Hadithi kali Faili namba 25

Mpauko

R.I.P
Jan 19, 2019
2,323
3,353
Mwandishi: RM the brave

faili namba 25

01


Hisia za kukumbatiwa na mtu pale kitandani zilinigutusha toka kwenye usingizi mzito,nilijigeuza kivivu na kukutana uso kwa uso na mpenzi wangu wa siku nyingi, Bibiana Mgaya.

Alikuwa ni binti mrefu kiasi, maji ya kunde, hakuwa mnene wala mwembamba huku akijaaliwa wowowo la wastani lililotosha kumpagawisha mwanaume yeyote rijali, akiwa na sura ya duara ambayo daima ilipambwa na tabasamu maridadi kabisa.

"mmmh umeshaamka"niliuliza swali la kipumbavu maana ni wazi kabisa kuwa Bibiana alikuwa macho.

"ndio mpenzi wangu saa moja hii jiandae uwahi kazini" aliongea kwa upole huku akiwa kajawa na tabasamu.

"eeeh saa moja hivi" niliulza kivivu huku nikijinyoosha.

"amka bwana"

"sawa mama naamka, hivi maji ya kuoga tayari? "

"ndio amka sasa" Bibiana aliongea huku akivuta shuka na kuliondoa mwilini mwangu.

"aaagh kwani saa moja tayari? " nililalama kizembe.

Safari hii sikupata majibu, Bibiana alishayoyoma zake kwenda sebuleni, niliamka na kuingia bafuni maana nyumba hii ya vyumba viwili pamoja na jiko, ilikuwa ni self container.

Ilinichukua dakika takribani 10 hivi kumaliza shida zangu, nilitoka bafuni na kuanza kuyatupia mangwanda yangu ya kazi, mangwanda ya rangi ya khaki!, kifuani ikipambwa na namba E. 1289 nilikuwa ni polisi, konstebo Jackson Makusu au afande Makusu kama wengi walivyozoea kuniita.

Baada ya kuhakikisha nipo sawa nilijongea sebuleni ambapo nilimkuta Bibiana akiwa anapakaa blueband katika silesi za mkate, aliinua uso wake na kuachia tabasamu pana kabla ya kuniambia "karibu chai mume wangu"

Nilimtazama kwa mahaba huku nikijipweteka pembeni yake katika sofa ile ya watu wawili, nikanawa mikono na kuanza kuifakamia chai ile ya maziwa pamoja na silesi za mkate hadi nilipohakikisha ya kuwa nimeshiba hasa.

"Bibiana"

"abee konstebo Makusu" aliitikia na kuingiza mzaha

"umeanza Bibiana nilishakuambia sitaki uniite hilo jina" nililalama

"jamani sasa nikuiteje"

"niite mume wangu Makusu"

"akaaaah mara ngapi nakuambia uje utoe posa kwetu unaishia kunipiga kalenda halafu mara hi unataka uitwe mume? " aliongea huku akirekebisha kofia yangu kichwani.

"sasa si ungenisikiliza kwanza na wewe, ni hivi nataka nichuhue likizo mwezi ujao ili nilete posa" nilisema.

"waooooo unasema kweli mpenzi wangu?" aliruka kwa furaha na kunikumbatia.

"ndio mpenzi wangu acha mimi niwahi kazini tutaongea zaidi baadae" nilisimama na kumbusu kwenye paji la uso, nikatoka nje na kuitia moto gari yangu ndogo aina ya Toyota Swift, safari ya kutoka Mtaa wa Magomeni kwenda kituo kikuu cha polisi Mtwara ilianza.

Ilinichukua dakika kumi na tatu kuwasili kituoni, moja kwa moja nilielekea katika lango la kuingilia na kumkuta konstebo Amina akiandika maelezo ya mze wa makamo niliyemkuta pale, "Makusu mkuu amesema ukifika umuone ofisini haraka" alizungumza Amina huku akiendelea kuandkaandika pasi na hata kunitazama.

Sikutaka kumuuliza chochote nilinyoosha korido moja kwa moja hadi nlipoufikia mlango ulioandikwa RPC niliyatazama maandishi yale kisha nikashusha pumzi kwa nguvu kuusaka ujasiri kisha nikagonga mlango taratibu, "pita" sauti nzito na kali ilisikika, nikasukuma mlango na moja kwa moja nilipiga hatua tatu kwa ukakamavu na kupiga saluti.

"afande" nilizungumza kwa ukakaavu.

"kaa kititi, kaa tafadhali" alizungumza huku akinionyesha moja ya viti kadhaa vilivyokuwa mbele ya meza, nilijongea taratibu na kukaa kitini

"hujamho bwana Makusu"

"sijambo shikamoo mzee"

"marahaba habari za kazi? "

"salama tu mzee"

"vizuri sana,kwanza napenda nikupongeze kwa mafanikio uliyoyapara hivi sasa wewe sio konstebo Makusu bali ni Sajini Jackson Makusu"alinitazama kwa chati huku akifungua mtoto wa meza na kutoa bahasha Akaiweka juu ya meza.

"Jeshi la polisi linajivunia kuwa na vijana wachapakazi na wazalendo kama wewe" mara hii alisimama na kujongea dirishani alitupa macho huku na huko kisha akanigeukia na kunikazia macho kwa sekunde kadhaa.

"ni takribani miaka mitano sasa umekuwa moja ya askari waadilifu na wachapakazi, sote tunafahamu dhima nzito ambayo jeshi letu la polisi limekabidhiwa, kuhakikisha ulinzi na usalama wa raia pamoja na mali zao na mara kadhaa umeweza kuhatarisha maisha yako kutetea haki na usalama wa raia" alisita na kuanza kupiga hatua kunifuata alinishika begani na kunyofoa beji yenye cheo changu cha konstebo.

Akaichukua bahasha aliyoiweka juu ya meza na kutoa beji,kuona vile nilisimama kwa ukakamavu, akaitazama beji ile kwa chati kisha akapachika begani mwangu, nilitoa saluti ya heshima nisiamini kama kweli leo hii nilikuwa ni sajini Jackson Makusu.

"kaa tafadhali sajini mpya bwana jackson Makusu" akafungua mtoto wa meza na kutoa bastola ndogo aina ya Barreta mm9 akaiweka mezani kisha akatoa box tatu ndogo za risasi nazo akaziweka mezani mwisho akatoa bahasha ndogo nayo akaweka mezani

"lakini sasa haya mambo hayatokei kwa bahati mbaya kijana bali yanatokea kwa sababu maalum, mara baada ya kukukabidhi siraha hii tambua wazi kwamba umepewa jukumu kubwa, na natumaini utalitekeleza kwa weledi wa hali ya juu, chukua siraha yako, bahasha hii ina vitambulisho vyako haya inuka kijana inuka mimi nimekwisha kumalizana na wewe" aliongea kwa msisitizo.

"lakini mkuu na...... "

"sajini Makusu nimekwambia mimi nimekwisha kumalizana na wewe toka nje"

"eeeh ntoke nje hivi"niliuliza kizembe maana ikishakuwa tabia yangu kuuliza maswali yasiyo na mantiki na tabia hii ilikwishaota mizizi.

nilimtupia macho RPC Lazaro Ahmad na kumuona wazi akiwa amekereka, nilipiga saluti na kuondoka huku nikikionea fahari cheo changu kipya, Sajini Makusu yaani nilikuwa naelekea kuanza kupigiwa saluti na mimi nilitabasamu.

Baada ya hatua mbili tu simu ilitoa mtetemo niliitoa mfukoni na kutupia macho kwenye kioo, ilikuwa ni namba mpya.

"haloo"

"haloo, sajini Jackson Makusu namba E.1289 kituo kikuu cha polisi Mtwara"

"ndio nani mwenzangu"

"Awadh Mpekula, meja Awadh mpekula toka makao makuu ya polisi dar es salaam kiongozi wa operesheni Faili namba 25 tafadhali fuata maelekezo" akavuta pumzi kama kwamba alitaka maneno yale yaniingie vilivyo.

"una masaa machache ya kujiandaa, tazama katika bahasha uliyopewa kuna tiketi ya ndege ya Air Tanzania ya saa kumi na moja jioni kuelekea mwanza" mlio hafifu wa kukatwa simu ulisikika.

Nikaitupia macho simu ile kwa sekunde kadhaa nisielewe maana ya matukio yale,"eti nimepandishwa cheo halafu tena niende mwanza kwenye operesheni Faili namba 25!" nilizungumza kwa sauti ya chini nikaifungua bahasha na kukutana na kitmbulisho changu kipya pamoja na tiketi ya ndege.

Nikapiga hatua moj kwa moja hadi katika gari yangu na safari ya kurudi nyumbani ikaanza njia nzima nilibaki nikiwaza naanzia wapi kumweleza Bibiana juu ya safari ile ya ghafla.

Niliwasili nyumbani na kumkuta Bibiana akiwa anafua, aliacha kufua na kunikazia macho ya mshangao.

"wewe mwanaume vipi unaumwa au"

"hivi unaniona kama mgonjwa sio" nilimuuliza huku nikiingia ndani.

Bibiana aliacha kufua na kunifuata nyuma, moja kwa moja nilipitiliza chumbani na kukaa kitandani, "hivi una nini wewe? " Bibiana aliniuliza huku nae akikaa pembeni yangu.

"kazi hazifanyiki mpenzi wangu muda wote nakufikiria wewe" nilizungumza huku nikitabasamu

"yani mwanaume wewe huishiwi vituko" alisema huku akiangua kicheko hafifu "hebu niambie bwana una nini mwenzetu maana naona kabisa haupo sawa"

"Bibiana"

"abee"

"nimepata safari jioni hii kwenda Mwanza" na taratibu niliona tabasamu likimyeyuka usoni, akanitazama kwa chati kisha akashusha pumzi.

"Bihiana" niliita bila majibu.

tayari macho ya Bibiana yalikwishazingirwa na machozi, hapo nikaanza kazi nyingine ya kumbembeleza na hatimaye aliridhia suala lile maana ni wazi hata asingelikubali ilikwa ni lazima niende.

Niliutumia mchana ule kujipumzisha ndani na hatimaye saa kumi na nusu ilinikuta Mtwara airport nikiagana na mpenzi wangu niliyempenda sana, Bibiana.

Nilikamilisha taratibu za pale uwanjani na moja kwa moja nikaingia ndani ya ndege ya shirika la ndege la Tanzania aina ya Bombadier Q400.

Hatimaye muda wa ndege kuondoka uliwadia, rubani alitutaka tuzime simu zetu na kufunga mikanda tayari kwa kuanza safari.

Nilifunga mikanda kisha nikaitwaa simu yangu na kuweka airplane mode, kisha moja kwa moja nikaingi katika ujumbe wa maneno, nilianza kusoma sms za mpenzi wangu Bibiana na zote alinitakia safari njema.

Nikaachana nazo kwa lego la kumpigia mara nifikapo Mwanza, macho yaangu yakatua kwenye ujumbe usiokuwa na namba zidi ya neno private nkafungua ujumbe ule na kukutana na maneno matatu tu HOTEL TILAPIA 17A.

****************************

MASAA MAWILI NYUMA

Bibiana baada ya kutoka airport alinyoosha barabara ya airport moja kwa moja hadi alipoifikia stendi ya daladala Mangamba kisha akapinda kulia kuifuata barabara ya Sabasaba.

Alinyoosha hadi alipofikia barabara ya bandari akakunja kushoto kuifuata baraara ya Mnarani mwendo wa dakika tatu akakunja kulia kuelekea soko kuu Mtwara.

Baada ya kufika sokoni akaangaza huku na huko kutafuta parking hadi alipobahatisha nafasi ndogo iliyolitosha vilivyo gari hii ndogo aina ya toyota Swift, akaegesha gari kabla ya kushuka na kuingia sokoni tayari kwa manunuzi ya mahitaji ya nyumbani.

Kitu pekee ambacho hakukijua wala kuwaza kichwani mwake ni kwamba alikuwa anafuatiliwa!

Gari nyeupe aina ya Toyota Prado old model ilikuwa imesimama upande wa pili mkabala na gari ya Bibiana, mwanaume mmoja pande la mtu, mrefu kiasi, mweupe,ndevu zake aliziweka kwa mtindo wa O huku akivalia tisheti nyeupe, jeans ya blue huku chini akiwa kavalia buti ngumu za rangi ya khaki "timbarland".

Akaitoa simu yake na kubofya mara kadhaa kabla hajaiweka sikioni na kusikilizia.

"Fred mko tayari?" aliuliza huku macho yake kayakaza kwenye gari ile ndogo.

"ndio kilia kitu kipo tayari, gari ya wagonjwa imepatikana pamoja na nyaraka zote zenye taarifa za mgonjwa" sauti ya Fred ilisikika.

"Good saa 11 na nusu muwe mmeshafika, kwa sasa yupo sokoni nitaondoka naye hadi kwake natumaini kila kitu kitakwenda kama tulivyopanga" aliongea na kukata simu.

Baada ya dakika takribani 10 Bibiana alionekana akitoka na moja kwa moja akaingia garini na safari ya kuelekea Magomeni ikaanza.

Ile Prado old model nayo ikaunga tela, safari ilichukua nusu saa hivi kufika nyumbani kwa sajini Makusu.

Bibiana akapaki gari na moja kwa moja akajitoma ndani, ile prado nayo ikapitiliza na kwenda kusimama katika duka lililokuwa umbali wa hatua mia moja hivi toka ilipokuwa nyumba ya sajini Jackson Makusu.

Ngo! Ngo! Ngo! Bibiana alishtushwa na hodi ile kwani hakuwa na mazoea yakupokea ugeni wowote hususani muda kama ule takribani saa moja kasoro.

Moja kwa moja akaachana na kutazama taarifa ya habari na kwenda kufungua mlango, hata hivyo alilakiwa na sura ngeni kabisa.

"karibu" aliitikia kwa mashaka kidogo

"asante naitwa Cliford Sanga, konstebo Cliford Sanga" alijitambulisha na kuendelea "nina maagizo yako kutoka kwa shemeji Makusu"

"karibu pita ndani" Bibiana alimkaribisha huku akifungua zaidi mlango na kumpisha Cliford.

Cliford alipiga hatua tatu na kusimama baada ya kusikia mlango ukifungwa, akageuka kumtazama Bibiana safari hii tabasamu likiwa limeyeyuka, hali hii ilimshtua Bibiana na kengele ya hatari ikalia kichwani mwake.

Hata hivyo bahati haikuwa yake kwani kabla hajachukua maamuzi yoyote tayari Cliford kwa kasi alimuwahi kwa kabali ya mkono wa kushoto kabla hajachomoa kitambaa cheupe na kumziba pua na mdomo, taratibu Bibina akalegea na kujilaza pale sakafuni.

Cliford akaitupia macho sebule ile nadhifu akalisogelea jokofu dogo, akafungua na kutoa juisi ya matunda iliyokuwa kwenye chupa ya maji Ndanda, hakuwa na haja na grasi akainua chupa ile na kupiga mafunda kadhaa.

Akajipwetea kwenye kochi na kuanza kutazama taarifa ya habari, muungurumo wa gari inayopaki nje ulimgutusha, akazima televisheni pamoja na taa pekee ya sebuleni iliyokuwa inawaka kwa wakati huo, akafungua mlango na kukutana na wanaume wawili huku mmoja akiwa kavalia koti la daktari.

Cliford aliwapa ishara ya kuingia ndani, wote wakashirikiana kumbeba Bibiana na kumpakiza kwenye gari ile yenye nembo ya Hospitali kuu ya Ligula, land cruiser mkonga.

"Nisubirini nikachukue juisi" Cliford alibwata baada ya kuona dereva akiondoa gari, akachumpa na kuingia ndani, akachukua juisi aliyoibakiza na kutoka mbio akajipakia garini.

Mwendo wa dakika tatu uliwafikisha barabara kuu inayoelekea Dar es salaam, dereva akaegesha gari pembeni kisha akamtazama Cliford.

"Clif nadhani mimi kazi yangu imeishia hapa" aliongea.

"Good job Eddie, sasa kaifate gari ya mzee pale dukani kwa mangi ukampelekee, sisi kama unavyoona moja kwa moja tunakwenda Dar" aliongea Ciford huku akishuka garini na kuzunguka upande wa dereva, Eddie akashuka na kuanza kuondoka kwa mwendo wa haraka.

"dokta hebu njoo ukae huku mbele" aliita huku akicheka

"ha ha ha Clif mara hii nishakuwa dokta" aliongea Fred huku akiingia garini.

"cheki koti lilivyokutoa mzee"

"endesha gari bwana wee" alilalama Fred maana aliona wazi Cliford alikuwa anamkebehi kwani hakubahatika hata kumaliza darasa la saba.

Cliford huku akiwa bado anacheka aliingiza gia na safari kuelekea Dar ikaanza, yapata saa mbili na nusu usiku.

