Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,475
- 39,987
VIDEO YA KUAGWA MASHUJAA
Na. M. M. Mwanakijiji
Sikutaka kutoa maoni yoyote kwa siku kadhaa nione kama watawala wetu wanatambua kuwa vifo vya wanajeshi wetu wakiwa kazini ni kitendo cha kishujaa wakati wote. Kinachoniudhi kuwa tunaishi bila kutambua mashujaa; yaani wale wanaojitoa maisha yao ili kuokoa wenzao.
Alipokufa yule mwanamama mjeshi kwenye ile ajali nyingine ya ndege ni watu jeshini zaidi waliona kitendo hicho ni cha kishujaa na labda mimi ni mtu pekee niliyeandika kutambua damu hiyo ya binti wa kitanzania ikimwagika. Nikiwa na ndugu waliolitumikia JWTZ kwa uadilifu na wengine kumwaga damu katika utumishi najikuta kila wakati ninasisima ninaposikia vitu kama hivi vinatokea.
Habari hii ilivyoripotiwa imeripotiwa pasipo kuelewa kwa njia rahisi tu kuwa Rubani Meja Cuthbert Leguna na Luteni Andrew Kijangwa waliamua kufanya kitu cha kujitoa mhanga kwa kukwepesha ndege hiyo kuangukia makazi ya watu na kujaribu kutua barabarani. Na hata hapo barabarani walipoona kuna basi la Simba Mtoto na gari la Watalii huku ndege yao ikienda kuanguka walijitahidi kulikwepesha na katika kufanya hivyo wao pekee ndio wamekufa katika tukio hilo la kusikitisha lakini lenye kila chembe ya ushujaa.
Taifa lisilo na shukrani linachukulia tu kuwa ni ajali na "ajali haina kinga" kumbe wapiganaji wetu wamekinga ajali kubwa zaidi kwani leo tungekuwa na kilio kikubwa zaidi. Sijui kama Rais wenu, waziri mkuu wenu, au hata wabunge wenu wameonesha shukrani yoyote Bungeni au mahali pengine popote kwa kitendo hiki cha kishujaa. Yaani, waliona ni bora wao wawili wafe kuliko makumi au mamia kuangamia!
Nikiwa nimelengwa na machozi na nikitambua uzalendo huu wa hawa vijana wapiganaji ambao licha kupoteza ndugu, baba, kaka na watoto katika familia zao wamepoteza vile vile hazina kubwa ya ujuzi na utaalamu katika Jeshi letu, utaalamu ambao taifa linatumia kiasi kikubwa sana kupata. Wakati ndege ni rahisi kununua (wakiacha ufisadi kidogo) maisha yao na uzoefu wa ujuzi wao hauwezi kurudishwa kamwe.
Ninatoa shukrani kutoka familia moja ya kijeshi kwenda familia nyingine, Ninawapigia saluti wapiganaji hawa na kusema asante kwa kitendo chao cha kizalendo na kishujaa kupita kiasi. Wakati mafisadi wenu wanaendelea kutanua na kubishana nani ale nini zaidi hapa leo wanalala mautini wale ambao labda hata baada ya siku chache hawatakumbukwa, familia zao zitarudishwa kijijini, watoto wao watakosa elimu n.k n.k Laiti tungejua kusema asante kwa kafara hii ya utumishi.
Asante Meja Leguna
Asante Luteni Kijangwa
Majina yenu yatabakia moyoni..
Mungu Ibariki Afrika
Mungu Ibariki Tanzania
Mlale salama enyi wana wa Tanzania, mlale salama mashujaa!!
Saluti!
Attachments
Last edited by a moderator: