Fumbo

Aug 1, 2016
7
17
FUMBO (01)

PUA za Leila ziliipokea harufu ya manukato iliyopozwa na kiyoyozi, mara baada ya kufungua mlango na kuingia ofisini. Chini, sakafu ilifichwa na zulia la sufi. Juu, taa zenye rangi anuwai zililizunguka dari mithili ya nyota zipendezavyo anga. Nusu ya kila dirisha ilifunikwa kwa mapazia ya rangi ya samli ilhali nusu ya pili ikikingwa na vioo. Mvuto wa ofisi na umaridadi wa samani zake, vilipambanua haiba na tajriba ya bosi anayeimiliki. Alitembea taratibu, akiyapita makochi yaliyopangwa kwa kuizunguka meza ya vioo katikati ya ofisi.

Mama Mbegu alikuwa ameketi nyuma ya meza ya duara, akiendelea kuperuzi kompyuta yake. Hata Leila alipomsabahi, bado hakujikalifisha kunyanyua uso wake, aliishia kuitika salamu hali macho yameganda kwenye kioo cha kompyuta. Leila akiwa amesimama asijue la kufanya, ndipo aliinua uso, akivua miwani na kuitenga mezani, na kwa mkono wake wa kushoto akamwashiria aketi. Kisha, akajitengeneza wigi lake, lenye mchanganyiko wa rangi nyeusi na kahawia, lililofunika kichwa pamoja na masikio, na kushuka hadi usawa wa mabega. Alipomaliza, akavitenga viwiko vya mikono juu ya meza kiasi cha kufanya bangili na pete za dhahabu kumeremeta.

Leila alivuta kiti kimoja, kati ya viwili vilivyopangwa mbele ya meza. Hata baada kuketi, bado alijihisi kama bado amesimama. Mapigo ya moyo yalimgomea kutulia. Kitendo cha kuitwa ofisini na mama Mbegu, ilikuwa ni sawa na mwanafunzi kuitwa na mwalimu wa nidhamu ofisini – ambapo kwa kawaida huwa haiingi yeyote bali kuna walakini.

“Enhe, una matatizo gani na Seba?” mama Mbegu alimrushia swali. Japo sauti yake ilikuwa tulivu na isiyo papara, walakini ilijaa shari.

“Hakuna tatizo, bosi,” Leila alijibu kwa indhari, huku akiminya macho yake kiudadisi.

Mama Mbegu alipandisha nyusi juu huku macho yake makubwa yaliyokolea wanja wa chini, akiyazungusha tamthili ya mtoto mwenye degedege.

“Unajua, muda niliopanga kuzungumza nawe ni dakika tano tu,” alisisitiza huku akiinua mkono kutazama saa, “na mpaka sasa umekwishatumia dakika mbili. Sasa, usipokuwa makini, nazo zitakwisha kabla sijajua cha kukusaidia. Umenipata?”

“Ndio bosi.”

“We ndiye msaidizi wa Seba, na mlipaswa mwende pamoja Kanada, kikazi. Nimeambiwa uligoma kusafiri naye, na bado unasema hakuna tatizo!”

Kimya kifupi kilitanda wakati wakitazamana. Leila aliinamisha macho chini, akihisi baridi ya hofu ikimzizima maungoni. Hakuwa amepanga kumwambia mtu yeyote kuhusu chochote baina yake na Sebastian. Lakini kwa kuhofia kisirani cha mama Mbegu, alifunua kinywa, “Seba amenikasirikia, bosi.”

Mama Mbegu aliachia ucheko hafifu, japo sauti iliyotoka haikuwa ya cheko halisi, bali ni kama madebe mabovu yaliyonyeshewa mvua.

“Kwa hiyo unasubiri nikuulize hadi sababu ya ugomvi wenu?”

“Hapana, bosi,” Leila alijibu haraka na kuendelea, “Seba alianzisha tabia mbaya. Kila mara alipoingia ofisini, alianza kunishikashika bila ridhaa yangu. Nikamwambia sipendi hiyo tabia. Akaacha. Ghafla, siku hiyo nilikuwa nimeinama kabatini nachuk–”

“Eh! Eh! Makubwa haya,” mama Mbegu alidakia huku tabasamu la ugwadu likijijenga usoni mwake. “Kwa hiyo mwenzetu kushikwa tu mpaka uandikiwe barua ya maombi?”

Kama ipo walau chembe ya aibu machoni mwa mama Mbegu, ingelihitajika darubini kuweza kuiona. Leila alipoinua uso kumtazama kwa tahayari, alikutana na uso mkavu usio na soni. Akaishia kuvuta pumzi nyingi na kuzitoa taratibu.

“Lakini bosi, nilikwishamweleza na akanielewa. Mimi ni mke wa mtu. Mume wangu akijua itak–”

“Atajuaje? Utaenda kumwambia? Au amekufunga Bluetooth mwilini?”

Leila hakujibu. Akainamisha kichwa chini.

Mama Mbegu aliinuka kitini. Akasimama na kujitengeneza kivazi chake; blauzi ya rangi ya hudhurungi iliyodariziwa kwa riboni za kahawia, na kubandikwa vishikizo vyeusi vilivyofunikwa kwa papi pana juu yake, viliupendezesha mwonekano wake. Sketi ya rangi ya damu ya mzee, iliyoishia juu ya magoti iliruhusu miguu yake minene kuonekana vizuri, kadri alivyopiga hatua kuelekea kwenye korido ndefu iendayo maliwatoni. Alipoifikia meza ndefu ya mninga iliyobanwa ukutani kando kando mwa korido, alisimama na kushika chupa ya chai. Akajimiminia kahawa kwenye kikombe kidogo. Akarudi nayo mezani.

“Seba anarudi leo usiku, na kwa taarifa nilizonazo, tayari anayo barua yako mkononi,” alisema huku akiweka kikombe cha kahawa mezani. “Hakuhitaji tena kazini.”

Leila alihisi misuli ya tumbo ikikakamaa. Ngurumo mithili ya radi zilirindima tumboni mwake. Taratibu, jasho likaanza kutengeneza chemchemi makwapani.

“Bosi nakuomba nisai–”

Mama Mbegu alimnyooshea kiganja kumzuia asiendelee kuzungumza. Akaketi na kusema, “Unaelewa namna nifanyavyo kazi na Seba. Hatuingiliani kwenye maamuzi. Nilipokutafutia nafasi ya kazi, nilimsisitiza mama Mainda akwambie kuwa, jukumu la kuipigania na kuilinda nafasi yako si langu tena. Nadhani alifanya hivyo. So, sitokuwa na mahali pengine pa kukupachika endapo Seba ameamua kukutimua.”

Leila alimeza funda la mate na kufanya koromeo lake kucheza saka-mke-wangu. Ndani ya muda mfupi, tayari uso ulimshuka mithili ya mbuzi anayesubiri kuchinjwa.

Tangu mzee Dominic Mbegu, mmiliki wa kampuni ya Crops Investment Limited, alipougua kiharusi na kushindwa kutimiza majukumu yake, mama Mbegu kwa kushirikiana na Sebastian Mbegu, mdogo wake mzee Mbegu, walisimamia na kuendesha kampuni. Mafanikio ya kampuni chini ya usimamizi wao, yalichagizwa na namna walivyolindana na kwa kila mmoja kuchunga mipaka waliyowekeana.

Mama Mbegu akaendelea, “Leila, bahati ikibisha hodi mlangoni, unainuka kwenda kuifungulia – usisubiri hadi na mlango ijifungulie.”

Leila aliinamisha kichwa huku mikono ameifumbata mapajani wakati mama Mbegu akizungumza. Alipoinua kichwa kutaka kusema neno, tayari alikuwa amechelewa.

“Endapo nami ningejifanya malaika kama wewe, leo nisingelikuwa bosi hapa. Nilianza kazi hii kama secretary wa mzee Mbegu, nikiwa nimekwishaolewa – kama wewe tu. Lakini ndani ya miezi yangu hiyo,”– alitandaza vidole vitatu vya mkono wa kushoto– “mitatu tu. Nikaanza kulipwa mshahara mkubwa kumzidi hata meneja. Unadhani humo ofisini nilikuwa namkenulia meno tu?”

Leila alifumba macho kwa fadhaa na izara. Kila silaha ya maneno aliyopanga kuitumia ilizidiwa nguvu na ulimi wa mama Mbegu.

“Mumeo yuko wapi?” mama Mbegu alivunja ukimya.

“Amekwenda Arusha.”

“Good.” Alinyanyua kikombe cha kahawa na kupiga funda moja, kisha akakirejesha mezani. “Seba anaingia leo. Saa moja usiku. Aliniomba nipeleke mtu akamsafishie nyumba. Sasa, huu ndo muda wa kucheza karata yako ya mwisho. Hakikisha ukitoka kazini unakwenda kufanya hiyo kazi. Akifika akukute kwake. Hapo sasa juhudi zako ndo zitaamua, ama akupe barua ya kukufukuza kazi au ya kukuongeza mshahara.”

Leila alifunua kinywa kusema, maneno yakakwama kwenye kuta za koromeo lake. Akabaki anahangaika mithili ya nzi aliyenasa kwenye utandu wa buibui.
***

Basi la Kilimanjaro Express liliwasili Kituo cha Mabasi jijini Arusha, na kupokelewa kwa shangwe na mbinja toka kwa wapiga debe. Mara baada ya kuegesha mahali pake, tayari likazungukwa na wajasiriamali – kila mmoja akinadi biashara yake kwa sauti kubwa, ili kukabiliana na sauti za muziki zilizohanikiza eneo lote la stendi.

Ikunji Almasi ni miongoni mwa abiria walioteremka mwishoni kabisa ili kukwepa rabsha za wasafiri waliokuwa wakiharakia kushuka, pamoja na bughudha za wajasiriamali waliokuwa nje ya basi. Bado hilo halikufaa kitu. Aliposhusha tu mguu mlangoni, alilakiwa na kundi la madereva bodaboda pamoja teksi; baadhi wakiwa juu ya pikipiki zao, wengine wakiwa wima – wote wakiwania abiria.

“Salaam aleykum, kaka,” kijana mmoja, aliyekuwa amesimama mbele kabisa ya mlango wa basi, alimlaki Ikunji kwa bashasha. “Habari za Dar?”

Kwa mazingira yale ya stendi, ilikuwa muhali kwa mtu asiyefahamiana naye kumlaki moja kwa moja kwa salamu ile. Hilo likachota nadhari ya Ikunji, akidhani pengine wanafahamiana.

“Waaleykum salaam,” alijibu akimtazama usoni kijana mrefu, mweusi, mwenye nyusi hafifu zilizoyazunguka macho yake makubwa. Kidevuni alifuga mzuzu mrefu. Alivalia suruali ya bluu na kubadhi za kahawia. Shati lake jeusi la mikono mirefu alilikunja nusu yake.

“Utahitaji teksi kaka?” kijana aliuliza kwa taadhima, akinyoosha mikono ili kupokea mkoba wa Ikunji.

Swali hilo ndilo lilimtanabahishia Ikunji kuwa, kijana yule alikuwa dereva teksi au shanta. Hakufanya haraka kumjibu wala kumpatia mkoba wake. Akaendelea kutembea taratibu kuelekea kwenye geti la kutokea.

“Nahitaji hoteli nzuri, lakini isiwe mbali sana,” Ikunji alisema baada ya kupiga hatua chache, akiinua mkono kutazama saa. “Nimeambiwa maeneo ya Sanawari kuna hoteli nzuri, na si ghali sana.”

Ikunji hakuwa mwenyeji wa Arusha. Hii ilikuwa mara yake ya pili kufika jijini humo. Mara ya kwanza ilikuwa ni takribani miaka mitano nyuma.

“Wala usijali bosi. Hapo Soweto tu kuna hoteli nzuri zaidi, na za bei poa. Nitakupeleka.”
Waliendelea kutembea hali Ikunji ameudhibiti mkoba wake ubavuni. Waliifikia teksi nje ya geti. Wakaingia na kuondoka. Kiasi cha dakika kumi, waliwasili nje ya uzio wa hoteli nzuri. White Rose Hotel. Ikunji alilipa nauli, akateremka na kuelekea ndani.

Nyuma ya meza ya mapokezi, aliketi msichana mweupe, mnene. Alivalia fulana nyeupe yenye ukosi mwekundu, aliyoshabihisha na kapelo nyeupe yenye chepeo nyekundu. Macho yake meupe yenye kiini cheusi, yalionekana vizuri nyuma ya miwani myeupe iliyoshikiliwa vema kwa mwamba wa pua yake pana.

“Nahitaji chumba,” Ikunji alisema baada ya kumsalimu.

Mhudumu alimsogezea Kitabu cha Wageni. Akamwekea na kalamu juu ya kitabu. Ikunji akajaza taarifa zake. Alipomaliza akarejesha kitabu pamoja na kiasi cha pesa alichotajiwa.

“Ghorofa ya pili,” mhudumu alisema huku akimkabidhi funguo, “chumba namba 225.”

Hapakuwa na lifti. Kwa hivi, ilimlazimu kupanda vidato vya ngazi kwa miguu. Mandhari ya hoteli pamoja na utulivu wake vilimfurahisha. Alihitaji sehemu tulivu kama ile. Hadi anafika ghorofa ya pili, ni mwanamume mmoja tu aliyepishana naye koridoni akikokota mabegi yake.

Alifungua mlango na kuingia. Alipowasha taa macho yake yalilakiwa na kitanda cha futi tano kwa sita, kilichowekwa upande wa kulia, kikiwa kimetandikwa shuka nyeupe pamoja na mito iliyovishwa foronya za rangi hiyo. Upande wa kushoto, kabati refu na pana lilipangana na jokofu dogo jeupe. Dari na marumaru vilishabihiana kwa rangi ya maziwa. Alikwenda kuketi kitandani huku akiuzungusha mkoba miguuni. Alipoufungua na kujiridhisha usalama wa vilivyomo, akaufunga na kuuweka juu ya meza ndogo, pembezoni mwa kitanda, kisha akjilaza chali.

Haikuchukua muda, alisimama na kujinyoosha viungo. Alitia mkono kwenye mfuko wa suruali na kutoa chaja ya simu. Akaisogelea swichi ya ukutani na kuibandika, kisha akaipachika simu. Ilikwishatimu saa mbili na robo usiku.

Aliingia msalani ambako macho yake yalipokelewa na kioo kirefu, kilichowambwa ukutani juu kidogo ya karo ya maji. Ndevu nyeusi zilimtapakaa mashavuni huku macho yakimlegea kwa usingizi na uchovu wa safari. Shati la mistari ya kahawia na njano pamoja na jinzi ya bluu, havikuonesha taathira ya safari, kwa sababu basi alilopanda, pamoja na ubora wa barabara, havikuruhusu vumbi kupenya ndani yake. Baridi kali iliyokuwa ikizizima kila kona ya jiji la Arusha, ilisababisha mpango wake wa kuoga uyeyuke tamthili ya mvua ya kiangazi juu ardhi kame. Akaishia kujimwagia maji kichwani na kurejea chumbani.

Njaa ilianza kumshambulia tumboni. Akachomoa simu kwenye chaji kabla haijajaza moto lau kidogo. Akachukua mkoba wake na kutoka nje kwenda kutafuta chakula.

Kwakuwa hakuwa akienda mbali, hakuona haja ya kukabidhi funguo. Alimpita mhudumu angali ameketi nyuma ya kaunta. Alitoka hadi nje kidogo tu ya hoteli, ulipo mgahawa wa chakula. Nyuma ya meza kubwa mgahawani, aliketi kwa kujilaza bwana mmoja mfupi, maji ya kunde na mnene kupindukia.

“Habari mzee?” Ikunji alimsalimu.

Bwana yule hakujitaabisha kufunua kinywa. Alitingisha kichwa kama ishara ya kuitika salamu.

Ikunji akaendelea, “Nifanyie chipsi kavu, ndizi mbili na mishikaki mitatu.”

Bwana yule alibaki vile vile amejilaza kizembe hali ya kuwa macho ameyafumba. Kifua chake kipana kilipanda juu na kushuka chini kadri alivyopumua. Baada ya sekunde kadhaa ndipo alichezesha mboni zake, kisha akafumbua jicho moja kivivu huku tumbo lake kubwa akilikuna kizezeta.

“Utakula hivyo hivyo kavu kama nyoka?”

Ikunji alihisi ghadhabu pamoja na cheko kwa mkupuo. Alitaka kununa, na papo hapo alitamani kucheka. Kila alichofanya mhudumu yule kilijaa mzaha na upuuzi. Ule msemo wa ‘mteja ni mfalme’ ulionekana mgumu kwa bwana yule kuliko msamiati wa ‘kuchina’.

“Okay, niwekee na juisi ya embe.”

Bwana yule alijiinua kidogo, akajitengeneza kitini, na kujinyoosha kwa nguvu hadi kishikizo cha shati kikaachia na kumwacha tumbo wazi. Hakujali hilo.

“Sasa, unaonaje kama ukilipa kabisa ili tukufanyie chap kwa haraka!”

“Ni bei gani?” Ikunji alimwuliza.

“Ukinipa elfu tano utakuwa umejitendea haki,” alijibu huku akiachama mdomo mithili ya mamba anayewinda wadudu.

“Ukifungua akaunti mtandaoni utapata followers wengi sana,” Ikunji alisema, huku akifungua wallet kutoa pesa.

“Kwa nini?”

“Yeah, mtandaoni watu hupendelea zaidi upuuzi.”

“Kwa hivyo unaona nafanya upuuzi hapa, siyo?” aliuliza kwa hamaki.

“Sijasema unachofanya hapa, bali unachoweza kunufaika nacho mtandaoni,” Ikunji alijibu na kumkabidhi pesa huku ametabasamu. “Kama hutojali niajiri nikufungulie akaunti mtandaoni.”

Bila kuongeza neno, aliikwapua pesa toka kwa Ikunji, akifuatisha na msonyo mrefu kama kasuku.

Kwa uvivu aliouonesha bwana yule, pamoja na kisirani chake, Ikunji aliiona dalili ya kusubiri chakula kwa zaidi ya nusu saa. Kwa hivyo, aliona aheri arudi chumbani kuchajisha simu yake, ndipo ashuke tena mgahawani kufuata chakula. Akaondoka.

Alipokifikia chumba na kutaka kupachika funguo kitasani, alishangaa kuona mlango uko wazi. Akakunja sura kiudadisi. Aliposhika kitasa na kusukuma mlango, papo hapo mlango ukadhibitiwa kwa ndani. Ikawa kama mashindano; wa ndani anauzuia – wa nje anausukuma. Alipouachia, ukajibamiza kwa nguvu. Alirudi nyuma hatua kadhaa akiwa bado hajaelewa kinachoendelea. Mwanzo alidhani amekosea chumba. Akainua macho kuangalia namba ya chumba juu ya mlango. Ni chumba namba 225.

Akiwa bado amesimama, macho yalipiga chini ya mlango. Mchirizi wa damu ukitokea chumbani, ulitiririka taratibu sakafuni. Alikunja ndita kiasi cha macho yake kusinyaa. Alihisi damu ikimsisimka kwa woga. Hakuwa tena na ujasiri wala sababu ya kuendelea kusimama. Alirudi hatua moja nyuma na kutimua mbio bila kugeuka.

Alipofika mapokezi aliangaza huku na kule, hakumwona mhudumu. Mtu mmoja tu alikuwa ameketi kwenye viti vya wageni akisoma gazeti. Kwa mtazamo wa Ikunji mtu yule alionekana kama ni mgeni anayemsubiri mhudumu, au ni mtu aliyekaa hapo mahsusi kumshikia nafasi mhudumu aliyetoka kwa dharura.

“Eti, mhudumu yuko wapi?” Ikunji alimsaili mtu huyo baada ya kumsogelea.

Mtu yule aliweka gazeti pembeni, akamtazama, kisha akarudisha macho gazetini kana kwamba hakusikia alichoulizwa.

“Samahani kaka, namuulizia mhudumu,” Ikunji alirudia.

“Ndo salamu hiyo?” alijibu bila kuondoa gazeti usoni.

“Aah!” Ikunji alirusha mikono hewani.

Aligeuza na kutoka nje. Hakuona busara kuendelea kubaki maeneo yale. Alivuka upande wa pili wa barabara na kwenda kusimama mkabala na hoteli. Alihakikisha mkoba haumponyoki kwa namna yoyote. Maswali mia–hamsini–kidogo yalimpitikia kichwani.

Kwanza alifikiri pengine ni mpangaji wa chumba jirani ndiye aliingia chumbani mwake kimakosa, na kwamba alipofika yeye na kufungua mlango kwa nguvu, ndipo ulimbamiza kichwani na kumtoa damu iliyokuwa ikichuruzika. Lakini kumbukumbu zake zote zilimwambia kuwa aliufunga mlango alipotoka.

Sasa ni nani aliyeingia? Alipata wapi funguo? Na dhamira yake ni ipi juu yangu? alijiuliza.

Kadri alivyojilazimisha kutafuta majibu, ndivyo maswali mengi yalichipuka kichwani mwake mithili ya uyoga kichuguuni. Hisia zake ziliposhindwa kumshawishi chochote, akaona ni busara kuondoka eneo lile. Lakini si kabla ya kumpigia simu mkewe kumjuza kilichomsibu. Na kisha Sudi Chotara, mmiliki wa mzigo aliotoka nao Dar es Salaam.
***

Sebastian Mbegu aliwasili nyumbani kwake majira ya saa mbili usiku, akitokea nchini Kanada. Mlango wa kuingilia ndani ulikuwa wazi. Hakushangaa kwa sababu alikwishapewa taarifa na mlinzi getini juu ya uwepo wa mgeni ndani. Aliingia sebuleni akiangaza huku na kule. Alikutanisha macho sako kwa bako na Leila aliyekuwa anapanga vyombo kabatini.

“Oh, Leila!” Sebastian alisimama na kuweka begi sakafuni.

Leila aliyekuwa amevalia shimizi nyepesi ya rangi ya samli, iliyoishia juu ya magoti, ikiacha wazi sehemu kubwa kuanzia mabegani hadi makwapani, aliachia tabasamu hafifu. Akaachana na vyombo kabatini na kumwelekea Sebastian. Kila hatua alizopiga, miguu ilipishana mithili ya Twiga. Mikono yake iliyotengeneza mbonyeo kwenye maungio ya viwiko, ilipepea taratibu mithili ya kishada kiendacho arijojo.

“Karibu, bosi,” Leila alimlaki kwa insafu, huku akiinama kuchukua begi.

Sebastian aliwahi kumshika mikono kabla hajakamata begi. Akamnyanyua huku akimtazama machoni. “Asante Leila. Unapendeza mno ukiwa katika kivazi cha nyumbani.”

“Asante,” Leila alisema na kukwepesha macho pembeni. “Pole kwa uchovu.”

“Aah, shukrani. Nilipokuona tu, uchovu wote ukayeyuka.”

Leila akatabasamu asiwe na la kuongezea.

“Nawe pole kwa usumbufu,” Sebastian alisema angali amemshika mikono. “Kusafisha jumba lote hili si kazi ndogo.”

“Usijali. Wanawake tumeshazoea shughuli hizi.”

Kimya kilitanda kila mmoja akipandisha na kushusha pumzi. Sebastian aliendelea kumchezea Leila viganja vya mikono yake kwa namna iliyoibua ghamu.

“Nilikumiss, Leila,” Sebastian alivunja ukimya.

“Mimi pia.”

Kama aliyekuwa akisubiri jibu hilo, Sebastian alimwinamia na kumbusu kwenye paji la uso. Kisha, akamzungushia mkono wa kushoto kiunoni ilhali wa kulia akiupeleka kichwani kumchezea nywele nywele.

Leila alihisi vipepeo vikimnyevua mwilini. Bila ajizi, naye akainua mkono wa kulia na kumwekea begani, hali ule wa kushoto akimwekea kifuani. Alihisi chemchemi ya asali ikimtiririka ndani ya uti wa mgongo wakati Sebastian alipopenyeza mikono ndani ya shimizi yake na kuipachua loki ya sidiria. Aliinua macho kumtazama wakati sidiria ikadondokea katikati ya miguu yao. Kasi ya upumuaji ilimwelemea. Akaachama mdomo.

Sebastian alitumia fursa hiyo kumpokea. Papi za midomo yao ziligandana kwa sekunde kadhaa, kabla Sebastian hajambeba Leila na kwenda kumbwaga taratibu kwenye makochi.

“Seba,” Leila alinong’ona, macho yakiwa nusu mduara kama mbalamwezi. “Please, naomba iwe siri.”

Kabla Sebastian hajajibu chochote, simu ya Leila iliyokuwa mezani iliita. Wakaganda kwa pamoja wakiisikilizia.

“Oh my God,” Leila alisema kwa mshituko, akimsukuma Sebastian pembeni. “Ikunji huyo anapiga simu.”

“Umejuaje kama ni yeye?”

“Mwito huo nimemsetia yeye.”

Akiwa amebakiwa na nguo ya ndani tu, Leila alisimama na kujongea mezani. Akaikwapua simu yake mezani huku akitweta. Aliendelea kuitazama ikiita hadi alipojiridhisha kuwa pumzi zake zimekwishatulia.

“Hallow!”

Kimya.

Akaita tena, “Hallow mume.”

Hakuna majibu. Akatoa simu sikioni na kuitazama. Bado ilikuwa hewani.

Alipoirejesha tena sikioni, pumzi nzito upande wa pili wa simu ilisikika ikipanda na kushuka. Alipotaka kuongea tena, ndipo akamsikia: “Leila, uko wapi?”

Dhambi huandamwa na hofu ya kukamatwa. Kuulizwa yuko wapi, kumlimfanya ahisi kugundulika. Taratibu mapigo ya moyo yakaanza kushika kasi kama garimoshi.

Sasa ajibu nini? Hayupo nyumbani. Hayupo kazini. Yuko kwa Sebastian.

“Ahm… niko… niko nyumbani. Kuna nini kwani?”

“Una–” Simu ilikatika kabla Ikunji hajamalizia alichokusudia kusema.

“My God,” Leila alisema, huku akiiondoa simu sikioni na kuitazama.

“Kuna nini mpenzi?” Sebastian alijiinua sofani na kumfuata Leila mezani.

“Iku ameniuliza niko wapi? Halafu sauti yake haiko sawa kabisa,” alimjibu huku macho yangali yameganda simuni. “Kuna kitu ametaka kusema lakini simu imekata.”

“Sasa wahi kumpigia kabla hajapiga tena. Jiamini. Akirudia tena swali hilo, mwambie uko maeneo ya nyumbani, jifanye hata uko dukani.”

“Je, kama kuna mtu aliniona nikiingia humu kwako ndo akampigia?”

Swali hilo lilimvuruga kichwa Sebastian. Akaanza kunusa harufu ya hatari. Sebastian na Ikunji walipata kuwa marafiki; Ikunji akiwa ni msimamizi kwenye kampuni ya Sebastian inayohusika na michezo ya bahati nasibu. Ilikuwa ni wiki baada ya mzee Dominic Mbegu, kaka yake na Sebastian, kuugua ghafla kiharusi kiasi cha kushindwa kufanya kazi, na kumteua Sebastian, kwa kushirikiana na mke wa mzee Mbegu, kusimamia makampuni yake, ndipo siku hiyo Sebastian alimjia Ikunji na habari iliyozaa uhasama baina yao.

“Niambie kaka,” Ikunji alimlaki Sebastian. “Ofisi mpya inakwendaje?”

“Nashukuru Mungu nimeingia na mguu wa bahati,” Sebastian alijibu huku akiketi. “Nimefika tu nimekutana na mwajiriwa mpya huyo; kifaa cha nguvu. Haraka nimemwamishia ofisini kwangu kama msaidizi wangu.”

Kengele ya hatari iligonga kichwani mwa Ikunji. Ni kipindi kama cha mwezi mmoja nyuma, Leila alikuwa ameajiriwa katika kampuni hiyo ya mzee Mbegu. Wakati huo walikuwa kwenye uchumba. Hofu yake ikawa, isijekuwa Sebastian anamaanisha Leila.

“Anaitwa nani?” Ikunji alimsaili.

Alipotajiwa jina la Leila, Ikunji alihisi kisu cha moto kikimchana katikati ya moyo wake. Baada ya Sebastian kumwaga sifa za Leila, ndipo Ikunji akamweleza kuwa Leila ni mchumba wake.

“Umeshaanza, kila mwanamke ni mchumba wako. Kwa huyu bora tugombane. Mwenye kisu kikali ndiye atakula nyama.”

Siku hiyo, baada ya kutoka kazini, Ikunji alikutana na Leila na kumsaili kila nukta kuhusu Sebastian. Leila alikiri kuhamishiwa ofisini kwa Sebastian, na alikiri kuwa Sebastian alianza kuonesha dalili za kuvutiwa naye. Kadri siku zilivyokwenda mbele, Sebastian alianza kudhihirisha ghadhabu zake kwa Ikunji. Kazi ikatawaliwa na nongwa na visasi. Majukumu yasiyotekelezeka yakaongezeka. Mifarakano ya mara kwa mara ikashamiri. Hatimaye ikamlazimu Ikunji kuacha kazi.

Ili kumkata ngebe Sebastian, mwezi mmoja baada ya kuacha kazi, Ikunji alifunga ndoa na Leila. Dhamira ya Ikunji ikawa ni kumwachisha kazi Leila pindi atakapopata ajira sehemu nyingine. Haikuwa hivyo, alipuyanga takribani mwaka mzima bila kupata kazi. Kila senti aliyohifadhi ilipukutika kama nywele kwenye kichwa cha mtoto mwenye vibarango. Akaanza kuishi kwa kutegemea mshahara wa mkewe.

Uhasama huo baina ya Ikunji na Sebastian, Leila aliufahamu vilivyo. Kwa hivi alijua bayana kuwa, endapo Ikunji amegundua kuwa ameingia nyumbani kwa Sebastian, hakuna ushawishi utakaopenya masikioni mwake ili kuuhadaa ubongo wake.

Bila kufanya zohali, Leila aliufanyia kazi ushauri wa Sebastian. Akabofya namba za Ikunji na kubandika simu sikioni.

Namba unayopiga kwa sasa haipatikani, tafadhali jaribu tena baadaye.

“Nahisi kuna kitu hakiko sawa, Seba,” Leila alisema. “Hapatikani. Acha tu niende.”

Sebastian alianza kuhisi mchoko wa safari ukimwingia ghafla. Moto wa mapenzi ulikwishawaka kichwani mwake. Kuachwa ghafla namna ile kulimsononesha.

“Leila, natamani kukuzuia usiende.”

“Usijali, Seba. Next time.”

Leila alimalizia kuvaa nguo zake. Akaita usafiri wa Uber na kuondoka.

****

Ikunji alisonya kwa ghadhabu baada ya simu yake kuishiwa chaji na kujizima. Hakuwahi kumwambia chochote Leila. Kibaya zaidi, hata Sudi Chotara hakumpigia simu tangu alivyowasili jijini Arusha.

Sudi Chotara ni mfanyabiashara wa madini, ambaye licha ya ukwasi mkubwa anaomiliki, hakuendekeza anasa wala ghururi za dunia. Alijitenga mbali na ayuni katika nyendo zake kiasi kwamba, akafanikiwa kudhibiti mawimbi ya umaarufu wake.

Urafiki wa Sudi na Ikunji hauna muda mrefu tangu walipofahamiana. Ni Sudi ndiye aliyeanza kuvutiwa na Ikunji, takribani miezi mitatu nyuma, alipofika Dar es Salaam kwa mfanyabiashara mwenziye wa dhahabu, ambapo Ikunji ni mfanyakazi.

“Vipi biashara?” Sudi alianza kumsaili Ikunji, aliyekuwa ameketi dukani.

“Aah kidogo kidogo kadri ya hali…kuna nyakati za maji kupwa na maji kujaa.”

Hivyo ndivyo mahusiano yao yalivyoanza kumea. Baada ya Sudi kugundua umakini wa Ikunji, alizidi kuimarisha mizizi ya ukaribu wao.

“Nafikiri tunahitaji kuzungumza kidogo kuhusu maisha,” Sudi alipata kumwambia Ikunji siku moja alipofika hapo dukani.

Baada ya muda wa kazi, walikutana maeneo ya Posta, kwenye mgahawa wa New Grano Coffee. Ikunji ndiye alikuwa wa kwanza kuwasili, robo saa kabla ya muda wa miadi. Kwa mshangao, alimkuta Sudi Chotara tayari ameketi mgahawani. Sudi akamlaki Ikunji kwa taadhima kubwa.

Baada ya kuketi na kusabahiana, Sudi alianzisha mazungumzo, “Kwanza, kama hutojali, ningependa kujua una muda gani tangu uajiriwe pale dukani, na una mkataba wa muda gani?”

Si swali lililompendezesha Ikunji. Akapiga kimya kwa sekunde chache akitafakari. Lakini kwakuwa alikwishaanza kuelewa dhamira ya Sudi, akajibu, “Sina mkataba. Bado sijaajiriwa rasmi.”

“Vema. Sasa, kuna kazi nataka tufanye pamoja. Nitakulipa vizuri.”

Ikunji alipandisha nyusi zake juu kama ishara ya kumtaka Sudi afafanue zaidi kuhusu kazi hiyo pamoja na malipo yake.

“Kwa ufupi, mimi na bosi wako tunafanya kazi kwa muda mrefu sasa. Lakini mwaka jana, alitaka kununua kizimba cha dhahabu Geita. Nikamkopesha pesa nyingi. Mpaka leo malipo yamekuwa tabu. Tukaafikiana kuwa, ataniachia soko hapo dukani ili nikilangua dhahabu kwa bei ya chini na kwenda kuuza kwa bei ya juu, nitajilipa kiasi cha gharama zangu. Nalo limeshindikana. Ananipa wateja watatu kati ya kumi mnaowapata.”

“Aah. Pole sana. Niliwahi kusikia hizo story hapo dukani nilipoanza kazi, lakini sikujua kama ziko kwa ukubwa huo.”

“Ndo hivyo. Sasa, kwakuwa wewe ndiye unayepokea wateja. Nataka tufanye kazi mimi na wewe bila kumshirikisha bosi wako.”

Kazi yenyewe ilikuwa ni Ikunji kudhibiti wafanyabiashara wa dhahabu, wanaofika dukani kuuza dhahabu zao na kupatana nao bei kabla hawajaingia ndani kuuza, kisha azilangue kwa niaba ya Sudi Chotara. Sudi aliahidi kuwa anamtumia pesa kwa ajili ya kufanikisha biashara ile. Kiasi alichopanga kumlipa, ni mara dufu ya alipwavyo hapo dukani. Ingelikuwa muhali kwa Ikunji kukataa ofa ile.

Biashara hiyo mpya ya siri, ilikuwa ni yenye tija kwa Ikunji. Akaifanya kwa ustadi na uangalifu mkubwa. Ikafika safari ya mwisho ambapo mzigo aliolangua ulikuwa mkubwa. Sudi akamtaka asafiri nao hadi Arusha, ili pamoja na mambo mengine, wapate wasaa wa kufanya makubaliano makubwa zaidi kibiashara. Ikunji akamfikia bosi wake. Akaomba ruhusa kwa kisingizio kuwa anaumwa. Aliporuhusiwa, akafanya safari ya siri kwenda Arusha.

Akiwa bado amesimama mkabala na hoteli, Ikunji aliendelea kutafakari ikiwa ni salama kwake kurudi hotelini au kuondoka. Hatimaye alikata shauri. Aheri ya nusu shari kuliko shari kamili. Alimfuata dereva bodaboda aliyekuwa ameketi juu ya pikipiki yake.

“Wapi nitapata hoteli nzuri? Isiwe mbali sana na hapa.”

Dereva bodaboda alimtazama Ikunji usoni kwa muda, akamwambia. “Kaka, naitamani kweli hela yako, lakini kama ni hoteli tu ingia hapo patakufaa.” Alimwonesha hoteli ile ile aliyoikimbia.

“Sihitaji mitaa hii.” Ikunji aliitazama hoteli aliyotoka, bado hakukuwa na dalili zozote za utata.

“Basi sawa,” dereva alijibu huku akivaa vizuri koti lake pamoja na kofia. “Twende Sanawari kuna hoteli nzuri pia.”

Ikunji alipanda pikipiki bila kuongeza neno. Wakaondoka. Mwendo wa dakika tano, waliwasili na kuegesha nje ya Nyati Inn Hotel. Akateremka na kulipa nauli aliyotajiwa, kisha akatembea kuelekea ndani. Pale Mapokezi, alilakiwa na mhudumu wa kiume. Safari hii, hakujaza majina halisi kwenye kitabu cha wageni, akihofia usalama wake. Baada ya kulipa akapatiwa ufunguo na maelekezo. Ghorofa ya tatu. Chumba namba 397. Kama ilivyo hoteli ya mwanzo, hii pia haikuwa na lifti. Hivyo alipanda juu kwa miguu.

Koridoni, ghorofa ya tatu, alikutana na mama mmoja mnene, mfupi, maji ya kunde, akitokea mwishoni mwa korido ile. Aliambaa upande wa kushoto ili kurahisisha upishanaji. Katika hali asiyoitegemea, mama yule naye alihama upande aliokuwa na kumfuata usawa wake. Walipokaribiana akasimama.

“Mambo,” mama yule alimsalimu huku ametabasamu.

Meno yake ya mbele yalikuwa ya rangi ya dhahabu. Alivalia fulana nyeupe yenye kola ya kijani, na bukta pana nyeusi iliyoshuka hadi chini ya magoti. Chini ya makwapa, juu ya fulana, aliongezea kujitanda kwa upande wa khanga. Miguuni alivaa raba nyeusi zenye ufito mweupe.

“Safi, shikamoo,” Ikunji alimwamkia.

“Karibu mdogo’angu.” Aliikwepa shikamoo. “Utahitaji chakula nikuletee?”

“Oh hapana, dada. Asante.”

“Hapa hotelini hawauzi chakula.” Aliweka chini mifagio pamoja na ndoo iliyokuwa na chupa za sabuni pamoja na vitambaa vya kusafishia vioo. “Kama ukitaka nitakufuatia kule mtaa wa pili. Wanatengeneza chakula safi kabisa; kuna biriani kuku, makange ya mbuzi, mandi ya kondoo, pia wanauza sek–”

“Sawa dada, nikihitaji kula nitakuagiza.”

“Poa mdogo’angu. Na kama umechoka sana, naweza kukuletea mtu wa kukufanyia masaji. Nina wasichana wazuri hapa. Wazuri mno. Ikiwa utapenda alale chumbani mwako, nitakuchagulia dogodogo.”

“Ondoa shaka. Nitakucheki,” Ikunji alimkatiza. Akamshika mkono na kumkabidhi noti. Walau akaweza kupata upenyo na kumpita.

Hadi Ikunji anaufikia mlango wa chumba, mama yule alibaki palepale akiendelea kushukuru kwa takrima aliyokirimiwa.

Ikunji aliingia chumbani akiwa amechoka akili kuliko mwili. Akaenda moja kwa moja kujibwaga kitandani. Chumba hakikutofautiana sana na kile alichokikimbia, kwa ajili hiyo, tukio zima likaanza kurindima kichwani mwake. Dhana ilimganda kichwani kwamba, ni wahalifu tu ndiyo waliofungua chumba chake ili wakwapue mkoba. Alihisi kuna watu wameshajua kuwa amebeba dhahabu. Changamoto ni kwamba hakujua wamejuaje, kwani zaidi ya mkewe, pamoja na mzee Kizamba, mume wa shangazi yake, hakuwahi kumwambia mtu mwingine yeyote kuhusu safari yake ya kupeleka dhahabu Arusha.

