FOCAC yaimarisha ukuaji wa ushirikiano wa kina kati ya China na Tanzania

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,000
1,019
Na Caroline Nassoro

1637543693442.png


Mkutano wa mwaka huu wa Baraza la Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC) unatarajiwa kufanyika mjini Dakar, Senegal, kuanzia tarehe 29 hadi 30 Novemba, mwaka huu.

Kaulimbiu ya mkutano huo kwa mwaka huu, ni “Kuimarisha Uhusiano wa China na Afrika na Kuboresha Maendeleo Endelevu ili Kujenga Jamii ya China na Afrika yenye Mustakabali wa Pamoja katika Zama Mpya.” Wawakilishi kutoka China na nchi za Afrika watakutana na kufanya tathmini ya kina ya utekelezaji wa matokeo ya Mkutano wa FOCAC uliofanyika Beijing mwaka 2018, na mshikamano wa China na Afrika katika mapambano dhidi ya janga la virusi vya Corona.

Tanzania imeshiriki kikamilifu katika shughuli za Baraza hilo, na kuunga mkono kuanzishwa kwake miaka 21 iliyopita. China na Tanzania zimedumisha mawasiliano ya kimkakati ndani ya mfumo wa FOCAC, kuimarisha ushirikiano wa kina wa kunufaishana, na kuboresha utekelezaji wa matokeo muhimu ya mikutano yote iliyopita ya FOCAC, hivyo kuleta msukumo mkubwa katika maendeleo ya pamoja ya Tanzania na China.

Thamani ya biashara kati ya Tanzania na China imeongezeka kwa karibu mara 50, kutoka chini ya dola za kimarekani milioni 100 mwaka 2000 hadi kufikia dola za kimarekani bilioni 4.58 mwaka 2020. Lakini pia uwekezaji wa jumla wa kampuni za China nchini Tanzania umezidi dola za kimarekani bilioni 7, huku kukiwa na miradi zaidi ya 700 ya uwekezaji.

Kwa miaka kadhaa sasa, China imekuwa mwenzi mkubwa wa biashara wa Tanzania, na pia chanzo kikuu cha uwekezaji wa kigeni. Miradi mikubwa imekamilika na kuwa ishara ya urafiki kati ya nchi hizo mbili, ikiwemo Ukumbi wa Mikutano ya Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere, Maktaba ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na pia Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete.

Ushirikiano kati ya China na Tanzania pia umegusa maeneo mbalimbali, ikiwemo miradi ya ujenzi wa miundombinu inayotekelezwa na kampuni za China. Baadhi ya miradi hiyo ni awamu ya tano ya reli ya SGR na upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam, na miradi ya ushirikiano wa kujenga uwezo wa uzalishaji kati ya China na Tanzania.

China pia imeiunga mkono Tanzania katika kupambana na virusi vya Corona, na mpaka sasa, nchi hiyo imetoa msaada wa dozi karibu milioni 3.5 za chanjo ya virusi vya Corona kwa Tanzania.

Kwa hayo machache, tunaweza kuona kuwa uhusiano na ushirikiano kati ya China na Afrika, Tanzania ikiwemo, chini ya mfumo wa FOCAC, umeweza kunufaisha pande zote husika na kuboresha sekta ya miundombinu, ambayo ni muhimu kwa maendeleo.
 
1 Reactions
Reply
Back
Top Bottom