Fanya Jambo Dogo Kuwasaidia Wasichana Hawa Wa Kitanzania(New Hope For Girls)

Makirita Amani

JF-Expert Member
Jun 6, 2012
1,781
3,074
Juzi jumapili (25/05/2014) nikiwa pamoja na marafiki tulipata nafasi ya kutembelea familia moja iliyojitolea kukaa na wasichana wanaoishi kwenye mazingira magumu.

Mama wa familia hiyo Bi. Consoler Eliya Wilbert alitupatia historia yake fupi na kile anachokifanya na ni kitu gani kilimsukuma kufanya anachofanya.

Kwa kifupi, Consoler wakati akiwa binti alipitia manyanyaso makubwa sana kutoka kwa ndugu aliokuwa anaishi nao. Aliteseka sana na kupitia vipigo vingi kitu ambacho kimemsababishia matatizo kwenye mgongo na hivyo kushindwa kufanya kazi ngumu.

Kutokana na matatizo yote aliyoyapitia alijiwekea ahadi kwamba iwapo hatokufa katika mateso hayo basi chochote kidogo atakachopata atawasaidia mabinti ambao wanapitia mazingira magumu kama aliyopitia yeye.

Hivi sasa consoler anaishi na mabinti 19 nyumbani kwake ambao wote wanatoka kwenye mazingira magumu sana, wengi ni yatima na wengine familia zao hazina msimamo na hivyo kujikuta mtaani. Kuacha mabinti hao 19 anaokaa nao nyumbani kwake, Consoler anawasaidia mabinti wengine zaidi ya 100 ambao huwa wanakwenda kwake kuchukua chakula na mahitaji mengine muhimu.

Katika familia yake Consoler anaishi na mume wake, watoto wao wamili wa kuzaa na hao mabinti wapatao 19
. Hiki ni moja ya vitu ambavyo nimeona vinafanywa na baadhi ya watanzania ambayo vina msaada mkubwa sana kwenye taifa letu. Consoler anafanya yote haya bila ya kupata msaada wa moja kwa moja kutoka serikalini au taasisi za wafadhili. Alianzisha kitu hiki kwa mapenzi yake mwenyewe na amekuwa akiendesha mradi huu kwa fedha kidogo anazopata na misaada kutoka kwa marafiki wanaoguswa na kile anachokifanya.

Tuliguswa sana na kitu hiki kizuri ambacho dada huyu ameamua kukifanya bila ya kutegemea kunufaika kwa njia yoyote ile. Consoler pia ameanzisha mradi mwingine wa kusaidia watoto wasiojua kusoma na kuandika. Anasema walifanya utafiti kidogo kwenye eneo la bonde la mto msimbazi na kugundua kuna mabinti wengi sana kati ya miaka 9 mpaka 13 ambao hawajapelekwa shule na hawajui kabisa kusoma na kuandika. Ametafuta eneo la darasa ambapo mabinti waliomaliza shule kupitia mradi wake wa kuwasaidia, wanawafundisha watoto hao wengine kusoma na kuandika.

Hiki ni kitu kikubwa sana kinachofanywa kwenye nchi yetu na mtu mmoja tu ambaye amejitolea maisha yake kuboresha maisha ya watu wengine.
Nakuomba wewe kama mtanzania kwa chochote ulicho nacho ugawe kidogo na kuwapatia mabinti hawa. Kwa chochote kidogo utakachotoa utaboresha maisha ya mabinti hawa kwa kiwango kikubwa sana.

Pamoja na moyo huu mzuri alionao Consola kwenye kuwasaidia mabinti kuna changamoto nyingi anazokutana nazo.
Kwanza kabisa kutokana na matatizo aliyopitia hawezi kufanya kazi yoyote inayohitaji muda hivyo yupo nyumbani muda wote na hana kazi. Mume wake ndio tegemeo kubwa kwake na kwa mabinti anaowasaidia.

Changamoto nyingine anazokutana nazo ni;
1. Udogo wa eneo na hivyo kushindwa kuchukua mabinti wengi zaidi ambao wanahitaji msaada wake.

2. Kodi ya nyumba kwani nyumba wanayoishi ni ya kupanga na kila mara wanapandishiwa kodi kitu ambacho hawawezi kukimudu.

3. Ada za shule za mabinti. Karibu mabinti wote wanakwenda shule na wengi wako kwenye shule za sekondari za binafsi. Wachache wamepata watu wa kuwasaidia ada ila bado wengi wanamtegemea yeye.

4. Hana ufadhili au chanzo chochote maalumu cha fedha anachotegemea ili kuwasaidia mabinti hawa.

5. Kushindwa kulipa walimu wa kufundisha mabinti ambao hawajui kusoma wala kuandika.

6. Vifaa vya upishi na shughuli nyingine za mikono kwa sababu ameanzisha mradi wa kupika kwenye semina mbalimbali.

7. Chakula, mavazi na mahitaji mengine muhimu kwa mabinti hawa.

Zipo changamoto nyingi sana ambazo Consoler alitueleza ambazo wewe kama mtanzania unaweza kumsaidia chochote kidogo ili akavuka changamoto hizi.

Kama upo dar es salaam unaweza kutembelea familia hii na kujifunza mambo mengi sana kutoka kwao. Familia hii inaishi Tabata, kufika hapo unapanda magari yanayoelekea tabata kimanga au segerea na kushuka kituo cha TABATA SHULE.


Kwa maelezo zaidi unaweza kuwasiliana na Consoler kwa mawasiliano yafuatayo;
Simu; 0715025565/0787025565 na email; consoler@newhopeforgirls.org
Hata kama upo mkoani unaweza kuwasiliana na Consoler na kuchangia chochote ulichoguswa kuchangia.

Kumbuka hakuna masikini sana ambaye hana cha kutoa na hakuna tajiri sana ambaye hana cha kupokea. Tuungane na mtanzania mwenzetu aliyeamua kuchukua hatua ya kuwasaidia wasichana walioko kwenye mazingira magumu.


Fanya jambo dogo kuboresha maisha ya wasichana hawa ambao ndio tegemeo la taifa letu.
Karibu sana, TUKO PAMOJA.
 
Kama taasis yake imesajiliwa anaweza kuomba Fedha kutoka halmashauri na balozi za jerumani, na Saudi. Balozi ya Korea wanatoa Fedha za kujenga nursery schools kwa CBOS
 
Kama taasis yake imesajiliwa anaweza kuomba Fedha kutoka halmashauri na balozi za jerumani, na Saudi. Balozi ya Korea wanatoa Fedha za kujenga nursery schools kwa CBOS

Habari mkuu, Unaweza kumpigia kwa namba zake hizo hapo juu ukamuelekeza vizuri kuhusiana na hili ulilosema hapa. Utakuwa umesaidia kwa kiasi kikubwa sana. Asante.
 
dah imenigusa ila kwa maono yangu tusimchangie fedha tu bali pia kumpa ushauri ambao utakua msingi katika kuwalea hawa mabinti
 
dah imenigusa ila kwa maono yangu tusimchangie fedha tu bali pia kumpa ushauri ambao utakua msingi katika kuwalea hawa mabinti

Ni kweli kabisa mkuu, ushauri wa kimawazo unahitajika sana. Unaweza kuwasiliana nae na pia hata kuwatembelea na kuwafundisha hao mabinti chochote kinachoweza kuwasaidia kwenye maisha.
 
Back
Top Bottom