From Mo's Blog: Exclusive Interview With January Makamba

Selemani

JF-Expert Member
Aug 26, 2006
947
292
Tuanze kwa kukushukuru kwa kukubali kuzungumza na blog yetu. Karibu sana!

Nashukuru kwa fursa hii. Hii ni mara yangu ya kwanza kabisa kufanya interview. Lakini nimekubali kufanya hii kwa sababu tatu:

1. Mo ni rafiki yangu na nimefurahi kwamba ameamua kuanzisha blog. Aliponieleza nia yake hii miezi kadhaa iliyopita, niliahidi kumsapoti kwa njia yoyote ile . Sasa kwa kuwa amesisitiza sana kwamba njia ya kumsapoti ni kwa mimi kufanya hii interview, baada ya mimi kusita sana, nikaona nitimize ahadi yangu, lakini nikiwa bado naamini kwamba sijafika mahali pa mimi kustahili interview kuhusu maisha yangu.

2. Nimefurahi amekubali ombi langu la kutozungumzia masuala ya kisera, ya Kiserikali au yanayohusiana na undani wa kazi ninayoifanya sasa. In essence, interview hii ni deliberately biographical.

3. Nilidhani ni muhimu wengi wetu, hasa vijana, tukaonyesha imani na njia hii mpya ya kupashana habari (blog), hata kama ni kwa kufanya mambo ambayo hatukuwahi kuyafanya huko nyuma kudhihirisha kwamba tunaiheshimu na kuipa umuhimu medium hii mpya.

Tungeanza na wewe kutupa historia yako (Elimu, Kazi, Maisha kwa ujumla):

Nilizaliwa tarehe 28 Januari 1974. Nalipenda sana jina langu kwasababu mara nyingi ninapojitambulisha kwa watu, automatically linaanzisha mazungumzo. Mara nyingi huulizwa kama nilizaliwa mwezi Januari ndio maana nikapewa jina hilo. Ukweli ni kwamba hiyo sio sababu per se. Sababu kubwa ni kwamba, wakati nazaliwa, Mzee wangu alikuwa na rafiki yake mkubwa aliyempenda sana aliyeitwa Januari. Akaamua kunipa jina lake kwa mapenzi yake kwa rafiki yake. Ilikuwa ni coincedence tu kwamba nilizaliwa mwezi wa kwanza. Lakini jina ambalo Babu yangu mzaa baba alinipa na alipenda kuniita kabla hajafariki mwaka 1984 ni Rajab, ambalo ni jina lake yeye. Kwahiyo hadi leo, kijijini kwetu Mahezangulu, Lushoto, hasa kwa wale wazee wa kule, na hata kwa bibi yangu, najulikana kama Rajab.

Nimesoma kwenye shule mbalimbali za msingi katika mikoa mbalimbali nchini, kadri wazazi wangu walivyohama kutoka kituo kimoja cha kazi kwenda kingine. Nilianzia Monduli mwaka 1981. Mwaka 1983, nikapelekewa kukaa na bibi mzaa mama kijijini Kituntu, karibu na Kyaka, Bukoba Vijijini. Mama yangu kwao amezaliwa peke yake, kwahiyo bibi alihitaji mjukuu wa kukaa naye kumsaidia. Ndio nikatolewa kafara. Hahahaha! Kwahiyo darasa la tatu, la nne na la tano, nimesoma kijijini. Siwezi kusahau maisha yale: asubuhi ni kupiga umande literally kwenda shule umbali wa kama kilomita nne na nusu hivi kutoka nyumbani, ukirudi saa tisa ni kwenda kuchunga mbuzi, ukisharudisha mbuzi zizini saa kumi na mbili jioni ni kwenda kuchota maji mtoni, usiku kazi ni kumsaidia bibi kuuza pombe ya ndizi inayoitwa lubisi (bibi alikuwa na kilabu maarufu pale kijijini).

Samahani hapa nime-digress kidogo kwa kukumbuka na kuelezea zaidi kipindi hiki. Lakini experience hii ni sehemu ya mimi. Siku hizi NGOs zinayaita haya “mazingira hatarishi”, lakini watoto wengi vijijini ndio maisha yao ya kila siku. Some make it, through pure luck or strength of character, some don’t.

Anyway, nilirudi kukaa na wazazi wangu tena wakiwa Lushoto kwahiyo nikasoma darasa la sita pale, Shule ya Msingi Kitopeni, na kwenda kumalizia darasa la saba shule ya Msingi Masiwani Tanga Mjini. Hapa Tanga Mjini niliingia na kusoma madras which was quite rewarding ingawa sikumaliza msahafu. Pamoja na kuhamahama, na dhahama za maisha ya kijijini, I have always done well in school. Sikumbuki kama nilishawahi kushuka chini ya nafasi ya nne.

Form one nilisoma Handeni Secondary School, hii ilikuwa ni shule mpya, sisi tulikuwa Form One ya pili – kulikuwa hakuna walimu, madawati, maabara, n.k. Form Two hadi Form Four nikasoma Galanos, Tanga Mjini. Wakati nikiwa Form Three nilichaguliwa Deputy Head Prefect pale Galanos. Form Five na Six nikawa Forest Hill Secondary School, Morogoro, ambapo siku ya graduation nilitunikiwa cheti cha Overall Best Student.

Anyway, wakati nasuburi kwenda university, nikaenda kutafuta kazi kwenye kambi za wakimbizi Kibondo na Kasulu mkoani Kigoma. Nikafanikiwa Kasulu. Ukiacha maisha ya kijijini na bibi, this was another rewarding experience kwenye maisha yangu. Nilipata responsibilities kubwa kadri muda ulivyoenda, hadi kufikia ngazi ya Assistant Camp Manager kwenye kambi ya Mtabila Extension au Mtabila II, ambayo literally niliianzisha mimi (baada ya kuwa Serikali imetoa eneo) from the scratch kwa maana ya kusimamia ujenzi wa infrastructure za kambi na kugawa plots kwa wakimbizi. Kwenye kazi hii ndipo kwa mara ya kwanza nilipokutana na kuanza ku-engage na kujenga urafiki na watu wa mataifa mbalimbali waliokuwa expatriates kwenye camps. Muda wa kwenda Chuo ulivyofika, sikwenda kwani nilinogewa na kazi, mwaka uliofuatia sikwenda tena kwani nilipata responsibilities kubwa zaidi kambini and I was making and saving good money.

Eventually nikapata Chuo Marekani. Nilianza Boston baadaye nikajiunga na St. John’s University, Minnesota. Hiki ni Chuo cha Wakatoliki Wabenedicto kilichokuwa katikati ya pori na lakes, a very beautiful and quiet place, katikati ya Jimbo la Minnesota. Pale, degree niliyochukua ni BSc in Peace and Conflict Studies. Niliamua kusoma hii kozi kutokana na experience yangu kwenya makambi ya wakimbizi. Nilitaka kuelewa ni kwa namna gani tunaweza kuzuia watu wasikimbie kabisa nchi zao, kwani maisha ya ukimbizi, kwa nilivyoyaona, ni ya udhalilishaji mkubwa sana na yanaondoa dignity ya mtu.

Wakati nikiwa St. John’s University, nilirudi tena kufanya research yangu na UNHCR kwenye makambi ya wakimbizi Kasulu na Kibondo lakini pia kwenye way stations ndani ya Burundi na DRC.

Baada ya kumaliza St. John’s, nikapata research assistantship kwenye ofisi ya Rais wa zamani wa Marekani, Mzee Jimmy Carter, Carter Presidential Centre, kule Atlanta, Georgia. Kazi hiyo ilinipeleka hadi kufanya kazi Sierra Leone, ambako pia nilijifunza mengi. Pia Atlanta ndiko nilikofanikiwa kukutana na mke wangu mpendwa, Mona, ambaye mwakani itakuwa miaka kumi tangu tujuane, na ambaye, pamoja naye, tuna mtoto mmoja wa kike wa miaka mitatu na nusu.

Baada ya Carter Center, nikajiunga na George Mason University, iliyoko maeneo ya Fairax, Washington DC metro area, kusoma Masters kwenye fani ile ile ya diplomasia na usuluhishi wa migogoro. Nilikuwa a very active graduate student kwa maana ya kushiriki mijadala na professional and advocacy associations mbalimbali pale DC. I created a vast network of friendships in DC ambayo hadi leo nafaidika nayo. Nikiwa graduate school, nilipata fursa ya kufanya internship Wizara ya Mambo ya Nje.

Baada ya kumaliza graduate school nikaomba kazi Serikalini na kuajiriwa na Wizara ya Mambo ya Nje kama Afisa wa Mambo ya Nje Daraja la Pili (Foreign Service Officer II). Nikiwa Wizara ya Mambo ya Nje, nilipata fursa ya kufanya kazi kwa karibu na Waziri wetu wakati ule (Mhe. Kikwete), hasa kwenye harakati za kutafuta suluhu ya mambo ya Burundi na DRC. Kwahiyo, wakati alipoamua kugombea Urais, akaniomba nichukue likizo isiyo na malipo Serikalini nisaidie kuwa errand boy kwenye kampeni yake, ku-organise makaratasi na notes zake, na kuchangia hapa na pale kwenye tafakuri za kuendesha na ku-organise kampeni yake wakati ule. Tulifanikiwa kufanya mambo mengi mapya na ya kisasa kwenye kampeni ile (including TV campaign ads kwa mara ya kwanza). Nilishukuru sana kupata fursa ya kuzunguka Mikoa yote na Wilaya zote nchini, kwa kweli kila kona ya nchi, kwa njia ya barabara na kujua na kujuana na watu na kujua kwa kina changamoto na fursa za maendeleo katika maeneo yote. Mhe. Kikwete alipofanikiwa kuchaguliwa, akaniteua nije kumsaidia hapa Ikulu na hapa ndipo nilipo hadi leo.

Kazi hii ni ya heshima kubwa sana na ni muhimu kui-approach with humility. In fact, kuna nyakati natafakari sana kwamba, katika kufanya kazi hii, inawezekana nafaidika zaidi mimi katika kujifunza kuhusu nchi yetu, Serikali inayoendeshwa, maamuzi yanavyofanywa, sera zinavyotengenezwa, na siasa na uongozi wa nchi kwa ujumla unavyoendeshwa, kulivyo Rais anavyofaidika na usaidizi wangu.

Wewe ni mtoto wa mwanasiasa (Mh. Yusuph Makamba), je unafikiria kuna mategemeo makubwa yanayokuja kama dhamana ukizaliwa kwenye familia maarufu ya kisiasa kama ya Makamba?

Kwanza kuna heshima kubwa kutambua kwamba mzazi wako ameyatoa maisha yake kwa utumishi wa umma. Kuna sacrifices ambazo kama familia lazima mzikubali kutokana na shughuli za Mzee.

Pili, kuwa na jina la Makamba kuna uzuri na ubaya wake. Uzuri wake ni kwamba wapo watu wengi katika sehemu mbalimbali za nchi hii ambao wamefanya kazi na baba na wanamheshimu sana. Kwahiyo tayari unayo network kubwa ya extended family ambao wengi wanakujua tangu uko mdogo na wanafurahishwa na wanajiona ni sehemu ya mafanikio yako, na wako tayari kukusaidia kwa ushauri au mambo mengineyo wakati wowote.

Lakini pia wapo ambao wanaona Mzee Makamba ni mtu fulani hivi hafai au mtu wa hovyo au wana kutokuelewana naye kimitizamo au kisiasa. Mara nyingi, katika mazingira ya kwetu hapa, hawa watu hawawezi kutofautisha kati ya mawazo na misimamo ya baba na mtoto. Kwahiyo, unajikuta unarithi marafiki na maadui wa baba yako hata bila ya wewe mwenyewe kutaka.

Vilevile, ukiwa mtoto wa mwanasiasa mara nyingi kuna dhana katika jamii yetu kwamba umeishi a privileged life na kwamba umeharibika au umedekezwa na kwamba huwezi kujisimamia mwenyewe. Hii si kweli. Maisha yetu sisi miaka yote yamekuwa ya kawaida sana. Nakumbuka Mzee wangu kwa mara ya kwanza amemiliki nyumba yake si muda mrefu uliopita, na ilikuwa ni nyumba ya makuti pale kijijini Kiomoni, Tanga. Wakati wa mvua, nyumba hii ilikuwa inavuja. Tunahamisha vitanda na furniture. Na wakati tunakaa Kiomoni tulikuwa tunasoma Masiwani, Tanga Mjini ambapo ni Kilomita 12, na tulikuwa tunaenda kwa mguu, ukibahatisha ni baiskeli, na lunch ilikuwa ni mihogo ya kuchoma na maji, mama alikuwa anatupa shilingi hamsini kila asubuhi. Lakini leo kila mtu anadhani maisha yako yote umekula mkate na siagi na umepelekwa shule kwa gari.

Hata hivyo, siamini kama kuishi maisha ya shida au ya starehe kunaweza kuwa kigezo cha wema au ubaya wa mtu na uwezo au udhaifu wa mtu.

Jambo jingine, ni kwamba kwa kutoka kwenye familia ya mwanasiasa, kwenye jamii yetu kuna perception kwamba mafanikio yako yote ni lazima umeyapata kwa kubebwa. Hata kama uwe na uwezo kiasi gani, hata kama uwe unachapa kazi kwa kiasi gani, utasikia “aaah, watoto wa wakubwa wale”. Basically, juhudi zako hazionekani. Lakini hili halisumbui sana kwa sababu kwa bahati nzuri wale wanaosema haya ni wale ambao hawajawahi kukutana na wewe au kufanya kazi na wewe. Wanaokujua wanatambua ukweli.

Pia kuna hii habari naulizwa kila siku kwamba unajisikiaje kumsoma Mzee wako kwenye magazeti kila siku kwa wale wanaomsifu na kwa wale wanaomponda. Ukishakuwa kwenye familia ya siasa, haya mambo unayazoea, na hayakusumbui wala kukunyima usingizi. Unasoma headline, ukifungua ukurasa wa pili wa gazeti ndio habari imeshakwisha, maisha yanaendelea kama kawaida.

Mwisho wa yote, dhamana kubwa ni kujitambua na kujiamini na kujua unachofanya, lakini pia na kutambua kwamba kila utakachofanya, hasa mambo ya hovyo, implications zake sio kwako tu, bali pia kuna implications za kisiasa kwa mzazi wako.

Kuna tetesi kuwa unataka kujiingiza kwenye siasa na hasa inasemekana unataka kugombea ubunge mwaka ujao, Je habari hizi ni za ukweli?

Tetesi hizi zimekuwepo tangu mwaka 2005. Ikifika wakati muafaka nitalizungumzia jambo hili.

Hata hivyo, nimekuwa nawashawishi vijana wengi kuingia kwenye utumishi wa umma, ikiwemo kwenye siasa na kwenye ajira Serikalini kwa kuwa naamini kuna a sense of responsibility kwa generation yetu na sisi ku-step up.

Tuelezee nchi ambazo umezitembelea duniani na ni mambo gani umejifunza nini huko unayoweza ku-share na vijana.

Kila sehemu tunayokwenda najaribu kupata muda kujifunza historia ya pale, siasa za nchi ile, changamoto za maendeleo walizonazo, na mambo wanayofanya kukabiliana nazo. Sidhani kama nafasi hapa inaruhusu kuelezea yote haya kwa nchi zote nilizopata kutembelea. Labda nielezee tu sehemu mbili ambazo tumetembelea hivi karibuni na mambo ambayo nimeyaona ya kujifunza (sitaongelea yale ya Kiserikali, ambayo ni mengi pia).

Wiki kadhaa zilizopita nimekuwa Cairo na Roma. Nilipopata muda mchache wa mapumziko, nilizunguka kwenye landmarks na museums za Roma na Cairo. Miji hii miwili ina historia kubwa kwa ancient civilisations na kwa dini zetu kuu tatu: Uyahudi, Uislam na Ukristo. Nimekumbushia elimu ya shuleni kuhusu historia ya Himaya kuu za zamani: Roman Empire na Ottoman Empire. Ukipitia landmarks za Roma – the colosseum, the pantheon, Roman Forum, kanisa la Mt. Peter, mahali alipouawa Julius Caesar, na sehemu nyingine nyingi - unajifunza kuhusu statecraft, historia ya Ukristo, na mambo mengineyo mengi. Ukiwa Cairo, kwa kwenda kwenye pyramids, kutembelea the Citadel, misikiti ya zamani ya Sultan Hassan na Sultan Ali, na kwenda kwenye national museum yao kupata maelezo ya kuhusu maisha ya Pharaohs, unajifunza kuhusu historia ya Uislamu na Uyahudi unashuhudia landmarks zinazotajwa kwenye Biblia na Kuran, unajifunza kuhusu ujenzi wa Himaya, basically unapata introduction ya Egyptology.

Kwahiyo kote huko unajifunza mengi, ikiwa pamoja na umuhimu wa taifa ku-preserve historia yake na ya watu wake kama msingi wa kujenga pride na uzalendo wa watu kwa nchi yao – lakini vilevile kujenga a soul of a nation.

Hata hivyo, najivunia zaidi na fursa niliyopata ya kuzunguka nchi yetu yote – kila kona kwa barabara – mara mbili: wakati wa kampeni na wakati nikifanya kazi hii niyayoifanya sasa. Nimejifunza mengi kuhusu nchi yetu, watu wake, na changamoto zake na fursa zilizopo za mabadiliko katika maisha yao. I will always be grateful kwa Mhe. Rais kwa fursa hii.

Wewe unajuana na unabadilishana mawazo na watu wengi nchini, ni viongozi gani nchini unafikiri ni mfano kwa vijana wanaofikiria kufuata nyayo zao kwenye siasa?

Wapo viongozi wengi walioitumikia na wanaoendelea kuitumikia nchi hii kwa uadilifu, kwa bidii, na kwa heshima mkubwa. Vijana hawawezi kupata shida katika kuchagua kati ya hao ni wapi wafuate nyayo zao.

Ni muhimu pia kutambua ni kwamba vijana wengi wanahamasika kuingia kwenye siasa kutokana na mafanikio ya vijana wa rika lao waliowatangulia kwenye siasa. Kwahiyo, ni muhimu sana kuwaunga mkono na kuhakikisha kwamba vijana wenzetu walioingia kwenye siasa, katika vyama vyote vya siasa, wanafanikiwa na wanafanya vizuri ili wengine nao wahamasike na waone kuwa inawezekana.

Hata hivyo, nadhani fursa za kuitumikia nchi na kushiriki kwenye mabadiliko sio lazima ziwe ndani ya siasa peke yake. Wako vijana wengi mjini hapa wanafanya mambo makubwa sana kwenye nyanja finance, kwenye kwenye ICT, kwenye NGOs ambao tayari ni leaders kwenye maeneo hayo. Kuna firm hapa mjini inaitwa Serengeti Advisers ya rafiki zangu kina Aidan, Bertram, Abdu pamoja na vijana wengine pale kina Chiume, Bakilana, Eneza – they are doing great things. Yupo pia rafiki yangu Rashid Shamte na vijana wenzake pale Push Mobile – mambo wanayofanya kwenye telecoms sector si madogo. Wapo vijana wengi hapa mjini, quietly they are making things happen. Na hawa nao pia tujaribu kufuata nyayo zao na tuwa-recognise pia kama viongozi, sio tu wale waliopo kwenye politics – kwa kuwa sio kila mmoja wetu atatoa mchango wake kwa ujenzi wa nchi yetu kupitia siasa.

Wewe ni kati ya vijana wanaobahatika kwenda nchi mbalimbali na kuwaona viongozi mbalimbali, ni kiongozi gani wa kimataifa unayemkubali kwa kazi yake?

Kila kiongozi anakabiliwa na changamoto mahsusi kulingana na hali, mazingira na nyakati ambazo nchi yake inapitia. Kwahiyo ni vigumu kuwapima viongozi wote duniani kwa rula moja. Vilevile, ni vigumu kuwapima viongozi ambao hawajamaliza muda wao madarakani kwasababu kwenye uongozi wa juu wa nchi, historia inaandikwa kila siku.

Je unaye role model ambaye amekuhamasisha au anakuhamasisha kupiga hatua mbele na kufika mbali kimaendeleo?

Ninao wawili. Wa kwanza ni baba yangu, Mzee Makamba. Ningependa nami niwe mzazi mwema kama alivyo yeye. Anaipenda familia yake, anajali sana ndugu hata wawe ni wa mbali kiasi gani, hakosi msiba wala harusi, ni mkweli siku zote, anaridhika na maisha yake ya kawaida, anajiamini, haogopi wala hatishwi na mtu, hakosi usingizi kwa criticism au kusemwa, anasema kile kilicho moyoni mwake, na haweki kinyongo na maisha yake ni ya furaha wakati wote. Kwasababu yuko hivyo, na sisi wanae tunahamasika kuwa hivyo. Na yuko tayari kujinyima na kujibana ili tusome na tujiendeleze. Na nadhani ana ka-store ka stories kama 3,000 hivi, na wakati wowote yuko tayari kuchomoa story yoyote ya kuvunja mbavu au ya kufundisha ambayo ni relevant kwa mazungumzo yanayoendelea.

Wa pili ni Rais Kikwete. Sijapata kukutana na mtu mwenye passion kuhusu maendeleo ya nchi na watu wake kama alivyo Rais. Ana bidii kubwa sana ya kazi wakati mwingine anaji-push kupita kiasi. Kama binadamu, ni mtu mwema sana. Na anapenda mambo yafanyike kwa viwango vya juu. Katika mazingira tuliyonayo sasa, tumepata bahati kuwa na kiongozi wa namna hii, ambaye uhuru wa watu kusema haumsumbui, na ambaye yuko confident in his own skin. Amefikia kile ambacho Dag Hammarskjold anaita “a maturity of mind”, ambapo watu wachache sana katika uongozi wanaweza kukifikia – fearlessness and capacity to endure uncertainty.

Muda wako wa mapumziko unautumiaje?

Muda wa mapumziko kwa kazi hii ni mara chache kuupata. Lakini ninapopata mara nyingi hukaa na familia kidogo. Mke wangu na mimi hupenda sana sinema, tangu tumejuana tulikuwa tunaenda sinema kwahiyo tunafanya hivyo hapa pia pale Mlimani City, tatizo ni kwamba wanachukua muda sana kuweka new releases.

Lakini pia nina interests kadhaa, hasa muziki na kusoma vitabu. Ni mwanachama wa a very vibrant reading group hapa Dar ambapo tunakutana kila mwanzo wa mwezi kujadili kitabu au article ambayo imechaguliwa kwa mwezi huo. Pia ni mjumbe wa Bodi ya Ushauri ya Tanzania House of Talent. Nashiriki kwenye shughuli mbalimbali za kijamii. Kwahiyo, nikipata mapumziko najikuta niko busy tena na mambo mengine ya kukutana na watu.

Lakini pia napenda kukaa na marafiki na kupiga story. Mo anajua, nikiwa around tunakutana kwa kahawa na kujadili mambo ya siasa, uchumi, maendeleo na ustawi wa vijana wa nchi yetu.

Tumesikia na tumeona kwenye blog yako kwamba wewe ni mtu wa kupenda vitabu. Ni vitabu vya aina gani? Na je sasa hivi unasoma kitabu gani. Na vitabu gani, masuala gani ya jumla, unaweza ku-recommend kwa vijana kutafakari na kujifunza?

Ni kweli, nina passion na vitabu na hakuna wakati ambapo sisomi kitabu. Kwa jumla my interests are broad. Ukija kwenye kamaktaba kangu nyumbani utakutana na collection ya a range of topics and books kuanzia Matt Ridley’s biography ya Francis Crick, hadi Mariama Ba’s So Long a Letter, hadi Emmanuel Levinas’ Totality and Infinity, hadi Frans de Waal’s Chimpanzee Politics - and so forth. So, I am very indiscriminating in what I choose to read.

Hata hivyo, kwenye kuchagua vya kusoma ninakuwa driven na interest za wakati huo. Kuna kipindi, kwa miezi hadi sita, nakuwa so fixated na topic fulani, labda public health, basi nakuwa nasoma thoroughly vitabu au literature kuhusu public health. Baadaye, kwa kuhamasishwa na some article or a conference or a great conversation or a documentary, naanza something else.

Kwa sasa, niko obssessed na hii idea ya economic development na kwanini nchi zinatofautiana kwa hatua na kasi ya maendeleo. Kwahiyo, nasoma vitabu viwili kwa mpigo sasa (mimi ni mmoja wa wale wenye tabia mbaya ya kusoma vitabu viwili kwa mpigo): How Rich Countries Got Rich and Why Poor Countries Stay Poor, kimeandikwa na Erik Reinert na kingine ni Kicking Away the Ladder: Development Strategy in Historical Perspective, kimeandikwa na Ha-Joon Chang. Hawa wawili wana-share a leftist leaning hasa kuhusu role ya mifumo na taasisi za kimataifa kwenye kuleta au kukandamiza maendeleo. Lakini kikubwa najifunza kwa sasa ni a remarkable history of economics itself.

Kuhusu vitabu gani na-recommend vijana wasome au mambo gani ya kutafakari na kujifunza. Hili ni gumu kidogo manake viko vitabu vingi sana ambavyo ni muhimu na mambo vilevile ni mengi kwa vijana kuzingatia.

Cha msingi ni kwamba, kwanza, kijana ni lazima awe na consciousness kama mtu, kama mwanadamu. Hapa napendekeza vitabu vya falsafa, hasa Martin Heidegger’s Being and Time (mwalimu wangu wa philosophy St. John’s, Father Rene McGraw, alikuwa mwanafunzi wa Heidegger) na philosophers wengine ambao wanakusukuma saa zote kuwa self-aware na utu wako na matendo yako.

Pili, kijana wa Kibongo ni muhimu awe conscious kwamba yeye ni Mtanzania na azingatie the idea kwamba citizenship maana yake ni community, kwamba matendo yako yote, hata kutupa barabarani chupa tupu ya maji ya Kilimanjaro, lazima yazingatie kwamba tunaishi kwenye community, hata unapopokea simu ukiwa kwenye daladala, namna na ukubwa wa sauti unayoitumia kuongea ni suala la citizenship. Kujenga a sense of responsibility to the community ni muhimu sana kwa vijana. La sivyo tutakuwa tunaishi kama wanyama tu, kila mtu akitaka yeye ndio awahi foleni, a-divert bomba la maji mtaani liende kwake peke yake, n.k. Kitabu cha Robert Putnam, kinachoitwa Bowling Alone, kilinifungua macho kwenye masuala haya (ingawa context yake ni Marekani).

Tatu, kijana ni muhimu ajue historia ya nchi yake na sacrifices walizochukua wazee wetu huko nyuma hadi kufikia nchi yetu ikawa huru na kuwa kama ilivyo leo. Vitabu kwa ajili ya elimu hii viko vingi sina haja ya kuviorodhesha. Nne, kijana ni lazima awe na basic idea kuhusu challenges za mahali anapoishi na angalau ajisumbue kutafakari kuhusu majawabu yake – kwa mfano, kwa sisi wa Dar es Salaam, kwa miaka kumi ijayo changamoto kubwa tatu: upatikanaji wa maji pamoja na handling ya majitaka, energy kwa kupikia na city transport. Katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita, bei ya mkaa (cooking energy ya majority) imeongezeka kutoka shilingi 7,000 hadi shilingi 40,000 kwa gunia, radius ya eneo mkaa unakopatikana imeongezeka beyond Bagamoyo, kuelekea mapori beyond Mikumi na sasa watu wanaikwangua Selous. Mto Ruvu, source kubwa ya maji jijini Dar, inapungua volume by 6 percent every year. Kijana lazima asumbuke kutafakari haya mambo. Sio jukumu la Serikali au viongozi pekee. Tano, kijana ni lazima ajue mambo yanayoendelea duniani na kujaribu kutafuta rationale na implications za kila tukio.

Kwa ujumla, katika mambo yote haya, suala kubwa ni kuwa kuwa curious. Kijana akiwa curious atatafuta habari au atajisumbua kwa tafakuri. Mfano, ukisoma The Economist kila wiki kwa mwaka mzima ni elimu kubwa sana.

