HALI ya Uchumi wa Nchi; Serikali ya CCM yaonywa kwa kufunga milango ya kufikiri

Tumaini Makene

JF-Expert Member
Jan 6, 2012
2,642
6,071
HOTUBA YA MSEMAJI MKUU WA KAMBI YA UPINZANI- OFISI YA RAIS MIPANGO MHE. CHRISTINA LISSU MUGHWAI (MB), KUHUSU TAARIFA YA HALI YA UCHUMI KWA MWAKA 2011 NA MPANGO WA MAENDELEO WA TAIFA KWA MWAKA 2012– 2013

Utangulizi
Mheshimiwa Spika, Kwa mujibu wa Kanuni ya 96(6) ya Kanuni za Kudumu za Bunge, 2007, naomba kuwasilisha maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kuhusu taarifa ya hali ya uchumi kwa mwaka 2011/2012 na mpango wa maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2012/13 kama ulivyowasilishwa na Mhe. Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Mahusiano na Uratibu.

Mheshimiwa Spika,

Kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema na kutuwezesha kuwa hapa siku hii ya leo. Kwa masikitiko makubwa napenda kutoa salaam za rambi rambi kwa familia, ndugu, jamaa, wapenzi na viongozi wote wa CHADEMA kwa msiba mkubwa wa kuondokewa na mmoja wa waasisi wa chama chetu Mzee Mohamed Ally Nyanga "Bob" Makani. Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi, na aipe familia yake moyo wa Subira na Ustahimilivu katika kipindi hiki kigumu.

Mheshimiwa Spika, Pongezi za pekee ziwaendee viongozi wote, wanachama na wafuasi wote wa CHADEMA kwa kazi kubwa na yenye mafanikio makubwa wanayoendelea kuifanya katika kukiimarisha na kukijenga chama nchi nzima.

Mheshimiwa Spika,Ili Mpango wowote ufanikiwe katika malengo yaliyokusudiwa, ni lazima kuwe na dhamira ya dhati ya kuutekeleza. Kambi ya Upinzani imebaini kwamba Serikali haina dhamira ya dhati ya kuutekeleza Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka mitano kwa kushindwa kutenga fedha za kutosha kugharamia miradi ya maendeleo kama ilivyoainishwa katika Mpango. (Rejea Mpango wa Maendeleo 2012/13: na Bajeti ya Serikali kama ilivyowasilishwa).

MAPITIO YA MWENENDO WA UCHUMI WA TAIFA 1. Ukuaji wa Pato la Taifa Mheshimiwa Spika, Takwimu za Serikali zinaonyesha kuwa mwaka 2011 Pato halisi la Taifa lilishuka kwa kiwango cha asilimia 0.6 ikilinganishwa na mwaka 2010. Kwa maana kwamba 2011 ukuaji wa Pato la Taifa ulikuwa asilimia 6.4 na mwaka 2010 ulikuwa ni asilimia 7.0. Sekta ndogo ya mawasiliano ndiyo iliyoongoza kwa ukuaji wa asilimia 19.0, sekta ya uzalishaji viwandani asilimia 7.8, sekta ya kilimo ilipungua kutoka asilimia 4.2 mwaka 2010 hadi asilimia 3.9 mwaka 2011.

Mheshimiwa Spika, Sura ya kwanza ya kitabu cha Hali ya Uchumi wa Taifa Katika mwaka 2011 inakiri kwamba kulikuwa na ukuaji mdogo wa pato la taifa. Hata hivyo, Serikali inamlaumu Mwenyezi Mungu kwa kusababisha ukuaji huo usioridhisha wa pato la taifa: "Kiwango kidogo cha ukuaji kilitokana na hali mbaya ya ukame iliyojitokeza katika sehemu mbalimbali nchini ambapo imeathiri sekta ya kilimo." Hata hivyo, Mheshimiwa Spika, katika hali inayohitaji maelezo zaidi kutoka Serikalini, Serikali inadai - katika aya ya 234 ya kitabu hicho hicho – kwamba:

"Mwaka 2011,uzalishaji wa mazao ya chakula hususani ngano, mihogo, maharage, ndizi na viazi uliongezeka ikilinganishwa na mwaka 2010 kutokana na hali nzuri ya hewa na mtawanyiko mzuri wa mvua kwa ustawi wa mazao."
Mkanganyiko huu ni dalili ya ukosefu wa umakini katika kuandaa taarifa muhimu za Serikali na unaitia Serikali hii aibu!

