Francis12
JF-Expert Member
- Sep 30, 2016
- 7,533
- 22,276
Naamini Chadema watavuka Katika hili, haya hutokea taasisi inapokua
Na Dotto Bulendu
Kupishana mawazo ndani ya taasisi ni kitu ambacho kipo kote duniani,kikubwa kupishana huku kuwe kifalsafa, kiitikadi Na kimsimamo ili baada ya hatua hiyo kuifanye taasisi hiyo Kuwa imara zaidi.
Kupishana ndani ya taasisi hakujaanza na akina Halima Mdee hii leo, CHADEMA ilishawahi kuingia Kwenye mgogoro na Viongozi wake vinara na wengine wakatoka ndani ya CHADEMA na kutoka kwao hakukuidhoofisha CHADEMA na wala hakukuwa ishara ya udhaifu wa Kiuongozi.
Kupishana ndani ya CHADEMA kulisababisha akina Kaburu, Slaa, Zitto, Kitila n.k watoke CHADEMA lakini CHADEMA haikuwahi kufa zaidi ndiyo ikazidi kujijenga kutoka Mijini mpaka vijijini.
Zitto alipotoka CHADEMA haukuwa mwisho wake wa Kisiasa bali ndiyo ukawa mwendelezo wa kukua kwake Kisiasa na leo anaongoza Chama Kikuu cha Upinzani Visiwani Zanzibar.
Hata kabla CCM haijazaliwa,ndani ya TANU kulikuwa na mivutano mikubwa iliyosababisha baadhi ya makada wake mashuhuri na wenye nguvu kukimbia nchi na wengine kuwekwa kizuizini,baadhi ya makada waliopishana waziwazi na Mwalimu walikuwa akina Oscar Kambona,Fortunatus Masha, Christopher Kasanga Tumbo, James Mapalala, Kasela Bantu n.k
Kule Zanzibar pamoja na kusudio la kutaka kufutilia mbali kinachoitwa Uchaguzi wa vyama Vingi baada ya ule wa Mwaka 1963,ndani ya ASP na baadae CCM hakukuwahi Kuwa Salama bali watu walipishana kimsimamo,Wapo Wazanzibar walilazimika kuondoka Zanzibar na kuja Bara kufanya kazi Kwenye Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania baada ya kushindwana na Hayati Karume.
Mzee Aboud Jumbe yeye akiwa Kiongozi mkubwa ndani ya Chama na Rais wa Zanzibar aliendesha harakati za kubadili Muundo wa Muungano, Kama wasingekuwa akina Maalim Seif labda leo kusingekuwa na Tanzania, jaribio la Mzee Jumbe lilisababisha Mwaka 1984 avuliwe madaraka ya Urais wa Zanzibar na nafasi ndani ya CCM na kupelekwa kizuizini Kigamboni DSM. Lakini haikuwa kifo cha CCM wala haikutafsiriwa Kama udhaifu wa Uongozi wa Mwalimu.
Hata baada ya Uchaguzi wa Mwaka 1985, Wazanzibar wengi na wana CCM waliamini aliyekuwa Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Maalim Seif Sharif atapigishwa na Chama na kuwania Urais wa Zanzibar, lakini CCM walimkata Maalim aliyekuwa na nguvu Zanzibar wakampitisha AbdulWakil, uamuzi huu ulipingwa na wana CCM wengi pamoja na waZanzibar Hali iliyosababisha wengi kususia Uchaguzi wa Mwaka 1985.
Baada ya Uchaguzi CCM ikianza mchakato wa Kuwasaka iliyowaita wazi ndani ya Chama na ikawatimua akina Maalim Seif,Juma Duni, Hamad Rashid n.k,hili halikuonekana Kuwa ni udhaifu ndani ya CCM na Serikali bali likizidi kuijenga CCM.
Mwanzoni mwa miaka ya 90,aliyekuwa Katibu Mkuu wa CCM Marehemu Horace Kolimba alizungumza hadharani Kuwa CCM imepoteza Dira(huyu Ni mtendaji mkuu wa Chama), alihojiwa Kwa Maneno yake hayo lakini kupishana huku hakukuitwa kifo cha CCM bali kuliwafanya CCM kujiimarisha zaidi.
Mwaka 1993,ndani ya Bunge la CCM na ndani ya Baraza la wawakilishi kuliibuka hoja mbili,Zanzibar walifikia azimio la kujiunga na OIC huku bara kundi la wabunge lilianzisha vuguvugu la kuirejesha Tanganyika, hoja ambayo Ni kinyume na Msimamo wa chama,Viguvugu hili lilisababisha aliyekuwa Waziri Mkuu John Malecela katuhumiwa vikali na Mwalimu Nyerere na kulazimishwa aachie ngazi nafasi ya Uwaziri Mkuu.
Hata Mwaka 1995,Jakaya Kikwete alimlaumu aliyekuwa Katibu Mkuu wake Marehemu Lawrence Gama Kuwa anamfanyia rafu Kwenye mbio zake, Jakaya alisema hana imani na Katibu Mkuu(jiulize unawezaje kukosa imani na Mtendaji mkuu wa Chama?)kupishana Kwenye taasisi kupo tu.
Wengi waliamini mgogoro wa NCCR Mageuza Mara baada ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 1995, utaiua kabisa NCCR,lakini ndiyo imepoteza nguvu yake iliyokuwa nayo wakati wa Mrema lakini bado Wapo.
Kupishana ndani ya Taasisi kulisababisha CCM kuwapoteza Kwa mkupuo Mawaziri wakuu wake wawili, Edward Lowasa na Fredrick Sumaye ambao walifuatwa na makada wa CCM wakiwemo baadhi ya wenyeviti wa mikoa lakini CCM haikufa.
Baada ya Uchaguzi CCM ili fukuza Mwenyekiti wake wa jumuiya wa Wanawake Bi Sofia Simba na baadae ikamtimua kada wake Bernard Membe kutokana na kutofautiana ndani ya taasisi lakini CCM haikufa.
CUF iliwatumia Wabunge wa Viti maalum, ikakumbwa na mgogoro mkubwa wa kiuongozi iliosababisha kundi kubwa la Viongozi na wanachama wake kuachana na CUF, lakini Kwenye Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2020 CUF imepata jimbo Moja upande wa Bara, pamoja Na Kwamba kweli CUF imepoteza nguvu yake hususani visiwani Zanzibar.
My take
Kupishana huku kwa Viongozi wa Chadema kutumike kuwajenga zaidi na Zaidi, walivuka Kwenye mengi naamini na hili watavuka.
Bado naamini Halima Mdee ana nafasi ndani ya Chama alichokulia, Halima amekaa Chadema kama mwanachama kwa zaidi ya miaka 16 ana miaka zaidi ya 20 ya kufanya Siasa.
Kama Bi Sofia Simba aliteleza, akatafakari na baadae kukiri makosa na kurejeshwa ndani ya CCM,Bado naiona nafasi ya Halima na wenzake ndani ya Chadema.
Hakuna aliyewahi amini kama ipo siku Zitto atakaa na Chadema kupanga mikakati dhidi ya CCM, lakini Zitto Mwaka 2020 aliungana na Chadema dhidi ya CCM.
Taasisi inapokuwa, mambo ya kupishana huwa ni mambo ya kutarajia, ndani ya taasisi mbali na Maono na Dira ya taasisi, pia waliomo ndani nao wana Dira na Maono yao binafsi.
Bado naamini tofauti hizi zitawafanya Chadema kuwa imara zaidi ya jana.