Doa la vipepeo (Jasusi wa kweli hashindwi na codes za jasusi muovu)

Kudo

JF-Expert Member
Nov 2, 2017
1,809
6,081
RIWAYA; DOA LA VIPEPEO

NA; BAHATI MWAMBA

SIMU; 0758573660.



-----1-----

Ulikuwa ni muda sahihi kwa kila mmoja kurejea nyumbani, muda ambao jua lilikuwa limeanza kuiacha Mashariki yake na kwenda kwa mchepuko wake bi. Magharibi. Harakati za hapa na pale zilianza kufungwa, watu walianza kujipa uchovu ili mradi tu, warejee majumbani mwao kupambana na masimango ya nyumba zao. Wale wenye gubu, ilikuwa ni wakati wa majuto kwa panya na mbu ambao huishia kuona na kusikia vibweka usiku kucha, kiasi cha kuwanyima uhuru wa kubarizi kwenye vyandarua na kuta za baridi.

Muda huu ni muda ambao huko mwituni, wanyama wakali nao walikuwa wanafunga hesabu za mawindo, huku wanyonge wa pori wakipumua na kulishukuru jua kuzamia kwa mchepuko wake, huku wakilaani ukali wa mke halali mashariki; licha ya kuwapa kula,mwanga na virutubisho, ila aliwachosha kwa kuwapa adhabu ya hekaheka za kunusuru uhai wao. Lakini licha ya kushukuru huko, wapo wanyama ambao muda huo kwao, ndio muda sahihi wa kuingia mawindoni, kuvizia na kujipatia shibe.
Hali hii ilikuwa ni furaha kwa bwana jua, ambae alifurahi kuona kwake na, mchepuko wake kunafaidisha viumbe wa Mungu kwa namna tofauti, hivyo kufanya iwe ni ratiba yake ya kila siku na wakati wote.

Wakati jua anazidi kujichimbia nyumba ndogo, Duniani kulikuwa na mambo mengi yanatokea, usiku huu wa rasharasha, usiku ambao haujaenda eda, kulikuwa na mwanamichezo mmoja, akijaribu kumalizia muda wake wa mazoezi ndani kwake. Hakuonekana kuwa na wasiwasi hata kidogo, alipiga balizi, kisha akapiga miinuko kadhaa, alojinyoosha na kujipinda kwa utalaamu, huku akiacha viungo vyake vikubali kwa kutoa sauti ya mvunjiko.

Mwanamichezo huyu, alikuwa ni kocha wa timu ya vijana ya Azan, timu ambayo ilikuwa inafanya vyema chini ya mkufunzi huyo raia wa Burundi. Makazi yake yalikuwa Sinza. Alikuwa akiishi kwenye nyumba ya waajiri wake ambao walikuwa ni kampuni ya Azan. Ilikuwa nyumba nzuri yenye hadhi yake, nyumba iliozungushiwa ukuta mrefu na juu yake kukapita nyaya za umeme.

Kocha huyu licha ya kuishi nyumba nzuri na kubwa, lakini hakuwahi kuwa na mke wala mtoto na, hakuna aliewahi kujua kuhusu familia yake.

Aliishi peke yake.

Aliendelea na mazoezi yake, lakini kwenye ukuta wake wenye nyaya za umeme, kulikuwa na kiumbe mwenye moyo wa nyama na miguu miwili yenye vidole vitano. Mtu yule alikuwa anamalizia kuhifadhi mkasi mdogo aliotumia kukata nyaya zile na sasa alikuwa amesimama wima akitizama upande wa mlango wa nyumba ile.

Mtu yule alikuwa amevaa mavazi meusi, kuanzia juu hadi chini kwenye raba zake. Alipokwisha kuhakikisha hakuna anaemuona pale ukutani, aliruka sarakasi moja kavu na kutua chini bila kutoa ukelele, kisha alipiga hatua fupi fupi kama vile alitarajia kuona jambo uani pale. Mtu yule hakunyoosha upande wa mlango uliokuwa wazi, bali alipita upande wa nyuma wa nyumba ile, kisha alitumia mlango wa jikoni kuingia ndani ya nyumba ile.

Muda wote huo, kocha hakujua yanayojiri, wala kuhisi kuna mtu wa ajabu atakuwa kamtembelea ndani kwake. Aliendelea kupiga zoezi jepesi, aliporidhika alielekea chumbani kwake na alipotoka, alikuwa amevaa taulo tu akielekea bafuni.

Wakati yeye akielekea bafuni,mgeni wake yeye alielekea sebuleni,ambapo alichukua simu iliokuwa mezani na kuipachika kwenye chaji na kuwasha,kisha alikaa nyuma ya jokofu kubwa na kutulia kimya.

Kwa nini alifanya vile, hakuna aliejua.

Kocha wa timu ya Azan alipotoka kuoga, alipitiliza chumbani kwake, huko hakukaa sana alirejea sebuleni, ambapo alianza kutafuta kitu, mara akasita na kushangaa.

Hakuwa ameweka simu yake kwenye chaji, alishangaa imejiweka vipi pale na yeye anajua aliiacha mezani.

Ajabu hii!.
Aliifuata simu ile, nayo ikaanza kuita. Kocha aliruka nyuma na kutoa macho kama teja aliefumaniwa.

Aliiogopa simu yake mwenyewe.

Simu ile iliita na kukata.

Kocha bado alikuwa anajaribu kuweka kumbukumbu zake sawa, hakuwa yeye alieweka pale ile simu. Taratibu alianza kuisogelea tena, mara ikaita tena.

Wakati huu aliamua kuipokea, ilikuwa simu ya mmoja wa waajiri wake.

Kocha alikuwa katikati ya maongezi, hata wakati mgeni wake alipotoka mafichoni, yeye hakuwa na habari kabisa, aliendelea kupanga mikakati ya timu yake kusafiri mkoani kwa ajili ya mchezo wa kujipima nguvu na timu moja maarufu.

Kocha alistuka akishikwa nyuma ya shingo na mkono ambao ulikuwa umevaa glavu. Alipojaribu kujitikisa, alipigwa teke la mgongo na kumfanya abinukie mbele, na hilo likawa kosa, mana mgeni alimbinua shingo na kukaa kama mtoto analazimishiwa uji wa chumvi.

Kila alipojaribu kujitikisa, hakupata sehemu ya kushika ili ajinasue na kabali ile matata.

Kocha alianza kuvuta pumzi kwa nguvu, hilo ndilo lilitegemewa na mgeni, kwani alizidi kumbinua kocha kwa kumwekea goti katikati ya uti wa mgongo.

Kocha alishindwa kuhimili kabali ile ya aina yake, aliaza kuishiwa pumzi huku macho yake yakianza kuona kiza kizito, huku masikio yake yakianza kusikia kelele za kuzomea za mashabiki wa timu alizozifunga.

Dakika mbili badae, mgeni alikuwa anamlaza chini taratibu, kisha alichukua simu na kuirejesha tena kwenye chaji, kisha alimvuta kocha hadi karibu na simu, kisha alimuinua na kumshikisha simu ile na kuipachika sikioni.

Alipohakikisha maiti ya kocha imeshika vyema simu ile, aliingia mfukoni mwake na kutoa kitu kidogo mithili ya punje ya mtama na kuipachika kwenye spika ya simu. Alipomaliza alisogea pembeni kidogo na kubonyeza saa yake, punde ukatokea mlipuko wa kiasi kidogo, lakini ulikuwa ni mlipuko uliobomoa kichwa cha kocha kuanzia upande wa kushoto kwenda juu na kufanya awe kama papai lilokatwa kipande.