In the end, vitabu ambavyo kwa kufikiria haraka haraka huwa na-recommend kwa watu: Guns, Germs and Steel: The Fates of Human Societies by Jared Diamond; na Tuesdays with Morrie cha Mitch Albom.

Sahamani nikurudishe nyuma kidogo, wewe umesoma university Marekani na kule tunasikia college maisha ya kule ni furaha wakati wote na ni experience kubwa ambayo watu huwa hawasahau. Unaweza kutuambia mambo ambayo huwezi kusahau ulipokuwa college?

Ni kweli uliyosema, lakini yote yanategemea ni college gani mtu alienda. Kwanza, mimi nilienda college nikiwa tayari nimekwishafanya kazi kwenye kambi za wakimbizi huku Tanzania, kwahiyo ingawa nilikuwa sio mtu mzima sana, lakini nilikuwa kidogo na heshima yangu kwahiyo sikufanya sana fujo campus. Pili, University niliyoenda haikutoa sana fursa hivyo. Kilikuwa ni Chuo cha Wakatoliki in a real sense (ingawa dini nyingine walikuwa wanasoma na mtu hukulazimishwa kusoma theology na kwenda kanisani), kwa maana ya kwamba kulikuwa na Seminary pale pale lakini kubwa zaidi kulikuwa na Monastery pamoja na monks wa Benedictine na majoho yao meusi. Zaidi ya nusu ya wahadhiri wangu walikuwa monks. Kwahiyo haya mazingira yalikuwa kidogo na “utakatifu”.

Jambo ambalo siwezi kusahau college labda ni moja. Kwanza, pale University nilipata nafasi ya kufanya kazi kwenye nursing home ya monks – yaani kituo ambacho wale watawa (monks) wameshakuwa wazee sana au wagonjwa kwahiyo wamepelekwa kusubiri kufariki. Sasa, imagine saa zote umekaa na hawa watu ambao maisha yao yote wamejitolea kuwa watawa, kuwa watumishi wa mungu, halafu wewe unakuwa rafiki yao wakati wana-contemplate death na wana-reflect maisha yao yote. Mazungumzo yangu na wao, in fact mazungumzo yao ya mwisho mwisho duniani, kuhusu faith, immortality na ethics siwezi kuyasahau.

Sina maana ya kusema maisha yangu yamekuwa ya kitakatifu milele. Nimefanya fujo za ujana huko Sekondari na High School pia. Na bado I am not a perfect person, na kila siku ni siku ya jitihada ya kuwa a better person, a better father, a better husband, a better citizen, a better public servant.

Asante kwa mahojiano hayo, je ungependa kuwapa ujumbe gani vijana wenzako wa Tanzania?

Nashukuru tena kwa fursa hii. Naomba niseme kwamba 70 percent of Tanzanians are under the age of 30. Umri wa wastani wa Watanzania ni miaka 17. Kwahiyo, Taifa letu ni taifa la vijana – ndio tuliojaa. Kwa msingi huo, kwanza, ni muhimu kwa vijana kujitokeza ku-shape the future ambayo tunaitaka - sio kwa maneno tu au kwa mijadala pekee, bali kwa vitendo. Pili, kama tunataka kujenga jamii inayo-focus kwenye mambo ya msingi ya maendeleo, pa kuanzia ni kwenye mahusiano baina yetu: tupendane, tusaidiane, tusichukiane, tusikandiane

Blog yetu inamshukuru January kwa kufanya mahojiano hayo na sisi......tunaamini tumejifunza mengi kutokana na interview....Keep up the good work Jan......
 
Good interview.

Tunahitaji vijana wa pande mbili hizi CCM na Upinzani wenye mawazo, kujisomea na kuijua nchi ili siku ya siku nchi iwe na serikali ya wajuvi! Tukishinda wapinzani, kheri. Wakitushinda kina Januari, kheri. Ndo tufike huko. Watu waone kuwa serikali zaweza kubadilika bila kuathiri dola na Taifa letu.

Safi Januari.......
 
Propaganda hizi za Makamba family i cant bear at all!

Mwangalie Januari kama Januari. Hii ya kulinganisha na baba zao kwa kuwa tunawajua, sie ambao baba zetu hawajulikani tungekubali kulinganishwa nao?
'judge the content.......'
 
Ukianza kusoma tu, kitu cha kwanza unachoona ni kwamba interview haina credibility, ni mtu na crony wake wameamua kufanya mchezo wa kuigiza.Hicho ndicho kitu cha kwanza kabisa unachoona, kabla ya kingine chochote.
 
Safi sana January, nimeipenda interview yako.
Jamani mtoto wa fisadi sio fisadi, angalia uwezo wa mtu na wala usimfananishe na mzazi wake.
Hima vijana kwenye siasa........ tunahitaji change kwa taifa letu, na sisi vijana ndio tunaweza kuleta change za kweli.
 
Safi sana January, nimeipenda interview yako.
Jamani mtoto wa fisadi sio fisadi, angalia uwezo wa mtu na wala usimfananishe na mzazi wake.
Hima vijana kwenye siasa........ tunahitaji change kwa taifa letu, na sisi vijana ndio tunaweza kuleta change za kweli.

Weeeweee; hiyo ngumu..., mtoto wa fisadi asiwe fisadi?! Bado sijakubali.
 
Ukianza kusoma tu, kitu cha kwanza unachoona ni kwamba interview haina credibility, ni mtu na crony wake wameamua kufanya mchezo wa kuigiza.Hicho ndicho kitu cha kwanza kabisa unachoona, kabla ya kingine chochote.

Dawg..you just beat me to the punch! Hata mimi nilikuwa nawaza hivyo hivyo. I'm like...kumbe hawa ni washikaji...from there I lost interest...
 
Hii imewekwa vizuri kuserve purpose za mwaka kesho. Ukiona mwana siasa anasema "wakati ukifika" ujue huyo tayari anasema "ndiyo".