Mheshimiwa Spika
, Kama ilivyokuwa kwa mwaka 2010, serikali imeendelea kukiri kuwa ukuaji huu wa pato la taifa haukupunguza umaskini kama ilivyotarajiwa kwasababu sekta zilizokuwa haraka hazitoi ajira kwa wananchi wengi hasa waliopo vijijini ambao wanategemea kilimo. Ni lini sasa serikali itaweka bayana mikakati inayotekelezeka itakayowafanya wananchi waliowengi wanufaike na ukuaji huo wa uchumi? Waziri Kivuli wa Fedha atakaposoma bajeti mbadala ataweka bayana mikakati itakayoelekeza ukuaji wa uchumi kwa wananchi walio wengi na hasa wa kipato cha chini na waishio vijijini.

2.
Mfumuko wa Bei

Mheshimiwa Spika, Kuongezeka kwa kasi kwa bei za bidhaa na huduma kuliathiri sana Bajeti ya Serikali ya mwaka unaokwisha. Wakati Mfumuko wa Bei mwezi Julai mwaka wa Fedha 2011/2012 ulikuwa asilimia 13, ulifikia asilimia 19.2 mwezi Novemba mwaka huo wa Fedha. Hii maana yake ni kwamba, Bajeti ya Serikali iliyopitishwa na Bunge mwezi Juni 2011, ilipunguza uwezo wake wa kununua bidhaa na huduma kwa takribani asilimia 6. Hii ni sawa na shilingi 780 bilioni kuyeyuka katika Bajeti katika kipindi cha miezi Minne tu ya utekelezaji wa wake. Aidha kufikia mwezi Desemba 2011, mfumuko wa bei ulifikia asilimia 19.8 na mfumuko wa bei za chakula ulipanda hadi asilimia 25.6 kutoka asilimia 6.3 Desemba 2010. Kutokana na kasi hiyo ya ukuaji wa Mfumuko wa Bei ni dhahiri kwamba, sehemu kubwa ya Bajeti na hasa Bajeti ya Maendeleo ilishindwa kutekelezeka.

Mheshimiwa Spika,

Hali ni mbaya zaidi kwa wananchi kwani Mfumuko wa Bei za vyakula umekua kwa kasi kubwa mno. Ofisi ya Takwimu imeonyesha kuwa wakati mfumuko wa Bei za vyakula ulikuwa asilimia 14.8 mwezi Julai, umefikia asilimia 24.7 mwezi Novemba 2011. Ukilinganisha na bei za vyakula mwaka 2010, mwananchi amepoteza uwezo wa kununua chakula kwa zaidi ya robo kati ya Novemba 2010 na Novemba 2011. Jumla ya vyakula ambavyo mwananchi alinunua kwa shilingi 10,000 mwaka 2010, sasa atanunua kiwango kile kile kwa shilingi 12,500. Bei za vyakula zimeongezeka kwa kiwango hiki wakati kipato cha mwananchi kipo palepale. Mwathirika mkubwa wa mfumuko wa bei ni mwananchi wa kawaida mwenye kipato cha chini.

Mheshimiwa Spika,

Ukiangalia kwa undani utakuta mfumuko wa bei wa bidhaa kama mchele, sukari, nyama na samaki umekua maradufu. Bei ya mchele imekua kwa asilimia 50, sukari asilimia 50, nyama asilimia 30 na Samaki kwa takribani asilimia 40. Bidhaa hizi zote ni muhimu sana kwa mahitaji ya chakula kwa wananchi walio wengi.

Mheshimiwa Spika,

Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaona kuwa Serikali hadi muda huu imeshindwa kutoa suluhisho la mfumuko wa bei ambao kwa kiasi kikubwa unachangiwa na bei za vyakula. Serikali imeendelea kutoa sababu za bei kupanda bila kutoa majawabu. Wananchi wamechoka kusikia sababu za mfumuko wa bei, wanataka kuona hatua mwafaka zinachukuliwa kudhibiti mfumuko huu wa bei na hivyo kupunguza ukali wa maisha kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika,

Katika hotuba mbadala ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kwa mwaka wa fedha 2008/2009 kwa mujibu wa Hansard za Bunge tulipendekeza yafuatayo:

"Mheshimiwa Spika, bei za mafuta ya dizeli kwa makao makuu ya mikoa kwa tarehe 16-31 mei 2008 ilikuwa kama ifuatavyo kwenye baadhi yamikoa, Dar es salaam 1,654.09 petrol na 1,884.89 kwa dizeli kwa lita huku mafuta ya taa yakiwa 1,488.24 kwa lita, Kagera 1,748.93 petrol na 1,979.73 kwa dizeli kwa lita huku mafuta ya taa yakiwa 1,583.08 kwa lita, Kigoma 1,930 petrol na 2,080 dizeli kwa lita huku mafuta ya taa 1,550 kwa lita na hali katika mkoa wa Mbeya 1,850 petrol na 2,000 dizeli kwa lita huku mafuta ya taa 1,500 kwa lita na Zanzibar diseli ni wastani wa shs.1850 . Kati ya wastani wa bei ya 1800/- kwa lita. Hizi ni bei za mijini, vijijini ambako kuna umasikini uliokithiri na mahitaji ya nishati kwa ajili ya usafiri,kilimo n.k. wastani wa bei ni Tshs.2,200/- kwa lita.

Hivyo hivyo kwa bei za bidhaa nyingine kama cement,mabati n.k. Je, umasikini utapungua wakati sehemu kubwa ya jamii inaishi vijijini. Mhe.Spika,Nchi kama India bei za vijijini na mijini ni tofauti na ndio maana wamemudu kuzalisha chakula cha kutosha".

Mheshimiwa Spika,

Asilimia kubwa ya watanzania wanaishi maeneo ya vijijini na vipato vyao ni vidogo. Haiingii akilini kuwa bei za bidhaa na huduma za vijijini ni kubwa kuliko za mijini kama kweli kuna nia ya kuwakwamua wananchi walio wengi wa vijijini.

Mheshimiwa Spika,

Kambi ya Upinzani tunazidi kusisitiza ushauri tulioutoa kipindi hicho kuwa ufanyiwe kazi, kwani asilimia kubwa ya watanzania wanaishi maeneo ya vijijini na vipato vyao ni vidogo. Ni lazima sasa Serikali ipange bei maalum za nishati kwa maeneo ya vijijini ili kuongeza uzalishaji na kuwapunguzia gharama za maisha. Tuige mfumo huu kutoka nchi ya India ambao ulifanikiwa kwa kiasi kikubwa.

3. Thamani ya Shilingi ya Tanzania

Mheshimiwa Spika,

Thamani ya shilingi ya Tanzania imeendelea kushuka ukilinganisha na fedha za kigeni, na hii inatokana na kukosekana kwa mikakati thabiti ya kuhakikisha kuwa shilingi inaimarika kwenye soko na hasa kutokana na sera mbovu za kiuchumi na usimamizi usio makini. Kushuka kwa thamani ya Shilingi licha ya kupanda kwa mauzo yetu nje kwa sekta zote mbili tunazotegemea sana (Madini na Utalii) kunaacha maswali mengi kuhusiana na chaguo letu kuhusu Hifadhi ya Fedha za kigeni.

Mheshimiwa Spika,

Kambi ya Upinzani inaunga mkono ushauri uliotolewa na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma kwamba sasa Benki Kuu ya Tanzania ianze kutunza sehemu ya Hifadhi ya nchi katika Dhahabu. Benki Kuu inunue dhahabu kutoka kwa wachimbaji wadogo na pia tuangalie uwezekano wa kutoza sehemu ya mrahaba katika sekta ya madini kama ‘dhahabu safi' (‘pure gold').


4. Misaada na mikopo ya Kibajeti

Mheshimiwa Spika,

Serikali katika hotuba yake inasema kuwa kwa kipindi cha Julai 2011 hadi Machi 2012 ilipokea misaada na mikopo toka nje ya asilimia 85 ya makadirio ya Tshs.bilioni 869.4 kwa kipindi hicho.

Mheshimiwa Spika,

Kambi ya Upinzani inaelewa kabisa umuhimu wa fedha hizo toka nje, lakini ni kweli fedha hizo zinatumika kuleta maendeleo kwa wananchi? Fedha hizo zilikopwa kwa miradi gani hasa ya maendeleo?


Mheshimiwa Spika,

Mambo hayo yote ambayo Kambi ya Upinzani itayapa msukumo katika Hotuba ya bajeti yake mbadala ni mambo ambayo kwa kiasi kikubwa utatuzi wake ni lazima uhusishe mtazamo mpana wa kiuchumi.

5. Deni la Taifa

Mheshimiwa Spika,

deni la taifa linaonekana kuongezeka kwa kasi ya ajabu sana na hivyo kupelekea Taifa kuwa na mzigo mkubwa sana wa madeni. Kwa mujibu wa Hotuba ya Bajeti ya Mipango iliyowaslishwa Bungeni Tarehe 14.06.2012, Uk. 12, aya ya 25 inaonyesha kuwa deni la Taifa limeongezeka kwa asilimia 15.4 kati ya March 2011 hadi March 2012 kutoka Tsh trilioni 17.6 hadi Tshs Trilioni 20.3. Cha kushangaza ni kwamba serikali inatuambia kuwa deni hilo linahimilika ilihali wananchi ambao ndio walipaji wa deni hilo wako hohehahe kimaisha. Aidha, hoja kwamba deni hili linahimilika inatia shaka kwa vile deni letu la nje halijawahi kupungua katika kipindi cha miaka kumi iliyota.

Mheshimiwa Spika,

Katika hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kwa mwaka wa fedha 2011/2012 tulipendekeza ufanyike uchunguzi Maalumu kwenye Deni la Taifa ili Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali atuambie madeni haya tunayokopa kwa kasi ya namna hii tunayapeleka kweye miradi gani (Matumizi ya Madeni) na namna gani tunaweza kudhibiti Deni la Taifa. Mwaka huu pia tunarejea ushauri huo huo kwani mwenendo wa kukopa unatakiwa ujulikane na uwekewe uangalizi maalumu.


MAENDELEO KATIKA SEKTA ZA KIUCHUMI NA KIJAMII

Mheshimiwa Spika,

Sekta za kiuchumi na kijamii ndiyo kioo cha kutolea tathmini ni jinsi gani utendaji wa Serikali kwa kipindi kilichopita ulivyofanikiwa au ulivyoshindwa. Maoni ya Kambi ya Upinzani katika hili ni kwamba Serikali imeshindwa vibaya kuwaonyesha wananchi kuwa ipo na inafanya kazi.

Mheshimiwa Spika,

Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inahoji Serikali kushindwa kutoa fedha kwa wizara za Kisekta kama ambavyo zilikuwa zimetengwa na Bunge hili ili kufanya kazi. Lakini kwa masikitiko makubwa fedha hizo zilishindwa kupelekwa zote na hivyo kusababisha miradi na huduma za jamii kutokutekelezwa. Hili limejidhihirsha kwa Kamati sita za Bunge za Kudumu kukataa kupitisha bajeti za kisekta kwa kutaka maelezo ya utekelezaji wa bajeti iliyopita. Madai ya Kamati yalikuwa ni kwanini miradi haikutelezwa na pia ni kwanini fedha zinazoombwa ni kidogo kuweza kutekeleza miradi na huduma katika sekta hizo; kabla ya kupitisha bajeti hii mpya.

Mheshimiwa Spika
, Katika bajeti ya mwaka 2011/2012 sekta ya miundombinu ilitengewa jumla ya asilimia 20.6 ya jumla ya bajeti ya Tshs trilioni 13.5, na watanzania wote watakuwa ni mashahidi, je Reli ya kati imekarabatiwa pamoja na Injini zake na mabehewa kama tulivyoambiwa katika mwaka wa fedha unaoisha? Huku ni kulidanganya bunge pamoja na wananchi.

Mheshimiwa Spika
, Kwa maelezo zaidi kuonyesha jinsi gani Serikali imeshindwa kutekeleza bajeti iliyopita yatatolewa na wasemaji wakuu katika sekta mbali mbali za Uchumi na Kijamii. 1. Uwezeshaji wananchi Kiuchumi

Mheshimiwa Spika,
Kwa mwaka 2011 Serikali inasema iliendelea utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi kupitia mifuko ya Uwezeshaji na ilitoa mikopo yenye thamani ya Tshs. Bilioni 7.1 Kambi ya Upinzani inauliza uwezeshwaji huu unafanywa kwa kutumia kigezo gani? Kutokana na utafiti uliofanywa na Taasisi ya Utafiti wa Kuondoa Umasikini (REPOA), kuhusu upeo wa elimu kwa wananchi wanaoishi vijijini ambao wanajihusisha na ujasiria mali. Asilimia 16.2 hawana elimu ya shuleni bali elimu isiyo rasmi, asilimia 69.5 wana elimu ya msingi na asilimia 14.3 wana elimu ya Sekondari au elimu ya juu.

Mheshimiwa Spika,

Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inauliza kwa viwango hivyo vya elimu, je uwezeshaji wa kutoa fedha bila ya kutoa mafunzo ya biashara unaweza kuleta tija? Hii ni kutokana na ukweli kwamba idadi kubwa ya watanzania wanaishi vijijini, hivyo uwezeshaji kiuchumi wa namna yoyote ile ni lazima uangalie hali halisi kwa wananchi waishio vijijini. Bila mkakati wa kutoa elimu Kambi ya Upinzani inahesabu kuwa haya ni matumizi ambayo hayakufanyiwa tafiti na hivyo ni upotevu wa fedha za walipa kodi.

2. Miradi ya Kitaifa ya Kimkakati

Mheshimiwa Spika
,

Kabla ya kuangalia miradi ya kitaifa ya kimkakati, naomba kunukuu ukurasa wa 92 kifungu cha 4.3.1 katika mpango wa maendeleo wa miaka mitano toleo la kiswahili kama kama ambavyo ulipitishwa na kuwekewa Azimio na Bunge lako tukufu kama ifuatavyo: "kwa kuelewa kuwa wakati wote kutakuwa na miradi ya uwekezaji nje ya mpango, serikali, kuanzia sasa, itakuwa inatenga asilimia 35 ya makadirio ya mapato yake ya ndani kwa ajili ya kugharamia bajeti ya maendeleo kila mwaka."

Mheshimiwa Spika,

Kwa maana rahisi kulingana na nukuu hiyo ni dhahiri kuwa Serikali haina fedha, kwani makusanyo yote ya mapato ya ndani ni Tshs. Trilioni 9.08 wakati Matumizi ya Kawaida ni Tshs. Trilioni 10.6.

Mheshimiwa Spika,

Serikali imeainisha miradi ya Kitaifa ya Kimkakati ambayo italeta maendeleo ya haraka hususani katika kuchochea maendeleo ya maeneo mengine na hivyo kuongeza ajira, kukabiliana na matatizo ya kiuchumi yaliyopo sasa na pia kuongeza pato la Taifa. Uk. wa 25 aya ya 57 katika Hotuba ya Serikali ya taarifa ya Uchumi na Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2012/2013 inaeleza miradi husika. Aidha ukiangalia Hotuba ya Waziri wa Fedha kuhusu makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2012/2013 Uk.46 aya 78 (a) (i) inasema benki ya Exim China itatoa mkopo wa Dola za Marekani 1,225.3 utakaosimamiwa na TPDC. Cha kushangaza ni kuwa kwenye kitabu cha Miradi ya Maendeleo fedha hizo hazionekani, japokuwa TPDC ni taasisi ya Serikali.

Mheshimiwa Spika,

Huu ni udhaifu mkubwa katika mfumo wetu wa bajeti, kwani unawafanya wabunge wasijiridhishe ni nini wanapitisha. Hivyo basi, Kambi ya Upinzani inapendekeza kwamba Taasisi zote za umma yakiwemo mashirika taarifa zao za mapato na matumizi kwa mwaka wa bajeti ziwekwe kama viambatanisho kwenye Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka husika.

Mheshimiwa Spika,
Aya ya 78(a) (ii) katika kifungu kinachohusu Usafirishaji na Uchukuzi, Serikali imetenga kiasi cha Tshs. Trilioni 1.382.9 lakini kati ya fedha hizo Fedha zinazohusiana na Reli ya Kati ni Tshs. Bilioni 134.16 tu, na Wizara ya Uchukuzi imetengewa Fedha za Maendeleo Tshs.Tshs. Bilioni 252.8. Fedha zote zinazobaki ni kwa ajili ya Wizara ya Ujenzi.

Mheshimiwa Spika,

Mgawo wa fedha kwa ajili ya kuwekeza katika Reli ya Kati ambayo ni mojawapo ya Injini za uchumi zilikuwa hazitoshi na ndiyo sababu kuu kwa Waheshimiwa wajumbe kushindwa kuipitisha bajeti ya Wizara hiyo.

Mheshimiwa Spika,

Kumekuwa na hadaa kubwa sana kwa watanzania inayofanywa makusudi kwa wale waliopewa dhamana ya kuhakikisha kuwa wananchi wanapata huduma stahiki kulingana na kodi wanazolipa. Kitendo kilichofanywa na Waziri wa Uchukuzi, kuwaeleza wananchi akiwa katika Mkutano Jangwani kuwa Reli imepewa fedha za kutosha kununua Injini za kisasa na kutandaza mataruma ya kisasa na kupanda treni kutoka Dar kuja Dodoma ni hadaa kubwa inayotuumiza sisi wote kama nchi.

Mheshimiwa Spika,

Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kwa miaka yote ya nyuma tumekuwa tukisisitiza umuhimu wa Reli ya Kati na tumetenga fedha za kutosha kwa Reli ya Kati katika bajeti mbadala kama itakavyosomwa na Msemaji Mkuu wa Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Spika,

Katika miradi ya Kilimo kama ilivyoainishwa katika aya ya 60 ya Bajeti ya Hali ya Uchumi na Mpango, kwa kuoanisha na lengo la uwekezaji huo wa kuongeza ajira. Kambi ya Upinzani inaona kuwa uwekezaji huu utasaidia kujenga matabaka badala ya kuhamasisha vijana kuingia katika kilimo watakuwa ni manamba katika mashamba hayo na mwisho umasikini utazidi.

Mheshimiwa Spika,
Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inasisitiza kuwa uwekezaji ufanywe kwa Serikali kuwawezesha wananchi kumiliki mashamba madogo madogo kwenye maeneo ya mabonde husika kwa kutengeneza miundombinu na kuikodisha kwa wamiliki wa mashamba hayo. Nchi nyingi zinazozalisha mpunga kwa wingi kama Vietnam hawatumii mashamba makubwa bali ni mashamba madogo ili watu wengi wajihusishe na kilimo badala ya mtu mmoja tu na wengine kuwa vibarua.


MPANGO WA MAENDELEO WA TAIFA 2011/12 – 2015/16


MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO KWA MWAKA 2011/12 NA 2012/13

Mheshimiwa Spika,

Katika mjadala kuhusu Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano uliowasilishwa Bungeni mwezi Juni mwaka jana, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ilihoji, pamoja na mambo mengine, uwezo wa utekelezaji wa Mpango huo kama ulivyopitishwa na Bunge hili tukufu.

Kwa mfano, wakati Mpango unadai kwamba gharama zinazotarajiwa kwa utekelezaji wake ni takriban shilingi trilioni 8.6 kwa mwaka au shilingi trilioni 42.98 kwa kipindi cha miaka mitano ya utekelezaji wa Mpango, katika mwaka wa kwanza wa utekelezaji wake, Serikali ilitenga shilingi trilioni 4.9 tu. Katika kujaribu kuhalalisha mgawo huo pungufu, Serikali ilijitetea kwamba mwaka 2011/2012 ulikuwa ni mwaka wa mpito wa utekelezaji wa Mpango.


Mheshimiwa Spika,

Fedha zilizotengwa kwa ajili ya utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano kwa mwaka huu wa fedha zinathibitisha kwamba kauli ya Serikali kwamba mwaka 2011/2012 ulikuwa mwaka wa mpito kwa utekelezaji wa Mpango ilikuwa na lengo la kuwahadaa Watanzania.

Hii ni kwa sababu, shilingi trilioni 4.5 zilizotengwa kwa ajili ya utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo kwa mwaka 2012/2013 sio tu ni pungufu ya gharama tarajiwa ya shilingi trilioni 8.6 za kutekeleza Mpango kwa mwaka, bali pia ni pungufu ya fedha zilizotengwa kwa ajili hiyo kwa mwaka ulioitwa wa mpito! Ni wazi kwa hiyo – kama Serikali yenyewe ilivyosema kuwa "Mpango huu (ni) kipimo cha ufanisi wa Serikali na uchumi kwa ujumla" – kwamba Serikali hii ya CCM haijawa na ufanisi wowote katika utekelezaji wake wa Mpango na katika uendeshaji wake wa uchumi kwa ujumla!


Mheshimiwa Spika,

Serikali imeshindwa sio tu katika utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo kwa ujumla, bali pia imeshindwa kutekeleza ahadi yake yenyewe kwa Bunge hili tukufu. Kwa mujibu wa Mpango, "… Serikali, kuanzia sasa, itakuwa inatenga angalau asilimia 35 ya makadirio ya mapato yake ya ndani kwa ajili ya kugharamia bajeti ya maendeleo kila mwaka."

Kauli hii ya Serikali ilitiliwa nguvu na Azimio la Bunge hili tukufu la tarehe 8 Juni 2011. Hata hivyo, Serikali ilianza mwaka wa kwanza wa utekelezaji wa Mpango kwa kushindwa kutekeleza ahadi kwani ilitenga shilingi trilioni 1.87 au asilimia 26.2 ya mapato yote ya ndani yaliyokadiriwa kuwa shilingi trilioni 7.13.


Mheshimiwa Spika,

Hadithi ya mwaka huu ni mbaya zaidi kuliko ya mwaka jana. Hii ni kwa sababu, kati ya takriban shilingi trilioni 9 ambazo ni makadirio ya mapato ya ndani kwa mwaka huu wa fedha 2012/2013, Serikali imetenga shilingi trilioni 2.2 au asilimia 24.4 ya mapato ya ndani kwa ajili ya utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo.

Hii ina maana kwamba badala ya Serikali kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa Mpango ikilinganishwa na ulioitwa ‘mwaka wa mpito', Serikali hii ya CCM imepunguza ufanisi ikilinganishwa na makadirio ya mwaka huo wa mpito licha ya kwamba makadirio hayo yalikuwa pungufu ya lengo la Mpango na kinyume cha Azimio la Bunge.

Kwa ushahidi huu, ni wazi kwamba Serikali hii hii, ya chama hiki hiki, haina uwezo au nia ya kutekeleza Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano licha ya kuwa na nyuso tofauti katika safu za Serikali hiyo hapa Bungeni!


Mheshimiwa Spika
,

Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inatoa rai kwamba Bunge hili tukufu lisimamie Azimio lake la tarehe 8 Juni mwaka jana kwa kukataa kuipitisha bajeti hii na kuitaka Serikali iongeze kiasi cha fedha za ndani zilizotengwa kwa bajeti ya maendeleo kufikia shilingi trilioni 3.15 ambayo ni asilimia 35 ya mapato yote ya ndani kwa mwaka huu wa fedha 2012/2013. Kama bajeti yetu mbadala itakavyoonyesha, inawezekana sio tu kufikisha kiwango hiki bali pia kukizidisha endapo Serikali itakuwa makini katika ubunifu wa vyanzo vipya vya mapato ya ndani.

Mheshimiwa Spika,

Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaamini kwamba kama serikali iliyopo madarakani inashindwa kusimamia Mpango wa Maendeleo ambao umezinduliwa kwa mbwembwe nyingi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kupitishwa na Bunge hili tukufu, ni wazi kuwa Serikali hiyo haipaswi kuendelea kuaminiwa na wananchi kwamba ina uwezo au nia ya kusimamia maendeleo yetu na uchumi wa taifa letu. Serikali hii inapaswa kupumzishwa kwa manufaa ya nchi yetu ya sasa na ya vizazi vijavyo.


Mheshimiwa Spika,

Bajeti mbadala ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ya mwaka jana ilipendekeza kupunguza misamaha ya Kodi kufikia asilimia moja ya Pato la Taifa; kupunguza kodi na tozo kwenye Mafuta ya Petroli na Dizeli ili kupunguza mfumuko wa bei; kupunguza matumizi ya Serikali kwa kuondoa posho za vikao kwa watumishi na viongozi wote wa umma; na kuelekeza fedha zaidi kwenye Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu.

Kati ya mapendekezo hayo, Serikali ilitekeleza pendekezo la kuongeza fedha kwa Bodi ya Mikopo. Serikali ilipuuza au kushindwa kutekeleza mapendekezo mengine yaliyotolewa na Kambi Rasmi ya Upinzani ndio maana matatizo yanayowakabili wananchi yameendelea kuongezeka na hali yetu ya kiuchumi kwa ujumla imezidi kuwa mbaya kuliko kipindi kilichopita.


Mheshimiwa Spika,

Kwa mwaka huu wa fedha, Kambi Rasmi ya Upinzani Upinzani, sambamba na kurejea mapendekezo yake ya mwaka jana, inapendekeza mambo yafuatayo:

1. Kuanzia sasa, misamaha yote ya kodi lazima iidhinishwe na Bunge hili tukufu kupitia Kamati yake ya Fedha na Uchumi ili kuhakikisha kwamba haizidi asilimia moja ya Pato la Taifa;

2.
Kuongeza bajeti ya maendeleo hadi kufikia asilimia 35 ya mapato ya ndani na kuelekeza nyongeza hiyo kwenye maendeleo vijijini hasa kujenga miundombinu kama vile barabara, nishati, maji safi, afya na elimu;

3.
Kuelekeza fedha za kutosha kukarabati Reli ya Kati na kufufua njia za Reli za Tanga, Moshi na Arusha kwani usafiri wa reli ni nguzo muhimu kuinua uchumi wan nchi;

4.
Kuongeza wigo wa kutoza tozo ya ujuzi (Skills Development Levy) ili waajiri wote ikiwemo Serikali na mashirika ya umma walipe tozo hiyo tofauti na sasa ambapo sekta binafsi tu ndiyo inayochangia. Aidha, tunapendekeza tozo hii ipunguzwe kutoka asilimia 6 ya sasa mpaka kufikia asilimia 4 ambapo theluthi moja itaenda VETA na vyuo vya ufundi na baki itaenda kwenye Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu ili kukabili changamoto ya mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu;

5.
Kuongeza mapato ya ndani na kupunguza mikopo ya kibiashara kwa kuhakikisha mapato ya ndani yanafikia 20% ya pato la taifa kwa kufanya marekebisho ya kisheria na udhibiti ili kuiwezesha TRA kukusanya mapato zaidi kutoka kwenye kampuni za simu na kwenye shughuli za uchimbaji wa madini, mafuta na gesi asilia.

6.
Kuliandaa Taifa kuwa na uchumi wa gesi asilia kwa kuanzisha ama kuharakisha mchakato wa utungaji wa Muswada wa Sheria ya Gesi;

7.
Kupunguza au kufuta kodi kwenye bidhaa za vyakula vinavyotumiwa na wananchi walio wengi kwa muda maalum ili kushusha mfumuko wa bei;

Mheshimiwa Spika,

Mapendekezo haya ni mawazo ya Wabunge walio wachache katika Bunge hili tukufu. Katika utaratibu wa ‘wengi wape' unaotumiwa na Bunge letu na katika mazingira ya ushindani wa kisiasa katika nchi yetu, ni rahisi kudharau au kupuuza ushauri wa walio wachache kwa kutumia nguvu ya uwingi ya chama tawala. Endapo hilo litafanyika kuhusiana na mapendekezo haya, taifa letu litakuwa limekoseshwa fursa ya kuvuna utajiri na uzoefu wa kitaaluma wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni na matokeo yake hayatakuwa mema kwa ustawi wan chi yetu. Kama alivyosema Mahatma Gandhi:

"Mabadiliko ya kidemokrasia hayawezekani iwapo hatupo tayari kusikiliza upande mwingine. Tunafunga milango ya kufikiri wakati tunapokataa kuwasikiliza wapinzani wetu, au baada ya kuwasikiliza tunawafanyia mzaha. Kutokuvumiliana kunapokuwa ndio mazoea, tunajiweka katika hatari ya kutokujua ukweli."

Mheshimiwa Spika,

Baada ya kusema haya, naomba kuwasilisha.


------------------------------------------------
CHRISTINE LISSU MUGHWAI (MB)
MSEMAJI MKUU
KAMBI RASMI YA UPINZANI BUNGENI (MIPANGO)
18.06.2012
 
Back
Top Bottom