Diwani: Nimechoka kugeuzwa bodaboda

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
266
DIWANI wa Kata ya Kwakoa wilayani Mwanga, Dk. Rogers Msangi amekieleza kikao cha Baraza la Madiwani wilayani humo, kwamba amechoka kugeuzwa kuwa pikipiki ya kubeba abiria maarufu kama bodaboda kutokana na kubeba wagonjwa katika kata yake na kuiomba Halmashauri ya Wilaya kumpatia gari la wagonjwa.

Mbele ya kikao hicho chini ya Mwenyekiti wake,Theresia Msuya, Mbunge wa Mwanga, Profesa Jumanne Maghembe na Mkuu wa Wilaya hiyo, Athuman Mdoe, Diwani Dk. Msangi alisema wananchi wa Tarafa ya Jipendea wanateseka kwa kukosa gari la wagonjwa.

“Mheshimiwa Mwenyekiti katika kata yangu nimekuwa kama Bodaboda, ninatumia gari langu kubeba wagonjwa, sipati hata muda wa kulala...yupo mwalimu mmoja aling’atwa na nyoka nikalazimika kumpeleka hadi Hospitali ya KCMC, tusaidieni gari la wagonjwa,” alisema.

Alisema ni vyema kama halmashauri hiyo itatenga gari kwa ajili ya maeneo ya Tambarare, mbali na makao makuu ya wilaya, na kutoa mfano kuwa wagonjwa waliopo Mwanga Mjini hawawezi kukosa usafiri kwa kuwa wapo katika barabara kuu ya Dar es Salaam -Moshi.

Kutokana na maombi hayo Halmashauri ya Wilaya imetoa kipaumbele kwa wananchi wa tarafa hiyo iliyopo maeneo ya tambarare kwamba watapatiwa gari la wagonjwa kwenye vituo vya afya na zahanati za tarafa hiyo yenye kata tano.

Akizungumzia suala hilo Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Msuya alisema magari yatakayopatikana wakati wowote kuanzia sasa, moja litapelekwa katika tarafa hiyo ambayo wananchi wake hawana huduma ya gari la wagonjwa.

Msuya alisema kata zitakazonufaika mara baada ya kupatikana kwa gari hilo ni Kwakoa,
Kigonigoni, Jipe, Kivisini na Toloha ambako wanalazimika kubeba wagonjwa kwenye machela na wakati mwingine punda ili kuwapeleka hospitali wakati wanapozidiwa.

Katika hatua nyingine Mbunge ambaye pia ni Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Profesa
Maghembe aliwataka madiwani kuchangia hoja mbalimbali kwa kujali maendeleo ya wilaya kwa ujumla wake badala ya kila diwani kutaka eneo lake pekee lipewe kipaumbele.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom