husemwa hivi: “Mofulu ulekufuluo cha lyilyendi womoo ekufee kofuluka kulya ndewunyi kosongora mroe uwefeo, kocha na mafuo ghapfo”. Tafsiri yake. “Mchoro umejitengeneza kama vile mama alipokuwa akikuzaa, ukageuka tumboni mwake ukatanguliza kichwa ulipokuwa ukizaliwa, ukaja duniani u mzima na viungo vyako vyote”. Ufafanuzi wake. “Mtoto mzima anazaliwa na viungo vyake vyote”.

-Katika tundu ya hii Mofulu huwekwa udongo mwekundu uitwao “kimaande”; maana yake tendo hili ni kwamba wasichana wa rika wakiisha soma michoro hii na kuhitimu wakatembea na fimbo iliyokwisha chorwa hushindana na wasichana wengine au wavulana wajuao kwani yalikuwa mambo makubwa na ya kujivunia miaka hiyo. Msichana ambaye hakujifunza hayo alifanana na mtu ambaye hajasoma wa miaka hii. Inaonyesha kuhitimu katika masomo ya ujana.

-Mwisho wa mafundisho haya ya “Shigha” na “Mregho” Mwalimu wa haya mafundisho husema “Wana wako ngamempfunda mapfundo ghang’anyi, ngama nanyoe mupfunde wananyu. Hoi Ruwa malele, hee”. Tafsiri yake. “Wanangu nimewafundisha mafundisho makuu nanyi mpate kuwafundisha wadogo zenu. Ee Mungu na iwe hivyo milele”.
-Mambo mengi ya aina hii na mafundisho mengi haya yalitokea kabla ua pamoja na katika karne za 17, 18 mpaka 19 hivi lakini wakati kitabu hiki kinaandikwa miaka ya 1940’s mambo mengine yalikuwa yameanza kupotea. Hapa unaweza kuona kwamba Wachagga miaka ya nyuma kabisa hata kabla ya Wamisionari na Wakoloni waliweza kuwa na utaratibu wa kupeana elimu iliyotanua sana fikra zao na kukuza busara yao katika kukabiliana na mambo mengi ya maisha japo mengine ilihitaji kuboresha zaidi au kupatiwa mfumo mzuri zaidi katika kuitoa.

-Katika kila rika linaloingia katika utaratibu wa Wachagga miongoni mwa vijana wa rika huchaguliwa vijana kumi na wawili ambao hufundishwa siri za michoro juu ya mawe. Vijana wakiisha fundishwa mambo hayo hupelekwa kwa Mangi wakaapishwe wasitoe kamwe siri zinazohusu Mangi na nchi nzima. Vijana hawa watakuwa kazi yao ni kuaminiwa na kuwa wasiri wa Mangi na nchi. Iwapo nchi imepigwa vita , Mangi akalazimishwa kuondoka nchini mwake, baadhi ya vijana hawa watafuatana naye popote aendapo, na wengine watabaki nchini wakaaminiwa kuficha mali ya Mangi salama bila ya kumwonyesha mtu yeyote, mpaka hapo Mangi atakapoweza kurudi nchini mwake. Wao ndio wanaoanza kuarifiwa ikiwa Mangi anataka kuipelekea nchi jirani vita; pia wao ndio wapenzi wa Mangi wanaotumwa naye kwa ujumbe wa siri wowote.

NDOA
-Wachagga ni watu wa jamii moja na taifa moja lenye watu wa koo mbalimbali, nao wameishi kwa kuchanganyika sana toka karne nyingi zilizopita. Kwa hiyo desturi na kanuni za maisha yao ni moja katika maeneo yote ya Uchagga kutoka mashariki kwenda magharibi japo unaweza kukuta tofauti kidogo sana zinazotokana na tawala hizi na umbali wa kijiografia. Lakini desturi zao zote zina kiini kimoja na tofauti ndogo sana zilizopo si kubwa wala za maana sana. Desturi za maeneo yote ya Uchagga ni moja lakini mabadiliko huweko tu katika wingi wa mahari itolewayo. Sababu za kutoa mahari zilikuwa ni hizi zifuatazo; Wazee wa mvulana na wa msichana hutaka kukamilisha umoja utakaokuwako kati ya koo za mvulana na msichana. Umoja huu hukamilishwa , kwani mali na vyakula vitolewavyo ni vya ujamaa kati yakoo hizi mbili.

-Zamani ilikuwa baba wa mvulana akisaidiana na watu wa ukoo wake ndiye hutoa mahari. Ilikuwa hivi kwa sababu msichana anachukuliwa kama yuko chini ya mume wake atakayemuoa, yeye ndiye anamchukua msichana kwa kumchumbia na baadaye anamtoa kwa wazazi wake na kumpeleka nyumbani kwake kumwoa. Akishaolewa huwa sehemu ya ukoo wa mvulana. Mahari yanayotolewa hayakuchukuliwa kama bei ya kumnunua mke. Wazazi wa mvulana walitoa mahari ili kukamilisha ujamaa wa koo hizi mbili wakionyesha uwezo wao. Pia ilikuwa ni alama ya kuonyesha upendo baina ya koo hizo mbili, wazee wa mvulana kutoa mali kama shukrani kwa ukoo wa msichana kwa kupewa huyo msichana awe mchumba na baadaye mmoja wa wanawake wa ukoo wao. Ilikuwa pia njia mojawapo ya kuweza kukutanisha watu wa koo nyingine mbalimbali wakajuana, na taifa la wachagga likaimarika zaidi. Mahari ilitolewa kwa nia safi; Hakuna Mchagga aliyekubali kusamehewa kulipa mahari japo mara nyingi familia za binti zilikuwa zikisamehe mahari ikiwa huyo bwana hana uwezo mkubwa.

Jinsi Mvulana na Msichana Walivyochumbiana
-Zamani katika Taifa la Wachagga watu walifunga uchumba baada ya kuonana uso kwa uso katika sherehe au ngomani, au, baada ya kuongozwa na wazazi au dada, mvulana alimwendea msichana na kumtaka wafunge uchumba. Mvulana afikapo kwa msichana humwuliza “Mimi ninakupenda sana na ninataka uwe mchumba wangu; je nawe unanipenda kiasi hicho?” Ikiwa msichana anampenda humjibu, “Ndiyo nakupenda lakini kwanza ukapatane na wazazi wangu, wakikubali basi mimi nitakubali pia kuwa mchumba wako”.

-Mvulana hurudi nyumbani kwao, na kuwaeleza wazazi wake kuwa amekwisha kubaliana na msichana fulani, iliyobakia ni kuwashawishi wazazi wake msichana. Wazazi wake mvulana humjibu, “Sasa usifanye haraka wala sisi hatutataka kuonana na wakwe zako mpaka kwanza tumechunguza tabia za huyo binti na desturi zake, vile vile mpaka tumejua habari za ukoo wao toka hapo zamani kama kuna maradhi mabaya kama ukoma, wizi, uchoyo, ufukara na mengineyo.

Kadhalika msichana naye humweleza mama yake humuuliza “Nimpende huyu kijana?”, Mama naye humwambia, “Ngoja kwanza nitachunguza habari za ukoo wao, kama si watu wakali na wachoyo, wavivu, waongo na wenye laana”. Pande zote mbili, yaani wazazi wa mvulana na wa msichana watapima katika mashauri haya, kila upande peke yake. Jambo moja kubwa ambalo wazazi wa pande zote wanaloangalia ni kama baina ya koo hizo mbili wamewahi kushtakiana mbele ya Mangi kwa madai kwa jambo lolote, basi watu hawa hawakuozana kamwe.

-Basi baada yahapo taratibu nyingine za uchumba ziliendelea kwa pande zote mbili kukaribishana nyumbani kwa pombe na kuchinja, walikunywa na kucheza sana mpaka hatua ya uchumba kukamilika. Baada ya hatua ya uchumba kukamilika ziliweza kuanza taratibu za ndoa ambazo nazo zilihusisha michakato mingi sana, hasa sherehe za kualikana pande zote mbili watu wakanywa, wakala, wakacheza sana ngoma na kusherehekea, kujua kucheza vizuri ilikuwa kati ya mambo yaliyoangaliwa sana na wachumba na watu waliotaka kuchumbiana. Katika maeneo yote ya Taifa la Uchagga ilikuwa ni mwiko kumfanyia harusi ya desturi binti ambaye hakuwa bikra. Heshima ya harusi iliyozingatia desturi za kichagga ilikuwa anafanyiwa tu binti aliyeweza kutunza usichana, hivyo mabinti wa enzi hizo walikuwa wanakuwa mabikra mpaka kufikia kuolewa.

-Baada ya taratibu zote kukamilika mpaka hatua zote za uchumba mahari na harusi kuandaliwa na maharusi wote kupewa mafunzo mbalimbali ya harusi zao, sasa mzee wa kuongoza maharusi huanza kuwaoza hawa wawili na kuthibitisha kama ni kweli waliozwa mbele ya mashahidi wawe mume na mke waliooana kwa sheria ya Kichagga. Mbele ya mashahidi wale wawili ambao ni wadhamini kwa Kichagga hujulikana kama “Wakara” ambao pia waliwabeba bibi na bwana arusi na watu wengine walioko pale nje, mzee huyu wa kuongoza mambo ya harusi huchukua mkono wa kulia wa bwana kisha akauchukua nao wa kulia wa bibi harusi, na huuweka ule wa mume juu ya mkono wa mwanamke, na kuushikilia hapo akisema, Mbarilie ichu nyi mka opfo”, yaani “Mpokee huyu ni mkeo”. Bwana harusi ndipo humchukua mke ndani ya nyumba. Wakiingia wale wadhamini huwafuata; wakiisha kuingia ndani ya nyumba ndipo huachiana ile mikono mbele ya wale wadhamini.

KIFO NA MAZISHI YA WACHAGGA
-Mchagga yeyote alisemekana hawezi kufa kiurahisi isipokuwa kwa kukosea yeye mwenyewe, yaani ikiwa hakutimizi desturi za ukoo wake au kwa bahati mbaya akiugua na hivi huweza kufa upesi. Kwa hiyo mara auguapo humbidi kufikiri matendo yake kabla hajaugua, yaani alijaribu kufikiri kama alipuuzia kufanya wajibu uliompasa au ikiwa hakutimiza desturi zake za kutambika, au ikiwa amewahi kutokewa na kitu gani katika maisha yake ambacho ni asili ya bahati mbaya kama kurogwa au kuugua. Mchagga akikaribishwa hawezi kula au kunywa kitu chochote mpaka mwenye nyumba aonje chakula au kinywaji hicho mbele yake, aliogopa sana kurogwa. Hii pia ni moja wapo ya sababu wachagga walikuwa hawali ndani ya sahani mtu peke yake, wote hulia sahani moja.

-Mchagga alijaribu kutambikia kwa mizimu pia kama alifikiri labda kuna namna jamaa zake wa huko kuzimu wanamtaka afanye jambo ambalo amekuwa akilipuuzia. Lakini kama bado itashindikana basi alirudi kwa Mungu(Ruwa) ambaye aliamini yeye ndiye mwamuzi wa mwisho na mwenye mamlaka yote. Ilisemekana kwamba Mungu “Ruwa” hana uchu na mali ya mtu kama mizimu, yeye ni tajiri na karimu wala hana uchu sana na roho za watu. Hii ndiyo sababu Mchagga hakukimbilia kwake kwanza, aliwahi mizimu kwanza. Ndugu na jamaa za mgonjwa walichinja ng’ombe mjamzito wakati wa mchana jua likiwa utosini kumwomba “Ruwa” amponye mgonjwa wao. Hilo ndilo lilikuwa tumaini la mwisho lililokuwa kwa mgonjwa na jamaa zake.

-Majina ya sifa za “Ruwa” Wachagga wanazomtaja nazo wakati wanamtambikia na kumwomba, na maana yake ni haya; “Ruwa, fumvu lya mku”, maana yake ni kusema Mungu ni kama mlima wa kale na kale kama Kilimanjaro. “Ruwa Matengera” maana yake, Mungu anawatunza wanadamu kuwalisha maisha na kuwalinda katika hatari nyingi. “Ruwa molunga soka na mndo”, maana yake, Yeye ni Muumba na Mwenye kuunganisha watu kama katika taratibu ya ndoa, mtu na mke wake. “Ruwa”, maana yake ni mkuu achunguliaye watu kwa kuwatunza katika maisha yao kama jua wakati wa mchana. Iwapo Ruwa alimpenda alichukua kiumbe chake, kwani zote ni rehema zake kuishi au kufa. Iwapo mgonjwa amekufa, basi, loo! Kwa wachagga ni kama kinyume cha upendo wa Ruwa: watu hulia na kuhuzunika sana kiasi kwamba wengine hutamani hata kufa naye marehemu.

-Mchagga akifariki taratibu za kumzika ziliandaliwa ambpo alioshwa vizuri na kuvishwa sanda ambayo ilikuwa ni ngozi ya mnyama, kaburi lilichimbwa la urefu kama wa mita sita yakatandazwa majani ya mgomba ndani ya kaburi na miti aina ya “sale” pembezoni mwa kaburi kisha marehemu akawekwa ndani yake akiwa ameketi akiutazama mlima Kilimanjaro kisha wakafukia kwa kufuata utaratibu maalum. Mchagga akifariki kama alikuwa ameoa/ameolewa alizikwa ndani ya nyumba yake lakini kama alikuwa kijana ambaye bado hajaoa/hajaolewa basi alizikwa shambani nje ya nyumba.

Taratibu nyingine kama za kuanua tanga na mambo ya mirathi zilifuata. Baada ya mwaka mmoja kaburi walifukua kaburi kwa kuchimba kutokea nje ya nyumba kuingia ndani wakaondoa mifupi yote na kufukia upya. Mfupa wa fuvu la kichwa na mkono wa kulia waliliweka tofauti na mifupa mingine. Mifupa ilikusanywa ikawekwa kwenye kigae kama kibakuli hivi wakafunika na juu kisha wakatengeneza sehemu moja shambani katikati ya shamba la migomba sehemu yenye miti ya “masale” wakatengeneza kama mawe au mafiga matatu na kubandika moja juu ya yale matatu, ambapo walikuwa wameshachimba na kufukia ile mifupa iliyokuwa imefunikwa na vigae na kuweka juu yake ndani ya yale mawe/mafiga matatu wakaweka lile fuvu na kichwa na mkono wa kulia. Hapo ndipo ilipokuwa nyumba ya milele ya marehemu.

-Kama marehemu alikuwa na mke aliweza kurithiwa na ndugu wa marehemu kwa kufuata utaratibu maalum. Kama marehemu alikuwa ameoa halafu akafa kabla hajapata mtoto basi mke wake aliweza kurithiwa na ndugu wa marehemu, ambapo ndugu huyu akizaa mtoto na mke wa marehemu watoto hao watakuwa ni watoto wa marehemu na watamwita huyu ndugu wa marehemu baba mdogo licha ya kwamba ndiye baba yao mzazi na endapo atakuwa hawajali au kuwahudumia vizuri wanaweza kumfukuza nyumbani kwao. Watoto wao humtambua marehemu kama baba yao halisi.