Damu ilianza kutoka, na kusambaa hovyo pale ndani. Mgeni muuaji alianza kuondoka ndani ya nyumba ile, huku akiwa ameua bila kuacha alama ya ushahidi na hiyo ilikuwa ni sheria namba moja. Na kwa kifo cha kocha, maofisa wangeishia kujua alilipukiwa na simu wakati anaongea na simu ikiwa chaji. Muaji akiwa mbali na hisia feki za maaskari.

Wakati muuaji anaondoka ndani ya nyumba ya kocha, kulikuwa na mtu mwingine anaingia pale, akiwa amevaa sawa na yule alietoka, mtu huyu yeye alikuwa ni mfupi tofauti na yule wa mwanzo. Aliingia ndani ya nyumba ile kupitia dirishani,alipofika aliishia kukutana na maiti ya kocha ikiwa na simu iliolipuka pembeni yake.
Mtu yule alitoa simu janja yake na kupiga picha moja, kisha alitoa kibahasha kidogo sana na kukirusha chini ya uvungu.
Kibahasha kile kilikuwa kimeandikwa herufi moja iliochanganywa na namba. Ilisomeka hivi “F3”,Kisha aliondoka mle ndani kwa kupita njia tofauti na alioingilia.

Nyumba ya kocha ilikuwa imetembelewa na watu wawili, huku mmoja akiua na mwingine akiacha ujumbe wenye maana aliojua yeye, na dhahiri alieua hakujua kama ameonwa na mtu alieacha ujumbe.

Lakini kwa nini huyu aue na huyu aache ujumbe, kwanini?..


*****

Nb; Riwaya hii itaanza kuuzika kuanzia jumamosi ya wiki hii....

Ahsanteni nyote mlioshirikiana nami kwa kidogo mlichonacho,ahsanteni kwa wote mlionunua riwaya zilizopita na zitakazokuja...
Na kwa kidogo hicho, nimefanikiwa kupangiwa tarehe ya upasuaji ili kuondoa Figo ilioharibika.

Ahsanteni sana na karibuni kwa kazi hii mpya.
 
RIWAYA; DOA LA VIPEPEO

NA; BAHATI MWAMBA

SIMU; 0758573660


SEHEMU YA PILI



Nyumba ya kocha ilikuwa imetembelewa na watu wawili, huku mmoja akiua na mwingine akiacha ujumbe wenye maana aliojua yeye, na dhahiri alieua hakujua kama ameonwa na mtu alieacha ujumbe.

Lakini kwa nini huyu aue na huyu aache ujumbe, kwanini?

Hakuna aliejua sababu zaidi ya wao wahusika wenyewe.

Mtu wa pili kuingia nyumbani kwa kocha, ambae ndie mtu wa mwisho kutoka nyumbani kwa kocha, yeye aliamua kuendelea na ziara yake jirani na maeneo yale. Kulikuwa na nyumba moja ambayo alihitaji kuitembelea usiku ule. Mtu huyu ni kama hakujali kabisa kile alichokiona nyumbani kwa kocha.

Mtu huyu alipofika usawa wa nyumba alioikusudia, aligeuka kushoto na kulia kutazama kama kuna mtu yeyote aliekuwa anamfuatilia. Alipohakikisha hakuna mtu, alijongea taratibu na kuufikia ukuta, aliutazama kwa sekunde kadhaa, kisha akatoa glavu na kuzivaa. Alipomaliza alizijaribu kwa kuushika ukuta, alipohakikisha zinafaa kwa kazi alioikusudia, alianza kuukwea ukuta ule huku akisaidiwa glavu zile maalumu kwa kupandia kuta na miamba mirefu.

Tofauti ya ukuta huu na ule wa kocha, ukuta huu ulikuwa unavipande vingi vya chupa kwa juu, hivyo alipofika juu, alitulia kidogo na kujivuta kwa kasi hadi alipotua chini na kuachia ukelele mdogo usiostua. Alifanya vile kukwepa kudhurika na chupa zile.

Alijinyanyua na kutembea bila wasiwasi, macho yake yalikuwa sambamba na dirisha moja alilokuwa amelikusudia kabla na baada ya kuingia pale. Ni dhahiri aliijua nyumba ile.
Hakuhangaika na kukwepa taa zilizokuwa zinawaka sebuleni, wala hakutaka kuhadaika na kelele za watoto waliokuwa wakitizama filamu za Tom na Jerry.

Yeye alikusudia kuingia bila kuwastua wale watoto ama mtu yeyote aliekuwa pale sebuleni.

Alipolifikia dirisha lile, alijaribu kusukuma kioo lakini kilikuwa kimefungwa kwa ndani, haraka alingiza mkono mfukoni mwake na kutoa chuma kidogo chenye muundo wa bikari, kisha alikapachika kwenye kioo na kuzungusha kwa duara, aliporidhika alikirudisha mfukoni mwake na kukivuta upande wake kipande cha kioo alichokata. Alipokwishakitoa, aliingiza mkono na kufyatua kabali ya kioo na kukisukuma pembeni, kisha alipita na kuingia ndani, ambapo alijikuta akitokea jikoni na ndio ilikuwa kusudio lake.

Kutokea pale jikoni, kushoto kwake kulikuwa na korido ambapo ukiifuata utatokea kwenye chumba kikubwa cha mmiliki wa nyumba ile.
Mtu yule alitembea kwa hatua za kunyata na kisha aliishia mlangoni mwa chumba alichokikusudia.

Alitulia kidogo na kusikiliza, aligundua kuna mtu ndani ya chumba kile, ni kama ambavyo alikuwa anajua kuhusu ratiba ya pale ndani ya mtu aliemfuata.

Aligonga kidogo na kutulia. Kukawa kimya.

Aligonga tena na mara hii kwa nguvu kidogo.

Mara ikasikika sauti ya mwanamke pale ndani, ikimruhusu aingie.

Ni dhahiri mwenyeji wa chumba kile alijua ni watoto au mfanyakazi ndie anaehitaji kuingia.

Mgongaji alitabasamu kiupande, kisha aliusukuma mlango taratibu na kuingia ndani, ambapo alikutana na mwanamke mwenye umri wa kukadiria miaka sitini kasoro moja hivi. Mwanamke yule alionekana mrembo licha ya ngozi yake kuanza kupukutisha nyama za urijali.

Mwanamama yule alitoa macho ya kuhoji, huku akiwa ameshika taulo lake akishindwa kumalizia kuusitiri utu wake.

“Wewe ni nani na umeingiaje hapa!” Mama alihoji kwa kigugumizi cha woga.
Badala yake hakupata jibu, bali mtu yule alikisogelea kitenza mbali na kuwasha radio na kuweka sauti ya juu kidogo.

Mama yule dhahiri alijua mambo si mambo, haraka aliachia taulo lake hadi chini na kubaki mtupu, lakini hakujali,mikono yake yenye kasi ilikuwa inaiwahi bastola yake kitandani, lakini kasi ya mgeni ilikuwa kubwa na kumsukuma kidogo kumpotezea mwelekeo,mama hakutaka kukubali kirahisi, alitaka kujipambania, lakini aliwahiwa kwa kofi zito usoni,kofi lilomtoa kwenye ufahamu wake kwa sekunde kadhaa na hata aliporudi kwenye utimamu alikutana na kitu ambacho hakukitarajia. Mgeni wake alikuwa ameshika chupa ya marashi anayojipulizia mwili mwake.
Mtu yule alikuwa anayapuliza marashi yale usoni pake na kwa kuwa halikuwa tukio la kutegemea, alijikuta akivuta pumzi nyingi ili kukwepa kile alichohisi mgeni wake alikikusudia, lakini alikuwa amechelewa sana, kwani alipovuta pumzi, alivuta harufu kali ya marashi. Alianza kukohoa hovyo huku akijaribu kuzuia asivute harufu kali ya marashi, lakini haikusaidia, alikuwa amevuta harufu nyingi kiasi koo lilikauka na hata majimaji yanayokaa puani kulainisha vinyweleo,yalikuwa yamekimbia kwa adha ile.

Mgeni alikuwa na hakika na kazi yake, hivyo hakutaka kuendelea kuhangaika na mwanamke yule aliekuwa mtupu na utu uzima wake mbele ya kijana yule mdogo aliekuwa amefunika uso wake kwa kitambaa maalumu.

Mwanamke yule alizidi kupambania uhai wake, huku dhahiri akionekana kuhitaji kunywa maji ili kupooza koo lililokuwa limekauka na pua zikiwa kavu na zilizoenea harufu ya manukato ya bei kubwa.

Mtu yule alitoa kibahasha kidogo kilichokuwa na sawa na bahasha aliokuwa ameiacha nyumbani kwa kocha. Bahasha hii pia ilikuwa na herufi moja na namba “F3”. Bahasha ile aliitupa uvunguni mwa kitanda na alianza kuondoka, lakini ni kama alikumbuka kitu, haraka alirudi na kuinama uvunguni, ambapo aliitoa ile bahasha, kisha aliandika namba mbili tu na kuitupa tena kule uvunguni. Alipomaliza aligeuka upande ule ambao alikuwa mwanamke akijitahidi kukohoa ili aweke sawa koo lake.

Jamaa aliona picha kubwa ikiwa ukutani, picha ilikuwa ya mwanamama yule akiwa kwenye mavazi ya kipolisi yaliojaa nyota begani.

Ni kama hakuijali picha ile, badala yake aliondoka na kupitia njia ile ile aliokuwa amekujia.

Lakini mtu yule alikuwa anajua kabisa, si rahisi kujua yule mwanamke ambae alikuwa ni mstaafu wa jeshi la polisi, atakuwa ameuawa.

Kitu kimoja alichohakikisha ni kuwa mauaji ya kocha alioyashuhudia, yanaendana sawa na mauaji alioyafanya yeye kwa msataafu yule na afisa habari wa timu ya Azan.

Muuaji alitokomea huku nyuma akiacha msiba mzito na wenye utata mwingi, lakini ulikuja kuumiza vichwa vya watu kwa namna tofauti tofauti. Kuna wale ambao hawakukitegemea, lakini wapo waliokitegemea. Lakini ilikuwa ni kizungumkuti zaidi kwa idara ya usalama, ambayo ilishindwa kujua kama yale mauaji yalikuwa yanahusiana ama ni tofauti, lakini pia haikuonekana kuwa ni mauaji, ni kama kocha alilipukiwa na simu huku mstaafu akivuta hewa nyingi ya manukato kiasi alishindwa kupumua vyema.

Lakini kilichostua mamlaka za ulinzi na usalama ni jumbe zenye mfanano, zilizokutwa kwenye maeneo ya vifo vilipotokea, lakini pia vifo kuwahusu viongozi wa timu moja.

Walakini ukajaa, utata ukaibuka, mauaji yaliongezeka na fumbo likasilia kwenye herufi na namba zinazoachwa na muuaji ama wauaji.

Suala likawa gumu kwa jeshi la polisi, hivyo faili la kesi likatua kwa kutengo maalumu chini ya kamishina Zenge wa Zenge na hapo ndipo ukawa mchezo wa vipepeo.
 
