Dunia ikiwa inaadhimisha Siku ya Wakimbizi, ni kweli maisha ya wakimbizi yameboreshwa?

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,006
1,026
VCG111387645655.jpg

Pili Mwinyi

Kila ifikapo Juni 20, dunia inaungana kuadhimisha Siku ya Wakimbizi Duniani. Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilizindua rasmi siku hii mwaka 2000, na tangu wakati huo, jamii ya kimataifa inatumia siku hii kuangalia njia za kuboresha maisha ya wakimbizi.

Wengi wetu tunajua kwamba wakimbizi wanalazimika kuacha nyumba zao kwa sababu ya vita, ugaidi, au majanga mengine, lakini kukimbia nchi zao mara nyingi huwa ndio mwanzo wa safari ngumu mbele yao.

Wakimbizi wengi hujikuta wakiishi katika kambi hadi wapate makazi mapya, baadhi ya makazi hayo yakiwa ni hatari au hayana vifaa vya kutosha kwa ajili ya maisha ya muda mrefu. Licha ya hayo wakimbizi siku zote huwa hawana kauli katika nchi wanazohamia, na mchakato wa urasimu katika kutafuta makazi yao mapya unaweza kuchukua miaka mingi.

Migogoro ya wakimbizi duniani kote imechukua nafasi kubwa au imekuwa ikigonga vichwa vya habari katika miaka ya hivi karibuni, kwa hivyo ni muhimu zaidi sasa kuliko wakati wowote ule kutoa msaada na kuipa umuhimu Siku ya Wakimbizi Duniani.

Kauli mbiu ya mwaka huu ni "Kwa pamoja tunajiponya, tunajifunza na kung'aa, Upatikanaji wa huduma za afya na msaada wa kimatibabu huokoa maisha.” Chini ya kauli mbiu hii iliyotolewa na Umoja wa Mataifa, dunia itapata kushirikishwa zaidi hasa katika kuleta mabadiliko na kuwaondolea madhila wakimbizi.

Mkataba wa mwaka 1951 ambao ni kanuni inayopinga kuwarejesha wakimbizi nyumbani unaorodhesha haki na pia kusisitiza wajibu wa wakimbizi katika nchi wanazohifadhiwa. Kwa mujibu wa kanuni hii, mkimbizi hapaswi kurudishwa katika nchi ambayo anakabiliwa na vitisho vikali kwa maisha yake au uhuru wake. Wakimbizi ambao wanachukuliwa kama ni hatari kwa usalama wa nchi, au waliopatikana na hatia ya uhalifu mbaya, ama kuchukuliwa kama hatari kwa jamii, hawawezi kupata ulinzi kama huu.

Wakimbizi katika nchi mbalimbali huwa wanakabiliwa na manyanyaso na vitendo vikubwa vya dhuluma. Changamoto zinazoendelea kuwakumba katika nchi walizokimbilia, ni pamoja na kubaguliwa katika sehemu za utoaji huduma kama vile hospitalini na nyinginezo. Na kama haitoshi wanawake na wasichana mara kwa mara huwa wanyanyaswa kimwili na kingono.

Ni hivi majuzi tu tumekuwa tukisia habari kwamba Uingereza na Rwanda wameingia makubaliano ya kuwahamishia wakimbizi wanaoingia Uingereza kinyume cha sheria kwenda nchini Rwanda. Ingawa kwa mujibu wa makubaliano Rwanda itasaidiwa kifedha kuwahudumia wakimbizi hao, lakini tulitarajia kuona nchi kubwa kama Uingereza ikibeba wajibu na moyo wa kibinadamu, na sio kurusha mpira kwa nchi nyingine.

Hatua hii ya Serikali ya Uingereza imekosolewa vikali ikioneana ni kama inafanya biashara ya kuuza binadamu. Kwa kuona ubaya wa jambo hili, Mahakama ya Haki za Binaadamu ya Ulaya imeingia kwenye vuta nikuvute kubwa za kisheria na serikali ya Uingereza, ambao walitoa rufaa mfululizo zikilenga kuzuia hatua ya kufukuzwa watu kwenye orodha ya serikali.

Tunaweza kusema kwamba juhudi za watetezi hawa wa haki za binadamu zimezaa matunda baada ya Uingereza kusitisha safari ya ndege ya kwanza ya wakimbizi iliyokuwa imepangwa kufanyika Jumanne ya terehe 14. Hata hivyo Waziri wa Mambo ya Ndani wa Uingereza Priti Patel anasema nchi yake bado haijakata tamaa kwani inaendelea kujipanga upya kwa ajili ya safari nyingine.

China ikifuata moyo wa kibinadamu, baada ya kurejeshewa kiti chake halali katika Umoja wa Mataifa mwaka 1971, imekuwa mstari wa mbele kushirikiana bega kwa bega na Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Matifa (UNHCR) katika masuala ya wakimbizi.

Moja ya juhudi zake ni kuliunga mkono shirika hilo kutoa msaada wa kibinadamu kwa wakimbizi laki kadhaa katika Afrika, Asia na Mashariki ya Kati, na kuwanufaisha katika sekta za elimu, afya, makazi, vitu vya dharura, maji ya kunywa na chakula.

Mwezi Mei mwaka 2017 Wizara ya Biashara ya China na UNHCR zilitia saini Mkataba wa Ushirikiano wa kiuchumi na kiufundi kati ya China na UNHCR katika Mkutano wa Baraza la Ushirikiano wa Kimataifa wa “Ukanda Mmoja, Njia Moja”, ambapo serikali ya China ilitoa ahadi ya kutoa msaada wa dola za kimarekani milioni nane kwa ajili ya Mfuko wa Ushirikiano kati ya Kusini na Kusini. Wizara ya Biashara pia itatenga dola za kimarekani milioni mbili ili kuipa UNHCR katika juhudi zake za kuunga mkono shirika hilo kukabiliana na hali ya dharura.

Baada ya janga la COVID-19 kuibuka, China inashirikiana na UNHCR kutoa ufadhili kupitia mfuko wa Ushirikiano wa Kusini na Kusini kuwasaidia wakimbizi na watu waliokimbia makazi. Makampuni ya China pia yametoa msaada wa kukabiliana na janga hilo barani Afrika.

Mbali na hayo, Mfuko wa ulinzi wa viumbe anuwai na maendeleo ya kijani wa China (China Biodiversity Conservation and Green Development Foundation) umeshirikiana na UNHCR kuunga mkono mradi wa miaka mitatu wa nishati safi, ili kutoa mpango wa ufumbuzi wa suala la nishati safi kwa wakimbizi elfu 20 wa Afghanistan nchini Pakistan pamoja na jamii iliyowapokea nchini humo. China pia ni mchangiaji mkubwa wa shughuli za kibinadamu duniani za UNHCR.

Kadiri nguvu zake zinavyoendelea kuongezeka, ndivyo itakavyozidi kuonesha umuhimu wake katika utoaji wa misaada kwa wakimbizi duniani.
 
Back
Top Bottom