MAZISHI YA WAMANGI
-Mangi walizikwa mchangani kama watu wengine, lakini kabla ya kuzikwa walitiwa ndani ya chombo cha mti uliochongwa ndani yake wazi kama mzinga wa nyuki mkubwa kama pipa. Kifo cha Mangi hapo zamani kilifichwa sana, pia siku hizo Mangi alikuwa haonekani na watu wote kama aonekanavyo siku hizi. Kazi zake nyingi zilifanywa na nduguye na mawaziri na wachili wa mtaani. Watu matajiri vile vile walisaidia nchi kwa kila njia wakapewa heshima na wao walikomesha fitina katika nchi wakimtii Mangi wao tu na watu wengine walikubali wakiona wale wakubwa na wazee wa nchi wamejiweka chini ya utawala.

Basi walificha habari za kifo cha Mangi kwa muda wa mwaka mmoja watu wasijue, hasa watu wan chi majirani, kwa sababu jambo kama hili likijulikana mapema ilikuwa pengine maadui walishambulia nchi hii katika msiba wao mkubwa huu na kuuharibu, na nchi itachafuka kabla ya kumtawalisha mtoto mrithi wa Umangi. Basi kifo chake kilifichwa, watu wakadanganywa kuwa Mangi ni mzima wa afya wakati ng’ombe zikichinjwa na pombe kunyweka sana, watu wajirusha usiku kucha wakisherehekea. Nyimbo za kumsifu Mangi na watu wake ziliimbwa na mambo mengine mengi, hapo Mangi alikwisha kufa kitambo.

-Jambo hili hujulikana tu kwa ndugu mrithi wa Mangi, waziri, mama wa Mangi, watoto na ndugu zake wakubwa na pengine kwa watu wakubwa wa nchi tu. Mambo haya ya kuficha kifo cha Mangi yakiendelea kwa muda basi waziri na ndugu za Mangi huanza kutengeneza habari za kumtawalisha mtoto mrithi wa marehemu; wale watu wakuu wa nchi na wachili wakubwa waliitwa kuapa kwamba watakaa kwa uaminifu na utii chini ya utawala mpya.

Wakimaliza huandaa siku maalum ya kumtawalisha mtoto mrithi wa nchi wa marehemu; wale watu wakuu wa nchi na watu wote wa nchi waliitwa, ng’ombe wengi walichinjwa na pombe nyingi ilitengenezwa. Mambo ya taratibu za kumtawalisha Mangi yalifanywa na watangulizi wa nchi. Watu huambiwa Mangi mzee sasa na hali yake sio nzuri, kwa hiyo mwanawe ametawalishwa aongoze nchi; mwenye akili zake hujua Mangi ameshafariki, lakini wengi huchukua habari hizi kama walivyoambiwa na wazee wakuu wa nchi. Wakishamaliza hizi taratibu na kuimarisha nchi basi waziri au ndugu mkubwa wa Mangi alitangaza wazi kwamba Mangi mzee alikufa na kuwaambia kwamba wako kwenye msiba mkubwa. Watu walilia na kuhuzunika sana lakini nchi ilikuwa imara kwa sababu watu wakubwa walikuwa wanaelewa siri zote.

IMANI YA WACHAGGA “RUWA”
-Wachagga huamini “Ruwa”(Mungu) kwamba ni Mkuu kupita mizimu yote wanayotambikia. Huyu Ruwa hasumbui wanadamu kwa sababu ndogondogo kama vile mizimu iwasumbuavyo ikiwa haikutambikiwa. Tambiko alilotolewa Ruwa ni tofauti na tambiko la mizimu kwa hali na sababu.

Wachagga humjua Ruwa toka kwa wakale wao. Hawa walisema kuwa wanadamu na viumbe vyote ni lipuko la Ruwa. “Walipasuka” kutoka kwake. Walimpa Ruwa heshima wakimtaja kwa majina haya manne yaelezayo heshima na kazi zake.
(a) “Ruwa” maana yake, aeneaye popote kama jua limulikalo ulimwenguni mwote pasiwepo kiumbe ama kitu kiwezacho kujificha
(b) “Matengera” maana yake, aleaye viumbe vyote kwa taratibu zake kwa amani.
(c) “Fumvu lya Mku” maana yake, mlima wa kale
(d) “Molunga Soka na Mndo”, maana yake ni kwamba kwa uwezo wake kila kiumbe chake chenye uhai huwa na taratibu ya kuwa mke na mume, watu wakazaliana, kama vile kuunga shoka na mundu, jambo ambalo ni gumu sana.
-Wakaamini kwamba yeye kwake ni juu “nginenyi” (kwenye jiwe kubwa la rangi ya samawati lionekanalo mbinguni). Kwa majina hayo manne Ruwa, Matengera, Fumvulya Mku, na Molunga Soka Na Mndo, ni sifa zake pekee na ndizo nguzo za imani ya Mchagga. Wachagga wamtambikiapo Ruwa huua beberu mweusi kabisa kila mahali ama mwekundu au mweupe kabisa, asiye na doa lolote, ambaye hakukatwa mkia, kwani kwa desturi Wachagga hukata mbuzi beberu mikia kabla hawajaweza kupanda. Huyu mbuzi huuliwa mahali palipoinuka kwenye kilele cha nyumba ya kichagga, majina yale manne ya heshima zake hutajwa na mzee mkuu wa ukoo wa huyo mgonjwa anayetambikiwa, na jamaa zake hutazama juu “nginenyi” na kuomba Ruwa amponyeshe mtu wao.

-Mzee huyu husema maneno ya namna hii: “Iyoe Ruwa Mangi Matengera, Iyoe Fumvu lya Mku, Molunga Soka na Mndo, lokuinenga ndaina yi ya ufano lopfo ili ukire mndu chu odu hoi na hoi Mangi”. Akiisha sema hivyo mbuzi huuawa. Mbuzi mwenyewe hatemewi mate kama wale wa kutambikia mizimu. Saa za kutambikia Ruwa zilikuwa wakati jua limesimama katikati angani, yaani ni kama saa sita mchana. Ikiwa kuna mawingu basi walibahatisha tu. Wakishamchinja walikula nyama wakaenda zao. Hali kadhalika ikiwa mnyama aliyechinjwa ni ng’ombe, alitafutwa ndama mwenye rangi moja tu au ng’ombe wa miguu minane yaani ng’ombe mwenye mimba. Ruwa alitambikiwa/kutolewa sadaka ikiwa nchi ina njaa kuu au maradhi makali.

-Wachagga waliamini kwamba watu wa jamii zote walilipuka kutoka kwa Ruwa na polepole wakajaa ulimwenguni. Husema kuwa Ruwa anawapenda kwa sababu hawasumbuliwi naye kama vile wachawi na mizimu wanavyosumbua kwa kutaka gharama na tambiko za namna nyingi kila siku. Tambiko/sadaka kwa Ruwa ni moja na hutolewa kwa sababu moja tu. Katika imani ya wachagga hakukuwa na shetani, mapepo wala malaika.

-Lakini pamoja na yote hayo kwa sababu ya kutishwa sana na uchawi na mizimu karibu wingi wa matambiko ulitolewa kwa mizimu. Wazee waamkapo kila asubuhi walifungua nyumba wakatoka nje na kutazama upande wa kaskazini kunako mlima Kilimanjaro na kuinua kichwa wakatema mate mara nne, “Tuu, tu, tu, tu”, wakamwita Ruwa kwa majina na sifa zile nne na kumshukuru kwa uzima walioamshwa nao kwa asubuhi alfajiri tu, na ni wazee wanaume tu wenye mamlaka ya kufanya hivyo; wanawake wajane wazee pia huweza kufanya hivyo. Hivyo ndivyo Wachagga walivyomjua Ruwa kuwa ni mkuu kupita viumbe vyote; nay a kuwa Ruwa ndiye mwenye nguvu kupita mizimu yote juu ya roho za binadamu, kwani kwake ndiko walimwengu walikolipuka wakaja kuzaliana duniani.

“MIZIMU”
-Wachagga zamani waliamini na kutambikia mizimu, yaani watu wao walio marehemu. Waliamini mtu akishakufa bado alikwenda kuishi tena kule kuzimuni, lakini si kwa mwili huu tulio nao. Walisadiki kuwa hawa mizimu hula na kunywa, na kuweza kuja tena duniani na kudai haki zao walizokuwa wakipata kwa jamaa zao. Wajapo kudai sehemu zao kwa jamaa zao walikuwa wakija wakati wowote wanapotaka; lakini hawaonekani na mtu yeyote kwa sura yao bali huonekana kama katika ndoto au fahamu. Walijua kama mtu alikuwa na maovu mengu hapa duniani, hata huko kuzimuni atapata taabu, yaani hataweza kuonana na jamaa zake na kuweza kukaa nao huko.

Jamaa zake huku duniani wakifanya tambiko kwa kumuombea kwa ndugu zake wampokee na kushirikiana naye huko ahera ndipo anapopata nafasi nzuri ya kuonana na wale wamjuao na kukaa nao. Walijua pia kuwa Wamangi wafapo walikwenda kutawala tena huko ahera kama hapa duniani. Waliamini ya kuwa ikiwa mtu analo tendo baya ambalo hakuwahi kulitengeneza akiwa hapa duniani, aendapo akafa tendo lile ovu litamfuata mpaka aombewe na jamaa zake wa hapa duniani. Ikiwa hakuombewa kwa tambiko ili apate msamaha huko kuzimu, huyu mtu atapewa mahali pake yake asiweze kuonana na jamaa zake; mwishoni atapelekwa katika ahera ya tatu iitwayo “Kiragaifu”, maana yake ni ahera ya watu ambao hutokomea kabisa hata wakawa kama majivu. Jamaa walio hai hawataweza kukutambikia tena kwa kuwa tambiko la watu wa duniani haliwezi tena kuwafikia.

-Kazi ya mizimu ni kudai sehemu na taratibu zao walizokuwa wakitendewa walipokuwa hai hapa duniani. Waliombwa msamaha kwa makosa waliofanyiwa na watu wa hapa duniani, wakatakiwa pia watoe msaada kwa kuondoa maradhi waliyowaletea watu au jamaa zao hapa duniani. Huombwa kwa tambiko.

USAWI (UCHAWI) KWA WACHAGGA
-Katika nchi ya Uchagga tuliogopa sana “usawi” (uchawi) toka zamani sana. Huu uchawi ulitisha watu wote, wakubwa kwa wadogo, waume kwa wake, watoto mpaka Wamangi. Ulitisha kuliko magonjwa ya kifua kikuu na ndui. Kwani mtu mzima aliweza kula na mgonjwa wa kifua kikuu lakini haikuwa jambo rahisi kwa Mchagga kula na mtu aliyetuhumiwa kuwa ni mchawi. Tulitishwa hivi kwa miaka mingi na hata watoto walirithi uoga ule na mpaka sasa; kutokana na kuugopa sana uchawi ulipata nguvu na kutawala sana roho zilizouamini.

Wazee walisimulia habari za uchawi kwamba hakuna anayejua uchawi ulivyo isipokuwa mchawi mwenyewe , na haujulikani kwa watu wote kwa kuwa mambo yenyewe ni siri ya wachawi wenyewe. Hata hivyo tulikuwa tukisikia kutoka mataifa mengine kuhusu mambo makubwa sana yanayofanywa na wachawi wa mataifa hayo ambayo huku kwetu hayakuwepo wala kuwezekana kama miujiza mikubwa.

-Kwa hakika uchawi ulitisha sana katika nchi ya Uchagga, na mpaka sasa hofu ile bado iko, lakini tukifikiri na kuangalia jinsi uchawi wa namna mbalimbali unavyofanyika bila shaka tunaona hakuna uchawi wa kweli. Hadithi nyingi huzungumzwa juu ya uchawi lakini ukiuliza ni mti gani aliye mchawi ili uambiwe siri ya uchawi wake hutampata. Wachawi walihukumiwa kwa kupewa dawa inayolevya sana iitwayo “kimanganu” maana yake, kitu kinachomaliza ubishi wa mtu mkaidi. Dawa hii iliwafanya waongee kila kitu kuelezea namna wanafanya uchawi lakini walishindwa kusema na mwisho waliishia kusingizia wamefanya jambo fulani baada ya maumivu makali ili waachiliwe tu lakini sio kweli.

-Mimi nathubutu kusema kuwa Wachagga huzungumza siku hizi habari za uchawi wa namna hizi kwa kusikia tu lakini hawajui; Na hata wale waliokuwa wakiuamini sana kutafuta waganga wawasaidie zamani, walikuja kuudharau na kutoa habari za maisha yao walipokuwa wakiogopa uchawi. Hofu imeendelea kuwapo kwa sababu tulizaliwa katika woga, na mpaka sasa bado kuna Wachagga wanaogopa uchawi licha ya kwamba hawaujui. Tumeweza kuona kwamba Wachagga walishaudharau uchawi zamani baada ya kudadisi na kukutana na uzushi mwingi na kuogopeshana ndio maana huwezi kupata Mchagga mganga wa kienyeji wa zama hizi kwani shida hizo za uchawi ambazo zinawafanya watu kwenda kwa waganga kwa Wachagga zilitoweka zamani hivyo waganga hawakuwa wanahitajika tena, lakini hata hivyo utakuta watoto wanaozaliwa siku hizi na kukutana nawatu wa jamii nyingine ambao bado wako nyuma kwa maswala haya na bado wanahofia mambo ya uchawi wanawaogopesha upya na wanaendelea kuamini na kuogopa uchawi kiasi cha kufikiria kutafuta waganga wa kienyeji.

MCHAGGA WA LEO
-Mwandishi Mangi Petro Itosi Marealle ameona kwamba Mchagga wa leo ameingiliwa na tamaduni nyingi sana za kigeni na zimekuja bila utaratibu kiasi cha kumuathiri sana, tamaduni hizi zimeenezwa sana kwa msaada wa dini za kigeni na serikali lakini zaidi hasa kwa dini za kigeni. Ukweli ni kwamba katika tamaduni na desturi za kichagga yalikuwepo mambo mazuri sana yanayofaa na mambo mengine yasiyofaa. Lakini ni jukumu letu kuendeleza mambo mazuri yanayofaa ambayo ni mengi sana na kuboresha yale yasiyofaa yenye kufaa kuboresha na yasiyofaa kabisa kuachana nayo ndipo kuchanganya na baadhi ya kigeni ambayo tumeona yanafaa na yatatusaidia katika Nyanja mbalimbali.

Mwandishi ameona sisi kama taifa la Uchagga tunapaswa kufanya kazi kwa bidii na kujenga utaratibu wa kujenga mashule mengi pamoja navyuo ambapo tutafundisha mambo mema ya kwetu yatakayoweza kukuza na kuendeleza ustaarabu wetu katika nyanja zote za maisha.

Mwandishi anasema kupitia ujamaa wa Wachagga tayari tumeanza vizuri licha ya changamoto mbalimbali lakini kwa kupitia chama cha ushirika cha Wachagga KNCU(Kilimanjaro Native Cooperative Union), ambacho ndicho chama kikongwe kabisa cha Ushirika barani Afrika kilichoanzishwa mwaka 1933 tumejenga vyuo kama vile Chuo Cha Ushirika Moshi, mashule kama vile Lyamungo Sekondari n.k. , pamoja na miradi mingine kama ya maji, barabara n.k., baada ya kujitoza ushuru mkubwa katika zao la mibuni hivyo tunapaswa kuzidi kufanya kazi zaidi na kujenga mashule zaidi na vyuo vingi ambavyo tutaweza kufundisha watoto wetu wote, wenye kutokea kwenye familia zenye uwezo na wasio na uwezo katika kuelekea kuwa na jamii bora na iliyostaarabika sana.

-Mwandishi ameona tunaweza kusaidiana hata na wageni wa kizungu wale wenye nia njema, wenye utaalamu wa mambo mbalimbali wakatusaidia katika kuimarisha watu wetu na kujenga taasisi imara zenye mifumo bora na endelevu katika kukuza ustaarabu wetu huku tukiimarika tamaduni zetu nyingi nzuri bila kuziacha na kukimbilia moja kwa moja tamaduni za kigeni ambazo nazo zina mapungufu maengi na mbaya zaidi nyingi haziendani moja kwa moja na sisi kwa maana sio asili yetu.

MAONI YANGU
-Nimesoma kitabu hiki pamoja na vitabu vingine vingi pamoja na uzoefu kiasi niliopata katika maisha mpaka hapa nilipofika, sisi binadamu ni watu tuna historia ndefu sana na kila jamii ya watu waliendelea kupiga hatua za kimaendeleo kadiri ya juhudi na akili walizotumia katika mambo yao ya kila siku, naweza kusema kwamba sisi Wachagga na Waafrika wengine kwa ujumla tuna mambo mazuri ya kwetu ambayo sio lazima kuyaacha yote tuna mambo mengi sana bora katika tamaduni na desturi zetu tunaweza kuwa tunayafanya ambayo tutakuja kujivunia na watoto wetu watajivunia hasa kadiri tutakavyoendelea kujitambua. Sisi Waafrika hususan Watanzania tumekuwa ndio watu tunaoongoza kwa kutojitambua duniani kwa sababu ya kushindwa kuthamini na kujivunia vitu vyetu na kukaa kufikiri vya watu ndio vitu bora.

-Leo naomba niwaase Wachagga kuna mambo mawili tunaweza kuyaanza kama mfano wa kwamba tumeanza kujitambua na mengine yakafuata;
(i) Lugha ya kichagga,
(ii) Majina ya kichagga.

Enyi Wachagga hebu tujitahidi kuhakikisha tunaendeleza hii lugha isipotee, fundisha mtoto wako nyumbani na jitahidi kuwa unaiongea naye mara kwa mara huwezi kujua huko mbeleni akawa mtu mwenye kujitambua na mwenye uwezo mkubwa hata akaianzishia taasisi ya kuiendeleza na kuitumia, hivi ni vitu ambavyo vizazi vijavyo ambavyo vitajitambua sana vitatulaumu sana na kutuona mazuzu kwa kuviacha vipotee ambapo muda huo watakuwa wanaongea Kichina na Kiingereza tu halafu vya kwao havijulikani, ni aibu na itakuwa ni ujinga wetu ambao tuko sasa na tunaweza kuchukua hatua.

Jambo la pili ni majina ya kichagga, yewomii, wachagga hebu tuacheni kujichoresha na majina tusiojua hata yanatokea wapi, sisi wachagga tumejaliwa kuwa na majina mengi mazuri sana ya kichagga ambayo ndio alama na fahari yetu. Wewe unaenda nchi za watu huko China, Ulaya, Uarabuni, Amerika, unaonekana kabisa wewe ni mweusi/mwafrika unaulizwa jina unaona ufahari sana kutaja sijui Careen/Mourine/Brian/Johnson, aisee unajichoresha sana, yaani wanakuona boya sana usiyejitambua nawe unajikuta unashangilia sana, sisi wazazi wetu tusiwalaumu sana kutuita majina haya yasiyo ya asili yetu lakini sisi tusirudie makosa kwa watoto wetu jamani tuna majina ya kiafrika mengi mno.

-Hivi umeowahi kuona Mchina anaitwa James au George au Irene au hata Muhindi anaitwa Charles au Diana, wote wana majina ya sijui Park, sijui Lee au Rajesh, Suthir, Sunil, sasa unafikiri wao haya majina ya Charles hawayajui, kwamba wewe tu ndio unayajua?, Hapana wamekataa kujichoresha, basi ningependa kuomba tujikaze tutumie haya majina yetu bora, tena hakikisha unajua maana yake kabisa, acha kuwaza kwamba sio zuri, jina lolote ukilizoea ni zuri ni akili yako tu ndio imeharibiwa, wangapi wanaitwa majina ya kichagga na ni mazuri tu kwao?

Post itakayofuata nitaweka majina mengi sana ya kichagga ya kiume na ya kike halafu utachagua hapo unaloona ni bora zaidi kwa ajili ya mtoto wako tafadhali. Halafu usije kusema hili la kichagga ni la nyumbani halafu hilo la wazungu ndio la kiofisi au shule, hapana hilo la kichagga ndilo linatakiwa lipewe hadhi ya kiofisi, jamani wachagga tuzingatie hili maana ndio mwanzo wa kujitambua sasa kama Wachagga.

-Mwisho nisistize jamani Wachagga tununue hiki kitabu tukisome, ni kitabu kizuri na muhimu zaidi ni kwamba tumeandikiwa sisi Wavulana na Wasichana wa Uchagga, ni kitabu kizuri kusomwa na kijana mwingine yoyote wa kiafrika kwa ajili ya kujua namna ya maisha yetu yalivyokuwa lakini pia kinatuongezea kujiamini sisi kama Wachagga kujielewa zaidi na kujua nguvu yetu ilikuwa wapi. Katika kitabu hiki pia kuna hadithi tatu nzuri sana za kichagga za zamani zilizotungwa kwa weledi wa hali ya juu na ubunifu mzuri sana. Kumbuka kila jamii duniani ina hadithi zake nyingi za kufikirika hivyo na wachagga tulikuwa na waandishi wabunifu karne nyingi zilizopita waliokuwa na uwezo wa kutunga hadithi bora nzuri na za kusisimua.

Kuna hadithi za;
(i) Hadithi ya Mregho(binti mrembo sana) wa kichagga miaka hiyo
(ii) Hadithi ya Morile na Mangi Tembo Lya Mori, nayo nzuri sana
(iii) Hadithi ya kuhusu Mlima Kilimanjaro.

-Pia nisisitize sana kwamba mambo mengi nimechambua hapa kwa juu juu sana kuhusu kitabu hiki hivyo usipokisoma utakuwa kuna kitu kikubwa hujakipata, kuna vitu nimejaribu kuchambua kwa undani kidogo lakini viko vingi sana nimegusa juu juu, ni kitabu cha Kiswahili kinachoeleweka vizuri na kitakusaidia kuwa mwanzo mzuri hata kama nawe unataka kuwaandikia watu wa taifa lililokuwa la Uchagga jambo lolote ambalo unasukumwa kuwaandikia. Mwandishi wa kitabu hiki amesisitiza kwamba anategemea Wachagga mtajitahidi kuandika kazi nyingine zaidi kama hizi kwa faida ya jamii yenu na pia amesema mambo mengi makubwa yanatarajiwa yafanywe na ninyi. Pata nakala yako ya kitabu hiki tuendelee kujitambua zaidi na zaidi.

WASIFU WA MWANDISHI WA KITABU HIKI, MANGI PETRO ITOSI MAREALLE
-Mangi Petro Itosi Marealle alizaliwa tarehe 13 Juni 1906 katika kijiji cha Lyamrakana, Marangu, wilaya ya Moshi Vijijini. Alikuwa mtoto wa mwisho wa kiume wa Mangi Ndegoruo Kilamia Marealle. Mama yake alikuwa ni Elise Makyalenyi Morio, binti wa Mangi Tengia wa Mriti, Rombo.

-Babu yake Mangi Petro Itosi Marealle alikuwa ni Mangi Ndaalio aliyetawala kuanzia Kirua Vunjo mpaka Useri Rombo. Hata hivyo utawala wake ulisambaratika alivyokufa kabla hata mtoto wake mmoja wa kiume hajafikia umri wa kutawala. Ndugu yake Kinabo, alitawala mahali pake na aliwafukuza mke wa Ndaalio, mama Nderero na watoto wake wawili Ndegoruo Kilamia na Mlatie. Mama huyu na watoto wake walikimbilia kwanza kwa Mangi wa Kirua Vunjo, kwa Mangi Rindi wa Old-Moshi na mwisho kwa Mangi Sina wa Kibosho. Wakimbizi hawa walipokelewa vizuri sana na Mangi Sina na baada ya vijana Ndegorio Kilamia na Mlatie kuwa watu wazima, Mangi Sina alikuja kumpiga vita Mangi Kinabo wa Marangu akamshinda na kumtawalisha Mangi Ndegoruo Kilamia.

-Mangi Ndegoruo Kilamia alitawala kwa busara, na alikuwa mkulima hodari wa kahawa. Watawala wa kimasai walipomtembelea walimpa jina la kimasai “Meliari”, lenye maana ya mtu asiyechoka. Hicho ndicho kilikuwa chanzo cha jina Marealle. Alikuwa mtu wa kwanza Mwafrika kujenga ghorofa huko Marangu.

-Mangi Ndegoruo Kilamia alikufa mwaka 1916, akiwa na umri wa miaka 70. Mtoto wake wa kiume wa pili, Joseph Mlang’a alitwalishwa kuwa Mangi wa Marangu.

-Wakati huo huo mdogo wake ambaye ndio mwandishi wa kitabu hiki, Mangi Petro Itosi Marealle, alipelekwa shule ya Mission ya Ngaruma ya hapo kijijini mwaka 1913. Alijifunza kusoma, kuandika na kuhesabu kwa lugha ya Kichagga. Kuanzia mwaka 1915 mpaka 1918 shule ilifungwa kwa sababu ilikuwa wakati wa vita kuu ya Kwanza.

-Baada ya vita, shule ilifunguliwa akaendelea kusoma. Mwaka 1925 alichaguliwa kwenda shule ya kati huko Tanga. Mwaka 1926 shule mpya ya serikali ilifunguliwa Old Moshi na wanafunzi wote waliotoka wilaya ya Moshi, akiwemo Petro Itosi Marealle, walirudishwa Old Moshi. Alimaliza masomo ya miaka 4 na kufanya mtihani wa Taifa mwaka 1929. Alipata shahada.

-Mwaka 1930, aliajiriwa katika shule ya watoto wa machifu, Tabora, kama karani. Kazi hii aliifanya kwa mwaka mmoja ndipo akachaguliwa na wananchi kurithi Umangi wa jadi wa eneo la Marangu, baada ya kaka yake Joseph Mlang’a kujiuzulu. Alikuwa Mangi wa Marangu mpaka mwaka 1946, alipochaguliwa kuiongoza tarafa ya Vunjo kama “Mwitori”, akisaidiwa na Wamangi saba. Alishikilia uongozi huo hadi mwaka 1961.

-Mwaka 1961, Mangi Petro alijiuzulu Umangi na kupokea madaraka mapya katika Chagga Council kama Executive Officer upande wa Ustawi wa Jamii. Tarehe 17 Februari 1962 alichaguliwa na Chagga Council kuwa Makamu wa Rais wa kwanza wa Wachagga wakati utawala wa Umangi wa jadi ulipofutwa.

-Tarehe 18 Oktoba 1962, aliitwa na Serikali kushika madaraka ya Mwenyekiti wa Local Government Service Commission. Aliifanya kazi hadi alipostaafu mwaka 1978.

Mangi Petro Itosi Marealle alifariki dunia mwezi Mei, 1982.

Home sweet home
IMG_20181119_123845.jpeg
BeautyPlus_20190509164005481_save-1.jpeg
FB_IMG_15708665285155661.jpeg
FB_IMG_15932612089829924.jpeg
FB_IMG_15932611894206566.jpeg
FB_IMG_15932612181078764.jpeg
FB_IMG_15932612461834529.jpeg
FB_IMG_15932612629333810.jpeg
FB_IMG_15932612695535872.jpeg
FB_IMG_15932612758241646.jpeg
FB_IMG_15932612992840491.jpeg
FB_IMG_15932612811878862.jpeg
 
Mkuu sijaisoma ila umeandika tittle iliyo kwa mipango yangu kuandika kitabu cha kuenzi tawala na tamaduni za uchagani tokea enzi za ukoloni nimepanga kuanza rasmi 2024 kulingana na ubizy wa ratiba.

Najua kufikia mwaka huo 2024 nitakuwa na nafasi nzuri kwenye sekta ya Utalii hivyo kuweza kufanya hiyo kazi kwa ufanisi na manufaa zaidi kwa taifa na kizazi cha baadae. Mungu akijaalia nitakutafuta
 
Nzuri nimejitahid kuisoma kwa Kasi ya 5g ,IPO vizuri nimepnda methali za mule Hadi Leo zinaishi,anyway mi ni mchaga ila icho kichaga ni cha marangu sikielewi ila fresh ni vyema kuwapa wanetu culture hata lugha tu itatosha, namshukuru Bibi,babu na mama kwa kunirithisha lugha
 
Hicho kitabu kipo kaka
Mkuu sijaisoma ila umeandika tittle iliyo kwa mipango yangu kuandika kitabu cha kuenzi tawala na tamaduni za uchagani tokea enzi za ukoloni nimepanga kuanza rasmi 2024 kulingana na ubizy wa ratiba.
Najua kufikia mwaka huo 2024 nitakuwa na nafasi nzuri kwenye sekta ya Utalii hivyo kuweza kufanya hiyo kazi kwa ufanisi na manufaa zaidi kwa taifa na kizazi cha baadae. Mungu akijaalia nitakutafuta
 
Kweli kabisa
Nzuri nimejitahid kuisoma kwa Kasi ya 5g ,IPO vizuri nimepnda methali za mule Hadi Leo zinaishi,anyway mi ni mchaga ila icho kichaga ni cha marangu sikielewi ila fresh ni vyema kuwapa wanetu culture hata lugha tu itatosha, namshukuru Bibi,babu na mama kwa kunirithisha lugha
 
MAISHA YA MCHAGA DUNIANI NA AKHERA

UCHAMBUZI WA KITABU *Maisha Ya Mchagga Hapa Duniani Na Ahera” By Mangi Petro Itosi Marealle*
Mangi Petro Itosi Marealle Alikuwa Mangi Mwitori Wa Vunjo, Uchagga. Baba Yake Alikuwa Ni Mangi Ndegoruo Kilamia “Marealle”, Aliyekuwa Mangi Wa Marangu Ambaye Alikuwa Mtoto Wa Mangi Ndaalio Aliyetawala Kuanzia Kiruo Vunjo Mpaka Usseri, Rombo. Kwa Hiyo Mangi Petro Itosi Marealle Alikuwa Mjukuu Wa Mangi Ndaalio Aliyetawala Kuanzia Kirua Vunjo Mpaka Usseri, Rombo.

Mangi Petro Itosi Marealle*
Mangi Petro Itosi Marealle Aliyekuwa Kijana Msomi Na Mwenye Kujitambua Sana Alifanya Utafiti Mkubwa Na Kufikia Mwaka 1946 Aliandika Kitabu Hiki Ili Kuhifadhi Tamaduni Nzuri Na Mambo Mengine Mazuri Ya Nchi Ya Uchagga Yaliyoonekana Kuelekea Kuathiriwa Na Mwingiliano Na Jamii Nyingine Za Kigeni Kutoka Maeneo Tofauti Ya Dunia. Lengo Hasa La Mwandishi Mangi Petro Itosi Marealle Ilikuwa Ni Kuhifadhi Mambo Haya Mazuri Katika Kitabu Hiki Ambacho Ni Zawadi Kwa Vijana Na Wasichana Wa Uchagga Ambao Anategemea Watatunza Kuenzi Na Kurithisha Tamaduni Hizi Nzuri Kwa Vizazi Vinavyofuata, Alikuwa Anategemea Jamii Hii Ya Wachagga Itaendelea Kustaarabika Na Kukua Bila Kuiacha Misingi Yake Na Tamaduni Zake Ambazo Ndio Zitasababisha Jamii Hii Kuendelea Kuwepo Na Kuendelea Kufanya Vizuri Zaidi Na Zaidi Bila Kupoteza Asili Hii Iliyodumu Kwa Maelfu Ya Miaka

Mwandishi Wa Kitabu Hiki Mangi Petro Itosi Marealle Pia Amegusia Kwa Kiasi Maendeleo Yaliyoletwa Na Wachagga Mpaka Kufikia Mwaka 1946 Kupitia Kile Alichokiita “Ujamaa Wa Wachagga” Chini Ya Chama Cha Ushirika Cha Wachagga Cha KNCU(Kilimanjaro Native Cooperation Union) Ambacho Ndio Chama Kikongwe Kabisa Cha Ushirika Katika Barani Afrika Kilichoanzishwa Mwaka 1933.

Sasa Twende Pamoja Katika Uchambuzi Wa Kitabu Hiki Ambacho Alikiandika Kama “Dedication” Kwa Vijana Na Wasichana Wa Uchagga Akitarajia Kutokea Hapa Wafanye Mambo Makubwa Na Pia Kuandika Vitabu Vingine Vingi Na Bora Zaidi.

Maisha Ya Mchagga Hapo Zamani Yalikuwa Katika Mpangilio Kuanzia Kabla Mimba Haijatungwa Mpaka Mwisho Wa Maisha Yake Hapa Duniani

Utaratibu Uliofutwa Kabla Ya Kuzaliwa Mtoto;
-Kabla Ya Mtu Kuoa kwa desturi alichagua mke wa umbo na sura nzuri aliye wa ukoo bora au ukoo wa watu makini wasio na matatizo ya asili kama vile magonjwa na mambo mengine yasiyofaa. Kabla ya kufanya chochote ilitakiwa wawe wameoana kwanza kwa kufuata taratibu zote zilizopangwa. Ni tofauti na sasa ambapo mtu unakutana na mtu mjini wala hujui alipotoka, hujui asili yake huelewi matatizo ya kwao unalazimisha tu kuingia naye kwenye maisha hammalizi hata mwaka mnashindwana au mnabaki katika ndoa ya kujilazimisha katika maisha au unaishia kuzaa watoto wenye tabia za ajabu au magonjwa ya ajabu ajabu.

-Ilikuwa inashauriwa wanapokutana mke na mume kwa ajili ya kupata mtoto wasiwe wamekunywa pombe kwani inaweza kumuathiri mtoto atakayezaliwa. Wakiwa wameingiliana usiku kama mwanamke anataka kuzaa mtoto wa sura na umbo zuri ilhali mume hana sura nzuri basi mwanamke hutoka nje asubuhi kutazama maua ya mgomba na maua ya mwitu yaitwayo “machemeri” kwa muda kabla ya kurudi ndani. Wakati wa ujauzito pia mwanamke alikuwa anakula udongo wa kichuguu akiamini kwamba kwa kufanya hivyo mtoto atakayezaliwa atakuwa mwenye afya na nguvu pia wakati huu wa mimba mwanamke hula udongo mwekundu uitwao “kimaande” kutokana na uchu wa mimba.
Wakati Wa Kuzaliwa Mtoto

-Baba na mama mkwe ambaye ni mama wa mume ndio huhangaika sana wakati wa kuzaliwa mtoto. Wanaweza kumwita mkunga kusaidia kuzalisha kama wataona ni vyema, kama mkungwa asipokuwa mama mkwe anaweza tu kuwa mama mwingine ambaye kwa kichagga huitwa “mkeku moende mana”. Mtoto akishazaliwa mkunga huagiza majani yaitwayo kwa kichagga “masunzuku” ambayo huyachovya ndani ya maji ya uvuguvugu na kisha kumfuta nayo mtoto mwili mzima na kumpaka siagi mwili mzima. Mtoto wa umri huu huitwa “mnangu”, maana yake mtoto mchanga.

-Mtoto hupewa dawa fulani ili akitumia maziwa ya mama yasimdhuru kisha hupewa maji ya chemchemi au ndizi iitwayo “mrarao” iliyovumbikwa ndani ya majivu ya moto kabla ya kumenywa ili ipate kuiva vizuri na kuwa laini. Ndizi hii ikishaiva hutafunwa na kutemewa mtoto kinywani ameze. Chakula hiki cha kwanza huitwa “kelya ketocha mana ulaka” maana yake, chakula cha kutoboa koo la mtoto.

-Ilikuwa hairuhusiwi kumwona mtoto kabla yakutimiza miezi mitatu kutokana na imani kadhaa zilizokuwepo. Alama ya kuonyesha nyumba au mahali palipofanywa marufuku ni kusimika mti uitwao kwa kichagga “sale” ulio na majani yaliyopigwa fundo na kusimikwa karibu na mlango wa nyumba ya mzazi. Mtoto apatapo umri wa mwezi mmoja mama huanza kumpikia chakula cha ndizi kinachotiwa maziwa yasiyochacha ndani ya chungu kidogo kiitwacho kwa kichagga “kitosho” na kukipakulia katika kisahani kidogo cha mti ambacho huitwa “iriko” au “kimborikoe”. Kila mlo wa mtoto huitwa kwa kichagga “ndutsa”.

-Mtoto huweza kuwa na tabia mbaya ambazo huaminika kwamba amerithi kwa wazazi hasa baba, au wakati mama ni mjamzito huenda baba au mama alimcheka mtu mwenye sura mbaya, au kucheka mlio wa wanyama au ndege na kadhalika. Tabia hizi ambazo huitwa kwa kichagga “mbaka mbicho” baada ya kugundulika huondolewa kwa mtoto kuoshwa kwa maji yaliyotafutwa ya mvua au chemchemi asubuhi mapema. Taratibu hii ya kuondoa “mbaka mbicho” haifanywi mara moja tu hufanyika tena mtoto aanzapo kubalehe.

-Mtoto akifikisha umri wa miezi mitatu huitwa “mkoku” naye hutafutiwa Yaya ambaye huitwa kwa kichagga “Mori” maana yake mwezi. Yaya huyu hukaa na mtoto wakati wazazi wapo katika shughuli. Na ikiwa wazazi hawawezi kumwajiri yaya, huwa ni kazi yao kumtunza kwa zamu.

Wimbo ambao Yaya humwimbia mtoto wa miezi mitatu ni huu
“Mana kutsie he, eh kutsie, He, nyi kiki kyakapa mana kalia;
“Nyi kiki kyakapa mnangu kalia; He kutsie mana kutsie”.
Maana yake
”Mtoto jinyamazie he, kitu gani kimempiga mtoto akalia, ni kitu gani kilimpiga malaika akalia, jinyamazie mtoto, jinyamazie”.
-Mtoto huendelea kutunzwa mpaka anapofikia kuota meno na hapo hufanyika sherehe kubwa ya kumwimbia na kumshangilia sana na kuchinjiwa mnyama. Kuota meno ni hatua muhimu na ni swala zito sana kwa mchagga na ndio maana ukimpiga na kwa bahati mbaya ukamng’oa jino mchagga kwa desturi utalipa ng’ombe jike na mbuzi mmoja kama fidia.

-Yaya huendelea kumtunza mtoto na kumfundisha vitu vingi kadiri anavyokuwa, humsaidia utamkaji wa maneno mbalimbali, humwelekeza aina nyingi za vitu, miti wadudu, wanyama na vitu ambavyo atahitaji kuchezea kadiri anavyoendelea kukua. Ilikuwa ni marufuku pia mtoto kutumia mkono wa kushoto hivyo ilikuwa ni kazi ya yaya kuhakikisha mtoto anazoe kutumia mkono wa kulia na alipokuwa anakuwa mgumu kutumia mkono wa kulia yaya aliripoti hilo kwa wazazi ambao waliufunga mkono wa kushoto na kitu kizito ili atumie ule wa kulia.

-Mtoto anapoendelea kukua hubadilishiwa mapishi ya chakula chake yakawa tofauti kidogo na yale ya kwanza, mtoto huanza kupikiwa chakula kiitwacho “kimantine” ambacho kwa sehemu kubwa ni chakula cha ndizi.

-Basi mtoto akiendelea vizuri na hatua ya kutembea wazazi waliweza kumpa yaya wake ruhusa aende zake ikiwa wazazi hawa si watu wenye wanyama wengi au upendo; mama na baba watamtunza mtoto wenyewe. Yaya alipewa ujira wake kumlea mtoto. Ujira wa Yaya ni mbuzi mmoja. Jinsi Mchagga ajuavyo kutunza mali yake ya wanyama, wazazi wa yaya wakiwa wema walimsaidia yaya kubadilisha yule mbuzi wapate ng’ombe kwa kumpa mbuzi mwingine wakawa wawili.

Ikiwa wazazi wa mtoto na wa yaya ni watu wanaopendana, yaya aliweza kuzidi kumsaidia mtoto kwa muda zaidi ya mwaka mmoja, lakini gharama huwa ile ile, yaani mbuzi mmoja na chakula. Yaya hodari, mwenye utii na kusaidia vema mtoto alipendwa , na amalizapo kazi yake ya kulea mtoto hakusahaulika kwa wazazi wa mtoto wala kwa mtoto akuapo. Alikaribishwa nyumbani kila mara.

Kumchagulia mtoto jina
-Mtoto akifikisha umri huu baba na mama humchagulia jina. Basi mtoto mzaliwa wa kwanza ikiwa babu yake ni marehemu huitwa jina la babu wa upande wa baba, na ikiwa babu yake yu hai ataitwa jina la babu wa babu wake. Binti hupewa jina la bibi mkubwa. Wazaliwao baadaye hupewa majina ya wajomba zao, au majina yanayoendana na vitendo vilivyowatokea wazazi au watu wan chi nzima vya furaha au vya kuhuzunisha. Mfano mara kwa mara husikia Mchagga akiitwa “Ndemasa”. Maana yake “Nilichuma mali, Mungu ni mwema”, vile vile kwa jina hili likiwa limeongezwa mwishoni “Ndemasandalye” maana yake ni nyingine yaani “Nilichuma mali lakini sikuitumia”, labda kwa kuwa iliharibika, ilipotea au alinyang’anywa na kadhalika.

Mwingine humwita mtoto “Ngao”, Maana yake amekumbuka jinsi siku moja au wakati mmoja alipokuwa akipigana vita ngao yake ikamsaidia sana, ama kwa msaada wa kitu chochote kilichomlinda na kumfaa siku za shida. Mwingine humwita mtoto “Kirama” maana yake “Umoja ni nguvu”. Mwingine humwita mtoto “Maangie” maana yake “Aliyeshangiliwa”. Mwingine humwita mtoto “Kikari” maana yake “Shujaa” au “Jasiri” na kadhalika.

-Hakika majina ya Wachagga mengi yana sababu zake. Hufuata ukoo na mambo za hali za watu. Mengine ni kwa ajili ya ushujaa, hata mengine ni kama siri ya historia, kwa mfano “Msagoni” maana yake amezaliwa wakati usio na ng’ombe. Wanawake hupewa majina ya bibi na mengine ya vitendo kama vile “Mkunde”(Aliyependeka). Mkamsuri(Mwanamke Tajiri). Au huitwa majina ya ukoo au ya mahali katika nchi, na majina hasa yanayotokana na vitendo vya taabu na furaha.
-Mtoto akifika umri huu hubadilisha chakula na kuanza kula vyakula vya watu wazima na kula muda ambao watu wazima wanakula, wazazi hawajali tena kwamba mtoto anahitaji kuendelea kujaliwa vyakula vya afya ili azidi kuimarika anapoendelea kukua. Kati ya makosa ambayo wazazi wa Kichagga hufanya ni kutokuweka nguvu tena kwenye kujali malezi ya mtoto hasa kiafya kutokana na kujishughulisha sana na kazi na hivyo mara mwingine hupelekea mtoto hudhoofika kiafya. Mtoto huendelea kufundishwa kazi ndogo ndogo za nyumbani na shughuli za kilimo, biashara na ufugaji. Waendapo shamba huchukua ndizi mbivu za kula au chakula. Chakula cha kulia shamba kwa Kichagga huitwa “kichau”.

-Basi tukiangalia katika umri huu binti huwa amezidishiwa kazi zake kuliko mtoto wa kiume wa rika lake. Watoto wa kiume hufundishwa ufugaji pamoja na shughuli nyingi za kijasiri. Watoto wote wa kike na wa kiume hufanya michezo mbalimbali ya kutumia nguvu kama vile kupigana na mieleka, kuruka juu ya miti na kutengeneza mashimo na mahandaki wanakojificha na kukimbizana. Watoto wa kiume walipigana vita vya michezo viitwavyo “kimandolu”, wakijiweka tayari na silaha zao hizi, na katika mapigano haya mtu aweza kuumia lakini ni hali ya mchezo tu. Nao watoto wa kike huenda sokoni, kulima na kuchuma majani ya ng’ombe. Katika michezo yao ya wakati huu ambayo ni ya juhudi sana, iwapo yuko mvulana au msichana aliaye hovyo kwa sababu ya maumivu ya michezo, wenzake humwimbia wimbo wa kumcheka ili aache kulia. Wimbo wenye ndio huu;

“Manene korio kelya kya mbuonyi, Mikasia ukoriosepfo kingi”.
Maana yake; Mlialia hovyo alishwe chakula cha puani badala ya mdomoni na kikiisha azidhishiwe kingine huko huko puani.

-Watoto wadogo hukaa nyumbani lakini wakifikia umri mkubwa wa kubalehe huchukuliwa kwenda kukaa na bibi na babu ili wafundishwe na kulelewa nao. Wakiwa kwa bibi na babu yao hujifunza mengi na kufanya kazi nyingi za mikono. Chakula kikiwa jikoni bibi huwasimulia hadithi nyingi za Kichagga kwa mfano hadithi ya Mregho ambayo nitaielezea baadaye.

-Watoto wa kiume hucheza mchezo wa “Oro” ambao mwandishi ameuelezea vizuri huku kwenye kitabu, ni mchezo mzuri wa ushindani na unaoweza kuburudisha sana watazamaji. Mchezo huu ulifaa sana kwa kuwafundisha watu kuweza kulenga wanyama wanaokimbia na adui vitani mikuki. Uliwafundisha pia umoja na utaratibu wa kufanya vita, kwani taratibu na sheria za mchezo huu ni ngumu na zilifuatwa kwa uangalifu sana. Huu ni mchezo ambao tungeweza kuundeleza na kuwa hodari sana katika huu mchezo na ukatupatia umaarufu mkubwa na manufaa ya kiuchumi.

-Kwa wastani wasichana walikaa kwa bibi zao kwa muda usiopungua miaka minane, watoto wa kiume hukaa muda mfupi zaidi kwa sababu wao huwa na mashughuli mengi yanayohusika na utawala wa Mangi wao na kusaidia nchi siku za shida.
Mafundisho babu na bibi wafundishayo watoto kama hawa wakati huu wa usiku ni kama haya;-

Hiki ni kichagga cha zamani kidogo kwa hiyo kuna baadhi ya misamiati imeshamezwa sana na Kiswahili kwa siku hizi, hivyo usijali sana kama kuna baadhi ya maneno yatakupa utata kuyaelewa.

“Mafundo ga mku ni matetera”. Maana yake: mafundisho na methali ya watu wetu wa kale huongoza maisha vema. Methali zenyewe ni hizi;-
i. “Meku o ngoru kalima na ngocha”. Tafsiri yake: “Mzee wa heshima alima akivaa majani”. Ufafanuzi wake ni huu: “Usiwaache wazazi wako katika hali ya shida, hasa wakiwa hawana nguo za kusitiri miili yao; wasaidie upesi.
ii. “Pora yako ngamekurina iyoe ngama undine-wo”. Tafsiri yake: “Ewe kijana wangu uliye jandoni nimekutahiri nawe kesho unitahiri”. Ufafanuzi wake: “Wazazi wamewalea na sasa hawana nguvu tena, kwa hiyo wasaidieni na muwaheshimu”.

iii. “Ipfo nuka kuipfo mdi mlotsu nyama”. Tafsiri yake: “Huko porini kuna mti mzuri wenye nyama”. Ufafanuzi wake: “Enyi watoto mnaopenda kuchungulia mizigo ya watu iliyofungwa kama kwamba mna nyama ndani, jihadharini; mkifuata desturi hii itawaletea madhara. Msidhani kila mzigo mnaouona una nyama ndani.

iv. “Ndewon ngungu, ndanwone chilyilyi”. Tafsiri yake: “Nimemwona mwewe bila kuona kundi la watu lililokusanyika kwa kusudi fulani”. Ufafanuzi wake: “Uendapo kuwinda porini ukaona kwa mbali ndege wakirukaruka karibu yake, ukadhani ni tai wanaruka karibu na mzigo wa nyama usifanye haraka. Chungulia polepole upate kuhakikisha: inaweza kuwa maharamia wamechoka, wakaketi chini ya mti ya mti ule na kutupa viatu vyao angani ili kushawishi wapiti njia au wawindaji wadhani kuwa viatu vile ni ndege warukao, wafuate mnyama aliyeko chini ya mti, na hivi maharamie wawarukie na kuwafanyia uharamia.

v. “Nyiku ndaina ndutu ya oro ilewuta pfinya ikakima ndafu?”. Tafsiri yake: Ni wapi beberu mdogo alipopata nguvu akaweza kumwonea beberu mkubwa maksai?”. Ufafanuzi wake. “Hata ukiwa na nguvu namna gani au uwezo, usijaribu kumwonea baba, kaka, au mkubwa wako yeyote. Waheshimu na kuwasaidia kwani ndio waliokulea”.

vi. “Kipfilepfile kirundu kechiwa mvuo kilawe”. Tafsiri yake: “Manyunyu ya kiwingu kidogo kilijaribu kwa mvua kisiwe”. Ufafanuzi wake: “Usione mawingu angani ukasema kwamba mvua itanyesha, jaribu kutumia maji ya mfereji ili kunywesha shamba lako”.

vii. “Koicho umbe lo Mangi lomkapo ma ulatire”. Tafsiri yake: “Ukisikia tarumbeta la Mangi likipigwa usikose kwenda”. Ufafanuzi wake: “Lazima uhudhurie kwenye mahitaji yote ya mtawala wako, ukikosa kuhudhuria utaweza kuadhibiwa. Pengine nchi yako iko katika hatari kubwa, na unahitajiwa usaidie”.

viii. “Nyi kiki kyaworo mregoni?”. Tafsiri yake: “Ni kitu gani kimenaswa kwenye mtego?”. Ufafanuzi wake: “Unapotembea ukashtukia mtego ambao umenasa mnyama, na ikiwa hujui mwenye mtego usimwondoe Yule mnyama. Ukimwondoe na mwenyewe akapata kujua, anaweza kukudhuru wewe na nchi yako”. (Methali hii imepata kutokea maeneo ya Kilimanjaro. Kwa mfano mtu wa maeneo ya Kirua Vunjo aliondoa mnyama ambaye alikuw amenaswa katika mtego uliotegwa na mtu wa maeneo ya Kilema iliyo jirani. Watu wa Kilema walipogundua, waliwadai watu wa Kirua mwishowe wakalipwa kwa sehemu ya Kirua ambayo ilichukuliwa na kuwa sehemu ya Kilema.

ix. “Mtoori o umbe nyi mka”. Tafsiri yake: “Mwenye kutoa habari za siri zako ni mwanamke”. Ufafanuzi wake: “Usizungumze siri na mwanamke hasa siri ya ng’ombe na mali nyingine ya wanyama walioko nyumbani.” (Sababu ya methali hii ni kuwa wanawake huenda kukata majani na humo huenda na humo huenda wakizungumza habari za mali bwana zao walizonazo. Kwa njia hii hutokea Mangi akadai ushuru wa utawala wake kwani amekwisha sikia kwamba fulani anayo mali kadha wa kadha kwa sababu ya uvumi wa mazungumzo ya wanawake).

x. “Ndaiya Mawuki-o-Kisima-Makyaala”. Tafsiri yake: Niite Mawuki bin Kisima wa Mtaa wa Kyaal”. Ufafanuzi wake: (Watu wa Mtaa wa Kyaala eneo la Marangu husemwa kuwa ni watu bahili, kwa hiyo wakikusaidia kitu watakuharibia).
xi. “Ipfue limwi soromu, gengi gakusoroma gakafo”. Tafsiri yake: “Nyani mmoja ametoka lakini huongezeka kidogo kidogo wakazidi”. “Ufafanuzi wake: “Ukiona watu watembeao mmoja mmoja mpakani mwa nchi yenu, kama vile nyani wanavyotembea wakienda kuiba mahindi, nenda pole pole uwachungulie, na wakiwa maadui nenda upesi umpashe Mangi habari”.

xii. “Lya Marashire lilepfaama lyikeera nyama ya Ndafu”. Tafsiri yake: “Manukato yamenukia kupita nyama ya beberu maksai”. Ufafanuzi wake: “Uendapo ukatumwa na Mangi ukamkuta mke wake, ambaye hunukia manukato, usipite karibu yake. Ukipita karibu yake unaweza kuambukizwa harufu ya yale manukato ya mke wake, na ukirudi kwa Mangi, akakusikia ukinukia manukato ya mke wake, ataweza kukudhania umezini na mke wake, hivyo utakuwa katika hatari ya kuuawa”.

xiii. “Aiyo mbero ngifunje kungo, ikalemberia Mkocha”. Tafsiri yake “Huyo ndege anayefanana na kipanga, amevunjika bawa lake, akamsingizia mtu aitwaye Mkocha(maana yake mtu mchokozi).” Ufafanuzi wake: “Usimwone kilema ukamcheka au kucheza naye ukazidi kumuumiza, unaweza kutozwa fidia”.

xiv. “Mooro mecha nyi ga mbogo, ka mooro ga nguwe nyi kiki?” Tafsiri yake. “Urithi mzuri ni wa nyati, je urithi wa nguruwe una faida gani?” Ufafanuzi wake: “Usifanye urafiki na kufanya ukahaba na mwanamke mjane, kwani unaweza kumaliza mali yako kwa kumhonga, na ukijaaliwa kuzaa mtoto, utachukuwa taabu zake zote na za mtoto. Ukizini na mwanamke mwenye bwana utalipa fidia mara moja tu, mke atabaki na mume wake”.

xv. “Molaa tengoni nyi mooru o saro una kigoro kii wanda, mbororo tsikayenda kwi?” Tafsiri yake. “Mwenye kulala katika kibanda kidogo kinachojengwa nyuma ya nyumba kubwa ni sawa sawa na mzinga wa nyuki wenye kitu kisichojulikana ndani yake”. Ufafanuzi wake. “Usimwoe mwanamke mgeni bila ya kuwajua wazazi wake na tabia zao na asili ya ukoo wake. Usiangalie uzuri wa mwili kuliko tabia na asili ya ukoo wake, anaweza kuwa na magonjwa mabaya ambayo yataharibu ukoo wako”.

Watoto hujifunza methali zote hizi na nyinginezo nyingi pamoja na mambo mengi ya kuhusu jamii ya kichagga na maisha kwa ujumla.
-Msichana anapoendelea kukua alifundishwa mambo mbalimbali ya kuhusu nafasi yake kama mwanamke hasa katika ndoa, mafundisho haya yaliitwa “shigha” na “mregho” ambapo waliweza kujifunza mambo mengi ambayo yaliwasaidia katika maisha yao. Msichana ambaye hakufundishwa “shigha” na “mregho” tunaweza kumfananisha na mtu ambaye hajasoma na yule ambaye alifundishwa mambo haya alipata heshima kubwa sana katika jamii. Wanaume walifundishwa mafundisho ya “ngasi” na waliweza kujifunza “mregho” wakiamua.

-Kuna mchoro uliokuwa kama fimbo uliokuwa na maeneo mawili moja ya juu kama mfuniko uliitwa “MSHINGO” na eneo la chini ambalo ndio sehemu kubwa liliitwa “MREGHO”, ambayo ilikuwa na sehemu nyingi zilizogawanyika zenye michoro aina tofauti tofauti na kila mchoro ulikuwa na maana yake. Vijana hawa walifundishwa namna ya kuchora mchoro huu wa “mregho” ambao ulichorwa katika mti ulioitwa “mringonu” kwa kukata michoro kwenye maganda yake ungali mbichi na kuacha ukakauka. Urefu wake ni kama mkongojo mzima, unaweza kuwa mfupi zaidi, bora tu michoro iweze kuenea na kusomeka.

-Kila aina ya mchoro huu una maana yake ambao huelezwa kwa mafumbo. Imegawanyika katika sehemu mbalimbali kadiri ya maeneo ya uchagga yaliyokuwa na michoro yao. Sehemu zenyewe za fimbo hii ni kama zifuatazo;-
i. Kirongocha: Huu ni mchoro wa upande wa chini wa fimbo ambako kumepekechwa tundu mbili ndogo fupi, moja ni kubwa kuliko nyingine. Wachagga huitaja sehemu hii hivi: “Kirongocha kilekurongocha cha lilya wakeku(bibi wakubwa) akurongocha kawada njia yeende mana, ma kima alalewada njia yeende mana nyi kwui awu na wama wawechiida wache ilufee?”
Tafsiri yake: “Kirongocha ni kipekecho kilichopekechwa kama vile bibi alivyoumbwa akawa na viungo vya uzazi akaweza kumzaa baba na mama, kwa sababu kama hakuwa na njia ya uzazi asingaliweza kuwazaa wazazi wetu. Ufafanuzi wake; Farji ya mwanamke

ii. Moselu: Hii ni picha ya kitu kilichochongeka, nayo husemwa hivi; Moselu alikuseluo cha lilya mendi awu na wama waseluo nyi ambo(kisu cha kutahiri) lilya mendi warino wakayeremka mbiu yawo wakawa wandu warine, wakakundana, wakaalikana, naaho wakafee wana wakaghorokia uruka lu na Mangi yawo meendi ghalya neenu”.

Tafsiri yake: “Moselu ni kkitu kilichochongeka kama vile wazazi walivyotahiriwa kwa kile kisu cha kutahiria walipokuwa katika ujana wao wakatakata, wakapendana, wakaoana wakazaa na wana ambao wamesimamia nchi wakasaidiana na Mangi wao mpaka hivi leo.

Ufafanuzi wake: “Tohara ya wazazi ni takaso kabla ya ndoa”.
-Sehemu ya 3, 11, nay a 15 zote huitwa kwa jina la “MSHINGO”, maana yake ni kizibo. Mshingo wa kwanza husemwa hivi; “Mshingo ulekushinga cha Msanya akushinga lya Ndaalyio lya mendi au wusunyi”.
Tafsiri yake: “Kizibo kimejiziba kama vile Msanya(jina la mwanamke) alivyojiziba alipokuwa na mimba ya mtoto wake Ndaalyio”.

Ufafanuzi wake: “Mwanamke mwenye mimba haingii mwezini”.
Sehemu nyingine za mshingo zinazidi kueleza kwa mafumbo kama fumbo hili mambo yanayohusu mwanamke kuingia mwezini.

iv. Sehemu ya 4, 6, 8, 10, 12, 16 na ya 18 huitwa kwa jumla “MREGHO” maana yake “Mchoro”. Zote zina miviringo ambayo jumla yake ni miviringo 65. Hueleza habari za mtoto anavyopata viungo vyake katika tumbo la mama yake. Kila mviringo unataja kiungo kimoja na kazi yake jinsi mifano ifuatayo inavyotuonyesha.

a. “Mregho ulekuregha cha kiki, ulekuregha cha ili mndu mka akurega na monoke usunyi, more ochiumba kaghamba lako nyi ashimbo nyi ndewu numa kakoya nyi more. Tafsiri yake: “Mchoro umejichora kama vile mwanamke mzito anapokuwa na mimba ya kwanza akadhani kwamba amevimbiwa, lakini kwa sababu ya kujua “Shigha” na “Mregho” akafahamu kwamba hakuvimbiwa bali kichwa cha mtoto kinaumbwa katika tumbo lake. Ufafanuzi wake: Kichwa cha mtoto kinaumbwa katika tumbo la mama.

b. “Mregho ulekuregha cha kiki, ulekuregha cha simba ikakuregha na monoyo ikawara mawoko maapfinya ikaowesha mando goose ikawona nyama”. Tafsiri yake: “Mchoro umejichora kama vile simba jike mwenye mimba alivyojitunza hivi kwamba mtoto aliye tumboni akapata mikono yenye nguvu, akatisha wanyama wote porini, akapata nyama za kula”. Ufafanuzi wake: “Mikono ya mtoto inaumbwa tumboni mwa mama yake ili apate kufanya nayo kazi ajipatie riziki yake.
c. “Mregho ulekuregha cha kiki, ulekuregha cha kilodanga(sungura) akuregha na monoke karosa maru gearanyia”. Tafsiri yake: “Mchoro umejichora kama sungura aliye na mimba alivyomlea mwanawe tumboni akaota masikio ya kusikiliza”. Ufafanuzi wake: “Mtoto anaota masikio tumboni mwa mama yake”.

d. “Mregho ulekuregha cha kiki, ulekuregha cha njofu ikuregha na monoyo ikalya na mara ga mtsuru ilyi iwei na uroo woyo imana lyikawada madende maapfiya gechumia ipfo ngurunyi. Tafsiri yake: “Mchoro ulijichora kama vile tembo alivyolea mimba yake kwa kula majani ya msituni, mtoto wake akapata miguu ya nguvu ili aweze kutembea msituni”. Ufafanuzi wake: “Mchoro unaonyesha miguu ya mtoto inaumbwa tumboni mwa mama yake”.

e. “Mregho ulekuregha cha kiki, ulekuregha cha mbeta ikuregha na ialeya lyalo likachewara meso makaramtsu yekuringa na mlasi”. Tafsiri yake. Mchoro umejichora kama njiwa alivyojichora na makinda yake yakapata macho ya kumwezesha apate kujificha mwindaji anapokaribia. Ufafanuzi wake: “Macho yanakuwa tumboni mwa mama yake”.
Michoro hii ya Mregho huendelea kutajwa hivi kwa mafumbo, kila mviringo ukatajiwa mnyama fulani mwenye uzuri wa mwili au kiungo kinachopatana na uzuri au kiungo kile cha mtoto kinachoumbwa katika tumbo la mama.

Sehemu ya 5, nay a 7 huitwa “MOLEMA”. Maana yake ni mchoro ulikunjwa. Huitwa hivi kwa sababu kila sehemu ina michoro saba iliyokunjika, hivi jimla ya michoro ni kumi na mine. Kila mmoja wa michoro hii unaeleza kwa mafumbo habari, kazi na taratibu za utawala wa Mangi, kama mifano ifuatayo inavyotuonyesha.

a. “Molema ulekulema cha Mangi alema uruka kalusanyia handu hamwi lulanyanyarike”. Tafsiri yake: “Mchoro umekunjika kama Mangi alivyokunja nchi akaikusanya pamoja ili isitawanyike”. Ufafanuzi wake. “Mangi ndiye mlinzi wa nchi, huzunguka nchi yake akajishughulisha hivi ili watu wake wasitawanyike, bali wawe pamoja chini yake. Hivi Mangi huikunja nchi akaikusanya”.

b. “Molema ulekulema cha njofu ikulema ikashaa mana kawada membe, Mangi kawutaho membe tso karing natso uruka na wusuri woke”. Tafsiri yake: Mchoro umejikunja kama ndovu alivyojikunja akazaa mtoto, akaota pembe, Mangi akazichukua pembe hizi akalinda nchi na utajiri wake”. Ufafanuzi wake: “Pembe za tembo ni zenye thamani sana, kwani kwazo Mangi hulinda nchi pamoja na utajiri wake(kwa mfano watu wakichukuliwa mateka Mangi hulipa pembe za tembo ili kuwakomboa; au ikiwa nchi ina deni la nchi nyingine Mangi hulipa pembe za tembo.

c. “Molemo ulekulema cha uruka lo Mangi lukulema na marasa yalo na ngyuruka tsa mrasenyi”. Tafsiri yake: “Mchoro umejikunja kama nchi ya Mangi ilivyojikunja mipakani inapopakana na nchi za majirani”. Ufafanuzi wake: “Matengenezo ya utawala kati ya nchi za majirani”.

d. “Molema ulekulema cha Mangi na njama tsake kulya mengenyi yake kasungusiapfo wandu na moondu yawo woose, uruka lukoramia”. Tafsiri yake. “Mchoro umejikunja kama vile Mangi aketivyo na raia zake kwenye uwanja wa baraza, akaweza kuonana na kuamua mashauri ya raia wote. Ufafanuzi wake: Kuamua mashauri ya watu.
Michoro hii huendelea kutaja mafundisho ya namna hii kwa mafumbo.

Sehemu ya 9, 13 na ya 17 huitwa “MONJARO”, maana yake ni “Michoro” au “Mchoro” wa mkwaruzo. Hii ni michoro ambayo katika sehemu zote imo jumla ya michoro 25. Kila mmoja hueleza kwa mafumbo mbalimbali, shughuli zote zinazohusu raia wa nchi na ubora wake, kama ukulima, biashara, ufugaji, mapishi na vinginevyo. Mifano ifuatayo inaonyesha jinsi mafumbo haya yanavyotajwa.

a. Monjaro alekucharuo cha wandai, ma sile wandai nyi kwi muwechirema shelya” Tafsiri yake: “Mchoro umejikwaruza kama ardhi ilivyotokea kwani ardhi isingalikuwako tungelilima wapi tupate chakula?”. Ufafanuzi wake: “Ukulima”
b. Monjaro alekucharuo cha mtsana o menya akucharua na ng’anya yake lilyamandi alutsanyia ng’ori ikalasa umbe waka wakanyo mlaso”. Tafsiri yake: “Mchoro umejikwaruza kama vile mhunzi alivyojikwaruza alipokuwa akitufulia chuma cha mshale ya kutobolea vena ya ng’ombe akiwa hai ili wanawake wazazi wapate damu yake yenye nguvu wainywe. Ufafanuzi wake: “Uhunzi”.

c. Monjaro alekucharuo cha mmbe ikucharuo kulya mmba ko Msanya(jina la mwanamke) ikashaa lukanyopfo maruwa, na sari yealyia nginda”. Tafsiri yake: “Mchoro umejikwaruza kama vile ng’ombe alivyojikwaruzo kwenye nyumba ya Msanya akazaa, tukapata mazima ya kunywa na mbolea ya kustawisha mashamba yetu. Ufafanuzi wake: “Kwa ufugaji wa ng’ombe tunapata maziwa ya kuwapa mama wazazi na mbolea ya kustawisha mashamba yetu”.

Sehemu ya 21 “MOFULU” , hii ndio mwisho wa fimbo na ni tundu dogo iliyopekechwa ndani, nayo husemwa hivi: “Mofulu ulekufuluo cha lyilyendi womoo ekufee kofuluka kulya ndewunyi kosongora mroe uwefeo, kocha na mafuo ghapfo”. Tafsiri yake. “Mchoro umejitengeneza kama vile mama alipokuwa akikuzaa, ukageuka tumboni mwake ukatanguliza kichwa ulipokuwa ukizaliwa, ukaja duniani u mzima na viungo vyako vyote”. Ufafanuzi wake. “Mtoto mzima anazaliwa na viungo vyake vyote”.

-Katika tundu ya hii Mofulu huwekwa udongo mwekundu uitwao “kimaande”; maana yake tendo hili ni kwamba wasichana wa rika wakiisha soma michoro hii na kuhitimu wakatembea na fimbo iliyokwisha chorwa hushindana na wasichana wengine au wavulana wajuao kwani yalikuwa mambo makubwa na ya kujivunia miaka hiyo. Msichana ambaye hakujifunza hayo alifanana na mtu ambaye hajasoma wa miaka hii. Inaonyesha kuhitimu katika masomo ya ujana.

-Mwisho wa mafundisho haya ya “Shigha” na “Mregho” Mwalimu wa haya mafundisho husema “Wana wako ngamempfunda mapfundo ghang’anyi, ngama nanyoe mupfunde wananyu. Hoi Ruwa malele, hee”. Tafsiri yake. “Wanangu nimewafundisha mafundisho makuu nanyi mpate kuwafundisha wadogo zenu. Ee Mungu na iwe hivyo milele”.
-Mambo mengi ya aina hii na mafundisho mengi haya yalitokea kabla ua pamoja na katika karne za 17, 18 mpaka 19 hivi lakini wakati kitabu hiki kinaandikwa miaka ya 1940’s mambo mengine yalikuwa yameanza kupotea. Hapa unaweza kuona kwamba Wachagga miaka ya nyuma kabisa hata kabla ya Wamisionari na Wakoloni waliweza kuwa na utaratibu wa kupeana elimu iliyotanua sana fikra zao na kukuza busara yao katika kukabiliana na mambo mengi ya maisha japo mengine ilihitaji kuboresha zaidi au kupatiwa mfumo mzuri zaidi katika kuitoa.

-Katika kila rika linaloingia katika utaratibu wa Wachagga miongoni mwa vijana wa rika huchaguliwa vijana kumi na wawili ambao hufundishwa siri za michoro juu ya mawe. Vijana wakiisha fundishwa mambo hayo hupelekwa kwa Mangi wakaapishwe wasitoe kamwe siri zinazohusu Mangi na nchi nzima. Vijana hawa watakuwa kazi yao ni kuaminiwa na kuwa wasiri wa Mangi na nchi. Iwapo nchi imepigwa vita , Mangi akalazimishwa kuondoka nchini mwake, baadhi ya vijana hawa watafuatana naye popote aendapo, na wengine watabaki nchini wakaaminiwa kuficha mali ya Mangi salama bila ya kumwonyesha mtu yeyote, mpaka hapo Mangi atakapoweza kurudi nchini mwake. Wao ndio wanaoanza kuarifiwa ikiwa Mangi anataka kuipelekea nchi jirani vita; pia wao ndio wapenzi wa Mangi wanaotumwa naye kwa ujumbe wa siri wowote.

NDOA
-Wachagga ni watu wa jamii moja na taifa moja lenye watu wa koo mbalimbali, nao wameishi kwa kuchanganyika sana toka karne nyingi zilizopita. Kwa hiyo desturi na kanuni za maisha yao ni moja katika maeneo yote ya Uchagga kutoka mashariki kwenda magharibi japo unaweza kukuta tofauti kidogo sana zinazotokana na tawala hizi na umbali wa kijiografia. Lakini desturi zao zote zina kiini kimoja na tofauti ndogo sana zilizopo si kubwa wala za maana sana. Desturi za maeneo yote ya Uchagga ni moja lakini mabadiliko huweko tu katika wingi wa mahari itolewayo. Sababu za kutoa mahari zilikuwa ni hizi zifuatazo; Wazee wa mvulana na wa msichana hutaka kukamilisha umoja utakaokuwako kati ya koo za mvulana na msichana. Umoja huu hukamilishwa , kwani mali na vyakula vitolewavyo ni vya ujamaa kati yakoo hizi mbili.

-Zamani ilikuwa baba wa mvulana akisaidiana na watu wa ukoo wake ndiye hutoa mahari. Ilikuwa hivi kwa sababu msichana anachukuliwa kama yuko chini ya mume wake atakayemuoa, yeye ndiye anamchukua msichana kwa kumchumbia na baadaye anamtoa kwa wazazi wake na kumpeleka nyumbani kwake kumwoa. Akishaolewa huwa sehemu ya ukoo wa mvulana. Mahari yanayotolewa hayakuchukuliwa kama bei ya kumnunua mke. Wazazi wa mvulana walitoa mahari ili kukamilisha ujamaa wa koo hizi mbili wakionyesha uwezo wao. Pia ilikuwa ni alama ya kuonyesha upendo baina ya koo hizo mbili, wazee wa mvulana kutoa mali kama shukrani kwa ukoo wa msichana kwa kupewa huyo msichana awe mchumba na baadaye mmoja wa wanawake wa ukoo wao. Ilikuwa pia njia mojawapo ya kuweza kukutanisha watu wa koo nyingine mbalimbali wakajuana, na taifa la wachagga likaimarika zaidi. Mahari ilitolewa kwa nia safi; Hakuna Mchagga aliyekubali kusamehewa kulipa mahari japo mara nyingi familia za binti zilikuwa zikisamehe mahari ikiwa huyo bwana hana uwezo mkubwa.

Jinsi Mvulana na Msichana Walivyochumbiana
-Zamani katika Taifa la Wachagga watu walifunga uchumba baada ya kuonana uso kwa uso katika sherehe au ngomani, au, baada ya kuongozwa na wazazi au dada, mvulana alimwendea msichana na kumtaka wafunge uchumba. Mvulana afikapo kwa msichana humwuliza “Mimi ninakupenda sana na ninataka uwe mchumba wangu; je nawe unanipenda kiasi hicho?” Ikiwa msichana anampenda humjibu, “Ndiyo nakupenda lakini kwanza ukapatane na wazazi wangu, wakikubali basi mimi nitakubali pia kuwa mchumba wako”.

-Mvulana hurudi nyumbani kwao, na kuwaeleza wazazi wake kuwa amekwisha kubaliana na msichana fulani, iliyobakia ni kuwashawishi wazazi wake msichana. Wazazi wake mvulana humjibu, “Sasa usifanye haraka wala sisi hatutataka kuonana na wakwe zako mpaka kwanza tumechunguza tabia za huyo binti na desturi zake, vile vile mpaka tumejua habari za ukoo wao toka hapo zamani kama kuna maradhi mabaya kama ukoma, wizi, uchoyo, ufukara na mengineyo.

Kadhalika msichana naye humweleza mama yake humuuliza “Nimpende huyu kijana?”, Mama naye humwambia, “Ngoja kwanza nitachunguza habari za ukoo wao, kama si watu wakali na wachoyo, wavivu, waongo na wenye laana”. Pande zote mbili, yaani wazazi wa mvulana na wa msichana watapima katika mashauri haya, kila upande peke yake. Jambo moja kubwa ambalo wazazi wa pande zote wanaloangalia ni kama baina ya koo hizo mbili wamewahi kushtakiana mbele ya Mangi kwa madai kwa jambo lolote, basi watu hawa hawakuozana kamwe.

-Basi baada yahapo taratibu nyingine za uchumba ziliendelea kwa pande zote mbili kukaribishana nyumbani kwa pombe na kuchinja, walikunywa na kucheza sana mpaka hatua ya uchumba kukamilika. Baada ya hatua ya uchumba kukamilika ziliweza kuanza taratibu za ndoa ambazo nazo zilihusisha michakato mingi sana, hasa sherehe za kualikana pande zote mbili watu wakanywa, wakala, wakacheza sana ngoma na kusherehekea, kujua kucheza vizuri ilikuwa kati ya mambo yaliyoangaliwa sana na wachumba na watu waliotaka kuchumbiana. Katika maeneo yote ya Taifa la Uchagga ilikuwa ni mwiko kumfanyia harusi ya desturi binti ambaye hakuwa bikra. Heshima ya harusi iliyozingatia desturi za kichagga ilikuwa anafanyiwa tu binti aliyeweza kutunza usichana, hivyo mabinti wa enzi hizo walikuwa wanakuwa mabikra mpaka kufikia kuolewa.

-Baada ya taratibu zote kukamilika mpaka hatua zote za uchumba mahari na harusi kuandaliwa na maharusi wote kupewa mafunzo mbalimbali ya harusi zao, sasa mzee wa kuongoza maharusi huanza kuwaoza hawa wawili na kuthibitisha kama ni kweli waliozwa mbele ya mashahidi wawe mume na mke waliooana kwa sheria ya Kichagga. Mbele ya mashahidi wale wawili ambao ni wadhamini kwa Kichagga hujulikana kama “Wakara” ambao pia waliwabeba bibi na bwana arusi na watu wengine walioko pale nje, mzee huyu wa kuongoza mambo ya harusi huchukua mkono wa kulia wa bwana kisha akauchukua nao wa kulia wa bibi harusi, na huuweka ule wa mume juu ya mkono wa mwanamke, na kuushikilia hapo akisema, Mbarilie ichu nyi mka opfo”, yaani “Mpokee huyu ni mkeo”. Bwana harusi ndipo humchukua mke ndani ya nyumba. Wakiingia wale wadhamini huwafuata; wakiisha kuingia ndani ya nyumba ndipo huachiana ile mikono mbele ya wale wadhamini.

KIFO NA MAZISHI YA WACHAGGA
-Mchagga yeyote alisemekana hawezi kufa kiurahisi isipokuwa kwa kukosea yeye mwenyewe, yaani ikiwa hakutimizi desturi za ukoo wake au kwa bahati mbaya akiugua na hivi huweza kufa upesi. Kwa hiyo mara auguapo humbidi kufikiri matendo yake kabla hajaugua, yaani alijaribu kufikiri kama alipuuzia kufanya wajibu uliompasa au ikiwa hakutimiza desturi zake za kutambika, au ikiwa amewahi kutokewa na kitu gani katika maisha yake ambacho ni asili ya bahati mbaya kama kurogwa au kuugua. Mchagga akikaribishwa hawezi kula au kunywa kitu chochote mpaka mwenye nyumba aonje chakula au kinywaji hicho mbele yake, aliogopa sana kurogwa. Hii pia ni moja wapo ya sababu wachagga walikuwa hawali ndani ya sahani mtu peke yake, wote hulia sahani moja.

-Mchagga alijaribu kutambikia kwa mizimu pia kama alifikiri labda kuna namna jamaa zake wa huko kuzimu wanamtaka afanye jambo ambalo amekuwa akilipuuzia. Lakini kama bado itashindikana basi alirudi kwa Mungu(Ruwa) ambaye aliamini yeye ndiye mwamuzi wa mwisho na mwenye mamlaka yote. Ilisemekana kwamba Mungu “Ruwa” hana uchu na mali ya mtu kama mizimu, yeye ni tajiri na karimu wala hana uchu sana na roho za watu. Hii ndiyo sababu Mchagga hakukimbilia kwake kwanza, aliwahi mizimu kwanza. Ndugu na jamaa za mgonjwa walichinja ng’ombe mjamzito wakati wa mchana jua likiwa utosini kumwomba “Ruwa” amponye mgonjwa wao. Hilo ndilo lilikuwa tumaini la mwisho lililokuwa kwa mgonjwa na jamaa zake.

-Majina ya sifa za “Ruwa” Wachagga wanazomtaja nazo wakati wanamtambikia na kumwomba, na maana yake ni haya; “Ruwa, fumvu lya mku”, maana yake ni kusema Mungu ni kama mlima wa kale na kale kama Kilimanjaro. “Ruwa Matengera” maana yake, Mungu anawatunza wanadamu kuwalisha maisha na kuwalinda katika hatari nyingi. “Ruwa molunga soka na mndo”, maana yake, Yeye ni Muumba na Mwenye kuunganisha watu kama katika taratibu ya ndoa, mtu na mke wake. “Ruwa”, maana yake ni mkuu achunguliaye watu kwa kuwatunza katika maisha yao kama jua wakati wa mchana. Iwapo Ruwa alimpenda alichukua kiumbe chake, kwani zote ni rehema zake kuishi au kufa. Iwapo mgonjwa amekufa, basi, loo! Kwa wachagga ni kama kinyume cha upendo wa Ruwa: watu hulia na kuhuzunika sana kiasi kwamba wengine hutamani hata kufa naye marehemu.

-Mchagga akifariki taratibu za kumzika ziliandaliwa ambpo alioshwa vizuri na kuvishwa sanda ambayo ilikuwa ni ngozi ya mnyama, kaburi lilichimbwa la urefu kama wa mita sita yakatandazwa majani ya mgomba ndani ya kaburi na miti aina ya “sale” pembezoni mwa kaburi kisha marehemu akawekwa ndani yake akiwa ameketi akiutazama mlima Kilimanjaro kisha wakafukia kwa kufuata utaratibu maalum. Mchagga akifariki kama alikuwa ameoa/ameolewa alizikwa ndani ya nyumba yake lakini kama alikuwa kijana ambaye bado hajaoa/hajaolewa basi alizikwa shambani nje ya nyumba.

Taratibu nyingine kama za kuanua tanga na mambo ya mirathi zilifuata. Baada ya mwaka mmoja kaburi walifukua kaburi kwa kuchimba kutokea nje ya nyumba kuingia ndani wakaondoa mifupi yote na kufukia upya. Mfupa wa fuvu la kichwa na mkono wa kulia waliliweka tofauti na mifupa mingine. Mifupa ilikusanywa ikawekwa kwenye kigae kama kibakuli hivi wakafunika na juu kisha wakatengeneza sehemu moja shambani katikati ya shamba la migomba sehemu yenye miti ya “masale” wakatengeneza kama mawe au mafiga matatu na kubandika moja juu ya yale matatu, ambapo walikuwa wameshachimba na kufukia ile mifupa iliyokuwa imefunikwa na vigae na kuweka juu yake ndani ya yale mawe/mafiga matatu wakaweka lile fuvu na kichwa na mkono wa kulia. Hapo ndipo ilipokuwa nyumba ya milele ya marehemu.

-Kama marehemu alikuwa na mke aliweza kurithiwa na ndugu wa marehemu kwa kufuata utaratibu maalum. Kama marehemu alikuwa ameoa halafu akafa kabla hajapata mtoto basi mke wake aliweza kurithiwa na ndugu wa marehemu, ambapo ndugu huyu akizaa mtoto na mke wa marehemu watoto hao watakuwa ni watoto wa marehemu na watamwita huyu ndugu wa marehemu baba mdogo licha ya kwamba ndiye baba yao mzazi na endapo atakuwa hawajali au kuwahudumia vizuri wanaweza kumfukuza nyumbani kwao. Watoto wao humtambua marehemu kama baba yao halisi.

MAZISHI YA WAMANGI
-Mangi walizikwa mchangani kama watu wengine, lakini kabla ya kuzikwa walitiwa ndani ya chombo cha mti uliochongwa ndani yake wazi kama mzinga wa nyuki mkubwa kama pipa. Kifo cha Mangi hapo zamani kilifichwa sana, pia siku hizo Mangi alikuwa haonekani na watu wote kama aonekanavyo siku hizi. Kazi zake nyingi zilifanywa na nduguye na mawaziri na wachili wa mtaani. Watu matajiri vile vile walisaidia nchi kwa kila njia wakapewa heshima na wao walikomesha fitina katika nchi wakimtii Mangi wao tu na watu wengine walikubali wakiona wale wakubwa na wazee wa nchi wamejiweka chini ya utawala.

Basi walificha habari za kifo cha Mangi kwa muda wa mwaka mmoja watu wasijue, hasa watu wan chi majirani, kwa sababu jambo kama hili likijulikana mapema ilikuwa pengine maadui walishambulia nchi hii katika msiba wao mkubwa huu na kuuharibu, na nchi itachafuka kabla ya kumtawalisha mtoto mrithi wa Umangi. Basi kifo chake kilifichwa, watu wakadanganywa kuwa Mangi ni mzima wa afya wakati ng’ombe zikichinjwa na pombe kunyweka sana, watu wajirusha usiku kucha wakisherehekea. Nyimbo za kumsifu Mangi na watu wake ziliimbwa na mambo mengine mengi, hapo Mangi alikwisha kufa kitambo.

-Jambo hili hujulikana tu kwa ndugu mrithi wa Mangi, waziri, mama wa Mangi, watoto na ndugu zake wakubwa na pengine kwa watu wakubwa wa nchi tu. Mambo haya ya kuficha kifo cha Mangi yakiendelea kwa muda basi waziri na ndugu za Mangi huanza kutengeneza habari za kumtawalisha mtoto mrithi wa marehemu; wale watu wakuu wa nchi na wachili wakubwa waliitwa kuapa kwamba watakaa kwa uaminifu na utii chini ya utawala mpya.

Wakimaliza huandaa siku maalum ya kumtawalisha mtoto mrithi wa nchi wa marehemu; wale watu wakuu wa nchi na watu wote wa nchi waliitwa, ng’ombe wengi walichinjwa na pombe nyingi ilitengenezwa. Mambo ya taratibu za kumtawalisha Mangi yalifanywa na watangulizi wa nchi. Watu huambiwa Mangi mzee sasa na hali yake sio nzuri, kwa hiyo mwanawe ametawalishwa aongoze nchi; mwenye akili zake hujua Mangi ameshafariki, lakini wengi huchukua habari hizi kama walivyoambiwa na wazee wakuu wa nchi. Wakishamaliza hizi taratibu na kuimarisha nchi basi waziri au ndugu mkubwa wa Mangi alitangaza wazi kwamba Mangi mzee alikufa na kuwaambia kwamba wako kwenye msiba mkubwa. Watu walilia na kuhuzunika sana lakini nchi ilikuwa imara kwa sababu watu wakubwa walikuwa wanaelewa siri zote.

IMANI YA WACHAGGA “RUWA”
-Wachagga huamini “Ruwa”(Mungu) kwamba ni Mkuu kupita mizimu yote wanayotambikia. Huyu Ruwa hasumbui wanadamu kwa sababu ndogondogo kama vile mizimu iwasumbuavyo ikiwa haikutambikiwa. Tambiko alilotolewa Ruwa ni tofauti na tambiko la mizimu kwa hali na sababu.

Wachagga humjua Ruwa toka kwa wakale wao. Hawa walisema kuwa wanadamu na viumbe vyote ni lipuko la Ruwa. “Walipasuka” kutoka kwake. Walimpa Ruwa heshima wakimtaja kwa majina haya manne yaelezayo heshima na kazi zake.
(a) “Ruwa” maana yake, aeneaye popote kama jua limulikalo ulimwenguni mwote pasiwepo kiumbe ama kitu kiwezacho kujificha
(b) “Matengera” maana yake, aleaye viumbe vyote kwa taratibu zake kwa amani.
(c) “Fumvu lya Mku” maana yake, mlima wa kale
(d) “Molunga Soka na Mndo”, maana yake ni kwamba kwa uwezo wake kila kiumbe chake chenye uhai huwa na taratibu ya kuwa mke na mume, watu wakazaliana, kama vile kuunga shoka na mundu, jambo ambalo ni gumu sana.
-Wakaamini kwamba yeye kwake ni juu “nginenyi” (kwenye jiwe kubwa la rangi ya samawati lionekanalo mbinguni). Kwa majina hayo manne Ruwa, Matengera, Fumvulya Mku, na Molunga Soka Na Mndo, ni sifa zake pekee na ndizo nguzo za imani ya Mchagga. Wachagga wamtambikiapo Ruwa huua beberu mweusi kabisa kila mahali ama mwekundu au mweupe kabisa, asiye na doa lolote, ambaye hakukatwa mkia, kwani kwa desturi Wachagga hukata mbuzi beberu mikia kabla hawajaweza kupanda. Huyu mbuzi huuliwa mahali palipoinuka kwenye kilele cha nyumba ya kichagga, majina yale manne ya heshima zake hutajwa na mzee mkuu wa ukoo wa huyo mgonjwa anayetambikiwa, na jamaa zake hutazama juu “nginenyi” na kuomba Ruwa amponyeshe mtu wao.

-Mzee huyu husema maneno ya namna hii: “Iyoe Ruwa Mangi Matengera, Iyoe Fumvu lya Mku, Molunga Soka na Mndo, lokuinenga ndaina yi ya ufano lopfo ili ukire mndu chu odu hoi na hoi Mangi”. Akiisha sema hivyo mbuzi huuawa. Mbuzi mwenyewe hatemewi mate kama wale wa kutambikia mizimu. Saa za kutambikia Ruwa zilikuwa wakati jua limesimama katikati angani, yaani ni kama saa sita mchana. Ikiwa kuna mawingu basi walibahatisha tu. Wakishamchinja walikula nyama wakaenda zao. Hali kadhalika ikiwa mnyama aliyechinjwa ni ng’ombe, alitafutwa ndama mwenye rangi moja tu au ng’ombe wa miguu minane yaani ng’ombe mwenye mimba. Ruwa alitambikiwa/kutolewa sadaka ikiwa nchi ina njaa kuu au maradhi makali.

-Wachagga waliamini kwamba watu wa jamii zote walilipuka kutoka kwa Ruwa na polepole wakajaa ulimwenguni. Husema kuwa Ruwa anawapenda kwa sababu hawasumbuliwi naye kama vile wachawi na mizimu wanavyosumbua kwa kutaka gharama na tambiko za namna nyingi kila siku. Tambiko/sadaka kwa Ruwa ni moja na hutolewa kwa sababu moja tu. Katika imani ya wachagga hakukuwa na shetani, mapepo wala malaika.

-Lakini pamoja na yote hayo kwa sababu ya kutishwa sana na uchawi na mizimu karibu wingi wa matambiko ulitolewa kwa mizimu. Wazee waamkapo kila asubuhi walifungua nyumba wakatoka nje na kutazama upande wa kaskazini kunako mlima Kilimanjaro na kuinua kichwa wakatema mate mara nne, “Tuu, tu, tu, tu”, wakamwita Ruwa kwa majina na sifa zile nne na kumshukuru kwa uzima walioamshwa nao kwa asubuhi alfajiri tu, na ni wazee wanaume tu wenye mamlaka ya kufanya hivyo; wanawake wajane wazee pia huweza kufanya hivyo. Hivyo ndivyo Wachagga walivyomjua Ruwa kuwa ni mkuu kupita viumbe vyote; nay a kuwa Ruwa ndiye mwenye nguvu kupita mizimu yote juu ya roho za binadamu, kwani kwake ndiko walimwengu walikolipuka wakaja kuzaliana duniani.

“MIZIMU”
-Wachagga zamani waliamini na kutambikia mizimu, yaani watu wao walio marehemu. Waliamini mtu akishakufa bado alikwenda kuishi tena kule kuzimuni, lakini si kwa mwili huu tulio nao. Walisadiki kuwa hawa mizimu hula na kunywa, na kuweza kuja tena duniani na kudai haki zao walizokuwa wakipata kwa jamaa zao. Wajapo kudai sehemu zao kwa jamaa zao walikuwa wakija wakati wowote wanapotaka; lakini hawaonekani na mtu yeyote kwa sura yao bali huonekana kama katika ndoto au fahamu. Walijua kama mtu alikuwa na maovu mengu hapa duniani, hata huko kuzimuni atapata taabu, yaani hataweza kuonana na jamaa zake na kuweza kukaa nao huko.

Jamaa zake huku duniani wakifanya tambiko kwa kumuombea kwa ndugu zake wampokee na kushirikiana naye huko ahera ndipo anapopata nafasi nzuri ya kuonana na wale wamjuao na kukaa nao. Walijua pia kuwa Wamangi wafapo walikwenda kutawala tena huko ahera kama hapa duniani. Waliamini ya kuwa ikiwa mtu analo tendo baya ambalo hakuwahi kulitengeneza akiwa hapa duniani, aendapo akafa tendo lile ovu litamfuata mpaka aombewe na jamaa zake wa hapa duniani. Ikiwa hakuombewa kwa tambiko ili apate msamaha huko kuzimu, huyu mtu atapewa mahali pake yake asiweze kuonana na jamaa zake; mwishoni atapelekwa katika ahera ya tatu iitwayo “Kiragaifu”, maana yake ni ahera ya watu ambao hutokomea kabisa hata wakawa kama majivu. Jamaa walio hai hawataweza kukutambikia tena kwa kuwa tambiko la watu wa duniani haliwezi tena kuwafikia.

-Kazi ya mizimu ni kudai sehemu na taratibu zao walizokuwa wakitendewa walipokuwa hai hapa duniani. Waliombwa msamaha kwa makosa waliofanyiwa na watu wa hapa duniani, wakatakiwa pia watoe msaada kwa kuondoa maradhi waliyowaletea watu au jamaa zao hapa duniani. Huombwa kwa tambiko.

USAWI (UCHAWI) KWA WACHAGGA
-Katika nchi ya Uchagga tuliogopa sana “usawi” (uchawi) toka zamani sana. Huu uchawi ulitisha watu wote, wakubwa kwa wadogo, waume kwa wake, watoto mpaka Wamangi. Ulitisha kuliko magonjwa ya kifua kikuu na ndui. Kwani mtu mzima aliweza kula na mgonjwa wa kifua kikuu lakini haikuwa jambo rahisi kwa Mchagga kula na mtu aliyetuhumiwa kuwa ni mchawi. Tulitishwa hivi kwa miaka mingi na hata watoto walirithi uoga ule na mpaka sasa; kutokana na kuugopa sana uchawi ulipata nguvu na kutawala sana roho zilizouamini.

Wazee walisimulia habari za uchawi kwamba hakuna anayejua uchawi ulivyo isipokuwa mchawi mwenyewe , na haujulikani kwa watu wote kwa kuwa mambo yenyewe ni siri ya wachawi wenyewe. Hata hivyo tulikuwa tukisikia kutoka mataifa mengine kuhusu mambo makubwa sana yanayofanywa na wachawi wa mataifa hayo ambayo huku kwetu hayakuwepo wala kuwezekana kama miujiza mikubwa.

