Fikra za Nyerere, utapiamlo wetu na umeme wa mgawo

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,316
33,125
HUENDA isiwe rahisi kiasi hicho kwetu sisi kutatua kiini cha matatizo yetu makubwa endapo mitazamo yetu (kuhusu matatizo yetu) na hatua tunazochukua ni zile za kuzuia tatizo moja baada ya jingine lisituumbue. Inaelekea hatujatambua umuhimu na namna ya kufuata kiini cha tatizo ili kukishughulikia.

Â

Yapo mambo mengi yanayotokea leo hapa nchini na namna yanavyoshughulikiwa ni kielelezo tosha kwamba hatuwezi kamwe kutoka hapa tulipo – kama kweli tunataka kupiga hatua – kwa kuendekeza mazoea na kuchukua maamuzi ya kutosheleza maslahi binafsi (kama kushinda uchaguzi) au ya wakati.

Â

Moja ya mambo makubwa ambayo tungeweza kujifunza kutoka kwa Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere ni uwezo wake mkubwa wa kutambua kiini cha matatizo yaliyotukabili sisi kama binadamu na kama taifa changa baada ya uhuru na akawashawishi wenzake kuendesha nchi kwa falsafa ambayo ingesaidia kushughulikia kiini kile.

Â

Kwanza Mwalimu, alitambua kuwa Waafrika walikuwa wamepitia madhila mengi mno tokea wakati wa utumwa hadi ukoloni ambapo walidharauliwa, wakafedheheshwa, wakatumikishwa, wakanyonywa na wakati huo huo wakipuuzwa. Akatambua kuwa falsafa ambayo ingefaa kuongoza nchi ni ile ambayo ingewaongoza watu kutambua na kuthamini utu wa kila binadamu.

Â

Mwalimu alitambua pia kwamba mfumo wa dunia uliokuwepo wakati tunapata uhuru ulikwishatengeneza mirija mirefu ya wababe wa dunia kuendelea kuzinyonya nchi zilizokuwa zimejitawala.

Bado wababe wale walikodolea madini na rasilimali zingine muhimu kutoka bara hili na hawakuwa tayari kuona mirija yao ikikatwa hivihivi.

Â

Falsafa ya Mwalimu ililenga kumpa Mtanzania jeuri ya kutodharauliwa, kutodhalilishwa, kutonyonywa na kutokaliwa kichwani.

Mwalimu alilenga kumjengea Mtanzania fikra za kujiamini kwamba anaweza kujitegemea kwa lolote kama angetaka. Ni dhahiri kuwa bila uwezo wa kujitegemea huwezi kuishi na wajanja wengine usidharauliwe, usinyonywe na hata kupuuzwa kwani utaonekana juha.

Â

Na madhali kwa kipindi kirefu sasa tumekuwa tukiendesha nchi yetu bila misingi inayoelekezwa na falsafa ya utu, tumejikuta tukipiga hatua kwenda nyuma katika maeneo mengi ikilinganishwa na wakati wa Mwalimu.

Â

Tumekuwa tukirudi nyuma katika elimu kiasi kwamba, miaka ya 1990 karibu nusu ya watoto wa Tanzania walikuwa hawaandikishwi kwenda shule.

Wakati wa Mwalimu tulifikia pahala zaidi ya asilimia 95 ya watoto wetu wakawa wakiandikishwa shule, tena zenye walimu, vifaa na mahitaji mengine muhimu kama chakula.

Japokuwa yapo mawazo kuwa walimu wa UPE walichangia kushusha kiwango cha elimu, bado ualimu wa wakati ule ulikuwa na heshima.

Â

Leo hii utafiti unaonyesha kuwa karibu nusu ya walimu wote nchini wanatamani kukimbia fani yao. Kwa hiyo kama taifa tunaendesha mambo huku tukijiridhisha kuwa tutaleteana maisha bora katika mazingira ambayo asilimia karibu 50 ya walimu wetu wanafundisha bila kupenda, achilia mbali kuwa shule nyingi hazina maabara wala vifaa muhimu vya kufundishia, hivi hatutwangi maji kwenye kinu?

Â

Tukirejea katika sekta za kilimo, ufugaji na uvuvi (ambazo ziliajiri watu wengi wakati wakoloni wanaondoka) tunabaini kuwa zote zimezidi kuzorota.

Wakulima wanazidi kuwa maskini zaidi kadri ardhi yao inavyozidi kuchoka na wafugaji wengi wanaendelea kuishi maisha waliyoishi mababu wa mababu wao huku wakikabiliwa na tishio la kutoweka mifugo yao kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa.

Tujiulize hili wimbi la wafugaji maarufu kuhamia mijini kufanya shughuli za ulinzi na wakulima kuja kutembeza fulana tatu mijini limesababishwa na nini?

Â

Na hata katika masuala ya afya, tumepiga hatua nyingi sana nyuma. Zile kampeni kabambe za wakati ule za mtu ni afya na mafunzo mengine kupitia elimu ya watu wazima zilipunguza mno vifo na maradhi yaliyokuwa yakiwasumbua wananchi wengi.

Japokuwa kuna taarifa kwamba kampeni za kudhibiti Ukimwi na Malaria zinaonyesha matumaini, bado kuna ukweli kwamba fedha nyingi za wahisani zimetolewa kwa ajili ya utafiti, kampeni na matibabu ya eneo hilo.

Lakini maradhi kama kipindupindu ambayo yalipaswa kutokomezwa siku nyingi, yanaendelea kuua watu kwa sababu labda hakuna wafadhili wa kusaidia kutokomeza ugonjwa huo wa aibu.

Â

Lakini kama asilimia karibu 40 ya watoto wetu walio chini ya miaka mitano leo wanakuwa na utapia mlo na wanadumaa hata kiakili itakuwa si busara sana kushangaa ni kwa nini bado tunasumbuliwa na kipindupindu.

Hawa watoto wenye utapiamlo huwa wanakua na hata husoma na pia (kama alivyowahi kusema Idd Simba) kufikia kushika madaraka mbalimbali na kufanya maamuzi muhimu kwa mustakabali wa taifa letu.

Â

Hili si jambo la kupuuzia hata kidogo. Hili la nusu yetu kuwa tumedumaa akili likichanganywa na ukweli kwamba, tumepuuza elimu kwa muda mrefu kiasi kwamba kule wanafunzi wetu wengi wanakwenda kuhesabu madarasa na kuondoka na vyeti pasipo maarifa kamili na ujuzi wowote wa kubadili hali za maisha yao, lina majibu mazito kuhusu ni kwa nini leo tuna mgawo wa umeme.

Â

Tatizo la mgawo wa umeme si Richmond wala Dowans. Tatizo ni kiini ambacho Mwalimu Nyerere alijaribu kuelekeza fikra za wananchi kukibaini na kukishughulikia, lakini muda wake wa kufanya hivyo haukutosha.

Hata leo hii tukinunua, au kutaifisha, mitambo ya Dowans bado kiini cha tatizo kitabaki pale pale. Miaka karibu 50 baada ya uhuru, hata baada ya kuuza sana madini, viwanda, mashirika na kadhalika.

Hata kuvutia sana wawekezaji bado ni asilimia 12 tu ya wananchi inayofikiwa na umeme tena usio wa kutegemewa. Kwamba tuko radhi tutumie mabilioni kwa ajili ya starehe za kirasimu, lakini si kuelekeza fedha zetu kidogo katika vipaumbele kama umeme wa uhakika ambao ni muhimu mno kwa uchumi wa nchi. Tusilolijua litatusumbua.

http://www.mwananchi.co.tz/newsrids.asp?id=15390
 
Back
Top Bottom