eti vigumu mwanamke kumwacha mwanaume wa zamani

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
Wiki iliyopita katika safu hii nilikumegea msomaji wangu kisa cha jamaa mmoja akitaka ushauri kuhusu mkewe anayempeleka puta, huku akilazimisha talaka na kisha siku chache baadaye anaomba mume amrejee. Kama siyo kigeugeu mwanamama huyu ni kitu gani?
Hata baada ya kumrejea, bibie, mama wa mtoto mmoja, ambaye alikiri kisa cha kuomba talaka kilitokana na bwana wa nje aliyemzuzua na kumtaka aombe talaka ili wakafunge naye ndoa.
Utakumbuka msomaji wangu mwishoni mwa makala ile niliuliza maswali ya kujadili kwamba je, mtu aliyeoa au kuolewa ambaye kabla alikuwa na mahusiano na mtu fulani, je, ni rahisi kuua mahusiano hayo? Au kwa maneno mepesi; Ukipata chungu kipya cha zamani utakitupa?
Naam. Wapo baadhi ya wasomaji waliosoma makala ile na kutuma maoni yao kupitia e-mail ya safu hii iliyoko mwishoni. Msomaji wa kwanza anawasilisha maoni yake kama ifuatavyo;
“Habari dada Flora, mimi ni mume wa mtu na nina watoto. Nachangia kidogo mada hiyo japo nimechelewa. Kinachomsumbua jamaa ni hali yake ya umasikini.
Zamani kidogo wanaume walisisitiziwa kuoa wanawake wanawali (vigoli). Mawifi walihakikisha kaka yao kachukua kitu kipya kabisa dada zangu walifanya hivyo.
Nijuavyo mimi na hasa uzoefu wangu kutokana na umri nilio nao, ni vigumu sana mwanamke kuachana na mwanaume ambaye alitembea naye na wakaachana bila kugombana.
Wanawake huwakumbuka sana watu wa kwanza kuanza nao mapenzi. Siyo hao tu, bali pia waliowahi kuwapenda tofauti na wanaume ambao wapenzi wao wa zamani wakishaolewa hawawatamani tena. Mfano mimi nawaonea kinyaa kabisa wanawake walioolewa.
Mshauri huyo jamaa atafute maisha, kisha atafute mke ambaye atakuwa wa kwake. Hii kuchangia mwanamke huyo kiruka njia asubiri Ukimwi. Dawa ya Babu Loliondo haijathibitishwa mpe anwani yangu pepe nimpe mfano LIVE. Waliojifanya kuwabembeleza, wanawake wawapende, wengi wameteketea, mwanamke habambelezwi huwa anampenda mtu mmoja tu hata kama ni maskini.
Nimewaona wanawake walioacha kazi zao za maana wakawafuata waume wanaoganga njaa na wakaishi nao kwa raha mustarehe. Mwanaume mwenye akili zake atapata kazi tu, acha hawa mazezeta wa mjini wanaokimbizana na mgambo wa jiji kila uchao.
Ni mimi baba mwenye furaha ya ndoa pekee hapa Dar, kwa sasa nami nasoma nchini Marekani, lakini sina Pressure na mke wangu. She loves me no matter what (mke wangu ananipenda kwa liwalo lolote). Hivi ndivyo anavyomalizia msomaji wetu huyu ambaye hakutaka jina lake litajwe kuhusu maoni yake.
Msomaji mwingine anaanza ujumbe wake namna hii; “Da Flora, ndoa ni ngumu endapo utakuwa hujui thamani yake. Huyu mama hajui thamani ya mume wake kwa hiyo hamfai wala asiumize kichwa kwani hatakuwa na furaha ijapokuwa anampenda. Maisha ni amani, huku furaha ikifuata sasa huyo mume wake kwa sasa hana amani maana muda wote anawaza kusalitiwa.
Hakuna ndoa ya aina hiyo na ni kweli ndoa ina umuhimu wake pale penye upendo wa kweli na inauma sana kuachana na mtu unayempenda sana na kumpa nafasi kubwa ndani ya nafsi yako. Ndoa inajengwa na heshima, upendo na kuvumiliana na vinapotoweka vitu hivi inakuja dharau, jeuri na kiburi.
Kipindi hiki ni kigumu sana inabidi usome nyakati je, mbele ya hapo kuna nini. Mimi kwa ushauri wangu aangalie anataka nini ndani ya maisha yake. Hiki ni kitu ambacho kimenikuta na hakika niliumia sana maana nilimuacha mke niliyempenda ila sasa nina amani namuomba Mungu anipe furaha”, anamalizia maoni yake msomaji wetu huyu.
Msomaji mwingine anaanza hivi;”Nampa pole sana kijana ambaye anachezewa na mke ambaye hana msimamo wa maisha wala hajui anachokitaka katika maisha yake. Nasaha yangu bora atengane naye kwani ipo hatari ya kumpeleka pabaya na mke ambaye anaonyesha wazi maslahi kayaweka mbele. Ajaribu sana kuikataza nafsi yake kumpenda mtu inaonyesha ni adui na anaweza kumsababishia janga kubwa wakati wowote. Bora aachane naye kishoka huyoo!
Wenu Mzee Salim.
Mwingine anasema, “Kila mtu anajua kupenda, ila inapofika hatua kama hii, sioni kama kuna utu katika hili. Huyu mwanamke amegeuka na kuwa mnyama na haoni umuhimu wa ndoa yake, huyu mwanamke anachezea maisha ya huyu bwana ila bwana huyu kwa upendo alio nao kwa mwanamke huyu, amekuwa kipofu.
Yaonyesha dhahiri kuwa mwanamke huyu hana mwelekeo wowote wa kuishi na bwana huyu, hivyo ni juu ya bwana huyu kuchukua maamuzi. Kumpenda kwako kusiwe kigezo na sababu ya kufa kwako. Nakushauri uamke hapo ulipolala”.
Msomaji mwingine anasema, “Mimi sioni haja ya huyu jamaa kupanic na kuchukua uamuzi huu na kuuacha ule na kukimbia huku na kule. Huyo ni mke na yupo kwenye himaya yako, chukua maamuzi kama mwanaume na usifanye pupa. Kaa chini fikiri mara mbili na utambue umuhimu wako katika maisha yako, kisha mgeukie mkeo na umwambie lile unaloona linafaa kwa manufaa yako na ya familia yako. Hakuna asiyelijua gonjwa lililopo sasa la ukimwi. Hivyo chukua uamuzi kuokoa maisha yako na usisikie ya ndugu wa mkeo. Wewe hutakuwa wa kwanza kuacha mke.
Mimi Devisie
Msomaji wangu nikuachie utafakari barua pepe hizo kujua maoni ya wenzetu hao na kama unao mchango mwingine unakaribishwa . Hadi wiki ijayo.
fwingia@yahoo.com
flora.wingia@guardian.co.tz
Wasalaam.
 
Back
Top Bottom