RIWAYA; DOA LA VIPEPEO
NA; BAHATI MWAMBA
SIMU; 0758573660 SEHEMU YA PILI
Nyumba ya kocha ilikuwa imetembelewa na watu wawili, huku mmoja akiua na mwingine akiacha ujumbe wenye maana aliojua yeye, na dhahiri alieua hakujua kama ameonwa na mtu alieacha ujumbe.
Lakini kwa nini huyu aue na huyu aache ujumbe, kwanini? Hakuna aliejua sababu zaidi ya wao wahusika wenyewe. Mtu wa pili kuingia nyumbani kwa kocha, ambae ndie mtu wa mwisho kutoka nyumbani kwa kocha, yeye aliamua kuendelea na ziara yake jirani na maeneo yale. Kulikuwa na nyumba moja ambayo alihitaji kuitembelea usiku ule. Mtu huyu ni kama hakujali kabisa kile alichokiona nyumbani kwa kocha. Mtu huyu alipofika usawa wa nyumba alioikusudia, aligeuka kushoto na kulia kutazama kama kuna mtu yeyote aliekuwa anamfuatilia. Alipohakikisha hakuna mtu, alijongea taratibu na kuufikia ukuta, aliutazama kwa sekunde kadhaa, kisha akatoa glavu na kuzivaa. Alipomaliza alizijaribu kwa kuushika ukuta, alipohakikisha zinafaa kwa kazi alioikusudia, alianza kuukwea ukuta ule huku akisaidiwa glavu zile maalumu kwa kupandia kuta na miamba mirefu.
Tofauti ya ukuta huu na ule wa kocha, ukuta huu ulikuwa unavipande vingi vya chupa kwa juu, hivyo alipofika juu, alitulia kidogo na kujivuta kwa kasi hadi alipotua chini na kuachia ukelele mdogo usiostua. Alifanya vile kukwepa kudhurika na chupa zile. Alijinyanyua na kutembea bila wasiwasi, macho yake yalikuwa sambamba na dirisha moja alilokuwa amelikusudia kabla na baada ya kuingia pale. Ni dhahiri aliijua nyumba ile.
Hakuhangaika na kukwepa taa zilizokuwa zinawaka sebuleni, wala hakutaka kuhadaika na kelele za watoto waliokuwa wakitizama filamu za Tom na Jerry.
Yeye alikusudia kuingia bila kuwastua wale watoto ama mtu yeyote aliekuwa pale sebuleni.
Alipolifikia dirisha lile, alijaribu kusukuma kioo lakini kilikuwa kimefungwa kwa ndani, haraka alingiza mkono mfukoni mwake na kutoa chuma kidogo chenye muundo wa bikari, kisha alikapachika kwenye kioo na kuzungusha kwa duara, aliporidhika alikirudisha mfukoni mwake na kukivuta upande wake kipande cha kioo alichokata. Alipokwishakitoa, aliingiza mkono na kufyatua kabali ya kioo na kukisukuma pembeni, kisha alipita na kuingia ndani, ambapo alijikuta akitokea jikoni na ndio ilikuwa kusudio lake.
Kutokea pale jikoni, kushoto kwake kulikuwa na korido ambapo ukiifuata utatokea kwenye chumba kikubwa cha mmiliki wa nyumba ile.
Mtu yule alitembea kwa hatua za kunyata na kisha aliishia mlangoni mwa chumba alichokikusudia.
Alitulia kidogo na kusikiliza, aligundua kuna mtu ndani ya chumba kile, ni kama ambavyo alikuwa anajua kuhusu ratiba ya pale ndani ya mtu aliemfuata.
Aligonga kidogo na kutulia. Kukawa kimya.
Aligonga tena na mara hii kwa nguvu kidogo.
Mara ikasikika sauti ya mwanamke pale ndani, ikimruhusu aingie.
Ni dhahiri mwenyeji wa chumba kile alijua ni watoto au mfanyakazi ndie anaehitaji kuingia.
Mgongaji alitabasamu kiupande, kisha aliusukuma mlango taratibu na kuingia ndani, ambapo alikutana na mwanamke mwenye umri wa kukadiria miaka sitini kasoro moja hivi. Mwanamke yule alionekana mrembo licha ya ngozi yake kuanza kupukutisha nyama za urijali.
Mwanamama yule alitoa macho ya kuhoji, huku akiwa ameshika taulo lake akishindwa kumalizia kuusitiri utu wake.
“Wewe ni nani na umeingiaje hapa!” Mama alihoji kwa kigugumizi cha woga. Badala yake hakupata jibu, bali mtu yule alikisogelea kitenza mbali na kuwasha radio na kuweka sauti ya juu kidogo.
Mama yule dhahiri alijua mambo si mambo, haraka aliachia taulo lake hadi chini na kubaki mtupu, lakini hakujali,mikono yake yenye kasi ilikuwa inaiwahi bastola yake kitandani, lakini kasi ya mgeni ilikuwa kubwa na kumsukuma kidogo kumpotezea mwelekeo,mama hakutaka kukubali kirahisi, alitaka kujipambania, lakini aliwahiwa kwa kofi zito usoni,kofi lilomtoa kwenye ufahamu wake kwa sekunde kadhaa na hata aliporudi kwenye utimamu alikutana na kitu ambacho hakukitarajia. Mgeni wake alikuwa ameshika chupa ya marashi anayojipulizia mwili mwake.
Mtu yule alikuwa anayapuliza marashi yale usoni pake na kwa kuwa halikuwa tukio la kutegemea, alijikuta akivuta pumzi nyingi ili kukwepa kile alichohisi mgeni wake alikikusudia, lakini alikuwa amechelewa sana, kwani alipovuta pumzi, alivuta harufu kali ya marashi. Alianza kukohoa hovyo huku akijaribu kuzuia asivute harufu kali ya marashi, lakini haikusaidia, alikuwa amevuta harufu nyingi kiasi koo lilikauka na hata majimaji yanayokaa puani kulainisha vinyweleo,yalikuwa yamekimbia kwa adha ile.
Mgeni alikuwa na hakika na kazi yake, hivyo hakutaka kuendelea kuhangaika na mwanamke yule aliekuwa mtupu na utu uzima wake mbele ya kijana yule mdogo aliekuwa amefunika uso wake kwa kitambaa maalumu.
Mwanamke yule alizidi kupambania uhai wake, huku dhahiri akionekana kuhitaji kunywa maji ili kupooza koo lililokuwa limekauka na pua zikiwa kavu na zilizoenea harufu ya manukato ya bei kubwa.
Mtu yule alitoa kibahasha kidogo kilichokuwa na sawa na bahasha aliokuwa ameiacha nyumbani kwa kocha. Bahasha hii pia ilikuwa na herufi moja na namba “F3”. Bahasha ile aliitupa uvunguni mwa kitanda na alianza kuondoka, lakini ni kama alikumbuka kitu, haraka alirudi na kuinama uvunguni, ambapo aliitoa ile bahasha, kisha aliandika namba mbili tu na kuitupa tena kule uvunguni. Alipomaliza aligeuka upande ule ambao alikuwa mwanamke akijitahidi kukohoa ili aweke sawa koo lake.
Jamaa aliona picha kubwa ikiwa ukutani, picha ilikuwa ya mwanamama yule akiwa kwenye mavazi ya kipolisi yaliojaa nyota begani.
Ni kama hakuijali picha ile, badala yake aliondoka na kupitia njia ile ile aliokuwa amekujia.
Lakini mtu yule alikuwa anajua kabisa, si rahisi kujua yule mwanamke ambae alikuwa ni mstaafu wa jeshi la polisi, atakuwa ameuawa. Kitu kimoja alichohakikisha ni kuwa mauaji ya kocha alioyashuhudia, yanaendana sawa na mauaji alioyafanya yeye kwa msataafu yule na afisa habari wa timu ya Azan.
Muuaji alitokomea huku nyuma akiacha msiba mzito na wenye utata mwingi, lakini ulikuja kuumiza vichwa vya watu kwa namna tofauti tofauti. Kuna wale ambao hawakukitegemea, lakini wapo waliokitegemea. Lakini ilikuwa ni kizungumkuti zaidi kwa idara ya usalama, ambayo ilishindwa kujua kama yale mauaji yalikuwa yanahusiana ama ni tofauti, lakini pia haikuonekana kuwa ni mauaji, ni kama kocha alilipukiwa na simu huku mstaafu akivuta hewa nyingi ya manukato kiasi alishindwa kupumua vyema.
Lakini kilichostua mamlaka za ulinzi na usalama ni jumbe zenye mfanano, zilizokutwa kwenye maeneo ya vifo vilipotokea, lakini pia vifo kuwahusu viongozi wa timu moja.
Walakini ukajaa, utata ukaibuka, mauaji yaliongezeka na fumbo likasilia kwenye herufi na namba zinazoachwa na muuaji ama wauaji.
Suala likawa gumu kwa jeshi la polisi, hivyo faili la kesi likatua kwa kutengo maalumu chini ya kamishina Zenge wa Zenge na hapo ndipo ukawa mchezo wa vipepeo.
kipaji unacho mkuu. Hongera
naomba usiache kunitag ukiendelea
 
RIWAYA; DOA LA VIPEPEO

NA; BAHATI MWAMBA

SIMU; 0758573660


SEHEMU YA TATU


Walakini ukajaa, utata ukaibuka, mauaji yaliongezeka na fumbo likasilia kwenye herufi na namba zinazoachwa na muuaji ama wauaji.

Suala likawa gumu kwa jeshi la polisi, hivyo faili la kesi likatua kwa kutengo maalumu chini ya kamishina Zenge wa Zenge na hapo ndipo ukawa mchezo wa vipepeo.

------------

-VIOLIN PUB.-

Usiku huu kulikuwa na makutano yasio rasimi ndani ya Violin Pub Masaki . Pub hii ilikuwa ina umaarufu mkubwa ndani na nje ya jiji. Umaarufu wake ulitokana na aina ya muziki unaopigwa pale kila siku, mziki wa ala fidla(violin), Zeze na piano.

Pub hiyo iliojizolea umaarufu mkubwa, ilikuwa inapata wageni kutoka nchi mbalimbali, Afrika na hata mabara mengine na, kubwa lilowapeleka pale ni muziki wa ala uliopigwa na wasanii waliojua kuvitumia vyombo hivyo ipaswavyo.

Licha ya kuwa sehemu ya watu kupata burudani, lakini kulikuwa na harakati nyingine zinaendelea ndani ya Pub, hasa kulingana na mazingira yake kutawaliwa na sehemu nyingi zenye kiza na taa hafifu, huku kukiwa na korido nyingi na maalumu kwa wateja maalumu wa ile Pub. Huduma nzuri ilikuwa ni moja ya kivutio kwa wateja waliofika pale kila mara.

Katika korido moja iliojitenga na zingine, kulikuwa na makutano ya dharura ya watu watano, lakini hadi usiku huo wa saa nne mmoja alikuwa hajafika ili kutimiza idadi kamili ya watu watano.

Watu hawa walikuwa na umri ulioenda miongo zaidi ya mitano. Kulikuwa na wale waliopita miongo sita na wengine walikuwa chini ya miongo mitano na nusu lakini si mitano kamili. Wote hawa walikuwa ni wastaafu kwenye serikali ya Jamhuri ya muungano wa Tanzania, ambapo walikuwa wameshika nyadhifa mbalimbali katika serikali kuu.

Usiku huu kuna jambo la muhimu lilikuwa limewakutanisha, lakini walikuwa wanazidi kupata mashaka zaidi kuona mtu wa tano na waliemtegemea, akiwa hajafika na simu yake haipokelewi.

“Unajua sielewi mambo haya jama” Alizungumza mzee mmoja aliekuwa amevaa pensi kubwa na sendo nyeusi, huku akiwa amefunika kitambi chake na tisheti nusu, ni dhahiri haikuwa yake.

“Acha kupagwa Masawe, bado mapema na uzuri alituambia anakuja” Alisema Mzee mwingine, ambae yeye alikuwa amevaa suti iliokuwa inatoa harufu fulani ya uchafu usiotisha, ni dhahiri aliitoa kwenye rundo la nguo chafu.


“Kwa hiyo naona ushaniona mi kanyaboya wa kupagawa hovyo sio.!” Masawe alimaka na kumkata jicho aliempa ushauri.

“Sasa kama hujapagawa kwa nini umevaa kimelembe?” Alihoji yule Mzee mwenye suti chafu.

Kauli ile ilimfanya Mzee Masawe ajitazame, kisha akatikisa kichwa na kusikitika.

“Kweli nimepagawa, yani na heshima yote nimevaa hivi kweli!!” Masawe alijishangaa.

“Tatizo lako unapagawa sana na haraka, wakati mambo madogo haya” Mwenye suti chafu aliendelea kunanga.

Masawe alimtizama, kisha akacheka kivivu.

“ Haya mimi napagawa kizembe, vipi wewe ulievaa msuti mchafu kama kikagula!” Masawe nae alitoa dongo.

Wote waliokuwa mle walicheka, akiwemo Mzee Kihengu ambae alikuwa amevaa suti chafu.

“Jamani kila mtu kapagawa kwa kifo cha bi Mwendampya, hakuna alietegemea kabisa bwana” Alizungumza Mzee mmoja aliekuwa amekaa kimya muda mwingi.

Wakiwa bado wanajadili, mara kuna mtu alitokeza na kuwafuata wale wazee.

“Walau sasa tutahema, tulikuwa tuna wasiwasi na afya yako bwana” Masawe alimwambia alieingia.

“Nimechanganyikiwa kiasi nimesahasu simu yangu mezani” Alijibu bwana yule.

Ulipita ukimya wa sekunde kadhaa, kila mmoja akijaribu kuwaza lake.

“Jamani hili jambo limekaaje kwani, mana naona kaondoka mtu ambae hatukuwa tumepanga iwe hivyo.” Mzee kihengu alianzisha mjadala.

“Kifupi hakuna ambae anajua kitu gani kimetokea, lakini halina ubishi nae kauawa” Mzee Mazengo ambae alikuwa kimya muda mwingi, alitoa hoja yake.

“Lakini kwa nini auewe muda ule ule aliokufa kocha? Aina ya kifo chake ni ya kitalaamu sana jama” Masawe alitoa hoja yake.

“Kiukweli hakuna anaejua jambo hili limetokeaje, lakini naamini Bi. Mwenda kauawa, japo hatuna uthibitisho wa ripoti kamili” Mzee alieingia mwishoni alisema.

“Lakini mnamwini mtu tuliempa kazi?” Masawe alihoji.

“Aah, hilo halina ubishi, jamaa anajua bwana, sifa zake zipo na ameonesha kwa wale tuliotaka awaondoe” Mzee Kihengu alijibu.

“Unajua Masawe Unataka kukosea, unaanza vipi sasa kukosoa utendaji wake mapema namna hii?” Mazengo aliongea kwa ukali kidogo.

“Sio kama ninahofu ya kazi yake, lakini huyu mtu kumbukeni ni Psycho na watu wa namna hii wanapenda sana kuuwa, tena kwa akili nyingi sana na wao wanafurahia hali hiyo, asije kuwa anataka kutoka na sisi ohoo” Masawe alilalama.

“Unaogopa kifo kwani?” Aliuliza Kihengu.

“Naogopa vipi, wakati lazima nife, lakini sio kwa mateso ya jitu lenu lile” Masawe alijibu.

“Sema jitu letu, au umesahau wewe ndie uliempokea uwanja wa ndege?” Mzee Mazengo alihoji.

“Sasa nani kamuuwa Mwendampya?” Masawe alirudi kuhoji.

“Hakuna anaejua, kikubwa tusiogope kufa, mana mchezo wetu ni wa kifo asilimia tisini” Mzee alieingia mwishoni alisema.

“Afu Masawe usijisahaulishe kama wewe ni muuaji” Kihengu alimwambia Masawe.

“Nani muuaji, sema sisi wauaji bwana.” Masawe alihamaki.

“Aah, kwa hiyo tushakuwa wauaji tena” Mazengo alishangaa.

“Kwani ulimlipa nani pesa? Si ulilipa muuaji, kwa hiyo wewe nae muaaji.” Masawe alimaka.

“Aah kwa hiyo tunahatia sio!” Mazengo alizidi kushangaa .

“Sio hatia tu, tuna kesi ya kujibu mahakamani!” Masawe alikazia.

“Masawe usitutishe bwana, polisi hawawezi kujua.!” Kihengu alipozea hamaki ya Mazengo.

“Wee thubutu, nimekuwa RPC, zaidi ya miaka thelathini, najua serikali inachelewa tu, ila inatakufikia tu, kikubwa jambo hili tulifanye haraka, tuhame nchi kwa muda.!” Masawe alizidi kutetea hoja zake.

“Aisee! Kweli bwana, nimekuwa muuaji eti” Mazengo alizidi kuhamaki.

“Sio muuaji tu, muaji wa kutisha..hebu…” Masawe alikatishwa na Mzee aliengia mwishoni.

“Hebu Masawe, acha kututisha bwana, wote tumehudumu huko, na tunaouwezo wa kukwepa msala huu, ndio mana tulimuita yule jamaa mtalaamu wa kupanga mauaji bila kustukiwa na lengo ni kuondoa wote wanaojua jambo hili kwanza.”

“Tatizo hawa wanataka tujadili hili jambo kama watakatifu, ndo mana nimewambia tusijitoe kwenye hatia kwanza.” Masawe alijibu.

“Sawa, lengo ni kutaka kujua Bi Mwendampya amekufaje na kwa nini na ni nani alimuua!” Mzee alieingia mwishoni aliwarejesha wenzie kwenye lengo la kukutana.

“Wakati nakuja hapa, yule bwana mdogo alinambia kuna vitu wamevikuta sehemu zote na vinafanana, kiasi inaonekana imewastua maofisa na kuhisi ni mauaji ya kupangwa.” Masawe aliwambia wenzie.

“Wamekuta vitu gani tena” Kihengu alihoji.

“kuna bahasha ndogo isio na kitu ndani, ila kwa juu ina herufi moja na namba na inasomeka “F3”…”

“F3?” Walijikuta wote wakishangaa kwa pamoja.

“Vipi mmetambua lolote?” Masawe aliwahoji wenzie.

“Afu huwa unajitia utoto Masawe, tungejua tungeshangaa?” Mzee kihengu alimaka.

“aaah, naona unaleta uzuzu, nitakumbushia enzi yangu bwana we, yani nauliza unaniita mtoto ebo!” Masawe alimaka.

“Hebu tulieni bwana, mambo gani hayo sasa!”

“Sikia Nzaya, unajua Kihengu, ananichukulia mimi wa kuokota tu, aisee mi nachafua si mchezo ohoo!” Masawe alitupia mkwara mwingine.

“Haya Mwakinyo, tumekusikia RPC wa zamani.” Nzaya alimtuliza Masawe.

Nzaya ndie Mzee alieingia mwishoni.

“Sasa niliwambia huyu mtu atakuwa anahusika mkanikatalia, kwa nini kwa Kocha kuwe na bahasha sawa na ile iliokutwa kwa Mwendampya?” Masawe alihoji wenzie.

“Lakini hii inafikirisha sana ujue. Kwani kijana anasemaje yeye!” Mazengo nae alihoji huku akimtizama Kihengu.

“Kuhusu Zozo kuuwa nakataa, mana alipomaliza kwa Kocha, alinitaarifu, kisha akasema anaenda kupumzika hadi apewe kazi nyingine” Kihengu alijibu.

“Hata mimi naungana na Kihengu, hawa wauaji wa kulipwa huwa wanaheshimu sana mikataba yao, sio rahisi kuuwa mshirika wake hata kidogo” Nzaya aliungana na Kihengu.

“Unajua wakati tunachagua mtu sahihi, tuliita serial killer, huyu sifa yake kuu ni mgonjwa yani anamtatizo ya ubongo, kitalaamu Psychology, anafurahi akiua, anapanga mipango yake kwa umakini, na kuwapa polisi ugumu wa kuamua kesi, hivyo kumbukeni hapa na tuna serial killer, hatuna Hitman wala mamluki, hapa tumeita mgonjwa wandugu.” Masawe aliwambia wenzie.

Ukimya ulichukua hatamu.

“Pamoja na yote, lakini hawezi kubadilika, wala hana sababu ya kutugeuka bwana.” Nzaya alikataa.

“Lakini unawajua watu wa aina hiyo kweli, wao huwa wanafurahia kuua, afu wanaenda kupiga selfie kituo cha polisi na polisi hawezi mpata, furaha yao waone polisi wanahangaika, au anaotaka kuwua anahangaika…..” Masawe aliendelea kuwazindua wenzie.

“Sasa kama ndie, kwa nini aache yale maneno kwenye vibahasha?” Mazengo alihoji.

“Hapo ndo utata unaanzia, kwa nini aache hicho kibahasha, ana maana gani?” Kihengu nae alihoji.

“Sina hakika kama Zozo anatugeuka, mi nadhani kuna jicho la mwewe linatuchora, kiasi linataka kutuchanganya tu.” Mazengo alizungumza.

“Unaweza kuwa sahihi, kuna kidudu mtu anataka kutuharibia mipango” Nzaya aliunga hoja.

“Hapa kuna mchezo wa danadana jamani, tuwe makini na ikibidi tusitishe suala hili!” Masawe aliwashauri wenzie.

“Aah wapi, haiwezekani hata kidogo, tuko mwishoni kabisa, jambo tumelisubiri miaka kumi, tunasitishaje kizembe namna hii” Mazengo alimaka.

“Ila kweli, afu ujue tunakesi ya kujibu, tumepanga mauaji ya kocha, na wale wawili, kujitoa ni kujigeuza mbuni kuficha kichwa mchangani huku mwili upo nje.” Nzaya nae alishauri.

“Hapa babaya sasa!” Masawe alisikitika.

“Wewe si mstaafu na unatishia kucharaza mkono, unakuwaje muoga sasa!” Kihengu alimzodoa Masawe.

Vilifuata vicheko vya chini chini.
Watu waliokuwa kwenye dharura ile, waliwafahamu vyema Kihengu na Masawe, ambao ni marafiki wa kushibana na hakuna aliewahi kumnunia mwenzake, zaidi huzodoana na kuishia kucheka, hivyo haikuwa mara ya kwanza wao kuzodoana.

Kikao kile kilivunjwa baada ya kuwepo makubaliano fulani, mipango kabambe ilipangwa, huku kila mmoja akiwa na jukumu la kujilinda yeye kama yeye, kisha waliondoka ndani ya Violin Pub.

Lakini wakati wanaondoka, kulikuwa na mtu akiwasindikiza na macho makavu yenye hila juu yao.

Ila wao hawakujua, waliamini kiza kilichokuwa ndani ya Pub ile nzuri na ya kuvutia.
 
RIWAYA; DOA LA VIPEPEO

NA; BAHATI MWAMBA

SIMU; 0758573660


SEHEMU YA NNE


Kikao kile kilivunjwa baada ya kuwepo makubaliano fulani, mipango kabambe ilipangwa, huku kila mmoja akiwa na jukumu la kujilinda yeye kama yeye, kisha waliondoka ndani ya Violin Pub.

Lakini wakati wanaondoka, kulikuwa na mtu akiwasindikiza na macho makavu yenye hila juu yao.

Ila wao hawakujua, waliamini kiza kilichokuwa ndani ya Pub ile nzuri na ya kuvutia.

****
Ahsubuhi ilikuja ikiwa na mambo mengi, lakini liloshika vichwa na masikio ya watu ni kifo cha kocha wa timu ya vijana ya Azan. Mashabiki wa timu hiyo waligubikwa na simanzi, huku chanzof cha kifo chake, kikihusanishwa na mlipuko wa simu wakati alipokuwa anaichaji huku akiwasilana. Magazeti yalipambwa na habari ile ya kuhuzunisha.
Mashabiki waliumia zaidi kwa kuwa walipata misiba miwili ndani ya klabu moja, alikufa kocha na alikufa afisa habari wa timu ile iliokuwa inazidi kujizolea mashabiki kila pande ya nchi. Mtaani ukazuka mjadala kuhusu vifo vile, lakini sababu za vifo zilitowesha kabisa hisia za watu juu ya vifo vile.

Simanzi ilitanda, huku mwili wa kocha yule raia wa Burundi ukiandaliwa kusafirishwa na mwili wa afisa habari, Bi Mwendampya, ukitarajiwa kuagwa kwa heshima za kiaskari kwa kuwa alikuwa ni mstaafu wa cheo cha juu kabisa ndani ya jeshi la polisi.

Ahsubuhi hiyo wakati hayo yakiendelea, kulikuwa na jambo lingine linaendelea sehemu fulani ndani ya jiji la Dar es laam.

Kulikuwa na mtu amekaa juu ya jengo fulani akisubiri kitu, huku akiwa ameshika bunduki kubwa ya kudungulia. Mtu yule alikuwa amevaa nguo nyeusi, usoni akiwa amefunga na kitambaa cheupe, alikuwa ni mrefu kwa wajihi.

Mtu yule alikuwa amekaa pale zaidi ya saa mbili, huku kila mara akitizama geti la nyumba fulani. Nyumba ile ilikuwa kando ya barabara.

Ndani ya nyumba ile, kulikuwa na kijana mwenye umri wa miaka kama thelathini hivi, kijana yule alikuwa anamalizia kuvaa nguo zake za kazi na mezani kwake kulikuwa na faili lililokuwa limeambatanishwa vibahasha viwili.

Alikuwa ni ofisa wa jeshi la polisi mwenye cheo cha koplo.

Koplo ndie aliekuwa ameshika jalada la uchunguzi wa vifo vya kutatanisha vya kocha na afisa habari wake. Alikuwa amekusanya taarifa kadhaa za muhimu kuhusu vifo vile.

Koplo huyu hakuwa koplo wa kawaida, alikuwa ni zaidi ya koplo na alikuwa ndani ya kitengo cha operesheni maalumu chini ya kamishina Zenge wa Zenge.

Koplo Juli tangu aingie kwenye uchunguzi ule,ndani ya saa chache alikuwa amefanikiwa kubaina mambo yenye kutia ukakasi, hivyo haraka aliwasiliana na kitengo chake na kutoa taarifa, kisha akatuma baadhi ya nyaraka muhimu kwa njia ya mtandao, kisha alipiga picha bahasha zile ndogo na kutuma kwa kamishina Zenge wa Zenge.

Hivyo ahsubuhi hiyo alikuwa anajiandaa kwenda kuripoti kituoni kwake, kisha aendelee na uchunguzi wa kipolisi huku akitoa taarifa kitengo maalumu .

Koplo Juli alitoka ndani ya nyumba yake, akiwa amebeba mkoba wenye nyaraka zote kuhusu kesi ile.

Wakati koplo Juli anafungua geti lake, mdunguaji alikuwa ametulia akimtizama; koplo alitulia getini huku akitizama saa yake.

Alikuwa anangojea Uber. Ilikuwa ni kawaida yake kutumia usafiri huo kila siku, hakutaka kununua gari, wala pikipiki, akiwa na nia ya kukaa mbali na hisia za watu juu ya kazi yake halali.

Kitu ambacho hakujua, hata mdunguaji nae alikuwa anangojea Uber, ili akamilishe kazi yake, mazingira yaliruhusu kufanya kile alichotaji kufanya.

Dakika kumi baadae, kulikuwa na taxi inasogea mitaa ile, mdunguaji alipoona nae aliweka sawa bunduki yake.

Kutokea kule ilikokuwa taxi, hadi getini kwa koplo Juli, kulikuwa na mteremko wa kiasi, hivyo wakati gari inakaribia mdugunguaji alilenga tairi ya mbele, kiasi gari ilianza kuserereka kwa kasi kubwa huku ikipoteza mwelekeo. Koplo alipokuja kutahamaki, alijikuta akiwa amejaa kwenye taxi ile, kisha alirushwa juu na kutupwa chini kwa nguvu na, bahati mbaya hakuinua hata uso wake kuona lolote lililofuatia.

Dakika moja iliofuata, kuna pikipiki ndogo ilipita mitaa ile na kuuchukua mkoba wa koplo, kisha ulikaguliwa kidogo na kurejeshwa chini haraka sana, kisha pikipiki iliondoka kwa kasi sana eneo lile.

Yote yalitokea kwa sekunde chache sana, kiasi ilihitaji mtu mwenye elimu kubwa kuelewa kilichotokea.

Mdunguaji alikunja bunduki yake, kisha akaiweka kwenye begi na kuondoka juu ya jengo lile na kutokomea anakojua.

Watu walianza kusogea eneo la tukio na taarifa zilifika trafiki kwa kuwa ilikuwa ni ajali ya gari kumgonga ofisa wa jeshi la polisi.

Wakati watu wanazidi kusogea, ilitokea pikipiki moja na kusimama, aliekuwa juu yake alishuka na taratibu alifika eneo lile na kuanza kushangaa. Lakini mtu yule kuna kitu alitoa mfukoni mwake na kukirusha karibu na tairi ya taxi ilioleta ajali, kisha alipanda pikipiki yake na kuondoka kwa kasi kubwa.

Hakuna raia alieona tukio lile, lakini mdunguaji aliekuwa sambamba na raia wale akitaka kuhakikisha kazi yake, aliona tukio la mtu yule, lakini bahati mbaya sana hakumuona sura yake.

Mdunguaji alipigwa na butwaa.

Kwa nini!.
Kwa sababu alitumwa kumuua koplo, ili asifikishe vibahasha vile kwa uongozi wake, lakini vibahasha vilishachukuliwa na wale waliokuwa kwenye pikipiki, lakini kinaletwa kibahasha kingine tena.
Ile ilikuwa ni maana mbaya kwa mdunguaji, lakini ilikuwa ni hatari kwake, kwa sababu aliona kila tukio analotumwa kufanya, yule anaeacha vibahasha anajua, tena anajua hadi eneo la kufanyia tukio.

Mdunguaji alibaki kujiuliza, kama jamaa anajua mipango yake, kwa nini hazuii na badala yake anaacha afanye kisha yeye anaenda kuacha bahasha?.

Hakika lilikuwa ni swali gumu kwa mdunguaji yule, alietumia akili nyingi kufanikisha tukio lile.

Alipiga hatua ili aokote bahasha ile, lakini aligundua kuna watu zaidi ya wawili wanamtizama na walikuwa ni maofisa wa jeshi la polisi waliofika pale haraka.

Mdunguaji alilaani kitendo kile, badala yake alioendelea kusogea mbele na kulipita gari lile taratibu kama vile hakuwa na nia na jambo fulani.
 
RIWAYA; DOA LA VIPEPEO

NA; BAHATI MWAMBA

SIMU; 0758573660


SEHEMU YA TANO.


Aliipokea taarifa ya kifo cha koplo kwa namna ya tofauti kabisa. Aliona kuna hujuma zitakuwa zimefanyika, sio rahisi eneo lile kutokea ajali ya kuweza kumtoa mtu uhai.

Haraka alimwagiza Honda aliekuwa nae ofisini, alihitajika mtu makini aina ya Honda, kuchunguza kwa kina zaidi. Ilihitajika jicho pana, hatua kwa hatua ili kufanikisha kujua hila ya aina yoyote iliotumika.

Haraka Honda alichukua pikipiki yake na kuelekea eneo la tukio.

Honda hakuchukua muda murefu kufika eneo la tukio. Aliegesha pikipiki yake mbali kidogo, kisha alitembea kwa miguu kuelekea eneo la tukio, eneo ambalo watu walikuwa bado wanashangaa kilichotokea.
Honda alikuta askari wa barabarani wakimalizia kuchora ramani ya tukio la ajali. Honda aliamua kujichanganya na watu ili aone kinachofanywa na askari wale. Subira yake hiyo, haikwenda bure, macho yake yalikuwa yanacheza kama yale ya kinyonga. Kucheza huko hakukuwa na bahati mbaya, yaliona kile alichostahili kuona kwa wakati ule.

Watoto wawili walikuwa wameshika bahasha ndogo wakiishangaa, bahasha ile waliiokota mbali kidogo na walipokuwa maofisa wanaopima ajali. Macho yake yaliwafuata hatua kwa hatua, hadi walipoiacha chini na kuwahi shule. Taratibu alipiga hatua na kuisogelea, kisha akainama na kuikota.


Hakika macho yake hayakumdanganya, ile ilikuwa ni bahasha yenye herufi moja na namba, yani “F3”. Honda aliona inafanana sawa na zile walizokuwa wametumiwa na Koplo Juli.
Lakini ile bahasha kuna kitu cha ziada alikiona, kitu kile alikuwa amekiona kwenye zile picha za bahasha alizokuwa ametumiwa na Koplo. Japo kulikuwa na ufanano, lakini haukuwa ufanano sawa.

Honda aliichukua na kuifutika mfukoni mwake, kisha aliendelea kuwa shuhuda wa yale aliokuwa ameyakuta pale.

Alichagua sehemu nzuri ambayo ilimwezesha kuona mengi kwa wakati mmoja. Macho yake yalicheza kama njiwa pori aliekoswa na mtego.

Bado bahati ilikuwa kwake, macho yake aliyapeleka pale ilipokuwa gari ilioleta ajali. Kuna cha ziada aliona na haikuwa rahisi kwa mtu wa kawaida kugundua kasoro ile.

Kuna kishungi cha risasi kilikuwa kimenasa karibu na rimu ya gurudumu, kishungi kile kilikuwa kimesababisha tairi kupasuka na kukiacha kikiwa kimenasa pale kutoka.

Honda alitoa simu yake mfukoni, na kwa uficho alipiga picha eneo lile, kisha alisogea sehemu iliokuwa na mkusanyiko wa watu.
Alipowafikia, aligundua walikuwa wanamsikiliza dereva wa gari ilioleta mauti ya ofisa wa jeshi la polisi. Dereva alikuwa anajaribu kutoa maelezo ya awali kwa ofisa wa jeshi la polisi kuhusu namna alivyoanza kukosa mwelekeo, baada ya gurudumu moja la upande wa kushoto kupasuka na akiwa kwenye mwendo wa kawaida sana.

Honda alitathimini namna ambavyo ajali ilitokea, kisha akahusanisha na kishungi cha risasi alichikiona, hapo akihitaji ofisa aulize swali muhimu sana ambalo binafsi lingempa mwanga fulani.

Kwa sababu wakati wote huo, alikuwa hajui ni namna gani risasi ile ilipigwa, je ilipigwa na mtu wa karibu au mtu wa mbali, na ni nini lengo la huyo mtu kupiga risasi gurudumu la gari.

Hatimae ofisa mmoja aliuliza lile swali ambalo lilikuwa muhimu kwa Honda.

“Ulihisi gurudumu la gari yako limepasuka ukiwa eneo gani?” Ofisa alihoji.

“Ni wakati nakianza kile kibonde pale!!” Dereva alijibu huku akionesha kidole eneo aliloanzia kupata hitilafu.

“Je! Kulikuwa na mtu mitaa hiyo, ama kisiki ama kitu gani ulichokuwa umeona kabla hujapata hitilafu.” Ofisa alihoji swali lingine zuri lenye manufaa kwa Honda.

“Hakukuwa na kitu chochote maeneo yale.!” Dereva alijibu, kisha ofisa alimuelekeza kupanda ndani ya karandinga, ili taratibu zingine zifuate.

Honda aliondoka taratibu, akiwa anaungana na watu wengine waliokuwa wanatawanyika eneo la ajali. Hatua zake ziliishia kwenye kiteremko alichokisema dereva, alijaribu kuona ni wapi aliepiga risasi alijibanza, lakini eneo lile na maelezo ya dereva, kusingeweza kuwepo na mtu mwingine na dereva asimuone, lakini alipojaribu kupima maneno ya dereva, hakuona kama dereva anahatia kabisa, ni dhahiri hata yeye alikuwa hajui kilichotokea hadi apate ajali ya namna ile na kumuua mteja wake wa kila siku.

Honda aligeuza macho yake kila pande na hatimae aliingiwa na shaka na jengo moja refu lilokuwa linatazamana na barabara ile. Honda alijaribu kutumia hisia zake kumweka mdunguaji eneo lile, kisha akaipitisha gari maeneo yale, akapiga hesabu za namna koplo alivyokuwa amekaa getini.

Honda alishusha pumzi nyingi, kisha akajiwazia.

“Huyu mtu alikuwa na uwezo wa kumuua koplo, lakini aliamua kutumia gari ili ionekane ni ajali ya kawaida…” Honda aliguna baada ya mawazo hayo.

“Ni serial killer, alietumwa kama mamluki, analipwa pesa, japo binafsi yake anapenda kuua… Nani anampa pesa na kwa nini aue?” Honda alizidi kujiweka kwenye maswali mengi yasio na majibu.

Aliendelea kuwaza kifo cha koplo, hakuona kama ni kifo cha bahati mbaya, ni cha kupangwa na lengo ni kuzima juhudi za kutambua mauaji ya kocha na msitaafu Bi. Mwendampya.

“Kwanini kocha auae siku moja na afisa habari wake?” Honda alizidi kujiuliza,mara akili yake ikakumbuka vibahasha vyenye herufi moja na namba, kisha kwa wino hafifu kunaonekana namba mbili nyingine.

Je muuaji anaweza kuwa ni mmoja? Na kwa nini anaacha vibahasha, anataka kuacha ujumbe gani?.... Honda alizidi kujipa maswali zaidi.

Aliona eneo lile pekee, haiwezi kumpa majibu aliyotaka, alielekea kwenye pikipiki yake na kisha aliondoka eneo lile taratibu sana.

Kitu alichoamini ni kuwa, hakuna muuaji duniani, aiseacha nyayo zake nyuma. Hivyo ni lazima wauaji ama muuaji huyo, atakuwa anaacha alama zake nyuma yake, japo inahitaji umakini mkubwa kujua kosa lake na ukalitumia kumtafuta hadi akapatikana.

****

Safari ya Honda iliishia nyunbani kwa kocha wa timu ya Azan. Aliegesha pikipiki yake mbali kidogo, kisha alitembea kwa miguu hadi getini. Alikutana na utepe wa njano, uliomuonya yeyote asiehusika, kuingia eneo lile.

Alitizama pande tatu za dunia, huku ile ya nne ikiwa imekingwa na nyumba ya kocha, hakuona mtu katika pande hizo alizofanikiwa kuziona.

Utulivu aliokutana nao pale, ulimhakikishia hakukuwa na mtu yeyote katika nyumba ile.

Alisukuma lango la na kuingia ndani. Nyumba ilikuwa kimya kabisa, alipiga hatua zake na kuelekea ndani.

Alipoingia ndani, alianza ukaguzi wake hatua kwa hatua, alianzia chumbani, kisha alielekea jikoni.

Macho yake yalitua kwenye dirisha lilokuwa wazi upande wa kulia wa jiko.

Honda aliingiwa na mashaka, alisogea hadi karibu na dirisha lile, aliona linatosha kupitisha mifupa 206, hivyo muuaji alipita pale wakati wa kuingia na kutoka. Lakini Kama alipita upande ule, ina mana hakupita getini, alipita wapi sasa wakati anaingia pale ndani!.

Honda alirejea sebuleni, alikutana na damu ikiwa imetapakaa chini na hakukuonekana kufanyika usafi wa aina yoyote. Alitizama kwa makini ili aone kama kulifanyika nguvu yoyote, lakini hakuna sehemu alioona. Honda alisogea hadi kwenye jokofu kubwa lilokuwa pale, aliangalia namna swichi zake zilivyokaa, kisha akaenda hadi nyuma ya jokofu lile.

“Yawezekana muuaji alikaa eneo hili, ikawa rahisi kumuua kocha kwa kupitia nyuma na kisha alimlaza hapa chini” Honda alizidi kujiwazia.

Aliondoka sebuleni na kuelekea kwenye chumba, alichohisi ndicho kilitumiwa na marehemu kulala, alitulia kwa dakika kadhaa na kukizoea, kisha alianza kufanya upekuzi tena, mara hii akienda hadi maliwatoni, huko macho yake yalimwonesha kitu kingine kabisa ambacho hakukitarajia.

Dirisha la maliwato, lilikuwa ni dirisha kubwa kidogo, lakini halitoshi kupitisha mtoto wa miaka saba, lakini yeye alikuwa na hakika anaweza kupita kwa kutumia ujuzi wa mafunzo maalumu.

Kioo cha dirisha kilikuwa kimevunjwa, pia kulikuwa na tope pale maliwato, kuashiria alipita mtu mwenye viatu.

Honda alibaki na swali lenye utata.

Je alieuwa alipitia pale, ama alipitia kule jikoni, na kama alipitia jikoni, ni nani aliepita pale dirishani?

Likabaki swali bila jibu.

Honda alitoka nje ya nyumba ile, kisha akaelekea upande aliohisi muaji alipita na kutokea jikoni.

Macho yake yaliona kile alichotarajia, nyaya zilikuwa zimekatwa, muuaji alikata na kudondoka ndani ya ua.

Honda hakuridhika, alielekea upande ule aliohisi mtu alipita na kuingia kupitia maliwato, napo viashiria vilionesha kuna mbabe alipita pale.

Kulikuwa na mti mkubwa uliodondoshea matawi yake pale uwani kwa kuufunika ukuta, lakini pia aliona majani yakiwa yamedondoka, kuashiria alishuka nayo wakati anatua ama anapanda juu ya mti ule.

Honda alishindwa kujua mahusiano ya watu wale, lakini alishindwa kujua umuhimu wa kocha yule katika sakata lile, kiasi afuatwe na watu wawili kwa nyakati sawa ama tofauti.

Kama ana umuhimu, basi kifo chake kitakuwa sawa na kifo cha bi Mwendampya.

Hakika Honda alitatizika.

Aliamua kuondoka mazingira yale, huku akutarajia kwenda nyumbani kwa Bi. Mwendampya.

Na huko alikutana na jambo jipya tena.
 
9 Reactions
Reply
Back
Top Bottom