Habari kwa ufupi

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,792
287,994
Zitto: Sijatumia maneno ya kejeli
na Salehe Mohamed
Tanzania Daima

MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (CHADEMA), amesema maneno yaliyomo kwenye barua aliyomwandikia Spika Samuel Sitta, ni ya msingi na si kejeli wala dharau kama anavyoeleza spika huyo.
Alisema, mambo hayo ya msingi yanapaswa kufanyiwa kazi na Spika badala ya kukwepeshwa kama anavyofanya sasa kwa kudai barua hiyo imejaa maneno ya dharau na kejeli kwa Bunge.

Akizungumza na Tanzania Daima kwa njia ya simu jana, Zitto alisema hawezi kumwandikia Spika barua ya kejeli kwa kuwa anamheshimu kutokana na umri, cheo na ukomavu wake katika siasa.

Alisema Bunge ni mahali pa heshima, ndiyo maana alitumia busara kuandika barua hiyo akitaka haki itendeke.

"Siwezi kuandika maneno ya kejeli wakati nina hoja za msingi na ninahitaji zifanyiwe kazi ili niweze kupata haki yangu na kusafishwa jina langu," alisema Zitto.

Aidha, Zitto alifafanua kuwa hawezi kwenda mahakamani kama iliyoelezwa na Spika kwa vyombo vya habari hadi atakapopata majibu ya barua yake.

"Mimi nilimpelekea barua kutaka adhabu niliyopewa ya kusimamishwa bungeni Agosti mwaka jana ipitiwe upya hivyo naye anapaswa kunijibu kwa maandishi, baada ya hapo nitajua cha kufanya," alisisitiza Zitto.

Desemba 24 mwaka jana, Zitto aliwasilisha barua kwa Sitta, akitaka kupitiwa upya kwa adhabu aliyopewa ya kusema uongo bungeni.

Alisema kusimamishwa huko kulimfanya aonekane muongo ndani na nje ya Bunge, hivyo anamtaka Spika na baadhi ya mawaziri kuchukuliwa hatua kwa madai ya kuueleza umma kwamba yeye ni mwongo huku wakishindwa kuthibitisha madai yao.

Baada ya kupokea barua hiyo, Spika kupitia Katibu wake, Daniel Eliufoo, alitoa taarifa kwa vyombo vya habari akieleza kuwa Zitto atapelekwa kwenye Kamati ya Maadili na Madaraka ya Bunge kwa kuwa barua yake imejaa kejeli, ufedhuli na ubabe dhidi ya Bunge na Spika.

~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*
CHADEMA yataka maandamamo kupinga bei ya umeme

na Charles Ndagulla, Moshi
Tanzania Daima


CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimewataka Watanzania kufanya maandamano ya amani kupinga kupanda kwa gharama za maisha ikiwamo ongezeko la bei ya nishati ya umeme.
Changamoto hiyo imetolewa mwishoni mwa wiki mjini hapa na Mbunge wa Viti Maalumu, Lucy Owenya (CHADEMA), alipozungumza na waandishi wa habari.

Alisema kupanda kwa gharama za maisha ni matokeo ya sera mbovu chini ya serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na uongozi unaoendekeza matumizi mabaya ya mali za Watanzania.

Owenya, alikuwa akizungumzia hatua ya Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji nchini (EWURA) kukubali ombi la Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kupandisha viwango vya bei ya umeme kwa asilimia 21.7.

Alisema hatua hiyo itawafanya Watanzania wengi hasa waishio vijijini kushindwa kuunganishiwa nishati hiyo na kuonya kuwa uharibifu wa mazingira utaendelea kwa wananchi kukata miti kama nishati mbadala.

Alisema nishati hiyo mbadala ni ghali kutokana na ukweli kwamba ni nishati inayoharibu mazingira, kwani wananchi wengi wataendelea kuharibu misitu kwa kukata miti na kuchoma mkaa.

Hata hivyo, mbunge huyo alisema kupanda mara kwa mara kwa gharama za maisha ni matokeo ya kuwepo mikataba mibovu inayosainiwa na watawala ukiwamo wa IPTL.

Alisema kampuni hiyo ni mzigo na imekuwa ikiligharimu mamilioni ya fedha taifa kila mwezi, kwani hata Watanzania wasipotumia umeme ni lazima wailipe IPTL.

~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~

Mkurugenzi wa tiba MNH afariki

na Lucy Ngowi
Tanzania Daima

MKURUGENZI wa Huduma na Tiba Saidizi katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dk. Dalmas Dominicus (56) amefariki dunia ghafla mwishoni mwa wiki iliyopita, kijijini kwake Shirati, mkoani Musoma.
Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano, Aminiel Aligaesha, alitoa taarifa hiyo kwa vyombo vya habari akieleza kuwa alipokea habari za kifo hicho kutoka kwa ndugu wa marehemu kwa njia ya simu.

Katika taarifa hiyo, Aligaesha alieleza marehemu Dk. Dominicus alianza likizo Desemba 14, mwaka jana na baadaye kwenda kijijini kwake kwa ajili ya mapumziko ya sikukuu za Noeli na mwaka mpya.

"Akiwa nyumbani kwake usiku wa kuamkia Desemba 29 mwaka jana marehemu aliugua ghafla na kufariki dunia kabla ya kufikishwa hospitali," ilieleza sehemu ya taarifa hiyo na kuongeza kuwa marehemu alizaliwa Wilaya ya Tarime, mkoani Mara Agosti mwaka 1951.

Ilieleza kuwa, marehemu alijiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kitivo cha tiba, Julai mwaka 1974 na kupata shahada ya kwanza ya udaktari Mei, 1979.

Aprili mwaka 1989 marehemu alijiunga na Chuo cha Tiba cha Chuo Kikuu cha Ryukyus, Japan na kupata stashahada yake ya uzamili ya udaktari Machi 23, 1993.

Aliteuliwa kuwa mkuu wa Idara ya Tiba na Dharura toka 1995 hadi 2003. Pamoja na mambo mengine alikuwa mratibu wa huduma za tiba binafsi na baadaye kuwa mkurugenzi wa huduma za tiba saidizi hadi mauti yalipomfika.

~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*~*

Polisi waimarisha ulinzi mpaka wa Kenya

na Richard Mwangulube, Arusha
Tanzania daima

JESHI la Polisi limeimarisha ulinzi katika maeneo yote ya mpaka wa nchi ya Kenya na Tanzania kutokana na vurugu zinazoendelea katika nchi jirani ya Kenya hivi sasa.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, Basilio Matei, alisema jana kuwa polisi wamechukua tahadhari zote kukabiliana na vitendo vya uhalifu katika mpaka wa nchi hizo mbili.

"Hali si shwari kabisa nchini Kenya kutokana na matokeo ya uchaguzi mkuu uliomalizika katika hali ambayo baadhi ya wagombea hawakubaliani nayo, hali ambayo imesababisha kuwepo na fujo ambazo zinaweza kusababisha baadhi ya watu kukimbilia Tanzania bila utaratibu," alisema.

Kamanda Matei, alisema mbali na kuimarisha ulinzi mpakani pia jeshi hilo limeimarisha doria katika maeneo yote ya wilaya za mkoa huo hasa katika wilaya za Ngorongoro na Longido ambazo ziko mpakani na Kenya.

Wakati huohuo, Kamanda Matei, alisema Polisi wamesimamisha mabasi yote ya abiria yanayosafiri kati ya Dar es Salaam, kupitia Arusha-Kenya, kwenda Kampala, hadi hali itakapokuwa imetengamaa nchini Kenya.

Alisema mabasi hayo ni lazima kwa sasa yasitishe safari kwenda Kampala kutokana na kutokuwepo na usalama katika nchi ya Kenya hivi sasa.

Ametoa wito kwa wamiliki wa mabasi hayo kuwa na subira pamoja na uvumilivu katika suala hilo hadi hali itakapokuwa shwari.




 
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimewataka Watanzania kufanya maandamano ya amani kupinga kupanda kwa gharama za maisha ikiwamo ongezeko la bei ya nishati ya umeme.

Sina uhakika kama kuandamana na kupinga peke yake kunaweza kusaidia. Matatizo ni mengi yanayosababisha gharama ya maisha kupanda, ikiwwmo kupanda kwa bei za mafuta. Tuangalie other altenatives za energy. I wish kungekuwa na makampuni mengine yanayotoa huduma ya umeme! Natamani bidhaa za solar zingekuwa within the reach! Natamani technolojia ya kuzalisha umeme kutumia biogas kwa small scale(septic tanks) ingekuwa promoted, ili wananchi wawe na altenatives nyingine.

Ni vizuri pia watu wakademonstrate ili kuionyesha serikali kuwa wananchi wamechoka kimaisha.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom