diana chumbikino
JF-Expert Member
- May 29, 2018
- 428
- 368
Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Dkt. Reginald Mengi ametunukiwa tuzo maalum na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Arusha, Mhashamu Isaac Amani kutambua mchango wake katika kusaidia jamii.
Pia Dk. Mengi ameahidi kutoa Tsh. Bilioni 1 kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa miundombinu ya Shule ya Sekondari Jumuishi ya Mtakatifu Pamakio iliyoko Kijiji cha Kimashuku, Hai mkoani Kilimanjaro.
Shule hiyo ilizinduliwa jana na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa. Wakati wa uzinduzi huo, Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Arusha, Mhashamu Isaac Amani, alisema Kanisa Katoliki limemtunuku tuzo maalum ya Msamaria Mwema (Good Samaritarian Special Needs Awards) kutokana na kutambua mchango wake katika kusaidia jamii ya watu wenye ulemavu nchini kufikia ndoto zao.
Pia alisema kanisa hilo limemtunuku tuzo maalum ya ‘Innovative Leadership Award in Special Needs In Education’ Rais John Magufuli kwa kutambua mchango wa serikali katika kutoa huduma bora na shirikishi kwa Watanzania wote.
Katika hotuba yake, Dk. Mengi alisema Waziri Mkuu amekuwa akishiriki kwa kiwango kikubwa katika mipango yake ya kusaidia watu wenye ulemavu na hivi karibuni alishiriki ufunguzi wa Reginald Mengi Disability Foundation na amekuwa akimpa mawazo ya kusaidia watu wenye ulemavu.