-Kwa hakika uchawi ulitisha sana katika nchi ya Uchagga, na mpaka sasa hofu ile bado iko, lakini tukifikiri na kuangalia jinsi uchawi wa namna mbalimbali unavyofanyika bila shaka tunaona hakuna uchawi wa kweli. Hadithi nyingi huzungumzwa juu ya uchawi lakini ukiuliza ni mti gani aliye mchawi ili uambiwe siri ya uchawi wake hutampata. Wachawi walihukumiwa kwa kupewa dawa inayolevya sana iitwayo “kimanganu” maana yake, kitu kinachomaliza ubishi wa mtu mkaidi. Dawa hii iliwafanya waongee kila kitu kuelezea namna wanafanya uchawi lakini walishindwa kusema na mwisho waliishia kusingizia wamefanya jambo fulani baada ya maumivu makali ili waachiliwe tu lakini sio kweli.

-Mimi nathubutu kusema kuwa Wachagga huzungumza siku hizi habari za uchawi wa namna hizi kwa kusikia tu lakini hawajui; Na hata wale waliokuwa wakiuamini sana kutafuta waganga wawasaidie zamani, walikuja kuudharau na kutoa habari za maisha yao walipokuwa wakiogopa uchawi. Hofu imeendelea kuwapo kwa sababu tulizaliwa katika woga, na mpaka sasa bado kuna Wachagga wanaogopa uchawi licha ya kwamba hawaujui. Tumeweza kuona kwamba Wachagga walishaudharau uchawi zamani baada ya kudadisi na kukutana na uzushi mwingi na kuogopeshana ndio maana huwezi kupata Mchagga mganga wa kienyeji wa zama hizi kwani shida hizo za uchawi ambazo zinawafanya watu kwenda kwa waganga kwa Wachagga zilitoweka zamani hivyo waganga hawakuwa wanahitajika tena, lakini hata hivyo utakuta watoto wanaozaliwa siku hizi na kukutana nawatu wa jamii nyingine ambao bado wako nyuma kwa maswala haya na bado wanahofia mambo ya uchawi wanawaogopesha upya na wanaendelea kuamini na kuogopa uchawi kiasi cha kufikiria kutafuta waganga wa kienyeji.

MCHAGGA WA LEO
-Mwandishi Mangi Petro Itosi Marealle ameona kwamba Mchagga wa leo ameingiliwa na tamaduni nyingi sana za kigeni na zimekuja bila utaratibu kiasi cha kumuathiri sana, tamaduni hizi zimeenezwa sana kwa msaada wa dini za kigeni na serikali lakini zaidi hasa kwa dini za kigeni. Ukweli ni kwamba katika tamaduni na desturi za kichagga yalikuwepo mambo mazuri sana yanayofaa na mambo mengine yasiyofaa. Lakini ni jukumu letu kuendeleza mambo mazuri yanayofaa ambayo ni mengi sana na kuboresha yale yasiyofaa yenye kufaa kuboresha na yasiyofaa kabisa kuachana nayo ndipo kuchanganya na baadhi ya kigeni ambayo tumeona yanafaa na yatatusaidia katika Nyanja mbalimbali.

Mwandishi ameona sisi kama taifa la Uchagga tunapaswa kufanya kazi kwa bidii na kujenga utaratibu wa kujenga mashule mengi pamoja navyuo ambapo tutafundisha mambo mema ya kwetu yatakayoweza kukuza na kuendeleza ustaarabu wetu katika nyanja zote za maisha.

Mwandishi anasema kupitia ujamaa wa Wachagga tayari tumeanza vizuri licha ya changamoto mbalimbali lakini kwa kupitia chama cha ushirika cha Wachagga KNCU(Kilimanjaro Native Cooperative Union), ambacho ndicho chama kikongwe kabisa cha Ushirika barani Afrika kilichoanzishwa mwaka 1933 tumejenga vyuo kama vile Chuo Cha Ushirika Moshi, mashule kama vile Lyamungo Sekondari n.k. , pamoja na miradi mingine kama ya maji, barabara n.k., baada ya kujitoza ushuru mkubwa katika zao la mibuni hivyo tunapaswa kuzidi kufanya kazi zaidi na kujenga mashule zaidi na vyuo vingi ambavyo tutaweza kufundisha watoto wetu wote, wenye kutokea kwenye familia zenye uwezo na wasio na uwezo katika kuelekea kuwa na jamii bora na iliyostaarabika sana.

-Mwandishi ameona tunaweza kusaidiana hata na wageni wa kizungu wale wenye nia njema, wenye utaalamu wa mambo mbalimbali wakatusaidia katika kuimarisha watu wetu na kujenga taasisi imara zenye mifumo bora na endelevu katika kukuza ustaarabu wetu huku tukiimarika tamaduni zetu nyingi nzuri bila kuziacha na kukimbilia moja kwa moja tamaduni za kigeni ambazo nazo zina mapungufu maengi na mbaya zaidi nyingi haziendani moja kwa moja na sisi kwa maana sio asili yetu.

MAONI YANGU
-Nimesoma kitabu hiki pamoja na vitabu vingine vingi pamoja na uzoefu kiasi niliopata katika maisha mpaka hapa nilipofika, sisi binadamu ni watu tuna historia ndefu sana na kila jamii ya watu waliendelea kupiga hatua za kimaendeleo kadiri ya juhudi na akili walizotumia katika mambo yao ya kila siku, naweza kusema kwamba sisi Wachagga na Waafrika wengine kwa ujumla tuna mambo mazuri ya kwetu ambayo sio lazima kuyaacha yote tuna mambo mengi sana bora katika tamaduni na desturi zetu tunaweza kuwa tunayafanya ambayo tutakuja kujivunia na watoto wetu watajivunia hasa kadiri tutakavyoendelea kujitambua. Sisi Waafrika hususan Watanzania tumekuwa ndio watu tunaoongoza kwa kutojitambua duniani kwa sababu ya kushindwa kuthamini na kujivunia vitu vyetu na kukaa kufikiri vya watu ndio vitu bora.

-Leo naomba niwaase Wachagga kuna mambo mawili tunaweza kuyaanza kama mfano wa kwamba tumeanza kujitambua na mengine yakafuata;
(i) Lugha ya kichagga,
(ii) Majina ya kichagga.

Enyi Wachagga hebu tujitahidi kuhakikisha tunaendeleza hii lugha isipotee, fundisha mtoto wako nyumbani na jitahidi kuwa unaiongea naye mara kwa mara huwezi kujua huko mbeleni akawa mtu mwenye kujitambua na mwenye uwezo mkubwa hata akaianzishia taasisi ya kuiendeleza na kuitumia, hivi ni vitu ambavyo vizazi vijavyo ambavyo vitajitambua sana vitatulaumu sana na kutuona mazuzu kwa kuviacha vipotee ambapo muda huo watakuwa wanaongea Kichina na Kiingereza tu halafu vya kwao havijulikani, ni aibu na itakuwa ni ujinga wetu ambao tuko sasa na tunaweza kuchukua hatua.

Jambo la pili ni majina ya kichagga, yewomii, wachagga hebu tuacheni kujichoresha na majina tusiojua hata yanatokea wapi, sisi wachagga tumejaliwa kuwa na majina mengi mazuri sana ya kichagga ambayo ndio alama na fahari yetu. Wewe unaenda nchi za watu huko China, Ulaya, Uarabuni, Amerika, unaonekana kabisa wewe ni mweusi/mwafrika unaulizwa jina unaona ufahari sana kutaja sijui Careen/Mourine/Brian/Johnson, aisee unajichoresha sana, yaani wanakuona boya sana usiyejitambua nawe unajikuta unashangilia sana, sisi wazazi wetu tusiwalaumu sana kutuita majina haya yasiyo ya asili yetu lakini sisi tusirudie makosa kwa watoto wetu jamani tuna majina ya kiafrika mengi mno.

-Hivi umeowahi kuona Mchina anaitwa James au George au Irene au hata Muhindi anaitwa Charles au Diana, wote wana majina ya sijui Park, sijui Lee au Rajesh, Suthir, Sunil, sasa unafikiri wao haya majina ya Charles hawayajui, kwamba wewe tu ndio unayajua?, Hapana wamekataa kujichoresha, basi ningependa kuomba tujikaze tutumie haya majina yetu bora, tena hakikisha unajua maana yake kabisa, acha kuwaza kwamba sio zuri, jina lolote ukilizoea ni zuri ni akili yako tu ndio imeharibiwa, wangapi wanaitwa majina ya kichagga na ni mazuri tu kwao?

Post itakayofuata nitaweka majina mengi sana ya kichagga ya kiume na ya kike halafu utachagua hapo unaloona ni bora zaidi kwa ajili ya mtoto wako tafadhali. Halafu usije kusema hili la kichagga ni la nyumbani halafu hilo la wazungu ndio la kiofisi au shule, hapana hilo la kichagga ndilo linatakiwa lipewe hadhi ya kiofisi, jamani wachagga tuzingatie hili maana ndio mwanzo wa kujitambua sasa kama Wachagga.

-Mwisho nisistize jamani Wachagga tununue hiki kitabu tukisome, ni kitabu kizuri na muhimu zaidi ni kwamba tumeandikiwa sisi Wavulana na Wasichana wa Uchagga, ni kitabu kizuri kusomwa na kijana mwingine yoyote wa kiafrika kwa ajili ya kujua namna ya maisha yetu yalivyokuwa lakini pia kinatuongezea kujiamini sisi kama Wachagga kujielewa zaidi na kujua nguvu yetu ilikuwa wapi. Katika kitabu hiki pia kuna hadithi tatu nzuri sana za kichagga za zamani zilizotungwa kwa weledi wa hali ya juu na ubunifu mzuri sana. Kumbuka kila jamii duniani ina hadithi zake nyingi za kufikirika hivyo na wachagga tulikuwa na waandishi wabunifu karne nyingi zilizopita waliokuwa na uwezo wa kutunga hadithi bora nzuri na za kusisimua.

Kuna hadithi za;
(i) Hadithi ya Mregho(binti mrembo sana) wa kichagga miaka hiyo
(ii) Hadithi ya Morile na Mangi Tembo Lya Mori, nayo nzuri sana
(iii) Hadithi ya kuhusu Mlima Kilimanjaro.

-Pia nisisitize sana kwamba mambo mengi nimechambua hapa kwa juu juu sana kuhusu kitabu hiki hivyo usipokisoma utakuwa kuna kitu kikubwa hujakipata, kuna vitu nimejaribu kuchambua kwa undani kidogo lakini viko vingi sana nimegusa juu juu, ni kitabu cha Kiswahili kinachoeleweka vizuri na kitakusaidia kuwa mwanzo mzuri hata kama nawe unataka kuwaandikia watu wa taifa lililokuwa la Uchagga jambo lolote ambalo unasukumwa kuwaandikia. Mwandishi wa kitabu hiki amesisitiza kwamba anategemea Wachagga mtajitahidi kuandika kazi nyingine zaidi kama hizi kwa faida ya jamii yenu na pia amesema mambo mengi makubwa yanatarajiwa yafanywe na ninyi. Pata nakala yako ya kitabu hiki tuendelee kujitambua zaidi na zaidi.

WASIFU WA MWANDISHI WA KITABU HIKI, MANGI PETRO ITOSI MAREALLE
-Mangi Petro Itosi Marealle alizaliwa tarehe 13 Juni 1906 katika kijiji cha Lyamrakana, Marangu, wilaya ya Moshi Vijijini. Alikuwa mtoto wa mwisho wa kiume wa Mangi Ndegoruo Kilamia Marealle. Mama yake alikuwa ni Elise Makyalenyi Morio, binti wa Mangi Tengia wa Mriti, Rombo.

-Babu yake Mangi Petro Itosi Marealle alikuwa ni Mangi Ndaalio aliyetawala kuanzia Kirua Vunjo mpaka Useri Rombo. Hata hivyo utawala wake ulisambaratika alivyokufa kabla hata mtoto wake mmoja wa kiume hajafikia umri wa kutawala. Ndugu yake Kinabo, alitawala mahali pake na aliwafukuza mke wa Ndaalio, mama Nderero na watoto wake wawili Ndegoruo Kilamia na Mlatie. Mama huyu na watoto wake walikimbilia kwanza kwa Mangi wa Kirua Vunjo, kwa Mangi Rindi wa Old-Moshi na mwisho kwa Mangi Sina wa Kibosho. Wakimbizi hawa walipokelewa vizuri sana na Mangi Sina na baada ya vijana Ndegorio Kilamia na Mlatie kuwa watu wazima, Mangi Sina alikuja kumpiga vita Mangi Kinabo wa Marangu akamshinda na kumtawalisha Mangi Ndegoruo Kilamia.

-Mangi Ndegoruo Kilamia alitawala kwa busara, na alikuwa mkulima hodari wa kahawa. Watawala wa kimasai walipomtembelea walimpa jina la kimasai “Meliari”, lenye maana ya mtu asiyechoka. Hicho ndicho kilikuwa chanzo cha jina Marealle. Alikuwa mtu wa kwanza Mwafrika kujenga ghorofa huko Marangu.

-Mangi Ndegoruo Kilamia alikufa mwaka 1916, akiwa na umri wa miaka 70. Mtoto wake wa kiume wa pili, Joseph Mlang’a alitwalishwa kuwa Mangi wa Marangu.

-Wakati huo huo mdogo wake ambaye ndio mwandishi wa kitabu hiki, Mangi Petro Itosi Marealle, alipelekwa shule ya Mission ya Ngaruma ya hapo kijijini mwaka 1913. Alijifunza kusoma, kuandika na kuhesabu kwa lugha ya Kichagga. Kuanzia mwaka 1915 mpaka 1918 shule ilifungwa kwa sababu ilikuwa wakati wa vita kuu ya Kwanza.

-Baada ya vita, shule ilifunguliwa akaendelea kusoma. Mwaka 1925 alichaguliwa kwenda shule ya kati huko Tanga. Mwaka 1926 shule mpya ya serikali ilifunguliwa Old Moshi na wanafunzi wote waliotoka wilaya ya Moshi, akiwemo Petro Itosi Marealle, walirudishwa Old Moshi. Alimaliza masomo ya miaka 4 na kufanya mtihani wa Taifa mwaka 1929. Alipata shahada.

-Mwaka 1930, aliajiriwa katika shule ya watoto wa machifu, Tabora, kama karani. Kazi hii aliifanya kwa mwaka mmoja ndipo akachaguliwa na wananchi kurithi Umangi wa jadi wa eneo la Marangu, baada ya kaka yake Joseph Mlang’a kujiuzulu. Alikuwa Mangi wa Marangu mpaka mwaka 1946, alipochaguliwa kuiongoza tarafa ya Vunjo kama “Mwitori”, akisaidiwa na Wamangi saba. Alishikilia uongozi huo hadi mwaka 1961.

-Mwaka 1961, Mangi Petro alijiuzulu Umangi na kupokea madaraka mapya katika Chagga Council kama Executive Officer upande wa Ustawi wa Jamii. Tarehe 17 Februari 1962 alichaguliwa na Chagga Council kuwa Makamu wa Rais wa kwanza wa Wachagga wakati utawala wa Umangi wa jadi ulipofutwa.

-Tarehe 18 Oktoba 1962, aliitwa na Serikali kushika madaraka ya Mwenyekiti wa Local Government Service Commission. Aliifanya kazi hadi alipostaafu mwaka 1978.

Mangi Petro Itosi Marealle alifariki dunia mwezi Mei, 1982.

Mkuu hii nzuri sana na ni kweli hiki kitabu kinafaa sana kuhifadhiwa. Naweza kukipata wapi Mkuu? nImejaribu kusoma hapa lakini ningependa kopi ya kitabu,
 
17 Reactions
Reply
Back
Top Bottom