Baadhi ya Watu waliotoa ripoti za kuibiwa simu katika vituo vya Polisi Stakishari Ukonga Jijini Dar es Salaam na katika Kituo cha Kilwa Roads Police wanasema kila wanapofuatilia simu zao zilizoripotiwa kuibiwa huzikuta kwa watu ambao wamezinunua kutoka kwa watu waliopewa simu hizo na maafande.
Baadhi ya Simu zinazoripotiwa kupotea hazipatikani au aliyeibiwa huzungushwa hadi kufikia hatua ya kukata tamaa na kuacha kufuatilia kutokanana na usumbufu.
Lakini kiuhalisia baadhi ya askari hufuatilia kwa urahisi kabisa simu hizi na kuzipata na baadaye huziuza kupitia mnyororo wa watu wa katikati ili wasiweze kujulikana.
WIZI WA SIMU
Wizi wa simu si jambo geni kwa Dar es Salaam lakini uwepo wa usajili wa kadi za simu na maendeleo ya teknolojia kulileta matumaini ya kwamba sasa wizi huo utapungua, kwani aliyebiwa simu ataweza kuifuatilia simu yake kupitia IMEI Namba au Application maalumu.
USHUHUDA
Mmoja wa waathirika wa wizi wa simu kutoka Kituo cha Kilwa Road anasema aliripoti kuibiwa simu Novemba 2023, akakabidhiwa Askari wa kufuatilia suala lake hilo kituoni hapo.
Kwa mujibu wa muathirika huyo anasema Afande anayefuatilia simu yake alimshauri kuwa itachukua muda mrefu kwani hupeleka IMEI Namba nyingi TCRA kwa ajili ya ufuatiliaji, hivyo inaweza ikachukua muda mrefu.
‘Aliniambia aniunganishe na mtu ambaye anafuatilia kupitia Application ambayo hiyo Application ni bure hatua za mwanzo lakini baadaye itakupasa ulipie, nikakubali na nikaanza kuwasiliana na huyo mtu’.
Baada ya kuanza kufuatilia aliipata katika eneo la Kimara, akatakiwa kuilipia kiasi cha Shilingi 50,000 na nauli na malipo ya huduma ni 50,000, hivyo alilipa Shilingi 100,000 ili waweze kwenda na afande anayefuatilia kesi wakamkamate lakini walipofika eneo la tukio walimkuta ndugu yake na aliawaambia huyo mtu amesafiri lakini anakaa maeneo hayo na kupewa namba ya anayetumia simu hiyo ambaye alisema yupo Mkoani.
Walipoendelea kumbana mtu huyo akasema amenunua simu hiyo kutoka kwa Mgambo ambaye huyo Mgambo aliitoa kwa Afande fulani (akamtaja kwa jina).
Kilichofuata baada ya hapo simu haikupatikana tena japokuwa mhusika bado anaifuatilia mpaka sasa kwa matumaini kidogo ya kuipata.
Kesi nyingine ya Kituo cha Stakishari, Muathirika wa wizi alipoibiwa simu alijaribu kufuatilia mwenyewe kupitia Application na kuiona simu yake lakini ilipofika hatua ya kulipia alikwama, hivyo atafute msaada wa polisi.
Askari Polisi anayefuatilia kesi yake alimtaka kulipa Sh 120,000 ili aweze kumalizia ufuatiliaji lakini baada ya kulipa na kufuatilia kwa muda mchache, polisi alidai haioni simu hiyo popote kila anapoifuatilia, hivyo kesi iliishia hapo hapo na simu haijapatikana.
HALI HALISI
Hii ni mifano ya kesi katika kesi nyingi za namna hiyo. Ufuatiliaji wa simu iliyoibiwa kwa njia ya IMEI Namba unafanya kazi vizuri na simu ina uwezo wa kupatikana kwa urahisi sana lakini changamoto ni urasimu na vikwazo kutoka kwa baadhi ya Askari ambao wanaamua kuchukua jukumu la kuuza wao simu hizo na kesi kuishia hewani.
Pia soma ~ Waziri Bashungwa: Wanaolalamika kuibiwa Simu wanakutana na Nenda rudi nyingi kituo cha Polisi