Aliingia msalani akiwa na mkoba wa dhahabu kwapani. Safari hii alijilazimisha kuoga ili kuupumzisha mwili. Alipotoka akafungua runinga ili kupunguza mawazo. Kila idhaa aliyofungua haikumpa afua. Akaamua kuacha muziki ukiendelea kujiburudisha wenyewe. Alitamani kushika simu ili kuperuzi, lakini haikuwa na chaji. Na isivyo bahati, hakuwahi kuchukua chaja yake hotelini alikokimbia. Akabaki amejilaza chali kitandani akiendelea kuwaza hili na kuwazua lile. Usingizi usivyo na hiyana ukamchota.

Aliota amebebwa kwenye gari ya wagonjwa, akiwahishwa hospitalini baada ya kupigwa risasi na majambazi waliomvamia, ili kumwibia mkoba wa dhahabu. Aliyeongoza genge la majambazi waliomshambulia alikuwa ni Sudi Chotara. Na dereva wa gari la wagonjwa, aliyekuwa akihangaika kuokoa maisha yake ni Sebastian Mbegu. Alistaajabu mno. Iweje Sudi Chotara, ambaye ndiye tajiri yake mpya, amtumie majambazi kukwapua dhahabu zake mwenyewe? Halafu kwa vipi Sebastian Mbegu, ambaye ni adui yake mkubwa, awe ndiye dereva wa gari ya wagonjwa anayepambana kuokoa maisha yake?

Akiwa amelazwa kwenye machela, Ikunji alihisi maumivu makali ya kichwa, yaliyokuwa yakichagizwa na kelele za ving’ora vya gari hiyo ya wagonjwa.

“Zima hivyo ving’ora tafadhali,” Ikunji alimpigia kelele Sebastian.

“Bila ving’ora hatutopata nafasi ya kupenya kwenye foleni. Tunafanya hivi kwa ajili yako. Vumilia maumivu ya muda mfupi kwa ajili ya faraja ya muda mrefu,” Sebastian alijibu, akiendelea kukamatia usukani.

Sauti za ving’ora ziliendelea kupenya masikioni mwake. Kichwa kilizidi kumuuma mara dufu. Uzalendo ukamshinda. Akapiga kite kwa ghadhabu na kujiinua kwa nguvu kwenye machela. Nguvu aliyotumia kujiinua kwenye machela, ndiyo ilimnyanyua ghafla kitandani na kushituka toka usingizini.

Aliketi kitendani. Alijinyoosha mwili huku akitweta. Akaupapasa mkoba wake mchagoni. Kabla hajaitafakari ndoto aliyoota, aliduwaa macho yake yalipopiga kwenye saa ya ukutani. Ilikwishatimu saa kumi na mbili asubuhi. Siku ya pili jijini Arusha.

Ina maana nimepitiliza hadi asubuhi? alijiuliza kwa mshangao.

Akiwa ameketi kitandani ndipo alipogundua kuwa, sauti za ving’ora zilizomtaabisha usingizini, zilikuwa zikitoka runingani, ingawaje si kwenye gari ya wagonjwa kama alivyoota, bali kwenye magari ya polisi yaliyotanda nje ya jengo kubwa huku umati wa watu ukitapakaa mbele ya tepe za njano zilizofungwa na polisi, kuzunguka eneo lote la jengo hilo.

Ikunji alipikicha macho mara mbili, akihisi kulitambua jengo lililozungukwa na polisi runingani. Alipothibitisha hisia zake aliketi sawia, macho runingani, mikono mapajani. Ilikuwa ni White Rose Hotel. Hoteli ile ile alikokimbia usiku uliopita.

Baada ya hekaheka za maofisa wa polisi, walioonekana kupita huku na kule, kuchunguza hiki na kile, pamoja na kuzungumza hili na lile kupitia redio zao za upepo, hatimaye alionekana Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha, ACP Livinus Kamugisha, akithibitisha kutokea kwa tukio:
“…tulifika hapa mara baada ya kupigiwa simu na uongozi wa hoteli, ndipo tukakuta mwanaume mmoja ameuawa ndani ya chumba namba 225 kilichopo ghorofa ya pili.”

“Mungu wangu!” Ikunji alijitwisha mikono kichwani huku akisimama toka kitandani.

Chumba kilichotajwa ndicho alichokuwa amepanga na baadaye kukuta damu ikitiririka mlangoni. Kitendo cha mtu kukutwa ameuawa humo, kitamfanya kuwa mtuhumiwa namba moja. Ikunji alitulia kusikia sehemu ya mwisho ya maelezo ya Kamanda wa Polisi, yaliyourarua moyo wake mara elfu zaidi.

“…maiti imekwishatambuliwa. Ni mfanyabiashara wa madini, aliyefahamika kwa jina la Sudi Chotara.”

“No!” Ikunji alipayuka huku akisimama na kujipigapiga kichwani. “Sudi? Haiwezekani.”

Baada ya ACP Kamugisha kumaliza kuthibitisha tukio hilo, mtangazaji aliihitimisha taarifa ile, na vipindi vingine vikaendelea. Ikunji alijipigapiga kichwani akidhani yungali ndotoni.

Inawezekanaje? alijiuliza.

Bado hakuamini kila alichokiona na kukisikia. Kwamba mtu aliyemfuata jijini Arusha ndiye ameuawa, tena ndani ya chumba alichopanga yeye.

Ina maana ile damu iliyokuwa ikitiririka toka mle chumbani ilikuwa ni ya Sudi? aliendelea kuwaza.

Tukio zima likaanza kujirudia kichwani mwake.

***** NI NANI aliyemuua Sudi Chotara? Na iweje maiti yake ikutwe chumbani mwa Ikunji? Itakuwaje hatma ya Ikunji? Na vipi kuhusu Leila na Seba?

Tutaendelea na hadithi hii hapo kesho, ifikapo saa kumi na mbili jioni. Cha msingi hakikisha, unaLike, comment, na kuShare ili iwafikie wasomaji wengi zaidi.

Riwaya: Fumbo

Mtunzi: Maundu Mwingizi (Mwana balagha)
FB_IMG_1558102643837.jpeg


Sent using Jamii Forums mobile app
 
Kazi nzuri. Ila endelea na namba mbili kwenye uzi huu huu. Bila kufungua Uzi mwingine
 
FUMBO (03)

Ikunji alilala chali kitandani, mikono akiizungusha kisogoni. Alifanikiwa kupata chumba katika hoteli ya D&G baada ya kuwachomoka polisi. Jambo moja lilimdhihirikia bayana, kwamba imekwishajulikana kuwa yeye ndiye aliyepanga chumba ilimokutwa maiti ya Sudi Chotara. Makosa makubwa aliyoyakiri moyoni, ni kuandika taarifa zake halisi kwenye kitabu cha wageni hotelini, pamoja na kuendelea kutumia simu yake baada ya tukio lile.

Kuendelea kukimbia na kujificha kungemfanya atafisirike kuwa ni muuaji. Hivyo, alifikiria kujisalimisha polisi. Aliamini akielezea vizuri mkasa mzima angeweza kujinasua na kadhia ile. Lakini kila alipoyafikiria mapokezi ambayo angelipewa na polisi, kama mtuhumiwa wa mauaji, hamu yote ilimwisha. Alijitengezea taswira ya kitu cha kwanza ambacho polisi wangekifanya mara baada ya kumpata. Alijua isingelikuwa mahojiano ya mdomo, bali wangeanza na mchakato wa kumlainisha viungo kwa virungu na nyaya za umeme. Alijua ni lazima angelazimishwa kuutapika ukweli ambao hautambui. Aidha, alijua fika, kukosa kutapika walau chembe ya ukweli ambao polisi walitaraji kuusikia kutoka kwake, pasipo kujali endapo anao ama la, kungefanya viungo vyake vilemazwe badala ya kulainishwa. Hilo hakuwa tayari limfike.

Kwa kuwa alikwishafahamu, kwa namna yoyote ile, yeye ndiye mtuhumiwa namba moja, hivyo, ili kujinasua ilimbidi ahakikishe anakusanya kwanza walau dondoo chache kuhusu tukio hilo la mauaji, kabla ya kujikabidhi mikononi mwa pilisi.

Ni nani aliyemuua Sudi? Amemuua kwa maslahi gani? Kwa nini amuulie chumbani kwangu? Mtungo wa maswali ulizidi kujirefusha kichwani mwake.

Alisimama akijipigapiga kichwani. Alijaribu kila mbinu kuchangamsha kichwa ili kuchakata maswali yote. Mawazo yaliutafuna vilivyo ubongo wake, kiasi cha kupoteza mustawa wa utendaji kazi. Hakuna hata jibu moja lililompeleka kwenye ukweli. Kwa mara ya kwanza alihisi huenda kichwani mwake amebeba makamasi badala ya ubongo.

Je, inawezekana ilitokea tu kama sadfa? Kwamba wauaji hawakujua kuwa chumba walichokwenda kumwua Sudi Chotara, kilikuwa kimechukuliwa na mgeni wake? Kama sivyo, basi walipanga kuniangushia jumba bovu. Lakini je, walijuaje kuwa nitafikia chumba hicho? Ikunji alijiuliza.

Ikunji ni mpenzi mkubwa wa muziki, hususani wenye mdundo mzito kama hiphop. Lakini muziki aliopambana nao safari hii, mdundo wake ulitishia kumchana kifua.

Alitamani kumpigia simu mzee Kizamba kumjulisha kilichojiri baada ya kufanikiwa kuwakimbia polisi, lakini alihofia kutumia simu yake kwa kujua kwamba polisi wangejua mahala alipo kupitia simu hiyo. Hofu ya kuwasha simu, ikamkumbusha ujumbe aliotumiwa na namba mpya kmhusu mkewe. Aliielewa vema falsafa ile, kwamba mkewe ameshindwa kudhibiti nguo yake ya ndani. Maumivu ya kusalitiwa yaliubabua moyo wake mara dufu.

Je, nianze kumpigia Leila au nimtafute kwanza aliyenitumia huo ujumbe? alijiuliza.

Ukiwasha tu simu umejikamatisha! Indhari ilimpitikia kichwani mwake.
***

Sajini Kinabo alitembea taratibu kulielekea geti la hoteli ya White Rose, huku akiyasawiri mazingira yote kwa umakini mkubwa. Shughuli mbalimbali ziliendelea nje ya hoteli ingawaje hapakuwa na mtu aliyeonekana kutoka wala kuingia hotelini. Lakini mlango wa hoteli ulikuwa wazi. Kinabo akaingia.

“Hakuna huduma kaka,” msichana aliyekuwa ameketi kwenye kochi alisema.

Kinabo alipiga kite, akisema kwa mshangao, “Hivi duniani bado kuna wahudumu wa aina yako?”

Haraka msichana yule alishusha miguu sakafuni na kujitengeneza, akionesha kuhofishwa na kauli ile ambayo haukuelewa maana yake.

“Kwa nini?”

“Si wa karibu wala salamu.” Kinabo alijibu.

“Oh, nisamehe bure kaka yangu. Kichwa changu hakipo sawa kabisa leo.”

“Haya pole,” Kinabo alisema huku akiketi sofani, karibu na msichana yule. “Mi naitwa James. Nawe wanakuitaje?”

“Naitwa Maisara.”

“Oh, jina zuri sana japo mwenye jina ni mzuri zaidi ya jina lake.”

Maisara akashindwa kulizuia tabasamu lake.

Kinabo naye akatabasamu. “Sema hata ahsante basi, mrembo.”

“Haya asante.”

Kinabo aliyasanifu mazingira kwa haraka, lakini hakubaini kitu. Licha ya rabsha iliyotokea hotelini hapo, bado mazingira yalionekana nadhifu muda wote. Hapakuwa na dalili ya mtu mwingine mle ndani zaidi ya msichana huyo.

“HiI ndo hoteli yangu kila nifikapo Arusha, lakini sijawahi kukuona hata mara moja. Ni mfanyakazi mpya?”

“Hapana. Nina muda mrefu tu mbona.”

“Anha, basi yumkini tunapishana,” alijibu kwa bashasha kana kwamba wameshafunga urafiki, “Haya Mmari yuko wapi?”

“Mnafahamiana?”

“Ndo maana nikamuulizia.”

“Hayupo. Amechukuliwa na polisi tangu jana usiku.”

“Na polisi? Kunani tena?”

“Jana palitokea tukio la mauaji hapa.”

“My God! Wateja walifumaniana, au?”

Maisara alifunguka mkasa wote kama ambavyo naye alisimuliwa baada ya kuingia zamu hotelini asubuhi hiyo.

“Sasa kama aliyeuawa hakuonekana kuingia hotelini, iweje maiti yake ikutwe ndani?” Kinabo alichagua kudadisi eneo hilo, baada ya Maisara kuhitimisha simulizi.

“Ya kuacha tu mwenzangu,” alijibu huku akizungusha macho na kubetua mdomo. “Mmari akiamua kuingiza mtu utajua? Hao wanawake zake tu analala nao humu na hakuna anayejua wanakopitia.”

“Mmari naye aache ukware sasa, umri unasonga,” Kinabo alisema huku akicheka kwa sauti. “Sasa kama huwa hawapitishii mlango huu, huwa anawaingiza kwa ungo?”

Maisara akacheka akijibu, “Ndo maana nikakwambia ya kuacha tu.”

“Aisee poleni sana,” Kinabo alisema na kusimama. “Basi acha nikatafute chumba sehemu nyingine.”

“Haya. Karibu tena siku nyingine.”

Kinabo alitoa pochi katika mfuko wa nyuma, akafungua na kutoa noti mbili za shilingi elfu kumi kumi. Akampatia Maisara. “Haya utakunywa soda basi.”

Soda ya elfu ishirini? Maisara alijiuliza huku akishangaa. Lakini hakuzikataa.

“Ubarikiwe sana.”

“Kama hautojali, jioni nitarudi kukutembelea. Au hata kesho panapo majaaliwa,” Kinabo alisema huku akirejesha pochi mfukoni.

“Karibu,” Maisara alijibu huku akizitia mfukoni pesa zake. “Japo sijui kama utatukuta. Mwenye hoteli anaingia leo jioni toka Dar, huenda tukafunga kwa muda.”

“Oops! Kwa hiyo sitakuona tena?”

Maisara akatabasamu akisema, “Jamani simu si zipo.”

Ndicho nilichokuwa nasubiri, Kinabo aliwaza. Akatoa simu huku akimuuliza, “Unatumia mtandao gani?”

Akautaja. Kisha akataja na namba yake ya simu.

Kinabo alitoka hotelini huku akimalizia kuhifadhi namba simuni. Moja kwa moja akaenda kusimama upande wa pili wa barabara, mkabala na hoteli hiyo akiangaza huku na kule kutafuta usafiri.

“Unahitaji bodaboda, bosi?” Sauti ya kijana aliyetokea pembezoni mwa kichochoro ilimzindua Kinabo.

“Ndio, lakini sioni bodaboda hata moja hapa.”

“Njoo huku bosi. Bodaboda haziwezi kupaki hapo leo.”

Kinabo alimfuata hadi mbele kidogo. Kijana aliichomoa pikipiki yake uchochoroni na kuiwasha.

“Mbona unaificha mbali huku? Au hauna vibali mzee?” Kinabo alifanya kutania baada ya kupanda.

“Si bora ingekuwa vibali tu,” kijana alijibu, akivaa kofia. “Tunaelekea wapi bosi?”

“Sanawari Petrol Station, karibu na Kituo cha Polisi.”

Dereva akakitia moto chombo, safari ikanza.

“Kuna mtu ameuawa mle hotelini – White Rose. Sasa kama ujuavyo tena kamatakamata ya polisi, ndo maana tunafanya kazi kiujanja ujanja.”

“Nilisikia kuna mtu ameuawa ila sikujua kama ni hoteli hiyo. Ilikuwaje?”

“Aah hata najua basi! Mi nilikuwa nimepaki kijiweni kama kawaida, akatokea abiria mmoja anataka kupelekwa sehemu yenye hoteli nzuri, nikampeleka Sanawari.”

Kwa nini umpeleke mbali ilhali hapo karibu kuna hoteli? Kinabo alitamani kumtupia swali hilo, badala yake akasema. “Duh bodaboda mnawaza pesa tu! Yaani hapo jirani kuna hoteli lakini ukaona umpeleke mbali ili upate pesa.”

“Hapana. Mi siko hivyo. Nilimwonesha White Rose Hotel, akakataa, ndo nikampeleka Nyati Inn, Sanawari. Niliporudi sasa ndo nikakuta umati umefurika.”

Kwanini akatae hoteli iliyo karibu? Kinabo aliishia kugunia tumboni. Ilikuwa ni kama bahati ya mtende kuota jangwani au mbuzi kufia kwa muuza supu.

“Aisee, binaadamu tumekuwa kama wanyama,” Kinabo alijaribu kubadili mada. “Basi ukute alifumaniwa na mke wa mtu.”

“Sudi mtu muungwana, hawezi kufanya uchafu huo.”

“Hakuna muungwana kwenye mapenzi. Kila mtu ana udhaifu wake.”

“Na hata kama angeamua kufanya hivyo, kwa utajiri alionao, asingeweza kupeleka mwanamke kwenye hoteli ya hadhi ya chini kama ile.”

Mazungumzo yao yalishamiri hadi walipofika mwisho wa safari. Kinabo alimtaka asimame pembeni mwa Kituo cha Polisi. Akatii. Alipoegesha tu, Kitabo aliteremka na kwenda kusimama mbele.

“Hivi nikihitaji baadaye uniijie tena utaweza?”

“Ndo kazi yangu bosi.”

“Poa.” Kinabo alitoa pesa mfukono na kulipa nauli yake. “Basi nipe namba yako ya simu. Nikiwa tayari nitakupigia.”

Dereva bodaboda alipokea nauli huku akitaja namba zake za simu. “Jina andika Isaka.”

Baada ya Isaka kuondoka. Sajini Kinabo aliita bodaboda nyingine impeleke Nyati Inn Hotel. Alikwishamtilia shaka huyo kijana aliyegoma kuchukua chumba White Rose, na kutaka apelekwe Nyati Inn.
***

Ikunji alisimama mbele ya meza ya mapokezi akiwa amekwishabadili mavazi. Alivalia suruali ya kadeti na sweta la kijivu juu ya fulana nyeusi. Kichwani alivaa kapelo nyeusi yenye nembo nyeupe. Akakabidhi funguo kaunta na kutoka.

Alidhamiria kujaribu kufanya uchunguzi wa kifo cha Sudi. Kwa kuwa alitaka kucheza gizani, ilimpasa aanze kwanza kujifunza kufumba macho. Katika nukta ndogondogo zilizokuwapo mbele yake, aliamua kuanzia kulekule Nyati Inn Hotel. Ingawaje uwezekano wa kukamatwa ulikuwa mkubwa mno, lakini ili kushinda vita inayomkabili ilimbidi kuhatarisha usalama wake. Akachukua bodaboda nje ya hoteli na kuondoka. Kiasi cha dakika kumi, alikwishawasili maeneo ya Nyati Inn Hotel.

Badala ya kwenda kuingia hotelini, alikwenda kwenye duka kubwa la rejareja mkabala na hoteli. Akanunua sigara na kuiwasha papo hapo. Alipamaliza, akasogea pembezoni mwa duka na kusimama. Macho yalitazama mlango wa kuingilia hotelini wakati akipuliza angani moshi mweupe. Kuyaona tena mazingira ya hoteli ile, kukamrejeshea tena kumbukumbu za namna alivyonusurika kunaswa na polisi. Macho yakiwa bado yameganda hotelini, aliiona teksi nyeupe ikiwasili na kwenda kuegesha mbele ya hoteli. Kwa dakika tano, hakuna aliyeshuka.

Ni mapolisi? alijiuliza. Chambilecho wahenga, mguu ulioumwa na nyoka ugusapo jani hushituka. Alikwishanusurika kukamatwa na polisi, hivyo, kitu chochote chenye walakini kilimfanya azidishe umakini. Alitamani kuondoka kabla hajatimiza kilichompeleka. Kabla hajakata shauri kuondoka, akamwona Nyakanga akitoka hotelini na kuifuata teksi iliposimama.

Kinabo aliwasili eneo hilo wakati macho ya Ikunji yakiendelea kumakinika na Nyakanga. Kama ilivyokuwa kwa Ikunji, Kinabo naye hakufanya papara kwenda kuingia hotelini. Alisimama nje akiyasawiri mazingira. Kisha naye akelekea dukani, alikokuwa amesimama Ikunji. Ndilo eneo pekee palipokuwa na urahisi wa kusimama pasi na kuvutia nadhari za watu.

Ikunji alichomoa sigara mdomoni. Akautawanya moshi angani. Bado macho yake yaliganda kwenye teksi. Hakuweza kumwona mtu aliyekuwa akiongea na Nyakanga kwa sababu aliketi upande wa pili. Alipojaribu kumkazia macho dereva, akahisi kumtambua.

Nilimwona wapi? aliwaza. Kumbukumbu zilimgomea, lakini sura ilimjia.

Baada ya sekunde kadhaa za kuvuta kumbukumbu, hatimaye akamkumbuka. Alihisi vinyweleo vikitutumka juu ya ngozi yake. Kabla hajajua cha kufanya alihisi kuguswa begani. Machale yakamcheza. Alipogeuka, akakutanisha macho na Kinabo. Aliganda akimtazama bila kusema neno.
Kinabo alikuwa ametoa pakiti ya sigara kwenye mfuko wa shati. Akachomoa sigara moja na kuipachika mdomoni, kisha akapiga kidole gumba na cha kati, akiashiria kuomba sigara ya Ikunji ili awashie yake. Ikunji alitii mara moja.

“Mambo vipi?” Kinabo alimsalimu huku akipokea sigara.

“Poa poa.”

Baada ya kuwasha, alimrejeshea sigara na kumuuliza, “Ni mwenyeji mitaa hii?”

Ikunji alipokea sigara na kujibu, “Hapana.”

Wakati anamrejeshea sigara yake, Kinabo aligundua mikono ya Ikunji inatetemeka. Akamkazia macho usoni. Ikunji akakwepesha na kugeuka upande wa pili.

Teksi iliyosimama nje ya hoteli ilianza kuondoka taratibu. Akaonekana Nyakanga akirejea hotelini. Ikunji hakufanya ajizi. Haraka akaondoka dukani. Kinabo aliendelea kumtazama akielekea barabarani. Alishindwa kuelewa endapo alikuwa akitetemeka kwa hofu ya uhalifu au ni maradhi. Kinabo hakumtambua Ikunji, kwamba ndiye sababu ya yeye kuwapo pale.

Ikunji alisimamisha bodaboda iliyokuwa akipita barabarani na kupanda. “Tunaifuata teksi ile.”

“Inakwenda wapi?” dereva aliuliza huku akiingiza gia na kuondoa pikipiki.

“Popote inapokwenda.”

Njia nzima, Ikunji alihakikisha teksi haiwapotei machoni. Kauli ya mzee Kizamba kuwa, ni muhimu kumpata dereva aliyembeba siku alipowasili Arusha, ilirindima kichwani mwake. Alipanga kitokeo cha hapo White Rose, ndipo aelekee stendi kumsaka dereva huyo, lakini kwa bahati akamwona ndani ya teksi hiyo iliyomfuata Nyakanga hotelini.

Takribani dakika ishirini, teksi ilisimama nje ya nyumba moja ya matofari ya kuchoma. Maeneo ya Daraja Mbili. Ikunji na bodaboda wake, nao walisimama hatua kadhaa nyuma, mbali kidogo na teksi hiyo. Ikunji alichomoa kalamu na karatasi kwenye mkoba akanakili namba ya teksi kwenye sahani ya njano; tofauti na kanuni ya teksi kuwa na sahani nyeupe za namba.

Haikuchukua muda, abiria aliyekuwa ameketi pembezoni mwa dereva, aliyekuwa akiongea na Nyakanga kule hotelini, alisuasua kuteremka toka kwenye teksi kwa sababu ya unene. Alipoteremka, akabaki amesimama huku ameegemea mlango wa teksi. Alionekana kuzungumza mambo kadhaa kwa msisitizo, akiirusha mikono yake huku na kule. Pamoja na kwamba masikio ya Ikunji yasingaliweza kunasa chochote kwa umbali ule, walakini macho yake yalivuta vizuri taswira ya mtu yule. Alihisi kuwahi kumwona mahali. Alipotuliza zaidi macho akamtambua. Ni yule bonge aliyekuwa akimjibu kwa dharau na kedi, nje ya hoteli ya White Rose, kwenye mgahawa wa chakula.

Kengele ya hatari ilianza tena kurindima kichwani mwake.

Kitendo cha kumwona dereva wa teksi, aliyembeba stendi siku alipowasili na kumpeleka kwenye hoteli iliyomletea, akiwa ameambatana na mhudumu wa mgahawa wa hoteli ile ile, kulimzidishia tashwishi ya kudadisi mualaka baina yao. Alitamani kuwachunguza zaidi, lakini alielemewa na wasiwasi kiasi cha kupoteza mhimili wa kujiamini. Mgogoro mkubwa baina ya dhamira na hisia uliibuka moyoni mwake. Hakujua kipi sahihi kati ya kurudi nyuma na kuondoka au kusonga mbele na kuchunguza mengi zaidi. Alihofia kuufungua mlango asiojua namna ya kuufunga.
***

Baada ya kumaliza kuvuta sigara, Kinabo alivuka barabara na kwenda kuingia hotelini. Simon, aliyekuwa ameketi akitazama runinga alimlaki kama ilivyo desturi kwa wateja wengine.

Baada ya kusabahiana, Kinabo alimwonesha kitambulisho chake, akisema, “Naitwa Kinabo. Sajenti James Kinabo. Natokea Kituo Kikuu cha Polisi. Nahitaji kuangalia orodha ya wageni waliochukua vyumba juzi usiku hotelini kwako.”

Kumbukumbu za Simon zilirudi kwa afande Kisigino. Tayari alikwishamaizi kuwa uwepo wa Kinabo hotelini hapo, ni mwendelezo wa upelelezi wa tukio lile lile. Alivuta kitabu cha wageni kabla ya kuhoji zaidi. Akafunua ukurasa wa siku husika na kumkabidhi Kinabo.

Kati ya wateja watano waliochukua vyumba usiku, Kinabo alivutiwa na mmojawapo. “Naweza kumwona huyu Kaisi?”

“Hayupo,” Simon alijibu, akilaza mikono yake mezani. “Lakini pia haitwi Kaisi.”

Sajini Kinabo alifunika daftari na kumtazama Simon usoni. “Unamaanisha nini?”

Simon alianza kusimulia mkasa ulioibuka baada ya afande Kisigino kufika hotelini hapo, kumtafuta mtu ambaye ilikuja kugundulika kuwa ameghushi jina. Kinabo alipigwa butwaa, akijiuliza endapo mtu huyo anaweza kuwa ndiye mhusika wa mauaji ya Sudi.

“Unalikumbuka jina halisi la huyo kijana – ulilotajiwa na afande Kisigino?”

Kabla Simon hajajibu, Nyakanga alifika kaunta akijitupia mtandio kichwani. Akasimama pembezoni mwa Kinabo. “Nafika sokoni mara moja.”

“Sawa dada,” Simon alijibu, kisha akarudisha macho kwa Kinabo na kujibu, “Hapana. Sikulikariri.”

“Unaweza kunielezea mwonekano wake?”

“Ni mrefu, mweupe kiasi, nyusi zake ni nyeusi sana, na ndevu nyingi mashavuni. Pia, ana kitu kama kidoti cheusi karibu ya pua.”

Kinabo alihisi damu ikimsisimka. Sifa zote alizotajiwa zilimranda mtu aliyekuwa amesimama naye mbele ya duka, mkabala na hoteli hiyo, muda mfupi kabla hajaingia hotelini humo. Alikumbuka alivyomkaribia na kumgusa begani. Walivyotazamana. Na namna alivyoondoka ghafla. Suala la kwanini kijana yule alikuwa akitetemeka mikono, lilipata jibu kichwani mwake.
***

Ikunji alirudi tena na bodaboda maeneo yale yale, mbele ya duka la rejareja, mkabala na Nyati Inn Hotel. Safari hii hakutaka kusimama dukani, aliamua kwenda kuingia moja kwa moja hotelini. Hakujua kuwa mtu aliyemwazima sigara, ambaye ni ofisa wa jeshi la polisi, alikuwamo ndani ya hoteli akipeleleza kesi inayomhusu yeye. Alivuka barabara kwa uangalifu, moja kwa moja akielekea hotelini.

Kiu yake kubwa hapo mwanzo, ilikuwa ni kukutana na Nyakanga ili kumdodosa hali ilivyokuwa baada ya kufanikiwa kuwachomoka polisi. Sasa, kitendo cha kumwona Nyakanga akiongea na yule bonge, mhudumu wa mgahawa wa White Rose Hotel, tena akiwa amebebwa na dereva teksi aliyepanga kumtafuta, kilimzidishia shauku na sababu ya kuonana naye.

Kama mbwa aliyenusa mtara wa windo, alipoinua macho alimwona Nyakanga akitoka hotelini kwa madaha, akijitupia huku na kule mithili ya Nguruwe aliyekanyaga kaa la moto. Akiwa amekwishafika katikati ya barabara, Ikunji alipunguza mwendo asijuwe endapo amuwahi papo hapo nje ya hoteli, au asubiri kuona uelekeo wake kisha amfuate kabla hajafika mbali. Hakufanya papara ya kumwita wala haraka ya kumfikia. Alimwacha afike mbali kidogo ndipo akaanza kumfuata kwa nyuma.

Alipomkaribia akamwita, “Dada!”

Nyakanga aligeuka na kukutanisha macho na Ikunji. Alimkumbuka mara moja. Akabutwaika kumwona tena maeneo yale.

“Wewe! Umefata nini tena?”

“Nimekufuata wewe, dada,” Ikunji alijibu, akiangaza huku na kule. “Nimekuja kukushukuru.”

Nyakanga alimshika mkono na kumvutia pembeni ya barabara. Wakaenda kusimama kwenye uchochoro wa nyumba iliyokuwa karibu na kona ya barabara.

“Haya vipi mwenzangu?”

“Dada nakushukuru sana. Una moyo wa ajabu mno,” Ikunji alisema, akimtazama Nyakanga kwa jicho la huruma. “Nilijiapiza ni lazima nirudi kukushukuru. Nimefika muda mrefu hotelini kwenu, tangu wakati ule ulipotoka kuongea na mtu kwenye teksi, nikashindwa kukusemesha.”

“Aah muda ule nilitoka kuongea na Mufuruki, shemeji yako yule ila tumegombana, basi kila mara anajipitisha kuomba msamaha.” Nyakanga alianza kufungulia maneno kama ilivyo desturi yake. “Lakini usimwone bonge vile – bahili kama nini.”

“Sikumwona. Nilikuwa nimesimama upande ule wa dukani,” Ikunji alijibu, akionesha kwa mkono mwelekeo wa alikokuwa amesimama. “Nilimwona tu yule dereva teksi mwenye mzuzu.”

“Aah, ni Kibwana,” Nyakanga alijibu na kucheka, “Siyo dereva teksi yule.”

“Kumbe nani?”

Nyakanga alipigika kimya kama anayetafuta cha kujibu. “Aah wajanja wa mjini tu. Hebu kwanza niambie, una kesi gani?”

“Hata ni kesi basi, dada,” Ikunji alijibu, akiuzungusha mkoba wake kifuani. Akafungua zipu ya kati kumwonesha kilichomo.

Macho yalimtoka Nyakanga baada ya kukutana na dhahabu kwenye mkoba.

“Kumbe unafanya biashara ya madini? Uko vizuri mdogo wangu. Kwa hiyo wanakutaka nini? Kukudhulumu au? Mapolisi wa siku hizi njaa tupu – basi mwanzo nilidhani ni hii kamatakamata ya sakata la Sudi Chotara.”

“Hivi kwani hiyo issue ya Sudi nayo inaendeleaje?”

“Nasikia waliomuua, walitaka kumwangushia jumba bovu kijana aliyekodi chumba pale hotelini, lakini akawahi kukimbia.”

“Ina maana aliyekodi chumba siye muuaji?”

“Aah, mtu hawezi kuchukua chumba, akaandika majina yake halisi, kisha akaua humo humo chumbani na kukimbia,” Nyakanga alijibu.

“Huo kweli utata. Lakini kama ni kweli ameua, Polisi hawatamwacha kirahisi. Watamwandama kila kona hadi watampata.”

“Polisi hawawezi kumpata. Nasikia waliocheza hiyo dili waliwahi kuficha Kitabu cha Wageni kabla polisi hawajafika.”

“Kwa nini wakifiche sasa?” Ikunji alitupa tena ndoano.

“Nadhani wanahofia endapo polisi wangekipata hicho kitabu, wangemsaka hadi kumpata. Na endapo akihojiwa, ukweli utabainika kuwa si yeye aliyeua. Hapo wanajua itapelekea msako mkali dhidi ya wauaji halisi. Na kama hao wahusika wakiwahi kumpata mapema huyo kijana, watauua kupoteza ushahidi. Baadaye utashangaa kusikia ni wafuasi wa Sudi ndio wamelipa kisasi.”

Ikunji alihisi maini yakimtetemeka tumboni. Akasema, “Mmh! Kama muvi vile. Lakini dada, stori za mitaani si za kuamini sana. Si ajabu huyo huyo aliyepanga chumba, baada ya kumuua Sudi alitoka chumbani na kukibeba kitabu cha wageni na kutoweka nacho.”

“Kama alikuwa na mpango wa kumuua, kwanini sasa aliandika majina yake halisi halafu baadaye ajitaabishe tena kukiiba kitabu?”

Ikunji alitafakari hoja hiyo na kuibirua tena, “Yumkini hakupanga kuua, pengine ilitokea tu baada ya kuona pesa tamaa ikamjaa. Au pengine walitaka kudhulumiana mali ndipo kijana akamwahi tajiri.”

“Kama hivyo ndivyo, alipotoka chumbani baada ya kuua, na kwenda kaunta kubeba kitabu cha wageni, muda huo mhudumu wa mapokezi alikuwa anacheza mahepe?” Nyakanga alibetua mdomo upande kwa dhihaka. “Sasa kwa taarifa yako, watu wanajua mpaka kilipo hicho kitabu.”

Ikunji alihisi mwili umekufa ganzi. Akageuka huku na kule kuhakiki usalama. “Kwani dada hatuwezipata sehemu nzuri ya chakula, tupige stori?”

“Mmh, kwa leo sidhani. Hapa nimetoroka tu kidogo kazini, nakwenda sokoni fasta kuhemea chakula cha usiku. Leo nitaenda kulala kwa shemeji yako.”

“Sasa itakuwaje? Nilitaka baada ya stori mbili tatu nikupe na asante yako.”

Kusikia kwenda kupewa asante yake, Nyakanga akabadili maamuzi. “Mmh…inawezekana, lakini sijui kama Simon atakubali nitoke mapema. Ila nitaongea naye. Tunaweza kukutana pale King Garden? Wana vyakula pale si vya nchi hii; kuku wa kienyeji, sekela, mturo kwa ndizi, makange na k–”

“Okay,” Ikunji alimkatisha, “saa ngapi?”

“Saa moja kamili jioni,” alijibu na kutoa simu yake mfukoni. “Nipe namba yako nikifika nikupigie.”

“Namba si ndo ile wanaifuatilia. Niliitoa kwenye simu, na sijasili nyingine. Vitambulisho vyangu viko Dar.”

“Sasa itakuaje?”

“We huna kitambulisho unisajilie kwa muda tu?”

“Mmh, inaweza kuniletea matatizo endapo itatumika kufanya uhalifu.”

“Ndo maana nimesema kwa muda tu. Nitakaporejea Dar nitakukabidhi namba yako. Au unaweza hata kuirenew.”

Baada ya ushawishi wa Ikunji, Nyakanga hakuona sababu ya kupoteza miadi na mtu anayehitaji kwenda kumpa bahshishi, kisa namba ya simu tu.
***

Kinabo aliondoka kaunta na kwenda kusimama nje ya mlango wa hoteli. Akatupa macho upande wa pili wa barabara, kule dukani alikokutana na Ikunji. Hapakuonekana na mtu yeyote aliyesimama. Akawa anatazama eneo walilokuwa wamesimama, akakumbuka namna Ikunji alivyokuwa amemakinika na teksi iliyokuwa imeegesha mbele ya hoteli. Ikawa kama anamwona tena namna alivyowahi kupanda bodaboda baada ya ile teksi kuondoka. Japo hakuwa amemjua jina, lakini alikiri kuwa ndiye mtuhumiwa anayemsaka. Akarudi kaunta.

“Je, afande Kisigino alikwambia ni kwa nini anataka kumkamata?”

“Hakuniambia,” Simon alijibu.

“Na huyu dada mnene aliyetoka hapa ni nani?

“Nyakanga?” Simon aliuliza, kabla hajajibiwa akaendelea, “ni mhudumu wetu wa usafi.”

“Kuna muda alitoka nje kuongea na bwana mmoja kwenye teksi, ni nani yule?”

“Aah yule bonge? Anaitwa Mufuruki.”

“Anatokea wapi?”

“Ana mgahawa wa chakula pale White Rose, Soweto.”

Taa nyekundu ilianza kumulika kichwani mwa Kinabo. White Rose ndiko yalikotokea mauaji ya Sudi Chotara. Kitendo cha kumwona mmiliki wa mgahawa uliopo eneo la tukio, akiwasiliana kwa karibu na mhudumu wa usafi katika hoteli ambayo yawezekana ndiko mtuhumiwa alilala, kilimsisimua akili na kumchachafya ubongo. Taharuki ilimjaa kiasi kwamba alihisi chafya inataka kumtokea masikioni.

“Ni nani yake?” Kinabo aliuliza.

“Ni bwana’ake. Ila nasikia wametengana, sina hakika sana.”

“Kipindi afande Kisigino alipowasili, huyo dada alikuwa wapi?”

Simon alifumba macho na kuinua kichwa juu akitafakari. Alipofumbua akasema, “Nakumbuka kama alikuwa akideki hapo mbele.”

“Na wakati huyo kijana aliporudi hotelini, Nyakanga alikuwa wapi?”

“Sikumbuki vizuri. Ila baada ya kuwa tumemkosa chumbani, tuliporudi hapa tulimkuta akipanga magazeti hapo mezani.”

Kinabo alishusha pumzi. Akabaki akimtazama Simon ilhali mawazo yake yakisafiri kumfuata Nyakanga.

“Amesema anakwenda wapi?”

“Nani – Nyakanga? Nadhani sokoni.”

Kinabo alitoka bila kuaga. Akafuata njia aliyoelekea Nyakanga.

*****ENHEE MAMBO YANANOGA SASA. Kinabo amemshamhisi Nyakanga kumnusuru Ikunji. Je, atafanikiwa kumpata? Na atampata akiwa peke yake au atamfuma akiwa na Ikunji? Ni yepi mahusiano ya Mufuruki (tumbotumbo) na dereva teksi aliyembeba Ikunji? Kuna siri gani hapa katikati?
 
Back
Top Bottom