******************

TUKUTANE SEHEMU YA 2
 
Mwandishi anahitaji kuona angalau wasomaji 20 ili mambo yaendelee
 
***********02************

Niliangaza macho huku na kule nikitafuta usafiri wa tax ni takribani dakka15 toka ndege itue katika uwanja wa Kimataifa wa Mwanza, nilikerwa na upweke wa eneo hili kiasi kwamba hata usafiri ulikuwa wa kuokoteza hususani jioni hii ya saa mbili kasoro usiku.

"kaka unahitaji usafiri? " sauti ndogo ya kiume ilinigutusha, nikageuza macho yangu na kukutana na kijana mwembamba maji ya kunde, akivalia suruali ya kitambaa nyeusi na shati jeupe lisilopigwa pasi na chini akiwa na kiatu cheusi kilichojaa uchakavu huku kiwi nzito nyeusi ikipewa mzigo wa kuficha uchakavu huu.

"ndio nahitaji usafiri" nilimijibu huku nikijaribu kumtathmini kijana huyu, akiwa na sura ya upole na macho yake yalijionyesha wazi kuwa ni mtumiaji wa kirevi cha bangi.

"karibu naitwa Issa, twende garini bosi wangu nikufikishe wapi" alizungumza huku akitaka kunipokea begi langu lakini nilipuuia mapokezi yale, moja kwa moja akaongoza njia hadi katika moja ya magari yaliyoegeshwa eneo lile, tukajipakia katika gari aina ya Toyota spacio, issa akawasha gari na kutulia kusubiri maelezo.

"nipeleke Tilapia hotel"

"elfu thelathini tu boss"

"twende"

Sikutaka majadiliano nilichotaka ni kwenda Tilapia tu, issa akaondoa gari tukashika njia ya airport na mwendo mfupi tukaingia katika barabara ya Makongoro.

Baada ya mwendo wa dakika mbili gari jeusi aina ya toyota prado vx ilitupita kwa kasi, hakuna aliyejali si mimi wala dereva tax issa aliyezungumza kila mtu alikuwa kimya.


Baada ya dakika 7 hivi tukaipita round about ya standard chartered bank, nikavutika kuitazama gari nyeusi aina ya toyota prado VX ikiwa imepaki jirani ya ATM ya benki ya standard chartered bank, nikaikumbka vilivyo gari hii ndiyo iliyotupita dakika chache zilizopita, nikaipuuzia kwani sikuona kama kuna haja ya kuifikiria gari ile.

Tukiwa tunakaribia kuvuka daraja la mto Mirongo nikagutuka baada ya kuliona tena gari ile nyeusi ikiwa nyuma yetu, nikamtazam Issa, hakuonekana kuwa na habari yoyote juu ya gari ile nyuma yetu,

Nywele zilinisisimka na sasa nilihitaji kuwa na uhakika kama gari ile imatufuatilia ama laah sikutaka kuipuuzia.

"issa hivi kuna supermarket maeneo haya? "

"ipo, unataka tupitie? "

"ndio tafadhali pitia kaka"

Dakika tatu mbele Issa akaingia upande wa kulia mwa barabara na kusimamisha gari mbele ya jengo lililoandikwa WOTE MINI SUPERMARKET.

nikashuka na kutupia macho barabarani, VX ile ikapita kwa mwendo wa taratibu ikiendelea na safari, nikashusha pumzi na kuzama katika tafakuri fupi nisielewe maana ya kile kinachotokea, je nafuatiliwa au ni mawenge yangu tu? Sikupata jawabu la moja kwa moja.

"vipi kuna tatizo?" Issa aliuliza baada ya kuona nimesimama pembeni ya mlango wa gari.

"aaaah samahani kaka tuendelee na safari tu maana nimekumbuka nina nauli yako tu hapa"

"hahha ingia garini tuamshe au ka vipi nipatie kabisa hiyo nauli" sikumjibu nilitabasamu tu na kujipakia garini.

Safari hii nilikuwa makini sana kuitafuta ile VX nyeusi, lakini hadi tunafika round about ya Samaki Samaki Corner, sikuliona tena gari ile, tukaiacha barabara ya Makongoro na kuchukua barabara ya stesheni hadi old capri cabana, tukiwa tunakaribia kumaliza pori la saanane niligutuka baada ya kuiona tena VX ikitupita kwa kasi.

"hii gari siielewi kabisa" issa aliongea baada kuiona ile VX ilivyotupita kwa fujo.

"hata mimi inanitia mashaka sana, cheki inavyopunguza mwendo halafu mekaa katikati ya barabara"

"aisee tugeuze gari nishakosa amani mimi" issa aliongea huku akionekana wazi kuanza kuhamanika

"subiri hebu omba saiti tuone kama atatupisha"

Issa akaongeza mwendo na kuwasha indicator, Ile VX ikaacha saiti tukaanza kuipita, tukiwa sambamba, nikatupia macho gari ile.

haikuwa na tinted, niliweza kumuona dereva, kijana chotara wa kiarabu, kichwani akiwa na staili ipendwayo na vijana wengi yaani kiduku, nilimtazama kwa tuo na mara akashusha kioo.

"issa piga breki tunakufa" niliongea kwa hamaki baada ya kuona mdomo wa bastola ukielekea upande wetu, issa akaahika breki na sekunde chache tulishuhudia kioo cha mbele kikiwa kimetengeneza nyufa kuzunguka tundu dogo la risasi iliyoishia kupiga siti ya nyuma.

"hayawani huyu nuaura tufe, issa mfuate kwa kasi asituache" niliongea huku nikichomoa bastola yangu.gari ile iliongeza kasi na kupotea mbele yetu.

Tayari tulishaifikia barabara ya Capri Point, issa akakunja kushoto na kusimama pembeni ya duka la vipuri vya magari.

Issa hakuongea chochote alibaki palepale ameshika tama na kuegemea dirisha, nikamtazama ni wazi alikuwa akifikiria kuhusu kioo cha gari yake.

"hey tumefika au? " niliongea na kuagaza angaza macho, issa akanitazama kwa sekunde kadhaa.

"kioo" aliongea huku sasa akionekana kama anayetaka kulia

"kioo hiki nitamwambiaje bosi? Mi sina hela na ndio kwanza siku ya pili tangu bosi anikabidhi gari hii! " alilalama Issa

"nipe namba yako ya simu nikurushie pesa ukarekebishe kioo"

"hivi unajua thamani ya hiki kioo wewe? "

"ndio ni laki mbili na sabini"

"hivi una gari bosi? " issa aliulia kwa mshangao maana ni kweli kuwa kioo kile kiliuzwa shilingi laki mbili na sabini.

"nipe namba upesi"

issa akatoa karatasi na kuandika namba yake ya simu, nikamtumia laki tatu na ishirini kupitia huduma ya simbaning, niliona uso wa Issa ukichanua kwa tabasamu, akawasha gari.

Dakika kumi na mbili zilitosha kutufikisha nje ya majengo nadhifu ya hoteli ya kitalii ya Tilapial.

wahudumu nadhifu walinilaki nikasindikizwa hadi mapokezi, nikamkuta msichana mrembo kwelikweli akiwa kavalia sketi nyeusi na shati nyeupe yenye maandishi yaliyosomeka "welcome Tilapia Hotel" juu ya mfuko wa shati huku akinng'iniza kitambukisho chenye jina la Zainab Sanga.

"karibu sana" alinikaribisha huku aliachia tabasamu la kuvutia

"asante sana ni mgeni wa mwenye chumba namba 17A"

"Jackson Makusu" alisema na kutoa funguo ya kielektroniki mithiri ya kadi ya benki, akanikabidhi,kisha akabeba begi langu na kunitaka nimfuate.

Dakika mbili zilitsha kutufikisha upande wa mashariki mwa hotel hii ambako ilipakana na ziwa Victoria, safari yetu ikakomea mbele ya mlango wa chumba kilichosomeka 17A.

Zainabu akanitazama kisha akatabasamu na kuondoka kwa madaha, miondoko ile ikanifanya nikumbuke kuwa sikuwa nimemtaarifu Bibiana wangu kuhusu kuwasili kwangu salama.

Nikaketi katika sofa dogo iliyokuwemo mle chumbani, nikaitwaa simu yangu na kumpigia Bibiana, simu haikuwa inapatikana, nikaitupia simu kitandani na kuanza kukitathmini chumba hiki.

Kilikuwa ni chumba kidogo lakini nadhifu sana, kilitazamana na zwa Victoria, kilisanifiwa kwa mtindo wa kuvutia, kikisheheni choo na bafu, huku kikiwa na friji dogo ukutani, televisheni pamoja na kisimbuzi cha Dstv, niliridhishwa na chumba hiki nikajipweteka katika kochi dogo pekee chumbani mle.

Fikra zangu zikavutika kukumbuka tukio lililotokea muda mfupi uliopita, je! Ni nani yule bwana aliyejaribu kutuuwa kwenye ile tax?

Hapana yule bwana hakudhamiria kutuuwa kwani angedhamiria kutuuwa basi angeitoa bastola yake kwa kasi na kutuwahi, lakini kinyume chake aliitoa bastola yake na kuishikilia kwa sekunde kadhaa ili niione!

Alipoachia risasi pia alilenga mahali ambapo alikuwa na uhakika kuwa haitamdhuru mtu, lakini kwanini aliachia risasi moja tu? Alikuwa na nafasi ya kutuletea madhara endapo angepiga zaidi ya risasi moja.

Lakini kwa nini hakuficha uso? Kwanini alitabasamu? Ni nani yule bwana kwnini akakimbia baada ya kurusha ile risasi moja? Kikubwa zaidi ni kwamba tumetoka naye airport ina maana alikuwa anajua kuwa nitawasili hapa leo? Swali hili la mwisho lilinifanya niingiwe na woga kiasi chake.


Niligutushwa na mlio wa kufunguliwa kwa mlango, nikasimama kwa hamaniko nikakutana uso kwa uso na mwanaume mwenye mwili wa wastani lakini uliojengeka kimazoezi, akiwa na kitambi kwa mbali.

Alivalia jeans nyeusi, tishirt jeusi na alinyoa kwa mtindo wa afro, raba zake nyeusi zilizokuwa na utepe mweupe zilimfanya apendeze zaidi,akibebelea begi mkononi.

Nilimuona akibabaika na kurudi nyuma kutazama namba ya mlango kisha akanitupia macho ya mshangao.

"hiki ni chumba changu, chumba namba 17A" aliongea huku akiweka chini begi lake.

"kama uonavyo bwana kina mtu nadhani wamekosea kukupatia chumba"

"nadhani, lakini hizi funguo za kielektroniki haziaminiki kabisa tazama wewe una funguo yako nami nina funguo yangu lakini bado zimefungua mlango mmoja"

"hapana hicho ni chumba chenu wote" sauti nzito ilisikika na mara hii alitokeza mtu mzima wa makamo ya mwishoni, miaka 45-50 hivi, alivalia kaunda suti nyeusi iliyompendeza kwelikweli, mkononi akiwa amebeba bahasha kubwa.

Akampita yule bwana mgeni na kuingia chumbani alipofika mbele yangu akageuka kumtazama yule bwana mlangoni.

"kwahiyo wewe huingii ndani? " alizungumza huku akimkazia macho, yule bwana akaingia ndani na kufunga mlango kisha akabaki akiwa amesimama mbele ya mlango.

"naitwa Awadhi, Meja Awadhi Mpekula" alizungumza na kututupia macho kwa zamu

"nimesema naitwa Meja Awadhi Mpakulo, lakini naona mnang'aa macho tu hamjafundishwa heshima vijana? "

Nikamtupia macho ya kumtegea yule bwana mgeni, tukakutanisha macho kisha kwa pamoja tukakakamaa na kupiga saluti.

"Afande" tuliongea kwa pamoja.

Meja Awadhi akatutazama na kutabasamu, akapiga hatua za madaha huku mikono yake akiwa ameishikanisha nyuma.

"Sajini Jackson Makusu toka Mtwara kutana na Inspekta Harold Mlembuka toka Dares Salaam" akasita kisha akaitazama bahasha yake kwa sekunde kadhaa kisha akaingiza mkono na kuchomoka na faili dogo la buluu akalitupia kiandani.

Akazama tena katika bahasha na kutoa simu mbili za kisasa nyeusi,nazo akazitupia kitandani kisha akaanza kutembea taratibu, akafungua mlango akaondoka.
**********************************
NAAM!! SAJINI MAKUSU USO KWA USO NA INSPEKTA HAROLD... FAILI KITANDANI... JE! BIBIANA YUKO WAPI? TUKUTANE KESHO
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom