Dhariri ya Mobutu ilivyoleta fahari ya Lumumba baada ya miaka 61 kupita

Comred Mbwana Allyamtu

JF-Expert Member
Jun 28, 2016
348
847
TUNU NA FAHARI ALIYO ACHA LUMUMBA BAADA YA KIFO CHAKE NA DHALILI YA WATESI WAKE.

Na. Comred Mbwana Allyamtu (CMCA)
Sunday -3/07/2022
Marangu Kilimanjaro Tanzania.

Mwaka huu Patrice Émery Lumumba, shujaa wa uhuru na waziri mkuu wa kwanza wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, anatimiza miaka 97 toka kuzaliwa kwake, Lumumba alizaliwa tarehe 2 Julai mwaka 1925 katika mji ambao sasa unaitwa Lumumbaville.

Mbali na hilo wiki iliyopita ya tarehe 30 mwezi huu wa 6 mabaki ya Lumumba (jino lake) yalizikwa kwenye viwanja vya uhuru eneo la mtaa wa Limeté, katikati ya Jiji la Kinshasa, eneo hilo kuna mnala unaoitwa Tour de l’échangeur au Mnara wa Limete.

Ngoja nieleza kidogo hapa...

Huu mnala wa Tour de l’échangeur upo katika ya jiji la Kinshasa, mara nyingi mnara huu pia huitwa Mnara wa Eiffel wa Kongo, ujenzi wa mnara huo ulianza chini ya utawala wa Mobutu mwaka 1970 na ulikamilishwa na Joseph Kabila mwaka 2011, utaona ujenzi wake kuwa ulichukuwa mda refu kutoka kipindi cha Mobutu ujenzi ulisitiswa na kipindi cha utawala wa rais Joseph Kabila alianza tena ujenzi wake na kuukamilisha mwaka 2011.

Mnara huo umeundwa na nguzo nne ambazo zina urefu wa mita 210 kwenda Juu, mnara umewekwa nyuma ya sanamu la Patrice Lumumba na kushoto kuna jumba la makumbusho ya kumbukumbu ya Lumumba ambalo hufunguliwa kila siku asubuhi.

Mbele ya mnara huu ndio lilipo jengwa kaburi la Lumumba (ambapo jino lake limezikwa), juu ya kaburi hilo kuna sanamu kubwa la Patrice Lumumba.

Unaweza kuuliza kwanini serikali ya Kongo imeamua kuzika jino la Lumumba kwa sherehe kubwa kiasi hicho? Jibu la hilo na mengine ntaeleza huko mbeleni.

Ila kwasasa ntaeleza dhariri ya Mobutu ilivyo leta fahari ya Lumumba baada ya miaka 61 kupita.

Lumumba aliuwawa miezi michache tu baada ya kuingia madarakani, kifo cha Lumumba kiliinjiniwa na Ubelgiji na shirika la kijasusi la CIA la Marekani chini ya maelekezo ya Rais wa Marekani Eisenhower ambae ndie aliye idhinisha kuuawa kwa Lumumba, kuhusu hilo nimelieleza kwa upana kwenye makala yangu ya Operation Barracuda unaweza kuisoma kupita link hii Operation Barracuda: "Mission hatari ya kijasusi nchini Kongo"

Pamoja na hayo kifo cha Lumumba ndani ya nchi ya Kongo kiliratibiwa na kusimamiwa na Mobutu Seseseko Kuku Ngwendu Wazabanga Wazaire Ngwadu (Joseph Desiree Mobutu).

Huyu Mobutu aliyebariki mauaji ya kinyama ya Lumumba mpaka leo mwili wake aujazikwa Kongo, Serikali ya Kongo na wananchi waligoma mwili wake kurudishwa nchini Kongo japo kumekuwepo kwa maombi ya familia yake na watu wa kijijini kwao Gebdolite kutaka mabaki ya mwili wa Mobutu urejeshwe Kongo.

Mwili wa Mobutu umezikwa kwenye makaburi ya watu wa kawaida wasio wenyeji nchini Morocco, ikumbukwe kuwa Mobutu umauti ulimkuta nchini Morocco na kuzikwa huko baada ya serikali ya Kabila mzee kugomea mwili wake usirejeshwa Kongo kwa mazishi.

Mobutu umauti ulimkuta nchini Morocco ambako alikimbilia huko akitokea nchini Togo, baada ya kupinduliwa, umauti ulimfika mnamo tarehe 7 September 1997 baada ya kusumbuliwa kwa muda mrefu na ugonjwa wa Tezi dume.

Mazishi ya Mobutu hayakufanyika kitaifa, alizikwa na watu tisa kutia ndani familia yake na watu wa jiji la Rabat wanaozika watu wasio na ndugu.

Mwili wake ulizikwa bila heshima yoyote ile, hakuna yoyote kutoka Kongo aliye hudhuria kuondoa familia yake, Mobutu ambae alikuwa tajiri mwenye majivuno mwisho wake ulikuwa mbaya, alizikwa kama kibaka na hakuna aliye mpatia heshima za mwisho.

Mobutu kipindi kile Lumumba anauwawa aliamlisha mwili wa Lumumba uchomwe moto ili watu wasije kwenda kutoa heshima yoyote kwenye kaburi lake kwa kumuenzi, alio waamrisha kuchoma moto mwili wa Lumumba wao wakaamua kuutumbukiza kwenye tindikali mwili wa Lumumba ili kupoteza ushahidi wote.

Sasa turejee kwanini mabaki ya Lumumba yamezikwa kwa heshima zote za kitaifa?

Kwanza cha kuelewa ni kwamba, toka kifo cha Lumumba mpaka sasa imeshapita zaidi ya miaka 60, hakuna mahali mwili wake ulipatikana ili apewe heshima yake, Nikueleze tu ni kwamba nchini Kongo Patrice Lumumba anaheshimiwa kuliko kiongozi yoyote yule nchini Kongo DRC.

Machungu ya wakongo kumpoteza Lumumba yanaishi mpaka leo, Patrice Lumumba na Laurent Desiree Kabila utazamwa kama mashujaa wa taifa hilo.

Kumekuwepo mijadala kadhaa ya kumpa hadhi Lumumba kwa kuibadilisha jina uwanja wa ndege wa Ndjili kuitwa Patrice Lumumba, Picha yake kutiwa kwenye note ua sarafu, jengo la ikulu kuitwa Patrice Lumumba palace na siku maalumu ya kifo chake kuwa siku ya mapumziko.

Mpaka sasa Mji wa Katakakombe huko Sankuru umeitwa Lumumbavile, tarehe ya Uhuru kujumuishwa na kumbukumbu ya maisha ya Lumumba, mchakato wa kuibadilisha jina uwanja wa ndege wa Ndjili unaendelea, yote ni kumpa heshima stahiki Lumumba.

Lumumba alikosa yote hayo kwakuwa Mwili wake baada ya kuuwawa uliwekwa kwenye tindikali, huku wauwaji wakibakia na jino ambalo ndio mabaki yake ambayo hatimaye yamerejeshwa kutoka Ubelgiji na kuzikwa kuashilia heshima ya mwasisi wa taifa na shujaa wao ambae sehemu ya mwili wake hatimae imezikwa kwenye aridhi ya Kongo.

Kama nilivyo tangulia kusema huko nyuma kuwa operation ya kumuua Lumumba iliitwa "Operation Barracuda", sitoileza sana hapa ila ntaieleza kwa uchache sana ili uone unyama aliofnyiwa Lumumba na ujue kwanini wakongo wameamua kufanya mazishi ya kitaifa ya mapumziko siku tatu na kutembeza jeneza la mabaki ya Lumumba nchi nzima kuanzia Kinshasa, Lubumbashi, Kisangani, Lumumbavile,Bukavu, Goma na maeneo yote ya Kongo.

Nikukumbushe Operation Barracuda...

Alhamisi ya Juni 30, 1960, Congo ilijipatia uhuru kutoka kwa Ubelgiji, Waziri Mkuu Patrice Emery Lumumba akiwa na miaka 35, akawa kiongozi wa jamhuri hii mpya, Lakini hali ya amani na utulivu ikatoweka muda mfupi baadaye, Kikosi cha majeshi ya waasi kikazua vurugu kiasi kwamba Ubelgiji ilipeleka jeshi lake kulinda raia wake.

Siku chache baadaye, Jumatatu ya Julai 11, ya mwaka huo, Jimbo la Katanga, lililokuwa likiongozwa na Moise Kapenda Tshombe likajitenga. Umoja wa Mataifa ukaingilia kati kwa kutuma jeshi la kulinda amani.

Jumanne ya Januari 17, 1961, miezi sita tu baada ya uhuru wa Congo, Patrice Lumumba aliuawa katika Jimbo la Katanga. Februari 13, maofisa wa Jimbo la Katanga wakatangaza kifo cha Lumumba, lakini hakuna aliyewaamini, Hata wao hawakuziamini taarifa walizotoa, Lawama zikaanza kumiminika kutoka pande zote za dunia.

Urusi iliwashutumu mabeberu na kuitaka Marekani iondoe watu wake Congo, pia ikamtaka aliyekuwa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, Dag Hammarskjold, kujiuzulu kwa sababu alionekana kuwa kibaraka wa wakoloni.

Katika jiji la Moscow nchini Urusi watu waliandamana baada ya kupata taarifa za kuuawa kwa Lumumba, Katika jiji la Beijing, China, kulifanyika maandamano makubwa ya watu waliokadiriwa kuwa zaidi ya 100,000. Katika nchi mbalimbali raia walivamia balozi za Ubelgiji na kufanya uharibifu.

Ndani ya mwaka mmoja tangu kuuawa kwa Lumumba, Umoja wa Mataifa ulifanya uchunguzi na baadaye ikabainika kuwa hata Shirika la Kijasusi la Marekani (CIA) lilishiriki katika njama za kumuua Lumumba.

Katika ukurasa wa 198 wa kitabu “The African Liberation Struggle: Reflections” cha Godfrey Mwakikagile, jasusi wa Marekani, Stephen Andrew Lucas, ambaye alikuja Tanzania na kufundisha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alikuwa Congo na kufanya kazi chini ya mkuu wa CIA, Larry Devlin, wakati Lumumba alipokamatwa na kuuawa. Mwingine aliyekuwa Congo na baadaye akaenda Zanzibar ni Frank Carlucci.

Pamoja na Lumumba walikuwako wengine wawili waliokamatwa na kuuawa pamoja naye; Joseph Okito (alikuwa Naibu Spika wa Bunge la Congo) na Maurice Mpolo (alikuwa Waziri wa Vijana na Michezo). Watatu hao walisafirishwa kwa ndege kutoka Kinshasa hadi mji mkuu wa Kalonji wa Bakwanga (sasa unaitwa Mbuji-Mayi).

Wakiwa kwenye ndege aina ya DC-3, wote watatu waliteswa kikatili na walinzi wa Congo. Ndege ilipowasili anga la Bakwanga, rubani hakuweza kutua kwa sababu uwanjani hapo kulikuwa kumetapakaa matanki ya ujazo wa galoni 55.

Rubani aliamua kwenda kutua Uwanja wa Elisabethville (sasa Lubumbashi), na ndege ilipotua, Lumumba alikuwa anakaribia kuzirai kutokana na maumivu.

Ndani ya ndege walikuwa wakiteswa mbele ya Kamishna wa Ulinzi wa Congo, Ferdinand Kazadi na Kamishna wa Mambo ya Ndani wa Congo, Jonas Mukamba. Walipofikishwa Lubumbashi walipelekwa kwenye nyumba jirani na Uwanja wa Ndege wa Luano na kuendelea kuteswa.

Lumumba, ambaye uso wake uliharibiwa kiasi cha kutotambulika kutokana na vipigo na nguo zake zikiwa zimetapakaa damu, alisimamishwa kwenye kichuguu kikubwa huku akimulikwa na taa za magari.

Kwa amri ya Moise Tshombe, rais wa jimbo la Katanga ambaye naye alikuwa akipokea maelekezo kutoka Brussels, Lumumba aliteswa. Kikosi cha mauaji kilimtoa Lumumba katika nyumba alimokuwa akiteswa na kumsafirisha kwa mwendo wa dakika 45 hadi Katanga.

Hapo aliuawa na kikosi cha mauaji kwa kupigwa risasi kwa amri ya Kapteni wa Ubelgiji, Julien Gat, Aliyemfyatulia risasi ni askari wa Ubelgiji, kanali Carlos Huyghe, Mwingine aliyeshiriki kuwafyatulia risasi na kuwaua Okito na Mpolo ni kapteni Julien Gat.

Kupoteza ushahidi...

Baada ya kuuawa kwa risasi, miili ya watatu hao ilizikwa eneo walilouawa. Kwa hofu kwamba kaburi la Lumumba lingegundulika na baadaye lingeweza kugeuzwa kuwa eneo la heshima, Wabelgiji na vibaraka wao waliamua kupoteza ushahidi ambao ungeweza kuelekeza uliko mwili wake.

Jumatano ya Januari 18, ikiwa ni siku moja baada ya mauaji hayo, miili ya kina Lumumba ilifukuliwa na kupelekwa ndani zaidi msituni na kuzikwa upya karibu na mpaka wa Rhodesia (Zimbabwe) na Congo.

Usiku wa Jumapili ya Januari 22 ndugu wawili wa Ubelgiji Kamishna wa Polisi wa Ubelgiji, Gerard Soete na ndugu yake walikwenda tena kufukua miili ya Lumumba, Okito na Mpolo. Safari hii walikuwa na shoka na misumeno.

Waliikatakata miili hiyo vipande vipande kabla ya kuyeyusha mabaki yake kwa tindikali iliyokuwa imejaa kwenye pipa la petroli la lita 200. Baadaye Soete alikiri kwamba alitumia koleo kung’oa meno mawili ya Lumumba kwa ajili ya ukumbusho.

Operesheni Barracuda...

Katika kitabu cha “Encyclopedia of leadership: A-E” (ukurasa 925), George R. Goethals na Georgia Sorenson wanasema mpango wa kumuua Lumumba uliitwa ‘Operesheni Barracuda’ na uliandaliwa na Marekani, hususan CIA, ndipo Lumumba akakamatwa na Kanali Mobutu Oktoba 10, 1960.

Katika kikao kilichofanyika jijini Washington, Marekani iliamriwa Lumumba aondolewe madarakani na awekwe kiongozi ambaye angekubali kulinda maslahi ya Wamarekani nchini Congo.

Maagizo hayo yakatumwa kwa mkuu wa CIA nchini Congo, Lawrence Raymond Devlin. CIA wakaunganisha nguvu zao na Ubelgiji.

Agosti 1960, msaada wa kijeshi kutoka Urusi uliingia Congo, jambo ambalo halikuwapendeza Wamarekani na Wabelgiji. Ilikuwa lazima Lumumba aondoke kwa gharama zozote.

Ndipo wakamshawishi Rais wa Congo, Joseph Kasavubu, lakini waligonga mwamba. Devlin akaripoti taarifa hizo makao makuu ya CIA jijini Langley, Marekani, Agosti 24, 1960.

Dk Sidney Gottlieb, mtaalamu wa dawa, akapewa maagizo ya kutafuta sumu ya kumuua Lumumba na isijulikane kuwa Marekani imehusika, na iwe ni dawa ambayo chanzo chake ni Afrika.

Nakurudisha mwezi January...

Januari 1960 Wabelgiji walilazimika kuita mkutano katika jiji la Brussels, Ubelgiji, katika mkutano huo maalum ndipo ilipokubaliwa Congo watapewa uhuru wao Juni 30 ya mwaka huo.

Baada ya ghasia zilizozuka Oktoba 23, 1959 na kudumu hadi Oktoba 28, 1959 na baada ya Patrice Lumumba kukamatwa na kuhukumiwa kifungo gerezani baada ya chama chake kusababisha ghasia hizo, Serikali ya Ubelgiji ilichapisha ripoti kuhusu ghasia hizo.

Jumapili ya Novemba 1, 1959 Lumumba alikamatwa na Serikali ya kikoloni na kumhukumu kifungo cha miezi sita gerezani. Tofauti na ilivyodhaniwa awali, kifungo hicho kiliongeza umaarufu wa Lumumba. Katika ghasia hizo iliripotiwa watu 30 waliuawa.

Theodore Trefon katika kitabu ‘Reinventing Order in the Congo: How People Respond to State Failure in Kinshasa’ anasema ghasia zilizokuwa mbaya zaidi katika historia ya Congo ni zile za kati ya Januari 4 na 6, 1959. “Karibu raia wote Waafrika waliingia mitaani kufanya vurugu”.

Ghasia hizo zilianza polisi wa Ubelgiji walipovamia mkutano wa chama cha Abako na kuwatawanya wafuasi wake, Kwa mujibu wa andiko linaloitwa ‘The Congo Operation, 1960—63’ la Birendra Chakravorty, zaidi ya watu 100 waliuawa, Hata kabla ripoti hiyo haijachapishwa, mkutano uliofanyika mjini Brussels, Ubelgiji na kumalizika Jumanne ya Januari 13, 1959 uliamua kwamba wakati wa Congo kupewa uhuru wake umefika.

Mpango wa kuwakabidhi Wakongo Serikali ya kujitawala wenyewe uliandaliwa tangu Desemba 1955 na kutangazwa Februari 1956, Aliyeifanya kazi hiyo ni Profesa wa Ubelgiji kutoka Chuo Kikuu cha Antwerp aliyeitwa Anton Arnold Jozef “Jef” Van Bilsen.

Mpango huo ulipewa jina la “Thirty Year Plan for the Politial Emancipation of Belgian Africa”,
Alipendekeza kuwepo mpango wa miaka 30.

Pendekezo hilo la Desemba 1955 aliliita “Mpango wa Miaka 30”, Kwa maneno mengine, ikiwa ushauri wa Profesa Bilsen ungefuatwa, Congo ingejipatia uhuru wake mwaka 1985.
Karibu kipindi chote cha mwaka 1959 Congo iligubikwa na ghasia. Kuona hivyo, Januari 1960 Serikali ya Ubelgiji iliitisha mkutano mjini Brussels ambao vyama vyote vikubwa vya siasa na viongozi wa makabila makubwa ya Congo walihudhuria.

Mkutano huo ulitawaliwa na madai ya “uhuru sasa”. Baada ya shinikizo kuwa kubwa, Ubelgiji waliamua kwa shingo upande kuwapatia Wakongo uhuru wao ifikapo Juni 30 ya mwaka huo, Wakati wa kampeni za uchaguzi za Aprili 1960 vyama vingi viligombea viti vya ubunge.

Vyama vikubwa vilivyoshiriki uchaguzi huo ni MNC cha Patrice Lumumba kilichokuwa na sera ya kuiunganisha Congo yote iwe moja, na kingine ni kile cha Joseph Kasavubu cha Alliance des Bakongo (Abako), Katika uchaguzi uliofanyika kuanzia Mei 11 hadi 25, 1960, Lumumba na waungaji mkono wake walipata ushindi mkubwa wa viti bungeni akifuatiwa na Kasavubu, wakalazimika kugawana madaraka.

Kasavubu alikubali kuwa Rais wa nchi na Lumumba akiwa mtendaji mkuu wa serikali, yaani Waziri Mkuu, Juni 23, 1960 Lumumba aliapishwa kuwa Waziri Mkuu wa Congo na, Juni 30, 1960, ikawa ndiyo siku ya uhuru wa Congo.

Siku hiyo na siku tatu baadaye zikatangazwa kuwa siku za mapumziko ili raia washerehekee uhuru wao, Katika sherehe hizo kila kitu kilionekana kufanyika katika hali ya amani, Ofisi ya Lumumba ilikuwa na shughuli nyingi huku kukiwa na msururu wa watu kuingia na kutoka huku Lumumba akijishughulisha na ratiba ndefu ya mapokezi ya wageni.

Siku ya uhuru Lumumba alitangaza kuwa Jumapili ya Julai 3 ingekuwa siku ya msamaha wa jumla kwa wafungwa wote, Lakini tangazo hilo halikutekelezwa na Julai 4, Lumumba aliita kikao cha Baraza la Mawaziri kujadili machafuko ya wanajeshi wa Congo.

Wanajeshi wengi waliokuwa na matumaini makubwa kwamba mara baada ya uhuru kupatikana wangepandishwa vyeo na kuongezewa maslahi, walianza kufanya fujo baada ya kuona matarajio yao hayatimii, Ingawa ilikuwa ndani ya wiki moja tu tangu uhuru kupatikana, baadhi yao waliona kuwa Lumumba hatimizi matarajio yao haraka kama walivyotarajia awali.

Bunge lililokutana katika kikao cha kwanza tangu uhuru na kuanza kazi ya kutunga sheria, kilipiga kura ya nyongeza yao ya mishahara. Lumumba alishtushwa na kitendo hicho cha Bunge lake. Kwa kujua hatari ambayo ingesababishwa na kitendo hicho, Lumumba alikiita “upumbavu wa uharibifu.”
Julai 5,, Kamanda wa Jeshi la Congo, Jenerali Emile Janssens, ambaye alikuwa Mbelgiji, aliwaita maofisa wa jeshi na kuwataka wadhibiti hali ya amani. Alisisitiza kuwa hali ilivyokuwa kabla ya uhuru ndivyo itakavyokuwa baada ya uhuru. Lakini tangazo hilo halikutuliza hasira ya baadhi ya wanajeshi.

Siku iliyofuata yaani Julai 6 ambayo ilikuwa siku ya sita tu baada ya uhuru Lumumba aliwapandisha vyeo askari wa Congo kwa ngazi moja lakini hali ya ghasia ilipozidi kuwa mbaya, Lumumba alimfukuza kazi Jenerali Janssens.

Siku mbili baadaye, Ijumaa ya Julai 8, Lumumba aliwaondoa maofisa wote wa kijeshi wa Ubelgiji na kuweka wa Congo ingawa Wazungu kadhaa waliendelea kubaki jeshini kama washauri, Julai 9 Balozi wa Marekani Congo, Clare Hayes Timberlake, alituma taarifa kwenda Marekani, akidai Ubelgiji wakiingilia mgogoro wa Congo kutakuwa na maafa.

Julai 10 Ubelgiji walituma wanajeshi kwenda Congo kuwalinda raia wao na biashara zao. Kasavubu na Lumumba waliigeukia Marekani kuomba msaada wa kulipanga upya jeshi la Congo, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Marekani ikasema Marekani iko tayari kusaidia lakini chini ya usimamizi wa Umoja wa Mataifa na uongozi wa Ubelgiji.
Julai 11 Moise Tshombe akatangaza kuwa Jimbo la Katanga limejitenga na Congo na kisha akalitangaza kuwa liko huru huku akiiomba Ubelgiji walitambue na wapewe misaada.

Jumanne, Julai 12 Kasavubu na Lumumba waliiomba Marekani msaada kudhibiti uchokozi wa Wabelgiji na siku hiyo hiyo baraza la mawaziri lilikutana bila Lumumba na Kasavubu kuwapo kwenye kikao, na wakaomba wapewe wanajeshi 3,000 wa Marekani, Rais wa Marekani, Dwight David Eisenhower, aliamuru vikosi vya nchi yake, vikiwa na zana za kivita, kwenda Congo ikiwa Waziri Mkuu wa Urusi, Nikita Krushchev, angetuma majeshi yake kwenda huko.

Jumatano, Julai 13, Urusi iliutaka Umoja wa Mataifa kuzuia uchokozi wa Ubelgiji nchini Congo. Alhamisi ya Julai 14 Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio la kupeleka jeshi Congo. Siku hiyo hiyo Lumumba na Kasavubu wakawasiliana na Urusi na kuwaomba wafuatilie hali ya Congo. Urusi ilikubali.

Ijumaa, Julai 15, majeshi ya Umoja wa Mataifa yaliwasili Congo. Julai 16, baada ya kukutana na Lumumba, mwakilishi wa Umoja wa Mataifa nchini Congo, Ralph Bunche, aliripoti “Lumumba alikuwa kama kichaa na alitenda mambo kwa tabia za kitoto.” Lumumba na huyo Bunche hawakuelewana vizuri.

Baada ya hali kuzidi kuwa mbaya, Jumapili ya Julai 17 Lumumba alitishia kuwa atayaita majeshi ya Urusi ili yasaidie kuyaondoa majeshi ya Umoja wa Mataifa kama watashindwa kuyaondoa majeshi ya Ubelgiji ndani ya saa 72.

Ijumaa, Julai 15, majeshi ya Umoja wa Mataifa yaliwasili Congo. Julai 16, baada ya kukutana na Lumumba, mwakilishi wa Umoja wa Mataifa (UN) Congo, Ralph Bunche, aliripoti, “Lumumba alikuwa kama kichaa na alitenda mambo kwa tabia za kitoto.” Lumumba na Bunche hawakuelewana vizuri.

Baada ya hali kuzidi kuwa mbaya, Jumapili ya Julai 17 Lumumba alitishia kuwa atayaita majeshi ya Urusi ili yasaidie kuyaondoa majeshi ya Umoja wa Mataifa kama watashindwa kuyaondoa majeshi ya Ubelgiji ndani ya saa 72, Hali ya utulivu na amani ilipozidi kudorora Congo katika zile siku chache baada ya uhuru, Lumumba aliwatishia Umoja wa Mataifa kuwa atayaita majeshi ya Urusi ili yamsaidie kulinda amani Congo na kujikuta akirushiana maneno na Bunche.
Jumamosi Julai 9, 1960, ikiwa ni siku tisa tangu ijipatie uhuru, Serikali ya Congo ilibadili jina la jeshi kutoka ‘Force Publique’ na kuwa ‘Armee Nationale Congolaise’ (ANC).

Baraza la Mawaziri lilimteua Victor Lundula, mwafrika aliyepigana katika Vita Kuu II ya Dunia, kuwa jenerali wa kwanza mkuu wa majeshi ya Congo na kuchukua nafasi ya Jenerali Emile Robert Alphonse Janssens ambaye alikuwa Mbelgiji, Lumumba alimteua pia Joseph-Desire Mobutu kuwa mmoja wa mawaziri wadogo katika ofisi ya Waziri Mkuu, kama kanali na mnadhimu mkuu wa ANC, Kitabu ‘The Congo: From Leopold to Kabila: A People’s History’ cha Georges Nzongola-Ntalaja katika ukurasa wa 98 kinasema uteuzi wa watu hao wawili Lundula na Mobutu ulitolewa vibaya, “Lundula hakuwa na sifa zinazohitajiwa kuendesha jeshi la nchi, hususan jeshi jipya.

Na kwa Mobutu, Lumumba alifanya kosa kubwa kwa kuamini tu kwamba ana uwezo wa kusimamia jeshi kwa vile aliweza kuwasimamia watu wachache waliomzunguka.”
Kitabu hicho kinasema “(Lumumba) hakusikiliza uvumi uliosambaa uliodai Mobutu alikuwa wakala wa majasusi wa Ubelgiji na Marekani. Kwa kumteua Mobutu kushika wadhifa huo, tayari (Lumumba) alikuwa amemchagua Yuda wake mwenyewe.”

Mwandishi wa historia, Didier Ndongala Mumbata, alilifafanua zaidi katika kitabu ‘Patrice Lumumba, Ahead of His Time’. Mumbata anaandika kuwa matukio ya kati ya Julai na Septemba 1960 yalibadili sana uhusiano wa Lumumba na baadhi ya mawaziri wake na wanasiasa wenzake. Alionekana kupigana vita mwenyewe, Mambo yalipokuwa mazuri alizungukwa na marafiki na ‘wapongezaji’ wengine wa kweli na wa uongo. Mambo yalipokwenda mrama alijikuta yuko mwenyewe.

Mobutu, ambaye alikuwa rafiki yake wa karibu na ambaye awali alimteua kuwa msaidizi wake katika chama chake cha MNC, kisha akamwingiza serikalini baada ya kuwa waziri mkuu wa kwanza wa Congo, na baadaye akamfanya kuwa mnadhimu mkuu wa jeshi la Congo, alimsaliti na kujiunga na kambi ya Joseph Kasavubu. Wote wawili, Kasavubu na Mobutu walishiriki kwa kiasi kikubwa kumwangusha na kumuua Lumumba.

Familia ya Lumumba ilimjua sana Mobutu, Lumumba alikutana na Mobutu wakati yeye (Mobutu) akisomea uandishi wa habari mjini Brussels, Ubelgiji, Mobutu na Lumumba walikuwa na matamanio yaliyokaribia kufanana, Walitamani kuona Congo iliyo na umoja, walichukia kutawaliwa na wageni, Kwa ushawishi wa Lumumba, Mobutu aliingia katika siasa za Congo kupitia MNC, Mobutu alifanya kazi kama katibu muhtasi wa Lumumba. Yeye ndiye aliyeamua nani aonane na Lumumba na kwa muda gani.

Mwandishi Mumbata anasema kwa ujumla Mobutu ndiye aliyekuwa anapanga ratiba yote ya shughuli za kisiasa za Lumumba, Nyumbani kwa Lumumba kulikuwa kama nyumbani kwa Mobutu kwa sababu aliweza kwenda huko wakati wowote kadri alivyotaka na alikuwa akijihudumia vyakula na vinywaji kadri alivyoweza.
Sehemu kubwa ya maisha yake ya kikazi siku za mwanzo za harakati za siasa za Congo kuelekea siku ya uhuru, Mobutu alikaa nyumbani kwa Lumumba.

Hii ilimfanya awe karibu zaidi na Lumumba kuliko mwanasiasa yeyote duniani, Katika ukurasa wa 2562 wa kamusi ‘The 20th Century Go-N: Dictionary of World Biography, Volume 8’ iliyohaririwa na Frank Magill, inasimuliwa kuwa Lumumba alimwamini sana Mobutu, Mwandishi Didier Mumbata anasimulia: “Lumumba aliwaamini watu kirahisi, na haraka. Alikuwa mwema, alikuwa akimwambia mkewe kuwa Mobutu alikuwa rafiki yake sana na nyumbani kwake (Lumumba) ni nyumbani kwa Mobutu.

Lumumba alijua fika kuwa Mobutu alihitaji sana fedha kuikimu familia yake, lakini alikuwa akimwambia asijaribu kuisaliti Congo na watu wake kwa sababu ya fedha. Lakini Mobutu, kama alivyokuwa Yuda kwa Yesu (Kristo), alikuja kumsaliti rafiki yake huyo kwa Wabelgiji na Wamarekani.”

Hata hivyo, lilipokuja suala la kupata msaada wa kijeshi kutoka Urusi ili isaidie kuyaondoa majeshi ya Ubelgiji nchini Congo, ndipo Rais Kasavubu na Mobutu walipoungana kumpinga Lumumba, Lumumba alipoona hapati msaada wa haraka kutoka majeshi ya kulinda amani ya Umoja wa Mataifa, Julai 17, 1960 alitishia kuyaita majeshi ya Urusi ili yasaidie kuyaondoa ya Umoja wa Mataifa kama watashindwa kuyaondoa majeshi ya Ubelgiji ndani ya saa 72, Baadaye siku hiyo, Lumumba alitoa tishio jingine. Akasema ikiwa majeshi ya Umoja wa Mataifa hayatayaondoa majeshi ya Ubelgiji kabla ya Julai 20, watalazimika kuyaita majeshi ya Urusi kuwaondoa wao.

Julai 22, malori 100 ya kijeshi kutoka Urusi yaliwasili Congo, lakini hayakukabidhiwa jeshi la Umoja wa Mataifa. Katika Mkutano wa Usalama wa Taifa (NSC) nchini Marekani, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kijasusi la Marekani (CIA), Allen Dulles, aliwaambia wenzake mkutanoni kuwa alihisi “Lumumba amenunuliwa na Wakomunisti”. Mkutano huo ulihudhuriwa pia na Rais Dwight Eisenhower.

Julai 27, akiwa Umoja wa Mataifa, kwa mara nyingine Lumumba aliomba msaada Umoja wa Mataifa, Marekani na Urusi, alipozuru Washington, Lumumba alikwenda kukutana na Waziri Mdogo wa Mambo ya Nje wa Marekani, Douglas Dillon, ambaye baadaye alidai kuwa Lumumba ni “mwendawazimu” na kwamba “ni mgumu kushughulika naye.”

Agosti 1, akizungumza mbele ya Umoja wa Mataifa, Lumumba alimshutumu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Dag Hammarskjold, kwa kuyakatalia majeshi ya Umoja wa Mataifa kuishambulia Katanga.
Agosti 7, Lumumba alikwenda kwa siri Ghana alikokutana na Rais Kwame Nkrumah kuzungumza suala la nchi hizo kuungana, Agosti 8 Jimbo la Kasai Kusini nalo likatangaza kujitenga na Congo, Juma moja baadaye, Lumumba aliomba msaada wa kijeshi kutoka Urusi kudhibiti majimbo ya Katanga na Kasai yaliyojitenga.

Kesho yake, Agosti 16, Urusi wakatangaza kuwa huenda Congo wakahitaji kupatiwa jeshi la nje kuleta hali ya amani. Lumumba akasisitiza kuwa majeshi ya Umoja wa Mataifa yaondoke Congo.
Agosti 18 Urusi wakatuma kwenda Congo ndege 10 za kivita zenye rangi ya jeshi la Congo.

Baada ya kurejea Congo akitokea Marekani, Lumumba aliwaambia Rais Kasavubu na Mkuu wa Majeshi yake, Joseph Mobutu, kwamba ameamua sasa kuyaita majeshi ya Urusi, Kasavubu na Mobutu walimkatalia. Lakini Lumumba alikuwa ameshafanya uamuzi. Aliita majeshi ya Urusi ambayo yangemsaidia kuzuia kujitenga kwa jimbo la Kasai Kusini. Alifanikiwa, lakini mara baada ya mapigano kumalizika yalifuatiwa na mauaji ya watu zaidi ya 1,000 na wengine wapatao 250,000 kuyakimbia makazi yao.

Mara moja wakala wa CIA nchini Congo, Larry (Lawrence) Devlin, akatuma ripoti Washington ikidai kuwa Lumumba anajiandaa kufanya mapinduzi ya Kikomunisti, Mradi wa kwanza wa CIA wa kumshughulikia Lumumba ulianza mapema Agosti 1960 na ulipewa jina la ‘Operation Wizard’. Sehemu moja ya utekelezaji wa mpango huo ni kuwahonga waandishi wa habari wa ndani na nje ya Congo ili waandike habari mbaya za Lumumba, kufadhili maandamano ya kumpinga, na kuhonga wanasiasa watofautiane naye. Mpango huo ulisimamiwa na mkuu wa CIA nchini Congo, Larry Devlin na watu wake.

Katika kitabu ‘Shadow Warfare: The History of Africa’s Undeclared Wars’ cha Larry Hancock, aliyekuwa akiandika muhtasari wa mkutano huo ni Robert Johnson. Dulles alikaririwa akisema, “Kwa Lumumba, tunakabiliana na mtu wa aina ya Castro au mbaya kuliko Castro.”
Siku chache baadaye, kwa mujibu wa kitabu ‘The Assassination of Lumumba’ cha Ludo de Witte, Agosti 26 “Allen Dulles, mkuu wa CIA, alituma telegramu kwenda ofisi za CIA za Leopoldville chini ya Larry Devlin: Telegramu hiyo ilisomeka “Kuondolewa kwa Lumumba madarakani lazima kuwe jambo la lazima na la haraka ... Lazima lipewe kipaumbele cha kwanza katika shughuli zetu.”

Baadaye siku hiyo hiyo Dulles alituma ujumbe mwingine kwenda Congo uliosomeka: “Sasa ni uhakika kwamba iwapo (Lumumba) ataendelea kushikilia wadhifa wake (Uwaziri Mkuu) Ukomunisti utatawala ... Kung’olewa kwake lazima kupewe kipaumbele.”

Shirika la Kijasusi la Marekani (CIA) lilituma ‘ujumbe wa sumu’ kwenda Congo kwa ajili ya kumuua Waziri Mkuu wa kwanza wa nchi hiyo, Patrice Emery Lumumba, Ujumbe huo kwenda kwa aliyekuwa mkuu wa CIA, Congo, Lawrence (Larry) Raymond Devlin, ulipelekwa na wakala wa CIA aliyeitwa Sidney Gottlieb, Kwa mujibu wa uchunguzi uliochapishwa na Madeleine G. Kalb katika kitabu ‘The Congo Cables: The Cold War in Africa-From Eisenhower to Kennedy’, ulimwambia Devlin hivi: “Atajitangaza kama Joe kutoka Paris... ni muhimu uonane naye haraka mara atakapokupigia simu.

Atajitambulisha kwako kikamilifu na kukueleza kazi aliyokuja kuifanya.”
Ndipo jioni ya Jumatatu ya Septemba 26, Gottlieb aliwasili Congo, Devlin, aliyekuwa anafanya kazi ya ujasusi kwa mwamvuli wa ofisa wa ubalozi wa Marekani Congo, aliondoka ofisini kwake kwenda kukutana na mgeni wake.
Walipokuwa kwenye gari la Devlin, Gottlieb alimweleza kuwa “nimekuja Congo kukupa maelekezo kuhusu operesheni moja muhimu.”
Kitabu ‘Poisoner in Chief: Sidney Gottlieb and the CIA Search for Mind Control’ cha Stephen Kinzer kinasema Gottlieb aliwahi kuifanyia majaribio sumu yake kwa wafungwa, watumiaji dawa za kulevya, wagonjwa mahospitalini, washukiwa wa upelelezi, raia wa kawaida na hata wafanyakazi wenzake, na kote huko, alisema, alifanikiwa.

Gottlieb alikuja kujulikana kuwa ni ofisa pekee wa CIA aliyebeba sumu kutoka Amerika kwenda kumuua kiongozi wa nchi nyingine katika bara la Afrika, Akiwa nyumbani kwa Devlin katika ubalozi wa Marekani mjini Leopoldville, ndipo Gottlieb alipomfahamisha Devlin kuwa alikuwa amebeba vifaa vyenye sumu ya kumuua Waziri Mkuu Lumumba.
“Mungu wangu,” alishangaa Devlin. “Nani aliyeidhinisha hii operesheni?” Alihoji.

“Ni Rais (Dwight) Eisenhower,” alijibu Gottlieb. “Nilikuwapo wakati akiidhinisha, lakini Dick Bisell alisema Eisenhower anataka Lumumba aondolewe madarakani.” Wakati huo Dwight David “Ike” Eisenhower ndiye alikuwa Rais wa Marekani na Bisell alikuwa ofisa wa CIA aliyeshughulikia miradi mikubwa.

Gottlieb na Devlin wote walijikuta wameacha kuongea kwa dakika kadhaa, Devlin akawasha kwanza sigara kabla hajaendelea kuongea, Baadaye kidogo Gottlieb akavunja ukimya uliotawala “Ni jukumu lako kufanya operesheni hii, ni yako peke yako,” Gottlieb alimwambia Devlin “Maelezo ni yako, lakini lazima (operesheni) iwe safi, ifanyike kwa namna ambayo hakuna kitu kinachoweza kuacha nyuma alama yoyote ya kuihusisha serikali ya Marekani.”

Kisha akamkabidhi kasha la sumu alilotoka nalo Marekani “Chukua hii,” alimwambia “Kwa kilichomo humu ndani kikitumika hakuna mtu atakayejua kamwe kuwa Lumumba aliuawa" Baada ya hapo Gottlieb akaanza kumpa Devlin maelezo na maelekezo ya namna ya kufanya, Ingeweza kuwekwa kwenye kitu chochote ambacho kingeugusa mdomo wa Lumumba iwe ni mswaki au chakula, na hapo kazi ingekuwa imemalizika.

Sumu hiyo haikutengenezwa kwa namna ya kuua haraka, lakini kifo kingekuja baada ya saa kadhaa. Alimwambia pia kwamba hata kama kungefanyika uchunguzi wa sababu za kifo, kile ambacho kingeonekana ni zile sababu za kawaida tu.

Hata hivyo ilishindikana, hawakuweza kumwekea sumu kwa kile ambacho John Jacob Nutter alikisema katika kitabu chake, ‘The CIA’s Black Ops: Covert Action, Foreign Policy, and Democracy’, kwamba “Hata kuweka sumu kwenye chakula chake ilikuwa shida sana kwa sababu CIA haikuwa na mawakala ambao wangeweza kuingia jikoni kwa Lumumba.” Kwa hiyo CIA haikufanikiwa kumuua Lumumba kwa sumu, Kwa zaidi ya miongo miwili akiwa CIA, Gottlieb alikuwa ameelekeza nguvu na akili zake zote katika utafiti wa namna ya kuanzisha mfumo wa kudhibiti akili za mwanadamu lakini alijulikana zaidi kama “mtengenezaji mkuu wa sumu katika CIA.”

Tafiti zake zilikuwa zikifanyika kwa siri kubwa kiasi kwamba alipokuja kuacha kazi mwaka 1972 aliteketeza asilimia 80 ya nyaraka zilizokuwa na ripoti mbaya. Alilazimika kuyateketeza kabla ya kuondoka kazini. Asilimia kubwa ya nyaraka hizo inahususu kazi za Gottlieb.
Anne Collins, katika ukurasa wa 30 wa kitabu chake, ‘In the Sleep Room: The Story of the CIA Brainwashing Experiments in Canada’, anaandika kuwa nyaraka hizo zilikuwa na taarifa mbaya kiasi kwamba maelfu ya kurasa za nyaraka “ziliharibiwa kwa amri ya watu wawili: Mkurugenzi wa CIA Richard Helms, aliyestaafu mwaka 1973 na Dk Sidney Gottlieb, ambaye alihusika zaidi na nyaraka hizo.”
Ilidaiwa kuwa nyaraka hizo zingewekwa wazi zingezua kashfa kubwa zaidi duniani na huenda ingeufungulia ulimwengu sababu za kuifungulia mashtaka CIA kwa ukatili dhidi ya wanadamu.

Kitabu ‘Top Secret Government Archives: Missing Files and Conspiracy Paper Trails’ cha mwandishi wa habari za utafiti, Nick Redfern, kinaandika: “Kama tulivyoona, wakati hofu ilipotanda ndani ya CIA kwamba itajulikana kwa watu wa nje [ya CIA] mradi wa CIA [dhidi ya utu], mkurugenzi wa shirika hilo, Richard Helms na Sidney Gottlieb waliandaa mpango wa kuziteketeza moja kwa moja nyaraka hizo.

Nyaraka hizo zilijulikana pia kama ‘Mpango wa CIA wa kudhibiti akili za wanadamu’, Sehemu ya mradi huo ulikuwa ni kufanya majaribio juu ya ubongo wa mwanadamu kwa kuendeleza dawa ambazo zingeweza kutumiwa kudhoofisha uwezo wa mtu wa kudhibiti akili yake ili atamke yale asiyokusudia kuyatamka.

Mradi huo na mingine mingi iliandaliwa chini ya Ofisi ya Ushauri wa Kisayansi ya CIA kwa kuratibiwa na Maabara ya Vita ya Kibaiolojia ya Jeshi la Marekani, Nick Redfern anaendelea: “Kumbuka kuteketezwa nyaraka hizo kulivyofanikiwa; ni kwa kuzimwaga kwenye tanuri, mwaka 1973, katika kituo cha kumbukumbu cha CIA, kilichokuwa Warrenton, Virginia. Kwanini hili jambo lilikuwa la muhimu? Kwa sababu kugundulika siri zilizokuwa kwenye nyaraka hizo kungeonyesha ukatili dhidi ya mwanadamu uliofanywa na shirika hilo”, Hata hivyo, wakati watu wengi waliokuja kujulishwa kuwa ndugu zao walilishwa sumu iliyotengenezwa na Sidney Gottlieb, walianza kufungua mashtaka mmoja baada ya mwingine alianza kuitwa katika mahakama mbalimbali za nchini Marekani.

Wakati baadhi ya kesi hizo ziliendelea na nyingine zikiwa kwenye upelelezi, Gottlieb alifariki dunia Jumatano ya Machi 10, 1999 Jijini Washington.

Turudi Kinshasa...

Agosti 21, 1960 Waziri Mkuu wa Congo, Patrice Lumumba aliomba waziwazi msaada wa kijeshi Urusi. Siku tano baadaye, Agosti 26, baada ya kukataliwa na majeshi ya Umoja wa Mataifa (UN) kuishughulikia Kasai Kusini iliyojitenga, Lumumba alituma majeshi ya Congo yanayomtii kwenda Kasai Kusini.

Wanajeshi hao walikuwa katika ndege 15 za kijeshi za Urusi na malori 100. Nia ya Lumumba ni kulirejesha jimbo lililojitenga. Kufikia hatua hiyo, Allen Dulles alimtumia Devlin ujumbe akimwelekeza amuue Lumumba.

Mwishoni mwa Agosti maofisa wa Urusi waliwasili Congo. Kwa kuona Lumumba alikuwa akiegemea sana ushauri na misaada kutoka Urusi, Rais Joseph Kasavubu alianza kuingiwa na wasiwasi.

Septemba 5, Rais Kasavubu akamfukuza kazi Lumumba kama Waziri Mkuu wa Congo. Wakati huo huo Lumumba naye akamfukuza kazi Rais wake, Kasavubu. Kwa hiyo walifukuzana kazi, Kasavubu alimteua Joseph Ileo kuwa waziri mkuu badala ya Lumumba.

Septemba 9, hata baada ya kudaiwa kufukuzwa kazi, Lumumba aliidhinisha malipo ya dola milioni moja kwa wanajeshi wa Leopoldville (sasa Kinshasa). Mgogoro wa uongozi ukaongezeka kati ya Lumumba na Kasavubu.

Baada ya vuta nikuvute kati ya Lumumba na Kasavubu, mgogoro ukafikia kilele chake Septemba 5, 1960. Mgogoro ulisababishwa na kutoelewana kati ya Lumumba na Kasavubu kuhusu namna ya kushughulikia Jimbo la Katanga lililojitenga na Congo.

Siku hiyo serikali ya Congo ikapasuka vipande viwili. Kasavubu akamfukuza Lumumba kazi ya uwaziri mkuu na kuliomba jeshi la UN lichukue madaraka ya utawala Congo. Baraza la Mawaziri la Lumumba nalo likamfukuza Kasavubu kama Rais wa nchi, likimtuhumu kwa uhaini.

Septemba 14, 1960, kikao cha pamoja cha Baraza la Congo kikapiga kura na kumkabidhi Lumumba madaraka ya kuongoza nchi hadi hapo mgogoro wa uongozi utakapomalizika na tume ya kibunge ndiyo ambayo ingemwongoza.

Hadi hapo kulikuwa na kambi mbili za serikali, moja ya Joseph Ileo (baadaye alibadili jina na kujiita Sombo Amba Ileo) ambaye aliteuliwa na Kasavubu kama Waziri Mkuu badala ya Lumumba. Kambi nyingine ni ya Lumumba ikiwa na baraka za tume ya Bunge.

Katika kuhakikisha viwanja vya ndege na redio havitumiwi vibaya, majeshi ya UN yalivitwaa lakini hata baada ya Baraza la Congo kupiga kura kumpa Lumumba mamlaka ya kuendelea kutawala, siku hiyo hiyo, Jumatano ya Septemba 14, Mobutu alitangaza anatwaa madaraka ya nchi hadi Desemba 31 ili kuwapa muda Lumumba na Kasavubu waafikiane. Kisha akateua serikali ya mpito.

“Kuanzia sasa,” alisema Mobutu, “Kasavubu na Lumumba hawako madarakani... ni mpaka mwishoni mwa Desemba watakapokubaliana namna ya kuongoza pamoja.

Baada ya Mobutu kuwatoa madarakani Kasavubu na Lumumba, Kasavubu alikimbilia Brazaville kujificha wakati Lumumba akibaki Leopoldville kwenye nyumba ya makazi ya waziri mkuu akilindwa na majeshi ya Mobutu asitoroke.

Mkono mrefu wa Shirika la Kijasusi la Marekani (CIA) ulionekana. Mwandishi James Hunter Meriwether katika ukurasa wa 218 wa kitabu chake, ‘Proudly We Can be Africans: Black Americans and Africa, 1935-1961’ anaandika: “Katika kipindi chote cha misukosuko, maofisa wa Serikali ya Marekani walikuwa katika jitihada kubwa ya kumhamisha Mobutu, msaidizi binafsi wa Lumumba kabla bosi wake hajamteua kumfanya mnadhimu wa jeshi, kumhamishia kwenda kambi ya Kasavubu. Saa chache baada ya Kasavubu kutangaza kuliahirisha Bunge, Mobutu alitwaa madaraka kwa jina la jeshi.

“Aliahidi ‘kubatilisha’ nyadhifa za Kasavubu, Lumumba, Ileo na wanasiasa wengine hadi mwisho wa mwaka (1960). Aliwaita wanafunzi wa Chuo Kikuu Congo na wahitimu wengine wa vyuo kuendesha serikali. Aliwafukuza mabalozi wa Urusi na Czechoslovakia. Siku chache baadaye wakati CIA ilipomtahadharisha Mobutu juu ya njama za kumuua, Mobutu alibadilika, akaanza kuegemea upande wa Kasavubu aliyefuata matakwa ya nchi za Magharibi.

“Aliwaambia maofisa ubalozi wa Marekani kuwa angemkamata Lumumba na kuweka madaraka mikononi mwa serikali ya Ileo-Kasavubu mwishoni mwa Oktoba. Hata hivyo Mobutu hangeweza kumkamata Lumumba kwa sababu Lumumba alikuwa nyumbani kwake akilindwa na UN. Kwa hiyo, majeshi ya Mobutu walimzuia Lumumba asiondoke kwenye nyumba hiyo.”

Septemba 19 ‘Tume ya Wanavyuo’, ikiwa na wahitimu zaidi ya 30, ikaundwa ili kuendesha serikali ya mpito. Kuanzia hapo kamatakamata ilianza. Kasavubu aliondoka kwenda New York, Marekani kuhudhuria mkutano wa Baraza la Usalama la UN. Huko alitoa hotuba yake Novemba 8 na alitambuliwa kama Rais wa Congo licha ya kwamba Mobutu alijitangaza yuko madarakani na serikali ya mpito.

Novemba 27, 1960, siku ambayo Kasavubu alirejea kutoka New York, alikopeleka malalamiko yake UN na kisha akapokewa kwa shangwe na wanasiasa kadhaa wa Congo, ndiyo siku ambayo Lumumba aliondoka Leopoldville kwenda Stanleyville (Kisangani) kuanzisha upya mapambano ya kisiasa.

Hadi Novemba 27 alikuwa chini ya ulinzi wa UN nyumbani kwake Leopoldville lakini aliruhusiwa kutoka na kurudi nyumbani.

Akiwa nyumbani kwake, Lumumba aliona shamrashamra za mapokezi ya Kasavubu zikiendelea. Waliokuwa wamezingira eneo zilipokuwa zikifanyika shangwe hizo ni askari wa Mobutu.

Lumumba aliona atumie fursa hiyo kutoroka na kwenda Stanleyville ambako Antoine Gizenga, aliyekuwa naibu wake, alikuwa akiwaandaa wapambanaji ili kujipanga upya. Alitoroka kwake bila askari wa Mobutu kugundua.

Baada ya kuona kuwa hangeweza tena kurudi madarakani kwa njia za kawaida, hasa baada ya kurejea kwa Kasavubu kutoka UN, Lumumba aliona njia pekee ya kutwaa madaraka ni kuitwaa Leopoldville akitokea Stanleyville.

Wanasiasa wengine saba waliokuwa tayari kujiunga na Lumumba na waliokuwa kwenye baraza lake la mawaziri ni Christophe Gbenye, Joseph Mbuyi, Maurice Mpolo, Anicet Kashamura, Pierre Mulele na aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu, Barthelemy Mujanay. Msafara wao ulikuwa wa magari matatu, mojawapo liliibeba familia yake.

Baada ya Kasavubu na Mobutu na Wamarekani na Wabelgiji kugundua Lumumba ametoroka na familia yake, walianza kumsaka.

Viongozi wa Leopoldville walinuia kumkamata kwa gharama zozote. Shirika la huduma za kijasusi la kikoloni nchini Congo la Surete, chini ya Victor Nendaka Bika, liliingia kazini kumsaka Lumumba. Mkuu wa CIA Congo, Larry Devlin, na mshauri wa Kasavubu wa masuala ya usalama, Andre Lahaye, walishirikiana kikamilifu na taasisi ya Nendaka.

Ubelgiji walitoa ndege ndogo za kuruka karibu na usawa wa ardhi. Mbelgiji mshauri wa Mobutu, kanali Louis Marliere, alisambaza askari wa kuweka vizuizi barabarani na kwenye mito iliyofikiriwa Lumumba angeweza kupitia.

Mvua iliyokuwa inanyesha na vizuizi vya barabarani vilipunguza kasi ya Lumumba kutoroka. Kilichomchelewesha zaidi ni kusimama karibu kila kijiji alipowaona watu na kuanza kuwahutubia.

Huku akiendelea kusalimiana na watu kila alikopita, inaelekea Novemba 30 waliokuwa wanamtafuta wakiwa angani waliuona msafara wake. Kesho asubuhi, Alhamisi, alipita njia-panda ya mji wa Port Francqui karibu na mpaka wa Leopoldville na Kasai.

Alhamisi ya Desemba mosi, 1960, Patrice Lumumba, alikamatwa na majeshi ya serikali ya Congo baada ya kutoroka. Alikamatiwa eneo la Mweka, Jimbo la Kasai alipokuwa akielekea Stanleyville (sasa Kisangani) baada ya kutoroka Leopoldville (sasa Kinshasa) alikokuwa chini ya ulinzi wa Umoja wa Mataifa (UN), lakini akilindwa na majeshi ya Mobutu.

Ingawa msafara wao ulikuwa na watu kadhaa waliokuwa wakitoroka naye, ni Christophe Gbenye, Anicet Kashamura (aliyekuwa Waziri wa Habari) na Pierre Mulele (Waziri wa Elimu) tu walifanikiwa kumaliza safari yao.

Lumumba, Maurice Mpolo (aliyekuwa Waziri wa Vijana na Michezo) na Joseph Akito (makamu rais wa Baraza la Seneti) walikamatwa na kurejeshwa Kinshasa, lakini Joseph Mbuyi na Barthelemy Mujanay (aliyekuwa Gavana wa Benki Kuuo) waliuawa katika Jimbo la Charlesville.

Siku iliyofuata, wanajeshi 40 walimtoa Lumumba kutoka eneo walilomkamata la Lodi-Mweka na kumsafirisha kwa njia ya barabara hadi uwanja mdogo wa ndege wa Port Francqui ambako alisafirishwa kwa ndege kurudishwa Kinshasa ambapo waliwasili saa 11:00 jioni. Muda wote wakiwa angani, Lumumba na wenzake walikuwa katika mateso makubwa hadi ndege ilipotua na wao kuteremshwa na kupakiwa kwenye lori.

Lumumba alitoroka Kinshasa kwa kutumia gari aina ya Peugeot 403, mali ya mtu aliyeitwa Kamitatu Cleophas na ilikuwa ikiendeshwa na Mungul Diaka.

Johannes Fabian, mwandishi wa kitabu cha “Remembering the Present: Painting and Popular History in Zaire (uk 115)”, anasimulia kuwa Lumumba alikuwa katika gari hiyo ya rangi nyeusi, ingawa mwandishi mwingine, Anna Purna, katika ukurasa wa 285 wa kitabu “Dr. Lumumba’s Dream of Incest”, anasema gari hilo ni Peugeot lakini la rangi nyeupe.

Sehemu ya simulizi ya tukio hilo inasema baada ya kuvuka Mto Sankuru, alirudi kumchukua mkewe Pauline Opango Lumumba, na mtoto wao wa mwisho, Roland, waliokuwa ng’ambo ya mto, na ndipo alipokamatwa.

Wenzake, akiwamo Pierre Mulele, waliovuka mto na Lumumba, walifanikiwa kufika salama Port Francqui Desemba mosi.

Ijumaa, Desemba 2, 1960, muda mfupi kabla ya saa 11:00 jioni, ndege ya Congo DC-3 ilitua uwanja wa ndege wa Ndjili mjini Kinshasa. Ndani yake alikuwamo ofisa usalama wa Congo, Gilbert-Pierre Pongo, Lumumba na wanajeshi.

Pongo ni mmoja wa maofisa usalama wa serikali ya Congo waliomfuatilia Lumumba hadi kumkamata.

Umati wa watu uwanjani hapo ulikuwa ukisubiri kuona wanaoshuka kwenye ndege hiyo. Miongoni mwa waliokuwa kwenye umati huo ni waandishi wa habari, wapigapicha, maofisa wa serikali na wa jeshi la ANC.

Lumumba alikuwa wa pili kushuka, akiwa nyuma ya Pongo ambaye sasa alionekana kama shujaa kwa kuwezesha kukamatwa kwa Lumumba. Mikono ya Lumumba ilifungwa nyuma kwa kamba. Picha zilizopigwa siku hiyo zinamuonyesha alikuwa amevaa shati jeupe.

Lumumba na mateka wengine wawili walisukumwa kuingia kwenye lori kusubiri safari nyingine. Mwandishi wa kitabu cha “The Assassination of Lumumba”, Ludo de Witte anaandika kuwa kwa faida ya wapigapicha, mwanajeshi mmoja alimkamata Lumumba na kunyanyua kichwa chake juu ili apigwe picha.

Kwa mujibu wa kitabu hicho, mwangalizi mmoja wa UN aliyekuwa uwanjani hapo, alisema Lumumba alipoteza miwani yake na shati lake lilitapakaa damu, na kulikuwa na damu iliyovia kwenye shavu lake la kushoto.

Mateka hao walipelekwa kambi ya jeshi ya Binza karibu na makazi ya Mobutu. Waandishi waliokuwa kambini hapo wakati Lumumba anawasili, walisema alikamatwa na kuonyeshwa kwa wapigapicha ili apigwe picha. Wakati huo Mobutu naye alikuwa akiangalia.

Baadaye alitupwa ardhini huku akipigwa na wanajeshi waliomzunguka. Kisha Pongo akapaza sauti kuwataka wanajeshi hao wazidi kumpiga.

Baada ya kumkamata Lumumba, Pongo alipandishwa cheo na kuwa kapteni. Alitumwa kwenda Bukavu, lakini huko alikamatwa.

Januari mosi, 1961, siku 16 kabla Lumumba hajauawa, Pongo alitumwa na Mobutu kuongoza shambulio kwenye mji wa mpakani wa Bukavu, ikiwa ni jaribio la kulirejesha eneo hilo kwenye himaya ya Mobutu. Hata hivyo, alikamatwa na kuwekwa mahabusu katika mji wa Kisangani na mahabusu wengine ambako maofisa walitoa sharti la kumuachia kama Lumumba naye angeachiwa. Lumumba hakuachiwa na hivyo Pongo naye hakuachiwa.

Februari 20, 1961, ikiwa ni siku tatu baada ya Lumumba kuuawa, Pongo na wenzake 14 waliuawa na wafuasi wa Lumumba.

Wakati wakiwa bado wanamshikilia na kumtesa Lumumba, mwanajeshi mmoja alisoma ujumbe ulioandikwa kwenye karatasi ukidaiwa kuwa uliandikwa na Lumumba mwenyewe akidai kuwa yeye ndiye kiongozi halali wa serikali ya Congo.

Baada ya kuusoma ujumbe huo, mwanajeshi mmoja aliichukua karatasi hiyo, akaikunjakunja na kuisukumiza mdomoni mwa Lumumba. Baada ya hapo Lumumba alipelekwa chumba kingine ambako mateso dhidi yake yaliendelea.

Siku hiyo usiku, mkuu wa Idara ya Usalama ya Congo, Victor Nendaka, alimpeleka Lumumba mahabusu. Kwa mujibu wa Alfred Cahen, mwanadiplomasia kijana aliyewasili Congo muda mfupi baada ya Lumumba kushushwa kwenye ndege na ambaye alikuwa rafiki wa karibu wa Nendaka, alisema baadaye Nendaka alimwambia kuwa alimfungia Lumumba kwenye gereji ya aliyekuwa mkuu wa ujasusi katika serikali ya kikoloni, Kanali Frederic Vandewall.

Aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Ubelgiji, Pierre Wigny, alikaririwa akisema Desemba 3 alipokea telegramu kutoka ubalozi wa Ubelgiji mjini Brazzaville.

“Alitendwa kikatili sana usiku wa tarehe 2 kuamkia 3 na makomando waliochoma hata ndevu zake,” unasema ujumbe huo.

Bomboko aliingilia kati kutuliza hasira, lakini hakufaulu. Kwa mujibu wa walioshuhudia, “waliomtesa Lumumba ni watu wakatili sana”.

Justin Marie Bomboko Lokumba ni mwanasiasa wa Congo ambaye hakuaminiwa na Lumumba. Akiwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Congo, alishiriki katika kukamatwa kwa Lumumba.

Ujumbe huo kwa njia ya telegramu ulitumwa na Robert Rithschild akiwa ubalozi wa Ubelgiji mjini Kinshasa. Katika ujumbe mwingine alioutuma Brussels siku hiyo, Rothschild alisema: “Hatua muhimu zinachukuliwa kuhakikisha kuwa Kasavubu anawadhibiti mahabusu.”

Vyombo vya habari vya kimataifa vilipiga picha wakati Lumumba akiadhibiwa na askari wa Congo katika uwanja wa ndege wa Ndjili na kisha kwenye kambi ya Binza.

Balozi wa Marekani nchini Congo, Clare Hayes Timberlake, alituma telegramu kwenda kwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Christian Archibald Herter, akimsihi ajitahidi kuzuia kusambaa picha za mateso ya Lumumba kwa sababu “zinaweza kutengeneza bomu la atomiki”.

Picha hizo zilianza kutia simanzi na hasira maeneo mengi ya dunia ambako zilionekana kwenye vyombo vya habari.

Wanasiasa kadhaa walianza kutilia shaka uwezo wa UN, wakihoji wanawezaje kuwalinda Wabelgiji walioko Congo lakini wanashindwa kumlinda Lumumba anayekubaliwa na Bunge na wabunge wa nchi yake.

Nchi kadhaa za Afrika zilitishia hata kuondoa wanajeshi wao katika jeshi la UN lililokuwa Congo, UNOC.

Hata hivyo UN haikushinikiza Lumumba aachiwe, pamoja na kukiri alikuwa na kinga ya Bunge.

Majeshi ya UN hayakufanya chochote zaidi ya kutazama hali ilivyokuwa inakwenda nchini Congo kuhusu Lumumba.

Pamoja na kwamba majeshi ya Umoja wa Mataifa yalikuwa Congo kulinda usalama, hayakuingilia kati kwa muda wote ambao Patrice Lumumba alikuwa akiteswa. Huenda hii ni kwa sababu Ubelgiji na Marekani hazikumtaka Lumumba. Akiwa mahabusu alifanikiwa kuandika barua mbili kwa msaada wa wanajeshi waliokuwa wakimtii. Endelea…

Jumamosi ya Desemba 3, Patrice Lumumba alihamishwa na wanajeshi na kupelekwa kambi ya Hardy iliyoko Thysville. Kwa mujibu wa waandishi wa habari waliokuwapo wakati wa kuhamishwa huko, Lumumba alionekana kuwa na maumivu makali kiasi kwamba alipata shida kupanda lori, na uso wake ulikuwa na alama za vipigo.

Kambi hiyo ilikuwa chini ya Kanali Louis Bobozo. Bobozo, ambaye ni mpwa wa Mobutu, baadaye akawa mkuu wa majeshi ya Congo kuanzia 1965 hadi 1972. Alikuwa ni sajenti tu wakati Congo ikipatia uhuru lakini alipandishwa vyeo haraka.

Katika kambi hiyo kulikuwa na mahabusu wengine wa kisiasa, mmoja wao ni Georges Grenfell ambaye alikuwa waziri katika serikali ya Lumumba.

Aliyekuwa mwakilishi wa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN) nchini Congo, Balozi Rajeshwar Dayal, aliandika kuhusu hali ya Lumumba. “Inasemekana ana maumivu makali yanayotokana na majeraha aliyopata alipowasili. Kichwa kimenyolewa nywele na bado mikono yake imefungwa kwa nyuma. Amefungiwa kwenye mahabusu ambayo haina hadhi ya utu na ni hatari sana kwa afya,” aliandika.

Telegramu ambayo Dayal alimtumia katibu mkuu wa UN, Dag Hammarskjold Desemba 5, iliripoti mazungumzo yaliyofanyika.

“Wanajeshi wa Morocco walioko UN Congo kambi ya Thysville wameripoti kuwapo majadiliano makali kati ya ANC (Jeshi la Congo) kuhusu wanavyomtendea Lumumba. Mabishano hayajatulia,” alisema.

Desemba 22, Dayal alituma ujumbe mwingine kwenda UN ukisema: “Uhalifu unaoendelezwa kwa Lumumba umeanza kuwakera (Kasavubu na Mobutu) kwa sababu umeanza kuwagawa wanajeshi.”

Januari 4, 1961, zikiwa ni siku 13 kabla ya kifo chake, Lumumba alifanikiwa kupenyeza barua mbili kutoka rumande. Ya kwanza ilikuwa ni ujumbe kwa viongozi wa UN, ambayo alieleza hali halisi ya mahabusu ya Camp Hardy.

“Niko hapa na wengine saba waliokuwa wabunge, miongoni mwao ni rais wa seneti, M. Okito (akimaanisha Joseph Okito) mfanyakazi wa serikali na dereva. Jumla yetu tuko 10. Tumewekwa hapa tangu Desemba 2, 1960. Chakula tunacholetewa mara mbili kwa siku ni kibaya sana,” aliandika Lumumba.

“Kwa siku nne sijala zaidi ya ndizi. Nimemweleza daktari wa Msalaba Mwekundu aliyeletwa kuniona; kanali wa Thysville alikuwapo. Nimetaka niletewe matunda ... Ingawa daktari aliruhusu, wanajeshi wa hapa wamekataa wakisema wana amri kutoka juu, kwa Kanali Mobutu.

“Madaktari wameelekeza tutembee [mazoezi] kila jioni nje ya mahabusu, lakini kanali na mkuu wa wilaya wamekataa. Nguo nilizovaa kwa siku 35 hazijaoshwa. Nimezuiwa kuvaa viatu. Kwa ufupi tunaishi katika hali isiyovumilika. Zaidi, sijapata taarifa zozote za mke wangu na familia yangu na sijui waliko. Nilipaswa nitembelewe naye, kama ilivyo katika sheria za Congo.”

Katika barua ya pili aliyomtumia mpwa wake aliyeitwa Albert Onawelo, Lumumba alitoa maelezo ya ziada kuhusu hali yake, pia akaelezea msaada fulani alioupata kutoka kwa baadhi ya wanajeshi.

“Niko hapa na wasaidizi saba, mmoja wao ni Joseph Okito. Tumefungiwa mahabusu gizani mfululizo tangu Desemba 2, 1960. Chakula tunachopewa (chikwangue na wali) unakera na ni kichafu na naweza kukaa siku tatu hadi nne bila kula. Kwa kweli hali ni mbaya kuliko hata wakati wa ukoloni. Kama akitokea askari akatupa ndizi za ziada, anakamatwa na kuadhibiwa. Pamoja na tabu zote kuna baadhi ya wanajeshi wanakuja kwa siri kunisaidia,” aliandika.

Mwisho wa barua hiyo, Lumumba alionyesha pia kuhusu mke wake wa tatu, Pauline Kie “anaendelea vizuri na hufika kila mara na kuwaachia ujumbe (wa Lumumba) wanajeshi walio upande wetu”.

Mwanzoni mwa Januari 1961, katibu mkuu wa UN, Dag Hammarskjold alizuru Congo na kujikuta akipokewa kwa maandamano ya wafuasi wa Lumumba.

Wakati mwanaharakati Cleophas Kamitatu alipojaribu kumpa Hammarskjold barua kutoka kwa Lumumba iliyoelezea hali katika mahabusu walimoshikiliwa, alionyesha kukasirika na kumwelekeza ampatie msaidizi wake.

Kamitatu, kwa kukasirishwa na majibu aliyopewa na Hammarskjold, naye aliandika barua yake yenye maneno yanayofanana na yale ya Lumumba.

“M. Lumumba amekuwa akiteswa kikatili kwa siku 35. Kwa siku zote hizo ameruhusiwa kuoga mara tatu tu. Anapewa chakula kinachostahili kupewa mbwa... Nguo alizovaa zimekaa mwilini kwa siku 35. Anaishi shimoni. Hakuwahi kufikishwa mahakamani, na hata mkewe amezuiwa kumwona,” aliandika.

Ingawa barua hizo ziliwafikia maofisa wa UN nchini Congo, hawakuchukua hatua yoyote kurekebisha hali ya mambo.

Hali ya wasiwasi ilikuwa ikizidi kutanda katika kambi aliyowekwa Lumumba na wenzake. Msaidizi wa Kanali Bobozo, Luteni Jacques Schoonbroot, alikuwa anasisitiza kuwa ghasia zinazozuka zinasababishwa na itikadi za kisiasa na kwamba kulikuwa na kikundi cha wanajeshi wa Congo katika kambi hiyo kilichomtii Lumumba.

Jumanne, Desemba 27 Kanali Bobozo aliarifiwa na msiri wake kuwa huenda Lumumba angetoroka au kutoroshwa. Aliamua mwenyewe kwenda kumfungia Lumumba na kuondoka na funguo.

Siku hiyo usiku alikwenda tena mwenyewe mahabusu alimofungiwa Lumumba kuwazuia makumi ya wanajeshi waliokuwa wamepanga kumtoa.

Kwa mujibu wa Luteni Schoonbroot kama alivyokaririwa na kitabu cha “Assassination of Lumumba”, Kanali Bobozo aliwaambia wanajeshi hao akisema “nyiye hamna la kufanya. Kama mnataka kumuachia mfungwa yeyote, labda muanze kwanza kuniua mimi.” Baada ya kauli hiyo, wanajeshi hao walianza kuondoka mmoja baada ya mwingine.

Siku iliyofuata walikamatwa baadhi ya wanajeshi kutokana na jaribio lao la kumtoa Lumumba mahabusu. Baadaye ukazuka uvumi kwamba Lumumba alikuwa anatendwa vizuri mahabusu na alikula sikukuu ya Krismasi na maofisa wa kambi hiyo.

Luis Lopez Alvarez, raia wa Hispania aliyekuwa rafiki wa karibu na Lumumba, alikaririwa na Stephen Weissman katika kitabu cha “American Foreign Policy in the Congo 1960-1964”, akisema Lumumba alimlaumu sana balozi wa Marekani Congo kwa kuonekana kukaa upande wa watesi wake.

Wakati hayo yakiendelea, serikali ya Ubelgiji ilikuwa na hofu sana na Lumumba kiasi kwamba ilituma ujumbe wa telegramu kwenda Kinshasa ikiwasisitiza “watilie maanani hatari ambayo ingesababishwa na Lumumba ikiwa ataachiwa huru”. Siku iliyofuata ukatumwa ujumbe kwa njia ya telegramu kutoka Congo kwenda Ubelgiji ukisema serikali ya Mobutu isingeruhusu Lumumba kuachiwa huru.

Muda mfupi baadaye, maofisa wa Congo mjini Kinshasa walianza kutafuta namna ya kumpoteza kabisa Lumumba.

Jumapili ya Januari 8, 1961, wanasiasa wawili wa Congo; Albert Delvaux na Cyrille Adoula walikwenda Katanga kuzungumza na rais wa eneo hilo, Moise Tshombe, kuhusu kumhamishia Lumumba huko.

Siku iliyofuata, wanasiasa wa Congo walishauriana na Rais Joseph Kasavubu na mkuu wa majeshi, kumhamisha Lumumba. Kamishna wa Ulinzi wa Congo, Fredinand Kazadi alisema kuhamishwa kwa Lumumba ni kwa muhimu sana ili kuepusha machafuko yaliyokuwa yananukia Thysville.

Siku iliyofuata, kamishna wa mambo ya ndani, Damien Kandolo, aliondoka kwenda Boma kwa ajili ya maandalizi hayo. Ubelgiji ilikuwa ikifuatilia kwa karibu hatua zote hizi.

Kulingana na simulizi za G. Heinz na H. Donnay katika kitabu cha “Lumumba: The Last Fifty Days”, aliyekuwa kiungo kati ya watesi wa Lumumba na serikali ya Ubelgiji ni Andre Lahaye, Mbelgiji aliyekuwa mshauri mkubwa wa mkuu wa Idara ya Usalama ya Congo, Victor Nendaka.

Aliyesaini barua ya kumtaka Nendaka amtoe Lumumba Thysville na kumpeleka Katanga ni Rais Kasavubu. Mpango wa usafiri wa ndege uliandaliwa na Kandolo Damien.

Kuanzia hapo Lahaye alifanya kazi kubwa akituma taarifa za mara kwa mara na hatua kwa hatua kwenda Brussels kwa lengo la kuelezea namna Lumumba alivyokuwa anashughulikiwa.

Wakati Lumumba akiwa bado mikononi mwa watesi wake, Rais Kasavubu wa Congo alikuwa kwenye shinikizo kali kuhusu hatima ya Lumumba.

Kwa kuona hivyo, Januari 2, 1961, Kasavubu aliitisha mkutano ambao ungewajumuisha wanasiasa mbalimbali wa Congo. Pia wanasiasa wa Afrika na Asia waliokuwa wafuasi na watetezi wa Lumumba, walikuwa wanakutana Casablanca wakitaka aachiwe mara moja.

Kuongezea uzito wa hilo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Dag Hammarskjold alipanga kurudi tena Congo Januari 10. Viongozi wa kisiasa wa Congo waliogopa kwamba kama wangemwachia huru Lumumba, huenda UN wangeshinikiza arudi madarakani.

Mapema asubuhi ya Januari 13, nidhamu katika kambi ya Camp Hardy ilianza kutoweka. Wanajeshi wa kambi hiyo walikataa kupokea amri yoyote kutoka kwa wakubwa zao hadi walipwe stahiki zao, baadhi yao wakitaka Lumumba aachiwe huru.

Baadaye siku hiyo hali ilivyozidi kuwa mbaya Kasavubu, Mobutu, Bomboko na Nendaka waliitana na haraka kuelekea kambini kujadiliana na wanajeshi hao.

Baadaye ukazuka uvumi kwamba Januari 14, Lumumba angekuwa huru na hivyo wanajeshi wanaomtii waliokuwa Katanga wangekuwa njiani kuelekea Kinshasa.

Wanajeshi waliokuwa Katanga tayari walishateka eneo lote la kaskazini hata kabla machafuko ya Thysville. Viongozi walishahamishia familia zao Brussels, Ubelgiji.

Januari 13, mkuu wa Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA) nchini Congo, Lawrence Raymond Devlin, alituma ujumbe Marekani akisema serikali ya Congo inaweza kuanguka wakati wowote na kama Marekani hawatachukua hatua za haraka, maslahi yake nchini humo yatakuwa hatarini. Nchini Ubelgiji, mikutano ya haraka ilifanyika kuhusu hali ya kisiasa ya nchi hiyo.

Mwandishi wa habari, Kwame Afadzi Insaidoo katika ukurasa wa sita wa kitabu chake cha “Ghana: A Time to Heal & Renew the Nation” amelikariri jarida la The Economist la Februari 24-Machi 2, 2007, Vol. 382, No. 8517, ukurasa wa 95, kuhusu maendeleo ya hali nchini Congo.

“Bw. (Larry) Devlin alikula njama na mkuu wa jeshi la nchi, Joseph Mobutu, ambaye ni sajini aliyepandishwa cheo hivi karibuni, kumkamata Waziri Mkuu (Lumumba),” ameandika akinukuu jarida hilo.

Wakati Lumumba alipozidi kusababisha matatizo na nchi ikatumbukia kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe, Rais Dwight Eisenhower (wa Marekani) alitoa amri ya kumuua Lumumba, kwa mujibu wa Bw. Devlin.

Kwa mujibu wa kitabu “Betrayal of Trust: The Collapse of Global Public Health” cha Laurie Garrett, uamuzi wa Marekani kumuua Lumumba ulikuja baada ya mawasiliano ya mara kwa mara kati ya mkurugenzi mkuu wa CIA, Allen Dulles na mkuu wake katika kituo cha Congo, Larry Devlin.

Katika taarifa moja ya telegramu iliyotumwa Marekani, Devlin aliripoti kuwa “kuna jitihada za kuifanya Congo kuwa ya kikomunisti”.

Katika mkutano wa Baraza la Usalama wa Taifa la Marekani, ilitengenezwa mipango ya kuivuruga Congo kwa kutengeneza ghasia za mara kwa mara kiasi cha Lumumba kushindwa kutawala.

Kubwa zaidi lililofanyika ni kupandikiza mgogoro wa uongozi ambao hatimaye ulimfanya Lumumba kupoteza cheo chake.

Ghasia zilikuwa za mara kwa mara katika miji mingi ya Congo. Ghasia za Camp Hardy ziliwasukuma maofisa wa Congo kumhamishia Lumumba sehemu nyingine. Baadhi ya wanasiasa wa Katanga, Kasai na Kinshasa walihakikisha wanazuia njia zozote za kumwachia Lumumba.

Mipango ya kumtoa Lumumba mjini Kinshasa kwenda Katanga ilikamilika. Jimbo la Katanga lilikuwa linaongozwa na mmoja wa mahasimu wake kisiasa, Moise Tshombe.

Walioongoza kikao cha mipango ya kumhamisha ni Kandolo Damien na Andre Lahaye, Mbelgiji aliyekuwa mshauri mkubwa wa mkuu wa Idara ya Usalama Congo, Victor Nendaka.

Nendaka alikuwa ofisini kwake mjini Kinshasa wakati Kandolo alipomwendea akiwa na waraka ulioonyesha ratiba ya ndege itakayotumika. Andre Lahaye naye alikwenda ofisini kwa Nendaka alikokutana tena na Kandolo.

Kabla ya hapo, Jumanne ya Desemba 6, 1960, Kanali Joseph Mobutu aliitisha mkutano na waandishi wa habari na kuwaambia kuwa Lumumba yuko katika mikono salama.

Aliwaonyesha waandishi hao kile alichosema kuwa ni cheti cha daktari kinachoonyesha kuwa Lumumba yuko katika hali njema sana kiafya.

Aliwaambia Lumumba atashtakiwa kwa kosa la kusababisha ghasia katika jeshi na kuwatesa baadhi ya wabunge. Mobutu hakutaja tarehe ambayo Lumumba angeshtakiwa.

Januari 16, mkuu wa kikosi cha usalama, Victor Nendaka Bika, alikutana na wanasiasa wa Congo katika ofisi za Shirika la Ndege la Ubelgiji, Sabena, na kupanga kuwa watamhamisha Lumumba kutoka Bakwanga na kumpeleka Elizabethville.

Operesheni hiyo ingefanyika jioni. Hiyo ilikuwa ni siku moja kabla ya mauaji ya Lumumba. Wanasiasa wawili Fernand Kazadi na Jonas Mukamba walitakiwa washiriki kumsafirisha Lumumba.

Kushikiliwa kwa Lumumba kulianza kuitisha Ubelgiji tangu siku ile majeshi ya Mobutu yalipozingira makazi yake. Uvumi ulisambaa kwamba jimbo la Katanga lilitaka kubadilishana wafungwa na Kinshasa na kwamba Lumumba angekuwemo.

Uliposambaa sana uvumi huo, Waziri wa Mambo ya Afrika nchini Ubelgiji, Harold d’Aspremont Lynden aliwasiliana na maofisa wa serikali yake waliokuwa Congo akiwataka wazuie mazungumzo hayo.

Jumapili ya Januari 14, msiri na mtu wa karibu na Lynden aliyejulikana kwa jina la Meja Jules Loos, na ambaye ni mmoja wa walioshiriki njama za kumuua Lumumba, kwa mujibu wa kitabu “Patrice Lumumba, Ahead of His Time” cha Didier Ndongala Mumbata, alimpelekea Lynden mbinu nyingine za “kumalizana na Lumumba”.

Hiyo ni baada ya kukerwa na magazeti ya Congo kuhusu maasi ya kijeshi ya Thysville ambako Lumumba alikuwa anashikiliwa.

Loos alimshauri Luteni Kanali Louis Marliere, ofisa wa kijeshi wa Ubelgiji nchini Congo kumpeleka Lumumba Katanga kwa hasimu wake, Moise Tshombe.

Lynden alituma ujumbe wa siri kwa Luteni Kanali Marliere na Meja Loos akiwataka wahakikishe Lumumba anaondolewa na wampeleke sehemu nyingine ya siri, lakini yenye ulinzi mkali zaidi.

Januari 16 alimtumia Tshombe ujumbe akimsihi amchukue Lumumba na amshikilie huko Katanga. Hata hivyo ujumbe huo ulifika jioni wakati Tshombe alishafanya uamuzi wake.

Mipango ya kumpeleka Lumumba Katanga iliandaliwa Kinshasa. Tshombe alikubaliana nayo. Mmoja wa maofisa wa serikali aliyeidhinisha kuhamishwa kwa Lumumba na kupelekwa Katanga ni Albert Delvaux, ambaye awali alikuwa waziri wa Lumumba kabla ya mgogoro wa uongozi na alikuwa pia ni mmoja wa maofisa wa Kasavubu waliosaini kuondolewa kwa Lumumba na Justin Marie Bomboko mwaka 1960.

Baadaye Delvaux alikuwa waziri katika baraza la mawaziri la Joseph Ileo ambaye alikuja kuwa Waziri Mkuu wa Congo.

Katika kipindi chote cha mwanzoni mwa Januari 1961, Delvaux alikuwa na harakati nyingi za kuwaweka pamoja akina Kasavubu, Tshombe na Mobutu kuhusu suala zima la Lumumba.

Asubuhi ya Januari 16, wakati mshauri wa Kasavubu wa masuala ya usalama, Andre Lahaye na mkuu wa shirika la huduma za kijasusi la kikoloni, Victor Nendaka, wakijadiliana namna ya kumsafirisha Lumumba kumpeleka Katanga, aliyekuwa akisimamia mawasiliano baina ya Tshombe na Kasavubu ni Delvaux.

Hatimaye jioni ya Jumatatu ya Januari 16, muda mfupi baada ya tafakuri na majadiliano mengi, Nendaka alipanda ndege kuelekea mjini Thysville (sasa ni Mbanza-Ngungu) alikokuwa anashikiliwa Lumumba. Usiku wa siku hiyo alilala katika hoteli mojawapo ya mji huo.

Januari 17, 1961, Lumumba na mahabusu wenzake wawili, yani Waziri wa Vijana, Mourice Mpolo na Makamu wa Rais wa Seneti, Joseph Okito, ambao walikamatwa pamoja wakiwa njiani kutorokea Stanleyville, awalichukuliwa kutoka Kambi ya kijeshi ya Thysville iliyopo Jimboni Kasai na Mkuu wa Usalama wa Mobutu, Victor Nendaka, akifuatana na askari watatu wa kabila la Baluba na kupelekwa uwanja wa ndege wa Moanda, Lumumba alipo wasili uwanjani, walikaribishwa kwa vipigo vizito kutoka kwa askari wa Kibelgiji na Katanga, kisha kutupwa nyuma ya gari kupelekwa kwenye nyumba pweke, maili mbili kutoka hapo, nyumba iliyolindwa na majeshi ya Kibelgiji na Polisi chini ya Afisa wa Kibelgiji.

Hapo tena, Tshombe na mawaziri wake walishiriki kumpiga na kumtesa kinyama bafuni, kisha watesi hao wakatoka wametapakaa damu mwilini, Huku wakiwa wamelewa chakali, walitangaza Lumumba “auwawe mara moja”.

Ilipo fika usiku wa saa 4:00, tarehe hiyo hiyo 17/1/1961 Lumumba na wenzake wawili walichukuliwa kwa gari hadi kwenye vichaka, maili 30 toka Thysville, Tshombe akiongoza msafara, akiwamo pia Kamishna wa Polisi wa Kibelgiji, Frans Verscheure na walengaji shabaha kutoka Marekani.

Walipofikishwa eneo lililokusudiwa wakapekuliwa, wakiwa wamevaa kaptura na fulana tu, walianza kuuwawa, Huku Lumumba alikuwa wa mwisho kuuawa kwa kupigwa risasi na kikosi cha Askari wenye shabaha na kisha kuzikwa huko huko porini, Kesho yake ya tarahe 18/1/1961 serikali ya Moise Tchombe ikatangaza habari za uongo kwamba Lumumba na wenzake waliuawa na wanavijiji wenye hasira walipokuwa wakijaribu kutoroka kizuizini.

kwa kuhofia kuvuja kwa taarifa za unyama walio fanya, Usiku uliofuata, askali hao wa Uberigiji walikwenda kufukua miili ya Lumumba na wenzake, baada ya kufukuliwa ilisafirishwa hadi Kasenga, maili 120 Kaskazini Mashariki mwa Elizabethville, ambako ilikatwakatwa vipande vipande na kutupwa kwenye pipa la tindikali (Sulphuri acid), na kuyeyuka, mafuvu yao yakasagwa unga, mifupa na meno yakatupwa kwa kutawanywa porini wakati wauaji walipokuwa wakirejea Elizabethville, Asubuhi ya tarehe 20/1/1961, jasusi Larry Devlin aliitaarifu Washington DC kwa code kuwa "Mission 009321 operation Barracuda is over".

Kule Washington mtu wa kwanza kupata taarifa juu ya kukamilika kwa operation barracuda alikuwa Waziri wa kigeni Jonh Dulles, haraka akamtaalifu mkurugenzi wa CIA, Allan Dulles, na baadae taarifa zikamfikia rais Dwight Eisenhower, Wakati huo Dwight Eisenhower ndio alikuwa anakwenda kumaliza muhura wake wa mwisho madarakani.

Hata rais aliye mfuata wa 35 Jonh F Kennedy aliendeleza kulinda masrahi ya Marekani nchini Kongo kupitia Shirika lake la Ujasusi la CIA, liliendelea kuhakikisha na kudhibiti nyendo za watawala wa Kongo ili wasije kuegemea upande wa Ukomunisti, Kwa kuthibitisha hili mwandishi Martin Meredith Kwenye kitabu chake cha "The State Of Africa, ameandika, kuwa "Mobutu kwenye safari yake ya kwanza Washington, Mei, 1963, akiwa Mkuu wa Majeshi kwenye Serikali ya Joseph Kasavubu, Rais wa Marekani, John Kennedy alimtamkia Mobutu, "Jenerali, isingelikuwa wewe, Ukomunisti ungetamalaki Kongo", huku Mobutu akimjibu, "Ninafanya niwezalo mheshimiwa raisi".

Martin Meredith kwenye kitabu chake cha "The State Of Africa" ameandika "After operation barracuda completed and his coup in 1965, Mobutu remained on the CIA's payroll for sometime and received regular briefings from Larry Devlin , the CIA station chief in Leopoldville." ( Meredith, State Of Africa, pg 294).

Baada ya "operation Barracuda" kukamilika na Lumumba kuuwawa, hatimae tarehe 21 January 1961, Kasavubu alimteua Mobutu kuwa mkuu wa majeshi ya Kongo, na miezi kadhaa iliyofuata Cyrille Adoula akachaguliwa kuwa Waziri mkuu, Kwa kipindi hiko chote.

Kulikua na mapambano yaliyokuwa yakiendelea kati ya majeshi ya Mobutu wakishirikiana na vikosi vya UN dhidi ya wapiganaji wa Serikali ya Antone Gizenga na yale ya katanga iliyoongozwa na Moise Tshombe, majeshi ya Moise Tshombe yalishindwa nguvu na Tchombe mwenyewe kukimbilia Northern Rhodesia (Zambia kwa sasa) na baadae Uhispania, Lakini mwaka 1964, Tshombe aliitwa kurudi nchini, ambapo Kasavubu alimteua kuwa waziri Mkuu.

Katika kipindi chake cha uwaziri mkuu Tchombe, alikabiliwa na machafuko kutoka kwa waasi, wakiongozwa na bwana Pierre Mulele na Gizenga, Huyu Pierre Mulele alikuwa mfuasi wa Patrice Lumumba, na aliongoza mapambano dhidi ya serikali kwa lengo la kutaka kumuondosha madarakani Rais Kasavubu, Mapigano yaliendelea kwa muda mrefu sana kati ya wapiganaji wa Mulele na majeshi ya serikali yakishirikiana na majeshi ya UN, Mwisho wa siku Mulele alizidiwa nguvu na kukimbilia nchini Congo-brazzaville.

Ndimi: Comred Mbwana Allyamtu
Copyrights of this article reserved
written by Comred Mbwana Allyamtu

•Napatika Kwa mawasliano
Comred Mbwana Allyamtu
+255679555526 (WhatsApp).
+255765026057.
Email- mbwanaallyamtu990@gmail.com

Copyright 2022, All Rights Reserved.
View attachment 2280287View attachment 2280289View attachment 2280290View attachment 2280288View attachment 2280292View attachment 2280291View attachment 2280293View attachment 2280294
FB_IMG_1656595699810.jpg
FB_IMG_1656869203297.jpg
FB_IMG_1656868960557.jpg
FB_IMG_1656868952789.jpg
FB_IMG_1656595585532.jpg
FB_IMG_1656595605329.jpg
FB_IMG_1656595564452.jpg
FB_IMG_1656595484652.jpg
FB_IMG_1656595496005.jpg
FB_IMG_1655799687053.jpg
FB_IMG_1654349738051.jpg
FB_IMG_1654356730904.jpg
FB_IMG_1654349726559.jpg
FB_IMG_1654349709181.jpg
FB_IMG_1654349692086.jpg
FB_IMG_1654349606596.jpg
FB_IMG_1654349553935.jpg
FB_IMG_1654340362853.jpg
FB_IMG_1654340358769.jpg
 
Kabla sijamaliza kusoma uzi huu, nakushauri umtafute mtaalamu wa lugha ya Kiswahili awe anahariri kazi zako kabla hauja-post.

Uandishi wako haujanyooka sana mkuu, na kwa kuwa kazi zako zinafika mbali ni vyema ziwe zimeandikwa kwa lugha(Kiswahili) fasaha.

Kwenye suala la matini sina shaka nalo sana.
 
Kabla sijamaliza kusoma uzi huu, nakushauri umtafute mtaalamu wa lugha ya Kiswahili awe anahariri kazi zako kabla hauja-post.

Uandishi wako haujanyooka sana mkuu, na kwa kuwa kazi zako zinafika mbali ni vyema ziwe zimeandikwa kwa lugha(Kiswahili) fasaha.

Kwenye suala la matini sina shaka nalo sana.
Sijakuelewa unaposema haijanyooka
 
Asante sana mwandishi kwa historia hii, nilikuwa nasikia kwa rasha rasha tu, kuhusu kifo cha lumumba leo. Nimepata kufahamu kamili, kama unahistoria nyingine kuhusu. Congo naomba upatie??
 
Kaz nzuri mleta mada

Naomba kuuliza baada ya mobutu kuwatimua kasavubu na lumumba alikasimu madaraka na baadae kasavubu akarud Kama rais na mobutu akawa mkuu wa majeshi

Je mobutu aliupataje urais wa nchi? Kwa kula (demokrasia) au alimpindua kasavubu?
 
Huo ni mtindo wa uandishi wa frash back.....

Nilijua anatoa jambo la msingi kumbe ni hilo
Nilichomaanisha sio mtiririko wa matukio isipokuwa huwa una makosa mengi sana ya uandishi wa maneno ya lugha ya Kiswahili. Matumizi ya R na L bado ni tatizo sana kwako.

Mafano, japo ni Kiingereza, umeandika frash back badala ya flash back.
Au neno DHARIRI hapo kwenye kichwa habari huenda ulimaanisha DHALILI.

Kwa hili naomba ulifanyie kazi. Usishupaze shingo yako

Kuhusu mitindo ya uandishi sina tatizo nayo maana naijua kiasi. Kuna mbele-nyuma, nyuma-mbele, kuna kioo pia a.k.a sengerenyuma.
 
DHARIRI YA MOBUTU ILIVYO LETA FAHARI YA LUMUMBA BAADA YA MIAKA 61 KUPITA.

Na. Comred Mbwana Allyamtu (CMCA)
Sunday -3/07/2022
Marangu Kilimanjaro Tanzania.

Mwaka huu Patrice Émery Lumumba, shujaa wa uhuru na waziri mkuu wa kwanza wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, anatimiza miaka 97 toka kuzaliwa kwake, Lumumba alizaliwa tarehe 2 Julai mwaka 1925 katika mji ambao sasa unaitwa Lumumbaville.

Mbali na hilo wiki iliyopita ya tarehe 30 mwezi huu wa 6 mabaki ya Lumumba (jino lake) yalizikwa kwenye viwanja vya uhuru eneo la mtaa wa Limeté, katikati ya Jiji la Kinshasa, eneo hilo kuna mnala unaoitwa Tour de l’échangeur au Mnara wa Limete.

Ngoja nieleza kidogo hapa...

Huu mnala wa Tour de l’échangeur upo katika ya jiji la Kinshasa, mara nyingi mnara huu pia huitwa Mnara wa Eiffel wa Kongo, ujenzi wa mnara huo ulianza chini ya utawala wa Mobutu mwaka 1970 na ulikamilishwa na Joseph Kabila mwaka 2011, utaona ujenzi wake kuwa ulichukuwa mda refu kutoka kipindi cha Mobutu ujenzi ulisitiswa na kipindi cha utawala wa rais Joseph Kabila alianza tena ujenzi wake na kuukamilisha mwaka 2011.

Mnara huo umeundwa na nguzo nne ambazo zina urefu wa mita 210 kwenda Juu, mnara umewekwa nyuma ya sanamu la Patrice Lumumba na kushoto kuna jumba la makumbusho ya kumbukumbu ya Lumumba ambalo hufunguliwa kila siku asubuhi.

Mbele ya mnara huu ndio lilipo jengwa kaburi la Lumumba (ambapo jino lake limezikwa), juu ya kaburi hilo kuna sanamu kubwa la Patrice Lumumba.

Unaweza kuuliza kwanini serikali ya Kongo imeamua kuzika jino la Lumumba kwa sherehe kubwa kiasi hicho? Jibu la hilo na mengine ntaeleza huko mbeleni.

Ila kwasasa ntaeleza dhariri ya Mobutu ilivyo leta fahari ya Lumumba baada ya miaka 61 kupita.

Lumumba aliuwawa miezi michache tu baada ya kuingia madarakani, kifo cha Lumumba kiliinjiniwa na Ubelgiji na shirika la kijasusi la CIA la Marekani chini ya maelekezo ya Rais wa Marekani Eisenhower ambae ndie aliye idhinisha kuuawa kwa Lumumba, kuhusu hilo nimelieleza kwa upana kwenye makala yangu ya Operation Barracuda unaweza kuisoma kupita link hii Operation Barracuda: "Mission hatari ya kijasusi nchini Kongo"

Pamoja na hayo kifo cha Lumumba ndani ya nchi ya Kongo kiliratibiwa na kusimamiwa na Mobutu Seseseko Kuku Ngwendu Wazabanga Wazaire Ngwadu (Joseph Desiree Mobutu).

Huyu Mobutu aliyebariki mauaji ya kinyama ya Lumumba mpaka leo mwili wake aujazikwa Kongo, Serikali ya Kongo na wananchi waligoma mwili wake kurudishwa nchini Kongo japo kumekuwepo kwa maombi ya familia yake na watu wa kijijini kwao Gebdolite kutaka mabaki ya mwili wa Mobutu urejeshwe Kongo.

Mwili wa Mobutu umezikwa kwenye makaburi ya watu wa kawaida wasio wenyeji nchini Morocco, ikumbukwe kuwa Mobutu umauti ulimkuta nchini Morocco na kuzikwa huko baada ya serikali ya Kabila mzee kugomea mwili wake usirejeshwa Kongo kwa mazishi.

Mobutu umauti ulimkuta nchini Morocco ambako alikimbilia huko akitokea nchini Togo, baada ya kupinduliwa, umauti ulimfika mnamo tarehe 7 September 1997 baada ya kusumbuliwa kwa muda mrefu na ugonjwa wa Tezi dume.

Mazishi ya Mobutu hayakufanyika kitaifa, alizikwa na watu tisa kutia ndani familia yake na watu wa jiji la Rabat wanaozika watu wasio na ndugu.

Mwili wake ulizikwa bila heshima yoyote ile, hakuna yoyote kutoka Kongo aliye hudhuria kuondoa familia yake, Mobutu ambae alikuwa tajiri mwenye majivuno mwisho wake ulikuwa mbaya, alizikwa kama kibaka na hakuna aliye mpatia heshima za mwisho.

Mobutu kipindi kile Lumumba anauwawa aliamlisha mwili wa Lumumba uchomwe moto ili watu wasije kwenda kutoa heshima yoyote kwenye kaburi lake kwa kumuenzi, alio waamrisha kuchoma moto mwili wa Lumumba wao wakaamua kuutumbukiza kwenye tindikali mwili wa Lumumba ili kupoteza ushahidi wote.

Sasa turejee kwanini mabaki ya Lumumba yamezikwa kwa heshima zote za kitaifa?

Kwanza cha kuelewa ni kwamba, toka kifo cha Lumumba mpaka sasa imeshapita zaidi ya miaka 60, hakuna mahali mwili wake ulipatikana ili apewe heshima yake, Nikueleze tu ni kwamba nchini Kongo Patrice Lumumba anaheshimiwa kuliko kiongozi yoyote yule nchini Kongo DRC.

Machungu ya wakongo kumpoteza Lumumba yanaishi mpaka leo, Patrice Lumumba na Laurent Desiree Kabila utazamwa kama mashujaa wa taifa hilo.

Kumekuwepo mijadala kadhaa ya kumpa hadhi Lumumba kwa kuibadilisha jina uwanja wa ndege wa Ndjili kuitwa Patrice Lumumba, Picha yake kutiwa kwenye note ua sarafu, jengo la ikulu kuitwa Patrice Lumumba palace na siku maalumu ya kifo chake kuwa siku ya mapumziko.

Mpaka sasa Mji wa Katakakombe huko Sankuru umeitwa Lumumbavile, tarehe ya Uhuru kujumuishwa na kumbukumbu ya maisha ya Lumumba, mchakato wa kuibadilisha jina uwanja wa ndege wa Ndjili unaendelea, yote ni kumpa heshima stahiki Lumumba.

Lumumba alikosa yote hayo kwakuwa Mwili wake baada ya kuuwawa uliwekwa kwenye tindikali, huku wauwaji wakibakia na jino ambalo ndio mabaki yake ambayo hatimaye yamerejeshwa kutoka Ubelgiji na kuzikwa kuashilia heshima ya mwasisi wa taifa na shujaa wao ambae sehemu ya mwili wake hatimae imezikwa kwenye aridhi ya Kongo.

Kama nilivyo tangulia kusema huko nyuma kuwa operation ya kumuua Lumumba iliitwa "Operation Barracuda", sitoileza sana hapa ila ntaieleza kwa uchache sana ili uone unyama aliofnyiwa Lumumba na ujue kwanini wakongo wameamua kufanya mazishi ya kitaifa ya mapumziko siku tatu na kutembeza jeneza la mabaki ya Lumumba nchi nzima kuanzia Kinshasa, Lubumbashi, Kisangani, Lumumbavile,Bukavu, Goma na maeneo yote ya Kongo.

Nikukumbushe Operation Barracuda...

Alhamisi ya Juni 30, 1960, Congo ilijipatia uhuru kutoka kwa Ubelgiji, Waziri Mkuu Patrice Emery Lumumba akiwa na miaka 35, akawa kiongozi wa jamhuri hii mpya, Lakini hali ya amani na utulivu ikatoweka muda mfupi baadaye, Kikosi cha majeshi ya waasi kikazua vurugu kiasi kwamba Ubelgiji ilipeleka jeshi lake kulinda raia wake.

Siku chache baadaye, Jumatatu ya Julai 11, ya mwaka huo, Jimbo la Katanga, lililokuwa likiongozwa na Moise Kapenda Tshombe likajitenga. Umoja wa Mataifa ukaingilia kati kwa kutuma jeshi la kulinda amani.

Jumanne ya Januari 17, 1961, miezi sita tu baada ya uhuru wa Congo, Patrice Lumumba aliuawa katika Jimbo la Katanga. Februari 13, maofisa wa Jimbo la Katanga wakatangaza kifo cha Lumumba, lakini hakuna aliyewaamini, Hata wao hawakuziamini taarifa walizotoa, Lawama zikaanza kumiminika kutoka pande zote za dunia.

Urusi iliwashutumu mabeberu na kuitaka Marekani iondoe watu wake Congo, pia ikamtaka aliyekuwa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, Dag Hammarskjold, kujiuzulu kwa sababu alionekana kuwa kibaraka wa wakoloni.

Katika jiji la Moscow nchini Urusi watu waliandamana baada ya kupata taarifa za kuuawa kwa Lumumba, Katika jiji la Beijing, China, kulifanyika maandamano makubwa ya watu waliokadiriwa kuwa zaidi ya 100,000. Katika nchi mbalimbali raia walivamia balozi za Ubelgiji na kufanya uharibifu.

Ndani ya mwaka mmoja tangu kuuawa kwa Lumumba, Umoja wa Mataifa ulifanya uchunguzi na baadaye ikabainika kuwa hata Shirika la Kijasusi la Marekani (CIA) lilishiriki katika njama za kumuua Lumumba.

Katika ukurasa wa 198 wa kitabu “The African Liberation Struggle: Reflections” cha Godfrey Mwakikagile, jasusi wa Marekani, Stephen Andrew Lucas, ambaye alikuja Tanzania na kufundisha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alikuwa Congo na kufanya kazi chini ya mkuu wa CIA, Larry Devlin, wakati Lumumba alipokamatwa na kuuawa. Mwingine aliyekuwa Congo na baadaye akaenda Zanzibar ni Frank Carlucci.

Pamoja na Lumumba walikuwako wengine wawili waliokamatwa na kuuawa pamoja naye; Joseph Okito (alikuwa Naibu Spika wa Bunge la Congo) na Maurice Mpolo (alikuwa Waziri wa Vijana na Michezo). Watatu hao walisafirishwa kwa ndege kutoka Kinshasa hadi mji mkuu wa Kalonji wa Bakwanga (sasa unaitwa Mbuji-Mayi).

Wakiwa kwenye ndege aina ya DC-3, wote watatu waliteswa kikatili na walinzi wa Congo. Ndege ilipowasili anga la Bakwanga, rubani hakuweza kutua kwa sababu uwanjani hapo kulikuwa kumetapakaa matanki ya ujazo wa galoni 55.

Rubani aliamua kwenda kutua Uwanja wa Elisabethville (sasa Lubumbashi), na ndege ilipotua, Lumumba alikuwa anakaribia kuzirai kutokana na maumivu.

Ndani ya ndege walikuwa wakiteswa mbele ya Kamishna wa Ulinzi wa Congo, Ferdinand Kazadi na Kamishna wa Mambo ya Ndani wa Congo, Jonas Mukamba. Walipofikishwa Lubumbashi walipelekwa kwenye nyumba jirani na Uwanja wa Ndege wa Luano na kuendelea kuteswa.

Lumumba, ambaye uso wake uliharibiwa kiasi cha kutotambulika kutokana na vipigo na nguo zake zikiwa zimetapakaa damu, alisimamishwa kwenye kichuguu kikubwa huku akimulikwa na taa za magari.

Kwa amri ya Moise Tshombe, rais wa jimbo la Katanga ambaye naye alikuwa akipokea maelekezo kutoka Brussels, Lumumba aliteswa. Kikosi cha mauaji kilimtoa Lumumba katika nyumba alimokuwa akiteswa na kumsafirisha kwa mwendo wa dakika 45 hadi Katanga.

Hapo aliuawa na kikosi cha mauaji kwa kupigwa risasi kwa amri ya Kapteni wa Ubelgiji, Julien Gat, Aliyemfyatulia risasi ni askari wa Ubelgiji, kanali Carlos Huyghe, Mwingine aliyeshiriki kuwafyatulia risasi na kuwaua Okito na Mpolo ni kapteni Julien Gat.

Kupoteza ushahidi...

Baada ya kuuawa kwa risasi, miili ya watatu hao ilizikwa eneo walilouawa. Kwa hofu kwamba kaburi la Lumumba lingegundulika na baadaye lingeweza kugeuzwa kuwa eneo la heshima, Wabelgiji na vibaraka wao waliamua kupoteza ushahidi ambao ungeweza kuelekeza uliko mwili wake.

Jumatano ya Januari 18, ikiwa ni siku moja baada ya mauaji hayo, miili ya kina Lumumba ilifukuliwa na kupelekwa ndani zaidi msituni na kuzikwa upya karibu na mpaka wa Rhodesia (Zimbabwe) na Congo.

Usiku wa Jumapili ya Januari 22 ndugu wawili wa Ubelgiji Kamishna wa Polisi wa Ubelgiji, Gerard Soete na ndugu yake walikwenda tena kufukua miili ya Lumumba, Okito na Mpolo. Safari hii walikuwa na shoka na misumeno.

Waliikatakata miili hiyo vipande vipande kabla ya kuyeyusha mabaki yake kwa tindikali iliyokuwa imejaa kwenye pipa la petroli la lita 200. Baadaye Soete alikiri kwamba alitumia koleo kung’oa meno mawili ya Lumumba kwa ajili ya ukumbusho.

Operesheni Barracuda...

Katika kitabu cha “Encyclopedia of leadership: A-E” (ukurasa 925), George R. Goethals na Georgia Sorenson wanasema mpango wa kumuua Lumumba uliitwa ‘Operesheni Barracuda’ na uliandaliwa na Marekani, hususan CIA, ndipo Lumumba akakamatwa na Kanali Mobutu Oktoba 10, 1960.

Katika kikao kilichofanyika jijini Washington, Marekani iliamriwa Lumumba aondolewe madarakani na awekwe kiongozi ambaye angekubali kulinda maslahi ya Wamarekani nchini Congo.

Maagizo hayo yakatumwa kwa mkuu wa CIA nchini Congo, Lawrence Raymond Devlin. CIA wakaunganisha nguvu zao na Ubelgiji.

Agosti 1960, msaada wa kijeshi kutoka Urusi uliingia Congo, jambo ambalo halikuwapendeza Wamarekani na Wabelgiji. Ilikuwa lazima Lumumba aondoke kwa gharama zozote.

Ndipo wakamshawishi Rais wa Congo, Joseph Kasavubu, lakini waligonga mwamba. Devlin akaripoti taarifa hizo makao makuu ya CIA jijini Langley, Marekani, Agosti 24, 1960.

Dk Sidney Gottlieb, mtaalamu wa dawa, akapewa maagizo ya kutafuta sumu ya kumuua Lumumba na isijulikane kuwa Marekani imehusika, na iwe ni dawa ambayo chanzo chake ni Afrika.

Nakurudisha mwezi January...

Januari 1960 Wabelgiji walilazimika kuita mkutano katika jiji la Brussels, Ubelgiji, katika mkutano huo maalum ndipo ilipokubaliwa Congo watapewa uhuru wao Juni 30 ya mwaka huo.

Baada ya ghasia zilizozuka Oktoba 23, 1959 na kudumu hadi Oktoba 28, 1959 na baada ya Patrice Lumumba kukamatwa na kuhukumiwa kifungo gerezani baada ya chama chake kusababisha ghasia hizo, Serikali ya Ubelgiji ilichapisha ripoti kuhusu ghasia hizo.

Jumapili ya Novemba 1, 1959 Lumumba alikamatwa na Serikali ya kikoloni na kumhukumu kifungo cha miezi sita gerezani. Tofauti na ilivyodhaniwa awali, kifungo hicho kiliongeza umaarufu wa Lumumba. Katika ghasia hizo iliripotiwa watu 30 waliuawa.

Theodore Trefon katika kitabu ‘Reinventing Order in the Congo: How People Respond to State Failure in Kinshasa’ anasema ghasia zilizokuwa mbaya zaidi katika historia ya Congo ni zile za kati ya Januari 4 na 6, 1959. “Karibu raia wote Waafrika waliingia mitaani kufanya vurugu”.

Ghasia hizo zilianza polisi wa Ubelgiji walipovamia mkutano wa chama cha Abako na kuwatawanya wafuasi wake, Kwa mujibu wa andiko linaloitwa ‘The Congo Operation, 1960—63’ la Birendra Chakravorty, zaidi ya watu 100 waliuawa, Hata kabla ripoti hiyo haijachapishwa, mkutano uliofanyika mjini Brussels, Ubelgiji na kumalizika Jumanne ya Januari 13, 1959 uliamua kwamba wakati wa Congo kupewa uhuru wake umefika.

Mpango wa kuwakabidhi Wakongo Serikali ya kujitawala wenyewe uliandaliwa tangu Desemba 1955 na kutangazwa Februari 1956, Aliyeifanya kazi hiyo ni Profesa wa Ubelgiji kutoka Chuo Kikuu cha Antwerp aliyeitwa Anton Arnold Jozef “Jef” Van Bilsen.

Mpango huo ulipewa jina la “Thirty Year Plan for the Politial Emancipation of Belgian Africa”,
Alipendekeza kuwepo mpango wa miaka 30.

Pendekezo hilo la Desemba 1955 aliliita “Mpango wa Miaka 30”, Kwa maneno mengine, ikiwa ushauri wa Profesa Bilsen ungefuatwa, Congo ingejipatia uhuru wake mwaka 1985.
Karibu kipindi chote cha mwaka 1959 Congo iligubikwa na ghasia. Kuona hivyo, Januari 1960 Serikali ya Ubelgiji iliitisha mkutano mjini Brussels ambao vyama vyote vikubwa vya siasa na viongozi wa makabila makubwa ya Congo walihudhuria.

Mkutano huo ulitawaliwa na madai ya “uhuru sasa”. Baada ya shinikizo kuwa kubwa, Ubelgiji waliamua kwa shingo upande kuwapatia Wakongo uhuru wao ifikapo Juni 30 ya mwaka huo, Wakati wa kampeni za uchaguzi za Aprili 1960 vyama vingi viligombea viti vya ubunge.

Vyama vikubwa vilivyoshiriki uchaguzi huo ni MNC cha Patrice Lumumba kilichokuwa na sera ya kuiunganisha Congo yote iwe moja, na kingine ni kile cha Joseph Kasavubu cha Alliance des Bakongo (Abako), Katika uchaguzi uliofanyika kuanzia Mei 11 hadi 25, 1960, Lumumba na waungaji mkono wake walipata ushindi mkubwa wa viti bungeni akifuatiwa na Kasavubu, wakalazimika kugawana madaraka.

Kasavubu alikubali kuwa Rais wa nchi na Lumumba akiwa mtendaji mkuu wa serikali, yaani Waziri Mkuu, Juni 23, 1960 Lumumba aliapishwa kuwa Waziri Mkuu wa Congo na, Juni 30, 1960, ikawa ndiyo siku ya uhuru wa Congo.

Siku hiyo na siku tatu baadaye zikatangazwa kuwa siku za mapumziko ili raia washerehekee uhuru wao, Katika sherehe hizo kila kitu kilionekana kufanyika katika hali ya amani, Ofisi ya Lumumba ilikuwa na shughuli nyingi huku kukiwa na msururu wa watu kuingia na kutoka huku Lumumba akijishughulisha na ratiba ndefu ya mapokezi ya wageni.

Siku ya uhuru Lumumba alitangaza kuwa Jumapili ya Julai 3 ingekuwa siku ya msamaha wa jumla kwa wafungwa wote, Lakini tangazo hilo halikutekelezwa na Julai 4, Lumumba aliita kikao cha Baraza la Mawaziri kujadili machafuko ya wanajeshi wa Congo.

Wanajeshi wengi waliokuwa na matumaini makubwa kwamba mara baada ya uhuru kupatikana wangepandishwa vyeo na kuongezewa maslahi, walianza kufanya fujo baada ya kuona matarajio yao hayatimii, Ingawa ilikuwa ndani ya wiki moja tu tangu uhuru kupatikana, baadhi yao waliona kuwa Lumumba hatimizi matarajio yao haraka kama walivyotarajia awali.

Bunge lililokutana katika kikao cha kwanza tangu uhuru na kuanza kazi ya kutunga sheria, kilipiga kura ya nyongeza yao ya mishahara. Lumumba alishtushwa na kitendo hicho cha Bunge lake. Kwa kujua hatari ambayo ingesababishwa na kitendo hicho, Lumumba alikiita “upumbavu wa uharibifu.”
Julai 5,, Kamanda wa Jeshi la Congo, Jenerali Emile Janssens, ambaye alikuwa Mbelgiji, aliwaita maofisa wa jeshi na kuwataka wadhibiti hali ya amani. Alisisitiza kuwa hali ilivyokuwa kabla ya uhuru ndivyo itakavyokuwa baada ya uhuru. Lakini tangazo hilo halikutuliza hasira ya baadhi ya wanajeshi.

Siku iliyofuata yaani Julai 6 ambayo ilikuwa siku ya sita tu baada ya uhuru Lumumba aliwapandisha vyeo askari wa Congo kwa ngazi moja lakini hali ya ghasia ilipozidi kuwa mbaya, Lumumba alimfukuza kazi Jenerali Janssens.

Siku mbili baadaye, Ijumaa ya Julai 8, Lumumba aliwaondoa maofisa wote wa kijeshi wa Ubelgiji na kuweka wa Congo ingawa Wazungu kadhaa waliendelea kubaki jeshini kama washauri, Julai 9 Balozi wa Marekani Congo, Clare Hayes Timberlake, alituma taarifa kwenda Marekani, akidai Ubelgiji wakiingilia mgogoro wa Congo kutakuwa na maafa.

Julai 10 Ubelgiji walituma wanajeshi kwenda Congo kuwalinda raia wao na biashara zao. Kasavubu na Lumumba waliigeukia Marekani kuomba msaada wa kulipanga upya jeshi la Congo, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Marekani ikasema Marekani iko tayari kusaidia lakini chini ya usimamizi wa Umoja wa Mataifa na uongozi wa Ubelgiji.
Julai 11 Moise Tshombe akatangaza kuwa Jimbo la Katanga limejitenga na Congo na kisha akalitangaza kuwa liko huru huku akiiomba Ubelgiji walitambue na wapewe misaada.

Jumanne, Julai 12 Kasavubu na Lumumba waliiomba Marekani msaada kudhibiti uchokozi wa Wabelgiji na siku hiyo hiyo baraza la mawaziri lilikutana bila Lumumba na Kasavubu kuwapo kwenye kikao, na wakaomba wapewe wanajeshi 3,000 wa Marekani, Rais wa Marekani, Dwight David Eisenhower, aliamuru vikosi vya nchi yake, vikiwa na zana za kivita, kwenda Congo ikiwa Waziri Mkuu wa Urusi, Nikita Krushchev, angetuma majeshi yake kwenda huko.

Jumatano, Julai 13, Urusi iliutaka Umoja wa Mataifa kuzuia uchokozi wa Ubelgiji nchini Congo. Alhamisi ya Julai 14 Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio la kupeleka jeshi Congo. Siku hiyo hiyo Lumumba na Kasavubu wakawasiliana na Urusi na kuwaomba wafuatilie hali ya Congo. Urusi ilikubali.

Ijumaa, Julai 15, majeshi ya Umoja wa Mataifa yaliwasili Congo. Julai 16, baada ya kukutana na Lumumba, mwakilishi wa Umoja wa Mataifa nchini Congo, Ralph Bunche, aliripoti “Lumumba alikuwa kama kichaa na alitenda mambo kwa tabia za kitoto.” Lumumba na huyo Bunche hawakuelewana vizuri.

Baada ya hali kuzidi kuwa mbaya, Jumapili ya Julai 17 Lumumba alitishia kuwa atayaita majeshi ya Urusi ili yasaidie kuyaondoa majeshi ya Umoja wa Mataifa kama watashindwa kuyaondoa majeshi ya Ubelgiji ndani ya saa 72.

Ijumaa, Julai 15, majeshi ya Umoja wa Mataifa yaliwasili Congo. Julai 16, baada ya kukutana na Lumumba, mwakilishi wa Umoja wa Mataifa (UN) Congo, Ralph Bunche, aliripoti, “Lumumba alikuwa kama kichaa na alitenda mambo kwa tabia za kitoto.” Lumumba na Bunche hawakuelewana vizuri.

Baada ya hali kuzidi kuwa mbaya, Jumapili ya Julai 17 Lumumba alitishia kuwa atayaita majeshi ya Urusi ili yasaidie kuyaondoa majeshi ya Umoja wa Mataifa kama watashindwa kuyaondoa majeshi ya Ubelgiji ndani ya saa 72, Hali ya utulivu na amani ilipozidi kudorora Congo katika zile siku chache baada ya uhuru, Lumumba aliwatishia Umoja wa Mataifa kuwa atayaita majeshi ya Urusi ili yamsaidie kulinda amani Congo na kujikuta akirushiana maneno na Bunche.
Jumamosi Julai 9, 1960, ikiwa ni siku tisa tangu ijipatie uhuru, Serikali ya Congo ilibadili jina la jeshi kutoka ‘Force Publique’ na kuwa ‘Armee Nationale Congolaise’ (ANC).

Baraza la Mawaziri lilimteua Victor Lundula, mwafrika aliyepigana katika Vita Kuu II ya Dunia, kuwa jenerali wa kwanza mkuu wa majeshi ya Congo na kuchukua nafasi ya Jenerali Emile Robert Alphonse Janssens ambaye alikuwa Mbelgiji, Lumumba alimteua pia Joseph-Desire Mobutu kuwa mmoja wa mawaziri wadogo katika ofisi ya Waziri Mkuu, kama kanali na mnadhimu mkuu wa ANC, Kitabu ‘The Congo: From Leopold to Kabila: A People’s History’ cha Georges Nzongola-Ntalaja katika ukurasa wa 98 kinasema uteuzi wa watu hao wawili Lundula na Mobutu ulitolewa vibaya, “Lundula hakuwa na sifa zinazohitajiwa kuendesha jeshi la nchi, hususan jeshi jipya.

Na kwa Mobutu, Lumumba alifanya kosa kubwa kwa kuamini tu kwamba ana uwezo wa kusimamia jeshi kwa vile aliweza kuwasimamia watu wachache waliomzunguka.”
Kitabu hicho kinasema “(Lumumba) hakusikiliza uvumi uliosambaa uliodai Mobutu alikuwa wakala wa majasusi wa Ubelgiji na Marekani. Kwa kumteua Mobutu kushika wadhifa huo, tayari (Lumumba) alikuwa amemchagua Yuda wake mwenyewe.”

Mwandishi wa historia, Didier Ndongala Mumbata, alilifafanua zaidi katika kitabu ‘Patrice Lumumba, Ahead of His Time’. Mumbata anaandika kuwa matukio ya kati ya Julai na Septemba 1960 yalibadili sana uhusiano wa Lumumba na baadhi ya mawaziri wake na wanasiasa wenzake. Alionekana kupigana vita mwenyewe, Mambo yalipokuwa mazuri alizungukwa na marafiki na ‘wapongezaji’ wengine wa kweli na wa uongo. Mambo yalipokwenda mrama alijikuta yuko mwenyewe.

Mobutu, ambaye alikuwa rafiki yake wa karibu na ambaye awali alimteua kuwa msaidizi wake katika chama chake cha MNC, kisha akamwingiza serikalini baada ya kuwa waziri mkuu wa kwanza wa Congo, na baadaye akamfanya kuwa mnadhimu mkuu wa jeshi la Congo, alimsaliti na kujiunga na kambi ya Joseph Kasavubu. Wote wawili, Kasavubu na Mobutu walishiriki kwa kiasi kikubwa kumwangusha na kumuua Lumumba.

Familia ya Lumumba ilimjua sana Mobutu, Lumumba alikutana na Mobutu wakati yeye (Mobutu) akisomea uandishi wa habari mjini Brussels, Ubelgiji, Mobutu na Lumumba walikuwa na matamanio yaliyokaribia kufanana, Walitamani kuona Congo iliyo na umoja, walichukia kutawaliwa na wageni, Kwa ushawishi wa Lumumba, Mobutu aliingia katika siasa za Congo kupitia MNC, Mobutu alifanya kazi kama katibu muhtasi wa Lumumba. Yeye ndiye aliyeamua nani aonane na Lumumba na kwa muda gani.

Mwandishi Mumbata anasema kwa ujumla Mobutu ndiye aliyekuwa anapanga ratiba yote ya shughuli za kisiasa za Lumumba, Nyumbani kwa Lumumba kulikuwa kama nyumbani kwa Mobutu kwa sababu aliweza kwenda huko wakati wowote kadri alivyotaka na alikuwa akijihudumia vyakula na vinywaji kadri alivyoweza.
Sehemu kubwa ya maisha yake ya kikazi siku za mwanzo za harakati za siasa za Congo kuelekea siku ya uhuru, Mobutu alikaa nyumbani kwa Lumumba.

Hii ilimfanya awe karibu zaidi na Lumumba kuliko mwanasiasa yeyote duniani, Katika ukurasa wa 2562 wa kamusi ‘The 20th Century Go-N: Dictionary of World Biography, Volume 8’ iliyohaririwa na Frank Magill, inasimuliwa kuwa Lumumba alimwamini sana Mobutu, Mwandishi Didier Mumbata anasimulia: “Lumumba aliwaamini watu kirahisi, na haraka. Alikuwa mwema, alikuwa akimwambia mkewe kuwa Mobutu alikuwa rafiki yake sana na nyumbani kwake (Lumumba) ni nyumbani kwa Mobutu.

Lumumba alijua fika kuwa Mobutu alihitaji sana fedha kuikimu familia yake, lakini alikuwa akimwambia asijaribu kuisaliti Congo na watu wake kwa sababu ya fedha. Lakini Mobutu, kama alivyokuwa Yuda kwa Yesu (Kristo), alikuja kumsaliti rafiki yake huyo kwa Wabelgiji na Wamarekani.”

Hata hivyo, lilipokuja suala la kupata msaada wa kijeshi kutoka Urusi ili isaidie kuyaondoa majeshi ya Ubelgiji nchini Congo, ndipo Rais Kasavubu na Mobutu walipoungana kumpinga Lumumba, Lumumba alipoona hapati msaada wa haraka kutoka majeshi ya kulinda amani ya Umoja wa Mataifa, Julai 17, 1960 alitishia kuyaita majeshi ya Urusi ili yasaidie kuyaondoa ya Umoja wa Mataifa kama watashindwa kuyaondoa majeshi ya Ubelgiji ndani ya saa 72, Baadaye siku hiyo, Lumumba alitoa tishio jingine. Akasema ikiwa majeshi ya Umoja wa Mataifa hayatayaondoa majeshi ya Ubelgiji kabla ya Julai 20, watalazimika kuyaita majeshi ya Urusi kuwaondoa wao.

Julai 22, malori 100 ya kijeshi kutoka Urusi yaliwasili Congo, lakini hayakukabidhiwa jeshi la Umoja wa Mataifa. Katika Mkutano wa Usalama wa Taifa (NSC) nchini Marekani, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kijasusi la Marekani (CIA), Allen Dulles, aliwaambia wenzake mkutanoni kuwa alihisi “Lumumba amenunuliwa na Wakomunisti”. Mkutano huo ulihudhuriwa pia na Rais Dwight Eisenhower.

Julai 27, akiwa Umoja wa Mataifa, kwa mara nyingine Lumumba aliomba msaada Umoja wa Mataifa, Marekani na Urusi, alipozuru Washington, Lumumba alikwenda kukutana na Waziri Mdogo wa Mambo ya Nje wa Marekani, Douglas Dillon, ambaye baadaye alidai kuwa Lumumba ni “mwendawazimu” na kwamba “ni mgumu kushughulika naye.”

Agosti 1, akizungumza mbele ya Umoja wa Mataifa, Lumumba alimshutumu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Dag Hammarskjold, kwa kuyakatalia majeshi ya Umoja wa Mataifa kuishambulia Katanga.
Agosti 7, Lumumba alikwenda kwa siri Ghana alikokutana na Rais Kwame Nkrumah kuzungumza suala la nchi hizo kuungana, Agosti 8 Jimbo la Kasai Kusini nalo likatangaza kujitenga na Congo, Juma moja baadaye, Lumumba aliomba msaada wa kijeshi kutoka Urusi kudhibiti majimbo ya Katanga na Kasai yaliyojitenga.

Kesho yake, Agosti 16, Urusi wakatangaza kuwa huenda Congo wakahitaji kupatiwa jeshi la nje kuleta hali ya amani. Lumumba akasisitiza kuwa majeshi ya Umoja wa Mataifa yaondoke Congo.
Agosti 18 Urusi wakatuma kwenda Congo ndege 10 za kivita zenye rangi ya jeshi la Congo.

Baada ya kurejea Congo akitokea Marekani, Lumumba aliwaambia Rais Kasavubu na Mkuu wa Majeshi yake, Joseph Mobutu, kwamba ameamua sasa kuyaita majeshi ya Urusi, Kasavubu na Mobutu walimkatalia. Lakini Lumumba alikuwa ameshafanya uamuzi. Aliita majeshi ya Urusi ambayo yangemsaidia kuzuia kujitenga kwa jimbo la Kasai Kusini. Alifanikiwa, lakini mara baada ya mapigano kumalizika yalifuatiwa na mauaji ya watu zaidi ya 1,000 na wengine wapatao 250,000 kuyakimbia makazi yao.

Mara moja wakala wa CIA nchini Congo, Larry (Lawrence) Devlin, akatuma ripoti Washington ikidai kuwa Lumumba anajiandaa kufanya mapinduzi ya Kikomunisti, Mradi wa kwanza wa CIA wa kumshughulikia Lumumba ulianza mapema Agosti 1960 na ulipewa jina la ‘Operation Wizard’. Sehemu moja ya utekelezaji wa mpango huo ni kuwahonga waandishi wa habari wa ndani na nje ya Congo ili waandike habari mbaya za Lumumba, kufadhili maandamano ya kumpinga, na kuhonga wanasiasa watofautiane naye. Mpango huo ulisimamiwa na mkuu wa CIA nchini Congo, Larry Devlin na watu wake.

Katika kitabu ‘Shadow Warfare: The History of Africa’s Undeclared Wars’ cha Larry Hancock, aliyekuwa akiandika muhtasari wa mkutano huo ni Robert Johnson. Dulles alikaririwa akisema, “Kwa Lumumba, tunakabiliana na mtu wa aina ya Castro au mbaya kuliko Castro.”
Siku chache baadaye, kwa mujibu wa kitabu ‘The Assassination of Lumumba’ cha Ludo de Witte, Agosti 26 “Allen Dulles, mkuu wa CIA, alituma telegramu kwenda ofisi za CIA za Leopoldville chini ya Larry Devlin: Telegramu hiyo ilisomeka “Kuondolewa kwa Lumumba madarakani lazima kuwe jambo la lazima na la haraka ... Lazima lipewe kipaumbele cha kwanza katika shughuli zetu.”

Baadaye siku hiyo hiyo Dulles alituma ujumbe mwingine kwenda Congo uliosomeka: “Sasa ni uhakika kwamba iwapo (Lumumba) ataendelea kushikilia wadhifa wake (Uwaziri Mkuu) Ukomunisti utatawala ... Kung’olewa kwake lazima kupewe kipaumbele.”

Shirika la Kijasusi la Marekani (CIA) lilituma ‘ujumbe wa sumu’ kwenda Congo kwa ajili ya kumuua Waziri Mkuu wa kwanza wa nchi hiyo, Patrice Emery Lumumba, Ujumbe huo kwenda kwa aliyekuwa mkuu wa CIA, Congo, Lawrence (Larry) Raymond Devlin, ulipelekwa na wakala wa CIA aliyeitwa Sidney Gottlieb, Kwa mujibu wa uchunguzi uliochapishwa na Madeleine G. Kalb katika kitabu ‘The Congo Cables: The Cold War in Africa-From Eisenhower to Kennedy’, ulimwambia Devlin hivi: “Atajitangaza kama Joe kutoka Paris... ni muhimu uonane naye haraka mara atakapokupigia simu.

Atajitambulisha kwako kikamilifu na kukueleza kazi aliyokuja kuifanya.”
Ndipo jioni ya Jumatatu ya Septemba 26, Gottlieb aliwasili Congo, Devlin, aliyekuwa anafanya kazi ya ujasusi kwa mwamvuli wa ofisa wa ubalozi wa Marekani Congo, aliondoka ofisini kwake kwenda kukutana na mgeni wake.
Walipokuwa kwenye gari la Devlin, Gottlieb alimweleza kuwa “nimekuja Congo kukupa maelekezo kuhusu operesheni moja muhimu.”
Kitabu ‘Poisoner in Chief: Sidney Gottlieb and the CIA Search for Mind Control’ cha Stephen Kinzer kinasema Gottlieb aliwahi kuifanyia majaribio sumu yake kwa wafungwa, watumiaji dawa za kulevya, wagonjwa mahospitalini, washukiwa wa upelelezi, raia wa kawaida na hata wafanyakazi wenzake, na kote huko, alisema, alifanikiwa.

Gottlieb alikuja kujulikana kuwa ni ofisa pekee wa CIA aliyebeba sumu kutoka Amerika kwenda kumuua kiongozi wa nchi nyingine katika bara la Afrika, Akiwa nyumbani kwa Devlin katika ubalozi wa Marekani mjini Leopoldville, ndipo Gottlieb alipomfahamisha Devlin kuwa alikuwa amebeba vifaa vyenye sumu ya kumuua Waziri Mkuu Lumumba.
“Mungu wangu,” alishangaa Devlin. “Nani aliyeidhinisha hii operesheni?” Alihoji.

“Ni Rais (Dwight) Eisenhower,” alijibu Gottlieb. “Nilikuwapo wakati akiidhinisha, lakini Dick Bisell alisema Eisenhower anataka Lumumba aondolewe madarakani.” Wakati huo Dwight David “Ike” Eisenhower ndiye alikuwa Rais wa Marekani na Bisell alikuwa ofisa wa CIA aliyeshughulikia miradi mikubwa.

Gottlieb na Devlin wote walijikuta wameacha kuongea kwa dakika kadhaa, Devlin akawasha kwanza sigara kabla hajaendelea kuongea, Baadaye kidogo Gottlieb akavunja ukimya uliotawala “Ni jukumu lako kufanya operesheni hii, ni yako peke yako,” Gottlieb alimwambia Devlin “Maelezo ni yako, lakini lazima (operesheni) iwe safi, ifanyike kwa namna ambayo hakuna kitu kinachoweza kuacha nyuma alama yoyote ya kuihusisha serikali ya Marekani.”

Kisha akamkabidhi kasha la sumu alilotoka nalo Marekani “Chukua hii,” alimwambia “Kwa kilichomo humu ndani kikitumika hakuna mtu atakayejua kamwe kuwa Lumumba aliuawa" Baada ya hapo Gottlieb akaanza kumpa Devlin maelezo na maelekezo ya namna ya kufanya, Ingeweza kuwekwa kwenye kitu chochote ambacho kingeugusa mdomo wa Lumumba iwe ni mswaki au chakula, na hapo kazi ingekuwa imemalizika.

Sumu hiyo haikutengenezwa kwa namna ya kuua haraka, lakini kifo kingekuja baada ya saa kadhaa. Alimwambia pia kwamba hata kama kungefanyika uchunguzi wa sababu za kifo, kile ambacho kingeonekana ni zile sababu za kawaida tu.

Hata hivyo ilishindikana, hawakuweza kumwekea sumu kwa kile ambacho John Jacob Nutter alikisema katika kitabu chake, ‘The CIA’s Black Ops: Covert Action, Foreign Policy, and Democracy’, kwamba “Hata kuweka sumu kwenye chakula chake ilikuwa shida sana kwa sababu CIA haikuwa na mawakala ambao wangeweza kuingia jikoni kwa Lumumba.” Kwa hiyo CIA haikufanikiwa kumuua Lumumba kwa sumu, Kwa zaidi ya miongo miwili akiwa CIA, Gottlieb alikuwa ameelekeza nguvu na akili zake zote katika utafiti wa namna ya kuanzisha mfumo wa kudhibiti akili za mwanadamu lakini alijulikana zaidi kama “mtengenezaji mkuu wa sumu katika CIA.”

Tafiti zake zilikuwa zikifanyika kwa siri kubwa kiasi kwamba alipokuja kuacha kazi mwaka 1972 aliteketeza asilimia 80 ya nyaraka zilizokuwa na ripoti mbaya. Alilazimika kuyateketeza kabla ya kuondoka kazini. Asilimia kubwa ya nyaraka hizo inahususu kazi za Gottlieb.
Anne Collins, katika ukurasa wa 30 wa kitabu chake, ‘In the Sleep Room: The Story of the CIA Brainwashing Experiments in Canada’, anaandika kuwa nyaraka hizo zilikuwa na taarifa mbaya kiasi kwamba maelfu ya kurasa za nyaraka “ziliharibiwa kwa amri ya watu wawili: Mkurugenzi wa CIA Richard Helms, aliyestaafu mwaka 1973 na Dk Sidney Gottlieb, ambaye alihusika zaidi na nyaraka hizo.”
Ilidaiwa kuwa nyaraka hizo zingewekwa wazi zingezua kashfa kubwa zaidi duniani na huenda ingeufungulia ulimwengu sababu za kuifungulia mashtaka CIA kwa ukatili dhidi ya wanadamu.

Kitabu ‘Top Secret Government Archives: Missing Files and Conspiracy Paper Trails’ cha mwandishi wa habari za utafiti, Nick Redfern, kinaandika: “Kama tulivyoona, wakati hofu ilipotanda ndani ya CIA kwamba itajulikana kwa watu wa nje [ya CIA] mradi wa CIA [dhidi ya utu], mkurugenzi wa shirika hilo, Richard Helms na Sidney Gottlieb waliandaa mpango wa kuziteketeza moja kwa moja nyaraka hizo.

Nyaraka hizo zilijulikana pia kama ‘Mpango wa CIA wa kudhibiti akili za wanadamu’, Sehemu ya mradi huo ulikuwa ni kufanya majaribio juu ya ubongo wa mwanadamu kwa kuendeleza dawa ambazo zingeweza kutumiwa kudhoofisha uwezo wa mtu wa kudhibiti akili yake ili atamke yale asiyokusudia kuyatamka.

Mradi huo na mingine mingi iliandaliwa chini ya Ofisi ya Ushauri wa Kisayansi ya CIA kwa kuratibiwa na Maabara ya Vita ya Kibaiolojia ya Jeshi la Marekani, Nick Redfern anaendelea: “Kumbuka kuteketezwa nyaraka hizo kulivyofanikiwa; ni kwa kuzimwaga kwenye tanuri, mwaka 1973, katika kituo cha kumbukumbu cha CIA, kilichokuwa Warrenton, Virginia. Kwanini hili jambo lilikuwa la muhimu? Kwa sababu kugundulika siri zilizokuwa kwenye nyaraka hizo kungeonyesha ukatili dhidi ya mwanadamu uliofanywa na shirika hilo”, Hata hivyo, wakati watu wengi waliokuja kujulishwa kuwa ndugu zao walilishwa sumu iliyotengenezwa na Sidney Gottlieb, walianza kufungua mashtaka mmoja baada ya mwingine alianza kuitwa katika mahakama mbalimbali za nchini Marekani.

Wakati baadhi ya kesi hizo ziliendelea na nyingine zikiwa kwenye upelelezi, Gottlieb alifariki dunia Jumatano ya Machi 10, 1999 Jijini Washington.

Turudi Kinshasa...

Agosti 21, 1960 Waziri Mkuu wa Congo, Patrice Lumumba aliomba waziwazi msaada wa kijeshi Urusi. Siku tano baadaye, Agosti 26, baada ya kukataliwa na majeshi ya Umoja wa Mataifa (UN) kuishughulikia Kasai Kusini iliyojitenga, Lumumba alituma majeshi ya Congo yanayomtii kwenda Kasai Kusini.

Wanajeshi hao walikuwa katika ndege 15 za kijeshi za Urusi na malori 100. Nia ya Lumumba ni kulirejesha jimbo lililojitenga. Kufikia hatua hiyo, Allen Dulles alimtumia Devlin ujumbe akimwelekeza amuue Lumumba.

Mwishoni mwa Agosti maofisa wa Urusi waliwasili Congo. Kwa kuona Lumumba alikuwa akiegemea sana ushauri na misaada kutoka Urusi, Rais Joseph Kasavubu alianza kuingiwa na wasiwasi.

Septemba 5, Rais Kasavubu akamfukuza kazi Lumumba kama Waziri Mkuu wa Congo. Wakati huo huo Lumumba naye akamfukuza kazi Rais wake, Kasavubu. Kwa hiyo walifukuzana kazi, Kasavubu alimteua Joseph Ileo kuwa waziri mkuu badala ya Lumumba.

Septemba 9, hata baada ya kudaiwa kufukuzwa kazi, Lumumba aliidhinisha malipo ya dola milioni moja kwa wanajeshi wa Leopoldville (sasa Kinshasa). Mgogoro wa uongozi ukaongezeka kati ya Lumumba na Kasavubu.

Baada ya vuta nikuvute kati ya Lumumba na Kasavubu, mgogoro ukafikia kilele chake Septemba 5, 1960. Mgogoro ulisababishwa na kutoelewana kati ya Lumumba na Kasavubu kuhusu namna ya kushughulikia Jimbo la Katanga lililojitenga na Congo.

Siku hiyo serikali ya Congo ikapasuka vipande viwili. Kasavubu akamfukuza Lumumba kazi ya uwaziri mkuu na kuliomba jeshi la UN lichukue madaraka ya utawala Congo. Baraza la Mawaziri la Lumumba nalo likamfukuza Kasavubu kama Rais wa nchi, likimtuhumu kwa uhaini.

Septemba 14, 1960, kikao cha pamoja cha Baraza la Congo kikapiga kura na kumkabidhi Lumumba madaraka ya kuongoza nchi hadi hapo mgogoro wa uongozi utakapomalizika na tume ya kibunge ndiyo ambayo ingemwongoza.

Hadi hapo kulikuwa na kambi mbili za serikali, moja ya Joseph Ileo (baadaye alibadili jina na kujiita Sombo Amba Ileo) ambaye aliteuliwa na Kasavubu kama Waziri Mkuu badala ya Lumumba. Kambi nyingine ni ya Lumumba ikiwa na baraka za tume ya Bunge.

Katika kuhakikisha viwanja vya ndege na redio havitumiwi vibaya, majeshi ya UN yalivitwaa lakini hata baada ya Baraza la Congo kupiga kura kumpa Lumumba mamlaka ya kuendelea kutawala, siku hiyo hiyo, Jumatano ya Septemba 14, Mobutu alitangaza anatwaa madaraka ya nchi hadi Desemba 31 ili kuwapa muda Lumumba na Kasavubu waafikiane. Kisha akateua serikali ya mpito.

“Kuanzia sasa,” alisema Mobutu, “Kasavubu na Lumumba hawako madarakani... ni mpaka mwishoni mwa Desemba watakapokubaliana namna ya kuongoza pamoja.

Baada ya Mobutu kuwatoa madarakani Kasavubu na Lumumba, Kasavubu alikimbilia Brazaville kujificha wakati Lumumba akibaki Leopoldville kwenye nyumba ya makazi ya waziri mkuu akilindwa na majeshi ya Mobutu asitoroke.

Mkono mrefu wa Shirika la Kijasusi la Marekani (CIA) ulionekana. Mwandishi James Hunter Meriwether katika ukurasa wa 218 wa kitabu chake, ‘Proudly We Can be Africans: Black Americans and Africa, 1935-1961’ anaandika: “Katika kipindi chote cha misukosuko, maofisa wa Serikali ya Marekani walikuwa katika jitihada kubwa ya kumhamisha Mobutu, msaidizi binafsi wa Lumumba kabla bosi wake hajamteua kumfanya mnadhimu wa jeshi, kumhamishia kwenda kambi ya Kasavubu. Saa chache baada ya Kasavubu kutangaza kuliahirisha Bunge, Mobutu alitwaa madaraka kwa jina la jeshi.

“Aliahidi ‘kubatilisha’ nyadhifa za Kasavubu, Lumumba, Ileo na wanasiasa wengine hadi mwisho wa mwaka (1960). Aliwaita wanafunzi wa Chuo Kikuu Congo na wahitimu wengine wa vyuo kuendesha serikali. Aliwafukuza mabalozi wa Urusi na Czechoslovakia. Siku chache baadaye wakati CIA ilipomtahadharisha Mobutu juu ya njama za kumuua, Mobutu alibadilika, akaanza kuegemea upande wa Kasavubu aliyefuata matakwa ya nchi za Magharibi.

“Aliwaambia maofisa ubalozi wa Marekani kuwa angemkamata Lumumba na kuweka madaraka mikononi mwa serikali ya Ileo-Kasavubu mwishoni mwa Oktoba. Hata hivyo Mobutu hangeweza kumkamata Lumumba kwa sababu Lumumba alikuwa nyumbani kwake akilindwa na UN. Kwa hiyo, majeshi ya Mobutu walimzuia Lumumba asiondoke kwenye nyumba hiyo.”

Septemba 19 ‘Tume ya Wanavyuo’, ikiwa na wahitimu zaidi ya 30, ikaundwa ili kuendesha serikali ya mpito. Kuanzia hapo kamatakamata ilianza. Kasavubu aliondoka kwenda New York, Marekani kuhudhuria mkutano wa Baraza la Usalama la UN. Huko alitoa hotuba yake Novemba 8 na alitambuliwa kama Rais wa Congo licha ya kwamba Mobutu alijitangaza yuko madarakani na serikali ya mpito.

Novemba 27, 1960, siku ambayo Kasavubu alirejea kutoka New York, alikopeleka malalamiko yake UN na kisha akapokewa kwa shangwe na wanasiasa kadhaa wa Congo, ndiyo siku ambayo Lumumba aliondoka Leopoldville kwenda Stanleyville (Kisangani) kuanzisha upya mapambano ya kisiasa.

Hadi Novemba 27 alikuwa chini ya ulinzi wa UN nyumbani kwake Leopoldville lakini aliruhusiwa kutoka na kurudi nyumbani.

Akiwa nyumbani kwake, Lumumba aliona shamrashamra za mapokezi ya Kasavubu zikiendelea. Waliokuwa wamezingira eneo zilipokuwa zikifanyika shangwe hizo ni askari wa Mobutu.

Lumumba aliona atumie fursa hiyo kutoroka na kwenda Stanleyville ambako Antoine Gizenga, aliyekuwa naibu wake, alikuwa akiwaandaa wapambanaji ili kujipanga upya. Alitoroka kwake bila askari wa Mobutu kugundua.

Baada ya kuona kuwa hangeweza tena kurudi madarakani kwa njia za kawaida, hasa baada ya kurejea kwa Kasavubu kutoka UN, Lumumba aliona njia pekee ya kutwaa madaraka ni kuitwaa Leopoldville akitokea Stanleyville.

Wanasiasa wengine saba waliokuwa tayari kujiunga na Lumumba na waliokuwa kwenye baraza lake la mawaziri ni Christophe Gbenye, Joseph Mbuyi, Maurice Mpolo, Anicet Kashamura, Pierre Mulele na aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu, Barthelemy Mujanay. Msafara wao ulikuwa wa magari matatu, mojawapo liliibeba familia yake.

Baada ya Kasavubu na Mobutu na Wamarekani na Wabelgiji kugundua Lumumba ametoroka na familia yake, walianza kumsaka.

Viongozi wa Leopoldville walinuia kumkamata kwa gharama zozote. Shirika la huduma za kijasusi la kikoloni nchini Congo la Surete, chini ya Victor Nendaka Bika, liliingia kazini kumsaka Lumumba. Mkuu wa CIA Congo, Larry Devlin, na mshauri wa Kasavubu wa masuala ya usalama, Andre Lahaye, walishirikiana kikamilifu na taasisi ya Nendaka.

Ubelgiji walitoa ndege ndogo za kuruka karibu na usawa wa ardhi. Mbelgiji mshauri wa Mobutu, kanali Louis Marliere, alisambaza askari wa kuweka vizuizi barabarani na kwenye mito iliyofikiriwa Lumumba angeweza kupitia.

Mvua iliyokuwa inanyesha na vizuizi vya barabarani vilipunguza kasi ya Lumumba kutoroka. Kilichomchelewesha zaidi ni kusimama karibu kila kijiji alipowaona watu na kuanza kuwahutubia.

Huku akiendelea kusalimiana na watu kila alikopita, inaelekea Novemba 30 waliokuwa wanamtafuta wakiwa angani waliuona msafara wake. Kesho asubuhi, Alhamisi, alipita njia-panda ya mji wa Port Francqui karibu na mpaka wa Leopoldville na Kasai.

Alhamisi ya Desemba mosi, 1960, Patrice Lumumba, alikamatwa na majeshi ya serikali ya Congo baada ya kutoroka. Alikamatiwa eneo la Mweka, Jimbo la Kasai alipokuwa akielekea Stanleyville (sasa Kisangani) baada ya kutoroka Leopoldville (sasa Kinshasa) alikokuwa chini ya ulinzi wa Umoja wa Mataifa (UN), lakini akilindwa na majeshi ya Mobutu.

Ingawa msafara wao ulikuwa na watu kadhaa waliokuwa wakitoroka naye, ni Christophe Gbenye, Anicet Kashamura (aliyekuwa Waziri wa Habari) na Pierre Mulele (Waziri wa Elimu) tu walifanikiwa kumaliza safari yao.

Lumumba, Maurice Mpolo (aliyekuwa Waziri wa Vijana na Michezo) na Joseph Akito (makamu rais wa Baraza la Seneti) walikamatwa na kurejeshwa Kinshasa, lakini Joseph Mbuyi na Barthelemy Mujanay (aliyekuwa Gavana wa Benki Kuuo) waliuawa katika Jimbo la Charlesville.

Siku iliyofuata, wanajeshi 40 walimtoa Lumumba kutoka eneo walilomkamata la Lodi-Mweka na kumsafirisha kwa njia ya barabara hadi uwanja mdogo wa ndege wa Port Francqui ambako alisafirishwa kwa ndege kurudishwa Kinshasa ambapo waliwasili saa 11:00 jioni. Muda wote wakiwa angani, Lumumba na wenzake walikuwa katika mateso makubwa hadi ndege ilipotua na wao kuteremshwa na kupakiwa kwenye lori.

Lumumba alitoroka Kinshasa kwa kutumia gari aina ya Peugeot 403, mali ya mtu aliyeitwa Kamitatu Cleophas na ilikuwa ikiendeshwa na Mungul Diaka.

Johannes Fabian, mwandishi wa kitabu cha “Remembering the Present: Painting and Popular History in Zaire (uk 115)”, anasimulia kuwa Lumumba alikuwa katika gari hiyo ya rangi nyeusi, ingawa mwandishi mwingine, Anna Purna, katika ukurasa wa 285 wa kitabu “Dr. Lumumba’s Dream of Incest”, anasema gari hilo ni Peugeot lakini la rangi nyeupe.

Sehemu ya simulizi ya tukio hilo inasema baada ya kuvuka Mto Sankuru, alirudi kumchukua mkewe Pauline Opango Lumumba, na mtoto wao wa mwisho, Roland, waliokuwa ng’ambo ya mto, na ndipo alipokamatwa.

Wenzake, akiwamo Pierre Mulele, waliovuka mto na Lumumba, walifanikiwa kufika salama Port Francqui Desemba mosi.

Ijumaa, Desemba 2, 1960, muda mfupi kabla ya saa 11:00 jioni, ndege ya Congo DC-3 ilitua uwanja wa ndege wa Ndjili mjini Kinshasa. Ndani yake alikuwamo ofisa usalama wa Congo, Gilbert-Pierre Pongo, Lumumba na wanajeshi.

Pongo ni mmoja wa maofisa usalama wa serikali ya Congo waliomfuatilia Lumumba hadi kumkamata.

Umati wa watu uwanjani hapo ulikuwa ukisubiri kuona wanaoshuka kwenye ndege hiyo. Miongoni mwa waliokuwa kwenye umati huo ni waandishi wa habari, wapigapicha, maofisa wa serikali na wa jeshi la ANC.

Lumumba alikuwa wa pili kushuka, akiwa nyuma ya Pongo ambaye sasa alionekana kama shujaa kwa kuwezesha kukamatwa kwa Lumumba. Mikono ya Lumumba ilifungwa nyuma kwa kamba. Picha zilizopigwa siku hiyo zinamuonyesha alikuwa amevaa shati jeupe.

Lumumba na mateka wengine wawili walisukumwa kuingia kwenye lori kusubiri safari nyingine. Mwandishi wa kitabu cha “The Assassination of Lumumba”, Ludo de Witte anaandika kuwa kwa faida ya wapigapicha, mwanajeshi mmoja alimkamata Lumumba na kunyanyua kichwa chake juu ili apigwe picha.

Kwa mujibu wa kitabu hicho, mwangalizi mmoja wa UN aliyekuwa uwanjani hapo, alisema Lumumba alipoteza miwani yake na shati lake lilitapakaa damu, na kulikuwa na damu iliyovia kwenye shavu lake la kushoto.

Mateka hao walipelekwa kambi ya jeshi ya Binza karibu na makazi ya Mobutu. Waandishi waliokuwa kambini hapo wakati Lumumba anawasili, walisema alikamatwa na kuonyeshwa kwa wapigapicha ili apigwe picha. Wakati huo Mobutu naye alikuwa akiangalia.

Baadaye alitupwa ardhini huku akipigwa na wanajeshi waliomzunguka. Kisha Pongo akapaza sauti kuwataka wanajeshi hao wazidi kumpiga.

Baada ya kumkamata Lumumba, Pongo alipandishwa cheo na kuwa kapteni. Alitumwa kwenda Bukavu, lakini huko alikamatwa.

Januari mosi, 1961, siku 16 kabla Lumumba hajauawa, Pongo alitumwa na Mobutu kuongoza shambulio kwenye mji wa mpakani wa Bukavu, ikiwa ni jaribio la kulirejesha eneo hilo kwenye himaya ya Mobutu. Hata hivyo, alikamatwa na kuwekwa mahabusu katika mji wa Kisangani na mahabusu wengine ambako maofisa walitoa sharti la kumuachia kama Lumumba naye angeachiwa. Lumumba hakuachiwa na hivyo Pongo naye hakuachiwa.

Februari 20, 1961, ikiwa ni siku tatu baada ya Lumumba kuuawa, Pongo na wenzake 14 waliuawa na wafuasi wa Lumumba.

Wakati wakiwa bado wanamshikilia na kumtesa Lumumba, mwanajeshi mmoja alisoma ujumbe ulioandikwa kwenye karatasi ukidaiwa kuwa uliandikwa na Lumumba mwenyewe akidai kuwa yeye ndiye kiongozi halali wa serikali ya Congo.

Baada ya kuusoma ujumbe huo, mwanajeshi mmoja aliichukua karatasi hiyo, akaikunjakunja na kuisukumiza mdomoni mwa Lumumba. Baada ya hapo Lumumba alipelekwa chumba kingine ambako mateso dhidi yake yaliendelea.

Siku hiyo usiku, mkuu wa Idara ya Usalama ya Congo, Victor Nendaka, alimpeleka Lumumba mahabusu. Kwa mujibu wa Alfred Cahen, mwanadiplomasia kijana aliyewasili Congo muda mfupi baada ya Lumumba kushushwa kwenye ndege na ambaye alikuwa rafiki wa karibu wa Nendaka, alisema baadaye Nendaka alimwambia kuwa alimfungia Lumumba kwenye gereji ya aliyekuwa mkuu wa ujasusi katika serikali ya kikoloni, Kanali Frederic Vandewall.

Aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Ubelgiji, Pierre Wigny, alikaririwa akisema Desemba 3 alipokea telegramu kutoka ubalozi wa Ubelgiji mjini Brazzaville.

“Alitendwa kikatili sana usiku wa tarehe 2 kuamkia 3 na makomando waliochoma hata ndevu zake,” unasema ujumbe huo.

Bomboko aliingilia kati kutuliza hasira, lakini hakufaulu. Kwa mujibu wa walioshuhudia, “waliomtesa Lumumba ni watu wakatili sana”.

Justin Marie Bomboko Lokumba ni mwanasiasa wa Congo ambaye hakuaminiwa na Lumumba. Akiwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Congo, alishiriki katika kukamatwa kwa Lumumba.

Ujumbe huo kwa njia ya telegramu ulitumwa na Robert Rithschild akiwa ubalozi wa Ubelgiji mjini Kinshasa. Katika ujumbe mwingine alioutuma Brussels siku hiyo, Rothschild alisema: “Hatua muhimu zinachukuliwa kuhakikisha kuwa Kasavubu anawadhibiti mahabusu.”

Vyombo vya habari vya kimataifa vilipiga picha wakati Lumumba akiadhibiwa na askari wa Congo katika uwanja wa ndege wa Ndjili na kisha kwenye kambi ya Binza.

Balozi wa Marekani nchini Congo, Clare Hayes Timberlake, alituma telegramu kwenda kwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Christian Archibald Herter, akimsihi ajitahidi kuzuia kusambaa picha za mateso ya Lumumba kwa sababu “zinaweza kutengeneza bomu la atomiki”.

Picha hizo zilianza kutia simanzi na hasira maeneo mengi ya dunia ambako zilionekana kwenye vyombo vya habari.

Wanasiasa kadhaa walianza kutilia shaka uwezo wa UN, wakihoji wanawezaje kuwalinda Wabelgiji walioko Congo lakini wanashindwa kumlinda Lumumba anayekubaliwa na Bunge na wabunge wa nchi yake.

Nchi kadhaa za Afrika zilitishia hata kuondoa wanajeshi wao katika jeshi la UN lililokuwa Congo, UNOC.

Hata hivyo UN haikushinikiza Lumumba aachiwe, pamoja na kukiri alikuwa na kinga ya Bunge.

Majeshi ya UN hayakufanya chochote zaidi ya kutazama hali ilivyokuwa inakwenda nchini Congo kuhusu Lumumba.

Pamoja na kwamba majeshi ya Umoja wa Mataifa yalikuwa Congo kulinda usalama, hayakuingilia kati kwa muda wote ambao Patrice Lumumba alikuwa akiteswa. Huenda hii ni kwa sababu Ubelgiji na Marekani hazikumtaka Lumumba. Akiwa mahabusu alifanikiwa kuandika barua mbili kwa msaada wa wanajeshi waliokuwa wakimtii. Endelea…

Jumamosi ya Desemba 3, Patrice Lumumba alihamishwa na wanajeshi na kupelekwa kambi ya Hardy iliyoko Thysville. Kwa mujibu wa waandishi wa habari waliokuwapo wakati wa kuhamishwa huko, Lumumba alionekana kuwa na maumivu makali kiasi kwamba alipata shida kupanda lori, na uso wake ulikuwa na alama za vipigo.

Kambi hiyo ilikuwa chini ya Kanali Louis Bobozo. Bobozo, ambaye ni mpwa wa Mobutu, baadaye akawa mkuu wa majeshi ya Congo kuanzia 1965 hadi 1972. Alikuwa ni sajenti tu wakati Congo ikipatia uhuru lakini alipandishwa vyeo haraka.

Katika kambi hiyo kulikuwa na mahabusu wengine wa kisiasa, mmoja wao ni Georges Grenfell ambaye alikuwa waziri katika serikali ya Lumumba.

Aliyekuwa mwakilishi wa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN) nchini Congo, Balozi Rajeshwar Dayal, aliandika kuhusu hali ya Lumumba. “Inasemekana ana maumivu makali yanayotokana na majeraha aliyopata alipowasili. Kichwa kimenyolewa nywele na bado mikono yake imefungwa kwa nyuma. Amefungiwa kwenye mahabusu ambayo haina hadhi ya utu na ni hatari sana kwa afya,” aliandika.

Telegramu ambayo Dayal alimtumia katibu mkuu wa UN, Dag Hammarskjold Desemba 5, iliripoti mazungumzo yaliyofanyika.

“Wanajeshi wa Morocco walioko UN Congo kambi ya Thysville wameripoti kuwapo majadiliano makali kati ya ANC (Jeshi la Congo) kuhusu wanavyomtendea Lumumba. Mabishano hayajatulia,” alisema.

Desemba 22, Dayal alituma ujumbe mwingine kwenda UN ukisema: “Uhalifu unaoendelezwa kwa Lumumba umeanza kuwakera (Kasavubu na Mobutu) kwa sababu umeanza kuwagawa wanajeshi.”

Januari 4, 1961, zikiwa ni siku 13 kabla ya kifo chake, Lumumba alifanikiwa kupenyeza barua mbili kutoka rumande. Ya kwanza ilikuwa ni ujumbe kwa viongozi wa UN, ambayo alieleza hali halisi ya mahabusu ya Camp Hardy.

“Niko hapa na wengine saba waliokuwa wabunge, miongoni mwao ni rais wa seneti, M. Okito (akimaanisha Joseph Okito) mfanyakazi wa serikali na dereva. Jumla yetu tuko 10. Tumewekwa hapa tangu Desemba 2, 1960. Chakula tunacholetewa mara mbili kwa siku ni kibaya sana,” aliandika Lumumba.

“Kwa siku nne sijala zaidi ya ndizi. Nimemweleza daktari wa Msalaba Mwekundu aliyeletwa kuniona; kanali wa Thysville alikuwapo. Nimetaka niletewe matunda ... Ingawa daktari aliruhusu, wanajeshi wa hapa wamekataa wakisema wana amri kutoka juu, kwa Kanali Mobutu.

“Madaktari wameelekeza tutembee [mazoezi] kila jioni nje ya mahabusu, lakini kanali na mkuu wa wilaya wamekataa. Nguo nilizovaa kwa siku 35 hazijaoshwa. Nimezuiwa kuvaa viatu. Kwa ufupi tunaishi katika hali isiyovumilika. Zaidi, sijapata taarifa zozote za mke wangu na familia yangu na sijui waliko. Nilipaswa nitembelewe naye, kama ilivyo katika sheria za Congo.”

Katika barua ya pili aliyomtumia mpwa wake aliyeitwa Albert Onawelo, Lumumba alitoa maelezo ya ziada kuhusu hali yake, pia akaelezea msaada fulani alioupata kutoka kwa baadhi ya wanajeshi.

“Niko hapa na wasaidizi saba, mmoja wao ni Joseph Okito. Tumefungiwa mahabusu gizani mfululizo tangu Desemba 2, 1960. Chakula tunachopewa (chikwangue na wali) unakera na ni kichafu na naweza kukaa siku tatu hadi nne bila kula. Kwa kweli hali ni mbaya kuliko hata wakati wa ukoloni. Kama akitokea askari akatupa ndizi za ziada, anakamatwa na kuadhibiwa. Pamoja na tabu zote kuna baadhi ya wanajeshi wanakuja kwa siri kunisaidia,” aliandika.

Mwisho wa barua hiyo, Lumumba alionyesha pia kuhusu mke wake wa tatu, Pauline Kie “anaendelea vizuri na hufika kila mara na kuwaachia ujumbe (wa Lumumba) wanajeshi walio upande wetu”.

Mwanzoni mwa Januari 1961, katibu mkuu wa UN, Dag Hammarskjold alizuru Congo na kujikuta akipokewa kwa maandamano ya wafuasi wa Lumumba.

Wakati mwanaharakati Cleophas Kamitatu alipojaribu kumpa Hammarskjold barua kutoka kwa Lumumba iliyoelezea hali katika mahabusu walimoshikiliwa, alionyesha kukasirika na kumwelekeza ampatie msaidizi wake.

Kamitatu, kwa kukasirishwa na majibu aliyopewa na Hammarskjold, naye aliandika barua yake yenye maneno yanayofanana na yale ya Lumumba.

“M. Lumumba amekuwa akiteswa kikatili kwa siku 35. Kwa siku zote hizo ameruhusiwa kuoga mara tatu tu. Anapewa chakula kinachostahili kupewa mbwa... Nguo alizovaa zimekaa mwilini kwa siku 35. Anaishi shimoni. Hakuwahi kufikishwa mahakamani, na hata mkewe amezuiwa kumwona,” aliandika.

Ingawa barua hizo ziliwafikia maofisa wa UN nchini Congo, hawakuchukua hatua yoyote kurekebisha hali ya mambo.

Hali ya wasiwasi ilikuwa ikizidi kutanda katika kambi aliyowekwa Lumumba na wenzake. Msaidizi wa Kanali Bobozo, Luteni Jacques Schoonbroot, alikuwa anasisitiza kuwa ghasia zinazozuka zinasababishwa na itikadi za kisiasa na kwamba kulikuwa na kikundi cha wanajeshi wa Congo katika kambi hiyo kilichomtii Lumumba.

Jumanne, Desemba 27 Kanali Bobozo aliarifiwa na msiri wake kuwa huenda Lumumba angetoroka au kutoroshwa. Aliamua mwenyewe kwenda kumfungia Lumumba na kuondoka na funguo.

Siku hiyo usiku alikwenda tena mwenyewe mahabusu alimofungiwa Lumumba kuwazuia makumi ya wanajeshi waliokuwa wamepanga kumtoa.

Kwa mujibu wa Luteni Schoonbroot kama alivyokaririwa na kitabu cha “Assassination of Lumumba”, Kanali Bobozo aliwaambia wanajeshi hao akisema “nyiye hamna la kufanya. Kama mnataka kumuachia mfungwa yeyote, labda muanze kwanza kuniua mimi.” Baada ya kauli hiyo, wanajeshi hao walianza kuondoka mmoja baada ya mwingine.

Siku iliyofuata walikamatwa baadhi ya wanajeshi kutokana na jaribio lao la kumtoa Lumumba mahabusu. Baadaye ukazuka uvumi kwamba Lumumba alikuwa anatendwa vizuri mahabusu na alikula sikukuu ya Krismasi na maofisa wa kambi hiyo.

Luis Lopez Alvarez, raia wa Hispania aliyekuwa rafiki wa karibu na Lumumba, alikaririwa na Stephen Weissman katika kitabu cha “American Foreign Policy in the Congo 1960-1964”, akisema Lumumba alimlaumu sana balozi wa Marekani Congo kwa kuonekana kukaa upande wa watesi wake.

Wakati hayo yakiendelea, serikali ya Ubelgiji ilikuwa na hofu sana na Lumumba kiasi kwamba ilituma ujumbe wa telegramu kwenda Kinshasa ikiwasisitiza “watilie maanani hatari ambayo ingesababishwa na Lumumba ikiwa ataachiwa huru”. Siku iliyofuata ukatumwa ujumbe kwa njia ya telegramu kutoka Congo kwenda Ubelgiji ukisema serikali ya Mobutu isingeruhusu Lumumba kuachiwa huru.

Muda mfupi baadaye, maofisa wa Congo mjini Kinshasa walianza kutafuta namna ya kumpoteza kabisa Lumumba.

Jumapili ya Januari 8, 1961, wanasiasa wawili wa Congo; Albert Delvaux na Cyrille Adoula walikwenda Katanga kuzungumza na rais wa eneo hilo, Moise Tshombe, kuhusu kumhamishia Lumumba huko.

Siku iliyofuata, wanasiasa wa Congo walishauriana na Rais Joseph Kasavubu na mkuu wa majeshi, kumhamisha Lumumba. Kamishna wa Ulinzi wa Congo, Fredinand Kazadi alisema kuhamishwa kwa Lumumba ni kwa muhimu sana ili kuepusha machafuko yaliyokuwa yananukia Thysville.

Siku iliyofuata, kamishna wa mambo ya ndani, Damien Kandolo, aliondoka kwenda Boma kwa ajili ya maandalizi hayo. Ubelgiji ilikuwa ikifuatilia kwa karibu hatua zote hizi.

Kulingana na simulizi za G. Heinz na H. Donnay katika kitabu cha “Lumumba: The Last Fifty Days”, aliyekuwa kiungo kati ya watesi wa Lumumba na serikali ya Ubelgiji ni Andre Lahaye, Mbelgiji aliyekuwa mshauri mkubwa wa mkuu wa Idara ya Usalama ya Congo, Victor Nendaka.

Aliyesaini barua ya kumtaka Nendaka amtoe Lumumba Thysville na kumpeleka Katanga ni Rais Kasavubu. Mpango wa usafiri wa ndege uliandaliwa na Kandolo Damien.

Kuanzia hapo Lahaye alifanya kazi kubwa akituma taarifa za mara kwa mara na hatua kwa hatua kwenda Brussels kwa lengo la kuelezea namna Lumumba alivyokuwa anashughulikiwa.

Wakati Lumumba akiwa bado mikononi mwa watesi wake, Rais Kasavubu wa Congo alikuwa kwenye shinikizo kali kuhusu hatima ya Lumumba.

Kwa kuona hivyo, Januari 2, 1961, Kasavubu aliitisha mkutano ambao ungewajumuisha wanasiasa mbalimbali wa Congo. Pia wanasiasa wa Afrika na Asia waliokuwa wafuasi na watetezi wa Lumumba, walikuwa wanakutana Casablanca wakitaka aachiwe mara moja.

Kuongezea uzito wa hilo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Dag Hammarskjold alipanga kurudi tena Congo Januari 10. Viongozi wa kisiasa wa Congo waliogopa kwamba kama wangemwachia huru Lumumba, huenda UN wangeshinikiza arudi madarakani.

Mapema asubuhi ya Januari 13, nidhamu katika kambi ya Camp Hardy ilianza kutoweka. Wanajeshi wa kambi hiyo walikataa kupokea amri yoyote kutoka kwa wakubwa zao hadi walipwe stahiki zao, baadhi yao wakitaka Lumumba aachiwe huru.

Baadaye siku hiyo hali ilivyozidi kuwa mbaya Kasavubu, Mobutu, Bomboko na Nendaka waliitana na haraka kuelekea kambini kujadiliana na wanajeshi hao.

Baadaye ukazuka uvumi kwamba Januari 14, Lumumba angekuwa huru na hivyo wanajeshi wanaomtii waliokuwa Katanga wangekuwa njiani kuelekea Kinshasa.

Wanajeshi waliokuwa Katanga tayari walishateka eneo lote la kaskazini hata kabla machafuko ya Thysville. Viongozi walishahamishia familia zao Brussels, Ubelgiji.

Januari 13, mkuu wa Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA) nchini Congo, Lawrence Raymond Devlin, alituma ujumbe Marekani akisema serikali ya Congo inaweza kuanguka wakati wowote na kama Marekani hawatachukua hatua za haraka, maslahi yake nchini humo yatakuwa hatarini. Nchini Ubelgiji, mikutano ya haraka ilifanyika kuhusu hali ya kisiasa ya nchi hiyo.

Mwandishi wa habari, Kwame Afadzi Insaidoo katika ukurasa wa sita wa kitabu chake cha “Ghana: A Time to Heal & Renew the Nation” amelikariri jarida la The Economist la Februari 24-Machi 2, 2007, Vol. 382, No. 8517, ukurasa wa 95, kuhusu maendeleo ya hali nchini Congo.

“Bw. (Larry) Devlin alikula njama na mkuu wa jeshi la nchi, Joseph Mobutu, ambaye ni sajini aliyepandishwa cheo hivi karibuni, kumkamata Waziri Mkuu (Lumumba),” ameandika akinukuu jarida hilo.

Wakati Lumumba alipozidi kusababisha matatizo na nchi ikatumbukia kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe, Rais Dwight Eisenhower (wa Marekani) alitoa amri ya kumuua Lumumba, kwa mujibu wa Bw. Devlin.

Kwa mujibu wa kitabu “Betrayal of Trust: The Collapse of Global Public Health” cha Laurie Garrett, uamuzi wa Marekani kumuua Lumumba ulikuja baada ya mawasiliano ya mara kwa mara kati ya mkurugenzi mkuu wa CIA, Allen Dulles na mkuu wake katika kituo cha Congo, Larry Devlin.

Katika taarifa moja ya telegramu iliyotumwa Marekani, Devlin aliripoti kuwa “kuna jitihada za kuifanya Congo kuwa ya kikomunisti”.

Katika mkutano wa Baraza la Usalama wa Taifa la Marekani, ilitengenezwa mipango ya kuivuruga Congo kwa kutengeneza ghasia za mara kwa mara kiasi cha Lumumba kushindwa kutawala.

Kubwa zaidi lililofanyika ni kupandikiza mgogoro wa uongozi ambao hatimaye ulimfanya Lumumba kupoteza cheo chake.

Ghasia zilikuwa za mara kwa mara katika miji mingi ya Congo. Ghasia za Camp Hardy ziliwasukuma maofisa wa Congo kumhamishia Lumumba sehemu nyingine. Baadhi ya wanasiasa wa Katanga, Kasai na Kinshasa walihakikisha wanazuia njia zozote za kumwachia Lumumba.

Mipango ya kumtoa Lumumba mjini Kinshasa kwenda Katanga ilikamilika. Jimbo la Katanga lilikuwa linaongozwa na mmoja wa mahasimu wake kisiasa, Moise Tshombe.

Walioongoza kikao cha mipango ya kumhamisha ni Kandolo Damien na Andre Lahaye, Mbelgiji aliyekuwa mshauri mkubwa wa mkuu wa Idara ya Usalama Congo, Victor Nendaka.

Nendaka alikuwa ofisini kwake mjini Kinshasa wakati Kandolo alipomwendea akiwa na waraka ulioonyesha ratiba ya ndege itakayotumika. Andre Lahaye naye alikwenda ofisini kwa Nendaka alikokutana tena na Kandolo.

Kabla ya hapo, Jumanne ya Desemba 6, 1960, Kanali Joseph Mobutu aliitisha mkutano na waandishi wa habari na kuwaambia kuwa Lumumba yuko katika mikono salama.

Aliwaonyesha waandishi hao kile alichosema kuwa ni cheti cha daktari kinachoonyesha kuwa Lumumba yuko katika hali njema sana kiafya.

Aliwaambia Lumumba atashtakiwa kwa kosa la kusababisha ghasia katika jeshi na kuwatesa baadhi ya wabunge. Mobutu hakutaja tarehe ambayo Lumumba angeshtakiwa.

Januari 16, mkuu wa kikosi cha usalama, Victor Nendaka Bika, alikutana na wanasiasa wa Congo katika ofisi za Shirika la Ndege la Ubelgiji, Sabena, na kupanga kuwa watamhamisha Lumumba kutoka Bakwanga na kumpeleka Elizabethville.

Operesheni hiyo ingefanyika jioni. Hiyo ilikuwa ni siku moja kabla ya mauaji ya Lumumba. Wanasiasa wawili Fernand Kazadi na Jonas Mukamba walitakiwa washiriki kumsafirisha Lumumba.

Kushikiliwa kwa Lumumba kulianza kuitisha Ubelgiji tangu siku ile majeshi ya Mobutu yalipozingira makazi yake. Uvumi ulisambaa kwamba jimbo la Katanga lilitaka kubadilishana wafungwa na Kinshasa na kwamba Lumumba angekuwemo.

Uliposambaa sana uvumi huo, Waziri wa Mambo ya Afrika nchini Ubelgiji, Harold d’Aspremont Lynden aliwasiliana na maofisa wa serikali yake waliokuwa Congo akiwataka wazuie mazungumzo hayo.

Jumapili ya Januari 14, msiri na mtu wa karibu na Lynden aliyejulikana kwa jina la Meja Jules Loos, na ambaye ni mmoja wa walioshiriki njama za kumuua Lumumba, kwa mujibu wa kitabu “Patrice Lumumba, Ahead of His Time” cha Didier Ndongala Mumbata, alimpelekea Lynden mbinu nyingine za “kumalizana na Lumumba”.

Hiyo ni baada ya kukerwa na magazeti ya Congo kuhusu maasi ya kijeshi ya Thysville ambako Lumumba alikuwa anashikiliwa.

Loos alimshauri Luteni Kanali Louis Marliere, ofisa wa kijeshi wa Ubelgiji nchini Congo kumpeleka Lumumba Katanga kwa hasimu wake, Moise Tshombe.

Lynden alituma ujumbe wa siri kwa Luteni Kanali Marliere na Meja Loos akiwataka wahakikishe Lumumba anaondolewa na wampeleke sehemu nyingine ya siri, lakini yenye ulinzi mkali zaidi.

Januari 16 alimtumia Tshombe ujumbe akimsihi amchukue Lumumba na amshikilie huko Katanga. Hata hivyo ujumbe huo ulifika jioni wakati Tshombe alishafanya uamuzi wake.

Mipango ya kumpeleka Lumumba Katanga iliandaliwa Kinshasa. Tshombe alikubaliana nayo. Mmoja wa maofisa wa serikali aliyeidhinisha kuhamishwa kwa Lumumba na kupelekwa Katanga ni Albert Delvaux, ambaye awali alikuwa waziri wa Lumumba kabla ya mgogoro wa uongozi na alikuwa pia ni mmoja wa maofisa wa Kasavubu waliosaini kuondolewa kwa Lumumba na Justin Marie Bomboko mwaka 1960.

Baadaye Delvaux alikuwa waziri katika baraza la mawaziri la Joseph Ileo ambaye alikuja kuwa Waziri Mkuu wa Congo.

Katika kipindi chote cha mwanzoni mwa Januari 1961, Delvaux alikuwa na harakati nyingi za kuwaweka pamoja akina Kasavubu, Tshombe na Mobutu kuhusu suala zima la Lumumba.

Asubuhi ya Januari 16, wakati mshauri wa Kasavubu wa masuala ya usalama, Andre Lahaye na mkuu wa shirika la huduma za kijasusi la kikoloni, Victor Nendaka, wakijadiliana namna ya kumsafirisha Lumumba kumpeleka Katanga, aliyekuwa akisimamia mawasiliano baina ya Tshombe na Kasavubu ni Delvaux.

Hatimaye jioni ya Jumatatu ya Januari 16, muda mfupi baada ya tafakuri na majadiliano mengi, Nendaka alipanda ndege kuelekea mjini Thysville (sasa ni Mbanza-Ngungu) alikokuwa anashikiliwa Lumumba. Usiku wa siku hiyo alilala katika hoteli mojawapo ya mji huo.

Januari 17, 1961, Lumumba na mahabusu wenzake wawili, yani Waziri wa Vijana, Mourice Mpolo na Makamu wa Rais wa Seneti, Joseph Okito, ambao walikamatwa pamoja wakiwa njiani kutorokea Stanleyville, awalichukuliwa kutoka Kambi ya kijeshi ya Thysville iliyopo Jimboni Kasai na Mkuu wa Usalama wa Mobutu, Victor Nendaka, akifuatana na askari watatu wa kabila la Baluba na kupelekwa uwanja wa ndege wa Moanda, Lumumba alipo wasili uwanjani, walikaribishwa kwa vipigo vizito kutoka kwa askari wa Kibelgiji na Katanga, kisha kutupwa nyuma ya gari kupelekwa kwenye nyumba pweke, maili mbili kutoka hapo, nyumba iliyolindwa na majeshi ya Kibelgiji na Polisi chini ya Afisa wa Kibelgiji.

Hapo tena, Tshombe na mawaziri wake walishiriki kumpiga na kumtesa kinyama bafuni, kisha watesi hao wakatoka wametapakaa damu mwilini, Huku wakiwa wamelewa chakali, walitangaza Lumumba “auwawe mara moja”.

Ilipo fika usiku wa saa 4:00, tarehe hiyo hiyo 17/1/1961 Lumumba na wenzake wawili walichukuliwa kwa gari hadi kwenye vichaka, maili 30 toka Thysville, Tshombe akiongoza msafara, akiwamo pia Kamishna wa Polisi wa Kibelgiji, Frans Verscheure na walengaji shabaha kutoka Marekani.

Walipofikishwa eneo lililokusudiwa wakapekuliwa, wakiwa wamevaa kaptura na fulana tu, walianza kuuwawa, Huku Lumumba alikuwa wa mwisho kuuawa kwa kupigwa risasi na kikosi cha Askari wenye shabaha na kisha kuzikwa huko huko porini, Kesho yake ya tarahe 18/1/1961 serikali ya Moise Tchombe ikatangaza habari za uongo kwamba Lumumba na wenzake waliuawa na wanavijiji wenye hasira walipokuwa wakijaribu kutoroka kizuizini.

kwa kuhofia kuvuja kwa taarifa za unyama walio fanya, Usiku uliofuata, askali hao wa Uberigiji walikwenda kufukua miili ya Lumumba na wenzake, baada ya kufukuliwa ilisafirishwa hadi Kasenga, maili 120 Kaskazini Mashariki mwa Elizabethville, ambako ilikatwakatwa vipande vipande na kutupwa kwenye pipa la tindikali (Sulphuri acid), na kuyeyuka, mafuvu yao yakasagwa unga, mifupa na meno yakatupwa kwa kutawanywa porini wakati wauaji walipokuwa wakirejea Elizabethville, Asubuhi ya tarehe 20/1/1961, jasusi Larry Devlin aliitaarifu Washington DC kwa code kuwa "Mission 009321 operation Barracuda is over".

Kule Washington mtu wa kwanza kupata taarifa juu ya kukamilika kwa operation barracuda alikuwa Waziri wa kigeni Jonh Dulles, haraka akamtaalifu mkurugenzi wa CIA, Allan Dulles, na baadae taarifa zikamfikia rais Dwight Eisenhower, Wakati huo Dwight Eisenhower ndio alikuwa anakwenda kumaliza muhura wake wa mwisho madarakani.

Hata rais aliye mfuata wa 35 Jonh F Kennedy aliendeleza kulinda masrahi ya Marekani nchini Kongo kupitia Shirika lake la Ujasusi la CIA, liliendelea kuhakikisha na kudhibiti nyendo za watawala wa Kongo ili wasije kuegemea upande wa Ukomunisti, Kwa kuthibitisha hili mwandishi Martin Meredith Kwenye kitabu chake cha "The State Of Africa, ameandika, kuwa "Mobutu kwenye safari yake ya kwanza Washington, Mei, 1963, akiwa Mkuu wa Majeshi kwenye Serikali ya Joseph Kasavubu, Rais wa Marekani, John Kennedy alimtamkia Mobutu, "Jenerali, isingelikuwa wewe, Ukomunisti ungetamalaki Kongo", huku Mobutu akimjibu, "Ninafanya niwezalo mheshimiwa raisi".

Martin Meredith kwenye kitabu chake cha "The State Of Africa" ameandika "After operation barracuda completed and his coup in 1965, Mobutu remained on the CIA's payroll for sometime and received regular briefings from Larry Devlin , the CIA station chief in Leopoldville." ( Meredith, State Of Africa, pg 294).

Baada ya "operation Barracuda" kukamilika na Lumumba kuuwawa, hatimae tarehe 21 January 1961, Kasavubu alimteua Mobutu kuwa mkuu wa majeshi ya Kongo, na miezi kadhaa iliyofuata Cyrille Adoula akachaguliwa kuwa Waziri mkuu, Kwa kipindi hiko chote.

Kulikua na mapambano yaliyokuwa yakiendelea kati ya majeshi ya Mobutu wakishirikiana na vikosi vya UN dhidi ya wapiganaji wa Serikali ya Antone Gizenga na yale ya katanga iliyoongozwa na Moise Tshombe, majeshi ya Moise Tshombe yalishindwa nguvu na Tchombe mwenyewe kukimbilia Northern Rhodesia (Zambia kwa sasa) na baadae Uhispania, Lakini mwaka 1964, Tshombe aliitwa kurudi nchini, ambapo Kasavubu alimteua kuwa waziri Mkuu.

Katika kipindi chake cha uwaziri mkuu Tchombe, alikabiliwa na machafuko kutoka kwa waasi, wakiongozwa na bwana Pierre Mulele na Gizenga, Huyu Pierre Mulele alikuwa mfuasi wa Patrice Lumumba, na aliongoza mapambano dhidi ya serikali kwa lengo la kutaka kumuondosha madarakani Rais Kasavubu, Mapigano yaliendelea kwa muda mrefu sana kati ya wapiganaji wa Mulele na majeshi ya serikali yakishirikiana na majeshi ya UN, Mwisho wa siku Mulele alizidiwa nguvu na kukimbilia nchini Congo-brazzaville.

Ndimi: Comred Mbwana Allyamtu
Copyrights of this article reserved
written by Comred Mbwana Allyamtu

•Napatika Kwa mawasliano
Comred Mbwana Allyamtu
+255679555526 (WhatsApp).
+255765026057.
Email- mbwanaallyamtu990@gmail.com

Copyright 2022, All Rights Reserved.
View attachment 2280287View attachment 2280289View attachment 2280290View attachment 2280288View attachment 2280292View attachment 2280291View attachment 2280293View attachment 2280294View attachment 2280295View attachment 2280296View attachment 2280300View attachment 2280297View attachment 2280301View attachment 2280298View attachment 2280299View attachment 2280302View attachment 2280304View attachment 2280303View attachment 2280306View attachment 2280307View attachment 2280309View attachment 2280310View attachment 2280308View attachment 2280312View attachment 2280311View attachment 2280313View attachment 2280314
Stori nzur sn,ila ningependa kujua huyu Mobutu aliupataje uarais kutoka kwa Kasavubu
 
Kiukweli nimesoma mwanzo hadi mwisho,umefanya vizuri katika udadavuzi wako kuhusu mwenendo mzima wa utawala na masahibu yaliyomkuta Patrice Lumumba,chembe ambayo bado inaitesa bara la Afrika kwa kusaliti wananchi wake na rasilimali za nchi kwa tamaa za madaraka.bara la Afrika tutaendelea kutafunwa na dhambi hiyo kizazi hadi kizazi.
 
Kaz nzuri mleta mada

Naomba kuuliza baada ya mobutu kuwatimua kasavubu na lumumba alikasimu madaraka na baadae kasavubu akarud Kama rais na mobutu akawa mkuu wa majeshi

Je mobutu aliupataje urais wa nchi? Kwa kula (demokrasia) au alimpindua kasavubu?
Alipindua serikali yq Joseph kasa-vubu kwa msaada mabeberu
 
Alipindua serikali yq Joseph kasa-vubu kwa msaada mabeberu
Alipata misaada ya mabeberu kwa sababu Mobutu alikuwa kwenye payroll ya shirika la Ujasusi la marekani CIA
hata hivyo na yeye alivokuwa anatandikwa na Joseph Kabila senior mabeberu hao hao walimgeuka hawakumpa msaada wowote.
Marekani ni nchi ya kinafiki sana
 
Very touching story ahsante sana.Huwa najiwa na wazo tu lakini kama binadamu wengine vita vya Congo ni zimwi la Lumumba bado linawatafuna.
Kingine nilichojifunza UN ni chombo cha kinafiki kisicho na msaada na ndio maana Congo wameamua waondoke pia hicho chombo Marekani anajiona yeye kama kiranja mkuu inakuwaje chombo ni cha kimataifa wakashindwa kukomesha mauaji ya Lumumba.
Mnajua ni kwanini Marekani walifanya juu chini kuhakikisha anaangamizwa Lumumba?
Ni sababu ya utajiri wa madini wa Congo ukizingatia bomu waliloshusha la Atomic Japan madini ya Uranium yalitokea Congo hivyo walijua Ukomunist ukiingia Congo warusi wakiwepo ni kiama chao.
Jamaa alikufa kifo cha mateso ya hali ya Juu sana.
Raisi Kennedy raisi aliyefuata wa Marekani alifurahia kifo cha Lumumba na yeye akatwangwa riasi
Kitu nilichojifunza kwenye siasa usimuamini mtu wako wa karibu hayo ndio yalitokea kwa Thomas Sankara,na Milton Obote kwa Iddi Amini.
 
Back
Top Bottom