Dkt. Ghalibu Bilal agawa zawadi hewa kwa wanafunzi Bora

Sigwame

Member
Dec 8, 2012
71
13
Wakati wabunge wakiijia juu Wizara ya Elimu na Mafunzo kutokana na kuwepo kwa hali ya kuporomoka kwa kiwango cha elimu nchini, kashfa ya aina yake imeibuka ikihusisha wizara hiyo kumtumia Makamu wa Rais Dk. Gharib Bilal kuwapa zawadi hewa wanafunzi 10 bora wa mwaka jana.

Taarifa zilizozifikia NIPASHE zinasema tukio hilo ilifanyika Mei 10 wakati wa kilele cha Wiki ya Elimu nchini iliyofanyika mkoani Dodoma, ambapo Dk. Bilal alikuwa mgeni rasmi kwenye sherehe hizo.

Imefahamika kwamba viongozi wa wizara hiyo kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara ya Tawala ya Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) walimpatia Dk. Bilal bahasha tupu ambazo aliwapa wanafunzi hao kwa maelezo ndani yake kulikuwa na kiasi cha Sh. 250,000 kila moja.

Katika bahasha hizo za rangi tofauti moja ikiwa ya rangi ya khaki na nyingine nyeupe iliyofifia yenye nembo ya serikali, zilitolewa kwa wanafunzi kumi wa shule za sekondari waliofanya vizuri katika mtihani wa kidato cha nne mwaka 2013.

Katika mchanganuo huo, wanafunzi hao walitakiwa kupewa Sh. 500,000 kama zawadi kutoka serikalini, Sh. 250,000 kutoka Ubalozi wa China na Sh. 500,000 ya vocha ya kununua vitabu vya kiada na ziada.

Katika hali ya kushangaza, wakati wanafunzi hao walipoitwa jukwaani kukabidhiwa zawadi zao, waligundua ndani hakukuwa na kitu na kusababisha kuibuka kwa malalamiko kutoka kwa wazazi walioambatana nao.

HALI HALISI DODOMA
Baadhi ya wazazi wakiongea na NIPASHE walisema shughuli nzima ya utoaji tuzo haikuwa na mpangilio mzuri kitu ambacho kilisababisha wazazi na watoto wao kupata tabu walipokuwa mjini Dodoma.

Mmoja wa wazazi hao Caroline Marealle ambaye mtoto wake Joyceline Leonard (17), alikuwa mmoja wa wanafunzi waliozawadiwa, alisema dalili mbaya walianza kuiona mara baada ya kufika Dodoma siku moja kabla ya sherehe baada ya kutelekezwa na wizara hiyo ndani ya jengo la Sekondari ya Dodoma.

Alisema walijaribu kuwasiliana na mratibu wa elimu kutoka wizarani kwa ajili ya kupata maelekezo ya mahali watakapofikia na chakula, lakini alipotafutwa hakuwa na jibu la kutoa na kisha aliamua kuzima simu yake ya mkononi.

"Tulibaki tukihangaika pale shuleni hatujui wapi tuelekee, baada ya kukaa sana tuliamua tuwachukue watoto wetu tukaenda kutafuta sehemu ya kujistiri," alisema Marialle.

UTATA WAIBUKA UWANJANI
Siku ya pili yake ya Mei 10, wazazi na watoto wao walijumuika katika Uwanja wa Jamhuri ambako sherehe hiyo ilifanyika.

Uwanjani hapo pamoja na kuwepo kwa Makamu wa Rais, pia viongozi mbalimbali walihudhuria akiwamo Waziri wa Elimu na Mafunzo, Shukuru Kawambwa, Waziri wa Tamisemi, Hawa Ghasia, wakuu wa mikoa, wilaya, wabunge na viongozi mbalimbali.

Katika taarifa iliyotolewa na Kamishna wa Elimu nchini, Prof. Eustella Bhalalusesa iliyosomwa mbele ya Makamu wa Rais, ilionyesha zawadi zitakazotolewa ni halisi na kwamba imelenga kutekeleza kikamilifu mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN).

Katika taarifa hiyo ilieleza kwamba zawadi hizo za Sh. 250,000 zingekwenda kwa washindi 10 wa sekondari na Sh. 150,000 kwa washindi wa shule ya msingi.

Aidha, China ilitoa Sh. milioni 25 ambapo kwa wanafunzi 100 waliofanya vizuri wangepata Sh. 250,000 kila mmoja.

Aidha, Sh. 500,000 zilitolewa kama vocha ya vitabu na Mfuko wa Elimu nchini (TEA).

Mkanganyiko ulianza wakati wa kuitwa kwa majina ya wanafunzi bora wa sekondari, ambapo katika majina hayo mawili ya wanafunzi wa kike yalikatwa na nafasi zao zilijazwa na wanafunzi wa kiume walioshika nafasi ya 11 na 12 kitaifa.

Majina ya wanafunzi waliokatwa ambao pia walifika uwanjani kupata zawadi ni Janeth Urassa na Angel Ngulumba.

"Tuliambiwa majina yao yaliondolewa ili kupisha nafasi kwa wanafunzi wa kiume, kitu hicho kilisababisha simanzi kwa wazazi wa wanafunzi hao ambao walifika hapo kuona watoto wao wakipewa zawadi lakini ilishindikana," alisema mzazi mmoja wa wanafunzi hao ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini.

Wanafunzi waliotajwa na kutakiwa kufika mbele ya Makamu wa Rais ni Robina Nicholaus wa Shule ya Marian Girls, Magrath Kakoko (St Francis), Joyceline Marealle (Canossa), Safarina Mariki na Abby Sembuche (Marian Girls).

Wengine ni Sunday Mrutu kutoka (Anne Marie), Nelson Rugola Anthony na Emmanuel Mihuba Gregory (Kaizirege-Kagera), huku waliongezwa ni Razack Hassan (St Matthew’s) na Hamis Msangi (Eangles).

Utata zaidi ulendelea kuibuka pale ilipofika kipindi cha utoaji zawadi, ambapo kila mwanafunzi aliyeshuka kutoka jukwaani alionekana kushtuka baada ya kugundua bahasha zao hazikuwa na kitu ndani.

Kipindi hicho matangazo yalisikika uwanjani hapo kwamba kwenye bahasha kulikuwa na kiasi hicho kama kuwapa mkono wa hongera.
"Tulianza kuwa na wasiwasi na jambo hilo, tulianza kuhangaika kumtafuta mratibu atupe ufafanuzi zawadi za watoto zilikuwa wapi kwani tayari tuligundua wenzetu sio wakweli," alisema mzazi mwingine.

Baada ya kugundua jambo hilo walijaribu kuwatafuta wahusika, walipofanikiwa kuwapata waliwaambia jambo hilo lilifanyika kwa bahati mbaya hivyo waliahidi kulirekebisha haraka kwa kuwapa stahiki zao.

ZAWADI ZATOLEWA KINYEMELA
Kutokana na hali hiyo, wazazi waliokuwepo uwanjani hapo walianza kulalamika na kuwafuata viongozi wa wizara hiyo ili kutoa ufafanuzi juu ya suala hilo.

Hata hivyo, viongozi hao waliwataka wasubiri hadi mwisho wa sherehe ndipo watapewa pesa hizo.

Taarifa hizo zinasema katika kusubiria zawadi hizo ilibidi kukaa uwanjani kwa saa sita kuanzia majira ya saa 7:00 mchana wakati sherehe hizo zilipomalizika.

Lingine la kushangaza hata katika chakula kilichoandaliwa katika chuo cha Mt. Gasper, wanafunzi hao na wazazi hawakwenda badala yake waliachwa uwanjani wakiungua jua hadi jioni.

"Hakuna mtu aliyekumbuka kama wanafunzi waliachwa pale uwanjani, tulikaa pale bila kupata chakula wala maji hakuna aliyestuka," alilalamika Marialle.

Ilipofika muda wa saa 12:00 jioni maafisa kutoka wizarani walifika na kuanza kutoa pesa walizodai zimetoka serikalini pamoja na sh. Sh. 90,000 kwa kila mtu kama za kujikimu. Hata hivyo, pesa zingine zile za vocha na Ubalozi wa China hawakupatiwa kwa maelezo bado hatua muhimu hazijafikiwa.PESA ZA CHINA ZAYEYUKA
Sh. Milioni 40 zilizotolewa na China wa ajili ya kuwazawadia wanafunzi hao hazijulikani lini zitatolewa.

Uchunguzi wa gazeti hili umebaini pesa hizo zimetolewa kupitia Tamisemi na ilipaswa kutolewa kwa wanafunzi 100 kwa shule za sekondari na msingi zilizofanya vizuri nchini. Hata hivyo, kumekuwa na hali ya ukimya kutoka Wizara hiyo kuzungumzia namna ya utoaji wa pesa hizo kwa wahusika.

Alipotafutwa Naibu waziri wa Tamisemi anayeshughulikia Elimu, Kassim Majaliwa, kupitia simu yake ya mkononi, hakupatikana baada ya msaidizi wake aliyepokea simu kujibu Waziri huyo yupo kwenye kikao cha uchangiaji madawati mkoani Lindi.

WIZARA YAPATA KIGUGUMIZI
Alipotafutwa Kamishna wa Elimu Prof. Bhalalusesa kuzungumzia jambo hilo hakuwa tayari kuzungumzia kwa kile alichosema yupo kwenye kikao muhimu.

"Nakuomba ndugu mwandishi siwezi kuzungumzia suala hilo kwa sasa kwani nipo kwenye kikao muhimu naomba unielewe tafadhali," alisema.

TEA WAOMBA RADHI
Uongozi wa Mfuko wa Elimu (TEA) umeomba radhi kwa wazazi na wanafunzi kwa hali mbaya iliyojitokeza walipokuwa Dodoma, ambapo walisema jambo hilo halitajirudia tena.

Akizungumza na gazeti hili, Afisa Habari wa mfuko huo, Sylvia Gunze, alisema wamesikitishwa na mkanganyiko uliojitokeza na kueleza kwamba pesa zilizotolewa za vocha zingetolewa kuanzia jana.

"Kupewa vocha sio jambo geni kwa wanafunzi waliofanya vizuri, wizara husika ilikuwa ikifanya hivyo kila mwaka lakini mwaka huu kulikuwa na mkanganyiko kidogo hata hivyo, hali imetengemaa na wahusika wanaanza kulipwa," alisema Gumze.

Alisema kwenye bahasha walizopatiwa walifanya kosa la kutotoa ufafanuzi kuwa ndani yake kulikuwa na karatasi iliyoandikwa namba za simu ambazo wazazi wangezitumia kwa ajili ya kuwasiliana ili kupata pesa hizo.
CHANZO: NIPASHE
 
duuh hapo wizarani watu ni balaa wanawaza pesa na hivi walimu wamehamishiwa TAMISEMI so hakuna ulaji tena k hiy helyyote inayotokea lazima watu wapige haswaa
 
Na hao jamaa si wanaangalia mtu na mtu...yule jamaa yupo cool sana hivyo jamaa wametake advantage....ila wakashitakiwe kwani sio busara hata kidogo, eti wanaulizana ofisini.....anakuja nani kukabidhi...alafu wakiambiwa ni fulani.....wanashangilia na kubambika bahasha tupu....SO SAD....
 
Ooyooo kwanza huyo babu nai kachoka na uri ushamtupa mkona hivi anaomba lini muda wake ushie akapumzike pale kisongwe na hivi sasa hata huwo mkasi huwa hatimbie nao anabebewa na baunnsa wake na huku tena mnamzidishia kazi za kutoa sadaka wapi na wapi jamaani yaani hii ni kweli bongo
 
Nchi ya kisanii sanii tu kila kitu...mpaka kwenye elimu. Huyu makamu wa rais asipochukua hatua stahili lazima na yeye atakuwa ameshiriki kwenye hilo dili.

Kwanza haiwezekani kuwa yeye wakati anatoa hizo barua asifahamu kuwa hazina kitu lazima dili analijua tu....
 
Huo ni usanii uliopitiliza. Kwanza Wizara ya Elimu ni bora tu ivunjwe maana kila kitu kimeshahamia TAMISEMI, wao wamebaki na kazi ya kuchakachua viango vya ufaulu, sasa wanachakachua mpaka zawadi za wanafunzi.

HII NI ZAIDI YA AIBU NA NI FEDHEHA KUBWA SANA KWA MAKAMU WA RAIS

ONLY IN TANZANIA!!!!!!
 
Hakika kuishi kwingi ni kuona mengi. Sikutegemea katika maisha yangu kuwa itafika siku nchi yangu Tanzania ifanya madudu kama haya. SO SAD!!!!
 
Hizo zinaonekana kama pesa ndogo sana, lakini kwa wizara husika hizo ndio pesa ambazo huwa nje nje kuzipiga...
 
Na hao jamaa si wanaangalia mtu na mtu...yule jamaa yupo cool sana hivyo jamaa wametake advantage....ila wakashitakiwe kwani sio busara hata kidogo, eti wanaulizana ofisini.....anakuja nani kukabidhi...alafu wakiambiwa ni fulani.....wanashangilia na kubambika bahasha tupu....SO SAD....
Wamelikoroga lakini neno uwajibilkaji halipo tena vinginevyo Waziri na Katibu Mkuu wake walipaswa wawe wameachia ngazi
 
Hata wao waliopewa bahasha tupu ni wajinga hawakulalamika pale pale mpaka mtu mwingine aje aseme kwa niaba yao hii ndo hali ya watanzania tulivyo.
 
Hata wao waliopewa bahasha tupu ni wajinga hawakulalamika pale pale mpaka mtu mwingine aje aseme kwa niaba yao hii ndo hali ya watanzania tulivyo.

Injinia kitambo sana tangu umeachana na lile taasisi lenye ubabe. Mambo vipi lakini?
 
Hivi Wizara ya elimu mpaka ifanye madudu kiasi gani ndiyo hatua zichukuliwe? Kuna maana gani ya kuandaa sherehe kubwa hivyo wakati mambo ya msingi hayajakaa sawa?
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom