vukani
JF-Expert Member
- Dec 30, 2009
- 245
- 165
Hivi karibuni nilitoka kwenda kumtembelea rafiki yangu mmoja anayeishi maeneo ya Msasani. Eneo la Msasani ni eneo ambalo sijui nisemeje, lakini ni eneo ambalo linaishi watu wenye vipato tofauti tofauti, kuanzia wale wenye vipato vikubwa na wale wenye hali duni kabisa na maisha yanasonga mbele kama kawaida.
Nilifika kwa rafiki yangu majira ya saa kumi jioni, kwani anaishi eneo ambalo lina pilikapilika nyingi sana. Nilipofika nilimkuta amekaa kibarazani kwao akijisiomea novel zake. Alinikaribisha kwa bashasha na tukaanza kukumbushana stori zetu za zamani na vituko tulivyokuwa tukivifanya enzi zetu za shule.
Mnajua maisha ya shule huwa yana mambo mengi ya kukumbukwa maana ndipo mahali ambapo kuna kila aina ya ujinga, na werevu kidogo. Wakati tukiendelea kupiga soga, nilishangaa kuona kundi la wanaume wakiwemo wazee na vijana wakiwa wameizunguka meza upande wa pili wa barabara huku kila mmoja akiwa na kibakuli chake. Kulikuwa na vitu Fulani wanaokota juu ya meza na vijiti yaani tooth picks na kula huku wakiteremshia na kinywaji kilichopo ndani ya vibakuli vyao.
Nilijishikwa na udadisi, ikabidi nimuulize shoga yangu, kuwa ni kitu gani kinaendelea pale, shoga yangu linijuza kuwa mahali pale ni maarufu kwa uuzwaji wa supu ya pweza. Shoga yangu hakuishia hapo aliendelea kubainisha kuwa supu ya pweza imeibuka na kuwa maarufu siku za hivi karibuni hususana kwa vijana kwa kuwa inasemekana kuwa inaongeza nguvu za kiume.
Kwangu mimi hiyo ilikuwa ni habari mpya, nafahamu kuwa hapa jijini hasa maeneo ya Kariokoo ni kawaida kukuta vijana wakiwa wamebeba masinia yakiwa yamesheheni vipande vya pweza, ngisi na chachandu, wakitembeza mtaani, lakini hili la supu ya pweza sikulifahamu.
Nilimuuliza shoga yangu kama ninaweza kwenda mahali pale ili kupata habari zaidi, shoga yangu huyu kwa bahati nzuri anajua kuwa mimi ni mdadisi, na hakusita kunitania, "He nawe, najua hapo ushapata umbeya wa kuweka mtandaoni"
"Habari ndiyo hiyo shoga yangu hivi hapa nimeshapata udaku" nilimjibu.
Tulivuka barabara na kufika mahali pale, "Shifeya, ( Sio jina lake halisi) tunaona umetuletea mgeni hapa, karibu dada" alitudaka yule kaka muuzaji wa supu. Tulipofika pale tulikuta anazo chupa za chai kubwa maarufu kama thermos chini ya meza yake, ambazo nilijulishwa na mwenyeji wangu kuwa ndizo anazotumia kuhifadhia supu hiyo ya pweza.
Wale vijana na baadhi ya wazee tuliowakuta pale walionekana kufurahiya uwepo wetu pale na nilikaribishwa nijipatie vipande vya pweza na supu. Niliwashukuru kwa ukarimu wao na kuwaambia kuwa kwa bahati mbaya situmii pweza kwa kuwa nina mzio {Allergy} nao.
Kama kawaida nilifanya udadisi wangu, kwa yule kijana muzaji wa supu, kutaka kujua sababu supu ile ya pweza kupata umaarufu siku hizi tofauti na zamani,
"Unajua dada, supu ya pweza inafaida nyingi sana, kwanza ni kiburudisho, pili inaondoa uchovu, inachangamsha na pia…….si unajua yale mambo yetu yaleeee,"
"Mambo gani sasa, mbona humalizii" nilifanya udadisi,
"Weweee sasa unamficha nini kwani ni mtoto mdogo huyo?" alidakia kijana mwingine pembeni aliyekuwa na bakuli lake la supu. "Unajua sister supu ya pweza, pamoja na hizo faida alizokueleza, lakini faida kubwa kabisa ni kwamba inaongeza nguvu za kiume, yaani kama mwanaume anapata supu hii ya pweza halafu akutane na mwanamke, weee inakuwa ni shughuli pevu." Watu waliokuwa pale wote waliangua vicheko.
"Mweleze huyo akamjulishe shemeji, maana kama hayajua mambo haya, basi akiyajua itakuwa kazi kweli kweli"
"Tokeni zenu kule kwanza ninyi watu wa bara ndio mliosababisha mpaka pweza wamepanda bei siku hizi, kwani zamani pweza hakuwa ghali kiasi hiki lakini tangu mufahamu kuwa inafaa kwa majamboz, imekuwa taabu mpaka wamepanda bei" alisema mzee mmoja.
Mara akadakia kijana mwingine, "Huo sasa ni uongo, pweza wamepanda bei kutokana na kuenea kwa mahoteli na mighahawa ya kitalii hapa jijini, na ndio maana wakapanda bei"
Basi yalizuka malumbano mpaka nikashindwa nimsikilize nani na nimuache nani. Nilitoa ofa ya kuwanunulia chupa nzima ya chai iliyojaa supu ya pweza na kujiondokea zangu.
Hata hivyo kupitia malumbano yao nilikuja kufahamu kuwa mpaka miaka ya tisini supu ya pweza haikuwa maarufu kiasi hiki, lakini kutokana na hiyo sifa ya kuongeza nguvu za kiume, imetokea kuwa maarufu miaka ya 2000 na kuwafanya pweza kuwa ghali.
Yule kijana muuuza pweza alinijuza kuwa inamlazimu kwenda hadi Bagamoyo kuwafuatilia pweza kule, kwani hapa Ferry jijini Dar Pweza wamekuwa ni ghali mno kutokana na kupata umaarufu na pia kutokana na watu wa mahoteli na mighahawa ya kitalii kuwanunua kwa bei ya ghali.
Kule Bgamoyo napo hawakuwa ghali sana, lakini siku za karibuni wamekuwa ghali sana kutokana na wafanyabiashara wengi wa supu ya pweza jijini Dar kukimbilia kule kuwatafuta.
Sijafanya utafiti wa kina juu ya madai haya, hivyo msije mkaniuliza kama nina ushahidi na madai hayo.
Kama yupo mwenye changamoto juu ya mada hii anakaribishwa kwani mimi ni msimuliwaji tu.