FikraPevu: Waziri Chami ajibu mapigo sakata la TBS Bungeni

Halisi

JF-Expert Member
Jan 16, 2007
2,802
613
Waziri wa Viwanda na Biashara Dkt Cyril Chami amejitetea kwamba yeye na wizara yake hawamlindi Mkurugenzi Mkuu wa TBS Bwana Charles Ekelege kama alivyotuhumiwa na baadhi ya wabunge mjini Dodoma katika kikao cha Bunge kinachoendelea sasa.

Industry-and-Trade-Minister-Cyril-Chami-250x165.jpg


Dkt Chami amesema kilichotokea ni Wizara yake kufuata sheria na kanuni zote za usimamizi wa mashirika ya Umma kama zinavyoainishwa katika Waraka wa Msajili wa Hazina wa mwaka 2004 unaoelezea utaratibu wa wizara kufuata katika kuyasimamia mashirika ya umma yaliyo chini ya wizara hizo.

Amesema kwa kipindi chote cha uongozi wake, ameutumia utaratibu wa "eyes on, hands off" ambao ndio utaratibu unaokubalika wa kusimamia mashirika yaliyo chini ya wizara yoyote. Utaratibu huu unautaka uongozi wa wizara zote kuyasimamia mashirika ya umma lakini pia kutokuyaingilia katika utendaji wake wa kazi.

Dkt Chami anaeleza kuwa kwa mujibu wa sheria na taratibu, mamlaka ya kwanza ya usimamizi wa Shirika la Umma ni ile ya bodi za wakurugenzi ambayo mara nyingi wenyeviti wake ni wateule wa Rais.

"Wengi wanadhani Waziri anaweza kuamua kumsimamisha kazi Mkurugenzi wa Shirika la Umma bila kupata maoni ya Bodi na kibali cha Rais, lakini siyo sahihi. Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umma akituhumiwa na yeyote, kanuni zinaelekeza kuwa Waziri anapaswa kupata ushauri wa Bodi ya Wakurugenzi juu ya tuhuma zilizotolewa, na baada ya ushauri huo naye, kwa Wakurugenzi walioteuliwa na Rais, atamshauri Mheshimiwa Rais ipasavyo ili Mheshimiwa Rais aelekeze inavyofaa," alisema Dkt Chami.

"Hata hivyo, pale ambapo Bodi itaona kuwa uwepo wa Mkurugenzi mhusika ofisini wakati anachunguzwa utaufanya uchunguzi usiende vema, Bodi hiyo hiyo inaweza kuishauri Serikali ili Mkurugenzi husika asimamishwe kwa muda hadi hapo uchunguzi kamili juu yake utakapokamilika," anasema.

Dkt Chami alisema tuhuma kwamba TBS haifanyi kazi yake sawasawa zilitolewa kwa mara ya kwanza na waheshimiwa wabunge katika Bunge la Tisa, jambo lililomfanya Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kusimamia Mashirika ya Umma wakati huo, Mheshimiwa Kabwe Zuberi Zitto, aunde kamati Ndogo iliyoongozwa na Makamu wake wakati ule, Mheshimiwa Esterina Kilasi, aliyekuwa Mbunge wa Mbarali.

Taarifa ya Kamati hii ndogo iliyotiwa sahihi na Mheshimiwa Kilasi inaanisha changamoto, matatizo na mafanikio ya TBS katika ukaguzi wa magari nje ya nchi. Katika kuhitimisha taarifa yake, Kamati hiyo teule iliupongeza uongozi wa TBS na ule wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Masoko, kwa kulisimamia vema zoezi la ukaguzi wa magari pamoja na changamoto nyingi walizokuwa wanakumbana nazo.

Kamati ilitoa mapendekezo ya mambo ya kufanya ili kuboresha ukaguzi huo, mojawapo likiwa pendekezo kuwa TBS iwezeshwe kukagua magari nchi nyingi zaidi na la pili, TBS isijikite kwenye ukaguzi wa magari tu bali wakague na bidhaa nyingine. TBS na Wizara zikapokea na kuyafanyia mapendekezo hayo kazi.

Dkt Chami anasema moja ya mambo yaliyoonekana yanafaa kwa wakati ule ni kurekebisha sheria iliyoanzisha TBS ili, pamoja na mambo mengine, kuipa TBS jukumu la kukagua kwa lazima magari na bidhaa muhimu zinazoingia nchini kabla hazijasafirishwa kutoka katika nchi zilikozalishwa.

Ndipo Bunge likaipitisha sheria namba 2 ya mwaka 2009 inayolitaka shirika hilo kutekeleza zoezi hilo. Anasema Dkt Chami kuwa sheria hiyo iliyowasilishwa Bungeni na mtangulizi wake Mheshimiwa Dkt Mary Nagu na kupitishwa na Bunge mwezi Februari 2009 ilianza kutekelezwa Februari mosi 2012, baada ya Wizara kukamilisha uandishi wa kanuni za uendeshaji wa zoezi hilo na kanuni hizo kusainiwa na mtangulizi wake Dkt Nagu.

"Kazi ya TBS na Wizara ni kuitekeleza sheria hii iliyotungwa na Bunge. Kama Wizara na TBS tungeacha kuitekeleza sheria hii ya Bunge tungekuwa tumekwenda kinyume na sheria na taratibu za nchi yetu. Kama kuna matatizo ya utekelezaji, hapo ndipo tunakaribisha maoni ya kila mdau ili utekelezaji uende vema. Na kama sheria yenyewe haifai, taratibu ziko wazi zinazomruhusu mheshimiwa mbunge yeyote kupeleka kwa Mheshimiwa Spika hoja ya kuliomba bunge liibadili sheria husika, " alfafanua Chami.

Chami alisema njia ya pili ni wizara mama kuanza mchakato wa kuibadili sheria kwa kuipeleka kwenye Baraza la Mawaziri na baada ya kurithiwa, kuipeleka bungeni. Kwa sheria hii ambayo imeanza kutekelezwa Februari mosi 2012, itakuwa kichekesho kama TBS inaanza kuitekeleza sheria na baada ya miezi miwili Wizara inayoisimamia TBS iende tena kwenye Baraza la Mawaziri kuiomba sheria hiyo ibadilishwe, kabla hata ya kupata muda wa kutosha wa kutathmini utekelezaji wa sheria yenyewe.

"Jamani nitaonekana waziri wa namna gani endapo nitapendekeza mabadiliko katika sheria ambayo haina hata miezi mitatu katika utekelezaji? Si nitaonekana ndiyo nasukumwa na maslahi binafsi?" alihoji Dkt Chami.

Kuhusu madai ya utendaji kazi dhaifu wa TBS na kwamba yeye binafsi na Katibu Mkuu wake wanamlinda Ndugu Ekelege, Dkt Chami alikanusha vikali tuhuma hizo. Alijitetea kwa kusema kwamba hakuna wakati hata mmoja ambako Wizara yake imetakiwa kutoa ushirikiano katika jambo hilo ikasita au ikatoa taarifa zisizo sahihi.

Kwa mfano, mwezi August mwaka 2011 Mheshimiwa Zitto aliunda tena Kamati ndogo kwenda kukagua tena shughuli za makampuni yaliyokuwa yamepewa mikataba ya kukagua magari na TBS huko Singapore na Hong Kong. Japokuwa wabunge wale hawakuieleza wizara walichokiona huko, mara baada ya uongozi wa wizara kuona na kusoma kwenye vyombo vya habari jinsi wabunge wale walivyomtuhumu Mkurugenzi Ekelege tarehe 27 Januari 2012, Wizara iliomba kutoka Ofisi ya Spika taarifa ya ziara ya hao waheshimiwa wabunge na walichokiona huko ili Wizara iifanyie taarifa hiyo kazi. Dkt Chami alilieleza gazeti hili kwa masikitiko huku akiwa ameshikilia nakala ya barua kutoka kwa Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara kwenda kwa Katibu wa Bunge, kuwa hadi leo Wizara haijapokea taarifa hiyo.

Badala yake, Wizara ilipata barua kutoka Ofisi ya Bunge ikiutaka uongozi wa Wizara kukabidhi kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG) takwimu zinazoonyesha idadi ya magari yaliyokaguliwa na TBS na fedha zilizopatikana tangu TBS ilipoanzishwa mwaka 2002. Wizara ililifanyia kazi agizo hilo lililo kwenye barua ya tarehe 6 Februari 2012 na kukabidhi kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu taarifa hizo tarehe 18 Februari 2012.

"Taarifa yenye takwimu kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara ndizo zimemwezesha Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu kutoa taarifa yake inayotumiwa na waheshimiwa wabunge hivi sasa, sasa hapo mimi na Mama Mapunjo (Katibu Mkuu Viwanda na Biashara) tunamlindaje Ekelege?" alihoji Dkt Chami.

Dkt Chami, ambaye pia ni Mbunge wa Moshi Vijijini mkoani Kilimanjaro, alisema tuhuma nyingine anayotuhumiwa nayo ni ile ya kutokumsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu Ekelege kama ambavyo Kamati tatu zilizokaa Februari 10, 2012 ziliagiza. Katika utetezi wake, anasema aliomba barua kutoka Ofisi ya Spika juu ya agizo hilo lakini hadi jana alikuwa hajapokea barua hiyo japokuwa Bunge linaelezwa kwamba barua hiyo ipo.

"Hebu tupime sote. Katika kupata takwimu, Ofisi ya Bunge iliuandikia uongozi wa Wizara ikiagiza kwamba Wizara ipeleke takwimu zinazoihusu TBS kwa CAG. Kwa nini katika hili la kumsimamisha Mkurugenzi Mkuu tusipate maagizo ya maandishi pia kutoka ofisi ya Spika? Lipi rahisi, kutoa takwimu za magari au kumsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu wa TBS? Nina hakika hili la kumsimamisha kazi Mkurugenzi ni zito na lilihitaji barua pia, ikizingatiwa huyu ni mteule wa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania." Alifafanua Dkt Chami.

Dkt Chami anasema kama angepata barua hiyo asingesita kuomba ushauri wa Bodi na kuwasiliana na mamlaka ya uteuzi (Mheshimiwa Rais) juu ya jambo hilo ili kupata uamuzi wake, kama sheria inavyoelekeza.

Hata hivyo Dkt Chami alisema baada ya kusikia tuhuma nyingi hasa kupitia vyombo vya habari juu ya Mkurugenzi Mkuu wa TBS, alimuomba Mheshimiwa Rais aharakishe uteuzi wa Mwenyekiti mpya wa Bodi ya TBS ambayo ilikuwa imemaliza kipindi chake Desemba 2011. Mara baada ya Mheshimiwa Rais kumteua Ndugu Oliver Mhaiki kuwa Mwenyekiti mpya wa Bodi, Dkt Chami aliizindua Bodi hiyo mara na kuiagiza ifanyie kazi tuhuma zilizokuwa zimeenea kuhusu utendaji mbovu wa TBS na Mkurugenzi wake Mkuu na kuishauri Serikali mara moja.

"Mapendekezo hayo ya Bodi ndiyo yatafanyiwa kazi na Serikali. Mara nyingi Mawaziri wanaoamua kumsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu wa taasisi ya Umma bila kupata maoni ya Bodi husika wametuhumiwa kwenda kinyume cha kanuni, na hata kuonekana kusukumwa na maslahi binafsi katika uamuzi wao huo. Mimi naielekeza Bodi ifanye kazi yake na mapendekezo yake yatazingatiwa na Serikali kama inavyoelekezwa katika Waraka wa Msajili wa Hazina Kuhusu Mashirika ya Umma wa mwaka 2004, nimekosea wapi?" Alihoji Dkt Chami.

Anasema jambo lililomsononesha ni pale taarifa ya ukaguzi wa CAG juu ya TBS ilipotolewa kwa waheshimiwa wabunge bila yeye mwenyewe au Wizara kupewa nakala kwa kipindi cha wiki nzima.

Anasema kutokana na kusikia kuwa waheshimiwa wabunge wengi wanayo taarifa hiyo na hata Naibu wake kukiri bungeni kwamba taarifa imetoka wakati yeye hana, alikwenda kwa Katibu wa Bunge Dkt Thomas Kashillilah na kuiomba nakala ya taarifa hiyo. Kwa mastaajabu hata Dkt Kashillilah alisema alikuwa hajaipokea taarifa hiyo.

Alipouliza Wizarani aliambiwa nako pia hawajapatiwa taarifa hiyo. Katika ufuatiliaji, Katibu Mkuu wa Wizara yake alipiga simu ofisi ya CAG, nao wakakiri kuigawa kwa waheshimiwa wabunge na kudai kwamba eti walighafilikiwa wakaisahau Wizara husika.

"Ndugu mwandishi, hapa wasomaji wako na wapime wenyewe. Inawezekanaje taarifa ya CAG iliyoandikwa kutokana na takwimu zilizotolewa na Wizara yangu, iwafikie waheshimiwa wabunge huku Wizara yangu itakayotakiwa kuifanyia kazi taarifa yenyewe haipewi nakala, eti kwa kughafilika? Ni ukweli ofisi ya CAG walighafilikiwa, au jambo hili limesukwa ili kuniaibisha mimi mbele ya Watanzania, Rais aliyeniteua na hasa wapiga kura wangu wa Moshi Vijijini?" alihoji Dkt Chami

Anadai Dkt Chami kuwa waliopanga asipate nakala hiyo ya taarifa ya CAG walifanikisha lengo lao kwani katika kujumuisha taarifa ya Kamati yake ya Mahesabu ya Serikali Kuu, Mheshimiwa John Cheyo alimkebehi kwa kumwonyesha kama Waziri asiyejua kufuatilia mambo, ndiyo maana waheshimiwa wabunge walikuwa na nakala za taarifa hiyo na yeye hakuwa nayo. Alisema jambo hilo lilimdhalilisha sana lakini anamuachia Mungu aonaye siri za watu.

Dkt Chami alisema tuhuma nyingine zinazoelekezwa kwa Wizara yake ni kwamba makampuni yaliyopewa kazi ya ukaguzi wa magari nje yana uhusiano na watendaji wakuu wa wizara yake.

Anakumbusha kuwa ukiondoa makampuni haya makubwa matatu yaliyoanza kazi ya ukaguzi mwaka huu, na ambayo yote ni ya kigeni, makampuni yote matano yanayoendelea na ukaguzi wa magari yalipata tenda hizo mwaka 2007, yeye akiwa Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.

Hata Naibu Waziri Nyalandu, Katibu Mkuu Mama Mapunjo na Naibu Katibu Mkuu Dkt Mwinjaka walikuwa hawajateuliwa kuiongoza Wizara ya Viwanda na Biashara mwaka 2007. Anahoji kuwa kama makampuni hayo ni yale yale, iweje leo Watanzania wafanywe kuamini kwamba viongozi waandamizi wa Wizara ndio wamiliki wasio wa moja kwa moja (indirect owners) wa makampuni hayo?

Dkt Chami aliwaomba wale wote wanaomkosoa watambue kwamba yeye anafuata sheria, kanuni na taratibu za nchi, na kwamba kama asingefuata taratibu hizo, malalamiko juu yake yangekuwa makubwa kuliko yalivyo sasa. Kwa mfano, anadai kuwa kama angemsimamisha Mkurugenzi Mkuu wa TBS bila kupata barua Ofisi ya Spika na wala kuishirikisha Bodi ya Wakurugenzi katika uamuzi huo, sasa hivi angekuwa anatuhumiwa kwa kuvunja kanuni ya uendeshaji bora wa mashirika ya umma, na wengine wangedai kuwa ana maslahi binafsi.

"Jamani Waziri akimfukuza kazi au kumsimamisha Mkurugenzi wa Shirika la Umma bila kufuata sheria na kanuni zilizoainishwa analaumiwa na kutuhumiwa kuwa analinda maslahi binafsi. Waziri mwingine akifuata sheria na kanuni kabla ya kumsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu wa Shirika lingine la Umma, naye analaumiwa kwa kumlinda mkurugenzi husika na kuonekana kuwa naye ana maslahi binafsi. Kipi ni kipi? Naomba sote tukubali kuwa maadam nchi yetu inaendeshwa kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu, na kama mawaziri wameapa kuzilinda sheria na kanuni hizo, basi tukubali tu sheria na kanuni vichukue mkondo wake hata pale ambapo tuna hisia kali juu ya Mkurugenzi fulani. Kwa njia hiyo, haki haitakuwa inatendekea tu, bali pia itaonekana kuwa inatendeka," alizidi kufafanua.

"Kama Waziri, niliapa kuwa mwaminifu kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuilinda katiba ya nchi yetu na kumshauri Mheshimiwa Rais kwa ukweli na uaminifu. Nikikiuka sheria au kanuni za nchi ili nionekane tu kuwa shujaa huku nikimtosa mtu ambaye ametuhumiwa, na tuhuma hizo ziko katika hatua za kuhakikiwa, na zoezi hilo halijakamilika kadiri sheria inavyotaka, nitakuwa navunja kiapo hicho nilichokitoa huku nimeishika Biblia Takatifu," alimalizia Waziri Chami.


CHANZO: Dk. Chami ajibu mapigo sakata la TBS bungeni | Fikra Pevu | Kisima cha busara!
 
Yaani badala ya kutoa solution anatusomea sheria iliyounda mashirika ya umma ambayo ndo wamekazana kuhakikisha yote yanakufa.
 
Ukweli ni kwamba wanakumbuka shuka kumekucha, duh!! saa hizi "La kuvunda halina ubani"
 
CCM made an error of judgement with regard to what Tanzanians expect them to do. Sasa hivi kimekuwa kivuli cha wababaishaji. Wanategemea nini?
 
kweli anaumwa hadi akashindwa fuatilia taarifa inayomhusu ya CAG ?
 
Analalamika hakupewa taarifa na CAG, ina maana yeye hajui nini kinachoendelea hapo wizarani? Nani alitakiwa kuwa na taarifa kwanza, yeye au CAG. Yaani uchafu ufanyike wizarani kwako halafu unalalamika hukupewa taarifa? Sasa wizara inaongozwa na nani? Tangu mwenyekiti mpya wa bodi ateuliwe na waziri kutoa maagizo ifuatlie utendaji wa TBS ni nini kilifanyika? na kama hakuna ni nani anayewajibika?

Kwa kifupi tu ni kwamba Chami alipaswa kujua udhaifu wa TBS bila hata kusubiri kuletewa ripoti kutoka kwa mamlaka nje ya wizara yake. Yeye ndio msimamizi mkuu wa wizara na uzembe wote wizarani kwake yeye ndio anayewajibika. .
 
Huyu waziri bado anaumwa nadhani. Hajamuona Vicent Nyerere alivyowataja wenye kampuni bandia na jinsi sticker za inspection zinavyouzwa online? Hawa mawaziri wanahitaji kunyongwa aisee maana wanaboa mpaka bia yangu haishuki sasa nikisoma habari zao.
 
Mimi sioni kosa la ndugu chami ....kwani kwa maeleZo Yake ni kuwa bodi za mashirika ya umma ndio zenye mamlaka ya kushauri ..hatua za kinidhamu.......hajakataa kuchukua hatua ..ila anasubiri hatua zikamilike na hataki kukurupuka.....Nampa pole sana...ndio madhara ya kufanya kazi na rais msanii....kwake kuwatoa sadaka watendaji wake kwa mamlaka zilizo mikononi kwake imekuwa kawaida.....
Mnakumbuka waziri diallo aliondolewa barazani kati ya mambo aliyokuwa akilaumiwa ni kumfukuza kazi mkurugenzi wa idara ya wanyaama pori bila kupata kibali cha ikulu......kilichotokea ni nini....Yule mkurugenzi Alimgomea waziri ....na aliendelea kwenda ofisini wakawa wanapishana kwenye korido kwa karibu miezi miwili ...hadi taratibu za kumuadjibu zilipokubaliwa na hakufukuzwa Bali alipelekwa kuwa mkuu wa chuo mwika....

Fedheha hii ya kuogopa kuhitilafiana na mamlaka za uteuzi zilimkuta Pinda .....alipotamani kumfukuza kazi Jairo na asifukuzwe....akajifunza lilipokuja suala la mama Nyoni ...Pinda aliziba MDOMO wake...

Ifike mahali rais ache kuwatoa kafara watendaji wale........yeye pekee ndio mwenye uwezo wa kumsimamisha kazi mtu wakati wowote ...bila kulazimika kutoa sababu na simply akasema kwa manufaaa ya umma....kwenye tawala zilizopita habari Kama hizo zilikuwa maarufu taarifa za habari za saa Saba mchana....au mbili usiku..utasikia simply ..."dar es salaam....rais wa JAMHURI ya muungano wa Tanzania......Leo amemsimamisha .....kazi kwa manufaa ya umma ...kupisha uchunguzi.",,.."hakuna tarifa ya ziada iliyotolewa na ikulu." ......hii ni nguvu ya rais...yeye haitumii anataka mawaziri ambao hawana nguvu ya namna hiyo labda waamue kutumia ile staili ya Mrema enzi zile....ambayo inafaa tu pale nchi Inapokuwa chini ya mapinduzi ....na hiki ndicho kilichofanya mawaziri chini ya msuya wakamwambie Mwinyi hawawezi kufanya kazi na Mrema Kama naibu waziri mkuu.....

Nadhani rais anahusika kwa kiasi kikubwa na huu mchezo unaoendlea kwani sio Siri anayo mawasiliano makubwa sana na Chadema ie Zitto na Mbowe ....na hata Slaa......na anaweza kupenyeza Siri za namna hii indirect .......ili kuwapa wananchi ya kuongea .....ili kusogeza siku..,lakini kimsingi anawajenga Chadema na Kukimaliza chama chake .....na siku akikabidhi madaraka ...wana ccm wenzake watamfuata Msoga ........kumlilia kwa kukiangamiza kabisa chama ccm...na asilani wakimuacha.
 
Philemon, ukweli ni kwamba Chami anahusika na huu ufisadi au basi ni mzembe. Mbona Magufuli alimuondoa Mrema pale Tanroad na hakukuwa na lawama? Chami alishindwa nini kuwa wa kwanza kutoa taarifa kwa CAG na kwenye baraza la mawaziri kama alikuwa anaogopa kukiuka taratibu za kumfukuza Ekelege? Either hakujua (uzembe) au anausika (ufisadi)
 
Kila siku huwa nasema hizo sheria huwa wanazitunga zikiwa na matobo kwa makusudi kabisa ili wazitumie kufanya uzembe. Lakini pamoja na ubovu wa hizo sheria, bado kama waziri ni mkali anaweza kuhakikisha Mkurugenzi hafanyi ufisadi.

Hili litakuwa fundisho kwa wengine, kwamba serikali ipeleke miswada bungeni ambayo ina akili na haina matobo ya kuendeleza kulindana na kuweka mfumo mbovu wa uwajibikaji.
 
UZEMBE TU...

Per-diem moja ilikua inatosha kutoa copy kutoka kwa hao wabunge kama shida ilikua ni report.....aache kujitetea....babaa umechemka kubwaaaaaaaa
 
Kama ripoti ilisambazwa kwa wabunge ina maana iliwekwa kwenye pigeon hole za wabunge wote. Jee, yeye si Mbunge? hapo sasa. Saa nyingine kumtetea mtu kama huyu inakuwa muhali.

Angesema kitu kinachoeleweka ningemuelewa, kuwa maeiataarifu ofisi ya Rais kuhusu uozo wa TBS na hakupata jibu. Laakini anaongelea bunge ambalo halina mamlaka ya kumsimamisha kazi huyo Mkurugenzi. Kwanini badala ya kupeleka barua bungeni asipeleke kwa Rais?
 
......Dkt Chami anaeleza kuwa kwa mujibu wa sheria na taratibu, mamlaka ya kwanza ya usimamizi wa Shirika la Umma ni ile ya bodi za wakurugenzi ambayo mara nyingi wenyeviti wake ni wateule wa Rais.

"Wengi wanadhani Waziri anaweza kuamua kumsimamisha kazi Mkurugenzi wa Shirika la Umma bila kupata maoni ya Bodi na kibali cha Rais, lakini siyo sahihi. Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umma akituhumiwa na yeyote, kanuni zinaelekeza kuwa Waziri anapaswa kupata ushauri wa Bodi ya Wakurugenzi juu ya tuhuma zilizotolewa, na baada ya ushauri huo naye, kwa Wakurugenzi walioteuliwa na Rais, atamshauri Mheshimiwa Rais ipasavyo ili Mheshimiwa Rais aelekeze inavyofaa," alisema Dkt Chami.

Tunaambiwa kuwa Tatizo hapa ni "Mteuzi" ila mkubwa akikosea wadogo lazima wainuke haraka na kujitaja kuwa wao ndo waliokosea. Katiba mpya ianzie hapa, tumpunguze MAGUVU Rais yaani anajua kuteua lakini kutimua shida.
 
Ni kwamba unampa waraka wa kumfukuza kazi nakala kwa huyo aliyemteua akikataa unajiuzulu wewe period! Wacha abebe mzigo kwani alidhani atakuwa kiongozi milele?
 
Maelezo debe ya nini? Jiuzuru Baba , kwanini unang'ang'ania madaraka? Wakati huwezi?
 
UZEMBE TU...

Per-diem moja ilikua inatosha kutoa copy kutoka kwa hao wabunge kama shida ilikua ni report.....aache kujitetea....babaa umechemka kubwaaaaaaaa

Haukuwa na sababu ya kuweka quote ya thread hapa, mnatusumbua tunaotumia simu.
 
Back
Top Bottom