Hatujui matatizo yetu, halafu tunakimbilia kuongeza majimbo!

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,319
33,125
MWAKA 2007, Rais Jakaya Kikwete alikaririwa akisema haelewi ni kwa nini Tanzania bado ni fukara ingawa imejaliwa rasilimali nyingi za asili kuliko nchi nyingi za Bara la Afrika.

Rais Kikwete aliyasema hayo Oktoba 4, wakati wa mahojiano na Mhariri wa masuala ya Afrika wa gazeti la Financial Times, William Wallis na Mwandishi wa gazeti hilo,Tom Burgis. Alisema hata haelewi ni kipi ambacho bado hakijafanywa ili kuifanya Tanzania kuwa katika nchi zenye maendeleo mazuri katika bara la Afrika.

Kwa hakika, nimekumbuka kauli hii ya Rais Kikwete baada ya tume ya uchaguzi kutangaza kutaka kuongeza idadi ya majimbo ya uchaguzi na jinsi jambo hili lilivyopata ushabiki wa kisiasa. Ama kweli nakubali kwamba, Watanzania hawajui sababu za nchi yao kuwa maskini.

Tatizo hili la kushindwa kuelewa sababu za nchi yetu kuwa nyuma kimaendeleo mpaka sasa, linaashiria kuwa tumeshindwa kulipatia ufumbuzi.

Zipo baadhi ya nchi za Afrika kama vile, Rwanda, Malawi na Botswana ambazo hivi sasa zimetambua matatizo yao, uchumi wake sasa unapaa, lakini zikiwa hazina rasmali nyingi kama za kwetu. Hawa wajitambue na sasa wameamua kusonga mbele!

Tatizo kubwa ambalo linatusumbua Watanzania ni uvuvi wa kufikiri, matumizi mabaya ya fedha za umma na kukosa uzalendo ambao umesababisha viongozi wetu kufikiria zaidi maslahi yao badala ya taifa.

Hata suala hili karibu kila halmashauri nchini kutaka kuongeza majimbo ya uchaguzi kwa kigezo kwamba, ni ukubwa wa majimbo ya sasa ambayo yanawafanya wabunge washindwe kutekeleza wajibu wao, ni la kuongeza ulaji zaidi kwa wanasiasa wetu.

Tangu Tume ya uchaguzi nchini itangaze kufungua milango ya kupokea mapendekezo ya kuongezwa kwa majimbo ya uchaguzi halmashauri, sasa suala hilo limekamatwa na wanasiasa ambao hawaangalii vigezo vya kuongeza majimbo, wanachoangalia wao ni maslahi yao ama ya kuongezwa jimbo ili kupunguza ushindani katika uchaguzi ili CCM ishinde au mwanasiasa mmoja kupewa zawadi.

Sababu zinazotolewa kwamba, eti kutokana na ukubwa wa baadhi ya majimbo ya sasa yaliyopo, wabunge wake wanashindwa kuwafikia kirahisi wananchi wao na hivyo kushindwa kupata matatizo yao na kuyapeleka bungeni.

Mimi najiuliza iwapo suala hili litatekelezwa kabla ya uchaguzi huu ina maana kwamba, idadi ya wabunge tulionao 300 itaongezeka pengine kufikia 350 au 400 ambao watawakilisha Watanzania milioni 40.

Lakini wakati tukiendelea kushabikia kuongezwa kwa majimbo haya ya uchaguzi, India ambayo ina idadi ya watu zaidi ya bilioni moja sasa ina wabunge 530 tu, huku wabunge wake hawalalamiki kuwa wanashindwa kuwafikia wananchi wao.

Japan yenye jumla ya watu milioni 127, ina idadi ya wabunge 480 nayo ina bunge lenye nguvu kubwa ambalo linafanya kazi zake bila matatizo.

Labda watanzania tujiulize hivi ufanisi gani utaongezeka bungeni au katika majimbo yetu,kwa kuongeza idadi ya wabunge, kama hawa tulionao wengi wamegeuka kuwa wasindikizaji na wengine tunashuhudia wakilala?

Jambo lingine la kujiuliza hivi pamoja na umaskini tulionao kuna haja gani ya kuongeza wabunge ambao wanatumia mabilioni ya shilingi za walipa kodi kwa ajili ya kuwalipa mishahara, posho na viinua mgongo vya sh milioni 50, tunataka kuongeza tena gharama hizi?

Mimi siamini kwamba ufanisi wa wabunge utapanda baada ya kuongezeka kwa majimbo, hata kidogo, bali ufanisi wa wabunge utapanda kwa wao kujua wajibu wao na kuwajibika kwa wananchi.

Nadhani, tatizo letu bado ni lile lile la kushindwa kutambua sababu za kuwa maskini. Tunajua wazi kwamba, kuongeza majimbo ni kuongeza gharama wakati idadi ya wabunge tulionao sasa ni kubwa mno, ukilinganisha na idadi ya watu na hata ukubwa wa maeneo.

Kama India ambayo ina idadi kubwa mno ya watu wanaofikia sasa bilioni moja na zaidi na eneo kubwa la nchi lina wawakilishi bungeni 530 kwa nini sisi Watanzania milioni 40 tuendelee kuongeza majimbo?

Unadhani Wahindi na Wajapan kuamua kuwa na idadi ndogo ya wabunge ni wajinga, au tunadhani wao ni maskini zaidi kuliko sisi? Wanaelewa kwamba, kuwa na idadi kubwa ya wabunge sio kuwajibika.

Unaweza kuzifanya kila kata kuwa jimbo, lakini kama mfumo wa serikali hauwezi kuwa na mipango madhubuti ya maendeleo ya wananchi, kudhibiti na kuzuia mianya ya rushwa; utitiri huo wa wabunge hauwezi kusaidia chochote.
 
Back
Top Bottom