Mpita Njia
JF-Expert Member
- Mar 3, 2008
- 6,997
- 1,163
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Februari 16, 2009
Serikali ya Muungano ina dhamira gani kwa Zanzibar
Februari 16, 2009
Serikali ya Muungano ina dhamira gani kwa Zanzibar
Wapendwa Wanahabari,
Wakati Rais wa Jamhuri ya Watu wa China, Mhe. Hu Jintao, akimaliza ziara yake ya siku tatu katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, sisi Chama cha Wananchi (CUF), kwa niaba ya Watanzania wanaopendelea Muungano udumu katika misingi ya uadilifu na usawa, tumesikitishwa na kuondoka kwa Rais huyo bila ya kwenda Zanzibar.
Ambapo tukio hili linaweza kuonekana la kawaida tu katika macho yasiyoona mbali, katika duru za kisiasa na kidiplomasia ni pigo kubwa kwa dhamira ya Muungano wa dola mbili za Tanganyika na Zanzibar na dalili kwamba ile khofu waliyokuwanayo Wazanzibari kwa siku nyingi sana, sasa inazidi kuwa kweli. Khofu hiyo ni kwamba Serikali ya Muungano haina dhamira njema kwa hadhi na heshima ya Zanzibar katika uso wa dunia na kwamba inafanya kila lililo ndani ya uwezo wake ili Zanzibar iendelee kusahaulika duniani.
Wapendwa Wanahabari,
Itakumbukwa kwamba uhusiano baina ya Zanzibar na China ni mkubwa na wa muda mrefu zaidi kutokana na historia ya kudai uhuru na Mapinduzi ya 1964. China ilikuwa katika nchi za mwanzo mwanzo kuyatambua Mapinduzi ya Zanzibar kabla ya hata baadhi ya majirani wa Zanzibar hawajafanya hivyo, na pia kufunguwa ubalozi wake Zanzibar. Tangu wakati huo, serikali za China na Zanzibar zimekuwa na uhusiano na ushirikiano wa karibu sana. Kwa hivyo, ni jambo la kusikitisha, kushangaza na kutia khofu kwamba Rais wa Jamhuri hiyo anakuja nchini Tanzania, lakini hapangiwi kwenda Zanzibar, ambako kuna mizizi mirefu ya kimahusiano baina ya nchi hizo.
Wapendwa Wanahabari,
Huu ni mfano mmoja tu kati ya mifano ya hivi karibuni hasa tangu kuingia madarakani kwa Rais Jakaya Kikwete inayoonesha khitilafu katika dhamira ya Muungano panapohusika uwanja wa diplomasia na siasa na kimataifa. Mwaka jana alikuja nchini Rais wa Jamhuri ya Watu wa Komoro, Mhe. Mohammed Sambi, lakini naye pia hakupangiwa kwenda Zanzibar. Rais George Bush pia wa Marekani alikuja Tanzania na kukaa zaidi ya siku nne lakini pia hakupelekwa Zanzibar. Mahusiano baina ya Komoro na Zanzibar ni makubwa na ya karne nyingi na mahusiano kati ya Zanzibar na Marekani yanarudi nyuma tangu mwaka 1833 kwa kufunguliwa ubalozi rasmi wa Marekani mjini Zanzibar. Si stahiki hata kidogo ukweli huu kupuuziwa kwa makusudi katika uwanja wa siasa za kimataifa na kidiplomasia.
Wapendwa Wanahabari,
Sisi, CUF, tunasimamia imani kwamba Muungano huu ni baina ya dola mbili huru na zilizokasimu sehemu ya madaraka yake kwa serikali moja kuu, lakini wakati huo huo zikibakia na utambulisho wake ambao lazima utambuliwe na uheshimiwe. Kwa hivyo, tunachukulia vitendo kama hivi kama jitihada za makusudi za kuifanya jumuiya ya kimataifa isahau uwepo na hadhi ya Zanzibar. Tunatarajia wapangaji wa protokali wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania watazifanya ziara zijazo za wakuu wa nchi na au za wale wa taasisi ya kimataifa kuzingatia ukweli huo.
Imetolewa na
Salim Bimani,
Naibu Mkurugenzi,
Haki za Binaadamu na Mahusiano ya Umma,
The Civic United Front (CUF Chama cha Wananchi)
Party Headquarters
P.O. Box 3637
Zanzibar
Tanzania Tel: +255 777 414 112/414 100
cufhabari@yahoo.com
Weblog: Haki na Umma
Website: Kuhusu CUF