Dk Mselly Nzotta: Mtanzania anayetamba Kitaaluma Sweden(Je Kilichomo ndio Chanzo cha nyumba Lugoba?)

August

JF-Expert Member
Jun 18, 2007
8,391
4,056
Dokezo la Wadau



Dk. Mselly Nzotta: Mtanzania anayetamba kitaaluma Sweden



lC.gif
Godfrey Dilunga​


Aprili 6, 2011
rC.jpg

bul2.gif
Ni bingwa katika upembuzi wa chuma

bul2.gif
Apania kusambaza taaluma hiyo nchini


bul2.gif
Ikulu, Wizara ya Elimu, TIC wamuunga mkono

MACHI 30, mwaka huu, Mwandishi Wetu Godfrey Dilunga, alifanya mahojiano na mtaalamu wa masuala ya chuma (metallurgy) Dk. Mselly Nzotta, Mtanzania aliyeajiriwa katika kiwanda kikubwa cha chuma Sweden cha Uddeholm, akiwa Mtafiti Mwandamizi. Kutokana na utaalamu wake adimu Afrika ya Kati na Kusini, Dk. Nzotta ameanza mchakato na serikali ili kuanzisha chuo cha masuala ya chuma nchini, hasa ikizingatiwa kuwa Tanzania inaingia katika uzalishaji chuma Liganga. Yafuatayo ndiyo yaliyojiri katika mahojiano hayo.

Raia Mwema: Kwanza ungejitambulisha kwa wasomaji, kwa muhtasari tueleze historia yako.

Dk. Nzotta: Mimi ni Mtanzania, Shule ya Msingi nilisoma Ndungu, Wilaya ya Same, mkoani Kilimanjaro. Lakini kabla sijamaliza darasa la saba nikahamia kuendelea na masomo ya msingi katika Shule ya Msingi Amani, mkoani Tanga. Hapo Amani niliendelea kusoma darasa la tano hadi la saba.

Nilipomaliza elimu ya msingi nikafaulu na kupangiwa masomo ya sekondari kidato cha kwanza hadi cha nne katika Shule ya Sekondari Malangali, mkoani Iringa.

Kutoka Malangali, nikafaulu na kupangiwa masomo ya kidato cha tano na sita katika Shule ya Sekondari Kibaha, mkoani Pwani. Baada ya pale, nikaingia katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) katika masomo ya chemical engineering. Nilisoma chemical engineering kwa mwaka mmoja na nusu baadaye nikaitwa na NDC (Shirika la Maendeleo ya Viwanda) kwenda kusoma nchini Bulgaria. Kule Bulgaria nilikwenda kusomea mambo ya metallurgy (elimu ya masuala ya chuma).

Raia Mwema: Tueleze vizuri katika lugha ya kawaida isiyo ya kitaalamu, metallurgy ni nini hasa?

Dk. Nzotta: Metallurgy haina maana ya chuma moja kwa moja. Haina maana ya chuma ni kila metal (metali) inavyochujwa kutoka ore (mawe yenye madini) baada ya kuchimbwa mpaka kupata end-product (bidhaa ya mwisho kutengenezwa kwa mali ghafi hiyo). Huo mchakato wote wa kuchuja hadi kupata chuma ndiyo tunaita metallurgy.

Sasa katika metallurgy kuna aina tofauti. Kuna ferrous metallurgy ndiyo hiyo inayokwenda na kuwa chuma moja kwa moja, yaani mwishowe unapata chuma. Halafu aina nyingine ya pili kuna non-ferrous metallurgy hii ndiyo inayohusu products zisizo chuma ambazo ni kama vile aluminium au copper. Kwa hiyo ni maeneo mawili ya metallurgy. Kwa hiyo nilikwenda Bulgaria-Sofia kusomea metallurgy lakini nikibobea zaidi kwenye ferrous metallurgy.

Raia Mwema: Baada ya kurejea nchini kutoka masomoni Bulgaria uliendelea na shughuli hizo hizo na kule ulikwenda kusoma mwaka gani?

Dk. Nzotta: Baada ya kumaliza masomo hayo Bulgaria nilirudi NDC kwa kuwa tulipelekwa kusoma kwa ajili ya mradi wa chuma wa Liganga (mkoani Iringa). Tulipelekwa makundi mawili, mwaka 1982 na 1983 (wakati wa utawala wa Mwalimu Nyerere). Mimi niliondoka mwaka 1982 mwishoni.

Baada ya masomo na kurejea hapa nchini mwaka 1994 kwa ajili ya kufanya kazi inayohusu utaalamu tuliosomea, mambo hayakuwa kama ilivyopangwa. Wakatuambia kuwa mradi wa chuma Liganga haujakamilika.

Raia Mwema: Ulirudi ukiwa na kiwango gani cha elimu katika metallurgy?

Dk. Nzotta: Niliporudi nilikuwa na Master in Metallurgical Engineering (shahada ya uzamili). Sasa nilipoona mambo ya Liganga hayajawa tayari kama tulivyoelezwa, nikaona akili yangu na utaalamu wangu wote utaoza hapa (nchini). Kwa hiyo, nikaomba kwenda kusoma zaidi Sweden na nikapokelewa mwaka 1995 kwa ajili ya kuchukua masomo ya PhD (shahada ya uzamivu) upande wa Metallurgy.

Ikanichukua miaka minne kumaliza PhD. Nilimaliza Januari 1999. Unajua metallurgy ina mambo mengi. Sasa kule Sweden mimi nilikuwa najifunza mambo ya waste products (makapi)....ukishamaliza kuchoma chuma ndiyo unapata hizo taka. Kwa wakati ule nasoma kulikuwa na tatizo la kidunia juu ya namna ya kuondoa sulphur kutoka katika kwenye steel (chuma).

Katika lugha rahisi ni kwamba kama ilivyo kwenye matibabu ya daktari, daktari anapotaka kuchunguza au kujua afya ya mgonjwa anachukua vipimo kwa mfano vya haja kubwa au ndogo. Anakupima na kisha kutambua tatizo lako.
Hivyo ndivyo ilivyo kwenye masomo yangu kuhusu taka za vyuma. Ule uchafu (makapi) ndiyo unaotoa mwongozo wa kitaalamu katika kutambua chuma ina kiwango gani cha ubora. Ukishaona yale makapi ni mazima; yaani yenye ubora mzuri, basi, ni lazima chuma husika kiwe katika ubora sawa.

Raia Mwema: Tueleze ulisoma katika Chuo gani Sweden?

Dk. Nzotta: Nilipokuwa Sweden nilikuwa nasoma katika Sweden Royal Institute of Technology. Nimepata kuandika makala mbalimbali kuhusu metallurgy na tafiti zangu nyingi zipo kwenye mtandao wa google ukiandika jina langu unapata kila taarifa.

Raia Mwema: Utaalamu wako ni adimu nchini, kuna mpango gani wa kuhakikisha utaalamu huo unafundishwa nchini? Nini mchango wako?

Dk. Nzotta: Nilipokuwa pale Sweden chuoni Royal Institute of Technology, nilikuwa natambua kuwa Tanzania hakuna watalaamu wa metallurgy na wakati huo huo nchi yetu imejaa madini mbalimbali.

Kwa hiyo, kuanzia mwaka 1999 nikaanza mazungumzo na Royal Institute of Technology nikiwashawishi wasaidie kuanzisha chuo au maabara ya Material Science Tanzania hasa katika metallurgy.

Wazungu wakati wanatutawala, kwa maoni yangu naamini kwamba walitupa elimu zote kama mechanical engineering au medical lakini walichotunyima ni utaalamu huo kwa undani hasa wa material science (sayansi kuhusu malighafi). Walitunyima kabisa material science ambayo hata katika nchi zao ndiyo kiini cha maendeleo.

Huwezi kuendelea bila kujua namna ya kuongeza thamani bidhaa zako na ili kuongeza thamani lazima uwe na utaalamu au taaluma ya kufikia hivyo hatua kwa hatua.

Sitaki kuingia kwenye siasa, lakini nieleze tu kama ulivyouliza. Mpango wangu kuhusu utaalamu huu na Tanzania ulianza mapema wakati Rais wetu Jakaya Kikwete alipokuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.

Kule Sweden, pengine kwa sababu wanazo fedha za kutosha kiuchumi, kila mwanafunzi anayesoma shahada ya uzamili anakuwa na maabara yake yenye vifaa na akihitimu masomo yake vifaa hivyo vinatupwa.

Kwa hiyo, mimi nikaomba vile vifaa viletwe Tanzania ili kuanzisha maabara kwa ajili ya kufundisha wanafunzi wetu nchini hiyo material science.

Nilimueleza Kikwete (akiwa waziri), kwa sababu nilijaribu kuandika mapendekezo yangu huku Tanzania ili nisaidiwe kuhamisha tu vifaa hivyo kuleta Tanzania. Nilipenda vifaa viletwe Tanzania, na kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) tushirikiane kuanzisha masomo hayo (metallurgy).

Raia Mwema: Kwa wakati huo Waziri (Kikwete) alikueleza nini baada ya kueleza mawazo yako hayo yenye manufaa kwa Taifa?

Dk. Nzotta: Unajua kwa wakati ule akiwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa alikuwa pia amekwishawahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini, kwa hiyo nilijua anatambua umuhimu wa suala hilo.

Katika maelezo yangu kwake pia nilimuuliza kwamba kama anajua Tanzania ina dhahabu nyingi zaidi ya nchi ya Afrika Kusini, akanijibu kuwa ni ukweli anajua.

Kuna ramani niliyompa inayoonyesha kwamba kuna gold belt (mkondo/mkanda wa dhahabu) kutoka Ziwa Victoria umepitia katikati ya Tanzania, mkoani Dodoma mpaka kufika Afrika Kusini, lakini chimbuko lake ni Bukoba.

Nikamwuliza inakuwaje mwananchi wa Bukoba ana mali ya thamani kubwa chini ya ardhi kama hiyo, lakini hata kununua chumvi hawezi? Akanijibu kwamba; nimuandikie na akanipa anuani yake binafsi ili watu wengine wasinizubaishe katika ufuatiliaji wa mpango wangu.

Raia Mwema: Baada ya hapo nini kilifuata? Ulisaidiwa kuhamisha vifaa vya maabara kutoka Sweden?

Dk. Nzotta: Baada ya miaka kadhaa, wakaja (Kikwete) wakiwa na Mkapa (Rais) pale Sweden. Walivyokuja nikapata nafasi pia ya kujieleza kwa Mkapa. Tatizo lililokuwapo kwa wakati ule nilipokuwa najieleza nilimwita Mkapa “Mtukufu Rais”. Sasa kumbe huku nyumbani alikuwa amekwishakataza kuitwa hivyo. Mimi sikuwa na hizo taarifa, kwa hiyo nilikuwa kila mara nikimwita hivyo.
Alichukia sana nilipomwita “Mtukufu Rais”. Alikasirika kiasi cha maelezo yangu kutokuwa na maana tena kwake, na hakuna alichojibu zaidi ya kukasirika na kueleza kuwa watu wa Sweden “hatuna heshima”. Nilimweleza tena Waziri (Kikwete) lakini naye akasema hana cha kufanya tofauti na msimamo wa mzee (Rais).

Raia Mwema: Je, ulikata tamaa?

Dk. Nzotta: Hapana, sikukata tamaa. Kuna siku moja tukiwa ubalozini (Ubalozi wa Tanzania nchini Sweden) nilishauri kwamba kwa nini ubalozi wa Tanzania usianzishe database (hifadhi ya taarifa) ya Watanzania watalaamu? Unajua India ndiyo wanavyofanya, wanayo database ya wataalamu wao wote walioko nje ya nchi.

Hiyo inasaidia sana kwa sababu serikali inapokuwa na uamuzi wa mradi au jambo fulani unaohitaji watalaamu wa aina fulani, basi, inakuwa rahisi kwao kujua nani yuko wapi, na kumuita kwa sababu huyo ni Mtanzania; hata kama amechukua uraia wa nchi za nje.
Sasa pale ubalozini kulikuwa na ofisa mmoja ambaye kwa sasa yuko Ikulu (Dar es Salaam). Balozi hakuonyesha kuvutiwa sana na wazo hilo la database lakini huyo ofisa ubalozini pale alivutiwa na kuthamini. Ofisa mwenye anaitwa Mwaipaja kwa wakati ule alikuwa katibu wa balozi wetu Sweden.

Sasa, nilisahau kukueleza kuwa baada ya kumaliza masomo mwaka 1999 niliajiriwa na kiwanda cha chuma kule kule Sweden kinaitwa Uddeholm Tooling AB. AB ni kama Limited kwa hapa Tanzania.
Sasa yule Ofisa wa Ubalozi Mwaipaja akaja kunitembelea pale kiwandani kwetu na kukagua shughuli zangu, na kwa kweli mpaka leo yeye ndiye anayenihimiza; vinginevyo ni kama nilianza kukata tamaa.

Mwaka 2004 nikaja kwa nauli yangu wakati ule kulikuwa na Wizara ya Sayansi na Teknolojia, nikapangiwa nikutane na watu wa DIT (Dar es Salaam Institute of Technology) ili tuzungumzie suala la kuanzisha Steel Complex Tanzania (SCT) kwa ajili ya kutoa taaluma ya metallurgy kwa vijana wetu ili tunufaike zaidi na raslimali zetu.

Tukazungumza na mkuu wa DIT akaandika barua ili tuombe msaada SIDA (Shirika la Maendeleo la Sweden) kwa ajili ya kutafuta watalaamu, lakini nasikitika kwamba hapakuwa na msukumo au dhamira ya kutosha ya kisiasa.
Baadaye tena safari ya pili binafsi nikaja mwaka 2008. Nilikuja kama mwakilishi wa kampuni yangu ya Sweden nilikoajiriwa. Nikazungumza na watu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Unajua katika tunachokusudia kuanzisha (SCT) tumepanga katika maeneo tofauti ya utekelezaji au uendeshaji. Tumeona kwamba ili Tanzania iendelee watu au wanafunzi wafundishwe katika makundi makuu mawili.
Kundi la kwanza ni mafunzo ya kati (vocational training) lakini kundi jingine la pili ni watalaamu wa kiwango cha juu yaani chuo kikuu. Sasa nilifanya majadiliano na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, hii ni kwa ajili ya mafunzo au kuzalisha watalaamu wa kati (vocational) lakini pia nilijadiliana na Chuo Kikuu Dar es Salaam kwa ajili ya kuzalisha wataalamu wa kiwango cha juu.

Raia Mwema: Mwitikio wa Wizara na Chuo Kikuu Dar es Salaam ukoje? Kuna mwelekeo mzuri, hasa ukizingatiwa kuwa kuna ushindani wa kuzalisha watalamu katika nchi za Afrika Mashariki?

Dk. Nzotta: Watu waliojibu ilikuwa Wizara ya Elimu waliandika Memorandum of Understanding (hati ya maelewano) na Royal Institute of Technology (Sweden). Lakini tatizo ni kwamba walikosea wakaandika kwa upande wa vocational training pekee wakasema ndiyo inayowahusu.

Kwa hiyo, ikawa ule mkataba (hati ya maelewano) haukuweza kusainiwa ilibidi lazima pia tuwe na sehemu ya chuo kikuu. Mwaka jana nikaja tena na maofisa wa Royal Institute of Technology kutoka Stockholm na mwakilishi mwingine.
Sasa hapo Chuo Kikuu Dar es Salaam walizungumza na Royal Institute of Technology hadi wakafikia makubaliano lakini hadi leo chuo hicho hakijafanya mawasiliano tena na Royal Institute.

Raia Mwema: Ni kwa nini hawakufanya mawasiliano wakati haiwagharimu chochote kwa maana ya raslimali za uwekezaji?

Dk. Nzotta: Sijui hilo. Siwezi kulizungumzia, isipokuwa taarifa nilizonazo kutoka kwa wale jamaa wa Sweden ni kwamba hakuna mawasiliano yoyote waliyopata kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Kama nilivyokueleza, waliojibu na ambao ni kama vile wanayo nia ya dhati kufanikisha mpango huu wenye maslahi kwa Taifa ni Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, na hasa Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Profesa Dihenga na hata Waziri kwa kweli ameonyesha dhamira ya dhati.

Wizara imetusaidia sana. Baada ya wizara pia tulisaidiwa kukutana na watu wa NACTE (Baraza la Taifa la Mitihani) ambao nao kwa kweli wametuunga sana mkono. Tulipata ruhusa pia ya kutembelea kiwanda cha chuma cha M.M Steel (Dar es Salaam).

Raia Mwema: Vipi kuhusu kiwango cha utaalamu pale kiwandani M.M Steel. Tueleze kwa kuzingatia utaalamu wako.

Dk. Nzotta: Kwanza, hawa M.M Steel kuna wakati niliwahi kuhusika nao. Niliwahi kupinga namna ya uendeshaji wa mradi huo walipowahi kuniuliza maoni yangu kama mtaalamu.

Nilipokuja mwaka jana sikukubaliana na kiwanda kile kutengeneza sponge iron kwa sababu kiutaalamu, kwa kadri ninavyojua mimi na ndivyo ilivyo, ni kwamba ile iron ore (chuma ghafi iliyoko ardhini) ni mchanganyiko wa aina tatu tofauti. Kuna iron yenyewe, kuna vanadiuam na titanium.

Hizi aina zote ni kitu kimeshikana kwa pamoja sasa nikikwambia bei ya iron hiyo chuma kilo moja ni Crown 3 (fedha za Sweden) ambayo ni sawa na Sh. 600 za Tanzania kwa kilo, kwa kukadiria.

Vanadium bei yake kwa kilo moja ni Crown 600 ambayo ni kama zaidi ya Sh 100,000 za Tanzania kwa kilo, bei ya vanadium ni sawa na titanium. Swali kubwa hapa je, ni kwa nini utumie malighafi yenye vitu hivyo vitatu kuzalisha kitu kimoja pekee (chuma)? Kwa nini uzalishe iron pekee, unapeleka wapi vanadium na titanium ambazo ndizo zenye thamani kubwa zaidi ya iron?
Kwa nini wameng’ang’ania chuma na si vanadium au titanium? Kwa nini hiyo haizungumzwi katika hili Taifa? Kwa sababu kitaalamu kama atatumia kitu kama carbon kupunguza au kuchuja vanadium na titanium mabaki yanayopatikana (vanadium na titanium) yanakwenda wapi?

Raia Mwema: Utata huo unautafsiri vipi kitaalamu? Kuna uwezekano wa biashara nyingine ya siri hapo inayonufaisha ‘wajanja’ kimya kimya?

Dk. Nzotta: Kuna mawili hapo, nafikiri unanielewa. Nadhani kuna wanachokifanya. Inawezekana ni uzembe tu wa kupuuza mambo au pia inawezekana wanajua wanachokifanya kwa manufaa fulani.
Mimi niliwahi kuwakatalia Wizara ya Viwanda na Biashara pamoja na NDC kuhusu mradi huo, na hasa kutokana na utata huo lakini bado walitia saini mkataba na kazi inaendelea. Sitaki kuzungumzia hayo zaidi.

Raia Mwema: Kuna eneo jingine mlikotembelea kama mdau mkuu katika mpango huu wa elimu ya metallurgy nchini?

Dk. Nzotta: Ndiyo, tulikwenda Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) na kuzungumza na kiongozi wake anaitwa Ole Naiko. Tukazungumza naye akaonyesha kusitikishwa kwamba Tanzania haina watalaamu wa metallurgy, na ndiyo maana kuna hofu kuwa tunaibiwa.

Akatoa mfano wa dhahabu akatuambia; kumbe tunazo dhahabu za aina tatu, ile ya aghali zaidi ndiyo imezungukwa na madini ya sulphur sasa kwa sababu hawajui kuichambua hapa nchini inasafirishwa kupelekwa nje ya nchi.
Kwa hiyo, kimsingi naye aliunga mkono mpango wetu na pia tulikwenda Ubalozi wa Sweden nchini na kuwasilisha mapendekezo yetu (presentation). Nao pia walifurahia mpango huo na kuunga mkono.
Baada ya hapo tulikutana na Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo akaunga mkono. Kwa hiyo upande wa Serikali kuna baraka zao isipokuwa ule msukumo wa haraka kisiasa ndiyo unaohitajika. Tulitembelea pia VETA Arusha na Technical College.

Raia Mwema: Kwa kawaida mafunzo ya kiuhandisi hasa yanahitaji mafunzo kwa vitendo. Mpango wetu wa kutoa elimu unasemaje kuhusu hili? Mafunzo kwa vitendo itakuwaje?

Dk. Nzotta: Mpango wetu wa Steel Complex Tanzania- Mission (SCT) unaonyesha tutaanzisha chuo na wanafunzi wa kwanza watahitimu baada ya miaka mitatu ya kwanza.
Watafundishwa kwa level one, two na three inategemea na kozi watakazojiunga. Lakini kuna kitu kingine ni kwamba tunataka tukishawafundisha kuwe na viwanda vidogo vya metallurgy ili wafanye mafunzo kwa vitendo na hiyo ya viwanda vidogo ni awamu ya pili ya mradi.

Tulipokuwa kule Arusha tuliona pengo la kwanza ni kwamba tuna fursa hapa Tanzania ya kutengeneza vipuri lakini suala la mchakato wa kuyeyusha chuma na kuchuja hakuna maabara kwa kweli. Ni kama vile kuwandanganya wanafunzi na upotevu wa fedha.
Tunahitaji mpango huu ili tuweze kutoa elimu ya uhakika na itakayokuwa na viwango vya kimataifa katika suala hili la metallurgy.

Raia Mwema: Tueleze faida nyingine za ziada za mpango huu.

Dk. Nzotta: Mpango wote huu jukumu lake kuu ni kupunguza umasikini kwa kuibua ajira. Pia ni pamoja na kuinua uchumi. badala ya kuendelea kuuza bidhaa zikiwa ghafi ni lazima sasa tuwe na uwezo madhubuti wa viwango vya kimataifa katika kutouza bidhaa ghafi.
Nimepita pale Arusha kwa mfano, kuna tanzanite madukani ambazo mwananchi hawezi kununua kwa sababu bei ni aghali mno licha ya kwamba madini yale yanachimbwa Arusha. Lakini yamekuwa aghali kwa sababu yalichimbwa na kusafirishwa kwenda kutengenezewa bidhaa nje ya nchi.

Kama umesikia, wachina wamepewa ule mradi wa chuma Liganga. sasa itabidi tu waje na watu wao kwa sababu hapa nchini hatuna watalaamu tuliowaandaa. Watakuja na wataalamu wao na kwa hiyo kwa sehemu fulani mradi huo utakuwa ni kama vile wa kupunguza umasikini China na kuongeza umasikini Tanzania, kwa sababu watalaamu na kampuni zao ndizo zitakazofanya kazi na kulipwa fedha zitakazonufaisha uchumi wa China. Unakuwa unaimarisha suala la ajira China.

Raia Mwema: Unaweza kujua mko wataalamu wangapi wa aina yako nchini?

Dk. Nzotta: Kwa utaalamu katika kiwango changu (PhD-Metallurgy) sidhani kama yuko mwingine Afrika Mashariki na Kati. Nadhani ni Afrika Kusini ambako wapo kadhaa. Kuna Watanzania tulisoma nao Bulgraia wana masters (shahada za uzamili) lakini hawajazitumia. Sasa huwezi kusema, kwa maana hiyo, kuna watalaamu moja kwa moja kwa sababu miaka mingi imepita bila utaalamu wao kutumika.
hs3.gif


Simu:
0787-643151​
 
Back
Top Bottom