Gavana abanwa fedha za EPA; Adai serikali pekee ndiyo inajua matumizi yake

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797




*Adai serikali pekee ndiyo inajua matumizi yake
*Asema bei ya umeme imeongeza makali ya maisha


Na Tumaini Makene

MZIMU wa kashfa ya wizi wa fedha zilizoibiwa katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), Benki Kuu ya Tanzania (BoT), umeendelea kuibuka, ambapo
kamati ya bunge imembana Gavana Beno Ndullu aeleze kiasi cha fedha kilichorejeshwa, mahali zilipo na namna zilivyotumika.

Gavana Ndullu mbali ya kutoa maelezo mafupi kwa uangalifu , akisema kuwa hawezi kuwa 'msemaji wa hilo', alisema kuwa 'mwenye fedha hizo ni serikali...sisi ni watunzaji tu, wao wanajua namna wanavyozitumia."

Hayo yaliibuka jana katika kikao cha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) na BoT, ambapo kamati hiyo pia ilihoji juu ya hali ya uchumi nchini, hususan suala la kupanda kwa gharama za maisha kunakozidi kuwaathiri Watanzania kila kukicha.

Kwa muda mrefu sasa, tangu kuibuka kwa kashfa hiyo na serikali kupitia kwa Rais Jakaya Kikwete kusema kuwa watakaorejeshwa fedha hizo watasamehewa kosa hilo la jinai, kumekuwepo na mjadala mkubwa juu ya zilipo fedha zilizorudishwa na namna zilivyotumika, huku wengine wakihoji uhalali wa watuhumiwa wa kusamehewa makosa yao nje ya mahakama.

Hali hiyo ya sintofahamu juu ya fedha za EPA, sasa imekuwa ni moja ya ajenda nchini, baada ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Fedha za Serikali (CAG) kusema fedha hizo hazionekani popote. Pia baadhi ya vyama vya siasa kuhoji zilipo, kwani benki ya wakulima ambako rais mwaka 2008 aliahidi zitapelekwa, haijaundwa mpaka leo.

Wa kwanza kuulibua suala la EPA katika kikao cha jana, ni Mbunge wa Viti Maalum CCM, Bi. Ester Bulaya aliyetaka kupata ufafanuzi juu ya mahali ziliporejeshwa fedha hizo, iwapo zilipelekwa BoT au Benki ya Rasilimali Tanzania (TIB).

"Naomba kupata ufafanuzi kutoka kwa baba yangu Gavana juu ya fedha za EPA zilizorejeshwa, je, zilirejeshwa wapi...TIB au zilipelekwa straight forward BoT. Je, ni kiasi gani mpaka sasa kimepatikana. Hivi karibuni kuna kesi ya EPA imemalizika, je, BoT kama mdau mkubwa wa fedha hizi imejipanga vipi kimkakati.

"Kuhakikisha hawa waliohukumiwa hawafanyi udanganyifu wowote katika mali zao maana kuna fedha wanapaswa kulipa kama fidia kwa mujibu wa hukumu iliyotolewa," alisema Bi. Bulaya.

Mwenyekiti wa POAC, Bw. Zitto Kabwe alitia msisitizo wa kutaka kujua hasa fedha hizo zilikokwenda na zilivyotumika, na Gavana Ndullu alisema;

"Rais aliunda kamati maalumu kwa ajili ya kufuatilia fedha hizo...kazi yetu ilikuwa ni kuzitunza...tukiambiwa fungua akaunti zitoke zinatoka. Sitaki kuwa msemaji wa hilo, lakini katika zile bilioni 90 zilizothibitika, zilirejeshwa bilioni 69.6, ndiyo tulizopokea. Mgawanyo wake ulikuwa clear, bilioni 53 mwaka 2008 nadhani kama sikosei zilikwenda TIB," alijibu Gavana Ndullu kabla Bw. Kangi Lugola (CCM-Bunda) hajaingilia akisema;

"Mheshimiwa mwenyekiti nafikiri suala lako halijajibiwa vizuri, gavana ambaye ndiye anahusika na fedha hizi anasema anadhani hana uhakika, sasa..."

Ndipo Gavana Ndullu akaamua kujivua suala hilo akisema, "ieleweke vyema mheshimiwa mwenyekiti na wajumbe, mimi si mtoaji wa hizo fedha, sisi ni banker (watunzaji) tu. Hazina ndiyo tunaoshughulika nao. Serikali ndiyo inajua namna hizo fedha zinavyotumika. Kwanza sipaswi kulizungumzia suala hili, hata niliyoyazungumza nimeyasema tu, mpaka tupate mwongozo maalumu wa kufanya hivyo."

Katika suala la kupanda kwa gharama za maisha ambalo liliibuliwa na Mbunge wa Tandahimba, Bw. Juma Njwayo, aliyetaka kujua asilimia ya mfumuko wa bei mpaka sasa, jitihada zinazofanywa na BoT katika kudhibiti hali hiyo.

Akijibu suala hilo, Gavana Ndullu alisema mpaka Aprili mwaka huu, mfumuko wa bei ulikuwa umefikia asilimia 8.6, ukisababishwa na vitu vitatu, ambavyo ni kupanda kwa bei ya mafuta, ambayo imeathiri gharama za uzalishaji na usafirishaji, kupanda kwa bei ya umeme kwa asilimia 18 mapema mwaka huu, ambayo mbali ya kuathiri matumizi ya nyumbani pia imeathiri uzalishaji kwa gharama kuongezeka.

"Kitu kingine cha tatu ni bei ya chakula ambapo mpaka sasa imepanda mpaka kufikia asilimia 9, imekuwa ikipanda mwaka hadi mwaka na hii ndiyo sababu hasa ya chanzo cha mfumuko. Lakini tumekuwa tukijitahidi kudhibiti na katika mapendekezo yetu katika bajeti ijayo mtaweza kuona kwa takwimu. Tumekuwa hatuongezi ujazi wa fedha ili tusichochee bei zaidi.

Alisema takwimu zinaonesha kuwa mahitaji ya chakula ndiyo yanachukua sehemu kubwa ya asilimia ya matumizi katika familia, ambapo familia moja inatumia asilimia 46 ya mapato yake katika kila sh. 100 kwa ajili ya kununua chakula. Hivyo akakubali hoja ya Bw. Zitto na wabunge wengine kuwa BoT itoe ushauri thabiti juu ya umuhimu wa taifa kujikita katika uzalishaji wa chakula.

Katika hatua nyingine, Mwandishi Gladness Mboma anaripoti kuwa Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) imeendelea kuzibana halmashauri mbalimbali jana ikiwa ya Monduli mkoani Arusha, ikiitaka kueleza walikopeleka sh. milioni 123 walizopelekewa kwa ajili shughuli za maendeleo vijijini.

Hayo yalibainika jana wakati Kamati hiyo ilipokuwa ikichambua nyaraka mbalimbali za matumizi ya fedha za halmashauri ya Monduli, ambapo Mwenyekiti wa Kamati hiyo Bw. Augustino Mrema alihoji fedha hizo baada ya Mkaguzi wa Mahesabu za Serikali Kanda ya Kaskazini, Bw. Asalea Kihupi kuieleza kamati hiyo kwamba fedha zilizotengwa kwa ajili ya maendeleo vijijini hazijapelekwa kwa walengwa.

"Mkurugenzi Mtendaji ebu tueleze ni kwa nini fedha hizo hazijapelekwa vijijini mpaka leo na ziko wapi, na mmefanyia nini na kwa manufaa ya nani. Tunataka utueleze nidhamu ya fedha za serikali ziko iko wapi, maana maagizo ya kamati mmeyakaidi," alisema

Akijibu swali hilo, Mkurugenzi huyo, Bw. Samweli Mlay kwanza aliiomba kamati hiyo radhi kwa kushindwa kufikisha fedha hizo kunakohusika kwa madai kwamba walizitumia kutokana na matumizi mengi yanayozidi mapato ya ndani, ikiwa ni pamoja na kupokea ruzuku iliyoko chini ya viwango.

Bw. Mrema alimuuliza Mkurugenzi huyo kwamba ni nani aliyempa madaraka ya kutumia fedha za watu kwa shuguli nyingine, ambapo Bw. Mlay alikiri kufanya makosa na hakupewa ruhusa na mtu yoyote kutumia fedha hizo na kusisitizia kuzirejesha kwa wananchi kutoka katika vyanzo vyao vya mapato vya mwaka 2011.

 
Kama maelezo ya Gavana yanakubalika, huyo Gavana anafanya nini pale Benki Kuu na Wajumbe kwanini hawataki kwenda kuwahoji wahusika wenye uwezo na mamlaka ya kujibu?
 
Back
Top Bottom