Kweli ndege wanaofanana, huruka pamoja! Kikwete na mediocre wake hawaachani.
 
Good interview.

Tunahitaji vijana wa pande mbili hizi CCM na Upinzani wenye mawazo, kujisomea na kuijua nchi ili siku ya siku nchi iwe na serikali ya wajuvi! Tukishinda wapinzani, kheri. Wakitushinda kina Januari, kheri. Ndo tufike huko. Watu waone kuwa serikali zaweza kubadilika bila kuathiri dola na Taifa letu.

Safi Januari.......

Hii Interview imekuja wakati muafaka, kwani siku kama tatu nimesoma Interview ya kijana mwingine Mh. Zitto (CHADEMA) na sasa tunasoma interview ya kijana mwingine January (Bila shaka CCM ingawa hajasema kwenye Interview yake). Pamoja na kuwa hawa watu wawili wanatofautiana kwenye itikadi za vyama vyao lakini wote wanaamini kaika jambo moja la kuwawezesha vijana kuingia kwenye nyanja za kuongoza mabadiliko na baadaye kushiriki hasa kwenye maendeleo ya nchi yao.

Jambo lingine ambalo wote wawili wanafanana ni la kujisomea. wote wanonekana ni wasomaji wazuri wa vitabu, nawaona wanasoma vitabu vya aina mbali mbali sio vya fani zao walizosomea vyuoni tu.

utofauti wao, zitto yupo wazi nini anataka kufanya in future (labda kwasababu ni mwanasiasa) January hayupo wazi juu ya mipango yake ya baadaye.

Hata hivyo binafsi nachukua kama challenge kuwa vijana wengi tuo busy sana na maisha lakini tuchukue nafasi ya kushiriki kwenye kuleta mabadiriko chanya, iwe kwenye sekta ya demokrasia na siasa au maendeleo na jamii. Vijana walio nje ya sekta ya kisiasa watambuliwe mchango wao kwani nao ni sehemu ya wanaosukuma jamii hii kutoka sehemu kwenda sehemu bora zaidi. Kama tutakuwa na vijana wabunifu wengi nchi hii itapunguza kwa kiasi kikubwa tatizo la ajira na pia msukumo wa ukuaji wa uchumi utabadirika pia.

Hongereni January na Zitto, mumeonyesha njia. Naomba kukumbushwa, hivi Zitto ndiye mbunge mdogo kuliko wote wa kuchaguliwa toka uhuru? au toka mfumo wa vyama vingi uanze? au kwa bunge la sasa tu? (Msaada kwenye tuta)
 
Is there any new ideas to his article?Hamna la maana zaidi la kutuambia maisha yake kijijini Kyaka na kuuza kwake Lubisi kwenye kilabu ya bibi yake ili aonekenane ni "mwenzetu"na tumpitishe ktk wakati wa kura za maoni kwa"kura za huruma"!

Janaury,umewasaidia nini watz wa kawaida kwenye nafasi zako ulizowahi na unazozishiikilia ikiwa ni pamoja na wakazi wa kwenu Lushoto?Tueleze mikakati yako endelevu kuwasaidia watz kwa kutumia elimu yako sio kutusimulia haya mambo ya kuuza lubisi kijijini Kitandaguro-Rwamishenye!
 
Blog yetu inamshukuru January kwa kufanya mahojiano hayo na sisi......tunaamini tumejifunza mengi kutokana na interview....Keep up the good work Jan......

Mkuu tuwekee link ya hiyo blog hapa. Ni vizuri tunapotoa source kama zipo online basi tuweke na link zake maana tukipita kwenye hiyo blog tutaweza kujifunza mengi zaidi ya hii interview, vitu kama itikadi ya blog, story zingine zilizokuwa covered huko, n.k. Tupe link mkuu
 
Jamani mtoto wa fisadi sio fisadi, angalia uwezo wa mtu na wala usimfananishe na mzazi wake

Huyu kijana ni msaidizi na mshauri wa JK hivyo huwezi kumtenganisha na ufisadi kwani anatumikia utawala wa kifisadi. Hata huyo muuliza maswali naye yuko kundi hilo ndio maana kauliza maswali ya kumjenga wala hakuuliza upande mwingine wa sarafu.
 
Tuanze kwa kukushukuru kwa kukubali kuzungumza na blog yetu. Karibu sana!

1. Nilianzia Monduli mwaka 1981. Mwaka 1983, nikapelekewa kukaa na bibi mzaa mama kijijini Kituntu, karibu na Kyaka, Bukoba Vijijini.

2. Mama yangu kwao amezaliwa peke yake, kwahiyo bibi alihitaji mjukuu wa kukaa naye kumsaidia. Ndio nikatolewa kafara. Hahahaha!

3. Kwahiyo darasa la tatu, la nne na la tano, nimesoma kijijini. Siwezi kusahau maisha yale: asubuhi ni kupiga umande literally kwenda shule umbali wa kama kilomita nne na nusu hivi kutoka nyumbani,

4. ukirudi saa tisa ni kwenda kuchunga mbuzi, ukisharudisha mbuzi zizini saa kumi na mbili jioni ni kwenda kuchota maji mtoni, usiku kazi ni kumsaidia bibi kuuza pombe ya ndizi inayoitwa lubisi (bibi alikuwa na kilabu maarufu pale kijijini).

5. Anyway, nilirudi kukaa na wazazi wangu tena wakiwa Lushoto kwahiyo nikasoma darasa la sita pale, Shule ya Msingi Kitopeni, na kwenda kumalizia darasa la saba shule ya Msingi Masiwani Tanga Mjini.

6. Sikumbuki kama nilishawahi kushuka chini ya nafasi ya nne.

7. Form one nilisoma Handeni Secondary School, hii ilikuwa ni shule mpya, sisi tulikuwa Form One ya pili – kulikuwa hakuna walimu, madawati, maabara, n.k. Form Two hadi Form Four nikasoma Galanos, Tanga Mjini. Wakati nikiwa Form Three nilichaguliwa Deputy Head Prefect pale Galanos. Form Five na Six nikawa Forest Hill Secondary School, Morogoro,

8. ambapo siku ya graduation nilitunikiwa cheti cha Overall Best Student.

9. Anyway, wakati nasuburi kwenda university, nikaenda kutafuta kazi kwenye kambi za wakimbizi Kibondo na Kasulu mkoani Kigoma. Nikafanikiwa Kasulu.

10. Eventually nikapata Chuo Marekani. Nilianza Boston baadaye nikajiunga na St. John's University, Minnesota. Hiki ni Chuo cha Wakatoliki Wabenedicto kilichokuwa katikati ya pori na lakes, a very beautiful and quiet place, katikati ya Jimbo la Minnesota. Pale, degree niliyochukua ni BSc in Peace and Conflict Studies.

11. Wakati nikiwa St. John's University, nilirudi tena kufanya research yangu na UNHCR kwenye makambi ya wakimbizi Kasulu na Kibondo lakini pia kwenye way stations ndani ya Burundi na DRC.

12. Baada ya kumaliza St. John's, nikapata research assistantship kwenye ofisi ya Rais wa zamani wa Marekani, Mzee Jimmy Carter, Carter Presidential Centre, kule Atlanta, Georgia. Kazi hiyo ilinipeleka hadi kufanya kazi Sierra Leone, ambako pia nilijifunza mengi. Pia Atlanta ndiko nilikofanikiwa kukutana na mke wangu mpendwa, Mona, ambaye mwakani itakuwa miaka kumi tangu tujuane, na ambaye, pamoja naye, tuna mtoto mmoja wa kike wa miaka mitatu na nusu.

13. Baada ya Carter Center, nikajiunga na George Mason University, iliyoko maeneo ya Fairax, Washington DC metro area, kusoma Masters kwenye fani ile ile ya diplomasia na usuluhishi wa migogoro.


14. Baada ya kumaliza graduate school nikaomba kazi Serikalini na kuajiriwa na Wizara ya Mambo ya Nje kama Afisa wa Mambo ya Nje Daraja la Pili (Foreign Service Officer II). Nikiwa Wizara ya Mambo ya Nje, nilipata fursa ya kufanya kazi kwa karibu na Waziri wetu wakati ule (Mhe. Kikwete), hasa kwenye harakati za kutafuta suluhu ya mambo ya Burundi na DRC. Kwahiyo, wakati alipoamua kugombea Urais, akaniomba nichukue likizo isiyo na malipo Serikalini nisaidie kuwa errand boy kwenye kampeni yake, ku-organise makaratasi na notes zake, na kuchangia hapa na pale kwenye tafakuri za kuendesha na ku-organise kampeni yake wakati ule.

15. : tupendane, tusaidiane, tusichukiane, tusikandiane


....

- Ndugu Januari, ubarikiwe sana na ufike mbali sana mbele ya maisha yako maana historia ya maisha yako ni very humble na bado nakutakia safari ndefu na jema mbeleni na utanguliwe na Mungu wa Mbinguni na wako ni mfano wa kuigwa sana na vijana wengine nchini.

Bravo Januari!

William.
 
Muwe mnasoma na kitabu hiki The Mwembechai Killings and the political Future of Tanzania. kiko online.ili mjue wapi tumekota.
 
Muwe mnasoma na kitabu hiki The Mwembechai Killings and the political Future of Tanzania. kiko online.ili mjue wapi tumekota.
Inawezekana wenye nacho hawajakitangaza, si umeona cha Edwin Mtei last two weeks kilivyosikika ghafla na watu wengi tumeshakisoma, kuandika kitabu ni jambo moja, kukipublish ni jambo la pili, kukitangaza la tatu, na kuwafanya watu wasome au hata wanunue ni jambo lingine nalo. Tuwekee LINK
 
Vilevile, ukiwa mtoto wa mwanasiasa mara nyingi kuna dhana katika jamii yetu kwamba umeishi a privileged life na kwamba umeharibika au umedekezwa na kwamba huwezi kujisimamia mwenyewe. Hii si kweli. Maisha yetu sisi miaka yote yamekuwa ya kawaida sana. Nakumbuka Mzee wangu kwa mara ya kwanza amemiliki nyumba yake si muda mrefu uliopita, na ilikuwa ni nyumba ya makuti pale kijijini Kiomoni, Tanga. Wakati wa mvua, nyumba hii ilikuwa inavuja. Tunahamisha vitanda na furniture. Na wakati tunakaa Kiomoni tulikuwa tunasoma Masiwani, Tanga Mjini ambapo ni Kilomita 12, na tulikuwa tunaenda kwa mguu, ukibahatisha ni baiskeli, na lunch ilikuwa ni mihogo ya kuchoma na maji, mama alikuwa anatupa shilingi hamsini kila asubuhi. Lakini leo kila mtu anadhani maisha yako yote umekula mkate na siagi na umepelekwa shule kwa gari.

Kama haya ni kweli basi ndio maana Makamba anashindwa kukiongoza chama ,kwani hata maisha yake ameshindwa kuyaongoza atawezaje kuongoza chama kizima?
Kama amekuwa mkuu wa Mkoa, amefanya kazi jeshini akashindwa hata kujenga nyumba atawezaje kujenga CCM?

Mshahara wake alikuwa anafanyia kazi gani?
Nini kilikuwa kitu cha msingi kwake?
Ina maana nyumba kwake sio priority?
 
..sasa nimebaini kwamba mwenye matatizo ni JK, washauri wake wako OK.

..inaelekea January Makamba ana mipango ya kugombea ubunge.
 
Back
Top Bottom