Gharama ya Kuchagua - CCM waendelee kukataa Katiba Mpya

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,474
39,987
Na. M. M. Mwanakijiji

Uchaguzi umekwisha. Na muda wa kulalamikia watawala unaanza tena. Cha kushangaza wapo watu ambao hawaoni uhusiano wa uchaguzi wao na matokeo ya uchaguzi huo. Watanzania walipewa vyama mbalimbali vya kuchagua na wagombea mbalimbali; katika uchache wao wakajitokeza kwenda kupiga kura na kuchagua walichokichagua. Nikifumba macho kutokujali masuala ya uchakachuaji au lawama dhidi ya tume ya uchaguzi ukweli unabakia wenyewe kuwa wengi bado wameamua kuchagua watu wale wale, kutoka chama kile kile chenye sera zile zile.

Cha kushangaza miongoni mwa waliofanya hivi ndio wanasimama leo na kuanza kushangaa matokeo ya uchaguzi wao. Wapo ambao baada ya kuchagua walitegemea waone tofauti ya mfumo wa kutawala n.k Na wapo wengine ati nao wanaingia kwenye treni la kudai katiba Mpya!

CCM haikuahidi Katiba Mpya wala hakuna chama kilichokuwa na ajenda ya kuanza mchakao wa Katiba mpya isipokuwa Chadema! Vyama vingine vya upinzani navyo vilikuwa vinadokeza kuwa na haja ya kuwa na Katiba Mpya na NCCR hiyo ilikuwa ni jiwe lake la msingi. Lakini mamilioni ya Watanzania walichagua CCM na ajenda yake na wagombea wake. Hivyo, Watanzania wengi walijua kabisa siyo ajenda ya CCM kuwa na Katiba Mpya.

Hii maana yake ni kuwa mwana CCM yeyote wa kawaida au kiongozi anayesimama na kusema ati "tunahitaji Katiba Mpya" anataka kutuchezea akili! Alikuwepo wapi wakati wa kampeni kudai hilo? Kwanini hawakuingiza kwenye Ilani yao wakati suala hili linajulikana tangu 1992? Mkapa alikuwa madarakani kwa miaka 10 akijua kabisa kuwa watu wanalalamikia Katiba Mpya; serikali yake ilikataa badala yake ikafanya mabadiliko ya ajabu kabisa ya Katiba (kama yale ya 2005)! Sasa leo baada ya uchaguzi anasema ati Katiba mpya ni suluhisho na watu wanashangilia! tena ameenda kusemea ugenini (inanikumbusha majuto yake ya vifo vya Watanzania kule Pemba - alifanyia pia nje ya nchi). Wapo watu wanaona kaona mwanga!

Ndugu zangu, uchaguzi una gharama na matokeo yake. Wana CCM wasikubali haja ya Katiba Mpya kwani siyo ajenda yao na siyo ilani yao. Hivyo wasiwe kigeugeu; wang'ang'anie kutokuwa na Katiba Mpya.

Wakati huo huo vyama vilivyoahidi Katiba Mpya viendelee na msimamo wake na ikibidi vianzishe mchakato wake wenyewe wa suala hilo ili tunapoenda 2015 mstari uwe umechorwa wazi kabisa kati ya wanaotaka Katiba Mpya na wale wanaotaka kuendelea na mfumo huu huu. Kama CCM wameshindwa kusimamia mabadiliko makubwa ya Katiba hadi hivi sasa sidhani kama watakuwa katika nafasi ya kufanya hivyo sasa. Wao wameshinda hakuna Katiba Mpya kabla ya 2015.

Vyama vya upinzani kwa kulindana na sera zao na mipango yao waamue kuendelea na suala la hoja ya Katiba Mpya ili kwa mara nyingine walete hoja hiyo kama ilani kwenye uchaguzi mkuu wa 2015 ili wananchi wachague tena. Chama kitakachoshinda ndio kisimamie uandikaji huo wa Katiba Mpya kama ilivyokuwa kule Kenya.

Vinginevyo, CCM iitishe mkutano mkuu maalum (baada ya kupokea mapendekezo ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM) kuwa iwe ni ajenda ya CCM sasa kusimamia uandikaji wa Katiba Mpya. Ni baada ya hilo tu kwa haki kabisa wana CCM wataonekena wanazungumzia ajenda ya chama chao sasa hivi, Katiba Mpya ni ajenda ya upinzani - hususan Chadema - kwani wao walisema wangeanza mchakato wa kuandika katiba mpya ndani ya siku 100 za kushika madaraka.

Vyovyote vile ilivyo, tutambue uchaguzi una matokeo yake na matokeo yana gharama yake. Ndio maana binafsi sina muda wa kulalamikia Dowans, Richmond, n.k kwa sababu Watanzania wameamua kwa hiari yao kuishi na mambo hayo. Tena nimeshaanza kupoteza kabisa hamu ya kuzungumzia kashfa zijazo za serikali kwa sababu nitakuwa kana kwamba nilifikiria hazitatokea tena wakati tunajua sote kuwa uchaguzi haujabadilisha mfumo na wale chama tawala hakikuahidi hata mara moja mabadiko yoyote sasa sijui msingi wa watu kuombea mabadiliko unatokana na nini isipokuwa njozi za alinacha tu na dua za kuku.

CCM wameshinda uchaguzi, wanapongezana kwa ushindi huo, waache watutawale wapendavyo hadi siku ile Watanzania watakapoona kuwa "sasa imetosha". Nilidhani wangesema hivyo 2010 lakini inaonekana bado na uwezekano mkubwa sasa ni CCM kujitengeneza ili ifikapo 2015 WAtanzania wasiwakatae zaidi ya sasa. Yote ni gharama ya uchaguzi; na kila uchaguzi una matokeo yake na haya ndiyo matokeo ya uchaguzi wetu.

kwa miaka mitano ijayo.
 
Mkuu Mwanakijiji, umeeleweka vizuri sana. Tupo pamoja. Mtu akiamua kupita njia ya miiba na akionywa akakataa, akichomwa miiba asilalamike.
 
exactly... na wawe tayari kulipia gharama ya uchaguzi huo; kwa mfano, watu wa Dar wakilalamikia barabara mbovu au mazingira machafu inabidi tuwashangae!!

Mimi mbona nimeshaacha kushangaa!

Ila cha kushangaza zaidi wewe ukiwashangaa na wao wanakushangaa kwa nini unawashangaa!!!!
 
Mimi mbona nimeshaacha kushangaa!

Ila cha kushangaza zaidi wewe ukiwashangaa na wao wanakushangaa kwa nini unawashangaa!!!!

very true... na katika kukushangaa kwao huko wanaweza kukuona wewe unapandikiza "chuki binafsi" (whatever this means)!
 
Back
Top Bottom